Sunday 1 December 2019

Picha : AGPAHI YASHIRIKI MAADHIMISHO YA SIKU YA UKIMWI DUNIANI...SERIKALI YAONYA USHAMIRI MAAMBUKIZI YA VVU SHINYANGA

...

Na Kadama Malunde – Malunde 1 blog 
Shirika lisilo la kiserikali ya Ariel Glaser Pediatric AIDS Healthcare Initiative (AGPAHI) linalojihusisha na mapambano dhidi ya Virusi Vya UKIMWI na UKIMWI imeungana na serikali ya mkoa wa Shinyanga kuadhimisha Siku ya UKIMWI duniani Desemba 1,2019 kwa kutoa huduma mbalimbali zinazolenga kupunguza maambukizi mapya ya VVU.

Maadhimisho hayo kwa mkoa wa Shinyanga yamefanyika katika kijiji cha Negezi kata ya Ukenyenge wilayani Kishapu ambapo mgeni rasmi alikuwa Mkuu wa wilaya ya Kishapu Mhe. Nyabaganga Talaba kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Zainab Telack. 

AGPAHI imeshiriki katika maadhimisho ya siku ya UKIMWI duniani kwa kutoa elimu ya VVU na UKIMWI na maonesho ya shughuli zinazofanywa na AGPAHI ikiwemo ujasiriamali kwa vijana wanaolelewa na shirika hilo. 

Akizungumza kwa niaba ya wadau wanaoshirikiana na serikali katika mapambano dhidi ya VVU na UKIMWI,Meneja wa Shirika la AGPAHI Kanda ya Ziwa, Dkt. Nkingwa Mabelele amesema wadau ikiwemo AGPAHI wanaendelea kushirikiana serikali ili kuhakikisha maambukizi mapya ya VVU yanapungua. 

“Tunaendelea kushirikiana na serikali bega kwa bega ili kufikia asilimia 90 ya huduma za VVU na UKIMWI (malengo ya 90-90-90)”,amesema Dkt. Mabelele. 

“Tunataka asilimia 90 ya wananchi wote wanatambua afya zao,90% ya wanaogundulika kuwa na maambukizi ya VVU wanaingia katika mpango wa matumizi sahihi na ufuasi mzuri wa dawa na 90% inayobaki ni wale wote wanaotumia dawa kuhakikisha wanakuwa na kiwango cha chini cha VVU”,ameongeza Dkt. Mabelele. 

Alisema Tanzania bila UKIMWI inawezekana hivyo kuwaomba wadau na jamii kwa ujumla kushikamana na kushirikiana na serikali ili kuhakikisha maambukizi mapya ya VVU yanapungua. 

Kwa upande wake, Mkuu wa wilaya ya Kishapu, Mhe. Nyabanga Talaba alisema kutokana na utafiti uliofanyika hivi karibuni,mkoa wa Shinyanga hivi sasa una ushamiri wa maambukizi ya VVU ya asilimia 5.9 (THIS 2017) ambayo iko juu ya kiwango cha taifa cha sasa cha asilimia 4.7 (THIS 2017). 

“Tafsiri rahisi ya ushamiri wa asilimia 5.9 ina maanisha kuwa watu 5 hadi 6 kati ya 100 huambukizwa Virusi vya UKIMWI takribani kila saa moja inayopita kwa mkoa wetu wa Shinyanga”,alieleza Talaba kwa niaba ya mkuu wa mkoa wa Shinyanga. 

Talaba aliwahamasisha wananchi kuendelea kujitokeza kupima ili wajue afya zao huku akiwakumbusha wanaume kufanyiwa tohara ili kupunguza hatari ya kupata maambukizi ya VVU sambamba na kuachana na mila potofu zinazochochea maambukizi mapya ya VVU. 

“Tuendelee kuchukua tahadhari kwani UKIMWI bado upo na hauna chanjo wala tiba, bali una kinga na dawa za kufubaza makali ya VVU. Kama umepata maambukizi tafadhali endelea kutumia dawa za kufubaza makali ya VVU na zingatia lishe kwani kuwa na maambukizi ya VVU haimaanisi kuwa ndiyo mwisho wa maisha yako”,alisema Talaba. 

Mkuu huyo wa wilaya ametumia fursa hiyo kuyapongeza mashirika yanayoshirikiana na serikali katika mapambano dhidi ya VVU na UKIMWI na kuyaomba yaongeze nguvu zaidi ili kufikia malengo ya 90-90-90. 

Kauli mbiu ya maadhimisho ya siku ya UKIMWI duniani Desemba 1,2019 ni ‘Jamii ni chachu ya mabadiliko tuungane kupunguza maambukizi mapya ya VVU’.

ANGALIA PICHA HAPA CHINI

Mkuu wa wilaya ya Kishapu Mhe. Nyabaganga Talaba akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Zainab Telack kwenye kilele cha maadhimisho ya Siku ya UKIMWI Duniani  Desemba 1,2019 ambapo katika Mkoa wa Shinyanga yamefanyika katika Kijiji cha Negezi kata ya Ukenyenge wilayani Kishapu. Wa kwanza kulia ni Meneja wa Shirika la AGPAHI Kanda ya Ziwa, Dkt. Nkingwa Mabelele. Wa kwanza kushoto ni Mganga Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Dkt. Rashid Mfaume akifuatiwa na Kaimu Katibu Tawala mkoa wa Shinyanga Joachim Otaru. Picha zote na Kadama Malunde 1 blog
Mganga Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Dkt. Rashid Mfaume akizungumza wakati wa kilele cha maadhimisho ya Siku ya UKIMWI Duniani  Desemba 1,2019 ambapo katika Mkoa wa Shinyanga yamefanyika katika Kijiji cha Negezi kata ya Ukenyenge wilayani Kishapu.
Mratibu wa Kudhibiti UKIMWI mkoa wa Shinyanga, Dkt. Peter Mllacha akisoma taarifa ya UKIMWI mkoa wa Shinyanga kwenye kilele cha maadhimisho ya Siku ya UKIMWI Duniani  Desemba 1,2019 ambapo katika Mkoa wa Shinyanga yamefanyika katika Kijiji cha Negezi kata ya Ukenyenge wilayani Kishapu. 
Meneja wa Shirika la AGPAHI Kanda ya Ziwa, Dkt. Nkingwa Mabelele akizungumza kwa niaba ya wadau wanaoshirikiana na serikali katika mapambano dhidi ya VVU na UKIMWI.
Meneja wa Shirika la AGPAHI Kanda ya Ziwa, Dkt. Nkingwa Mabelele akizungumza kwenye kilele cha maadhimisho ya Siku ya UKIMWI Duniani  Desemba 1,2019 ambapo amesema wadau ikiwemo AGPAHI wanaendelea kushirikiana serikali ili kuhakikisha maambukizi mapya ya VVU yanapungua. 
Kushoto  ni Mkuu wa wilaya ya Kishapu Mhe. Nyabaganga Talaba (mwenye nguo nyekundu) akitembelea Banda la AGPAHI kwenye maadhimisho ya Siku ya UKIMWI duniani Desemba 1,2019. Katikati ni Meneja wa Shirika la AGPAHI Kanda ya Ziwa, Dkt. Nkingwa Mabelele (katikati) akimwelezea Mkuu wa wilaya ya Kishapu Mhe. Nyabaganga Talaba kuhusu shughuli zinazofanywa na shirika la AGPAHI ikiwemo kuhudumia watu wanaoishi na maambukizi ya VVU.
Meneja wa Shirika la AGPAHI Kanda ya Ziwa, Dkt. Nkingwa Mabelele akiendelea kumweleza Mkuu wa wilaya ya Kishapu Mhe. Nyabaganga Talaba kuhusu shughuli zinazofanywa na shirika la AGPAHI katika mapambano dhidi ya VVU na UKIMWI.
Mkuu wa wilaya ya Kishapu Mhe. Nyabaganga Talaba akiuliza swali kuhusu VVU na UKIMWI kwenye banda la AGPAHI.
Afisa Miradi Huduma Unganishi kwa Jamii AGPAHI mkoa wa Shinyanga Selephina Soteli akifafanua jambo kwa Mkuu wa wilaya ya Kishapu Mhe. Nyabaganga Talaba.
Mkuu wa wilaya ya Kishapu Mhe. Nyabaganga Talaba akiangalia sabuni ya maji iliyotengenezwa na vijana wanaolelewa na Shirika la AGPAHI ambao wameanzisha kikundi cha Ujasiriamali ili kujikwamua kiuchumi. Wa pili kushoto ni kijana Edson Jastine akieleza namna wanavyotengeneza sabuni na kumuomba Mkuu wa wilaya ya Kishapu Mhe. Nyabaganga Talaba kuwatafutia soko la kuuzia sabuni zao.
Mkuu wa wilaya ya Kishapu Mhe. Nyabaganga Talaba akiangalia sabuni zilizotengenezwa na vijana wanaolelewa na shirika la AGPAHI.
Mkuu wa wilaya ya Kishapu Mhe. Nyabaganga Talaba akiwapongeza vijana wanaolelewa na shirika la AGPAHI kwa kuanzisha kikundi cha ujasiriamali kinachowasaidia kujipatia kipato. Nyabaganga alitumia fursa hiyo kuwakumbusha wananchi kujishughulisha na kazi zitakazowasaidia kupata pesa ili ziwasaidie katika maisha yao.
Mkuu wa wilaya ya Kishapu Mhe. Nyabaganga Talaba na Wakurugenzi wa halmashauri za Kishapu (Stephen Ndaki) na Shinyanga (Hoja Mahiba) katikati wakiwaunga mkono vijana hao kwa kununua sabuni ambapo sabuni zote walizokuja nazo kwenye maonesho wakati wa maadhimisho ya siku ya UKIMWI duniani ziliisha baada ya Mhe. Talaba kuzipigia debe.
Mkuu wa wilaya ya Kishapu Mhe. Nyabaganga Talaba akiendelea kuuza sabuni zilizotengenezwa na vijana wanaolelewa na AGPAHI.
Wadau na wafanyakazi wa AGPAHI wakipiga picha ya kumbukumbu kwenye banda la AGPAHI wakati wa kilele cha maadhimisho ya Siku ya UKIMWI Duniani  Desemba 1,2019 ambapo katika Mkoa wa Shinyanga yamefanyika katika Kijiji cha Negezi kata ya Ukenyenge wilayani Kishapu.
Mkuu wa wilaya ya Kishapu Mhe. Nyabaganga Talaba akicheza muziki na akina mama wakati wa kilele cha maadhimisho ya Siku ya UKIMWI Duniani  Desemba 1,2019 ambapo katika Mkoa wa Shinyanga yamefanyika katika Kijiji cha Negezi kata ya Ukenyenge wilayani Kishapu.
Wanenguaji wa Kundi la Msanii wa Nyimbo za Asili Jibhela Ngelela kutoka kijiji cha Mayanji wilayani Kishapu wakitoa burudani wakati wa kilele cha maadhimisho ya Siku ya UKIMWI Duniani  Desemba 1,2019 ambapo katika Mkoa wa Shinyanga yamefanyika katika Kijiji cha Negezi kata ya Ukenyenge wilayani Kishapu.
Burudani ya sarakasi ikiendelea wakati wa kilele cha maadhimisho ya Siku ya UKIMWI Duniani  Desemba 1,2019.
Meza kuu wakifuatilia burudani.
Kijana akitoa burudani ya wimbo akielimisha kuhusu VVU na UKIMWI.
Wadau na wananchi wakiwa kwenye kilele cha maadhimisho ya Siku ya UKIMWI Duniani  Desemba 1,2019 ambapo katika Mkoa wa Shinyanga yamefanyika katika Kijiji cha Negezi kata ya Ukenyenge wilayani Kishapu.
Wanafunzi wakiwa kwenye maadhimisho ya Siku ya UKIMWI Duniani  Desemba 1,2019.
Wananchi na wanafunzi wakiwa kwenye  kilele cha maadhimisho ya Siku ya UKIMWI Duniani  Desemba 1,2019.
Mwalimu Kassim Mwenda akitoa ushuhuda jinsi alivyopata maambukizi ya VVU mwaka 2008 na mpaka sasa anaendelea kuishi kutokana na kuzingatia lishe na matumizi sahihi za dawa za kufubaza makali ya VVU.
Wadau wakiwa kwenye maadhimisho ya siku ya UKIMWI duniani Desemba 1,2019.
 Diwani wa kata ya Ukenyenge Mhe. Underson Mandia akizungumza wakati wa kufunga kilele cha maadhimisho ya Siku ya UKIMWI Duniani  Desemba 1,2019. Picha zote na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger