Wednesday 30 November 2016
FAHAMU JINSI FEDHA ZA TETEMEKO LA ARDHI MKOANI KAGERA ZILIVYOTUMIKA
Tuesday 29 November 2016
Ndege iliyokuwa imebeba wachezaji wa klabu ya soka ya Brazil imeanguka
Ndege iliyobeba watu 81 wakiwemo wachezaji wa klabu ya soka ya
Chapecoense kutoka Brazil imeanguka wakati ikikaribia kutua katika mji
wa Medellin nchini Colombia, mamlaka zathibitisha.
Taarifa kutoka eneo la tukio zinaarifu kuwa watu 76 wamefariki dunia huku watano wakipona.
Maofisa
wa uwanja wa ndege wa Medellin wamesema wachezaji wa Chapecoense
waliokuwa kwenye ndege hiyo walikuwa safarini kwenda kucheza fainali ya
Copa Sudemericana dhidi ya Atletico Nacional ya Medellin, Colombia.
Kutokana na ajali hiyo, mechi baina ya timu hizo iliyokuwa ichezwe kesho imeahirishwa hadi itakapotangazwa tena.
ASILIMIA 95 YA DARASA LA SABA WAENDA SEKONDARI, 28,638 WAKOSA SHULE 2017
WANAFUNZI 526,653 sawa na asilimia 94.8 ya waliofaulu mtihani wa darasa
la saba mwaka huu, wamechaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza mwakani
katika shule za sekondari za serikali katika awamu ya kwanza huku 28,638
wakishindwa kupangiwa shule katika awamu ya kwanza.
Kati ya wanafunzi hao, wasichana ni 268,052 sawa na asilimia 94.5 ya
wasichana waliofaulu na wavulana ni 258,601 sawa na asilimia 95.2 ya
wavulana waliofaulu. Wanafunzi waliosajiliwa kufanya mtihani wa darasa
la saba mwaka 2016 walikuwa 795,739, huku 244 wakifutiwa matokeo ya
mtihani kutokana na udanganyifu.
Katika mkutano wake na waandishi wa habari jana mjini hapa, Waziri wa
Nchi, Ofisi ya Rais anayeshughulikia Tawala za Mikoa na Serikali za
Mitaa (Tamisemi), George Simbachawene alisema wanafunzi waliochaguliwa
wamegawanyika katika makundi manne likiwemo la shule za bweni kwa wenye
ufaulu mzuri ambao waliochaguliwa ni 900 wavulana 480 na wasichana 420.
Alisema kwa shule za bweni za ufundi waliochaguliwa ni 1,005, shule za
bweni kawaida ni 780, shule za bweni kwa wenye ulemavu ni 723 na shule
za kutwa wanafunzi waliochaguliwa ni 523,245. Alisema jumla ya wanafunzi
3,408 sawa na asilimia 0.6 wamechaguliwa kwenda sekondari za bweni.
Jumla ya watahiniwa 555,291 walifaulu sawa na asilimia 70.36 ya
wanafunzi waliofanya mtihani, kati yao wasichana ni 238,753 sawa na
asilimia 51.1 na wavulana 271,538 sawa na asilimia 48.9.
Ufaulu umeongezeka kwa asilimia 2.52 ukilinganisha na asilimia 67.84 kwa
mwaka 2015. Simbachawene alisema katika uchaguzi huo, wanafunzi 28,638
hawakuchaguliwa katika awamu ya kwanza, na kuitaja mikoa ambayo
wanafunzi wamebaki ni Dar es Salaam (18,820), Arusha (4,752), Songwe
(1,465), Kigoma (1,208), Manyara (1,141), Lindi (608), Mbeya (406) na
Katavi (238).
Aidha, waziri huyo alisema kati ya wanafunzi 1,060,588 walioanza darasa
la kwanza 2010, wanafunzi waliosajiliwa kufanya mtihani wa darasa la
saba mwaka 2016 ni 795,739 sawa na asilimia 75 ya wanafunzi
walioandikishwa wakiwemo wasichana 422,562 sawa na asilimia 53.1 na
wavulana 373,177 sawa na asilimia 46.9 ya waliosajiliwa.
Akizungumzia udanganyifu, alisema watawavua madaraka kwa waliokuwa
waratibu elimu kata na walimu wakuu, kuwashitaki mahakamani na kupeleka
mashauri yao Tume ya Utumishi ya Walimu, baada ya udanganyifu kuongezeka
ambako watahiniwa 244 wamefutiwa matokeo mwaka 2016 ikilinganishwa na
wanane wa mwaka jana.
Alizitaja shule zilizohusika kwenye udanganyifu huo ni Shule ya Tumaini
na Little Flower za Sengerema mkoani Mwanza, Mikahamakumi iliyopo
Sikonge, Tabora ambazo ni za binafsi, wakati za serikali ni Kondi
Kasandalala iliyopo Sikonge, Tabora, Qash iliyopo Babati na St Getrude
iliyopo Madaba mkoani Ruvuma.
Aidha, alisema 10 bora za serikali ni Kazunzu iliyopo Halmashauri ya
Buchosa (Mwanza), Mwanahegele ya Maswa (Simiyu), Huruma ya Mbinga
(Ruvuma), Kabanga ya Ngara (Kagera), Butumba B (Jiji Mwanza), Masoko ya
Kilwa (Lindi), Lyambamgongo ya Bukombe (Geita), Kilimani ya Geita
Vijijini, Magufuli ya Chato na Nkome ya Geita Vijijini, Geita.
Alisema shule 10 zilizofanya vibaya ni Chohelo ya Mvomero (Morogoro),
ambayo ni ya mwisho kitaifa ikifuatiwa na shule za Iloliento, Longido
(Arusha), Mwalebi na Nchilila Meatu (Simiyu), Magingi ya Mvomero, Kilole
ya Lushoto, Tanga, Zege ya Korogwe, Tanga na shule tatu za Lubchi,
Kitengo na Mgata za Morogoro vijijini.
Breaking News:HAYA HAPA MAJINA ZAIDI YA 25000 YA WANAFUNZI FORM 6 WALIOCHAGULIWA KWA MUJIBU WA SHERIA KUJIUNGA VIKOSI MBALIMBALI VYA JKT AWAMU YA PILI 2016
Kama utahitaji kuangaliziwa jina lako/AU la ndugu yako kwa "usahihi" na "kasi ya ajabu" (ambapo utajibiwa ndani ya mda mfupi) kama umechaguliwa kujiunga na jkt na kambi uliyopangwa. tafadhali fanya yafuatayo;
SERIKALI YAKANUSHA KUHUSU WANAFUNZI WA DIPLOMA KUTOKWENDA DIGRII CHUO KIKUU
Monday 28 November 2016
SERIKALI Yapiga Marufuku Kusoma Degree Bila Kupita Form Six
Waziri wa Elimu na mafunzo ya ufundi Pro.Joyce Ndalichako amepiga marufuku wanafunzi kujiunga na masomo ya Shahada (degree) bila kupita kidato cha sita. Marufuku hiyo itaanza rasmi katikals mwaka ujao wa masomo. Prof.Ndalichako emesema mfumo wa elimu huria umechangia kuzalisha wasomi butu kwa kupokea wanafunzi dhaifu kitaaluma.
Ndalichako amesema wanafunzi wanaofeli kidato cha nne na kwenda kusoma certificate na baadae diploma ili wajiunge vyuo vikuu hawataruhusiwa kujiunga na masomo ya shahada (degree) kama hawajarudia (reseat) masomo yao na kupata alama za kwenda kidato cha tano, na wafanye mitihani ya kidato cha sita na kufaulu ndipo wajiunge vyuo vikuu.
Katika utaratibu huo, wanafunzi wa kidato cha nne watakaoruhusiwa kusoma shahada (degree) bila kupita kidato cha 5 na 6 ni wale waliofaulu kidato cha 4 na wakachaguliwa kwenda kusoma katika vyuo vya ufundi daraja la kati (Technicians). Lakini wale wanaokosa "credit" za kuendelea form five na kuamua kwenda certificate mwisho wao utakuwa diploma.
Kuhusu "foundation courses" kwa wanafunzi wa kidato cha sita walioshindwa kupata sifa za kusoma degree, Ndalichako amesema Foundation course haimuongezei mtu sifa.
"Kama mtu amemaliza kidato cha 6 akashindwa kufikisha "points" za kujiunga chuo kikuu, asidahiliwe kwa kusoma foundatiom course. Anapaswa kurudia mtihani wa kidato cha 6 kwa sababu baraza la mitihani linatoa fursa ya kurudia mara nyingi iwezekanavyo. Foundation course haimuongezei mtu sifa kama hana sifa zinazotakiwa kitaaluma" Amesisitiza Ndalichako.
RAIS Magufuli Ampongeza Paul Makonda
Magufuli ametoa kauli hiyo jana wakati akizungumza na Mkuu huyo wa Mkoa huo kwa njia ya simu wakati Makonda akiendelea na mkutano wa hadhara katika eneo la Mbezi Maramba Mawili jijini humo.
Amesema, juhudi anazozifanya Makonda ni za kuigwa na viongozi wengine katika mikoa yao kwani anasaidia kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili wananchi.
“Wananchi wana kero nyingi sana, lakini viongozi wao wangekuwa wanawasikiliza hata maswali wanayouliza hapo yasingeulizwa, nakupongeza sana Mkuu wa Mkoa natamani na viongozi wengine wangeiga mfano wako,”amesema Magufuli.
Rais alipigiwa simu na Makonda ili asaidie kutoa ufafanuzi kuhusu upana wa barabara zilizopo chini ya Wakala wa Taifa wa Barabara (Tanroads) baada ya wananchi kulalamikia kuvunjiwa maeneo yao ili kupisha ujenzi.
Katika ufafanuzi wake, Rais Magufuli alisema suala la barabara kutoka Ubungo hadi Ruvu tayari wameshalitolea ufafanuzi mara nyingi.
Amesema akiwa Waziri wa Ujenzi wakati serikali inataka kupanua barabara ya kutoka Ubungo kwenda Kibaha kulitokea malalamiko ya aina hiyo na kesi kuhusu suala hilo namba 137 ilifikishwa mahakamani ambapo serikali ilishinda na baadaye yalitolewa maelekezo kuhusu maeneo yaliyopo katika hifadhi ya barabara.
Amesema baada ya ushindi huo kutoka Mahakama Kuu walichukua hatua ya kubomoa nyumba zote zilizokuwa katika hifadhi ya barabara kwa mujibu wa sheria ya mwaka 1932 ambayo ilifanyiwa marekebisho mwaka 1949 ikafanyiwa tena marekebisho mwaka 1954 na mwaka 1965.
Amesema Sheria ya Ardhi namba 4 ya mwaka 1999 na Sheria ya Vijiji namba tano ya mwaka 1999 na Sheria ya Mipango Miji na Matumizi ya Ardhi ya mwaka 2007 zote zinatambua hifadhi ya barabara na kwa barabara ya Dar es Salaam kwenda Kibaha iliachwa kwa upana uliopo kama filta ya Jiji la Dar es Salaam.
“Mwito wangu kwa wananchi wazingatie sheria na sheria ni msumeno, tulitunga sheria sisi wenyewe hivyo ni wajibu wetu sisi serikali kusimamia sheria, lakini kama wanaona sheria haifai ni kiasi cha kwenda kulishauri Bunge libadilishe sheria ili barabara ya Ubungo iwe sentimita tano zipite bajaji tu, lakini ukweli unabaki palepale kwamba sheria ipo na haijawahi kubadilishwa,”amesema Rais Magufuli.
Aidha Magufuli aliipongeza Tanroads kwa kusimamia sheria kwani alisema itafika kipindi kutakuwa hakuna barabara nchini.
Rais Magufuli amesema pia kazi ya kuvunja nyumba zilizopo katika hifadhi ya barabara ipo pale pale kwa vile serikali imepata kiasi cha Sh bilioni 67 za kujenga barabara zinazobadilishana (interchange) katika eneo la Ubungo ambayo itakuwa ya ghorofa mbili au tatu ili kurahisisha usafiri.
“Ghorofa zote na majengo yatavunjwa bila fidia hata kama litakuwa jengo la Tanesco kwa sababu lazima tuzingatie sheria, lakini kama wananchi wataona wameonewa basi waende mahakamani,” alisema.
MTOTO WA MIAKA 11 ATUNUKIWA PHD TANZANIA
WAHITIMU, viongozi na wageni waliohudhuria Mahafali ya 32 ya Chuo Kikuu
cha Sokoine cha Kilimo (SUA) mkoani Morogoro, waliingiwa na simanzi
wakati mtoto, Tamar Aaron Mbogho (11), alipojitokeza na kupokea Shahada
ya Udaktari wa Falsafa (PhD), akimwakilisha mama yake Swai Sophia
Faustin ambaye alifariki dunia miezi sita kabla ya kufika siku ya
mahafali.
Tamar, mtoto pekee wa marehemu, ambaye baba yake mzazi ni Mkuu wa Wilaya
ya Mwanga, mkoani Kilimanjaro, Aaron Mbogho alifika katika hafla hiyo
akiwa ameambatana na ndugu zake kadhaa, tayari kwa ajili ya kupokea
heshima hiyo kwa niaba ya mama yake.
Gazeti hili liliweza kuwasiliana kwa njia ya simu na Mbogho akiwa katika
kituo chake cha kazi Mwanga ambapo alisema Tamar alifika katika hafla
hiyo kupokea shahada hiyo kwa niaba ya mama yake.
Kwa mujibu wa Mbogho, mkewe Dk Sophia alifariki dunia Mei 21, 2016,
wakati huo akiwa ameshahitimu masomo yake kikamilifu na alisema Tamar ni
mtoto wa pekee wa Sophia.
"Alikuwa ni mmoja wa wahitimu waliopaswa kutunukiwa shahada hiyo kwa
sababu tayari alishahitimu na kubakia muda wa mahafali, lakini bahati
mbaya akafariki dunia kabla ya muda kuwadia,” alisema na kuongeza.
"Binti yetu alipenda kwenda kuchukua shahada ya mama yake na
alisindikizwa na ndugu zake wa familia. Ameniambia malengo yake ni
kusoma kwa bidii ili aweze kupata Shahada ya Udaktari wa Falsafa kama
mama yake, " alisema Mbogho.
Katika mahafali hayo yaliyofanyika juzi katika Kampasi ya Solomon
Mahlangu, Mazimbu, wahitimu 61 walifuzu na kutunukiwa Shahada ya
Udaktari wa Falsafa ya Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo.
Naibu Makamu Mkuu Taaluma wa Chuo Kikuu hicho, Profesa Peter Gilla,
alisoma orodha ya watunukiwa ambapo pia alitaja jina la mwanafunzi
asiyekuwapo ambaye alifariki dunia, lakini akiwa amefuzu na anastahili
kupata Shahada ya PhD ya Chuo Kikuu hicho ambaye ni Sophia.
Hivyo, Mwenyekiti wa Mahafali hayo, Dk Benno Mrembuka, alimwongoza mtoto
Tamar kwenda kupokea shahada hiyo kutoka kwa Naibu Makamu Mkuu wa Chuo
Fedha na Utawala, Profesa Yonika Ngaga, hali iliyoleta simanzi na huzuni
kwa washiriki waliokuwepo katika mahafali hiyo.
Baadaye Tamar alielekezwa kufika mbele ya meza kuu ili kuwapa mkono
wageni mbalimbali ambao walitumia nafasi hiyo kumfariji kutokana na
kumpoteza mama yake mzazi ambaye alikuwa ni mhitimu.
Katika hatua nyingine, Makamu wa Mkuu wa Chuo Kikuu hicho, Profesa
Gerald Monela, alisema SUA imeendelea kutoa wahitimu wa Shahada ya
Sayansi na Ualimu katika masomo ya sayansi kwa ajili ya kukidhi mahitaji
makubwa ya walimu wa kufundisha shule za sekondari nchini.