Thursday, 4 September 2025

MAVUNDE AZINDUA KAMPENI KWA KISHINDO, AAHIDI KUIGEUZA MTUMBA KUWA MJI WA KISASA



Na Dotto Kwilasa,Dodoma

Mwanasiasa na mtumishi wa watu, Anthony Mavunde, amezindua rasmi kampeni zake za kugombea ubunge wa Jimbo la Mtumba kwa kishindo kikubwa, akiahidi mageuzi makubwa ya kiuchumi, kijamii na kimazingira katika jimbo hilo endapo atachaguliwa kuwa Mbunge.

Akizungumza na maelfu ya wananchi waliojitokeza kwenye uzinduzi huo leo Sept. 3,2025 Mavunde amesema kuwa anaomba ridhaa ya wananchi ili aendelee kuwatumikia kwa moyo mmoja, kwa kuwa amekuwa akiishi nao, anazifahamu changamoto zao, na ana nia ya dhati ya kuzitatua.

Mavunde ameeleza kwamba Serikali inawekeza zaidi ya shilingi bilioni 600 katika ujenzi wa mji mpya wa Serikali eneo la Mtumba, jambo ambalo ni fursa ya kipekee ya kufanya Jimbo hilo kuwa la kisasa, wa kuvutia na wenye huduma bora.

Amesisitiza kuwa uongozi wake utalenga kuhakikisha maendeleo hayo yanawanufaisha wananchi wa kawaida kwa kuwawekea miundombinu na huduma bora karibu yao.

Ameeleza kuwa tayari amejenga shule kadhaa zikiwemo Shule ya Msingi Chiwondo, Mkoyo, na Mahomanyika Sekondari ikiwa ni pamoja na ujenzi wa Shule ya Chahwa unaendelea.

Mavunde ameahidi kuwa kila kata au mtaa usio na shule, atahakikisha unapata shule ili kuondoa changamoto ya watoto kutembea umbali mrefu kutafuta elimu.

Aidha, amesema atapambana kuhakikisha michango ya mitihani ya Jumamosi inaondolewa ili kuwapunguzia mzigo wazazi.

Katika kuboresha miundombinu, Mavunde ameeleza kuwa atahakikisha barabara ya Hombolo – Mayamaya pamoja na barabara nyingine za ndani zinazopitika kwa shida zinajengwa kwa kiwango bora.

Ameahidi kununua greda maalum litakalotumika kwa matengenezo ya mara kwa mara ya barabara hizo ndani ya jimbo.

Kwa upande wa huduma ya maji, Mavunde amesema kuwa uwezo wa kuzalisha maji jijini Dodoma kwa sasa umefikia lita milioni 47 kwa siku na lengo lake ni kuhakikisha kila kata ikiwemo Hombolo, Ihumwa, na Mahomanyika inapata maji safi na salama kwa urahisi.

Amesema baadhi ya maeneo yenye uhitaji mkubwa huduma hiyo itatolewa bure, ili kuhakikisha kila mwananchi anapata huduma hiyo muhimu.

Mavunde amesema kuwa ili yote hayo yatimizwe anahitaji ushindi ili aendelee kuwa mtumishi wa kweli wa watu wa Mtumba huku akiahidi utumishi wa haki, uwazi, na maendeleo kwa vitendo kwa kuweka mbele maslahi ya wananchi wake.


Share:

Wednesday, 3 September 2025

HAYA HAPA MAGAZETI YA ALHAMISI SEPTEMBA 4,2025


Share:

ABIRIA WA SAFARI ZA USIKU WAPEWA ELIMU HATARI YA KULALA CHINI YA BASI



Na Mwandishi wetu Malunde 1 Blog 

Katika jitihada za kuimarisha usalama wa abiria wanaosafiri nyakati za usiku, Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Shinyanga kimeanzisha kampeni ya kutoa elimu kwa abiria kuhusu hatari zinazoweza kuwapata wanapochukua hatua zisizo salama wakiwa safarini, ikiwemo tabia ya kulala chini ya basi badala ya kukaa kwenye viti walivyopangiwa.

Elimu hiyo imetolewa na Sajenti David Ndimila wa Kikosi cha Usalama Barabarani mkoani humo, ambaye amesisitiza kuwa kumekuwa na ongezeko la abiria wanaoamua kujilaza chini kwenye njia ya kupita ndani ya basi, hasa nyakati za usiku wanapopatwa na usingizi.

Sajenti Ndimila amefafanua kuwa kitendo hicho si tu kwamba ni kinyume na kanuni za usalama wa abiria, bali pia ni hatari kubwa kwa maisha yao. 

“Kuna matukio ambapo basi linapata mtikisiko wa ghafla, iwe ni kutokana na hitilafu ya barabara au tukio la dharura la kuhitaji dereva kupunguza mwendo kwa haraka. Katika hali kama hiyo, abiria waliolala chini wako kwenye hatari kubwa ya kujeruhiwa, hasa kwa kugongwa na vitu vya ndani ya gari au kugonga sehemu ngumu kama viti au sakafu ya basi,” alieleza.

Katika kampeni hiyo, Sajenti Ndimila amezungumzia umuhimu wa abiria kufuata sheria ndogondogo za usalama barabarani ambazo mara nyingi hupuuziwa lakini zinaweza kuokoa maisha, na kusisitiza kuwa ni lazima abiria waketi kwenye viti vyao walivyowekewa na kufunga mikanda ya usalama wakati wote wa safari, bila kujali umbali au muda wa usafiri.

“Kufunga mkanda si kwa ajili ya kupendeza au kufuata mazoea, bali ni hatua ya msingi ya kujilinda dhidi ya ajali ambazo mara nyingine hutokea kwa ghafla.

Tunawaomba abiria wote wawe na uelewa na waache tabia ya kuchukulia poa masuala ya usalama barabarani,” ameongeza Sajenti Ndimila.

Aidha, ametoa wito kwa wamiliki na madereva wa mabasi kuhakikisha wanatoa elimu kwa abiria wao kabla ya kuanza safari, na kuwajibika kwa kuhakikisha kila abiria anakaa kwenye kiti na anafunga mkanda, Pia amesisitiza umuhimu wa madereva kuwakumbusha abiria kila wanapoanza safari ya usiku, kwani ni wakati ambao watu wengi hupatwa na usingizi na kufanya maamuzi yasiyo salama.

Kwa upande wao, baadhi ya abiria waliopokea elimu hiyo wamekiri kuwa hawakuwa wanatambua hatari ya kulala chini ya basi. 

“Nilikuwa nafikiri kulala chini kunaongeza usingizi au kupunguza uchovu, lakini sasa nimeelewa kuwa ni hatari zaidi,” amesema mmoja wa abiria waliokuwa safarini kuelekea Mwanza.

Kampeni hiyo inaendelea katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Shinyanga na imepokelewa kwa mikono miwili na wadau wa usafiri, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa taifa kupunguza ajali za barabarani na kulinda maisha ya watumiaji wa vyombo vya usafiri.

Share:

NAIBU WAZIRI CHUMI ASHIRIKI SHEREHE ZA KUADHIMISHA MIAKA 80 YA UHURU VIETNAM


Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Cosato Chumi, amemwakilisha Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mohamoud Thabit Kombo, ameshiriki kwenye maadhimisho ya miaka 80 ya Uhuru wa Vietnam yaliyofanyika jijini Dar Es Salaam. 

Maadhimisho hayo yamefanyika ikiwa ni pamoja na kuazimisha miaka 60 ya ushirikiano kati ya Vietnam na Tanzania.

Mhe. Chumi ameipongeza Vietnam kwa kuadhimisha miaka 80 ya uhuru taifa hilo na miaka 60 ya ushirikiano mzuri uliopo wa Kidiplomasia na Tanzania.

Mhe. Chumi amesema maadhimisho hayo yanaakisi mafanikio makubwa yaliyopatikana kijamii na kiuchumi kutokana na kufanya kazi kwa biddii, ustahilivu, na kufanya mabadiliko. Kwa miaka 80 sasa Vietnam imejenga uchumi thabiti, imara, na maendeleo endelevu. Vietnam inalenga kufikia nchi iliyoendelea ifikapo mwaka 2045.

Tanzania na Vietnam zinashirikiana katika maeneo ya uwekezaji, biashara, elimu, afya, kilimo pamoja na maendeleo ya sayansi na teknolojia kwa miongo sita iliyopita. 

Hivyo, Mhe. Chumi emesema Tanzania inatambua na kuthamini juhudi, mchango wa kujitolea na mapambano ya kihistoria baina ya Tanzania na Vietnam pamoja na wananchi wao.

Takwimu zinaonesha kuwa Vietnam ni nchi ya saba kwa kuwa soko kubwa la bidhaa za Tanzania ambapo mauzo ya bidhaa kutoka Tanzania kwenda Vietnam yameongezeka kutoka Dola za Kimarekani milioni 226.6 mwaka 2020 hadi Dola milioni 314.2 mwaka 2024 sawa na ongezeko la asilimia 38 katika kipindi cha miaka mitano iliyopita.

Kwa upande wake, Balozi wa Vietnam nchini, Mhe. Vu Thanh Huyen ameeleza dhamira ya Vietnam kuendeleza ushirikiano wa karibu na Tanzania, akisisitiza umuhimu wa kukuza biashara, uwekezaji na maendeleo ya teknolojia kama njia ya kukuza uchumi wa mataifa yote mawili.

Uhusiano wa Kidiplomasia kati ya Tanzania na Vietnam ulianza tangu mwaka 1965, na umefanikiwa kuimarisha ushirikiano wa uwili na wa kimataifa.
Share:

MADEREVA WA SERIKALI WATAKIWA KUDUMISHA NIDHAMU NA WELEDI KAZINI



Na Dotto Kwilasa,Dodoma

WAZIRI MKUU wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa, amewataka madereva wa Serikali kote nchini kufanya kazi kwa weledi, uadilifu na nidhamu ya hali ya juu ili kuhakikisha usalama wa maisha, mali na siri za Serikali.

Amesema madereva hao ni kiungo muhimu katika utekelezaji wa majukumu ya kila siku ya Serikali na hivyo wanapaswa kuwa mfano wa kuigwa katika mwenendo na maadili kazini.

Akizungumza leo Jumanne, Septemba 2, 2025, jijini Dodoma wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Chama cha Madereva wa Serikali Tanzania (CMST), Waziri Mkuu amesisitiza kuwa madereva wana wajibu wa kufanya ukaguzi wa magari kabla na baada ya safari kwa kuhakikisha wanajaza kikamilifu taarifa za safari na matengenezo.

"Mnatakiwa kutunza kumbukumbu hizo kwa uaminifu, acheni vitendo vinavyoweza kuhatarisha maisha ya watu, usalama wa mizigo na nyaraka za Serikali, au kuhatarisha hadhi ya utumishi wa umma, " Amesema na kuongeza;

Ni muhimu kuhakikisha mnavitumia vifaa vya kisasa vya usalama barabarani na kujiepusha na matumizi mabaya ya magari ya Serikali au kushiriki katika shughuli zinazoweza kuathiri ulinzi na usalama wa taifa,kumbukeni kuwa dereva ni muhimili wa usalama wa safari, abiria na nyaraka muhimu za Serikali,” amesema Waziri Mkuu Majaliwa.

Aidha, Waziri Mkuu amekipongeza Chama hicho cha Madereva wa Serikali kwa mchango wake katika kuboresha huduma za usafirishaji Serikalini na kuimarisha ustawi wa madereva. Ameahidi kuwa Serikali itaendelea kushughulikia changamoto zinazowakabili madereva.

Amesema , Serikali inajipanga kuboresha mazingira ya kazi, upatikanaji wa mafunzo ya mara kwa mara na uboreshaji wa maslahi ya madereva.

“Changamoto mlizowasilisha ni kielelezo cha kazi kubwa iliyopo mbele yetu ,Kwa ushirikiano wa karibu kati ya Serikali, waajiri na chama chenu, tutaendelea kusonga mbele kwa hatua madhubuti,” ameongeza.

Pia ametoa maagizo kwa waajiri kuhakikisha kuwa stahiki za madereva zinalipwa kwa wakati, ajira zinatekelezwa kwa mujibu wa muundo rasmi wa utumishi wa umma, na madereva wanapewa fursa za motisha kama ilivyo kwa watumishi wengine.

Amewataka waajiri kuzingatia haki za msingi za madereva ikiwa ni pamoja na mazingira bora ya kazi na usalama kazini.

Kwa upande wake, Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega, amesema kuwa madereva wa Serikali ni mhimili muhimu katika shughuli zote za kila siku Serikalini na kuwa nidhamu, uwajibikaji na uadilifu wao vina mchango mkubwa katika mafanikio ya taasisi za umma.

“Tutahakikisha kuwa ustawi wa madereva unakuwa kipaumbele chetu. Dereva akifanya kazi katika mazingira bora na yenye heshima, atatoa huduma bora kwa wananchi na Serikali kwa ujumla,” amesema Waziri Ulega.

Naye Katibu Mkuu wa CMST, Castro Nyabange, ameitumia fursa hiyo kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa hatua mbalimbali anazochukua kuboresha maslahi ya watumishi wa umma, ikiwemo madereva wa Serikali.

Amesema upandishaji wa mishahara na maboresho ya mazingira ya kazi umewagusa madereva moja kwa moja na kuahidi kuwa chama chao kitaendelea kushirikiana kwa karibu na Serikali katika kuhakikisha kuwa huduma zinazotolewa na madereva Serikalini zinaendelea kuwa za kiwango cha juu na za kuaminika.

Mkutano huo uliobeba kaulimbiu isemayo “Dereva wa Serikali, Epuka Ajali, Linda Gari Lako na Watumiaji Wengine wa Barabara na Oktoba Shiriki Uchaguzi Mkuu”, umehudhuriwa na zaidi ya madereva 2,500 kutoka Tanzania Bara na Zanzibar.

Aidha Mkutano huo unalenga kujadili changamoto, kubadilishana uzoefu na kuimarisha mshikamano kati ya madereva na Serikali katika kuboresha huduma kwa umma.



Share:

Tuesday, 2 September 2025

MIKAKATI UDHIBITI UPOTEVU WA MAJI CHALINZE YAWA DHAHIRI

Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) kupitia Mkoa wa Kihuduma Chalinze imedhibiti mivujo ya maji katika maeo ya Kiwangwa, Mwavi na Mwetemo wilayani Bagamoyo.

Akizungumzia kazi hiyo, Kaimu Meneja wa Mkoa wa Kihuduma Chalinze, Mhandisi Hafidhi Mketo amesema udhibiti huo umefanyika katika mabomba ya nchi 3', 2' na moja 1 na nusu ambayo wasambaza maji moja kwa moja hadi kwa wateja wa maeneo hayo.

"Kazi hii ina lengo la kusaidia kuongeza upatikanaji wa maji kwa wateja kwa kudhibiti upotevu wa maji, lakini pia tumeendelea kutoa elimu kwa wananchi ya ulinzi wa miundombinu ya maji pamoja njia rasmi za kutoa taarifa wakiona uharibifu wa miundombinu ili tuokoe maji yasipotee," amesema Mhandisi Mketo.

Kwa niaba ya wenyeviti wa maeneo hayo, Mwenyekiti wa kijiji Kiwangwa, Ndugu Ayubu Mziwanda amepongeza kasi ya Mamlaka katika kuimarisha huduma kwa kukarabati miundombinu kwa wakati na kupunguza upotevu wa maji katika maeneo yao ambapo kwa sasa huduma imeendelea kuimarika kwa wananchi.

Mpango mkakati wa Mamlaka ni kupunguza upotevu wa maji yanayozalishwa kutoka asilimia 52 ya sasa hadi kufikia asilimia 35 katika mwaka huu wa fedha 2025/2026 ili kuimarisha utoaji wa huduma ya uhakika kwa wakazi wa jiji la Dar es Salaam na Mkoa wa Pwani.
Share:

Wimbo Mpya: ELIZABETH MALIGANYA - SAMIA NYAHINGA

 

Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger