Tuesday 11 April 2017

JINSI SIMBA ILIVYOPATA USHINDI WA KIHISTORIA DHIDI YA MBAO UWANJA WA CCM KIRUMBA MWANZA

...
Simba wamepata ushindi wa kihistoria dhidi ya Mbao FC mechi ya ligi kuu Tanzania bara iliyochezwa kwenye uwanja wa CCM Kirumba mkoani Mwanza.

Mbao FC walianza kwa kutangulia kupata magoli mawili kipindi cha kwanza na kujiweka kwenye nafasi nzuri ya kuibuka na pointi tatu katika mchezo huo. Magoli ya Mbao yamefungwa na Bernard dakika ya 18 na dakika ya 33.
Hadi dakika ya 80 Simba ilikuwa nyuma kwa magoli 2-0 matokeo ambayo kama yangebaki hivyo dakika 90 zinamalizika basi Wekundu wa Msimbazi wangekuwa kwenye nafasi finyu ya kutwaa taji la ligi kuu msimu huu.
Mabadiliko yaliyofanywa na benchi la ufundi la Simba kwa kumtoa Pastory Athanas na nafasi yake kuchuliwa na Said Ndemla, Blagnon na Mavugo wakaingia kuchukua nafasi za Liuzio na Hamad ndiyo yaliyo badili mchezo na kuipa Simba ushindi wa kwanza Kanda ya Ziwa msimu huu baada ya kuchapwa 2-1 na Kagera Sugar Jumapili iliyopita.
Magoli ya Simba yamefungwa dakika za lala salama ambapo goli lao la kwanza limefungwa dakika ya 82 na Frederick Blagnon. Uzembe wa golikipa wa Mbao Erick Ngwegwe ambaye aliuacha mpira udunde kisha akashindwa kuudaka kwa usahihi ulitua miguuni mwa Blagnon akafunga goli la pili dakika ya 90+1 na kufanya matokeo kuwa 2-2.
Wakati kila mmoja akiamini mchezo utamalizika kwa sare ya Mbao 2-2 Simba, Mzamiru Yassin akaifungia Simba goli la tatu dakika ya 90+7 kwa shuti kali baada ya beki wa Mbao kupiga kichwa mpira ambao ulitua kwa Mzamiru kisha kiungo huyo wa Simba kuachia mkwaju uliomshinda mlinda mlango wa Mbao.
Ushindi huo unaifanya Simba ifikishe pointi 58 ikiwa imecheza mechi 26 na kurejea kwenye nafasi ya kwanza kwenye msimamo wa ligi kwa pointi mbili zaidi ya Yanga wanaoshuka kwenye nafasi ya pili lakini wakiwa na faida ya mechi moja mkononi.
Mbao inaendelea kubaki na pointi zake 27 ikiwa katika nafasi ya 13 kwenye msimamo wa ligi, pointi nne zaidi ya Toto Africans ambayo ipo katika timu tatu zitakazoshuka daraja.
Simba wataendelea kubaki jijini Mwanza wakisubiri kucheza dhidi ya Toto Africans timu ambayo imekuwa mwiba kwa ‘mnyama’ hususan mechi inapochezwa kwenye uwanja wa CCM Kirumba.
Mbao FC wamefungwa mechi zao zote (mbili) walizokutana na Simba msimu huu. Kabla ya kuchapwa 3-2 leo April 10, 2017, walifungwa 1-0 kwenye mchezo wa raundi ya kwanza uliochezwa October 20, 2016 kwenye uwanja wa Uhuru, Dar.
Swali ambalo mashabiki wengi wa Simba huenda wakawa hawajalipatia majibu ni kwanini Ibrahim Ajib, Laudit Mavugo, Said Ndemla na golikipa Daniel Agyei kuanzia nje wakati wanne hao wamekuwa wakifanya vizuri kwenye mechi za hivi karibuni?
Kikosi cha Simba kilichoanza kwenye mechi dhidi ya Mbao kiliongozwa na Juuko Murshid (nahodha), Peter Manyika Jr (GK), Hamadi Juma, Mohamed Hussein, Bessala Bokungu, James Kotei, Mzamiru Yassin, Juma Liuzio, Mohamed Ibrahim na Pastory Athanas.
Walionzia benchi ni Daniel Agyei, Mwinyi Kazimoto, Frederick Blagnon, Hija Ugando, Ibrahim Ajib, Said Ndemla na Laudit Mavugo.
Matokeo kutoka uwanja wa Manungu Complex, Turiani, Morogoro
Mtibwa Sugar 0-0 Azam FC
Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger