SERIKALI imewataka wahitimu wa darasa la saba waliomaliza mitihani yao jana nchini kote kutojihusisha na tabia au vitendo vyovyote vinavyohatarisha afya, usalama na maendeleo yao.
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu, ametoa onyo hilo leo katika tamko maalum alilolitoa kwa wanafunzi hao waliohitimu elimu ya msingi nchini kote.
Takwimu zinaonyesha kuwa, wanafunzi 795,761 (wavulana 372,883 sawa na asilimia 46.86 na wasichana 422,878 sawa na asilimia 53.14) walisajiliwa na kufanya mtihani wa darasa la saba mwaka huu.
“Hivyo ningependa kutumia fursa hii kuwaasa watoto waliomaliza darasa la saba kutojihusisha na tabia au vitendo vyovyote vinavyo hatarisha afya, usalama na maendeleo yao, kama vile kujihusisha kwenye masuala ya ngono, matumizi ya madawa ya kulevya na vileo katika kipindi hiki cha kusubiri matokeo ya mitihani yao,”amesema Ummy.
Amesema watoto wa Kike na Kiume wajitambue, na wajue kuwa wao ni hazina ya pekee katika maendeleo ya nchi.
Waziri Ummy amesema kipindi hiki wakitumie vizuri kwa kuwa waadilifu, waaminifu, wenye bidii na kuzingatia kanuni za nidhamu na tabia njema huku wakijiandaa kwa ajili ya kuendelea na elimu ya Sekondari.
0 comments:
Post a Comment