Monday 1 July 2019

Afisa Mtendaji Mkuu wa Safaricom,Bob Collymore Afariki Dunia

Ofisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya simu ya Safaricom, Bob Collymore amefariki dunia. Kwa mujibu wa taarifa kutoka Safaricom, matuti yamekuta Collymore asubuhi ya leo Jumatatu Juni 1, 2019 akiwa nyumbani kwake jijini Nairobi.

Vyombo vvya habari vya Kenya vimesema mwenyekiti wa kampuni hiyo Nicholas Ng'ang'a amesema afya ya Collymore ilikuwa mbaya kwa majuma ya hivi karibuni.

Collymore, alichukua likizo ya matibabu ya miezi tisa mwishoni mwa mwaka 2017 na kwenda Uingereza kwa ajili ya matibabu ya saratani na alirejea  Kenya Juni mwaka jana.

Collymore alianza kuongoza Safaricom mwaka 2010 kutoka kwa Michael Joseph ambaye kwa sasa ni mmoja wa wajumbe wa bodi ya kampuni hiyo.

Mwaka 2017 wanahisa walipiga kura kuongeza mkataba wa Bob Collymore kwa miaka miwili baada ya mkataba wake kuisha. Mkataba aliokuwa akiufanyia kazi ulikuwa unatarajiwa kufikia tamati mwaka 2020 na kumfanya kuwa Mkurugenzi aliyekalia kiti hicho kwa muda mrefu zaidi.

Viongozi kadhaa wakiwemo Rais Uhuru Kenyatta wametuma salamu za rambirambi kwa familia kutokana na kifo hicho.



Share:

MTENDAJI MKUU WA SAFARICOM AFARIKI DUNIA

Aliyekuwa ofisa mtendaji mkuu wa kampuni ya Safaricom nchini Kenya, Bob Collymore amefariki dunia leo asubuhi, Julai Mosi, 2019.

Taarifa iliyotolewa na mwenyekiti wa bodi ya wakurugenzi wa Safaricom, Nicholas Nganga imesema Collymore alikuwa anasumbuliwa na saratani kwa muda mrefu.

“Oktoba 2017 alienda Uingereza kwa matibabu na akarejea Julai 2018 kuendelea na majukumu yake huku akihudhuria hospitali kila ilipobidi. Mara ya mwisho alikuwa anatibiwa katika Hospitali ya Chuo Kikuu cha Aga Khan hapa Nairobi kabla hali yake haijawa mbaya zaidi,” amesema Nganga.

Raia huyo wa Uingereza ambaye hivi karibuni aliteuliwa kuwa mjumbe wa bodi ya taasisi ya saratani nchini Kenya, ameacha mke, Wambui Kamiru, na watoto wanne.

Kifo cha Collymore (61), kimetokea mwezi mmoja kabla hajastaafu kwani alipanga kuachia wadhifa huo Agosti mwaka huu.

Katika kipindi cha uongozi wake katika kampuni hiyo kubwa ya mawasiliano Afrika Mashariki,  imeweza kuisogeza mbele huduma ya M-Pesa iliyozinduliwa mwaka 2007, hivyo kuleta mageuzi katika sekta ya fedha Afrika.

Wakati Afrika ikisifika duniani kwa ubunifu huo, Collymore ni miongoni mwa watu muhimu katika maendeleo hayo ambayo sasa yanawanufaisha mamilioni ya wananchi huku ikirahisisha huduma za benki za biashara pia.

Tangu alipoanza kuiongoza kampuni hiyo mwaka 2010, Collymore amaeifanya Safaricom kuwa kampuni kubwa nchini Kenya inakohudumia wateja wawili katika kila watu watano wanaotumia simu ya mkononi.
Chanzo - Mwananchi
Share:

Picha : BODI YA USAJILI WA WABUNIFU MAJENGO (AQRB) YAWAJENGEA UWEZO WAANDISHI WA HABARI


Mwenyekiti wa Bodi ya Usajili wa Wabunifu Majengo na Wakadiriaji Majenzi (AQRB) Arch. Dkt Ludigija Bulamile akifungua mafunzo ya kuwajengea uwezo waandishishi wa habari Jijini Dar es Salaam yaliyoandaliwa na bodi hiyo kuhusu kuacha kuichanganya taaluma yao na ile ya wahandisi badala yake iuelimishe umma tofauti iliyopo baina ya taaluma hizo mbili na umuhimu wa kuwatumia wataalamu
hao wanapofanya ujenzi. Picha zote na Philemon Solomon
Kaimu Msajili wa Bodi ya Usajili wa Wabunifu Majengo na Wakadiriaji Majenzi (AQRB) Arch.Albert Munuo, akisoma taarifa kuhusu majukumu ya bodi hiyo (kulia) Mwenyekiti wa Bodi hiyo Dkt. Ludigija Bulamile.
Afisa Mkuu wa Sheria Bodi ya Usajili wa Wabunifu Majengo na Wakadiriaji Majenzi (AQRB) Ibrahim Mohamed akielezea makosa mbali mbali ya kisheria yanayofanywa yakiwemo yale ya uuzwaji wa ramani hadharani pasipo kufuata taratibu. 
Mwenyekiti wa Bodi ya Usajili wa Wabunifu Majengo na Wakadiriaji Majenzi (AQRB) Arch . Dkt Ludigija Bulamile akipitia taarifa mbali mbali za bodi hiyo.
Watumishi wa bodi hiyo wakiwa katika mafunzo ya kuwajengea uwezo waandishishi wa habari yaliyoandaliwa na bodi hiyo kuhusu kuacha kuichanganya taaluma yao na ile ya wahandisi badala yake iuelimishe umma tofauti iliyopo baina ya taaluma hizo mbili na umuhimu wa kuwatumia wataalamu hao wanapofanya ujenzi.
Afisa Mdhibiti Mwandamizi wa Bodi ya Usajili wa Wabunifu Majengo na Wakadiriaji Majenzi (AQRB) Mlezi Makuka (kushoto aliyesimama) akichangia mada yake wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo waandishishi wa habari yaliyoandaliwa na bodi hiyo kuhusu kuacha kuichanganya taaluma yao na ile ya wahandisi badala yake iuelimishe umma tofauti iliyopo baina ya taaluma hizo mbili na umuhimu wa kuwatumia wataalamu hao wanapofanya ujenzi.
Arch. Mbaraka Igangula akichangia mada.
QS.Mashaka Bundara akisisitiza jambo.
Arch.Joseph Ringo akichangia mada wakati wa mafunzo hayo.
Waandishi wa Habari wakichangia mada mbali mbali wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo yaliyoandaliwa na Bodi ya Usajili wa Wabunifu Majengo na Wakadiriaji Majenzi (AQRB) kuacha kuichanganya taaluma yao na ile ya wahandisi badala yake iuelimishe umma tofauti iliyopo baina ya taaluma hizo mbili na umuhimu wa kuwatumia wataalamu hao wanapofanya ujenzi.
Mwenyekiti wa Bodi ya Usajili wa Wabunifu Majengo na Wakadiriaji Majenzi (AQRB) Dkt. Ludigija Bulamile akijibu maswali.
Mwenyekiti wa Bodi ya Usajili wa Wabunifu Majengo na Wakadiriaji Majenzi (AQRB) Dkt. Ludigija Bulamile, Kaimu Msajili Albert Munuo pamoja na waandishi wa habari na wajumbe wa bodi hiyo wakiwa kwenye picha ya pamoja mara baada ya kumalizika kwa mafunzo hayo yaliyoandaliwa na Bodi ya Usajili wa Wabunifu Majengo na Wakadiriaji Majenzi (AQRB) 

 ****
BODI ya Usajili wa Wabunifu Majengo na Wakadiriaji Majenzi (AQRB) imewataka wanahabari nchini kuacha kuichanganya taaluma yao na ile ya wahandisi badala yake iuelimishe umma tofauti iliyopo baina ya taaluma hizo mbili na umuhimu wa kuwatumia wataalamu hao wanapofanya ujenzi.

Akizungumza wakati akifungua mafunzo ya
kuwajengea uwezo waandishishi wa habari yaliyoandaliwa na menejimenti ya bodi hiyo mwishoni mwa wiki Jijini Dar es salaam Mwenyekiti wa AQRB Dkt. Ludigija Bulamile alisema lengo ni kuwaelimisha waandishi shughuli na majukumu yake katika sekta ya ujenzi ili waweze kuuelimisha umma wa
watanzania faida na hasara za kutowatumia wabunifu majengo na wakadiriaji majenzi wanapofanya ujenzi wowote. 

Alisema kumekuwa na mkanganyiko wa utoaji taarifa
unaofanywa na waandishi wakati wanaripoti masuala yanayohusu taaluma hizo hivyo ili kuondoa mkanganyiko huo wanahabari wana kila sababu ya kuyatumia mafunzo haya kwa kuwaelimisha wengine kuzitumia kalamu zao
kuuelimisha umma tofauti za taaluma hizo.

'Elilimisheni jamii umuhimu wa kuwatumia wabunifu majengo na wakadiriaji majenzi katika ujenzi ili waweze kupata makazi bora, ambayo pia yatawapa nafuu kwenye gharama za ujenzi kulingana na matakwa,'alisema Bulamile. 

Aliongeza kufafanua zaidi sababu za wahandisi kufahamika zaidi na umma kuliko wabunifu majengo na wakadiriaji majenzi pamoja na kufanya kazi zinazoshabihiana kuwa ni pamoja na taaluma hiyo kuchelewa kuingia  nchini. 

"Mpaka sasa nchi nzima ina wataalamu wa taaluma hii wasiozidi 1,500 hili bado ni tatizo kulingana na idadi ya
watu na mahitaji yake," alisema Dkt. Bulamile na kuongeza bodi imeendelea kuongea na baadhi ya vyuo vikuu vilivyopo nchini vione umuhimu wa kufundisha taaluma hii ili kuongeza idadi ya wataalamu watakaowezesha kuibadili
sura ya nchi hapo baadae katika sekta ya ujenzi kwa kubuni majengo ya kisasa yanayoendana na wakati.

Kwa upande wake Kaimu Msajili wa bodi Mkadiriaji Majenzi
Albert Munuo alisema kuwa,pamoja na kusajili wataalamu wa fani hiyo na makampuni pia wanamajukumu ya kukagua miradi ya ujenzi inayoendelea ili kuona kama wataalamu wamehusika.

" Tumekuwa tukikagua ujenzi wa miradi mbalimbali 
mikubwa inayoendelea na kwamba kwa sasa tunajipanga kuutembelea mradi wa ujenzi wa reli ya kisasa SGR ili kujionea ni kwa namna gani Wabunifu Majengo na
Wakadiriaji Majenzi wameshiriki ,'alisema Munuo

Aliongeza kuwa AQRB ni taasisi ya serikali iliyopo chini ya
Wizara ya Ujenzi na kwamba mpaka sasa ina ofisi katika kanda tano ikiwepo Kanda ya Mashariki, kanda ya ziwa, kanda ya kaskazini ,nyanda za juu kusini na kanda
ya kati. 

Mafunzo hayo pamoja na kuhudhuriwa na baadhi ya waandishi kutoka vyombo mbalimbali zikiwepo televisheni, redio na magazeti pia wataalamu wengine wa ujenzi kutoka AQRB akiwepo mwanasheria wao alishiriki na kusema yapo makosa mbali mbali ya kisheria yamekuwa yakifanywa ikiwepo lile la uuzwaji wa ramani hadharani pasipo kufuata taratibu. 

Hata hivyo wataalamu hao waliongeza kutolea mfano kwa kusema asilimia 90 ya nyumba zilizojengwa Dar es salaam zimejengwa bila vibali na kusababisha hasara kwa jamii pale ambapo eneo hilo linapokuja kubainika kuwa si mahali sahihi kwa ujenzi wa makazi na kulazimika kubomolewa. 

Share:

Maelfu ya Wananchi waandamana Tena nchini Sudan .....7 Waripotiwa Kufariki dunia

Watu wasiopungua saba wanaripotiwa kuuawa nchini Sudan baada ya vikosi vya usalama vya nchi hiyo kutumia mkono wa chuma kuyatawanya maandamano ya wananchi ya kutaka utawala wa kiraia.

Taarifa zaidi zinasema kuwa, maandamano makubwa ya jana ya wananchi wa Sudan katika miji mbalimbali ya nchi hiyo ukiwemo mji mkuu Khartoum yaligeuka kuwa umwagaji damu baada ya vikosi vya usalama kuwavamia waandamanaji na kuwafyatulia risasi.

Wananchi hao walikuwa wakishiriki katika maandamano ya kutoa wito kwa Baraza la Kijeshi la Mpito la nchi hiyo kukabidhi madaraka ya nchi kwa utawala wa kiraia.

Duru za hospitali zinasema kuwa, watu karibu mia mbili wamejeruhiwa.

Baraza la Kijeshi la Sudan lilichukua madaraka tarehe 11 Aprili mwaka huu baada ya jeshi la nchi hiyo kumpindua Omar Hassan al-Bashir.  

Tangu Hapo, wananchi walianza kuandamana tena wakilitaka Jeshi likabidhi Madaraka ya nchi kwa utawala wa kiraia.


Share:

Waziri wa Viwanda na Biashara Akerwa na Watanzania Wanaobeza Ubora wa Korosho ya Tanzania

Waziri wa Viwanda na Biashara ,Innocent Bashungwa amekemea baadhi ya Watanzania wanaopotosha  na kukandia kuwa korosho ya Tanzania iliyopo kwenye maghala ,haina ubora ambapo amewapasha kuacha propaganda zisizo na tija kwa Taifa.

Ameyasema hayo mjini Kibaha alipotembelea kiwanda cha Kubangua Korosho cha Terra Cashew na kiwanda cha sabuni ya unga cha Keda vilivyopo wilayani Kibaha mkoani Pwani.

Bashungwa alisema kuwa korosho ya Tanzania ni bora na iko kwenye daraja la kwanza na la pili huku daraja la tatu likiwa ni kidogo sana.

“Tunaitangazia dunia kuwa korosho ya Tanzania ina ubora na viwango vinavyotakiwa na katika kuhakikisha ubora huo nimepita kwenye maghala yote 37 ambayo yanahifadhi korosho nikiwa na wataalamu tumehakiki na kujionea hali halisi,” alisema Bashungwa.

Alisema kuwa wameandaa taarifa za kila ghala na aina na ubora wa korosho hivyo wanunuzi wanaweza kupata taarifa zote juu ya korosho na aina wanayoitaka.


Share:

Maamuzi ya IGP Sirro na IGP wa Msumbiji kuhusu mauaji ya Watanzania 10

Mkuu  wa Jeshi la Polisi nchini (IGP), Simon Sirro amekutana na kufanya mazungumzo ya kina na Mkuu wa Jeshi la Polisi wa nchi ya Msumbiji, Bernardino Rafael kuhusu mauaji ya Watanzania 10 yaliyotokea Juni 26, mwaka huu, katika kijiji cha Mtole nchini Msumbiji.

Watanzania hao waliuawa kwa kupigwa risasi na wengine kushambuliwa kwa mapanga katika kijiji hicho kilichopo mpakani mwa Tanzania na Msumbiji pembezoni mwa mto Ruvuma, ambapo mkuu huyo wa jeshi la Msumbiji amekiri kuwepo kwa wahalifu nchini mwake.

Baada ya kikao hicho, IGP Sirro aliwaambia waandishi wa habari mjini Mtwara kuwa kwa pamoja wameweka mikakati ili kuhakikisha kuwa matukio kama hayo hayatokei tena, kwa lengo la kuendelea kukuza uhusiano na ujirani mwema baina ya mataifa hayo mawili.

Kikao hicho kilikuwa na lengo la kuweka mikakati ya pamoja kati ya nchi hizi mbili na kuweza kupambana na wahalifu, wanaofanya vitendo vya kuwatia hofu wananchi wa nchi zetu hizi mbili.

“Kama nilivyowaambia jana kuwa IGP wa Msumbiji atakuja tukae pamoja na tupange mikakati ya kuweza kupambana na hawa wahalifu wanaotusumbua Watanzania, lakini pia wanawasumbua watu wa Msumbiji,” alisema IGP Sirro.

Alisema katika kikao hicho wamekubaliana mambo yanayoweza kufanyika katika kukabiliana na wahalifu, ambao siku zote huwa hawana mipaka kwa hiyo isiwe sababu ya kuzifanya nchini hizi mbili kushindwa kupambana nao.

“Ili kukabiliana na uhalifu wa kuvuka mipaka ni lazima kuwe na ushirikiano wa nchi hizi mbili na kikubwa ni kubadilishana taarifa na kufanya doria za pamoja ili kundi hili la watu wachache ambao wamekuwa wakisumbua na kufanya uhalifu kwa watanzania watiwe mbaroni na sheria ziweze kuchukua mkondo wake na kuleta majibu yaliyokuwa sahihi.

“Hivyo tumeweka mikakati ya kuhakikisha wale wote waliohusika na mauaji ya Watanzania na watu wa Msumbiji wanakamatwa haraka sana na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria.”


Share:

Uturuki yamuonya vikali mbabe wa kivita wa Libya Jeneral Khalifa Haftar

Uturuki imesema kuwa vikosi vya kiongozi wa Libya Khalifa Haftar ”vitalengwa” ikiwa hawatawaachia huru haraka raia sita wa Uturuki. 

Vikosi vya Jenerali Haftar vilisema siku ya Ijumaa kuwa vitashambulia maslahi ya Uturuki kwa kuwa taifa hilo linaunga mkono serikali ya Libya inayoungwa mkono na jumuia ya kimataifa.

Pia walidai kuwa waliharibu ndege isiyo na rubani ya Uturuki kwenye anga la Tripoli.

Libya imekumbwa na machafuko na mgawanyiko tangu kuondolewa madarakani na kuuawa kwa aliyekuwa kiongozi wa taifa hilo, Muammar Gaddafi mwaka 2011.

Jenerali Haftar alianza mashambulizi dhidi ya serikali inayotambuliwa na jumuia ya kimataifa,(GNA) inayoongozwa na waziri mkuu Fayez al-Sarraj, mwezi Aprili.

Uturuki inaunga mkono GNA, inapeleka ndege zisizo na rubani, silaha na magari kwa ajili ya kusaidia juhudi za serikali kupambana na vikosi vya Jenerali Haftar, ambavyo vinadhibiti sehemu kubwa ya mashariki na kusini mwa Libya.

Jenerali Haftar kutoka jeshi la taifa la Libya (LNA) amesema atashambulia meli za Uturuki kwenye maji ya Libya na maeneo muhimu ya kibiashara ya Uturuki.

Pia amezuia ndege za kibiashara kutoka Libya kwenda Uturuki.

Mapema siku ya Jumapili, Uturuki ilisema ”italipa kisasi kwa kuchukua hatua kali zaidi” kwa vitisho vyovyote kutoka kwa vikosi vya Jenerali Haftar.

Waziri wa ulinzi wa Uturuki, Huluski Akar ameonya kuwa vikosi vya LNA vya Libya vitalipa mashambulizi yoyote watakayofanya dhidi ya maslahi ya Uturuki.

Uturuki imesema inataka kupunguza mapigano dhidi ya Jenerali Haftar, ambaye anaungwa mkono na Umoja wa falme za kiarabu na Misri.

Siku ya Alhamisi, GNA ilichukua mji muhimu wa Gharyan, mji ambao ni ngome ya vikosi vya bwana Haftar.

Credit:BBC


Share:

Habari Zilizopo Katika Magazeti Ya Leo Jumatatu 1 July





















Share:

Sunday 30 June 2019

Chadema Watoa Tamko Tundu Lissu Kuvuliwa Ubunge

Chama Cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA kimedai kuwa hatua ya Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu kuvuliwa Ubunge na kuzuiliwa kugombea Ubunge kwa miaka 5 inalenga kumzuia kutowania Urais kwenye Uchaguzi Mkuu kwa mwaka 2020.

Kauli hiyo ya CHADEMA imetolewa na Katibu Mkuu wa Chama Cha hicho, DR Vincent Mashinji wakati akizungumza na waandishi wa habari juu ya hatua ya maamuzi ya Spika kumvua Ubunge Tundu Lissu kwa kushindwa kuhudhuria Bungeni.

"Kuna ibara inamfunga Lissu kugombea ndani ya miaka mitano, na inambana hawezi kugombea Urais wa Tanzania kama hana sifa za kugombea Ubunge Tanzania, naomba tutafakari tukiwa tumebakiza mwaka mmoja kwenda Uchaguzi Mkuu 2020", amesema Mashinji.

"Muda wote ambao Spika anadai Lissu hajui alipo, Bunge limekuwa likimlipa mshahara, hili jambo si la kawaida, na watanzania wote wanajua Mama Samia Suluhu alikwenda kumsalimia Lissu Nairobi, na alienda kumpatia salamu za pole kutoka kwa Rais.", ameongeza Mashinji.

Mapema Ijumaa ya wiki iliyopita, Spika Job Ndugai alitangaza kumvua Ubunge Tundu Lissu kwa kile alichokidai kiongozi huyo kuwa na mahudhurio hafifu ndani ya Bunge.


Share:

MWANAFUNZI WA CHUO KIKUU AUAWA KWA KUPIGWA RISASI NDANI YA CHUMBA CHA MPENZI WAKE

Mwanafunzi wa chuo kikuu cha Kenyatta Felix Otieno  ameuawa kwa kupigwa risasi akiwa ndani ya nyumba ya mpenzi wake mtaani Ruiru nchini Kenya leo Jumapili Juni 30,2019.

Maafisa wa upelelezi kutoka kitengo cha Elite Special Prevention Unit wanashirikiana na polisi kufanya uchunguzi kubaini chanzo cha kifo cha mwanafunzi huyo.

 Imeripotiwa kuwa Otieno aliuwawa baada ya kupigwa risasi na watu wasiojulikana wakati mpenzi wake hakuwa nyumbani.

 Marafiki aliokuwa na chumbani waliweza kutoroka bila ya kupatwa na majeraha, Otieno alikimbizwa hospitalini ila aliaga dunia kabla ya kuhudumiwa na madaktari.

Akidhibitisha kisa hicho, afisa mkuu wa polisi wa Ruiru James Ngetich alisema uchunguzi umeanzisha ili kuwakamata waliohusika na mauaji hayo. 

" Tunafanya uchunguzi kubaini hao majambazi walikuwa akina nani na mbona walimlenga Otieno tu, madai mengi yameibuka ila hatutaki kubahatisha," Ngetich alisema kama alivyonukuliwa na gazeti la The Standard.

Chanzo - Tuko.
Share:

MFUNGWA AJIUA KWA KUJICHINJA NA WEMBE GEREZANI

 Agustino Moshi (70), mfungwa aliyekuwa anatumikia kifungo cha miaka 30 jela kwa ubakaji, amejiua kwa kujikata mshipa wa fahamu kwa kutumia wembe akiwa ndani ya Gereza la Karanga mkoani Kilimanjaro.

Tukio hilo linadaiwa kutokea Jumatatu ya Juni 25 ndani ya gereza hilo na kushuhudiwa na mkuu wa gereza hilo, Kamishina Msaidizi wa Magereza (ACP), Leonard Moshy.

Habari ambazo zimethibitishwa pia na ACP Moshy zinasema mfungwa huyo mwenye namba 648/2015 alijikata na wembe kwenye mshipa wa fahamu shingoni mara tatu.

“Huyo mzee alitokea gereza la Maweni Tanga akaletwa kwa rufaa kwa ajili ya kutibiwa KCMC sasa siku hiyo walizozana na ACP Moshy na ndio akaamua kujiua mbele yake,” kilidokeza chanzo chetu cha habari.

Kwa mujibu wa mtoa habari huyo, siku hiyo saa 8 mchana, mkuu wa gereza alifika ndani ya gereza kwa lengo la kuwapangia wafungwa kazi ya kwenda shambani, lakini mzee huyo akadai anaumwa.

“Huyo mzee alimwambia bwana jela (ACP Moshy) kuwa ana ED (kibali cha daktari cha kupumzika) lakini bwana jela akakataa na ndipo huyo mzee akasema basi ngoja afe tu,” alidokeza mtoa taarifa.

“Hapohapo akatoa kiwembe akaanza kujikata shingoni kwenye mshipa wa fahamu. Yaani anaushika anajikata damu zinatiririka. Kama mara tatu. Lilikuwa ni tukio la ghafla ambalo kila mtu hakulitarajia”.

Baadaye askari magereza walifanikiwa kumkimbiza katika zahanati ya gereza kwa ajili ya matibabu ya kuokoa maisha yake, lakini hata hivyo kutokana na majeraha hayo alifariki dunia.

Ofisa Uhusiano wa Hospitali ya Rufaa ya KCMC, Gabriel Chisseo alilithibitishia Mwananchi jana juu ya kupokelewa kwa mwili huo na kwamba hadi jana, bado ulikuwa umehifadhiwa hospitalini hapo.

Na Daniel Mjema, Mwananchi
Share:

SERIKALI IRINGA YAMPONGEZA DIWANI KWA KUOKOA MAISHA YA FAMILIA ZILIZOKOSA MATIBABU


Mkuu wa wilaya ya Iringa Richard Kasesela wa pili kushoto akiwa na diwani wa Mwangata Nguvu Chengula (mwenye suti nyeusi) na viongozi wengine wakimtazama mama wa watoto watatu ambao nusuru wapoteze maisha kwa kukosa huduma ya matibabu 
Na Francis Godwin, Iringa

Serikali ya wilaya ya Iringa imepongeza jitihada za diwani wa kata ya Mwangata Nguvu Chengula (CCM) za kuokoa maisha ya mkazi wa Mwangata D Amida Mgonakulima na wanae watatu wasife kwa kukosa matibabu baada ya kutelekezwa na ndugu wakiwa nyumbani.

Pongezi hizo zimetolewa na mkuu wa wilaya ya Iringa Richard kasesela leo baada ya kuwatembelea wagonjwa hao waliolazwa katika Hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Iringa wakiendelea na matibabu ,kuwa jitihada hizo zilizochukuliwa na diwani huyo ni za kupongezwa kwani bila kufanya hivyo uwezekano wa mwanamke huyo na wanae kupona ulikuwa ni mdogo.

“Nimefarijika sana kuona hali ya wagonjwa hao ikiendelea vizuri maana huyo mama wa watoto alianza kuoza kuanzia kiunoni kushuka chini na hakuwa na uwezo hata wa kusimama kitandani lakini kwa sasa afya yake inazidi kwenda vizuri hakika diwani Chengula kanusuru uhai wao “ alisema Kasesela .

Aidha alitoa agizo kwa viongozi wa serikali za mitaa katika wilaya ya Iringa kufanya msako nyumba kwa nyumba ili kujua watoto ama wagonjwa waliotelekezwa kwa kukosa huduma za matibabu.

“ Yawezekana kabisa wagonjwa hao ni baadhi tu ya wagonjwa wengi ambao wamefungiwa ndani bila kutibiwa sasa naagiza watendaji wa mitaa kupita nyumba kwa nyumba kukagua na kama kuna nyumba mlango utakutwa umefungwa fungueni kagueni ndani mkiwa na mwenye nyumba ili kujua ndani kuna nini “ alisema Kasesela.

Kasesela alisema tukio jingine kama hilo la Mwangata la mgonjwa kutelekezwa amelisikia kijiji cha Kisanga na amekwisha tuma watendaji kwenda kufuatilia na kuwa matukio yote hayo ni ya kikatili na hatakubali kuyasikia ama kuyaona ndani ya wilaya yake.

Kwa upande wake diwani Chengula alisema uamuzi wa kunusuru uhai wa wagonjwa hao ulikuja baada ya wananchi wake kutoa taarifa na kuwa ataendelea kuwasaidia wagonjwa hao hadi watakapopona.

 Chengula ambaye ameungana na mkuu huyo wa wilaya ya Iringa kukabidhi mahitaji mbali mbali zikiwemo nguo na mengine amejitolea kumsomesha motto wa darasa la tatu katika shule yake ya Sun Academy ambapo ada yake kwa mwaka ni zaidi ya shilingi milioni moja na kuwa atamlipia kwa miaka yote na kumwendeleza 

Share:

Mwili wakutwa kichakani umekatwa miguu, mkono na Kiuno

Mtu  ambaye hajafahamika mara moja, amekutwa kichakani akiwa amefariki dunia huku baadhi ya viungo vyake vikiwa vimeondolewa.

Tukio hilo lilitokea katika kitongoji cha Nunga, Kata ya Ngogwa wilayani Kahama baada ya wananchi kuukuta mwili huo ukitoa harufu, huku viungo kama mkono, sehemu za siri na miguu vikiwa vimeondolewa na watu wasiojulikana wanaodaiwa kutekeleza mauaji hayo.

Ofisa Mtandaji wa Kata hiyo, Michael Magoyi, amesema  kuwa tukio hilo, kutokana na hali ya mwili, limetokea siku za karibuni chini ya wiki moja na wananchi walipogundua walitoa taarifa kwa mwenyekiti wa kitongoji hicho.

"Taarifa ya kuokotwa kwa mwili huo nilizipata kwa mwenyekiti wa kitongoji cha Nuja ambaye alidai kwamba alipelekewa taarifa hizo na mwananchi aliyefahamika kwa jina la Thomas Shaban. Baada ya kupokea taarifa hizo, nilifika eneo la vichaka kisha nikapiga simu polisi ambao walifika haraka na kuokota kiwiliwili hicho.

Magoyi alisema tukio hilo limezua taharuki miongoni mwa wananchi hasa baada ya watu waliofanya uhalifu huo kukata viungo mbalimbali vya mwili wa mtu huyo kisha kutoweka navyo.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Kamishna Msaidizi (ACP) Richard Abwao, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba mtu huyo ambaye hajafahamika aliuawa na watu wasiojulikana kisha kutelekezwa porini.

Kamanda Abwao alisema baada ya wauaji kutekeleza tukio hilo, mwili huo waliusambaratisha kwa kuukata vipande vipande na kubakiza kichwa, mkono mmoja na kifua, huku viungo vingine kuanzia kiuno na miguu yake na mkono walitoweka navyo kwa lengo wanalofahamu wao.

Kutokana na tukio hilo, Abwao alisema Jeshi la Polisi mkoani Shinyanga linaendesha msako ili kuwabaini watuhumiwa wa mauaji, huku akiwasihi wananchi lilikotokea tukio hilo, kuwa wepesi kutoa taarifa ili kudhibiti matukio ya namna hiyo.


Share:

Unahitaji Kufanya Service ya Gari Weekend Hii? Je wewe ni Mmiliki wa Gari? Ni Fundi Magari au Muuza Spea? ...Hapa Tunahabari Njema Inayokuhusu

Habari njema kwa wamiliki wa Magari, mafundi na Wauza Spea za Magari. EDRIVE PRO wamekeletea mfumo ambao unawaunganisha pamoja na pindi gari lako likiharibika popote ulipo hutapata tena tabu ya kuhangaika kutafuta fundi au maduka ya spea

www.edrivepro.co.tz ni mfumo wa kufanya na kusimamia utengenezaji wa magari online.

1. Katika mfumo huu wamiliki wa magari, maduka ya spare, na mafundi wanajisajiri ama wanaweza kusajiliwa kwa kuwasiliana na mtoa huduma wetu kwa e-mail edriveprotz@gmail.com

2. Baada ya kujisali kulingana nafasi yako [ mmiliki wa gari, muuza spare, fundi ama mwandika makala juu ya magari] msimamizi wa mfumo atakuthibitisha katika mfumo na utatumiwa e-mail na mfumo.

Baada ya kudhibitishwa utaweza kupata huduma za uuzaji wa spare, matengenezo ya magari kwa wamiliki wa magari na mafundi kupata fursa za mateja wapya mtandaoni nchi nzima.

3. Kutokana na wahusika wote katika mfumo huu kuwa wamesajiliwa, huduma katika mfumo huu ni nafuu na za uhakika.

Karibuni mjisajili katika www.edrivepro.co.tz


NB: Weekend hii kuna ofa kabambe kama unahitaji matengenezo ya Gari yako.  Hii si ya kukosa, Jisajili sasa.


Share:

Gavana Shilatu Ashangazwa Na Diwani Kutofuatilia Upatikanaji Wa Mikopo Ya Vijana, Wanawake Na Walemavu.

Na Mwandishi wetu Mihambwe
Afisa Tarafa Mihambwe Emmanuel Shilatu amembana Diwani wa Chama Cha Wananchi (CUF) Kata ya Mkoreha Mhe. Ahmad Ally Ndende juu ya utolewaji wa mikopo ya Halmashauri kwa Vijana, Wanawake na Walemavu ili kuwakwamua Wananchi kiuchumi.

Hayo yamejitokeza kwenye mkutano na Wananchi wa Kijiji cha Dinyeke kata ya Mkoreha ambapo Gavana Shilatu aliitisha ili kusikiliza na kutatua kero za Wananchi zinazowakabili.

Gavana Shilatu alimuuliza Diwani huyo kuelezea ni vikundi vingapi mpaka sasa vimenufaika na mikopo nafuu kwa Vijana, Wanawake na Walemavu toka Halmashauri ikiwa yeye ni Mwenyekiti wa Kamati ya maendeleo ya kata.

*_"Hakuna wanufaika wa mikopo hiyo ya 10% toka Halmashauri kwani vikundi vingi havijasajiliwa na havina miradi."_*  Alijibu Diwani Ndende.

Gavana Shilatu alisisitiza kazi ya viongozi ni kuonyesha njia ya kuwakwamua Wananchi kiuchumi pasipo kukwepa majukumu wala kuingiza ubaguzi.

Gavana Shilatu alisisitiza kuwa viongozi tunatakiwa kuhamasisha Vijana, wanawake na walemavu kuwatengenezea mazingira ya kuwa na vikundi vyenye katiba vilivyosajiliwa na vyenye shughuli maalumu ili waweze kupata mikopo hiyo.

_"Sisi viongozi tunajukumu la kuwaonyesha njia Wananchi na si kutumia mwanya wa kutokuelewa kwao kama njia ya kuwakosesha *FURSA MUHIMU* kama ya Mikopo nafuu toka Halmashauri. Na mikopo hii inatolewa kwa haki pasipo ubaguzi wa kiitikadi."_  Alisisitiza Gavana Shilatu.

Katika mkutano huo ulihudhuliwa na Diwani kata ya Mkoreha, Mtendaji Kata ya Mkoreha, Mtendaji Kijiji cha Dinyeke, Serikali ya Kijiji cha Dinyeke pamoja na viongozi wa Vitongoji.


Share:

Waziri Kamwelwe Atoa Kauli Nzito Baada Ya Mgomo Bandarini

Waziri  wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Isack Kamwelwe, ametishia kuzinyima leseni kampuni tatu zilizoomba leseni kwa ajili ya kuendesha bandari kavu(ICDS) kwa tuhuma za kuhamasisha mgomo wa malori bandarini.

Wamiliki wa kampuni hizo wanatuhumiwa kuhamasisha madereva wa malori yanayotoa mizigo bandarini kufanya mgomo kuanzia jana mchana hadi usiku kwa lengo la kuondolewa kwa mizani ya kupima uzito wa magari hayo kabla ya kuanza safari zake kwa njia ya barabara.

Kamwelwe ameyaeleza hayo jana, alipofanya ziara ya kukagua mizani hizo kuona kama inasababisha foleni kama ilivyodaiwa na baadhi ya wafanyabiashara hao na kubaini kuwa lori moja linachukua sekunde 55 hadi dakika moja kupimwa uzito.

"Nimekuja nione kama kweli hizi mizani zinasababisha foleni, lakini nimekuta si kweli kwa sababu kuna mizani mbili na zote ni nzima na wanatumia si chini ya dakika moja kupima na kuondoka eneo hili," alisema Kamwelwe na kuongeza;

"Sasa nimeshabaini waliohusika kufanya mgomo huu ni kampuni tatu ikiwamo PrimeFuel ambao tunawaita ni 'Wahaini' kwa sababu lengo lao ni kukwamisha miradi ya Serikali na waliomba leseni za ICDS sasa tutawaonyesha kama sisi ni Serikali na walichofanya si sahihi"

Alieza zaidi kuwa, leseni ya wafanyabiashara wa ICDS zinatoka Julai 17 na wafanyabishara waliohusika kufanya hujuma hizo hawatapatiwa leseni zao kwa sababu wanakwamisha juhudi za Rais John Magufuli.


Share:

Polepole Awapa Makavu Wanachama CCM....."Usitumie uongozi kama mali yako"

Katibu  wa Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM)  Humphrey Polepole amesema ugonjwa mkubwa ndani ya CCM ni ubinafsi na kuwataka kuacha kupendekeza wagombea ambao wananchi hawawataki.

Aidha aliwataka viongozi wa chama wakiwemo mabalozi wa nyumba 10 kuacha kupanga safu za watu wanaowataka badala yake wahakikishe wanasimamia utaratibu.

Polepole alitoa maaelekezo hayo kwa makamisaa nchini kote kukisema Chama cha Mapinduzi kinachofanya kazi zake chini ya Rais John Magufuli ili wananchi waelewe .Aliyasema hayo jana Jijini Arusha katika kikao maalumu cha kupokea Ilani ya Uchaguzi wa CCM 2015/2020 katika kipindi cha robo tatu ya mwaka wa fedha Julai 2018 hadi Machi 2019.

Katibu huyo wa Itikadi na Uenezi alisema anayepanga safu, aliyepangwa katika safu, kanuni za chama zinatoa adhabu kwa wale wote waliosababisha ukiukwaji wa uchaguzi au uteuzi wa wagombea

“Chama hakiangalii mtu kwa sura, mtatandikwa adhabu kali, uongozi ni dhamana usitumie uongozi kama mali yako na wale wabaya nawaambia acheni kupanga safu na tunawakata wale wote wasioheshimu maadili ya chama…

"Acheni kupanga safu za uongozi na nitawasubiri kwenye sekretarieti nitahangaika na wewe ulalo ulalo hadi kieleweke kura hazipigwi na viongozi wa CCM zinapigwa na wanachama wa CCM hivyo achene mambo yenu,” alisema.

Alisema kwenye serikali za mitaa, vijiji na vitongoji wekeni watu wanaokubalika na kama mnaona hawakubaliki kata weka wengine na mwaka kesho kwenye udiwani, madiwani wa CCM wafanye mikutano katika kata zao na wasiofanya mikutano wote watajulikana.

Polepole alisema Tanzania imepata bahati ya kuwa na Rais wa kipekee kwani Rais Magufuli amevunja historia nchini katika kipindi cha mwaka mmoja na miezi sita rais amejenga hospitali za wilaya 67 na vituo vya afya 353 nchi nzima.

Alisema yapo mengi mazuri Rais Magufuli amefanya ikiwa ni pamoja na kutoa ndege yake kwa ajili ya wananchi kuipanda na amenunua ndege kubwa mbili mpya, ujenzi wa bwawa kubwa la kufua umeme wenye uwezo wa kuvuna megawati za umeme zaidi ya 2000.


Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger