Wednesday, 7 January 2026
Tuesday, 6 January 2026
RAIS MSTAAFU WA DKT. KIKWETE, AZINDUA JENGO LA AFISI YA UHAMIAJI NA MAKAZI YA ASKARI MICHEWENI, MKOA WA KASKAZINI PEMBA
RAIS MSTAAFU WA DKT. KIKWETE, AZINDUA JENGO LA AFISI YA UHAMIAJI NA MAKAZI YA ASKARI MICHEWENI, MKOA WA KASKAZINI PEMBA
Monday, 5 January 2026
CHADEMA WAJIFUNZE KUTOKA KITABU CHA HESABU: KUKIRI MAMLAKA SI UDHAIFU, NI HEKIMA INAYOEPUSHA ADHABU NA MAANGAMIZI
Katika kipindi ambacho jamii inakabiliwa na changamoto mbalimbali za kimaadili na kimfumo, somo la kale kutoka Kitabu cha Hesabu Sura ya 16 limeibuka kuwa dira muhimu kwa Watanzania. Uchambuzi wa tukio la kihistoria la uasi wa Kora, Dathani, na Abiramu unatoa onyo kali: Kukataa mamlaka zilizopo si tu kukiuka utaratibu wa nchi, bali ni kualika hukumu ya kimungu na maangamizi.
Kitabu cha Hesabu kinaelezea kwa kina jinsi Kora na wenzake walivyojitokeza kupinga uongozi wa Musa na Haruni. Kwa nje, walionekana kana kwamba wanatetea haki na usawa wa jamii, wakidai kuwa kila mtu ni mtakatifu. Hata hivyo, maandiko yanabainisha kuwa ndani yao kulikuwa na sumu ya kiburi na kiu ya madaraka yasiyo ya halali.
"Uasi huu haukuwa tu dhidi ya binadamu, ulikuwa ni uasi dhidi ya 'God’s Order' (Utaratibu wa Mungu). Mungu ni Mungu wa mpangilio, na anapoweka mamlaka, anategemea nidhamu na utii ili kulinda amani ya wengi," anasema mchambuzi wa maandiko.
Moja ya mambo ya kusikitisha katika simulizi hiyo ni pale Musa alipojaribu kuwaita wapinzani wake (Dathani na Abiramu) ili wazungumze kwenye meza moja ya maridhiano. Kwa dharau, walijibu: "Hatuji!" Msimamo huu wa kukataa mazungumzo na kudharau mamlaka ndio uliopasua mlango wa hukumu. Matokeo yake, ardhi ilipasuka na kuwameza wote waliohusika na uasi huo.
Hii ni fundisho kwa Watanzania wa leo; kwamba kukaa kwenye meza ya mazungumzo na kukiri mamlaka si udhaifu, bali ni hekima ya kiroho inayookoa taifa dhidi ya machafuko.
Ili taifa liendelee, ni lazima kuwe na msingi wa kuheshimiana kati ya viongozi na wananchi: Kukiri mamlaka kunajenga nidhamu na kuzuia "hukumu ya pamoja" inayoweza kuikumba jamii pale uasi unapotawala. Ni lazima kutofautisha kati ya kutoa maoni kwa staha na kufanya uasi kwa nia ya kubomoa. Hayo yanatokana na ukweli kuwa Mfumo wa Mungu unamtaka kiongozi kuwa na moyo kama wa Musa—moyo wa unyenyekevu na utayari wa kusikiliza malalamiko ya watu kabla hayajazaa chuki.
Ukisoma kitabu hicho unang'amua kwamba amani, uwajibikaji, na haki haviwezi kupatikana kupitia mivutano na uasi. Badala yake, vinapatikana pale kila mmoja anapokubali mfumo sahihi uliowekwa na Mungu na sheria za nchi.
"Tunahitaji umoja zaidi ya hapo awali. Unapokataa mamlaka, unachallenge msingi wa utulivu wa taifa. Hukumu ya uasi si lazima iwe ardhi kupasuka, inaweza kuwa kupotea kwa amani, kusimama kwa maendeleo, na kuvunjika kwa misingi ya kijamii," anaongeza mchambuzi huyo.
Watanzania wanahimizwa kuachana na kiburi cha moyoni kinachochochea uasi. Kukiri mamlaka ni ukomavu. Ni ujasiri wa kutambua kuwa sote tunahitajiana chini ya mwavuli mmoja wa uongozi ili kufikia nchi ya ahadi. Tuwe na hekima, tuepuke uasi, na tuchague meza ya mazungumzo kwa ajili ya mustakabali wa taifa letu. Kwa kufanya hivyo, tunaepuka laana ya maangamizi na kuvuta baraka za Mungu juu ya nchi yetu.
"Hekima ya kweli ni kujua kuwa uasi una mwisho wa mauti, lakini utii na maridhiano huleta uzima."
Sunday, 4 January 2026
SH MILIONI 500 ZA RAIS SAMIA KWA TAIFA STARS NI UWEKEZAJI, SI MATUMIZI
Hatua ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kutoa zawadi ya Shilingi milioni 500 kwa timu ya Taifa, Taifa Stars, baada ya kufuzu hatua ya 16 bora ya AFCON, imeibua mijadala mipana miongoni mwa wananchi. Wakati baadhi wakitazama zawadi hiyo kama matumizi ya ziada, uchambuzi wa kina wa kiuchumi na kijamii unaonesha kuwa huu ni uwekezaji muhimu katika kugeuza mpira wa miguu kuwa ajira rasmi badala ya kuishia kuwa burudani ya msimu pekee.
Dunia ya sasa inaitazama michezo kama sekta ya uzalishaji inayochangia kwa kiasi kikubwa katika Pato la Taifa kupitia mnyororo wa thamani.
Zawadi hii ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inatuma ujumbe mzito kwa vijana nchi nzima kuwa soka ni taaluma inayoweza kumhakikishia mchezaji kipato na heshima, sawa na udaktari au uhandisi.
Kwa kuwapa wachezaji uhakika wa kipato, tunajenga mazingira ya wao kuanza kuishi kama wataalamu (professionals), jambo ambalo ndilo msingi wa mataifa makubwa ya soka duniani kama Senegal na Nigeria ambapo wachezaji wao ni bidhaa zenye thamani ya mamilioni ya dola katika soko la kimataifa.
Katika upande wa diplomasia ya michezo, mafanikio ya Taifa Stars yanaitangaza Tanzania kwa kasi kuliko kampeni nyingine yoyote ya masoko. Kila mara timu yetu inapoingia uwanjani katika michuano ya kimataifa, bendera ya nchi inapepea mbele ya mabilioni ya watazamaji, jambo ambalo ni tangazo la bure kwa utalii na fursa za uwekezaji nchini.
Thamani ya matangazo hayo (Global Exposure) ni kubwa mara dufu kuliko kiasi kilichotolewa, kwani inajenga taswira ya taifa lenye ushindani na linaloinukia kiuchumi.
Vilevile, uwekezaji huu unaongeza thamani ya wachezaji wetu katika soko la usajili. Wachezaji wanapofanya vizuri na kupata hamasa, wanavutia maskauti wa klabu kubwa duniani, jambo ambalo linamaanisha kuongezeka kwa fedha za kigeni zinazoingia nchini kupitia mikataba yao. Hali hii inapunguza mzigo wa serikali katika kutengeneza ajira rasmi, kwani sekta ya michezo inaanza kufyonza maelfu ya vijana wenye vipaji kuanzia ngazi ya vijiji hadi taifa.
Pia ni muhimu kutambua kuwa fedha hizi zinachochea hamasa kwa kizazi kijacho. Mtoto aliyepo kijijini akiona juhudi za wachezaji zinatambuliwa na Mkuu wa Nchi, anapata ari ya kufanya mazoezi kwa bidii ili na yeye aifikie hatua hiyo. Huu ni uwekezaji katika rasilimali watu unaolenga kutengeneza "Kiwanda cha Vipaji" ambacho miaka ijayo kitachangia kukuza mzunguko wa fedha kupitia mauzo ya vifaa vya michezo, huduma za tiba za wanamichezo, biashara za habari na uchambuzi.
Kwa kuhitimisha, wakati serikali ikiendelea na miradi ya kimkakati kama barabara, elimu, na afya kupitia bajeti yake kuu, kutenga kiasi hiki kwa ajili ya Taifa Stars ni sehemu ya mikakati ya kukuza sekta binafsi na kuliingiza taifa katika uchumi wa kisasa wa michezo. Hii si kuchezea fedha, bali ni kuweka mbegu itakayozalisha matunda ya kiuchumi, kidiplomasia, na kijamii kwa miaka mingi ijayo, huku ikiondoa dhana ya soka kuwa jambo la bahati nasibu na kulifanya kuwa biashara kamili na ajira ya kudumu.
TAHADHARI: ‘UTANDAWAZI NI CHUI’, TUJILINDE NA UTEKAJI WA AKILI NA FIKRA

Katika siku za hivi karibuni, kumekuwa na mjadala mzito kwenye mitandao ya kijamii nchini, ambapo baadhi ya watu wameonekana kushabikia vitendo vya mataifa makubwa, hususan Marekani, kuvamia mataifa mengine huru na kuwaondoa madarakani viongozi waliochaguliwa na wananchi wao.
Hali hii imeibua maswali mazito kuhusu uzalendo wa baadhi ya Watanzania na uelewa wao wa siasa za kimataifa (Geopolitics), huku ikionekana wazi kuwa uvamizi huo mara nyingi hulenga kulinda maslahi ya taifa mvamizi na si demokrasia kama inavyodaiwa.
Wachambuzi wa mambo wameonya kuwa, kutoa sapoti kwa mataifa makubwa yanapovunja sheria za kimataifa ni ishara ya "kutekwa kiakili." Katika muktadha huu, msanii na mshairi wa kisasa, Lwaga Mwambande, ameibuka na shairi lenye tahadhari nzito kwa jamii, akisisitiza kuwa utandawazi na teknolojia vimekuwa silaha mpya zinazotumiwa na "adui" kuteka fikra za watu bila wao wenyewe kujua.
Sanaa ya Mwambande na Utekaji wa Akili
Kupitia shairi lake maarufu la “Tunatekwa Hatujui”, Mwambande anatumia lugha ya picha kuonya jinsi ambavyo binadamu wa sasa anavyopoteza uwezo wa kufanya maamuzi huru. Anasema:
“Tunatekwa hatujui, tunategwa hatujui, tunashikwa hatujui, akili ituingie.”
Mshairi huyu anaufananisha utandawazi na "chui" mwenye makucha ya "buibui," akimaanisha kuwa ni mfumo uliotengenezwa kwa ufundi mkubwa wa kunasa akili za watu kupitia runinga, vishikwambi, na simu janja. Kwa mujibu wa Mwambande, wakati watu wakisherehekea picha, vichekesho, na michezo ya kubashiri (kubeti) kwenye mitandao, wanashindwa kutambua kuwa muda wao na uwezo wao wa kufikiri unateketezwa.
Jiopolitiki na Maslahi ya Mataifa Makubwa
Kushabikia uvamizi wa taifa huru kwa kisingizio cha kuleta mabadiliko ni kukosa uelewa wa historia. Wanataaluma wanabainisha kuwa uvamizi wa kijeshi na kuingilia siasa za mataifa mengine mara nyingi hufuatiwa na uporaji wa rasilimali na kudhoofisha uhuru wa kiuchumi.
Mwambande anatoa tahadhari kuwa "adui" huja kwa namna ambayo hatumtambui, tukijiona hatuugui wakati akili zetu zimeshazidiwa. Katika beti zake, anauliza:
“Kaenda huko adui, ajua hatutambui, twaona hatuugui, akili ituingie.”
Hii ni sawia na wale wanaoshangilia machafuko yanayopandikizwa na mataifa ya nje, wakidhani ni ukombozi, kumbe ni mtego wa kutawaliwa upya kiakili na kiuchumi.
Wito wa Uzalendo na Fikra Huru
Ili kukabiliana na changamoto hizi, makala za wanataaluma na mashairi ya Mwambande yanapendekeza kuimarisha elimu ya fikra huru. Ni lazima Watanzania wajifunze kulinda maslahi ya ndani na kuhifadhi tamaduni zao badala ya kuwa mashabiki wa kila kinachotoka nje, hata kama kina madhara kwa amani ya dunia.
Mwambande anahitimisha kwa uchungu akisema kuwa tunacheka na vichekesho visivyotatua shida zetu, na kusoma vitabu hatutaki, jambo linalotufanya tubaki tukiwa "hatukui."
Ni wazi kuwa, katika ulimwengu huu wa utandawazi, silaha kubwa ya kujilinda si bunduki pekee, bali ni "Akili." Kama taifa, tunapaswa kuwa macho na wale wanaotaka kutugawa na kutufanya tushabikie uharibifu wa mataifa mengine, kwani gharama ya kupoteza amani na uhuru ni kubwa, na mara nyingi huanza kwa kutekwa kwa akili.




.jpeg)
.jpeg)


























GG