Sunday, 4 January 2026

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMAPILI JANUARI 4,2025


 GG
Share:

Saturday, 3 January 2026

SHAMRASHAMRA ZA MWAKA MPYA 2026: AMANI YA TANZANIA YASHINDA CHOKOCHOKO NA MAANDAMANO

Watanzania wameuanza mwaka mpya wa 2026 kwa kishindo cha furaha na amani ya kipekee ikiwa ni kielelezo cha wazi kuwa taifa hili ni kisiwa cha utulivu kisichoweza kutikiswa na chokochoko za kisiasa wala shinikizo la maandamano yasiyo na tija kupitia mitandao. 

Katika kila kona ya nchi kuanzia fukwe za Coco Beach jijini Dar es Salaam hadi viwanja vya Mwanga Community Center mkoani Kigoma na Nyerere Square jijini Dodoma wananchi wameonekana kuburudika kwa tabasamu na upendo wakidhihirisha ushindi dhidi ya mipango ya vurugu iliyokuwa ikipigiwa upatu hapo awali na watanzania wanaoishi na kula bata ughaibuni kupitia machafuko nchini Tanzania. 

Hatua hii ya wananchi kudharau na kubeza shinikizo la maandamano imetoa ujumbe mzito kuwa watanzania wa leo wanathamini amani kuliko mizozo na wameamua kushirikiana na serikali yao kuhakikisha hali inabaki kuwa shwari ili waendelee kufurahia matunda ya uwekezaji na ukuaji wa uchumi wa nchi yao.

Serikali imedhamiria kwa dhati na inaendelea kutekeleza wajibu wake wa kimsingi wa kulinda usalama wa raia na mali zao huku wananchi nao wakitekeleza wajibu wao wa kizalendo kwa kukataa kujiingiza katika mitego ya chuki na ukatili wa kisiasa mitandaoni. 

Taswira iliyojitokeza katika fukwe za Coco Beach inadhihirisha mshikamano wa hali ya juu ambapo wakazi wa Dar es Salaam na viunga vyake walijumuika kwa wingi pasipo hofu yoyote wakithibitisha kuwa Tanzania salama inasonga mbele kwa kasi ya ajabu. Hali kadhalika mkoani Mwanza na Kagera wananchi wameupokea mwaka kwa umoja na nidhamu huku wakazi wa Geita wakionyesha kuwa sehemu ya amani ya Tanzania kwa kuukaribisha mwaka mpya kwa utulivu uliopitiliza jambo linaloongeza imani kwa wawekezaji na watalii kuwa nchi hii ni sehemu salama zaidi duniani.

Ni vyema ikaeleweka kuwa amani tunayoiona si jambo la bahati mbaya bali ni matokeo ya utawala bora na umakini wa viongozi katika kusimamia haki na maslahi ya wote jambo ambalo limejenga imani kubwa kwa wananchi. 

Pamoja na furaha hiyo bado kuna haja ya kuimarisha maeneo ya starehe kama fukwe za Coco Beach kwa kuongeza mazingira ya kisasa ikiwemo maeneo ya watoto na huduma za mtandao ili kukuza zaidi utamaduni huu wa amani na utulivu. Ni wajibu wa kila mmoja wetu kuendelea kuwa mlinzi wa amani ya mwenzake na kuepuka ukatili wa kisiasa mitandaoni ambao unalenga kupandikiza chuki kati ya vijana wasanii na makundi mbalimbali ya kijamii kwani umoja wetu ndiyo fahari ya kizazi cha sasa na urithi wa vizazi vijavyo.

Kusherehekea mwaka mpya kwa amani kumezima kabisa sauti za wachache waliotaka kurudisha nyuma maendeleo ya taifa kupitia machafuko na badala yake kumeleta matumaini mapya ya ustawi wa jamii katika mwaka mzima wa 2026. 

Kwa utulivu huu wananchi wametoa onyo kwa wale wote wanaoendelea kupandikiza mbegu ya chuki mtandaoni kuwa watanzania wameshashtuka na hawatakuwa tayari kufuata mkumbo wa kuvunja amani kwa kisingizio chochote. 

Hakika mwaka huu uwe ni wa upendo na mshikamano ambapo kila tone la furaha lililoonekana katika sherehe hizi liwe ni chachu ya kufanya kazi kwa bidii huku tukilinda amani yetu ambayo ni ngao ya usalama na dira ya kuelekea Tanzania yenye mafanikio makubwa zaidi kimataifa.

Share:

CHIKAMBO AKAGUA MIUNDOMBINU KOROFI MASONYA TARURA YATOA AHADI YA SULUHISHO LA HARAKA

Mbunge viti maalum Tunduru Sikudhani Yassin Chikambo akiwa na meneja wa TARURA Wilaya ya Tunduru Mhandisi Kweka wakiwa wanakagua kivuko cha Masonya chenye changamoto kubwa kwa wakazi wa maeneo hayo 

Na Regina Ndumbaro Tunduru-Ruvuma 

Mbunge wa viti maalumu kutoka Wilaya ya Tunduru, mheshimiwa Sikudhani Yassin Chikambo amefanya ziara ya kukagua miundombinu korofi katika kata ya Masonya akiwa ameongozana na meneja wa TARURA Wilaya ya Tunduru, Mhandisi Kweka. 

Ziara hiyo imelenga kujionea changamoto zinazowakabili wananchi, hususani katika kipindi hiki cha mvua zinazoendelea kunyesha mara kwa mara wilayani humo.

Katika ziara hiyo  Sikudhani Chikambo ametembelea kivuko cha Masonya ambacho kimekuwa kero kubwa kwa wakazi na wakulima wa kata hiyo. 

Kivuko hicho kimeripotiwa kusababisha madhara makubwa kwa wananchi, hasa wakati wa mvua nyingi, hali inayokwaza shughuli za kiuchumi na usafiri wa wakazi wa eneo hilo.

Aidha, pia Chikambo ametembelea kijiji cha Nakayaya Mashariki (Misufini) ambako kuna changamoto kubwa ya barabara inayokatiza katika bonde hatarishi. 

Bonde hilo limeendelea kupanuka kutokana na mvua za mara kwa mara, hali inayohatarisha usalama wa wananchi na kuathiri mawasiliano ya barabara katika eneo hilo.

Chikambo ameambatana na katibu wa siasa na uenezi wa CCM wilaya ya Tunduru, Komredi Yanini Stambuli, pamoja na diwani wa kata ya Masonya, Saidi Bwanali. 

Kwa upande wake, meneja wa TARURA, Mhandisi Kweka, amesema amejionea changamoto hizo na kusisitiza kuwa ofisi yake itaanza kuchukua hatua mara moja ili kuboresha miundombinu hiyo na kuchagiza maendeleo ya wananchi wanaoathirika moja kwa moja na hali ya barabara na vivuko hivyo.


Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMAMOSI JANUARI 3,2026

Magazeti ya leo



Share:

Friday, 2 January 2026

WANANCHI KIJIJI CHA LAJA WILAYANI KARATU WAISHUKURU TASAF UJENZI SEKONDARI MPYA


Na Said Mwishehe,Michuzi TV-Karatu

WANANCHI Kijiji cha Laja katika Halmashauri ya Wilaya ya Karatu mkoani Arusha wameishukuru TASAF kukubali Mradi wa kupunguza Umaskini (OPEC) kutekelezwa katika Kiji hicho na kutoa fedha kutekelezwa mradi wa ujenzi wa mpya ya Shule ya Sekondari ambao umesaidia wanafunzi kuondokana na changamoto ya kutembea umbali wa kilometa nane kuisaka elimu.

Wakizungumza wakati wa ziara ya Mkurugenzi Mtendaji wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii(TASAF) Shedrack Mziray aliyekuwa akikagua utekelezaji wa mradi huo,wananchi wa Kijiji hicho wamesema kupitia Mfuko huo wamepata shule hiyo ambayo imeondoa changangamoto wanafunzi waliokuwa wanachaguliwa kujiunga Sekondari kutembea umbali mrefu.

Mkazi wa Kijiji cha Laja Christina Lucas amesema wakati shule haijajengwa katika maeneo hayo wanafunzi walikuwa wanateseka haswa watoto wa kike ambao ndio kundi lililokuwa linaathirika kwasababu wanakutana na adha nyingi.

“Uwepo wa shule hii imepunguza utoro usio wa lazima kwasababu kwa vyovyote vile mtoto akitoka nyumbani kilometa nane njiani anakutana na changamoto nyingi ,mara nyingine wanasindikizwa na bodaboda ambao baadhi yao ni hatari kwa usalama wa wanafunzi Wetu.

“Baada ya kupata mradi huu na shule kujengwa hivi sasa watoto wanakaa katika mabweni hivyo wanakuwa salama na ndio maana mpaka sasa hakuna mwanafunzi ambaye amepata ujauzito kwani wazazi tunafuatilia sana ,watoto wako salama.

Kuhusu TASAF amesema wananchi wa Kijiji cha Laja wanaipongeza na kuishukuru lakini wanatoa ombi la kujengewa majengo ya maabara pamoja na kuongezwa nyumba za walimu kwani zilizopo hazitoshi.

“Tunatamani kama itawezekana basi Rais wetu Dk.Samia Suluhu Hassan kupitia TASAF atuone tena kwa kutujengea Maktaba,mabweni na nyumba za walimu.Pia namshukuru Rais wangu kwa kuliona hili kwani hii shule hatukutegemea ingejengwa katika maeneo haya.

“Rais wetu ni msikivu ameangalia mpaka huku kwetu ambako tulisahaulika lakini sasa ametujengea shule ya kifahari ambayo pengine ilitakiwa ijengwe hata Karatu ila kwa sasa iko kijijini kwetu.”

Kwa upande wake Andrea Mtupa amesema wanafunzi wanaofaulu kwenda kidato cha kwanza walikuwa wanatembea umbali wa kilometa nane kwenda na kilometa nane wakati wa kurudi kila siku lakini hivi sasa TASAF kupitia mradi wa OPEC wamejengewa shule ya Sekondari ya kisasa.

Awali Ofisa Mtendaji Kijiji cha Laja Daniel Mpigachai amesema mradi wa ujenzi wa shule hiyo umegharimu Sh.774,946,675, ambapo TASAF kupitia OPEC awamu ya Nne walitoa fedha Sh. 659,505,275 na fedha Sh.115,441,400 ni mchango wa jamii ambao umejumuisha mchanga,Kokoto ,mawe,maji na nguvu kazi wakati wa ujenzi.

Kuhusu manufaa ya mradi amesema shule hiyo iliyosajiliwa Novemba 2023 ilianza rasmi mwaka 2024 kwa kupokea wanafunzi 26 wa Kidato cha kwanza, kwa sasa shule ina Jumla ya wanafunzi 63 ambao ni kidato cha kwanza na cha pili na wote wanakaa Bweni.

“Uwepo wa mradi huu umeondoa tatizo la utoro shuleni, wanafunzi kuongeza morali ya kusoma tofauti na awali walipokuwa wanasoma shule ya kata iliyo na umbali wa Zaidi ya kilometa 8 kutoka kijini kwetu, shule imepokea pia watoto wanaotoka viji vya jirani.

Aidha amesema kwa niaba ya Wananchi wa Kijiji cha Laja wanatoa ombi kwa TASAF kama fursa nyingine itajitokeza wanaomba mradi wa ujenzi Majengo mengine yaliyosalia kama Maabara, Maktaba, Nyumba nyingine za walimu na Madarasa.

Wakati huo huo Mkuu wa Shule ya Sekondari Laja Daniel Panga amesema shule hiyo iliyojengwa kisasa mbali kuondoa changamoto wanafunzi kutembea umbali mrefu imeleta hamasa kwa wanafunzi wanaosoma elimu ya msingi wanaamini ipo siku watajiunga na shule hiyo.
Share:

Thursday, 1 January 2026

WAKAZI WA JIJI LA DODOMA WAKISHEREHEKEA MWAKA MPYA 2026 KATIKA ENEO LA NYERERE SQUARE DODOMA LEO



Na Dotto Kwilasa, Dodoma

Wakazi wa Jiji la Dodoma leo wamejitokeza kwa wingi katika eneo la Nyerere Square kusherehekea kuupokea Mwaka Mpya 2026, huku shamrashamra na furaha zikitawala anga la jiji hilo kuu la Serikali.

Shughuli mbalimbali za burudani, muziki, michezo ya watoto, pamoja na vionjo vya chakula na vinywaji zimetawala katika eneo hilo kuanzia majira ya asubuhi hadi jioni ambapo katika kusherehekea tukio hilo, maeneo ya kandokando ya Nyerere Square yalipambwa kwa taa za rangi jambo lililoashiria kuwa wananchi wanaishi kwa amani.

Jambo hilo limeongeza hamasa kwa wakazi na wageni waliotembelea jiji hilo kwa ajili ya sikukuu.

Baadhi ya wananchi waliozungumza na Malunde Blog wamesema kuwa kuuanza mwaka mpya katika eneo hilo limekuwa tukio la kipekee  kwani linatoa fursa ya kuunganisha jamii, kuimarisha undugu na kutoa matumaini ya safari mpya ya mafanikio.

Sherehe hizo zimeendelea kwa amani na utulivu, huku vyombo vya ulinzi na usalama vikiwa katika uangalizi kuhakikisha kila mkazi anasherehekea katika mazingira salama na rafiki.

Mwaka Mpya 2026 umeanza kwa matumaini mapya kwa wakazi wa Dodoma na Watanzania kwa ujumla, huku wengi wakitamani mwaka huo kuleta maendeleo, neema na mafanikio katika nyanja mbalimbali za maisha.





Share:

DC NKINDA ACHUKUA HATUA ZA HARAKA KUTATUA KERO YA BARABARA MHONGOLO NA NYASHIMBI, KAHAMA



Na Neema Nkumbi, Kahama

Mkuu wa Wilaya ya Kahama, Mhe. Frank Nkinda, amechukua hatua za haraka kutatua changamoto ya miundombinu ya barabara katika mitaa na kata mbalimbali za Manispaa ya Kahama, kufuatia kero zilizowasilishwa na vijana wakati wa sherehe za Krismasi walipokutana naye kwa chakula cha pamoja.

Leo Desemba 31, 2025, DC Nkinda ametembelea Mtaa wa Mhongolo ambapo amesema hatua hiyo ni utekelezaji wa maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, aliyoyatoa katika hotuba yake wakati wa uzinduzi wa Bunge la 13, akiwataka watumishi wa umma kuwahudumia wananchi kwa vitendo na kuwaletea tabasamu wale waliomwamini na kumpa ridhaa ya kuwaongoza.

Akizungumza na waandishi wa habari, Nkinda amesema Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Kahama imefanikiwa kutafuta mtambo wa kuchonga barabara (greda) ili kuanza kushughulikia kero za barabara zilizoharibika katika maeneo mengi kutokana na mvua, akisisitiza kuwa lengo ni kuhakikisha wananchi hawakwami katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku, hususan shughuli za kujipatia kipato.

“Ninatoa shukrani zangu kwa Mheshimiwa Rais, kwani Serikali imetutengea fedha kwa ajili ya kumaliza changamoto ya miundombinu ya barabara, Hata hivyo, Ofisi ya Mkuu wa wilaya Kahama imeona ichukue hatua za haraka wakati tukiendelea kusubiri fedha hizo kutufikia,” amesema Nkinda.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Mtaa wa Nyashimbi, Kata ya Mhongolo, Emanuel Lutonja, amemshukuru Rais Samia pamoja na DC Nkinda kwa hatua hiyo, akisema ujio wa greda katika mtaa wake umepunguza kwa kiasi kikubwa kero za barabara zilizokuwa na madimbwi makubwa yaliyowaathiri wafanyabiashara, hususan bodaboda, bajaji na wajasiriamali walioko pembezoni mwa barabara.

“Barabara hii ni kiunganishi kikuu kati ya Nyashimbi, Mhongolo hadi mjini, hivyo ukarabati wake utasaidia sana wananchi wa mtaa huu kufanya kazi zao bila wasiwasi,” amesema Lutonja.

Naye Mjumbe wa Serikali ya Mtaa wa Mhongolo, Renatus Thomas, amesema jitihada za DC Nkinda zinastahili pongezi, akibainisha kuwa bila uongozi wake barabara hiyo isingetengenezwa kwa wakati hivyo amemuomba DC kuendelea na zoezi hilo kwani barabara nyingi za Mhongolo bado ni mbovu na zina madimbwi makubwa.

Mkazi wa Nyashimbi Sokoni, Japhet Kitima, amesema awali wafanyabiashara walipata changamoto kubwa kuingiza mizigo kwa magari kutokana na ubovu wa barabara, hali iliyosababisha hasara hivyo wanamshukuru DC kwa kuwaletea greda kwani sasa hali imeanza kubadilika.

Kwa upande wake, Zainabu, mkazi wa Mhongolo na mfanyabiashara wa chakula, amesema mashimo na matope yaliyokuwapo barabarani yalikuwa yakisababisha usumbufu mkubwa hasa magari yalipopita, huku mkazi mwingine wa Nyashimbi, Sharifa Ramadhan, ameeleza kuwa maji yaliyotuama barabarani yalikuwa yakirukia madukani mwao na kutoa harufu mbaya, hali iliyosababisha hata bajaji za mizigo kukataa kufika eneo hilo.

Sambamba na ukarabati wa barabara, DC Nkinda amewataka viongozi wa mitaa ya Mhongolo na Nyashimbi kuhakikisha mitaro iliyoziba kwa mchanga inazibuliwa ili kuruhusu maji kupita vizuri, akibainisha kuwa kuziba kwa mitaro ndiko chanzo kikuu cha uharibifu wa barabara nyingi.

Katika ziara hiyo, DC Nkinda ametembelea barabara ya Mhongolo Senta kuelekea KACU pamoja na barabara ya Mhongolo kuelekea Nyashimbi Sokoni, akisisitiza kuwa Serikali itaendelea kushughulikia kero za wananchi kwa vitendo na kwa wakati.
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger