Thursday, 6 April 2023
SHEIKH WALID KAWAMBWA AIPONGEZA PUMA ENERGY TANZANIA KWA KUWAUNGANISHA WATANZANIA
WAZIRI JAFO ATAKA UHIFADHI WA MAZINGIRA MLIMA KILIMANJARO KUENDELEZWA
Na Dotto Kwilasa, DODOMA.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt.Selemani Jafo ametoa wito kwa Watanzania kuhifadhi na kuutunza Mlima Kilimanjaro ili uendelee kuinufaisha nchi.
Ametoa wito huo leo Aprili 04, 2023 Bungeni Dodoma wakati akijibu swali la Mbunge wa Same Mashariki Mhe. Anne Kilango Malecela aliyetaka kufahamu mkakati wa Serikali katika kukabiliana na matukio ya uchomaji moto Mlima Kiliamanjro.
Mhe. Jafo amesema kuwa Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais kwa kushirikiana na Wizara ya Maliasili na Utalii ina dhamira ya dhati katika kuhakikisha matukio hayo yanakoma.
Amesema pamoja na Serikali kuunda timu ya kufanya utafiti wa matukio ya moto wananchi wana wajibu wa kuacha vitendo vya ukataji miti na uchomaji moto eneo la hifadhi ya Mlima Kilimanjaro.
Awali akijibu swali la msingi la Mbunge wa Hai, Mhe. Saashisha Mafuwe, Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Khamis Hamza Khamis amesema Serikali kupitia Taasisi mbalimbali za ndani ya nchi zikiwemo Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Chuo Kikuu Cha Kilimo cha Sokoine, na Chuo Kikuu cha Nelson Mandela vinaendelea kufanya tafiti kuhusu suala hili.
Hata hivyo amebainisha kuwa baadhi ya sababu zilizobainishwa kuchangia hali hiyo ni pamoja na kuongezeka kwa wastani wa joto duniani, shughuli za binadamu zisizoendelevu,ukataji wa miti na uchomaji moto misitu.
“Napenda kuchukua fursa hii kuhimiza uongozi na wananchi wa Mkoa wa Kilimanjaro kuongeza jitihada za kutunza Mazingira ya Mlima huo kwa kudhibiti uchomaji moto ovyo na kuongeza jitihada za kuhifadhi na kupanda miti,” amesema.
Katika hatua nyingine, Naibu Waziri Khamis amesema Serikali inahakikisha Mradi wa Kuhimili Mabadiliko ya Tabianchi kwa Kutumia Mifumo Ikolojia Vijijini (EBARR) unaotekelezwa kwenye Wilaya ya Kaskazini A, Unguja na Mradi wa Kurejesha Ardhi iliyoharibika Kuongeza Usalama wa Chakula katika Maeneo kame nchini (LDFS) unaotekelezwa katika Wilaya ya Micheweni, Pemba inakamilika kwa wakati.
Hivyo, amesema tayari Serikali imechukua hatua za kiutendaji kwa kuwataka waratibu wa miradi kitaifa kuhakikisha miradi inakamilika kikamilifu na kwa ubora.
Aidha, naibu waziri amesema Ofisi ya Makamu wa Rais (SJMT) imeendelea kuwasilina na Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais (SMZ) ili Kusimamamia utekelezaji wa miradi hiyo kwa upande wa Zanzibar ili Miradi hii ikamilike kwa wakati.
Mhe. Khamis ameyasema hayo wakati akijibu swali la Mbunge wa Chaani Mhe. Hamad Juma Usonge aliyeuliza
Serikali ina mpango gani wa kukamilisha Miradi ya muda mrefu ya mazingira na mabadiliko ya tabianchi inayotekelezwa Zanzibar.
MCHANGO WA SEKTA YA MADINI KWENYE PATO LA TAIFA WAZIDI KUONGEZEKA
Na Mwandishi wetu,TABORA.
IMEELEZWA kuwa katika kipindi cha Serikali ya Awamu ya Sita mchango wa Sekta ya Madini umeendelea kukua hadi kufikia asilimia tisa.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti wachimbaji wadogo wanaojishughulisha na shughuli za uchimbaji wa madini ya dhahabu Wilayani Nzega mkoani Tabora kupitia mahojiano maalum wamesema kuwa mafanikio hayo yametokana na usimamizi mzuri wa Serikali kupitia Tume ya Madini wa Sekta ya Madini hali iliyopelekea kuongezeka kwa uzalishaji wa madini unaofanywa na wachimbaji wadogo kwa kutumia teknolojia za kisasa.
Akizungumza kwa niaba ya wachimbaji wadogo wa eneo hilo, Peter Mashiri, kutoka Kikundi cha Msilale kilichopo katika eneo hilo amesema kuwa kuongezeka kwa mapato yatokanayo na Sekta ya Madini kumetokana na matumizi ya teknolojia za kisasa na jitihada za Serikali za kuhakikisha makundi yote yanashiriki katika sekta hiyo.
Akizungumzia manufaa ya kikundi hicho kwa jamii inayouzunguka mgodi wake Mashiri amesema kuwa kikundi cha Msilale kimesaidia kutoa ajira kwa vijana wanaozunguka mgodi ambapo hadi sasa watu zaidi ya 48 wameajiriwa.
“Tunaipongeza Serikali kwa namna inavyowajali wachimbaji wadogo kwa kutoa leseni kwa makundi hayo ambayo imesaidia kuongeza wigo wa ajira kwa wananchi na kuongeza pato la mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla, tunaiomba Serikali iendelee kuwagawia maeneo ambayo bado yanamilikiwa na wachimbaji wakubwa bila kuendelezwa.
Kwa upande wa Katibu wa kikundi hicho, Magreth Emmanuel amewataka wanawake kujitokeza kwa wingi kushiriki katika Sekta ya Madini kwa kuwa Serikali imeweka mazingira wezeshi.
Ameongeza kuwa uwepo wa Sekta ya Madini umefungua fursa na hamasa kwa wanawake wengi ambao kwa sasa wameanza kujihusisha na shughuli za uchimbaji, uchenjuaji, na biashara ya madini sambamba na kutoa huduma kwenye migodi ya madini na kujipatia fedha kwa ajili ya kujikimu na kuhudumia familia zao.
Naye Msimamizi wa Mazingira wa kikundi hicho amesitiza kuwa mgodi huo umeendelea kuboresha mazingira yake kwa kuweka mitambo ya kisasa ambayo inawasaidia kuingia na kutoka ndani ya migodi, tofauti na awali ambapo walikuwa wanatumia kamba kushuka chini jambo ambalo lilikuwa ni hatari kwa usalama wao.
Picha : MATUKIO YANAYOENDELEA MSIBA WA MFANYABIASHARA MAARUFU MUSOMA FOOD..MAZISHI YANAFANYIKA LEO KAMBARAGE
BENKI YA CRDB YAFUTURISHA WATEJA NA WADAU NA KUTOA CHAKULA KWA WATOTO YATIMA TABORA….RC BATILDA APONGEZA HUDUMA YA AL BARAKAH BANKING



.jpeg)

.jpeg)











