
Serikali imefanikiwa kuzalisha ajira zaidi ya 1,400 za vijana na wanawake kwenda kufanya kazi nje ya nchi katika kipindi cha mwezi Novemba 2025 hadi sasa ikiwa ni matokeo ya mahusiano mazuri yaliyopo kati ya Tanzania na nchi za nje ili kusaidia kupunguza tatizo la ajira.
Akizungumza kwenye hafla ya kuwaaga vijana 109 waliopata fursa ya kazi katika nchi za ughaubini leo (08 Januari 2026) jijini Dar es Salaam, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira na Mahusiano Deus Sangu alisema mafanikio hayo ni utekelezaji wa maono ya Rais Samia Suluhu Hassan katika kukuza ajira.
"Tangu Novemba mwaka 2025 hadi Januari mwaka huu Serikali imefanikisha vijana 1,432 kwenda kufanya kazi nje ya nchi ikiwa ni matokeo ya jitihada za Rais Samia Suluhu Hassan kukuza mahusiano ya kidiplomasia na mataifa ya nje", alisema Waziri Sangu.
Sangu alitaja mafanikio mengine ya Serikali kuwa ni pamoja na upatikanaji wa fursa za ajira 8,000 nje ya nchi ifikapo mwisho wa mwaka huu ambapo tayari nafasi za ajira 500 za madereva pikipiki zimetangazwa kwa nchi ya Falme za Kiarabu (UAE) na mchakato wa usaili utakamilika mwezi Februari mwaka huu.
Alitaja fursa nyingine ya ajira 50,000 nchini Japan za kukuza ujuzi kwa vijana kwenye sekta ya ujenzi ambapo majadiliano yanaendelea na yatakapokamilika vijana kote nchini watatangaziwa kuomba.
Waziri Sangu aliwahakikishaia vijana hao 109 walioagwa leo kuwa Serikali imeratibu suala la mikataba yao, usalama wao na mazingira ya kazi wanapokwenda kupitia Mabalozi wanaowakilisha nchi hivyo amewataka waende wakafanye kazi kwa weledi, nidhamu na kudumisha mila za Kitanzania.
Akizungumza awali Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira na Mahusiano Zuhura Yunus alisema kwenda kufanya kazi nje ya nchi ni fursa nzuri ya ambapo tukio la leo kuwaaga vijana 109 ni uthibitisho wa lengo la Serikali kuzalisha ajira kwa makundi ya vijana na wanawake.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Umoja wa Mawakala wa Ajira Tanzania Bara (TRAA) Abdallah Khalid Mohamed alisema ushirikiano kati yao na Serikali umefanikisha kupatikana kwa fursa za ajira nje ya nchi na ndani kwa watanzania wengi.
Mohamed aliongeza kuwa TRAA ilianzishwa mwaka 2000 imekuwa mdau mkubwa wa Ofisi ya Waziri Mkuu katika jitihada za kutafuta fursa za ajira kwa watanzania pamoja na kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo kwa watu.
Vijana hao 1,432 hadi sasa wamenufaika kwenda katika nchi za Ujerumani, Canada, Falme za Kiarabu (UAE), Qatar, Saudia Arabia, Kuwait, na Oman ambapo wanafanya kazi katika fani za ufundi umeme, ujenzi, uuguzi,ufundi magari, udereva wa magari na pikipiki na kazi za majumbani.






























