Tuesday, 25 August 2026

NMB: ELIMU ,UJUZI NI NGUZO UCHUMI WA KIPATO CHA JUU





Na Oscar Assenga, TANGA

BENKI ya NMB imesema uwekezaji katika elimu, ujuzi wa vitendo na ubunifu unaowawezesha Watanzania kutafuta suluhisho la changamoto zinazoikabili nchi ni muhimu katika kufikia uchumi wa kipato cha juu.

Kauli hiyo ilitolewa na Kaimu Meneja Mwandamizi wa Maabara ya Ubunifu ya NMB, Maria Mwamyalla, alipokuwa akitoa salamu za wadhamini kwa niaba ya wadhamini wote katika maadhimisho ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu yaliyofanyika mkoani Tanga.

Mwamyalla alisema kaulimbiu ya mwaka huu, “Elimu, Ujuzi na Ubunifu: Njia ya Kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050,” inaendana na mkakati wa NMB wa kuwekeza katika teknolojia, ubunifu, vijana na ujumuishaji wa kifedha.

Alisema kupitia Agenda 2030, benki hiyo imeweka teknolojia, ubunifu, uwekezaji kwa vijana na ujumuishaji wa kifedha kuwa sehemu muhimu ya mkakati wake wa ukuaji.

“Mwelekeo huo unaendana moja kwa moja na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, inayolenga kujenga uchumi wa ushindani unaotumia maarifa, ujuzi na teknolojia,” alisema.

Alisisitiza kuwa teknolojia pekee haiwezi kuleta matokeo yanayotarajiwa bila kuwapo kwa watu wenye maarifa na ujuzi wa kuitumia ipasavyo.


NMB yawekeza Sh bilioni 2 kwa vijana

Mwamyalla alisema kupitia NMB Foundation, benki hiyo imeendelea kuwekeza katika elimu na malezi ya uongozi kwa vijana, hususan wanaotoka katika familia zenye uwezo mdogo kiuchumi.

Alisema kupitia programu ya Nuru Yangu Scholarship and Mentorship, NMB imewekeza zaidi ya Sh bilioni mbili tangu mwaka 2022, kwa ajili ya kuwafadhili wanafunzi 121 katika vyuo vikuu 11 nchini.

Kwa mujibu wa Mwamyalla, wanafunzi hao wamekuwa wakisaidiwa mahitaji mbalimbali yakiwamo ada, malazi na vitendea kazi kama kompyuta mpakato.

Alisema wanafunzi 21 tayari wameingia katika soko la ajira, huku wengine 42 wakitarajiwa kuhitimu mwaka huu.

“Tunatarajia kufungua dirisha la tatu la programu hii mwezi Septemba mwaka huu,” alisema.
Wabunifu wanufaika

Aidha, Mwamyalla alisema NMB inaendelea kutekeleza programu ya SEP kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Save the Children pamoja na Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA).

Alisema programu hiyo inalenga kukabiliana na changamoto ya ukosefu wa ajira kwa kuwapatia vijana elimu ya vitendo katika maeneo mbalimbali, ikiwamo mafunzo ya ufundi stadi yanayotolewa na vyuo vya VETA.

Katika eneo la teknolojia na ubunifu, alisema NMB imewekeza zaidi ya Sh bilioni 232, huku sehemu kubwa ya suluhisho za kiteknolojia zikitengenezwa na wataalamu wazawa.

Alisema uwekezaji huo unalenga kujenga utaalamu wa Watanzania, kuimarisha usalama wa mifumo pamoja na kupunguza muda wa kupeleka bidhaa za kidijitali sokoni.

Alitaja miongoni mwa suluhisho hizo kuwa ni huduma ya NMB Mkononi, inayowawezesha wateja kupata huduma mbalimbali za kibenki kupitia simu zao za mkononi, ikiwamo kutuma na kupokea malipo ya kielektroniki.

Kwa mujibu wa Mwamyalla, huduma hizo zimechangia kupanua upatikanaji wa huduma za kifedha kwa zaidi ya wateja milioni 10 wa NMB.

Alisema kupitia programu ya PesaTek, iliyoanzishwa mwaka 2022, benki hiyo imezindua Innovation Sandbox na kuendelea kuwawezesha vijana pamoja na wabunifu katika sekta ya teknolojia kupima na kuendeleza suluhisho zao.

Mwamyalla alisema NMB itaendelea kushirikiana na Serikali na taasisi za elimu kuhakikisha elimu, ujuzi na ubunifu vinageuzwa kuwa suluhisho zinazochochea biashara na kuchangia maendeleo ya Taifa.

Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMANNE AGOSTI 25,2026





Magazeti



Share:

Monday, 24 August 2026

SERIKALI YAWEKA MAZINGIRA WEZESHI, WANAWAKE KUTUMIA TEKNOLOJIA NA FURSA ZA BIASHARA KUKUZA UCHUMI




Na Jackline Minja – WMJJWM, Arusha

Serikali imeendelea kuweka mazingira wezeshi kupitia programu mbalimbali za uwezeshaji wanawake kiuchumi, ikiwemo kuwawezesha kupata mitaji na mikopo kwa ajili ya kuanzisha na kuendeleza shughuli za kiuchumi.

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi, wakati akifungua Kongamano la Usimamizi wa Biashara na Uchumi lililoandaliwa na Wanawake Laki Moja, jijini Arusha, akisisitiza umuhimu wa wanawake kuwa na ujuzi wa kusimamia biashara zao ili ziweze kukua na kuwa endelevu.

Naibu Waziri Mahundi amewataka wanawake wajasiriamali kuwa na nidhamu na uwajibikaji kwa kutumia fursa zinazopatikana, ambapo amefafanua kwamba, uwezeshaji wa kiuchumi haupaswi kuishia katika upatikanaji wa mitaji pekee, bali unapaswa kuambatana na maarifa ya usimamizi wa fedha, utunzaji wa kumbukumbu, mipango ya biashara, masoko na matumizi ya teknolojia.

“Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, inaendelea kuweka mazingira wezeshi kwa wanawake kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi na kunufaika na fursa zinazotokana na ukuaji wa uchumi ,kupitia programu mbalimbali za uwezeshaji. Kwa mfano, kupitia utaratibu wa mikopo ya asilimia 10 ya mapato ya ndani ya Halmashauri, asilimia 4 hutengwa kwa wanawake, ili kuwawezesha kuanzisha na kuendeleza shughuli za kiuchumi,” alisemaNaibu Waziri Mahundi.

Aidha Naibu Waziri Mahundi amewataka wanawake kutumia teknolojia za kidijitali kutangaza bidhaa, kuwasiliana na wateja, kufanya malipo na kutafuta masoko mapya, huku akisisitiza kuwa mwanamke wa Tanzania anapaswa kuwa si mtumiaji wa teknolojia pekee, bali pia mbunifu, mzalishaji na mshiriki katika uchumi wa kidijitali.

Kwa upande wake, Mlezi na Kaimu Mtendaji Mkuu wa Mtandao wa Wanawake Laki Moja Tanzania, Tano Mwera, amesema kuanzishwa kwa mtandao huo kuna lengo madhubuti la kuwawezesha wanawake kupata ujuzi na elimu mbalimbali zitakazowasaidia katika shughuli zao za kiuchumi.

Tano amesema mtandao huo unalenga zaidi kuwajengea wanawake uwezo katika masuala ya biashara, kuwaongezea uelewa wa namna ya kuendesha shughuli zao kwa ufanisi na kuwawezesha kujenga uchumi imara ambao utasaidia kulinda na kuimarisha familia zao.

Kongamano hilo la Usimamizi wa Biashara na Uchumi limefanyika jijini Arusha na kuwakutanisha wanawake kutoka maeneo mbalimbali nchini pamoja na wadau wa maendeleo ya biashara na uchumi.


Share:

MICHEZO KWA WATUMISHI WA HALMASHAURI ITUMIKE KUIMARISHA AFYA, MSHIKAMANO, TIJA KIUTENDAJI - PRO. SHEMDOE

Na: OWM – TAMISEMI, Mbeya

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, amezitaka Halmashauri zote nchini kutumia michezo kama nyenzo ya kuimarisha afya, ustawi, mshikamano na tija kwa watumishi, ili kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi. 

Prof. Shemdoe ametoa wito huo Agosti 23, 2026 jijini Mbeya wakati akifungua rasmi Mashindano ya Michezo ya Watumishi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa Tanzania (SHIMISEMITA), kwa niaba ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba.

Akizungumza katika ufunguzi huo, Prof. Shemdoe amemshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuyarejesha tena mashindano ya SHIMISEMITA mwaka 2023 baada ya  kusitishwa, akitambua kwamba michezo ni sehemu muhimu ya kujenga afya ya mwili na akili, kuimarisha mahusiano kazini na kukuza ushirikiano miongoni mwa watumishi kutoka Halmashauri mbalimbali nchini.

 “Leo hii mmekutana watumishi zaidi ya 5,000 kutoka katika Halmashauri 177. Kila mmoja anao wajibu wa kujenga mahusiano mazuri na watumishi wa Halmashauri nyingine, kwani michezo ni afya, michezo ni kiunganishi. Hivyo, tumieni fursa hii kujenga afya zenu na kuimarisha ushirikiano miongoni mwenu,” amesema.

Aidha, Prof. Shemdoe amewataka Wakurugenzi wa Halmashauri kuhakikisha ushiriki wa michezo unawahusisha watumishi kutoka maeneo mbalimbali, badala ya watumishi wa Makao Makuu pekee. Amesema watumishi kutoka ngazi za kata, vijiji na vitongoji wanapaswa kupewa fursa ya kushiriki, kwa kuwa michezo itawajengea ari na morali ya kutekeleza majukumu yao, ikiwemo ukusanyaji wa mapato, ikizingatiwa kuwa mtumishi mwenye afya njema ya mwili na akili atatekeleza majukumu yake kwa ufanisi na kutoa huduma bora kwa wananchi.

Sanjari na hilo, Prof. Shemdoe amezitaka Halmashauri kuwaandaa na kuwajengea uwezo wananchi kutumia fursa zitakazotokana na Mashindano ya Soka kwa Timu za Taifa Barani Afrika (AFCON 2027). Amesema mashindano hayo si suala la michezo pekee, bali yatatoa fursa za kiuchumi, kijamii, kiutamaduni na hususan katika sekta ya utalii, ambayo ni miongoni mwa sekta muhimu katika kuiingizia Tanzania fedha za kigeni.

Kutokana na umuhimu wa michezo kwa afya na utendaji wa watumishi wa umma, Prof. Shemdoe amezitaka Halmashauri zote nchini kuhakikisha michezo ya SHIMISEMITA inawekewa kifungu katika bajeti zao na kutengewa fedha ili kuwawezesha watumishi kushiriki kikamilifu. Amesema uwekezaji katika michezo ni uwekezaji katika afya ya mwili na akili za watumishi, jambo litakalosaidia kuongeza morali, ufanisi na tija katika utekelezaji wa majukumu ya Serikali na utoaji wa huduma kwa wananchi.


Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Mhe. Beno Malisa, amemshukuru Prof. Shemdoe kwa Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI kuyaleta mashindano ya SHIMISEMITA mkoani Mbeya, na kuahidi kuwa uongozi wa mkoa umejipanga kuhakikisha usalama na ustawi wa wanamichezo wote wakati wa mashindano hayo. Aidha, Mhe. Malisa amemshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuridhia mashindano ya SHIMISEMITA kuendelea kufanyika nchini.

Naye, Katibu Mkuu wa SHIMISEMITA, Bw. Henry Kapella, ameiomba Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, ikiwa mlezi wa SHIMISEMITA, kuendelea kuzihimiza Halmashauri kutenga bajeti kwa ajili ya kuwawezesha watumishi kushiriki mashindano hayo kila mwaka. Ameshauri pia TAMISEMI kuweka kigezo cha uwepo wa fedha zilizotengwa kwa ajili ya michezo ya SHIMISEMITA katika mchakato wa kupitisha bajeti za Halmashauri, ili kuhakikisha watumishi wanapata fursa endelevu ya kushiriki michezo.

Mashindano ya SHIMISEMITA mwaka huu yamebeba kaulimbiu “Tuko Tayari kwa AFCON 2027,” ikiwa ni ujumbe unaosisitiza utayari wa Tanzania kutumia fursa za michezo, kuimarisha afya na mshikamano wa watumishi, pamoja na kunufaika na fursa za kiuchumi, kijamii, kiutamaduni na kiutalii zitakazotokana na AFCON 2027.
Share:

MTUMIE MICHEZO KUIMARISHA UCHUMI NA UMOJA: MWENYEKITI UVCCM KISHAPU

Mwenyekiti wa UVCCM Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga Jenipha Nangi akikabidhi zawadi kwa mshindi wa kwanza wa mashindano ya Nkwembele Cup Pemba Fc ya kijiji cha Mangu Kata ya Shagihilu Agosti 23, 2026 kabumbu lililosakatwa katiaka viwanja vya Shule ya msingi Mwanulu iliyoichapa Madrid Fc bao 1-0

Mwenyekiti wa UVCCM Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga Jenipha Nangi akizungumza alipokuwa mgeni rasmi wa kufunga ligi ya Nkwembele Cup ya Kijiji cha Mwanulu Agosti 23,3036 katika viwanja vya shule ya Msingi Mwanulu


Na Sumai Salum-Kishapu

Mwenyekiti wa UVCCM Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga Jenipha Nangi, amewataka vijana kutumia michezo kama fursa ya kuibua vipaji, kujenga nidhamu, kuimarisha umoja na kujitengenezea fursa za kiuchumi.


Jenipha ameyasema hayo wakati akifungua rasmi mashindano ya Nkwembele Cup 2026 kwenye Uwanja wa Shule ya Msingi Mwanulu yaliyoshirikisha timu 32 kutoka Kata mbalimbali za Wilaya hiyo, amesema michezo si burudani pekee, bali ni sehemu muhimu ya kuwaandaa vijana katika maisha, huku akiwataka kutumia vipaji vyao kwa manufaa yao binafsi na maendeleo ya jamii.


“Michezo si burudani tu, ni njia ya kujenga umoja, nidhamu na kuandaa viongozi wa kesho. Nikupongeze Mzee Robert Matius kwa uandaaji wa ligi hii kwani umeendelea kuunga mkono juhudi za Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuinua sekta ya michezo na kuwafungulia vijana fursa za maendeleo na ajira kupitia vipaji vyao, pia jukwaa linawawezesha vijana kushiriki katika shughuli zenye tija".
Wachezaji wa timu ya Pemba Fc ya Kijiji cha Mangu Kata ya Shagihilu wilayani Kishapu mkoani Shinyanga wakiwa kwenye picha ya pamoja na mgeni rasmi ya kufunga mashindano hayo Mwenyekiti wa UVCCM wilayani humo Jenipha Nangi Agosti 23,2026 katika viwanja vya michezo shule ya msingi Mwanulu


Pemba FC ya Kijiji cha Mangu, Kata ya Shagihilu, imeibuka bingwa baada ya kuifunga Madrid FC ya Mwanulu Kata ya Mwataga bao 1-0 bao pekee la ushindi lilifungwa na mshambuliaji Nado, mwenye jezi namba 7, katika dakika ya tatu ya kipindi cha kwanza cha mchezo.


Kwa ushindi huo, Pemba FC imejinyakulia Kombe la Nkwembele Cup, pamoja na Shilingi milioni moja, huku Madrid FC ikiwa mshidni wa pili na kupewa Shilingi laki tano.



Mashindano hayo ya Nkwembele Cup yamehusisha jumla ya timu 32 kutoka kata mbalimbali za Wilaya ya Kishapu, yakilenga kuibua vipaji vya vijana na kuimarisha mshikamano kupitia michezo.

Wachezaji wa timu ya Madrid Fc ya Kijiji cha Mwanulu Kata ya Mwataga wilayani Kishapu mkoani Shinyanga wakiwa kwenye picha ya pamoja na mgeni rasmi ya kufunga mashindano hayo Mwenyekiti wa UVCCM wilayani humo Jenipha Nangi Agosti 23, 2026 katika viwanja vya shule ya msingi Mwanulu

Kiungo namba saba Ramadhan Ally "Nado" wa timu ya Pemba Fc ya Mangu aliyewachapa Madrid Fc bao 1 dakika ya 3 ya kipindi cha kwanza

Mwandaaji wa ligi ya Nkwembele Cup Robert Matius







































































































































Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger