Sunday, 20 September 2026

DKT HUSSEIN MWINYI AMTEUA TENA OTHMAN MASOUD OTHMAN


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk Hussein Mwinyi, amemteua tena rasmi Othman Masoud Othman kuwa Makamu wa Kwanza wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, hatua inayofungua ukurasa mpya katika kukamilisha muundo wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK).

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Ikulu, uteuzi huo umeanza kutekelezwa mara moja huku Othman akitarajiwa kuapishwa rasmi katika hafla itakayofanyika Ikulu Zanzibar.

Hatua hii inafuatia mchakato wa ndani wa chama cha ACT Wazalendo kumteua kiongozi huyo ambaye pia ni Mwenyekiti wa chama hicho, kufuatia makubaliano ya ushirikiano yaliyosainiwa kati ya CCM na ACT Wazalendo mnamo mwezi Julai mwaka huu kwa lengo la kuimarisha siasa za maridhiano visiwani humo.

Uteuzi huu unakamilisha mfululizo wa hatua muhimu zilizochukuliwa na Dk Mwinyi, zikiwemo uteuzi wa Nassor Ahmed Mazrui na Omar Said Shaaban kuwa wajumbe wa Baraza la Wawakilishi kupitia nafasi za uteuzi wa rais, ambao tayari wameshaapishwa na kuanza majukumu yao.

Baada ya kuapishwa kwa Makamu huyo wa Kwanza wa Rais, mamlaka zinatazamiwa kukamilisha uteuzi wa baraza jipya la mawaziri ili kujaza nafasi nne zilizo wazi ikiwemo Wizara ya Afya, Wizara ya Utalii na Mambo ya Kale, Wizara ya Biashara na Maendeleo ya Viwanda, pamoja na Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais, hatua ambayo imepongezwa na viongozi mbalimbali wa vyama vya siasa nchini wakisema italeta mshikamano mkubwa na kuleta tija ya kimaendeleo kwa Wazanzibari wote.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMAPILI SEPTEMBA 20,2026


Magazeti

Share:

Saturday, 19 September 2026

LINDI YAFUNGUA MILANGO KWA WAWEKEZAJI WA MADINI MBUNGE MMUYA




Na Sheila Ahmadi, Ruangwa


Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ambaye pia ni Mbunge wa jimbo la Ruangwa, Kasper Mmuya, amesema Mkoa wa Lindi una fursa kubwa za madini ambazo zinahitaji kufanyiwa utafiti na kutangazwa zaidi ili kuvutia wawekezaji na kuongeza mchango wa sekta hiyo katika uchumi wa mkoa na Taifa.

Mmuya amesema hayo wakati akizungumza katika Maonyesho ya Madini ya Mkoa wa Lindi yanayofanyika Wilaya ya Ruangwa, akieleza kuwa maonyesho hayo yamekuwa jukwaa muhimu la kuibua na kutangaza fursa za madini zilizopo mkoani humo.

maonyesho hayo ya siku nne yamehusisha shughuli mbalimbali, ikiwemo ufunguzi, ziara za mabanda, mafunzo kwa wananchi na wadau wa sekta ya madini pamoja na siku ya kilele na kufungwa kwa maonyesho.

Aidha Mmuya amesema wazo la kuanzisha maonyesho hayo lililenga kuonyesha na kutangaza fursa za madini zinazopatikana Lindi ndani ya mkoa, nje ya mkoa na hata nje ya Tanzania.

" juhudi hizo zimeanza kuonyesha matokeo kutokana na kuongezeka kwa wadau wa sekta ya madini wanaofika mkoani humo na kuanza kufanya shughuli mbalimbali" Amesema Mbunge Mmuya

Vilevile Lengo lake lilikuwa ni kuonyesha fursa za madini zinazopatikana katika Mkoa wa Lindi na kuzitangaza ndani ya mkoa, nje ya mkoa na hata nje ya nchi yetu,” amesema Mmuya.

Katika hatua nyingine Lindi haipaswi kutegemea kilimo, uvuvi na ufugaji pekee katika kukuza uchumi wake, bali inapaswa kutumia kikamilifu fursa zinazopatikana katika sekta ya madini.


Hata hivyo mafunzo yaliyotolewa katika maonyesho hayo yamekuwa muhimu kwa wananchi, wachimbaji wadogo na wakubwa pamoja na wawekezaji, kwa kuwa yameeleza namna teknolojia inavyoweza kutumika katika uchimbaji, uchakataji na uongezaji thamani wa madini.

Naye Naibu Waziri wa Madini, Steven Kiruswa, ameongeza kuwa Serikali imeanza kuchukua hatua dhidi ya wamiliki wa maeneo ya utafiti wa madini ambao hawayaendelezi.

Kiruswa amesema katika Mkoa wa Lindi pekee, Serikali ilifuta leseni 98 mwaka uliopita na imefuta nyingine 100 mwaka huu, hatua inayolenga kuachilia maeneo ambayo hayajaendelezwa ili kutoa nafasi kwa wachimbaji na wawekezaji wenye nia ya dhati.

Vilevile Serikali sasa inachambua maeneo hayo ili kubaini kiwango cha utafiti kilichofanyika, huku maeneo ambayo hayajafanyiwa utafiti yakitarajiwa kuingizwa katika mpango wa utafiti wa Serikali.


Share:

STAMICO YACHUKUA TAHADHARI YA MVUA ZA EL NIÑO


NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

SHIRIKA la Madini la Taifa (STAMICO) limeanza kuchukua tahadhari kukabiliana na athari zinazoweza kusababishwa na mvua za El Niño, baada ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) kueleza kuwa mvua hizo zinatarajiwa kuimarika katika maeneo mbalimbali nchini kuanzia wiki ya nne ya Septemba hadi Oktoba mwaka huu.

Hayo yameelezwa wakati Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dkt. Ladislaus Chan’ga aliipokutana na menejimenti, wafanyakazi na wataalamu wa Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), kwa ajili ya kutoa elimu kuhusu hali ya El Niño na namna ya kutumia taarifa za hali ya hewa katika kupanga shughuli zao.

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO, Deusdedith Magara, amesema shirika hilo limechukua tahadhari kubwa kutokana na ukweli kwamba shughuli zake nyingi za uchimbaji, utafiti na uchenjuaji wa madini hufanyika katika maeneo ya porini ambayo yanaweza kuathiriwa na mvua kubwa.

Amesema mvua nyingi zinaweza kusababisha usumbufu katika shughuli za uchimbaji na shughuli nyingine zinazohusiana na madini, hali ambayo inaweza kuathiri uzalishaji na mapato ya STAMICO.

“Madini yanachimbwa porini, hayachimbwi mjini. Kwa hiyo watu wetu wametawanyika huko. Mvua ikinyesha sana sisi hatuwezi kuendelea na kazi kwa sababu kazi yetu ni kuchimba madini, kufanya utafiti wa madini na kuchenjua madini, na vyote hivyo mvua inaviathiri sana,” amesema.

Amesema mapato makubwa ya shirika yanatokana na shughuli zinazofanyika katika maeneo hayo, hivyo kuvurugika kwa operesheni kutokana na mvua kunaweza kuathiri pia mapato ya STAMICO.

Ameongeza kuwa STAMICO itaendelea kuwaelimisha watumishi wake waliotawanyika katika maeneo mbalimbali nchini na kuhakikisha wanafuatilia taarifa na maelekezo yatakayotolewa na TMA.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dkt. Chan’ga, amesema hali ya El Niño ipo na kwamba mamlaka hiyo inatarajia mvua kuanza kuimarika katika maeneo mbalimbali ya Tanzania katika kipindi cha mwisho wa Septemba na mwanzoni mwa Oktoba.

Amesema kuanzia wiki ya nne ya Septemba na wiki ya kwanza ya Oktoba, mvua zinatarajiwa kuanza kuimarika katika ukanda wa Ziwa Victoria, hususan mikoa ya Geita, Kagera, Mwanza, Shinyanga, Simiyu na Mara.

Dkt. Chan’ga amesema wiki ya kwanza na ya pili ya Oktoba mvua hizo zinatarajiwa kuanza katika Nyanda za Juu Kaskazini Mashariki, zinazojumuisha mikoa ya Arusha, Kilimanjaro na Manyara.

Amesema pia maeneo ya Pwani ya Kaskazini, yakiwamo Tanga, Dar es Salaam, kaskazini mwa Morogoro, Pwani, Mafia pamoja na visiwa vya Unguja na Pemba, yanatarajiwa kuanza kupata mvua katika wiki ya kwanza na ya pili ya Oktoba.

Kwa mujibu wa Dkt. Chan’ga, katika maeneo hayo mvua zinatarajiwa kuwa juu ya wastani hadi wastani.

Hata hivyo, amesema wananchi na taasisi mbalimbali wanapaswa kuendelea na shughuli zao za kawaida huku wakizingatia taarifa za hali ya hewa zinazotolewa na TMA.

Amesema TMA itaendelea kutoa utabiri wa msimu pamoja na taarifa za utabiri wa siku 10, siku tano na taarifa za kila siku ili kuwawezesha wadau kupanga na kutekeleza shughuli zao za kiuchumi na kijamii kwa kuzingatia mwenendo wa hali ya hewa.

“Wananchi waendelee na shughuli zao za kiuchumi na kijamii, lakini tuendelee kufuatilia ipasavyo taarifa za hali ya hewa zinazotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania,” amesema.

Dkt. Chan’ga pia amewataka wananchi kuzingatia maelekezo ya viongozi wa Serikali pamoja na ushauri wa wataalamu wa sekta mbalimbali ili kuimarisha mipango na maandalizi ya kukabiliana na athari zinazoweza kujitokeza kutokana na mwenendo wa hali ya hewa.

Amesema ushirikiano kati ya TMA na taasisi kama STAMICO ni muhimu katika kuhakikisha taarifa za hali ya hewa zinatumika ipasavyo katika kupanga na kutekeleza shughuli za uzalishaji.

Kwa upande wa STAMICO, Magara amesema elimu iliyotolewa na TMA imewasaidia watumishi kuelewa zaidi hali inayotarajiwa na namna ya kuendelea na shughuli zao huku wakizingatia tahadhari.

Amesema shirika litaendelea kufuatilia taarifa za TMA na kuchukua hatua kulingana na ushauri wa wataalamu ili kupunguza athari zinazoweza kujitokeza katika shughuli zake za uchimbaji, utafiti na uchenjuaji wa madini.

Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO IJUMAA SEPTEMBA 19,2026




Magazeti




Share:

Friday, 18 September 2026

MAKAMU WA RAIS AZURU DAMPO LA PUGU KINYAMWEZI


-Atoa siku saba Kupatikana kwa Suluhisho la Mgogoro wa Udhibiti wa Taka

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Deogratius John Ndejembi, amefanya ziara katika Dampo la Pugu Kinyamwezi jijini Dar es Salaam, ambapo amekagua hali ya udhibiti na usimamizi wa taka. 

Katika ziara hiyo, ameambatana na viongozi wa Halmashauri za Jiji la Dar es Salaam, viongozi wa Ofisi yake, Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Dkt. Immaculate Sware Semesi, pamoja na baadhi ya watumishi wa taasisi hiyo.

Mhe. Ndejembi amewaagiza viongozi wa Halmashauri za Jiji la Dar es Salaam, Wizara na taasisi husika kukutana na kujadili kwa kina njia bora na endelevu za kudhibiti taka katika dampo hilo. 

Amesisitiza umuhimu wa ushirikiano wa karibu miongoni mwa wadau hao ili kupata ufumbuzi wa kudumu wa changamoto zinazolikabili eneo hilo.

Katika kutekeleza maagizo hayo, ameelekeza viongozi hao kufikia makubaliano kuhusu njia bora za udhibiti wa taka na kuwasilisha kwake ripoti yenye mapendekezo ndani ya siku saba. 

Aidha, ameagiza kupuliziwa dawa maalum dhidi ya vimelea vya magonjwa katika maeneo yanayolizunguka dampo, hususan makazi ya wananchi walio jirani, ili kupunguza hatari ya kuenea kwa magonjwa yanayoweza kusababishwa na taka.

Sambamba na hilo, Makamu wa Rais amewataka viongozi na taasisi zinazohusika kushirikiana katika ukusanyaji na uwasilishaji wa takwimu sahihi za taka, ili taarifa zinazotolewa ziwe na uhalisia na kuendana. 

Amesema takwimu hizo ni muhimu kwa Serikali katika kupanga na kuchukua hatua stahiki za kukabiliana na changamoto za taka, kulinda afya za wananchi na kuhifadhi mazingira.
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger