Monday, 6 July 2026

RAIS MWINYI ATOA MILIONI 200 KUSAIDIA KITUO CHA IRSHAAD LUSHOTO, ARIDHIA OMBI LA PROF. SHEMDOE



Na OWM - TAMISEMI, Lushoto

Mhe. Alhaji Dkt. Hussein Mwinyi, Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar,  amekubali ombi la Mbunge wa Jimbo la Lushoto Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kwa kutoa mchango wa Shilingi Milioni 200 kwa ajili ya kuendeleza Kituo cha Elimu ya Kiislamu Irshaad (Irshaad Islamic Centre) kilichopo Lushoto, mkoani Tanga.

Fedha hizo zinatarajiwa kuwezesha utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo katika kituo hicho, ikiwemo kuboresha Chuo cha Ufundi, kuanzisha bustani ya kisasa, kujenga madrasa yenye kukidhi mahitaji ya wanafunzi, kujenga nyumba za walimu, jengo la kupokelea wageni, hospitali pamoja na ukumbi wa kisasa wa kufanyia shughuli mbalimbali za kielimu na kijamii.

Prof. Shemdoe alitoa ombi hilo Julai 5, 2026 wakati wa Sherehe ya Maulidi ya Kumswalia Mtume Muhammad S.A.W iliyoandaliwa na Sheikh Sharrif Hussein Ahmad Badawiyy wa Kituo cha Irshaad Islamic Centre Lushoto, ambapo Mgeni Rasmi alikuwa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi.

Katika hatua nyingine, Mhe. Rais Dkt. Hussein Mwinyi amekubali ombi la Rais wa Kituo cha Irshaad Islamic Centre Lushoto Sheikh Sharrif Hussein Ahmad Badawiyy la kumwomba awe mlezi wa kituo hicho, ambapo Mhe. Dkt. Dkt. Hussein Mwinyi ameahidi kuendelea kushirikiana na viongozi pamoja na wadau mbalimbali katika kukiendeleza ili kiwe kitovu cha utoaji wa elimu bora na maadili mema.

Sanjari na hilo, Mhe. Rais Dkt.  Mwinyi ameridhia pia ombi la Rais wa Kituo hicho cha Irshaad Islamic Centre la kumtaka kuridhia jina la Hayati Alhaji Ali Hassan Mwinyi, litumike katika eneo la bustani linalotarajiwa kujengwa katika Chuo cha Ufundi kilichopo ndani ya kituo hicho, ikiwa ni sehemu ya kumuenzi na kutambua mchango wa maendeleo alioutoa Hayati Alhaji Ali Hassan Mwinyi akiwa ni mlezi wa kituo hicho. 

Mhe. Prof. Shemdoe alimuunga mkono Mhe. Rais Dkt. Hussein Mwinyi kwa kuchangia Shilingi Milioni 20, Mkuu wa Mkoa wa Tanga Dkt. Batilda Burian  Milioni 5, Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Adam Malima Milioni 5, Mbunge wa Bumbuli Mhe. Mhandisi Ramadhani Hamza Milioni 5, Mwenyekiti wa CCM Mkoa Bw. Rajab Abdallah Milioni 3 na Mbunge wa Afrika Mashariki Mhe. Dkt. Abdullah Makame amechanga Milioni 5 na kufanya jumla ya fedha zilichangwa kuwa Milioni 248, hatua iliyoonyesha mshikamano wa viongozi hao katika kuunga mkono maendeleo ya elimu na ustawi wa jamii. 

Akizungumza mara baada ya hafla hiyo, Mhe. Prof. Shemdoe amemshukuru Mhe. Rais Dkt. Mwinyi kwa kukubali ombi hilo, akieleza kuwa msaada huo utakuwa chachu ya kuinua viwango vya elimu, ustawi wa jamii na huduma zinazotolewa katika kituo hicho, ambacho kimeendelea kuwa nguzo muhimu ya malezi na elimu kwa vijana wa Lushoto na maeneo jirani.

Aidha, Wananchi na viongozi waliohudhuria hafla hiyo wamempongeza Mhe. Rais Dkt. Mwinyi kwa kukubali maombi yaliyowasilishwa na Mhe. Prof. Shemdoe, wakieleza kuwa uamuzi huo utaacha alama ya kudumu katika maendeleo ya Kituo cha Elimu ya Kiislamu Irshad Lushoto na kuongeza fursa za elimu, ujuzi na huduma za kijamii kwa vizazi vya sasa na vijavyo.












Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMATATU JULAI 6,2026

Magazeti


 




Share:

Sunday, 5 July 2026

DKT. MUNISI: TAASISI ZA DINI NI WADAU MUHIMU KATIKA MAENDELEO YA TAIFA


Na: OWM (KAM)– Muleba, Kagera

Serikali imesema itaendelea kushirikiana na taasisi za dini katika kuimarisha utoaji wa huduma za kijamii na kujenga jamii yenye maadili, amani na mshikamano huku ikizipongeza kwa mchango wake mkubwa katika kukuza maendeleo ya Taifa.

Kauli hiyo imetolewa leo 4 Julai, 2026 na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Dkt. Eveline Wilbard Munisi alipomwakilisha Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, katika Harambee ya Ujenzi wa Kanisa la KKKT Usharika wa Ndolage Wilaya ya Muleba mkoani Kagera.

Akizungumza katika hafla hiyo Dkt. Munisi amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea kuthamini mchango wa taasisi za dini katika kujenga jamii yenye maadili, mshikamano na maendeleo endelevu Alisema ushirikiano kati ya Serikali na taasisi za dini ni msingi muhimu wa kuimarisha huduma kwa wananchi na kudumisha amani nchini.

Dkt. Munisi amewapongeza viongozi wa Kanisa Kamati ya Ujenzi na waumini wa Usharika wa Ndolage kwa kujitolea kufanikisha ujenzi wa kanisa hilo akieleza kuwa hadi sasa waumini wamechangia kazi na fedha zenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 265.8. Aliwataka waumini kuendelea kujitolea ili kuhakikisha nyumba hiyo ya ibada inakamilika kwa wakati.

Aidha amesema Kanisa linaendelea kuwa nguzo muhimu ya jamii kwa kutoa malezi ya kiroho na maadili, huduma za elimu na afya pamoja na kuwasaidia makundi yenye uhitaji Amesisitiza kuwa pamoja na kujenga nyumba za ibada ni muhimu pia kujenga jamii yenye upendo mshikamano na uwajibikaji ili kudumisha amani na maendeleo ya Taifa.

Kwa upande wake Askofu wa KKKT Dayosisi ya Kaskazini Magharibi Baba Askofu Dkt. Abednego Keshomshahara ameishukuru Serikali kwa ushirikiano unaoendelea kati yake na taasisi za dini katika utoaji wa huduma za kijamii ikiwemo elimu afya na huduma nyingine muhimu kwa wananchi Ametoa wito kwa Serikali kuendelea kuimarisha ushirikiano huo ili kuongeza ufanisi wa kuwahudumia wananchi.

Awali Mkuu wa Wilaya ya Muleba, Dkt. Abel Nyamahanga akitoa salamu za Mkoa amewapongeza viongozi na waumini wa Kanisa kwa hatua waliyoifikia katika ujenzi wa kanisa hilo Pia amepongeza mahubiri yaliyotolewa wakati wa ibada, akisema yamehimiza waumini kuchangia kwa hiari na kwa moyo wa kujitoa bila kulazimishwa.

Katika risala yao viongozi wa Kanisa wameiomba Serikali kushughulikia ujenzi wa barabara ya lami yenye urefu wa kilomita 4.8 kutoka Kamachumu hadi Hospitali ya Ndolage pamoja na kuongeza watumishi wa afya wanaolipwa kupitia ruzuku ya Serikali.

Akijibu maombi hayo Dkt. Munisi ameahidi kuyawasilisha katika mamlaka husika ili yafanyiwe kazi Aidha amewahamasisha waumini na wadau mbalimbali kuendelea kuchangia ujenzi wa Kanisa la KKKT Usharika wa Ndolage akisisitiza kuwa ushirikiano na mshikamano ni msingi muhimu wa maendeleo ya jamii na Taifa kwa ujumla.


Share:

Saturday, 4 July 2026

REKODI YA TRILIONI 37.96 ZA TRA NI USHAHIDI WA MAGEUZI YA RAIS SAMIA NA UCHUMI IMARA WA TANZANIA

 

Katika kipindi ambacho mataifa mengi duniani yanaendelea kukabiliana na changamoto za kiuchumi, Tanzania imeendelea kuandika historia mpya.

 Rekodi ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kukusanya Shilingi Trilioni 37.96 katika mwaka wa fedha 2025/2026, sawa na utekelezaji wa asilimia 105.24 ya lengo la Serikali, ni zaidi ya takwimu; ni kielelezo cha mafanikio ya uongozi, mageuzi ya kiuchumi na usimamizi madhubuti wa mapato ya ndani.

Mafanikio haya yanathibitisha kuwa dira ya maendeleo ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea kuzaa matunda.

Mageuzi ya Rais Samia Yameongeza Nguvu ya Uchumi

Tangu alipoingia madarakani, Rais Samia ameendelea kusimamia mageuzi makubwa katika sekta mbalimbali za uchumi kwa lengo la kujenga mazingira bora ya biashara, kuvutia wawekezaji, kuongeza uzalishaji na kupanua wigo wa walipakodi.

Sera ya "4R" (Maridhiano, Ustahimilivu, Mageuzi na Kujenga Upya) imeongeza imani ya sekta binafsi na washirika wa maendeleo, huku mazingira rafiki ya uwekezaji yakichochea ukuaji wa shughuli za kiuchumi nchini.

Matokeo yake sasa yanaonekana wazi kupitia ongezeko la mapato ya Serikali bila kutegemea misaada ya nje.

TRA Imebadilika Kutoka Mkusanyaji wa Kodi Pekee hadi Mshirika wa Maendeleo

Kwa miaka ya hivi karibuni, TRA imepitia maboresho makubwa ya kiutendaji.

Matumizi ya mifumo ya kidijitali, utoaji wa huduma kwa njia za kisasa, elimu kwa walipakodi na hatua madhubuti za kuziba mianya ya ukwepaji kodi vimeongeza ufanisi wa ukusanyaji wa mapato.

Badala ya kutegemea kuongeza viwango vya kodi, TRA imeendelea kupanua wigo wa walipakodi na kuboresha usimamizi wa mapato, hatua iliyowezesha kufikiwa kwa rekodi hii ya kihistoria.

Kaulimbiu ya TRA ya "Pamoja Tunajenga Taifa Letu" imeendelea kuonekana kwa vitendo kupitia ushirikiano kati ya Serikali, wafanyabiashara na wananchi.

Trilioni 37.96 ni Mtaji wa Maendeleo

Fedha zinazokusanywa na TRA ndizo zinazowezesha Serikali kutekeleza miradi mikubwa ya maendeleo inayogusa maisha ya Watanzania kila siku.

Katika miaka ya hivi karibuni, wananchi wameshuhudia ujenzi wa shule mpya, hospitali za kisasa, vituo vya afya, barabara, madaraja, miradi ya maji safi na salama, upanuzi wa huduma za umeme pamoja na uboreshaji wa huduma za kijamii nchini.

Aidha, mapato haya ndiyo msingi wa utekelezaji wa miradi ya kimkakati kama reli ya kisasa (SGR), uzalishaji wa umeme kupitia Bwawa la Julius Nyerere na miradi mingine inayolenga kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha biashara na uwekezaji katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Ushirikiano wa Walipakodi Unastahili Pongezi

Mafanikio haya yasingewezekana bila uzalendo wa walipakodi walioendelea kutimiza wajibu wao kwa hiari.

Biashara kubwa na ndogo, wawekezaji, wafanyakazi na wananchi kwa ujumla wameendelea kuchangia maendeleo ya Taifa kupitia ulipaji wa kodi, wakitambua kuwa kodi ndiyo injini ya maendeleo.

Kadri uelewa wa umuhimu wa kodi unavyoendelea kuongezeka, ndivyo Taifa linavyozidi kujijengea uwezo wa kugharamia maendeleo kwa kutumia rasilimali zake.

Tanzania Inaelekea Kwenye Uchumi Unaotegemea Mapato ya Ndani

Kuvuka lengo la makusanyo kwa zaidi ya asilimia 105 ni ishara kwamba Tanzania inaendelea kujenga uchumi imara unaotegemea nguvu zake yenyewe.

Hii inaongeza uwezo wa Serikali kutekeleza bajeti kwa wakati, kupunguza utegemezi wa mikopo yenye masharti na kuongeza uhuru wa kufanya maamuzi ya maendeleo kulingana na vipaumbele vya Taifa.

Ni hatua muhimu kuelekea dira ya kujenga uchumi shindani, jumuishi na unaowanufaisha Watanzania wote.

Rekodi ya kukusanya Shilingi Trilioni 37.96 si mafanikio ya TRA pekee, bali ni ushahidi wa mafanikio ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, usimamizi madhubuti wa Serikali na uzalendo wa walipakodi wa Tanzania.

Kadri Serikali inavyoendelea kuimarisha mazingira ya biashara, kuvutia uwekezaji na kuongeza ufanisi wa taasisi za ukusanyaji mapato, matarajio ya kuvunja rekodi nyingine katika miaka ijayo yanaendelea kuwa makubwa.

Hakika, mafanikio haya yanaonesha kuwa Tanzania ipo kwenye njia sahihi ya kujenga uchumi imara, unaojitegemea na wenye uwezo wa kugharamia maendeleo yake kupitia mapato ya ndani.

Rekodi hii ni ushindi wa Serikali, TRA na kila Mtanzania anayetekeleza wajibu wake wa kulipa kodi kwa maendeleo ya Taifa.


Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger