Monday, 8 June 2026

CHATANDA ATOA POLE KWA FAMILIA YA MKUU WA MKOA MSTAAFU MASHISHANGA


Na mwandishi wetu

Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa CCM (UWT) Taifa, Mary Pius Chatanda (MCC), leo Juni 6, 2026 amefika nyumbani kwa Mkuu wa Mkoa Mstaafu wa Mwanza, Ndg. Steven Mashishanga eneo la Nyasaka, jijini Mwanza, kutoa pole na faraja kufuatia msiba wa binti yao, Loyce S. Mashishanga.

Binti huyo alifariki dunia Juni 2, 2026 katika Hospitali ya Hindu Mandal, Mwanza Hindu Mandal Hospital, baada ya kuugua.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo ya faraja, Chatanda amewasilisha salamu za pole kwa niaba ya Jumuiya ya Umoja wa Wanawake wa CCM pamoja na Chama Cha Mapinduzi kwa ujumla, akisisitiza mshikamano na familia katika kipindi hiki kigumu cha majonzi.

Ameomba Mwenyezi Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi, na kuipatia familia uvumilivu, nguvu na subira ya kustahimili pigo hilo kubwa la kifamilia.

_“Sisi ni wa Mwenyezi Mungu na kwake tutarejea. Mwenyezi Mungu awape faraja na amani katika kipindi hiki cha huzuni,” imesema sehemu ya ujumbe huo wa rambirambi.





Share:

Sunday, 7 June 2026

VIJANA NA WASOMI MKOANI MWANZA WAHIMIZWA UZALENDO NA UJASIRIAMALI KATIKA KONGAMANO

Na Mwandishi Wetu

​Katika jitihada za kuimarisha chachu ya maendeleo, Kongamano la Wasomi lililoandaliwa na Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Seneti Mkoa wa Mwanza, limefanyika leo, Juni 07, 2026, katika Chuo cha Uvuvi Nyegezi, likilenga kuwajengea vijana uwezo katika nyanja za uongozi, uchumi, afya, na itikadi ya chama.

​Akizungumza katika kongamano hilo, Mgeni Rasmi ambaye ni Mwenyekiti wa Vyuo na Vyuo Vikuu Seneti Mkoa wa Mwanza, Kenneth Geremia, amewasisitiza vijana kuonesha mapenzi ya dhati kwa Chama Cha Mapinduzi. Kiongozi huyo mwenye maono mapana, amewataka wanachama kudumisha mshikamano na ushirikiano imara baina ya matawi yote ndani ya mkoa wa Mwanza ili kujenga chama chenye nguvu zaidi.

​Katibu wa Vijana UVCCM Kata ya Luchelele, Omary Msuya, aliyekuwa mratibu wa hafla hiyo (MC), ametoa wito mzito kwa kila kijana kufanya uwajibikaji na uzalendo kuwa kipaumbele chao cha kwanza katika ujenzi wa taifa, akisisitiza kuwa vijana ndio uti wa mgongo wa maendeleo.

​Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Vijana UVCCM Wilaya ya Ilemela, Salum Mtatulu, amewahimiza vijana kujitolea kwa hali na mali katika shughuli za kijamii na kisiasa, akibainisha kuwa uwajibikaji thabiti ndio msingi mkuu wa mafanikio ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).

​Katika kipengele cha elimu ya afya, Dkt. Misana Mulemwa kutoka Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Sekou Toure, ametoa elimu muhimu kwa vijana kuhusu umuhimu wa kulinda afya zao dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza kama shinikizo la damu, kisukali na maradhi ya moyo. Dkt. Mulemwa amewataka vijana kuchukua tahadhari dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza huku akisisitiza kuwa uzima wa kijana ndio nguvu ya uzalishaji taifa.

​Katika sekta ya uchumi, Pius Mtenya, mfugaji wa samaki kwa njia ya vizimba katika mtaa wa Sylvini, ameeleza namna mradi huo ulivyokuwa ukombozi wa kiuchumi kwa vijana wilayani Nyamagana. Mpenya, ambaye ni kielelezo cha mafanikio, amewahimiza vijana kuondokana na hofu na badala yake waunde vikundi ili kufaidika na mikopo yenye riba nafuu inayotolewa na serikali.

Nae, ​Mlezi wa Tawi Bi. Immaculata Ndalawa, ambaye ni Mwalimu katika Chuo cha Uvuvi Nyegezi, amewashauri vijana kuhudhuria mara kwa mara makongamano kama haya. Ndalawa amesema kongamano hizo zinawajengea uwezo wa kipekee vijana katika kuelezea na kusimamia vyema mafanikio ya serikali katika miradi ya maendeleo nchi nzima.

Pamoja na mambo mengine, Katibu Hamasa wa Kambarage SAUT, Perus Leonard, ametoa mwongozo kwa wanafunzi vyuoni kuhusu matumizi sahihi ya mitandao ya kijamii. Leonard, kijana mbunifu, amewataka vijana kugeuza mitandao hiyo kuwa fursa za kiuchumi kupitia uandaaji wa maudhui (content creation), biashara za mtandaoni, na kuanzisha asasi zisizo za kiserikali zitakazosaidia kutatua changamoto za kijamii kama vile kulea watoto yatima na utunzaji wa mazingira.

Share:

MIGODI YA BARRICK YA BULYANHULU NA NORTH MARA YAADHIMISHA SIKU YA MAZINGIRA KWA KUPANDA MITI NA KUFUATILIA MRADI WA UREJESHAJI UOTO ASILI MTO TIGHITE

Wafanyakazi wa Barrick Bulyanhulu wakiwa kwenye picha ya pamoja na wanafunzi baada ya kushiriki zoezi la upandaji wa miti kwenye maadhimisho ya siku ya mazingira duniani.
Afisa Mahusiano ya Jamii Mwandamizi wa Mgodi wa Barrick Bulyanhulu , Zuwena Senkondo akimwagilia mti baada ya upandaji katika maadhimisho ya siku ya mazingira duniani
Wafanyakazi wa Barrick North Mara wakipanda miti kando kando ya Mto Tighite katika maadhimisho ya siku ya mazingira duniani Wilayani Tarime , Mkoani Mara.
***

Kampuni ya Barrick inayoendesha shughuli zake nchini kwa ubia na Serikali kupitia kampuni ya Twiga, kupitia migodi yake ya Bulyanhulu na North Mara imeadhimisha Siku ya Mazingira Dunia 2026 kwa kushirikiana na jamii zinazoizunguka kwa kupanda miti, kufanya usafi kwenye shule na kukagua maendeleo ya mradi wa kurejesha uoto wa asili wa Mto Tighite uliopo wilayani Tarime.

Mgodi wa Barrick Bulyanhulu ulipo katika Halmashauri ya wilaya ya Msalala mkoani Shinyanga wafanyakazi wake walitembelea Shule ya Msingi Kakola A na kupanda miti pamoja na kufanya usafi pia ulitoa msaada wa miche ya miti ya matunda na kivuli ipatayo 2300.

Kwa upande wa Mgodi wa Barrick North Mara uliopo wilayani Tarime mkoani Mara, Wafanyakazi wake waliungana na jamii kutembelea na kukagua maendeleo ya mradi wa kurejesha uoto wa asili wa mto Tighite uliopo katika Kijiji cha Matongo unaofadhiliwa na mgodi huo kupitia shirika lisilo la Kiserikali la Jumuiya ya Watumiaji Maji Tighite Chini (JWMTC).

Kaimu Meneja Mazingira wa Barrick Bulyanhulu, Arespicius Onesmo akizungumzia kuhusu ushiriki wa Barrick Bulyanhulu katika maadhimisho ya mwaka huu,alisema ni mwendelezo wa utekelezaji wa mkakati wa kampuni ambapo suala la mazingira linapewa kipaumbele kikubwa.

“Tumeshirikiana na jamii kuadhimisha Siku ya Mazingira Duniani kwa kupanda miti, tumeanzia ndani ya mgodi ambapo wafanyakazi wa kila idara wameshirikiana na viongozi wao kupanda miti, na hii inaonesha uwajibikaji wa mgodi katika kulinda na kutunza mazingira vilevile mgodi una programu ya kutoa miche zaidi ya 20,000 katika shule zilizopo katika kata mbili za Bugarama na Bulyanhulu ili kuboresha mazingira”,alisema Onesmo.

Naye Meneja Mazingira wa Barrick North Mara, Frank Ngoloma alisema maadhimisho ya mwaka huu wameyafanya kwa kufuatilia maendeleo ya ukuaji wa miti ya asili iliyopandwa kandokando ya mto Tighite kwa ufadhili wa mgodi na wameridhishwa na usimamizi mzuri wa mradi huo na miti iliyopandwa mwaka jana inaendelea kustawi vizuri

Ngoloma alisema mradi huo ulizinduliwa wakati wa maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani mwaka jana kwa lengo la kurejesha uoto wa asili wa mto huo unaotegemewa na maelfu ya wananchi kwa ajili ya maji ya matumizi ya majumbani,kunywesha mifugo na shughuli za kilimo.

Akizungumzia ushiriki wa Barrick kushirikiana na jamii kuadhimisha Siku ya Mazingira Duniani kila mwaka, kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Msalala , Humphrey Peter aliupongeza Mgodi wa Bulyanhulu kwa kuthamini maadhimisho hayo na kuona umuhimu wa kushirikiana na jamii katika zoezi la kupanda miti ili kulinda mazingira.

“Tunaushukuru Mgodi wa Barrick Bulyanhulu kwa kutambua siku ya mazingira dunia, kati ya taasisi na mashirika yaliyopo katika wilaya yetu ni Barrick Bulyanhulu pekee ndio wanafanya tukio hili la kipekee na wanakuja kusaidiana na jamii kuboresha Mazingira ,” amesema Humphrey.

Naye Mwenyekiti wa JWMTC, Mwita Seri na Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji cha Matongo,Charles Ryoba wameushukuru mgodi wa Barrick North Mara kwa ufadhili na ushirikiano unaoendelea kutoa kwa ajili ya utekelezaji wa mradi wa kuboresha mazingira ya mto Tighite unaolenga kufanikisha upandaji wa miti ya asili 50,000 .

Kwa mujibu wa taarifa iliyosomwa, JWMTC iliomba Mgodi wa Barrick North Mara ukakubali kutoa shilingi milioni 36.7 kwa ajili ya kuotesha miche kwenye vitalu, kisha kupanda miti ya asili 50,000 katika eneo lenye ukubwa wa hekta 27 kandokando ya Mto Tighite.

Aidha, Mto Tighite ni miongoni mwa vyanzo muhimu vinavyochangia maji katika Mto Mara ambao unamwaga maji yake katika la ziwa la kimataifa - Ziwa Victoria upande wa Tanzania.

Kampuni ya Barrick katika mikakati yake endelevu moja ya sera katika uendeshaji shughuli zake mambo ya mazingira na mabadiliko ya tabianchi yanapewa vipaumbele katika utunzaji wa mazingira , kulinda vyanzo ya maji, uchafunzi wa hali ya hewa na kulinda uoto wa asili.
Wafanyakazi wa Barrick Bulyanhulu wakiwa kwenye picha ya pamoja na wanafunzi na wadau wengine mara baada ya zoezi la upandaji wa miti katika maadhimisho ya siku ya mazingira duniani
Wafanyakazi North Mara wakiongea na wananchi baada ya kutembelea mto Tighite
Wafanyakazi North Mara wakiongea na wananchi baada ya kutembelea mto Tighite

Share:

WALIMU FUNDISHENI VIZURI TUPATE TAIFA IMARA - PROF. SHEMDOE

Na OWM - TAMISEMI, Dar es Salaam

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe ametoa wito kwa walimu wote nchini  wa shule za awali, msingi na sekondari  kufundisha kwa umahiri ili taifa liwe imara na rasilimali watu yenye kutoa mchango katika ukuaji wa uchumi na ustawi wa jamii.

Prof. Shemdoe ametoa wito huo kwa walimu hao Juni 06, 2026 katika Ukumbi wa Maktaba mpya wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, wakati wa hafla ya utoaji wa zawadi kwa washindi wa shindano la taifa la stadi za ufundishaji kwa walimu wa awali, msingi na sekondari nchini.

“Kaulimbiu hii inayosema Ufundishaji Bora, Taifa Imara ina mashiko, hivyo  ninatoa wito kwa walimu mfundisheni vizuri, na wito huu si kwa walimu mlioshinda tu bali ni kwa walimu wote nchi nzima kwani mnapaswa kuzingatia  kuwa ufundishaji bora utatupatia taifa imara,” amesisitiza Prof. Shemdoe.

Ili kuwapatia motisha walimu 35 walioshinda katika shindano la taifa la stadi za ufundishaji, Prof. Shemdoe amewaelekeza wakurugenzi wa halmashauri zote ambazo walimu hao wanafundisha kuhakikisha wanawapatia kiwanja ili waendelee kubaki katika vituo vyao vya kazi na kulitumikia taifa, huku viwanja hivyo vikibaki kuwa ni kumbukumbu ya kudumu ya namna Serikali inavyothamini utendaji kazi wao.

Sanjari na hilo, Prof. Shemdoe amewataka walimu wengi zaidi kujitokeza kushiriki katika shindalo hilo mwakani ili  kuibuka washindi na kutambulika kitaifa kutokana na umahiri wao katika stadi za ufundishaji.

Aidha, Prof. Shemdoe amemshukuru na kumpongeza Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa kipaumbele kikubwa cha kuboresha miundombinu ya sekta ya elimu hususani katika eneo la ujifunzaji na ufundishaji, hatua ambayo imeongeza kiwango cha ufaulu wa wanafunzi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Elimu Tanzania (TET) Dkt. Aneth Komba amesema kuwa shindano hilo limejumuisha halmashauri zote 184 za Tanzania Bara na linaratibiwa na Serikali kupitia TET chini ya Programu ya kuboresha Elimu ya Awali na Msingi (BOOST) na Mradi wa kuimarisha Ubora wa Elimu ya Sekondari (SEQUIP).

Washindi wa shindano hilo la taifa la stadi za ufundishaji kwa walimu wa awali, msingi na sekondari wamepatiwa zawadi ya fedha tasilimu, kompyuta, kompyuta mpakato, vibao vya kidijitali na projekta kwa ajili ya shule zao ili kuongeza ufanisi katika ufundishaji na ujifunzaji.












Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMAPILI JUNI 7,2026


Magazeti
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger