Thursday, 28 May 2026

𝐌𝐀𝐅𝐔𝐍𝐙𝐎 𝐘𝐀 𝐔𝐎𝐍𝐆𝐎𝐙𝐈 𝐊𝐖𝐀 𝐖𝐀𝐊𝐔𝐔 𝐖𝐀 𝐒𝐇𝐔𝐋𝐄 𝐘𝐀𝐙𝐈𝐍𝐃𝐔𝐋𝐈𝐖𝐀 𝐑𝐀𝐒𝐌𝐈


SERIKALI imezindua rasmi Mpango wa Mafunzo ya Uongozi na Usimamizi wa Elimu kwa Wakuu wa Shule za Sekondari na Maafisa Elimu Kata nchini, hatua inayolenga kuimarisha ufanisi wa uongozi wa shule, usimamizi wa ufundishaji na ujifunzaji pamoja na kuimarisha ubora wa elimu nchini.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo Mei 28, 2026 mkoani Mwanza Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo, amesema mpango huo ni hatua muhimu katika kujenga uwezo wa viongozi wa elimu hususan wakuu wa shule za sekondari ambao kwa muda mrefu hawajapata mafunzo ya uongozi na usimamizi wa elimu kwa kiwango kinacholingana na mahitaji ya sasa ya mfumo wa elimu.

Amesema tofauti na walimu wakuu wa shule za msingi ambao wamekuwa wakipata mafunzo ya uongozi, wakuu wa shule za sekondari wamekuwa wakikosa fursa hiyo kwa kipindi kirefu, hali iliyofanya Serikali kuona umuhimu wa kuanzisha mpango huo wa kitaifa ili kuongeza ufanisi wa utendaji kazi na kuboresha utoaji wa elimu.

“Mpango huu ni fursa muhimu kwa viongozi wa shule kupata maarifa ya kisasa ya uongozi, utawala bora na usimamizi wa elimu ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku,” alisema Prof. Nombo.

Prof. Nombo ameeleza kuwa mafunzo hayo hayatawahusu wakuu wa shule pekee, bali yatawajumuisha pia wakuu wasaidizi wa shule za sekondari pamoja na Maafisa Elimu Kata kutoka Tanzania Bara na Zanzibar ili kuhakikisha viongozi wote wa elimu wanakuwa na uelewa unaofanana katika kusimamia ubora wa elimu.

Aidha, amesema Maafisa Elimu wa Mikoa na Halmashauri watashiriki kama wasimamizi wa utekelezaji wa mpango huo katika maeneo yao, hatua itakayosaidia kuhakikisha maarifa yanayopatikana yanaenda sambamba na maboresho ya mifumo ya usimamizi wa elimu.

Pamoja na hayo ameipongeza ADEM pamoja na VVOB-Tanzania kwa kuandaa na kufadhili mpango huo, akieleza kuwa ndani ya kipindi cha miaka mitano kuanzia 2025 hadi 2030, jumla ya viongozi wa elimu 16,000 wanatarajiwa kufikiwa, wakiwemo wakuu wa shule na wasaidizi wao 12,000 pamoja na Maafisa Elimu Kata 4,000.

Amesema mbali na mafunzo ya uongozi, mpango huo utatoa fursa za ufadhili wa masomo kwa Watanzania kupitia scholarships, huku akiwataka viongozi wa elimu kuchangamkia nafasi hizo kwa kuwa elimu ni mchakato endelevu usio na kikomo.

Amesema mafunzo hayo yatafanyika kwa muda wa miezi mitano kwa mfumo wa elimu masafa na ana kwa ana (blended learning), ambapo washiriki wataendelea kutekeleza majukumu yao ya kawaida huku wakijifunza na kutekeleza shughuli za kimradi zinazohusiana na usimamizi wa shule.

Amewataka viongozi wa elimu ngazi ya mkoa na halmashauri kutoa ushirikiano wa karibu kwa washiriki wa mafunzo ili kuwajengea mazingira rafiki ya kujifunza na kuhakikisha wanatimiza wajibu wao wa kikazi sambamba na mafunzo.

Aidha, amefafanua kuwa utekelezaji wa awamu ya kwanza utaanza mwezi Juni 2026 ukihusisha washiriki kutoka halmashauri 12 katika mikoa sita ya Mwanza, Mara, Kagera, Geita, Simiyu na Shinyanga, huku kila mkoa ukianza na halmashauri mbili.

Katika mafunzo hayo, washiriki watajengewa uwezo katika maeneo mbalimbali ya kitaaluma yakiwemo uandaaji wa mipango mkakati, ufunzaji na uatamizi, uthibiti ubora wa ndani wa shule, uongozi wa ufundishaji na ujifunzaji, usimamizi wa mtaala ulioboreshwa wa mwaka 2023 pamoja na usimamizi wa mtaala unaojenga umahiri.

Wakati huo huo, Prof. Nombo amesema Serikali inaendelea kufanya mageuzi makubwa katika sekta ya elimu kupitia utekelezaji wa mtaala ulioboreshwa, ujenzi na ukarabati wa shule, upatikanaji wa vifaa vya kufundishia na kujifunzia pamoja na uwekezaji katika elimu ya amali ili kuandaa wahitimu wenye maarifa, ujuzi na ushindani ifikapo mwaka 2050.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa ADEM, Dkt. Maulid J. Maulid amesema mafunzo hayo yana umuhimu mkubwa kwa wakuu wa shule za sekondari, hasa kutokana na ukweli kwamba kwa muda mrefu kundi hilo halijapata mafunzo ya kina ya kiuongozi na kiutendaji.

Amesema kupitia mafunzo hayo, wakuu wa shule watapata maarifa na mbinu mpya zitakazowawezesha kusimamia shule kwa ufanisi zaidi, kujenga mazingira bora ya kujifunzia na hatimaye kuboresha matokeo ya wanafunzi.

Uzinduzi huo umehudhuriwa na viongozi mbalimbali kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Wathibiti Ubora wa Shule, Maafisa Elimu wa Mikoa na Wilaya pamoja na wadau wa elimu, jambo linalodhihirisha uzito na umuhimu unaowekwa katika kuimarisha uongozi wa elimu nchini.
Share:

KUTOKA MSIKITI WA GADDAFI: WAUMINI WATAKIWA KUTII MAMLAKA NA KULINDA AMANI YA TAIFA




Shehe wa Mkoa wa Dodoma, Mustapha Rajabu Shaaban, amewataka waumini wa dini ya Kiislamu na jamii kwa ujumla kudumisha amani na mshikamano kwa kuwa wasikivu na wenye kutii mamlaka.

Akizungumza katika ibada ya Idd al-Adha kwenye Msikiti wa Gaddafi jijini Dodoma, Shehe Shaaban alisisitiza kuwa kukosekana kwa utiifu na usikivu ndiko kunakosababisha migogoro na umwagaji wa damu katika jamii.


Katika kuelezea umuhimu wa ibada ya kuchinja iliyohitimisha mwezi wa Dhulhijjah, kiongozi huyo alikumbusha kuwa ibada hiyo chimbuko lake ni historia ya Nabii Ibrahim na mwanawe Nabii Ismail.


Alieleza kuwa kisa hicho si hadithi tu ya kawaida, bali ni fundisho kubwa la jinsi Nabii Ibrahim alivyomshirikisha mwanawe kuhusu ndoto ya kumchinja, jambo linalofundisha umuhimu wa kuheshimiana, kusikilizana na kutii amri za Mwenyezi Mungu na mamlaka husika.

Mwisho, Shehe Shaaban aliwasihi wananchi kuendeleza utamaduni wa kuheshimiana ndani ya familia na kitaifa, huku akiwataka kuheshimu viongozi, taasisi, na vyombo mbalimbali vya kijamii na kidini.

Alitolea mfano kamati na tume zinazoundwa ndani ya Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA), akisisitiza kuwa kuheshimu mifumo hiyo ndiko kunakojenga ustawi wa jamii.
Share:

WENYE MAHITAJI MAALUM KUPEWA KIPAUMBELE MAFUNZO YA JKT



Na Dotto Kwilasa, Dodoma 

Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) limesema vijana wenye mahitaji maalum, hususan wenye ulemavu wa viungo, wamewekewa mazingira rafiki yatakayowawezesha kushiriki kikamilifu mafunzo ya uzalendo na stadi za maisha yanayoanza rasmi Juni mwaka huu.

Hatua hiyo imekuja sambamba na maandalizi ya kupokea jumla ya vijana 60,000 wa kidato cha sita kutoka shule mbalimbali Tanzania Bara na Zanzibar watakaoripoti katika makambi ya JKT kuanzia Juni 1 hadi Juni 7, 2026.

Akizungumza jijini Dodoma leo Mei 28, 2026 kwa niaba ya Mkuu wa JKT, Meja Jenerali Rajabu Mabele, Mkuu wa Utawala wa JKT, Brigedia Jenerali Hassan Mabena amesema vijana wenye mahitaji maalum watapangiwa katika Kambi ya Ruvu mkoani Pwani kutokana na uwepo wa miundombinu na huduma zinazokidhi mahitaji yao.

Amesema Serikali imeendelea kuboresha mfumo wa mafunzo hayo kwa kuongeza idadi ya vijana wanaopokelewa kutoka 40,000 hadi 60,000 mwaka huu ikiwa ni sehemu ya kuimarisha uzalendo, nidhamu na uwezo wa kujitegemea kwa vijana.

“Lengo ni kuwajenga vijana kuwa na maadili mema, uzalendo na stadi zitakazowasaidia katika maisha yao ya baadaye na katika kulitumikia taifa,” amesema Mabena.

Kwa mujibu wa Mabena, vijana hao watapangiwa katika makambi mbalimbali nchini ikiwemo Rwamkoma Mara, Msange Tabora, Mpwapwa na Makutupora Dodoma, Mafinga Iringa pamoja na Oljoro Arusha.

Makambi mengine yaliyotajwa ni Bulombora Kagera, Kanembwa na Mtabila Kigoma, Itaka Songwe, Luwa na Milundikwa Rukwa pamoja na Nachingwea mkoani Lindi.

Aidha, JKT limewataka vijana wote waliochaguliwa kuzingatia maelekezo ya kuripoti kwa wakati pamoja na kubeba vifaa muhimu vitakavyotumika wakati wa mafunzo, ikiwemo mavazi ya michezo, shuka, soksi na nyaraka muhimu za masomo na utambulisho.

Amesema mafunzo hayo hayalengi kuwapa vijana maarifa ya kijeshi pekee, bali pia kuwaandaa kuwa raia wenye nidhamu, uwezo wa kufanya kazi na kujitegemea hata kwa wale watakaokosa nafasi za kuendelea na elimu ya juu.

Programu ya mafunzo ya lazima ya JKT ilirejeshwa rasmi mwaka 2013 ikiwa na dhamira ya kuwajengea vijana moyo wa uzalendo na kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo ya taifa.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO ALHAMISI MEI 28, 2026

Magazeti Leo


















Share:

Wednesday, 27 May 2026

JUMUIYA ZA KIRAIA 126 ZIMESAJILIWA NCHINI 2025/26- WAZIRI KATAMBI



Na mwandishi wetu,Dodoma

Katika kipindi cha Julai 2025 hadi Aprili 2026, Jumla ya Jumuiya za Kiraia 126 zimesajiliwa Nchini, 12 kati yake zikiwa ni Jumuiya za kidini na 114 zisizo sa kidini.

Takwimu hizo zimebainishwa leo Jumatatu Mei 25, 2026 Bungeni Mjini Dodoma na Waziri wa mambo ya ndani ya Nchi Mhe. Patrobas Katambi wakati akisoma hotuba ya bajeti ya Wizara hiyo kwa mwaka 2026/27, akibainisha kwamba ukaguzi wa jumuiya 350 ulifanyika na Wizara yake katika kipindi kama hicho cha Julai 2025 hadi Aprili, 2026, lengo likiwa ni kufuatilia utekelezaji wa masharti ya usajili pamoja na kubaini mchango wa Jumuiya hizo katika maendeleo.

"Mhe. Spika, pia Wizara imeanzisha programu za ushirikishwaji ili kuimarisha uelewa na uwajibikaji wa viongozi wa jumuiya za kiraia katika uendeshaji wa jumuiya zao. Kupitia programu hiyo, jumla ya viongozi wa jumuiya za kidini na zisizo za kidini 2,500 walipatiwa mafunzo kuhusu uendeshaji wa jumuiya unaozingatia sheria na kuimarisha amani, utulivu na mshikamano wa kitaifa. 

Katika mwaka 2026/27, Wizara imetenga Shilingi bilioni 1.57 kwa ajili ya shughuli za usimamizi na uratibu wa Jumuiya za Kiraia nchini." Amesema Waziri Katambi.
Share:

Tuesday, 26 May 2026

WAZIRI SANGU AZINDUA BODI YA SABA YA USHAURI YA OSHA.


-Asisitiza Utekelezaji wa Viwango vya Kimataifa vya Usalama na Afya katika Maeneo ya Kazi

Na, OWM-KAM

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mheshimiwa Deus Sangu, amezindua Bodi ya Saba ya Ushauri ya Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA), iliyoanzishwa kwa mujibu wa Sheria ya Wakala za Serikali, Sura ya 245 Toleo la mwaka 2023 chini ya Kifungu cha 6 cha sheria hiyo.

Amezungumza hayo tarehe 25 Mei, 2026 wakati wa uzinduzi huo, Waziri Sangu amesema bodi hiyo ina jukumu la kutoa ushauri wa kitaalamu kwa OSHA ili kuimarisha utendaji wa taasisi hiyo na kuhakikisha mikakati inaendelea kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi, kwa kuzingatia dira, dhima na malengo ya Serikali.

Amesema kuwa miongoni mwa majukumu ya bodi hiyo ni kushauri kuhusu uandaaji na utekelezaji wa mpango mkakati wa OSHA, kufanya tathmini ya utendaji wa taasisi kupitia taarifa za mwaka na hesabu za wakala, pamoja na kutoa ushauri kuhusu maslahi na stahili za watumishi kwa lengo la kuongeza motisha, uwajibikaji na tija mahali pa kazi.

Katika hatua nyingine, Waziri Sangu ameielekeza bodi hiyo kusimamia utekelezaji wa mikataba ya kimataifa ya Shirika la Kazi Duniani (ILO) Na. 155 na 187 ili kuhakikisha viwango vya kimataifa vya usalama na afya mahali pa kazi vinaendelea kuzingatiwa nchini.

Aidha, ameitaka bodi hiyo kuimarisha mifumo ya utoaji huduma kwa njia ya kidijitali, ikiwemo mfumo wa Workplace Information Management System (WIMS), kwa lengo la kuongeza uwazi, ufanisi na kurahisisha utoaji wa huduma kwa wananchi na wadau mbalimbali.

"Majukumu haya yatekelezwe kwa kuzingatia sera, sheria, kanuni, taratibu na miongozo inayotolewa na Serikali pamoja na misingi ya uwajibikaji, uadilifu, ubunifu, ushirikiano kazini na uwazi" amesema Waziri Sangu.

Sambamba na hilo, amesema bodi hiyo inaanza majukumu yake katika kipindi muhimu ambapo Serikali inaendelea na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 pamoja na Mpango wa Nne wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano, huku uzinduzi wa Mpango Mkakati wa OSHA ukiwa chachu ya utekelezaji wa majukumu ya bodi hiyo.

Waziri Sangu pia ameisisitiza bodi hiyo kutekeleza wajibu wake kwa kuzingatia sera, sheria na miongozo iliyowekwa, huku akiitaka kutoa nafasi kwa menejimenti ya OSHA kusimamia shughuli za kila siku bila kuingiliwa. Amesema jukumu kuu la bodi ni kutoa ushauri na usimamizi wa kimkakati ili kuhakikisha kila upande unatekeleza wajibu wake ipasavyo.

Akizungumza Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri OSHA, Makwaia Makani, ameishukuru Serikali kwa imani iliyowaonesha na kuahidi kuwa bodi hiyo itatekeleza maelekezo yote yaliyotolewa kwa kuzingatia sheria, kanuni na miongozo iliyowekwa.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo, Bi. Zuhura Yunus, amewapongeza wajumbe wa bodi kwa kuaminiwa na kuteuliwa, akiwataka kutumia weledi na umahiri wao katika kuisimamia OSHA kwa manufaa ya taasisi na taifa kwa ujumla.

Naye Mtendaji Mkuu wa OSHA, Bi. Khadija Mwenda, amesema bodi zimekuwa na mchango mkubwa katika maendeleo ya taasisi hiyo na kwamba menejimenti ya OSHA ipo tayari kushirikiana na bodi mpya ili kuendelea kuimarisha utendaji na utoaji wa huduma.
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger