Monday, 18 May 2026

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMANNE MEI 2026


Magazeti
 

Share:

Wimbo Mpya : GUDE GUDE - DUNIA

 

Share:

SERIKALI KUENDELEA KUBORESHA MAZINGIRA YA BIASHARA KARIAKOO


NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

SERIKALI imesema itaendelea kuboresha mazingira ya biashara nchini ili kuhakikisha wafanyabiashara wa Kariakoo wanakuwa na ushindani wa kikanda na kimataifa huku ikiitaja Kariakoo kuwa moyo wa biashara wa Tanzania na injini muhimu ya uchumi wa taifa.

Hayo yameelezwa leo Mei 17, 2026 katika hafla ya Utoaji wa Tuzo za Biashara Kariakoo ambapo Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara, Bw. Aristides Mbwasi, aliyemwakilisha Waziri wa Wizara hiyo, amesema Kariakoo si eneo la kawaida katika historia ya biashara nchini bali ni alama ya uchapakazi, uthubutu na mafanikio ya Watanzania wengi.

Amesema Kariakoo imekuwa sehemu iliyojenga maisha ya maelfu ya wananchi, huku vijana wengi wakianza biashara kwa mitaji midogo na baadaye kuwa waajiri wakubwa.

“Kila siku maelfu ya watu wanaingia Kariakoo kufanya biashara, kununua bidhaa, kuwekeza na kusafirisha bidhaa kwenda ndani na nje ya nchi ikiwemo DRC, Burundi, Rwanda, Zambia, Malawi, Uganda na Comoro,” amesema.

Mbwasi amesema Serikali imeendelea kuweka mazingira bora ya biashara, uwekezaji na viwanda ili wafanyabiashara waweze kushindana katika soko la kimataifa.

Akizungumzia ujenzi wa Soko Kuu la Kariakoo baada ya janga la moto, amesema Serikali ilihakikisha soko hilo linajengwa upya kwa kiwango kikubwa zaidi ambapo mradi huo uligharimu takribani shilingi bilioni 28 na kuwa na zaidi ya maduka 2,000.

Amesema Serikali inaamini sekta binafsi ni mshirika mkuu wa maendeleo ya uchumi, ndiyo sababu imeendelea kuboresha mazingira ya biashara, kurahisisha uwekezaji, kupanua miundombinu ya masoko na kuimarisha huduma za kidigitali.

Aidha, amewahakikishia wafanyabiashara kuwa Serikali itaendelea kusikiliza changamoto zao na kuhakikisha wanapata mazingira yenye utulivu, uwazi na usalama wa mitaji yao.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kariakoo Business Awards, Zakayo Shushu, amesema tuzo hizo zimeanzishwa kwa lengo la kutambua ubunifu, uwekezaji na juhudi za wafanyabiashara wanaofanya biashara kwa uaminifu na weledi mkubwa.

Amesema tuzo hizo zinalenga kukuza biashara zinazoaminika pamoja na kuchochea ushindani wa kitaalamu ili wafanyabiashara wa Kariakoo waweze kushindana katika soko la ndani na la kimataifa.

“Tunataka kujenga mazingira ya ushindani wa kimataifa na kuhakikisha wafanyabiashara wetu wanakuwa sehemu ya ushindani mkubwa wa biashara duniani,” amesema.

Shushu ameongeza kuwa ajenda nyingine muhimu ni kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi pamoja na kuhakikisha sauti ya mlaji inasikilizwa na kuthaminiwa.

Amesema kwa kushirikiana na Serikali, wadau wa maendeleo na sekta binafsi, wamepanga kuanzisha majukwaa mbalimbali yatakayoinua Kariakoo pamoja na uchumi wa Tanzania kwa ujumla.

Aidha, amebainisha kuwa kuna mikakati ya kuanzisha mafunzo kwa wafanyabiashara pamoja na kampeni maalumu za kuitangaza Kariakoo duniani kama kitovu muhimu cha biashara.

Amesema maboresho ya miundombinu ya biashara, mazingira ya uwekezaji pamoja na utatuzi wa changamoto za wafanyabiashara yameendelea kuongeza imani ya wafanyabiashara kwa Serikali yao.

Share:

Sunday, 17 May 2026

CCM YAONYA SIASA ZA MAJITAKA KUVURUGA MAENDELEO YA JAMII



CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimeonya tabia ya baadhi ya wananchi kuruhusu itikadi na mipasuko ya kisiasa kuingilia au kuharibu kasi ya maendeleo ya nchi, huku ikionya uwapo wa uchochezi unaopelekea uharibifu wa miundombinu na miradi mikubwa inayotekelezwa na serikali kwa ajili ya manufaa ya jamii.

Kauli hiyo imetolewa na Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC), Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa CCM, Kenani Kihongosi, alipokuwa akikagua mradi wa ujenzi wa Shule ya Sekondari ya Nyasariso iliyopo Kata ya Bunagi, Wilaya ya Tarime mkoani Mara, ikiwa ni sehemu ya mwendelezo wa ziara yake ya kikazi ya kukagua uhai wa chama na miradi ya maendeleo mkoani humo.

Akizungumza na wananchi pamoja na wanachama mara baada ya kukagua mradi huo, Kihongosi alisema kumekuwa na wimbi la baadhi ya watu kuendekeza chuki za kisiasa zinazowapelekea kushiriki au kushabikia uharibifu wa mali za umma, jambo ambalo ni kurudisha nyuma uchumi vya taifa.

Alisisitiza kuwa wananchi wa Tarime na Watanzania kwa ujumla wanapaswa kuwa walinzi wa kwanza wa shule, vituo vya afya na miundombinu ya nishati ya umeme, badala ya kuwa wepesi wa kubomoa kwa kufuata mihemko ya wanasiasa.

Kihongosi alibainisha kuwa siasa zinapaswa kufanyika kama uwanja wa kushindanisha hoja na sio jukwaa la kubomoa nchi, akionya kuwa athari za uharibifu huo haziichagui vyama vya siasa bali zinamgusa kila mwananchi.

Alitolea mfano kuwa kitendo cha kuchoma moto shule kinawaumiza watoto wa masikini wanaolazimika kurudi nyumbani, huku uharibifu wa vituo vya afya au kukatwa kwa nguzo za umeme ukisimamisha mnyororo mzima wa uzalishaji kiuchumi na kuhatarisha maisha ya wagonjwa.


Katika ziara hiyo, viongozi wa chama walipokea taarifa ya mradi kutoka kwa Mkuu wa Shule hiyo ya Sekondari ya Nyasariso, Paschal Sobu, ambaye alieleza kuwa shule hiyo ya mchanganyiko inayochukua wanafunzi wa kidato cha kwanza hadi cha sita imejengwa kwa gharama ya shilingi bilioni 1.6.


Sobu alifafanua kuwa katika kiasi hicho cha fedha, serikali kuu ilichangia shilingi bilioni moja wakati kiasi kilichobaki cha zaidi ya shilingi milioni 600 kikitokana na mapato ya ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya Tarime.


Mkuu huyo wa shule aliongeza kuwa miundombinu iliyopo inajumuisha madarasa 13, ofisi tano za walimu, jengo la utawala, maabara za kisasa za masomo ya kemia na baiolojia, bwalo la chakula pamoja na jiko la kisasa linalotumia nishati safi ya kupikia.


Alibainisha kuwa kwa sasa shule hiyo ina jumla ya walimu 13, wakiwemo wanaume 10 na wanawake watatu, kukiwa na mwalimu mmoja wa kujitolea anayelipwa kupitia ushirikiano wa karibu kati ya wazazi na halmashauri hiyo.
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger