Thursday, 11 June 2026

GAVANA TUTUBA: MIGOGORO YA MASHARIKI YA KATI YAONGEZA CHANGAMOTO ZA KIUCHUMI SADC


MAGAVANA wa Benki Kuu za nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) wamekutana jijini Dar es Salaam kujadili mikakati ya kukabiliana na changamoto za kiuchumi zinazoendelea kujitokeza duniani, huku migogoro ya kimataifa na mfumuko wa bei vikitajwa kuwa miongoni mwa vihatarishi vikubwa vya ukuaji wa uchumi wa ukanda huo.

Akizungumza katika mkutano huo leo Juni 11, 2026 Jijini Dar es Salaam, Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Bw. Emmanuel Tutuba, amesema ukanda wa SADC unakabiliwa na mazingira magumu ya kiuchumi yanayochochewa na migogoro inayoendelea Mashariki ya Kati, hali inayohitaji nchi wanachama kuratibu kwa karibu sera zao za fedha na uchumi.

“Tumekutana katika kipindi ambacho ukanda wetu unakabiliwa na changamoto kubwa za kiuchumi zinazosababishwa na migogoro inayoendelea Mashariki ya Kati. Mkutano huu unatupatia fursa ya kutafakari kwa pamoja changamoto hizi na kuratibu mikakati ya kukabiliana nazo nchini Tanzania na katika ukanda wetu kwa ujumla,” amesema Bw. Tutuba.

Mkutano huo uliwakutanisha magavana wa benki kuu na maafisa wakuu wa sera za fedha kutoka nchi 16 wanachama wa SADC kwa lengo la kupitia mwenendo wa uchumi wa ukanda na kujadili hatua za kukabiliana na hatari mpya zinazoweza kuathiri maendeleo ya kiuchumi.

Majadiliano yamejikita katika kudumisha uthabiti wa bei, kuboresha mifumo ya malipo, kuimarisha ukwasi wa sekta ya benki na kuongeza upatikanaji wa mikopo nafuu kwa wananchi na sekta binafsi ili kuchochea ukuaji wa uchumi.

Aidha, nchi wanachama zimeendelea kutekeleza hatua za pamoja za kikanda pamoja na sera mahsusi za kitaifa zinazolenga kupunguza athari za changamoto za kiuchumi na kulinda ustahimilivu wa mifumo ya kifedha.

Bw. Tutuba alisema benki kuu za SADC zitaendelea kushirikiana katika kuboresha mifumo ya malipo, kuimarisha huduma za kifedha na kutumia teknolojia za kisasa ili kuongeza ufanisi wa sekta ya fedha na kusaidia ukuaji endelevu wa uchumi katika ukanda huo.

Licha ya changamoto zinazoikabili dunia kwa sasa, uchumi wa Tanzania umeendelea kuonyesha uimara. Sekta ya fedha imeendelea kuwa thabiti na salama, hali inayosaidia kupunguza athari za mishtuko ya kiuchumi kutoka nje ya nchi.

Kwa mujibu wa takwimu zilizowasilishwa katika mkutano huo, uchumi wa Tanzania ulikua kwa asilimia 5.2 mwaka jana na unatarajiwa kukua kwa asilimia 6.3 mwaka huu kutokana na uwekezaji unaoendelea pamoja na misingi imara ya uchumi wa taifa.

Hata hivyo, viongozi hao walibainisha kuwa pamoja na mfumuko wa bei kubaki ndani ya kiwango kinacholengwa na Benki Kuu, bado kuna umuhimu wa kuendelea kuchukua hatua za kuhakikisha ukuaji wa uchumi unaenda sambamba na uthabiti wa bei.

Kwa upande wa ukanda wa SADC, mkutano huo unatarajiwa kuibua mikakati ya pamoja ya kudhibiti mfumuko wa bei, kuimarisha mifumo ya malipo, kupanua huduma za kifedha na kuongeza upatikanaji wa mikopo nafuu huku ukihakikisha uthabiti wa sekta ya fedha unaendelea kulindwa.

Washiriki pia wanajadili namna ya kuharakisha matumizi ya teknolojia za malipo kidijitali na kuimarisha ushirikiano katika huduma za kifedha ili kusaidia ujumuishaji wa uchumi na biashara ndani ya ukanda wa SADC.

Mkutano huo umefanyika sambamba na maadhimisho ya miaka 60 ya Benki Kuu ya Tanzania, hatua inayotambua mchango wake katika usimamizi wa sera za fedha, maendeleo ya sekta ya fedha na mageuzi ya mifumo ya malipo yaliyosaidia kuongeza ujumuishaji wa kifedha na ufanisi wa miamala nchini.
Share:

TANZANIA NA CANADA ZAIMARISHA USHIRIKIANO KATIKA KUENDELEZA HAKI ZA WATU WENYE ULEMAVU

Na Mwandishi Wetu-New York,Marekani

Tanzania na Canada zimejadili fursa za kuimarisha ushirikiano katika kukuza haki, ujumuishwaji na ustawi wa watu wenye ulemavu katika kikao cha pande mbili kilichofanyika Juni 10, 2026 katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa New York, Marekani, pembezoni mwa Mkutano wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (COSP19).

Kikao hicho kiliwakutanisha Naibu Waziri wa Maendeleo ya jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum kutoka Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi na Katibu wa Bunge anayeshughulikia Masuala ya watu wenye Ulemavu Mhe. Leslie Church kutoka Canada pamoja na viongozi na wataalamu mbalimbali wa masuala ya watu wenye ulemavu kutoka pande zote mbili.

Akizungumza katika kikao hicho,Mhe. Mahundi ameeleza kuwa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 imeweka kipaumbele katika kujenga taifa jumuishi ambapo watu wenye ulemavu wanatambuliwa kama wadau muhimu wa maendeleo na wanapewa fursa sawa katika elimu, afya, ajira na kinga ya jamii. 

Pia, Pande hizo mbili zilijadiliana kuhusu namna ya kuimarisha ajira kwa watu wenye ulemavu, ambapo Tanzania ilieleza utekelezaji wa Sheria ya Watu Wenye Ulemavu ya mwaka 2010 inayotaka waajiri wenye wafanyakazi 20 au zaidi kuhakikisha angalau asilimia tatu ya watumishi wao ni watu wenye ulemavu na wenye sifa stahiki. 

Kwa Upande wake, Mhe. Leslie Church ameishauri Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania juu ya Uimarishwaji wa mifumo ya kinga ya jamii, uwezeshaji wa kiuchumi kwa watu wenye ulemavu na utoaji wa elimu kwa umma juu ya aina zote za ulemavu na uwezo wa kundi hili, hali itakayosaidia kuepuka unyanyapaa kwa watu wenye ulemavu ili kuimarisha maisha huru na kuongeza fursa za kiuchumi kupitia mafunzo ya ujuzi, mikopo na programu za kinga ya jamii.

Katika majadiliano hayo, Tanzania na Kanada zilionesha nia ya kuendelea kushirikiana katika maeneo ya uboreshaji wa sheria na viwango vya upatikanaji wa huduma kwa watu wenye ulemavu, ukusanyaji wa takwimu, utekelezaji wa sera na sheria za watu wenye ulemavu pamoja na programu za ajira jumuishi.

Kikao hicho kilihitimishwa kwa pande zote mbili kueleza utayari wa kuimarisha ushirikiano na kubadilishana uzoefu ili kuhakikisha haki za watu wenye ulemavu zinatambuliwa, kulindwa na kutekelezwa kikamilifu kwa manufaa ya jamii jumuishi na endelevu.


Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO ALHAMISI JUNI 11, 2026

Magazetini Leo
 

Share:

Wednesday, 10 June 2026

TANZANIA YAIELEZEA DUNIA HATUA ZILIZOPIGWA KATIKA KULINDA HAKI ZA WATU WENYE ULEMAVU


Na Mwandishi wetu-New York, Marekani.


Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi, ameieleza Jumuiya ya Kimataifa hatua kubwa zinazochukuliwa na Serikali ya Tanzania katika kulinda na kuendeleza haki za watu wenye ulemavu, wakati aliposhiriki Mkutano wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (COSP19) unaofanyika katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, Jijini New York, Marekani.

Mhe. Mahundi, ambaye amemuwakilisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Sera, Bunge na Uratibu na Wenye Ulemavu, Mhe. Profesa Palamagamba John Kabudi, amesema Tanzania imeendelea kuimarisha mifumo ya kisheria, kisera na kiutendaji ili kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata haki, fursa na huduma stahiki kama wananchi wengine.

Akiwasilisha taarifa ya nchi, Mhe. Mahundi amesema Tanzania imepiga hatua kubwa kupitia Sheria ya Watu Wenye Ulemavu Na. 9 ya mwaka 2010 kwa Tanzania Bara pamoja na Sheria Na. 8 ya mwaka 2022 ya Zanzibar, ambazo zimeweka msingi imara wa kulinda haki na ustawi wa watu wenye ulemavu.

“Masuala ya ulemavu yamejumuishwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na mipango mbalimbali ya maendeleo ili kuhakikisha hakuna anayebaki nyuma katika safari ya maendeleo ya taifa na kusema kuwa Serikali imeendelea kupanua upatikanaji wa elimu jumuishi, huduma za afya, huduma za urekebishaji na tiba, teknolojia saidizi, programu za uwezeshaji kiuchumi pamoja na huduma za hifadhi ya jamii kwa watu wenye ulemavu” amesema Mhe. Mahundi.

Aidha Mhe. Mahundi amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa uongozi wake madhubuti na dhamira ya dhati ya kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata huduma bora na fursa zinazowawezesha kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya nchi.

“Serikali ya Tanzania itaendelea kushirikiana na nchi wanachama, Umoja wa Mataifa, asasi za kiraia na watu wenye ulemavu wenyewe katika kuharakisha utekelezaji wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu na kujenga jamii jumuishi inayoheshimu usawa, utu na haki za kila mtu,” amesema Mhe. Mahundi.

Mkutano huo wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu umebeba kaulimbiu inayosema “CRPD at 20: Celebrating and Consolidating Achievements and Shaping the Next Phase of Implementation in a Changing World,” ukilenga kutathmini mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha miaka 20 tangu kuanzishwa kwa mkataba huo na kuweka mikakati ya kuendeleza utekelezaji wake duniani.
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger