Saturday, 20 June 2026

TBS YATIMIZA MIAKA 50, YAWEKEWA MKAKATI WA KUONGOZA UBORA AFRIKA



Na mwandishi wetu, Dodoma

Shirika la Viwango Tanzania (TBS) limepongezwa kwa mafanikio makubwa yaliyopatikana katika kipindi cha miaka 50 tangu kuanzishwa kwake, huku likitakiwa kuendelea kwenda sambamba na maendeleo ya teknolojia na mabadiliko ya soko la dunia ili kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania kimataifa.

Pongezi hizo zimetolewa na Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga,wakati wa maadhimisho ya kilele cha miaka 50 ya shirika hilo yaliyofanyika katika ofisi zake zilizopo Njedengwa jijini Dodoma, sambamba na uzinduzi wa kitabu kinachoelezea historia, mafanikio na mchango wa taasisi hiyo katika kukuza ubora wa bidhaa na huduma nchini.

Waziri Kapinga amesema TBS imekuwa nguzo muhimu katika kulinda afya na usalama wa wananchi kupitia usimamizi wa viwango vya bidhaa mbalimbali, huku ikichangia kwa kiasi kikubwa ukuaji wa sekta za uzalishaji, biashara na viwanda nchini.

Ameeleza kuwa katika kipindi hiki ambacho dunia inaendelea kubadilika kwa kasi kupitia teknolojia na ubunifu, TBS inapaswa kuwa na dhana ya kujitegemea zaidi kwa kuimarisha mifumo ya kisasa ya utoaji huduma na kuongeza uwezo wake wa kitaalamu ili kukidhi mahitaji ya soko la ndani na nje ya nchi.

"Tunapoadhimisha miaka 50 ya TBS, tunashuhudia mchango mkubwa wa taasisi hii katika kujenga imani ya bidhaa za Tanzania. Hata hivyo, ni muhimu kuendelea kuwekeza katika teknolojia, ubunifu na ushirikiano na sekta binafsi ili kuhakikisha bidhaa zetu zinakidhi viwango vya kimataifa," amesema Kapinga.

Aidha, Waziri huyo amesisitiza umuhimu wa TBS kuendelea kufanya kazi kwa karibu na sekta binafsi ili kuongeza ubora wa bidhaa zinazozalishwa nchini na kusaidia kutafsiri kwa vitendo maono ya Tanzania ya kuwa taifa lenye uchumi wa viwanda unaozalisha bidhaa zenye ushindani mkubwa katika masoko ya kikanda na kimataifa.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Dkt. Ashura Katunzi,amesema maadhimisho hayo ni fursa ya kutathmini mafanikio yaliyofikiwa na kuweka mikakati mipya ya kuifanya taasisi hiyo kuwa ya kisasa zaidi na yenye uwezo mkubwa wa kukabiliana na changamoto za karne ya 21.

Dkt. Katunzi amesema TBS itaendelea kuimarisha maabara za kisasa, kuongeza matumizi ya teknolojia za kidijitali na kuwekeza katika rasilimali watu ili kuhakikisha huduma za viwango zinakuwa bora zaidi, za haraka na zenye kuaminika.

"TBS inatambua kuwa dunia inabadilika kwa kasi kubwa, huku teknolojia na mazingira ya biashara vikibadilika, hivyo shirika hilo linapaswa kuendelea kuwa imara, bunifu na lenye uwezo wa kujibu changamoto mpya zinazoibuka."aamesema Dkt. Katunzi

Amebainisha kuwa kwa kipindi cha nusu karne, TBS imekuwa mhimili muhimu wa maendeleo ya viwanda na biashara nchini kwa kuhakikisha bidhaa zinazozalishwa na kuuzwa zinazingatia viwango vinavyotakiwa, jambo ambalo limeongeza imani ya walaji na kufungua fursa za biashara katika masoko mbalimbali duniani.

Naye Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo, Mariam Ditopile Mzuzuri, amesema TBS imekuwa mhimili muhimu katika kulinda maslahi ya walaji, kuimarisha ushindani wa bidhaa za Tanzania na kuchochea ukuaji wa sekta za uzalishaji nchini.

Ditopile amesema ipo haja ya kufanyika kwa mapitio ya kina ya Sera ya Ubora wa Bidhaa ili iweze kuakisi mabadiliko makubwa yaliyotokea katika nyanja za sayansi, teknolojia, biashara na uzalishaji tangu sera hiyo ilipoanzishwa.

"Tunapoipongeza TBS kwa mafanikio ya miaka 50, ni muhimu pia kuangalia mbele na kufanya maboresho yatakayoiwezesha taasisi hii kuendelea kuwa nguzo ya maendeleo ya viwanda, biashara na kilimo katika mazingira ya sasa ya kiteknolojia," amesema Ditopile.

Ditopile amesema imejijengea rekodi ya kuwa taasisi muhimu katika kuhakikisha bidhaa zinazozalishwa, kuuzwa na kutumiwa nchini zinakidhi viwango vinavyotakiwa kwa ajili ya kulinda afya, usalama na maslahi ya watumiaji.

Naye Katibu Mkuu wa Shirikisho la Viwango Afrika (ARSO), Dkt. Hermogene Nsengimana, amesema Julai 2026 Tanzania itakuwa nchi ya saba barani Afrika kupata Alama ya Ubora ya Afrika (Africa Quality Mark) kwenye bidhaa zake.

Amesema kwa hatua hiyo, Tanzania itaungana na Rwanda, Togo, Senegal, Ethiopia, Nigeria na Zimbabwe katika nchi zinazotumia alama hiyo ya ubora inayolenga kuimarisha viwango vya bidhaa barani Afrika.

Amesema Shirikisho la Viwango Afrika limekwisharatibu na kuoanisha takribani viwango 2,600 vinavyolenga sekta za kipaumbele ikiwemo usindikaji wa mazao ya kilimo, sekta ya magari, dawa na bidhaa za afya, usafirishaji na ugavi, pamoja na nguo na bidhaa za ngozi.

Ameeleza kuwa kwa sasa takribani bidhaa 500 katika ngazi ya Afrika zinapitiwa ili kupata Alama ya Ubora ya Afrika, hatua itakayosaidia kurahisisha biashara ndani ya Eneo Huru la Biashara la Afrika (AfCFTA).

Amesema bidhaa za Tanzania ambazo kwa sasa zinabeba alama ya TBS, zitapata fursa ya kuwekewa alama ya ubora ya Afrika, jambo litakaloongeza ushindani na upatikanaji wa masoko katika nchi mbalimbali za bara hilo.


Share:

CCM HAIHESHIMU KURA ZA MAONI?

 

Kila baada ya miaka mitano taifa letu hufanya uchaguzi wa kupata viongozi katika ngazi mbalimbali, ikiwemo wenyeviti wa vijiji na vitongoji, madiwani, wabunge na nafasi ya Rais wa nchi. Hivyo, kila chama cha siasa kina utaratibu wa kuwapata wawakilishi watakaopeperusha bendera ya chama husika.

CCM kama chama cha siasa kina utaratibu wa kufanya kura za maoni kwa watia nia wote. Hiki ni kipimo kimojawapo kinachowezesha na kurahisisha maamuzi ya vikao vya uteuzi wa mwisho ambao hufanywa na Halmashauri Kuu ya CCM Taifa.

MUUNDO WA CHAMA CHA MAPINDUZI

CCM mfumo wake wa kitaasisi umeanzia ngazi ya Shina hadi Taifa, na kila eneo la kiuongozi lina mamlaka sawia kwa mujibu wa Katiba ya CCM ya mwaka 1977.

SHINA ➜ TAWI ➜ KATA/WADI ➜ WILAYA ➜ MKOA ➜ TAIFA

MFUMO WA UONGOZI

Kila eneo lina mfumo wa uongozi ambao huchaguliwa kila baada ya miaka mitano na hili lina dhihirisha kuwa CCM ni chama cha siasa kinachoishi falsafa ya demokrasia ya kijamaa.

UONGOZI

➤ Mwenyekiti

➤ Katibu

➤ Katibu Mwenezi

➤ Wajumbe

Huu mfumo wa uongozi unaoanzia ngazi ya Tawi mpaka Taifa una mamlaka na majukumu yaliyoainishwa kwenye Katiba na Kanuni za CCM, ikiwemo Kanuni ya Uongozi na Maadili ya CCM.

HAKI ZA MWANACHAMA WA CCM

✓ Haki ya kuomba kuchaguliwa.

✓ Haki ya kuhudhuria na kutoa maoni.

✓ Haki ya kujitetea au kutoa maoni mbele ya kikao.

✓ Haki ya kumuona kiongozi kwa kufuata utaratibu.

SIFA ZA MWANA CCM

➤ Mtu anayeheshimu watu.

➤ Mtu anayependa kushirikiana na watu.

➤ Mtu mwenye kuamini kuwa kazi ni kipimo cha utu.

➤ Atalipa ada ya uanachama na kutoa michango.

➤ Mtu mwenye kujielimisha na kutumia elimu hiyo kwa manufaa ya umma.

➤ Mtu mwenye kuridhika na asiye penda vyeo na kujirimbikizia mali.

MAMLAKA YA VIKAO VYA MAAMUZI VYA CCM

Mfumo wa kihierakia wa kimamlaka unaofuatwa na CCM katika kufanya maamuzi ni kama ifuatavyo:

TAWI

Mkutano Mkuu wa Tawi ndiyo kikao chenye mamlaka ya juu katika shughuli za chama katika ngazi ya Tawi. Mfano, humchagua Mwenyekiti wa Tawi. Vikao vingine ni Kamati ya Siasa ya Tawi na Halmashauri Kuu ya Tawi.

KATA/WADI

Mkutano Mkuu wa Kata ndiyo kikao chenye mamlaka ya juu katika shughuli za siasa katika ngazi ya Kata, ikiwemo kumchagua Mwenyekiti wa CCM Kata.

WILAYA

Mkutano Mkuu wa Wilaya ndiyo kikao cha juu chenye mamlaka ya mwisho ya kimaamuzi, ikiwemo kumchagua Mwenyekiti wa CCM Wilaya.

MKOA

Ngazi ya Mkoa, Mkutano Mkuu wa CCM Mkoa ndiyo kikao cha juu cha maamuzi katika Mkoa chenye mamlaka ya kumchagua Mwenyekiti wa CCM Mkoa.

TAIFA

Kitaifa, CCM kimuundo ndiyo mamlaka ya mwisho ya kimaamuzi yenye wajibu wa kusimamia na kutoa maamuzi ya mwisho kuhusu kila jambo katika ngazi za chini.

VIKAO VYA CCM TAIFA

✓ Kikao cha Sekretarieti

Kikao hiki kinaundwa na:

➤ Katibu Mkuu wa CCM Taifa.

➤ Katibu wa Itikadi, Siasa na Mafunzo Taifa.

➤ Makatibu wa Jumuiya zote za CCM.

➤ Wakuu wa Idara za CCM Makao Makuu.

Jukumu kuu la Sekretarieti ni kuandaa na kuchakata agenda na shughuli za kiutendaji za CCM.

KAMATI KUU YA CCM TAIFA (CC)

Hiki ni kikao kinachoongozwa na Mwenyekiti wa CCM Taifa chenye mamlaka ya kuchambua kwa kina agenda za CCM na kuziwasilisha katika kikao cha Halmashauri Kuu ya CCM Taifa.

HALMASHAURI KUU YA CCM TAIFA (NEC)

Hiki ni kikao cha maamuzi kinachoundwa na wajumbe wa NEC.

Mamlaka ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa:

✓ Kuteua wagombea wa nafasi mbalimbali za chama na za dola ikiwemo wabunge, wenyeviti wa CCM wa mikoa na wilaya pamoja na viongozi wa jumuiya za CCM Taifa.

✓ Kusimamia itikadi na mwenendo wa CCM.

✓ Kusimamia utekelezaji wa Ilani ya CCM.

✓ Kupendekeza kwa Mkutano Mkuu wa CCM Taifa majina yasiyozidi matatu ya wanachama wanaogombea nafasi ya Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Hivyo, jukumu la mwisho la uteuzi wa wagombea wa ubunge, wenyeviti wa mikoa na wilaya ndani ya CCM kwa mujibu wa Katiba linafanywa na Halmashauri Kuu ya CCM Taifa.

MKUTANO MKUU WA CCM TAIFA

Hiki ndicho kikao kikuu cha CCM kupita vyote chenye mamlaka na madaraka ya mwisho ya kimaamuzi ya CCM.

✓ Kupanga siasa ya CCM na kusimamia utekelezaji wa shughuli zote za CCM.

✓ Kupokea taarifa na kufikiria taarifa ya kazi za CCM iliyotolewa na Halmashauri Kuu ya CCM Taifa na kutoa maelekezo ya mipango na utekelezaji wa siasa ya CCM.

✓ Kuandika Katiba au kuthibitisha mabadiliko ya vifungu vya Katiba ya CCM.

HUU NDIO MCHAKATO WA KURA ZA MAONI NDANI YA CCM

➤ Zoezi la kuchukua fomu, kuzijaza na kuzirejesha.

➤ Vikao vya Kamati za Siasa za Kata na Wilaya huketi na kupitia fomu zote na kutoa mapendekezo kwa vikao vya juu.

➤ Vikao vya Kamati za Siasa za Mkoa huketi na kupitia fomu zote pamoja na mapendekezo kutoka ngazi za chini.

➤ Kamati ya Siasa ya CCM Mkoa hupendekeza majina ya watia nia wa nafasi ya Udiwani watakaopigiwa kura za maoni katika Kata.

➤ Kikao cha Kamati ya Siasa Mkoa hutoa mapendekezo kwa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa kuhusu watia nia wa Ubunge.

➤ Sekretarieti ya CCM Taifa huchakata mapendekezo yote na kuyawasilisha Kamati Kuu na hatimaye Halmashauri Kuu ya CCM Taifa.

➤ Halmashauri Kuu ya CCM Taifa huteua majina matatu au zaidi yatakayopigiwa kura za maoni.

➤ Katibu wa NEC hutangaza majina ya walioteuliwa na kutoa maelekezo ya hatua zinazofuata.

BAADA YA KURA ZA MAONI

Ifahamike kuwa CCM hufuata kanuni na taratibu zote kwa mujibu wa miongozo na maadili yake katika kupata wagombea wa nafasi za dola.

VIKAO BAADA YA KURA ZA MAONI KWA NAFASI YA UDIWANI

➤ Kikao cha Kamati ya Siasa ya CCM Kata hutoa mapendekezo kwa kuzingatia matokeo ya kura za maoni.

➤ Kikao cha Kamati ya Siasa ya CCM Wilaya hujadili sifa za kila mgombea na kutoa mapendekezo kwa Mkoa.

➤ Halmashauri Kuu ya CCM Mkoa hupendekeza na kuteua jina moja miongoni mwa waliopigiwa kura za maoni.

VIKAO AWAMU YA PILI KWA NAFASI YA UBUNGE

➤ Kamati ya Siasa ya Wilaya hupitia na kutoa mapendekezo kwa kila aliyepigiwa kura za maoni.

➤ Kamati ya Siasa ya Mkoa hupitia na kuwasilisha mapendekezo kwa vikao vya Taifa.

➤ Kamati Kuu na Halmashauri Kuu ya CCM Taifa huteua jina moja miongoni mwa waliopigiwa kura za maoni.

Kwa msingi huu, yeyote aliyepigiwa kura za maoni ana nafasi ya kuteuliwa bila kujali idadi ya kura alizopata.

KURA ZA MAONI NA UTEUZI WA WAGOMBEA NDANI YA CCM

Kwanini kura za maoni?

✓ Kushirikisha wanachama katika maamuzi ya chama.

✓ Kuishi falsafa ya demokrasia ya kijamaa ya CCM.

✓ Kutathmini ukubalifu wa mtia nia katika jimbo, kata au wadi.

✓ Kuongeza uelewa wa watia nia kuhusu matakwa ya wanachama na wananchi.

✓ Kuongeza uimara wa chama katika ngazi za mashinani.

✓ Kurahisisha vikao vya maamuzi kwa kuwa na taarifa sahihi za watia nia.

JE, KURA ZA MAONI NDIZO KIGEZO PEKEE?

Kwa ujumla, kuna vigezo vingine vinavyozingatiwa, ikiwemo:

➤ Idadi ya kura za maoni alizopata.

➤ Maadili ya mtia nia.

➤ Uzoefu wa siasa za chama na serikali.

➤ Ukubalifu wa mtia nia kwa jamii ya eneo husika.

➤ Mchango wa hiari katika kazi za chama.

HITIMISHO

Ni dhahiri kwamba CCM kwa hapa Tanzania ndiyo chama pekee cha siasa chenye utaratibu mpana wa kupata wagombea katika nafasi mbalimbali za uongozi kwa kuwashirikisha wanachama wake.

Pia, kila mwana CCM ni muhimu akafahamu kuwa utaratibu wa uteuzi unaofanywa na Halmashauri Kuu ya Taifa hautegemei kigezo kimoja cha idadi ya kura za maoni pekee, bali huzingatia taarifa na vigezo mbalimbali.

Itikadi ya Ujamaa na Kujitegemea ndiyo nguzo muhimu katika kuijenga CCM.

Kila mwanachama ajitahidi kujielimisha kuhusu mfumo wa chama na namna unavyofanya kazi ili kuepusha sintofahamu zinazoweza kujitokeza baada ya kura za maoni.

Kura za maoni siyo uteuzi, bali ni mchakato wa kuelekea uteuzini. Uteuzi hufanywa na mamlaka na vikao vya kikanuni vya CCM katika kila ngazi.

MAKALA HII IMEANDIKWA NA:

JOHN FRANCIS HAULE

MKUU WA SOKO LA SAMUNGE, JIJINI ARUSHA

SIMU: 0756717987 AU 0711993907


Share:

MAGAZETI YA LEO JUMAMOSI JUNI 20, 2026

Magazetini Leo 








              
Share:

Friday, 19 June 2026

DC NGUBIAGAI ATEKELEZA AGENDA YA RAIS SAMIA YA UHIFADHI WA RASILIMALI, ZANA HARAMU ZA SH. MILIONI 73.6 ZATEKETEZWA UKEREWE

Mkuu wa Wilaya ya Ukerewe Cde. Christopher Ngubiagai akihutubia wananchi wa Gana katika mkutano
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe Ndg. Vicent Mbua akizungumza na wananchi wa Gana kuachana na uvuvi haramu

Na Mwandishi Wetu - Ukerewe

Mikakati ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ya kuimarisha usimamizi wa rasilimali za taifa na kuhakikisha sekta ya uvuvi inachangia kikamilifu ukuaji wa uchumi inaendelea kuzaa matunda, ambapo Wilaya ya Ukerewe imeendelea kuchukua hatua madhubuti dhidi ya uvuvi haramu.

Katika kuonesha dhamira hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Ukerewe, Christopher Ngubiagai, Juni 18, 2026 ameongoza operesheni ya kuteketeza zana haramu za uvuvi zenye thamani ya Shilingi milioni 73,615,000 katika Kisiwa cha Gana, Kijiji cha Kamasi, Kata ya Ilangala.

Hatua hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya Serikali ya kuhakikisha rasilimali za Ziwa Victoria zinalindwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho sambamba na kuimarisha uchumi wa wananchi wanaotegemea sekta ya uvuvi.

Akizungumza katika tukio hilo, Cde. Ngubiagai amesema Serikali haitamvumilia mtu yeyote atakayejihusisha na uvuvi haramu unaoharibu mazalia ya samaki na kuhatarisha ustawi wa sekta hiyo muhimu kiuchumi.

Aidha, amewahimiza wananchi kuachana na mbinu haramu za uvuvi na badala yake kutumia fursa zilizopo katika kuongeza thamani ya mazao ya samaki kupitia usindikaji, uhifadhi bora na biashara endelevu, hatua itakayochochea ukuaji wa uchumi wa kaya na taifa kwa ujumla.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe, Vicent Mbua, amewapongeza wananchi na wajumbe wa kamati kwa ushirikiano mkubwa wanaoendelea kuutoa katika mapambano dhidi ya uvuvi haramu.

Mbua amesema ushirikiano huo unaendana na dhamira ya Serikali ya kuhakikisha sekta ya uvuvi inakuwa endelevu na yenye tija kwa maendeleo ya wananchi na taifa.

Amesema halmashauri itaendelea kusimamia kikamilifu utekelezaji wa sheria za uvuvi ili kulinda mapato ya halmashauri na kuhakikisha wananchi wanapata samaki bora na wa kutosha.

"Kila mvuvi anapaswa kuzingatia sheria zinazomuongoza katika shughuli zake. Serikali itaendelea kudhibiti uvuvi haramu unaoharibu mazalia ya samaki na kuhatarisha uchumi wa wananchi," amesema Mbua.

Katika taarifa yake, Katibu wa Mwalo wa Gana, Charles Gunda, amesema zana zilizoteketezwa ni pamoja na timba pisi 1,627 na nyavu za makira inchi tatu pisi 80.

Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Ilangala, Petro Majura, ameonya kuwa hatua kali za kisheria zitaendelea kuchukuliwa dhidi ya wote watakaobainika kujihusisha na vitendo vya uvuvi haramu.

Naye Mkuu wa Idara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi wa Halmashauri hiyo, Godfrey Ayako, amesema Serikali inaendelea kutatua changamoto mbalimbali katika sekta ya uvuvi ikiwemo suala la upimaji wa mizigo ya dagaa ili kuongeza ufanisi na tija kwa wavuvi.

Sambamba na juhudi hizo, Cde. Ngubiagai amewahimiza wananchi kuunda na kusajili vikundi ili waweze kunufaika na mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na halmashauri, hatua inayodhihirisha dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kuwawezesha wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kiuchumi.

Hatua hizi zinaendelea kuonesha namna Serikali ya Rais Samia ilivyodhamiria kulinda rasilimali za taifa, kuimarisha uchumi wa buluu na kuhakikisha wananchi wanashiriki kikamilifu katika safari ya maendeleo ya Taifa.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO IJUMAA JUNI 19,2026

Magazeti





Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger