Friday, 1 May 2026

RAIS SAMIA: MSIDANGANYIKE, HAKUNA USTAWI BILA AMANI NA UTULIVU WA TAIFA

  

Rais Samia Suluhu Hassan amewataka wafanyakazi nchini kote kudumisha amani na utulivu akisisitiza kuwa hakuna ustawi wa mfanyakazi unaoweza kupatikana bila kuwepo kwa utulivu wa taifa. 

Aidha amewataka wafanyakazi nchini kuendelea kuchapa kazi na kwamba serikali itaboresha maslahi yao kadri uchumi unavyoendelea kuimarika.

Akizungumza mkoani Njombe kwenye maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi (Mei Mosi), Rais alibainisha kuwa ni wajibu wa kila mmoja kuhakikisha tofauti zilizopo hazigeuki kuwa sababu ya kuhatarisha misingi ya umoja na mshikamano iliyoachwa na waasisi wa taifa.

“Sasa ni wajibu wetu kuhakikisha kwamba tofauti zetu hazigeuki kuwa sababu ya kuhatarisha misingi ya amani, umoja na mshikamano tulioachiwa na waasisi wetu, tushikamaneni tufanye kazi, tujenge taifa letu na tujenge heshima ya nchi yetu,” alisema.

Alisisitiza kuwa kazi zenye staha ni nguzo imara kwa maendeleo kuelekea Dira ya Taifa 2050 na kuwataka Watanzania kushikamana katika kuijenga heshima ya nchi.

Katika hatua nyingine, Rais Samia alieleza namna Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi nchini (TUCTA) wakiongozwa na Rais wa Shirikisho  hilo, Tumaini Nyamhokya walivyompa pole kwenye kikao chao cha pamoja na kumtaka Rais achape kazi, wafanyakazi mwaka huu watafunga mkanda kutokana na mambo iliyopitia nchi baada ya uchaguzi.  lilivyompa pole kwa mambo mazito ambayo nchi imepitia.

“Katika kikao kile walikuja kunipa pole (Tucta)… hawakuwa na madai mapya waliniambia ‘mama wewe chapa kazi tutakuja kukudai mwakani,’ na mimi nikawaambia mwakani ikiwa tutachapa kazi na uchumi utakuwa kwa kiwango kinachoridhisha tutakuja kuangaliana”.

“Nataka niwahakikishie kwamba pamoja na changamoto zilizopo kadri uchumi unavyoendelea kuimarika tutaboresha maslahi ya wafanyakazi wetu, nawaomba tuendelee kuchapa kazi kwa bidii, weledi na uzalendo wa hali ya juu, kwa kufanya hivyo tutaendelea kukuza uchumi wa nchi yetu na kugawana vizuri ile keki ya taifa kama matunda na juhudi ya jasho letu,” alisema.

Alisema serikali ilitumia kiasi kikubwa cha fedha kwenye uchaguzi mkuu kwa vile uligharamiwa na serikali na kwa uharibifu uliotokea baada uchaguzi, kila fedha inayopatikana inatumika kwenye kurekebisha mali zilizoharibiwa na miundombinu iliyoharibiwa na mvua zinazoendelea kunyesha na kulipa madeni ya wafanyakazi na wakandarasi ili utakapoanza utekelezwaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 uanze kukiwa na mwelekeo mzuri unaoleweka. 

“Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya kazi na maslahi ya watumishi kwa kadri uchumi utakavyoruhusu, tutaendelea kuchukua hatua zaidi za kuimarisha ustawi wa wafanyakzi na kwa hivyo ndugu zangu chapeni kazi serikali ipo inawasikiliza na inawathamani,” alisema.Licha ya kuyumba kwa uchumi duniani, Rais Samia amewahakikishia wafanyakazi kuwa serikali inathamini mchango wao na itaendelea kuboresha maslahi yao kadri hali ya kifedha itakavyotengamaa. 

Aidha Rais alieleza kwa ufupi mambo makubwa yaliyofanywa katika kipindi cha pili cha serikali ya Awamu ya Sita katika sekta ya kazi ni kutoa ajira 12,000 za ndani katika sekta ya umma ajira 12,000...“hii ni kwa ujumla mbali na ambazo zimetangazwa na watu wanaendelea kuomba,” alisema. 

“Lingine serikali imeendelea kuratibu upatikanaji wa ajira nje ya nchi na vijana wa kitanzania 7,593 tumewapatia ajira nje ya nchi, mipango ya kutafuta fursa zaidi za ajira nje ya nchi inaendelea ili kupunguza changamoto za ajira kwa vijana wetu… na katika hili nakubaliana na Tucta kwamba tunahitaji kuwa na utaratibu wa wazi na usimamizi madhubuti wa Watanzania wanaokwenda kufanya kazi nje ili kuhakikisha haki na maslahi yao yanalindwa ipasavyo,” alisema.

Aliishukuru Tucta kuanzisha kitengo maalumu cha kushughulikia masuala hayo na kuilekeza Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano kuratibu na kusimamia kikamilifu suala hilo kwa kushirikiana na Wizara ya Mambo ya Nje na balozi.

“...kuratibu na kuharakisha…  najua kuna maombi mengi kutoa nje wanataka wafanyakazi kwa hiyo mratibu na muharakishe vijana wetu wapate kazi nje lakini msimamie maslahi yao,” alisema. 

Vilevile, Rais Dkt. Samia amesema Serikali itaendelea kuweka mkazo katika kukuza ujuzi,hususan kwa vijana, ili kuwaandaa Watanzania kushiriki kikamilifu katika uchumi wa kisasa unaohitaji maarifa, teknolojia na ubunifu.

“Dhamira ya Serikali ni kuona kila mfanyakazi anafanya kazi katika mazingira salama, yenye heshima, haki na yanayomwezesha kuchangia kikamilifu katika ujenzi wa Taifa,”amesema Rais Dkt. Samia.

Kwa upande wa Waziri Mkuu Dk Mwigulu Nchemba aliyekuwepo kwenye sherehe hizo, aliwataka wafanyakazi kutokana tamaa na badala yake wawe wavumilivu wanapokuwa maeneo ya kazi.  

Akiwasilisha Risala kwa niaba ya Wafanyakazi, Katibu Mkuu wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA), Ndugu Herry Mkunda, amepongeza jitihada za Serikali katika kuboresha maslahi ya wafanyakazi, ikiwemo nyongeza ya mishahara, kuboresha mazingira ya kazi na majadiliano ya wadau wa utatu, huku akiiomba Serikali kuendelea kuimarisha hifadhi ya jamii, usalama kazini na fursa za ajira.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano, Mheshimiwa Deus Sangu, amesema hatua zinazochukuliwa na Serikali imeimarisha huduma za jamii na mazingira ya uzalishaji, ikiwemo uwekezaji katika afya, elimu, miundombinu na sekta zakiuchumi zinazogusa moja kwa moja maisha ya wafanyakazi na wananchi.

Naye, Mwenyekiti wa Chama cha Waajiri Tanzania (ATE), Dkt. Oscar Mgaya, amepongeza hatua za Serikali katika kuboresha mazingira ya biashara na ajira, ikiwemo kuundwa kwaTume ya Rais ya Maboresho ya Kodi, akisema hatua hiyo itaongeza uwekezaji wa sekta binafsi na kutengeneza fursa zaidi za ajira zenye staha.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Shirika la Kazi Duniani (ILO) Kanda ya Afrika Mashariki, Bi. Caroline Mugala, ameipongeza Tanzania kwa kuimarisha ajenda ya kazi zenye staha, haki za kijamii na majadiliano ya wadau wa utatu katika sekta ya kazi.

Ameongeza kuwa, ILO itaendelea kushirikiana na Serikali katika utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa Kazi zenye Staha, kuimarisha sheria na viwango vya kazi, kukuza ujuzi kwa vijana na wanawake, pamoja na kuimarisha mifumo salama ya ajira kwa Watanzania wanaofanya kazi nje ya nchi.









Share:

WMA YASHIRIKI MAADHINISHO YA SIKU YA WAFANYAKAZI DUNIANI MEI MOSI


Wakala wa Vipimo (WMA) imeungana na wafanyakazi kutoka katika taasisi na mashirika mbalimbali nchi nzima kuadhimisha siku ya Wafanyakazi Duniani.

Siku ya Wafanyakazi Duniani huadhimishwa kila Mwaka tarehe 1 Mei na kaulimbiu ya Siku ya Wafanyakazi Duniani Mwaka 2026 ni "Kazi zenye Staha ni Nguzo Imara kwa Maendeleo Endelevu katika Utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050".

Wakala imeshiriki katika maadhimisho hayo Kitaifa Mkoani Njombe ambapo watumishi wa Mkoa huo wameongozwa na Afisa Mtendaji Mkuu wa WMA Bw. Alban Kihulla.

Pamoja na ushiriki wa Kitaifa kadharika, WMA imeshiriki kuadhimisha siku ya Wafanyakazi katika ngazi za Mikoa kupitia ofisi za Mikoa za Kivipimo.

Uongozi wa WMA unaendelea kuwahimiza watumishi wake kufanya kazi kwa weledi na kuhakikisha wanatoa huduma sahihi kwa wananchi kwa kusimamia matumizi sahihi ya Vipimo katika sekta mbalimbali.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO IJUMAA MEI 1,2026

Magazeti
 



Share:

UFAFANUZI WA KISHERIA WAKOMESHA MJADALA WA JWTZ KUWAPO BARABARANI OKTOBA 29

Katika mkutano na waandishi wa habari uliofanyika hivi karibuni, Tume ya Kuchunguza Matukio ya Baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025 ilitoa ufafanuzi wa kina kuhusu hoja ya kuwepo kwa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) mitaani wakati wa ghasia, licha ya kutotangazwa kwa hali ya hatari. 

Balozi Paul Meela, ambaye ni mjumbe wa tume hiyo, alieleza kuwa ushiriki wa jeshi ulikuwa wa kisheria na ulizingatia taratibu zilizowekwa ili kusaidia mamlaka za kiraia kurejesha utulivu.

Msingi wa ushiriki huo unapatikana katika Sheria ya Ulinzi wa Taifa, Sheria namba 24 ya mwaka 1966. Kwa mujibu wa ufafanuzi wa Balozi Meela, kifungu cha 21 cha sheria hiyo kinaruhusu jeshi kwenda kusaidia mamlaka za kiraia pale inapohitajika, bila lazima ya kutangazwa kwa hali ya hatari nchini kote.

 Hii ina maana kuwa sheria iliyoanzisha jeshi inawapa mamlaka ya kutoa msaada wa kiulinzi kwa vyombo vingine vya dola pale hali ya usalama inapohitaji nguvu ya ziada.

Aidha, utaratibu wa utendaji kazi wa jeshi katika mazingira hayo umeelezwa ndani ya kifungu cha 22 cha sheria hiyo ya mwaka 1966. Sheria inabainisha kuwa wanapokwenda kusaidia, askari wa jeshi wanakuwa na mamlaka au nguvu sawa na za polisi (police powers) kwa muda husika. 

Lengo la ushiriki wao si kuchukua nafasi ya polisi au kuwaondoa kazini, bali ni kufanya kazi kwa kushirikiana na vyombo vingine vya usalama vilivyopo ili kudhibiti vurugu na kulinda maisha na mali za wananchi.

Maelezo haya ya Tume yanalenga kuondoa mkanganyiko miongoni mwa wananchi na kutoa uelewa kuwa hatua hiyo ilikuwa ya kisheria na ililenga kulinda misingi ya amani ya taifa. 

Ni muhimu kuelewa kuwa ushiriki wa jeshi katika kusaidia mamlaka za kiraia ni sehemu ya wajibu wao wa kisheria pale usalama wa taifa na utulivu wa jamii unapotishiwa na vurugu zilizopangwa

Share:

Thursday, 30 April 2026

MIAKA 40 YA NEMC: NGUZO YA MAENDELEO ENDELEVU TANZANIA


Na Mwandishi wetu

Katika dunia inayokabiliwa na changamoto kubwa za mabadiliko ya tabianchi, ongezeko la uchafuzi wa mazingira na kupungua kwa rasilimali asilia, hadithi ya Tanzania inajitokeza kama mfano wa matumaini, uthabiti na maamuzi ya kimkakati. 

Maadhimisho ya miaka 40 ya Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) si tukio la kawaida ni kielelezo cha dhamira ya Taifa kulinda uhai wake huku likiendeleza uchumi wake.

Kuanzishwa kwa NEMC mwaka 1986 kulikuja katika kipindi ambacho dunia ilikuwa inaanza kutambua kwa kina uhusiano kati ya mazingira na maendeleo. Tanzania, kwa maono ya mbali, iliweka msingi wa taasisi itakayokuwa mlezi wa rasilimali zake kwa vizazi vya sasa na vijavyo.

DARUBINI YA MIAKA 40: MAFANIKIO YENYE ATHARI CHANYA

Kwa miongo minne, NEMC imejidhihirisha kama nguzo ya maendeleo endelevu. Zaidi ya miradi 35,000 imepitia Tathmini ya Athari kwa Mazingira (EIA), hatua iliyowezesha uwekezaji kufanyika kwa uwajibikaji mkubwa zaidi. Hii si takwimu tu—ni ushahidi wa namna Tanzania ilivyofanikiwa kuoanisha ukuaji wa uchumi na ulinzi wa mazingira.

Katika sekta ya viwanda na biashara, utoaji wa vibali zaidi ya 28,000 umeimarisha uzingatiaji wa viwango vya mazingira, hivyo kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika masoko ya kimataifa. Aidha, juhudi za kudhibiti uchafuzi zimeokoa taifa gharama kubwa ambazo zingetumika kurekebisha madhara ya kimazingira na kiafya.

Uwekezaji katika maarifa nao haujaachwa nyuma. Kupitia mafunzo na miongozo, wataalamu zaidi ya 12,000 wamejengewa uwezo, wakisambaza utaalamu huo katika taasisi za serikali, sekta binafsi na vyuo vya elimu ya juu.

MAZINGIRA KAMA MHIMILI WA UCHUMI

Mara nyingi, mjadala wa mazingira huwekwa kando kana kwamba ni suala la pembeni. Lakini ukweli ni kwamba mazingira ndiyo msingi wa uchumi wa Tanzania. Kilimo, ambacho kinaajiri sehemu kubwa ya Watanzania, kinategemea afya ya udongo na upatikanaji wa maji. Utalii, sekta muhimu ya mapato ya kigeni, unategemea uwepo wa bioanuai na mifumo hai ya ikolojia.

Misitu ya Tanzania, inayochukua zaidi ya nusu ya eneo la nchi, si tu makazi ya viumbe hai bali pia ni hifadhi kubwa ya hewa ukaa (carbon sink). Mikoko ya pwani inalinda fukwe dhidi ya mmomonyoko na kusaidia kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Kwa mantiki hiyo, kulinda mazingira si chaguo—ni uwekezaji wa moja kwa moja katika uchumi wa taifa.

CHANGAMOTO ZINAZOHITAJI HATUA ZA HARAKA

Pamoja na mafanikio haya, changamoto bado ni kubwa. Kila mwaka, Tanzania inapoteza maelfu ya hekta za misitu kutokana na shughuli za kibinadamu kama ukataji miti holela, kilimo kisicho endelevu na matumizi ya nishati isiyo rafiki kwa mazingira.

Athari za mabadiliko ya tabianchi—ikiwemo ukame, mafuriko na mabadiliko ya mifumo ya mvua—zinaendelea kuathiri maisha ya wananchi na sekta za uzalishaji.

Hizi ni changamoto zinazohitaji zaidi ya sera—zinahitaji mabadiliko ya mtazamo, teknolojia bunifu, na ushirikiano mpana wa wadau wote.

NGUVU YA USHIRIKIANO: SERIKALI, JAMII NA SEKTA BINAFSI

Moja ya mafanikio makubwa ya NEMC ni kuhamasisha ushiriki mpana wa wadau katika uhifadhi wa mazingira. Wananchi zaidi ya milioni 4.2 wamefikiwa na elimu ya mazingira—hatua inayojenga kizazi chenye uelewa na uwajibikaji.

Sekta binafsi nayo imeanza kuchukua nafasi muhimu kupitia uwekezaji katika teknolojia safi, urejelezaji na uzalishaji unaozingatia mazingira. Huu ni mwelekeo sahihi kuelekea uchumi wa kijani (green economy).

Kwa upande wa sera, maboresho ya sheria, kanuni na miongozo yameiweka Tanzania katika nafasi nzuri kimataifa, huku yakitoa mazingira wezeshi kwa uwekezaji unaozingatia uendelevu.

NEMC@40: ZAIDI YA MAADHIMISHO, NI WITO WA HATUA

Katika kuelekea kilele cha maadhimisho tarehe 29 Mei 2026, shughuli kama upandaji wa miti 40,000, utoaji wa elimu kwa maelfu ya wadau, na majadiliano ya kitaifa kuhusu mustakabali wa mazingira zinaashiria mwelekeo mpya wa hatua za vitendo.

Huu ni wakati wa kujiuliza: Je, tunataka kuacha urithi gani?

Je, tunataka vizazi vijavyo vikute misitu au jangwa? Mito yenye uhai au mito iliyokauka?

Majibu ya maswali haya yako mikononi mwetu.

HITIMISHO: UAMUZI WA LEO, MUSTAKABALI WA KESHO

Safari ya miaka 40 ya NEMC inaonesha wazi kuwa Tanzania ina uwezo wa kuwa kinara wa maendeleo endelevu. Lakini mafanikio ya kesho yatategemea maamuzi ya leo.

Kila Mtanzania ana jukumu: kupanda mti, kupunguza uchafuzi, kutumia rasilimali kwa busara, na kuhamasisha wengine kufanya hivyo.

Kwa pamoja, tunaweza kujenga taifa lenye mazingira salama, uchumi imara, na maisha bora kwa wote.

“Mazingira si urithi tulioupokea—ni dhamana tuliyoazima kutoka kwa vizazi vijavyo.”

#MazingiraYetuUhaiWetu – Tuyatunze, Yatutunze
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger