Sunday, 17 May 2026

SERIKALI KUENDELEA KUIMARISHA UWEZO WA KUZUIA,KUJIANDAA,KUKABILIANA NA MAAFA






Na Mwandishi wetu- MBEYA

Serikali imeendelea kuimarisha uwezo wa Kitaifa wa Kuzuia, Kujiandaa, Kukabiliana na Kurejesha hali baada ya maafa ili kuhakikisha wananchi wanaishi katika mazingira salama ya kuepuka madhara makubwa yatokanayo na maafa.

Kauli hiyo imetolewa na Katibu Tawala Msaidizi Mipango na Uratibu Ofisi ya Mkoa wa Mbeya, Dkt. Noah Sikwese wakati akifunga mafunzo kwa Wajumbe Wateule wa Timu ya Kukabiliana na Dharura (RERT), Waatalamu wa Unendeshaji wa Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura (REOCC) katika Mkoa huo yaliyoandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Idara ya Menejimenti ya Maafa.


Dkt. Sikwese, amesema timu za kukabiliana na dharura zimejengewa msingi muhimu wa utendaji utakaowezesha Mkoa kuwa na uwezo wa kujiandaa na kukabiliana na matukio ya dharura kwa haraka na ufanisi mkubwa .


“Timu hizi zitahusika katika kufanya tathmini za awali na za kina wakati wa maafa kubaini mahitaji halisi ya waathirika, pamoja na kuratibu upatikanaji wa rasilimali muhimu kwa ajili ya kukabiliana na athari za maafa,” alisema Dkt. Sikwese.




Pia, aliongeza kwamba mafunzo yamekuwa nyenzo muhimu katika kujenga na kuimarisha uwezo wa kitaalamu na kiutendaji kwa watumishi wanaohusika katika Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya dharura.


“Kuanzishwa kwa Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura Mkoa wa Mbeya ni hatua muhimu katika kuimarisha uratibu wa shughuli za usimamizi wa maafa. Kituo hiki kitawezesha ufuatiliaji wa matukio kwa ukaribu, ukusanyaji na uchambuzi wa taarifa kwa wakati, pamoja na kuimarisha mawasiliano miongoni mwa wadau,” alieleza.


Sambamba na hilo Dkt. Sikwese alifafanua kuwa, utekelezaji wa mafunzo hayo ulianza katika Mikoa a Mwanza, Arusha, Dodoma, ambapo hatua za kuanzisha Vituo vya Operesheni na Mawasiliano ya Dharura pamoja na kuimarisha Timu za kukabiliana na maafa zilianza kutekelezwa.







“Ni matarajio yangu mafunzo haya yataongeza ufanisi, uwajibikaji, ustahimilivu dhidi ya majanga katika Mkoa wetu wa Mbeya,”aliongeza.


Aidha, alitoa wito kwa wataalamu wote waliopatiwa mafunzo kuendelea kuyafanyia kazi maarifa na stadi, kudumisha nidhamu ya kazi na kujenga utamaduani wa ushirikiano wa kitaalamu huku akiwasisitiza kuendelea kufanya mazoezi ya mara kwa mara ya uokoaji na utoaji wa huduma ya kwanza kwa majeruhi au waliofikwa na maafa.


“Usimamizi wa maafa ni jukumu letu sote, kila mmoja ashiriki sasa na kuchukua hatua katika eneo lake ili kuokoa na kulinda maisha, mali na mazingira,” alisisitiza Dkt. Sikwese.




Ikumbukwe kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) kwa mujibu wa Sera ya Taifa ya Usimamizi wa Maafa yam waka 2004 (Toleo la 2025) pamoja na Sheria ya Usimamizi wa Maafa Na. 6 ya mwaka 202 imeipa jukumu la kuratibu masuala yote ya usimamizi wa maafa nchini.






Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMAPILI MEI 17,2026

Magazeti ya leo
 

Related Stories
Share:

Saturday, 16 May 2026

DIWANI MABAO AWASHUKURU WANANCHI NGOGWA KWA KUMPA IMANI YA UONGOZI, CCM YASISITIZA AMANI NA USHIRIKIANO


Diwani wa Kata ya Ngogwa katika Manispaa ya Kahama, Abel Mabao, akiwashukuru wananchi wa kata hiyo kwa imani waliomuonesha katika uchaguzi mkuu wa madiwani, wabunge na Rais uliofanyika Oktoba mwaka 2025

Na Neema Nkumbi, Kahama

Diwani wa Kata ya Ngogwa katika Manispaa ya Kahama, Abel Mabao, amewashukuru wananchi wa kata hiyo kwa imani waliomuonesha katika uchaguzi mkuu wa madiwani, wabunge na Rais uliofanyika Oktoba mwaka 2025, huku akiahidi kutowavunja moyo wananchi waliompa dhamana ya kuwa mwakilishi wao. 

Mabao amesema ataendelea kusimamia maslahi ya wananchi na kuhakikisha maendeleo yanapatikana katika maeneo mbalimbali ya kata hiyo.

Akizungumza mbele ya wananchi wa Ngogwa, Mabao amesema jukumu lake kubwa ni kufuatilia na kusimamia utekelezaji wa miradi ya maendeleo ndani ya kata hiyo, akisisitiza kuwa ataendelea kupigania upatikanaji wa huduma muhimu ikiwemo maji, barabara na umeme ili kuboresha maisha ya wananchi.

Amesema tayari ameanza kushirikiana na madiwani pamoja na viongozi wa serikali kuhakikisha miradi ya maendeleo inatekelezwa kwa vitendo huku akibainisha kuwa baadhi ya maeneo tayari yameingizwa katika mipango ya bajeti kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali kuanzia mwezi Julai mwaka huu.

Katika hatua nyingine, Mabao ameipongeza Serikali ya Chama Cha Mapinduzi chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kupeleka huduma za maendeleo kwa wananchi akitaja miradi ya maji, umeme pamoja na miundombinu kuwa ni miongoni mwa mafanikio yanayoonekana katika maeneo mbalimbali ya Kata ya Ngogwa.

Diwani huyo pia amewataka wananchi kuendelea kudumisha amani, mshikamano na ushirikiano ili kuharakisha maendeleo ya kata hiyo, amesema amani ndiyo msingi wa maendeleo na kwamba wananchi wanapaswa kushirikiana kwa karibu na viongozi wao ili kujenga jamii yenye ustawi na maendeleo endelevu.

Kwa upande wake, Katibu wa itikadi na uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Kahama, Joachim Simbila, amewataka wananchi kuendelea kulinda amani baada ya uchaguzi mkuu, akieleza kuwa amani ndiyo msingi wa maendeleo ya taifa na ustawi wa jamii, amesema wananchi wa Kahama wameonyesha ukomavu wa kisiasa kwa kushiriki uchaguzi kwa utulivu na kufanya maamuzi yao kwa amani.

Simbila amesema bila amani hakuna maendeleo, kwani hata biashara, uwekezaji na utekelezaji wa miradi ya maendeleo haviwezi kufanikiwa katika mazingira ya migogoro na vurugu.

Aidha, amegusia changamoto zinazoendelea kujitokeza duniani ikiwemo vita katika baadhi ya mataifa, akisema hali hiyo inaonesha umuhimu mkubwa wa kuendelea kuilinda amani iliyopo nchini Tanzania.

Naye Kaimu Katibu wa CCM Wilaya ya Kahama, Elia Wikunge, amewapongeza wananchi wa Kata ya Ngogwa kwa kuendelea kuonyesha ushirikiano na mshikamano katika shughuli mbalimbali za maendeleo ambapo amesema ushirikiano kati ya wananchi na viongozi wao ni msingi muhimu wa mafanikio ya maendeleo, huku akisisitiza kuwa CCM itaendelea kuwa karibu na wananchi katika kusikiliza changamoto zao na kushirikiana nao kutafuta suluhisho la maendeleo endelevu.
Share:

DKT.MIGIRO AIMARISHA USHIRIKIANO KIMATAIFA NA MABALOZI WA CUBA, VIETNAM, NA UN

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi, Dkt. Asha-Rose Migiro, kwa nyakati tofauti amekutana na kufanya mazungumzo na mabalozi wawili wanaoziwakilisha nchi zao katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mazungumzo hayo yamefanyika katika ofisi ndogo ya makao makuu CCM, Lumumba, jijini Dar es salaam.

Mabalozi hao ni Mheshimiwa Yordenis Despaigne Vera, Balozi wa Jamhuri ya Cuba na Mheshimiwa Vu Thanh Huyen, Balozi wa Jamhuri ya Kisoshalisti ya Viet Nam, wote wenye makaazi yao nchini Tanzania.

Mazungumzo hayo yalijikita katika kuendeleza na kuimarisha ushirikiano wa kihistoria kati ya CCM na vyama rafiki vya CPC–Cuba na CPV–Viet Nam, hususan katika maeneo ya uongozi, mshikamano wa vyama vya siasa na maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa manufaa ya wananchi wa nchi hizi mbili.

Katika hatua nyingine, Katibu Mkuu wa CCM, Dkt Migiro, alifanya mazungumzo na Mheshimiwa Susan Ngongi Namondo, Mwakilishi Mkaazi wa Umoja wa Mataifa nchini Tanzania, ambapo walijadiliana vipaumbele vya maendeleo ya jamii katika utekelezaji wa baadhi ya maeneo yaliyomo katika Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2025–2030 ambayo yanawiana na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, na Malengo ya Maendeleo ya Kimataifa (SDGs).
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger