Thursday, 4 June 2026

MBEYA CITY EXPO YATUMIKA KUELIMISHA WANANCHI KUHUSU HAKI ZA WALAJI





Na mwandishi wetu

Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Denis Londo, ametembelea banda la Tume ya Ushindani Tanzania (FCC) katika Maonesho ya Kimataifa ya Mbeya City Expo 2026 yanayoendelea katika viwanja vya Uhindini, jijini Mbeya, ambapo alipata fursa ya kujionea shughuli mbalimbali zinazotekelezwa na taasisi hiyo katika kulinda maslahi ya walaji na kuimarisha ushindani wa biashara nchini.

Katika maonesho hayo, FCC imekuwa ikitoa elimu kwa wananchi kuhusu haki za mlaji, namna ya kutambua na kuepuka bidhaa bandia pamoja na umuhimu wa ushindani wa haki katika shughuli za biashara.

Elimu hiyo imevutia mamia ya wananchi waliojitokeza kutembelea banda hilo na kupata ufafanuzi wa masuala mbalimbali yanayohusu biashara, ushindani na ulinzi wa walaji.

Akizungumza wakati akifunga Maonesho hayo yaliyodumu kwa siku tisa Mei 30, 2026 jijini Mbeya, Naibu Waziri Londo alisisitiza umuhimu wa kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu madhara ya bidhaa bandia, akieleza kuwa bidhaa hizo zinaathiri afya za watumiaji, kudhoofisha biashara halali na kupunguza mapato ya Serikali.

Kwa upande wake, Mkuu wa Kanda wa FCC - Nyanda za Juu Kusini Bw. Dickson Mbanga, amesema taasisi hiyo imejipanga kuendelea kuimarisha kampeni za utoaji elimu kwa wananchi ili kuwajengea uwezo wa kutambua bidhaa halisi na kuepuka kununua au kutumia bidhaa zisizo na viwango vinavyotakiwa.

Mbanga alisema Maonesho ya Mbeya City Expo yamekuwa jukwaa muhimu la kuifikia jamii kwa karibu na kutoa elimu inayolenga kuongeza uelewa kuhusu sheria za ushindani na hatua zinazochukuliwa dhidi ya wafanyabiashara wanaojihusisha na usambazaji wa bidhaa bandia.

“Tunatumia maonesho haya kuwafikia wananchi wengi zaidi na kuwaelimisha kuhusu hatari za bidhaa bandia na kumlinda mlaji. Lengo letu ni kuhakikisha watumiaji wanakuwa na taarifa sahihi zitakazowasaidia kufanya maamuzi bora wanaponunua bidhaa mbalimbali sokoni,” alisema Mbanga.

Aliongeza kuwa FCC itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa biashara na vyombo vya usalama katika kudhibiti bidhaa bandia zinazoingia sokoni, huku ikiendelea kuhamasisha wananchi kutoa taarifa wanapobaini uwepo wa bidhaa zinazotiliwa shaka.

Maonesho ya Mbeya City Expo 2026 yamewakutanisha wadau kutoka sekta mbalimbali za uchumi, biashara na uwekezaji, huku yakitoa fursa kwa taasisi za umma na binafsi kuonesha huduma, bidhaa na mafanikio yao kwa wananchi. Kupitia ushiriki wake, FCC imeendelea kuonesha dhamira ya Serikali ya kulinda walaji na kujenga mazingira ya biashara yenye ushindani wa haki .


Share:

MRADI WA FOLUR KUSHUSHA MIONGOZO YA KIMATAIFA MAENEO YA UTENDAJI ZANZIBAR








Na Anangisye Mwateba, Zanzibar

MRADI wa Mifumo ya Chakula, Matumizi ya Ardhi na Urejesho wa Mandhari ya Misitu nchini Tanzania (FOLUR), unatarajia kutoa mafunzo maalum kwa viongozi wa serikali za vijiji na shehia mbalimbali visiwani Zanzibar. Hatua hiyo inalenga kujenga uwezo wa kiutendaji na kuhakikisha jamii inatekeleza shughuli za mradi huo kwa kuzingatia viwango vya kimataifa.


Akifungua mafunzo hayo kwa maafisa ugani wa kilimo na misitu upande wa Zanzibar, Mratibu wa mradi huo, Bi. Miza Suleiman Khamis, alisema dhumuni kubwa ni kuwawezesha watendaji hao kubaini, kuepuka au kupunguza athari hasi zinazoweza kujitokeza kabla hazijaletea madhara wanajamii na mazingira yao.


Kwa upande wake, Msimamizi wa Kitengo cha Jinsia, Usalama wa Mazingira na Jamii wa mradi huo, Bw. Revocatus Kadoshi, alibainisha kuwa viongozi wa shehia na maafisa ugani watafundishwa miongozo minne mikuu.

Miongoni mwa miongozo hiyo ni Mpango wa Usimamizi wa Mazingira na Jamii (ESMP), unaohusu udhibiti wa matumizi ya rasilimali na kuzuia uhamishaji wa watu usio wa hiari.


Bw. Kadoshi alifafanua kuwa mwongozo huo unalenga kudhibiti na kupunguza athari za kimazingira na kijamii wakati wa utekelezaji wa mradi. Aliongeza kuwa hatua hiyo inaenda sambamba na matakwa ya Mwongozo wa Sera na Taratibu Jumuishi za Ulinzi wa Kijamii za Shirika la Uhifadhi wa Mazingira Duniani (WWF).


"Viongozi hawa pia watafundishwa kuhusu Usimamizi Shirikishi wa Visumbufu. Huu unalenga kulinda afya na usalama wa jamii kwa kudhibiti athari zitokanazo na matumizi ya viuatilifu na mbolea," alisema Bw. Kadoshi.


Aidha, mafunzo hayo yatahusisha mbinu za usimamizi wa mazingira zinazohakikisha ustawi wa jamii, usalama mahali pa kazi, pamoja na usafi wa mazingira wakati wote wa utekelezaji wa shughuli za mradi huo.

Vilevile Aliongeza kuwa, ili kuhakikisha usalama wa jamii, mradi umeweka utaratibu maalumu wa kupokea nakufanyia kazi malalamiko kutoka kwa mwanajamii au kikundi cha kijamii kuhusiana na shughuli zinazotekelezwa na mradi. Hii inalwnga kuhakikisha jamii inashiriki vema kwenye shighuli za mradi na wanakuwa na nafasi ya kutoa dukuduku au lalamiko wakati wowote.


Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO ALHAMISI JUNI 4,2026

Magazeti



Related StoriesView all
Share:

Wednesday, 3 June 2026

TEMESA NA TOYOTA WAJADILI MAGEUZI YA HUDUMA ZA MATENGENEZO YA MAGARI NCHINI




Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme Tanzania - TEMESA, Bw. Kheri Mahimbali, leo tarehe 02 Juni 2026 amekutana na viongozi wa kampuni ya TOYOTA Tanzania katika ofisi zao eneo la Posta, jijini Dar es Salaam ambapo pamoja na mambo mengine wamejadili kuhusu jitihada za Serikali katika kuendelea kuboresha huduma za matengenezo ya magari hapa Nchini.



Akizungumza katika kikao hicho, Bw. Mahimbali amesema TEMESA imejipanga kuhakikisha huduma za ufundi na matengenezo ya magari ya Serikali zinatolewa kwa viwango vya juu kwa kutumia teknolojia za kisasa na za viwango vya kimataifa.



“TEMESA inaona fursa kubwa katika kuimarisha ushirikiano na TOYOTA kupitia miradi ya pamoja itakayowezesha taasisi hizi mbili kubadilishana utaalamu kwa mafundi na kuongeza ufanisi wa huduma zinazotolewa kwa wadau wetu,” amesema Mtendaji Mkuu.

Kwa upande wake, Meneja Mkuu wa TOYOTA Tanzania, Bw. Jatin Pandya amehakikisha utayari wa kampuni hiyo kuendelea kushirikiana na TEMESA katika mafunzo ya kitaalamu kwa mafundi, ushauri wa kiufundi, matumizi ya teknolojia mpya na kuimarisha mifumo ya usalama wa magari.



“Sisi TOYOTA tunatanguliza usalama wa watumiaji wa magari na ubora wa huduma. Tunaamini ushirikiano huu utachangia kwa kiasi kikubwa kuimarisha huduma za matengenezo ya magari nchini na kujenga uwezo wa wataalamu wa ndani,” amesisitiza Pandya.



Aidha, mara baada ya kikao hicho, Mtendajji mkuu pia alipata fursa ya kufanya ziara fupi katika karakana za TOYOTA ili kujionea teknolojia mpya zinazotumika katika matengenezo ya magari.

Miongoni mwa mambo waliyojadili katika kikao hicho ni pamoja na uwezekano wa kuanzisha ushirikiano kupitia mfumo wa Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi - PPP. Hatua inayotarajiwa kuimarisha uwezo wa karakana na kuongeza ufanisi wa huduma katika sekta ya matengenezo ya magari.

Kikao hicho kimefungua ukurasa mpya wa ushirikiano kati ya TEMESA na TOYOTA, huku kikitarajiwa kuwa chachu ya mageuzi makubwa katika sekta ya ufundi
 wa magari nchini.
Share:

VYUO VIKUU MALAYSIA VYAANZA MAONESHO YA ELIMU DAR


Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Tanzania na Malaysia zimefungua ukurasa mpya wa ushirikiano katika elimu ya juu kupitia ubia wa vyuo vikuu, tafiti za pamoja, ubadilishanaji wa wanafunzi na wahadhiri, ufadhili wa masomo pamoja na ushirikiano katika sayansi na teknolojia.

Akizungumza katika kikao cha Kuimarisha Ushirikiano wa Elimu ya Juu Kati ya Tanzania na Malaysia** kilichofanyika katika Hoteli ya Serena, Dar es Salaam, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Daniel Mushi, amesema ujio wa ujumbe wa elimu kutoka Malaysia ni wa wakati muafaka wakati Tanzania ikiendelea kuimarisha na kutangaza kimataifa mfumo wake wa elimu ya juu.

Kikao hicho kiliandaliwa na kuratibiwa na Education Malaysia Global Services (EMGS), chini ya Wizara ya Elimu ya Juu ya Malaysia, kwa kushirikiana na Global Education Link Ltd (GEL).

Prof. Mushi amesema ujio wa ujumbe huo umevitambulisha vyuo vya Malaysia nchini Tanzania na kutoa nafasi kwa pande zote mbili kujadili maeneo ya ushirikiano yatakayowanufaisha wanafunzi, wahadhiri na taasisi za elimu ya juu.

Amesema Tanzania inatarajia kuona ushirikiano utakaoimarisha programu za pamoja, kubadilishana maarifa, tafiti, ubunifu na kuongeza uwezo wa taasisi za elimu ya juu nchini.

Kwa mujibu wa Prof. Mushi, Malaysia imepiga hatua kubwa katika kutumia elimu, teknolojia na ujuzi kama nyenzo ya mageuzi ya kiuchumi, jambo ambalo Tanzania inaweza kujifunza katika safari yake ya kujenga uchumi unaotegemea maarifa na teknolojia.

Amesema kipaumbele kinapaswa kuwekwa katika kuwaandaa wanafunzi wa Tanzania kwenye maeneo ya sayansi, hisabati, kemia, sayansi ya takwimu, ujifunzaji wa mashine na akili mnemba.

Aidha, amesema wanafunzi wanaotaka kusoma nje ya nchi wanapaswa kuandaliwa si kitaaluma pekee, bali pia kilugha na kitamaduni ili waweze kushindana na kufanikiwa katika mazingira ya kimataifa.

“Ushirikiano wa aina hii ni muhimu kwa sababu unawapa wanafunzi na taasisi zetu nafasi ya kupata maarifa mapya, mifumo mipya na njia mpya za kujenga rasilimali watu kwa maendeleo ya taifa,” amesema Prof. Mushi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Elimu ya Juu katika Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Stephen Maluka, amesema kikao hicho kimetoa jukwaa la vitendo kwa taasisi za Tanzania na Malaysia kujadili namna bora ya kujenga ushirikiano rasmi.

Amesema majadiliano yamelenga kuanzisha mahusiano ya moja kwa moja kati ya vyuo vikuu, wizara na taasisi za elimu kutoka nchi zote mbili kwa lengo la kuendeleza elimu, sayansi na teknolojia.

Prof. Maluka amesema Tanzania inahitaji ushirikiano unaokwenda zaidi ya udahili wa wanafunzi na kuingia katika maeneo ya tafiti za pamoja, programu za pamoja, ufadhili wa masomo, ubadilishanaji wa wahadhiri, maboresho ya mitaala na ushirikiano wa kitaaluma.

Amesema ufadhili wa masomo utasaidia wanafunzi wa Tanzania wenye sifa kupata nafasi za masomo Malaysia, hususan katika maeneo ambayo nchi hiyo imepiga hatua kubwa.

Aidha, amesema ubadilishanaji wa wahadhiri unaweza kusaidia kuongeza ubora wa ufundishaji, usimamizi wa tafiti na kuwapa wanataaluma uzoefu wa mifumo tofauti ya elimu ya juu.

Prof. Maluka ametaja teknolojia, sayansi ya takwimu na akili mnemba kuwa miongoni mwa maeneo muhimu ya ushirikiano wa baadaye.

Amesema ushirikiano katika maeneo hayo unaweza kusaidia Tanzania kuongeza uwezo katika teknolojia chipukizi na kuwaandaa wahitimu kwa dunia inayoongozwa na ubunifu na mabadiliko ya kidijitali.

“Sasa ni muhimu kutoka kwenye mazungumzo ya jumla na kuingia kwenye mifumo ya utekelezaji itakayoongoza ushirikiano kati ya taasisi,” amesema Prof. Maluka.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Global Education Link Ltd, Bw. Abdulmalik Mollel, amesema GEL inajivunia kuratibu mpango huo unaounganisha taasisi za Tanzania na vyuo vikuu pamoja na mamlaka za elimu kutoka Malaysia.

Amesema mpango huo hauhusu kutangaza fursa za kusoma Malaysia pekee, bali pia kujenga daraja la muda mrefu la elimu kati ya Tanzania na Malaysia.

“Ushirikiano huu unalenga kujenga daraja la kweli kati ya Tanzania na Malaysia katika elimu ya juu. Tunataka kuona vyuo vya pande zote mbili vikishirikiana katika tafiti, programu za kitaaluma, ubadilishanaji wa wanafunzi, ubadilishanaji wa wahadhiri na mafunzo yanayotegemea teknolojia,” amesema Mollel.


Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger