Tuesday, 7 April 2026
Monday, 6 April 2026
TUME YA UCHUNGUZI YAONGEZEWA MUDA TENA HADI APRILI 24,2026

Na Mwandishi Wetu Dodoma
MAMLAKA ya Uteuzi imeridhia maombi ya muda wa ziada kwa Tume ya Kuchunguza Matukio ya Uvunjifu wa Amani Wakati na Baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025 hivyo imeiongezea tena muda wa siku ishirini na moja (21) na kuitaka ikamilishe kazi kabla au ifikapo Aprili 24, 2026.
Mamlaka hiyo imeeleza sababu za kuongeza muda huo kwa Tume ni pamoja na kuiwezesha Tume kukamilisha uchambuzi wa ushahidi, taarifa na maoni yaliyopokelewa, kutoa fursa kwa wataalamu wa uchunguzi wa kisayansi kufanyia kazi baadhi ya vielelezo vipya vilivyowasilishwa.

Sababu nyingine ni kuiwezesha Tume kukamilisha maandalizi ya Ripoti itakayowasilishwa kwa Rais na kutoa fursa kwa Tume kuandaa tafsiri ya Ripoti hiyo.
Tume hiyo ilianza kutekeleza majukumu yake Novemba 20, 2025 na kutarajiwa kukamilisha kazi yake ndani ya kipindi cha siku 90. Hata hivyo, kutokana na sababu mbalimbali, Tume iliongezewa muda wa kukamilisha kazi na kutakiwa kuwasilisha Ripoti kwa Rais kabla au ifikapo April 3, 2026.
Hivyo, kufuatia nyongeza ya muda, wananchi waliendelea kujitokeza kwa wingi tofauti na matarajio ya Tume. Hivyo, Tume iliendelea kupokea ushahidi, taarifa na maoni zaidi. Kwa sababu hiyo, Tume haikuweza kukamilisha kazi yake ndani ya muda wa nyongeza uliotolewa na hivyo kulazimika kuomba muda wa ziada ili kukamilisha kazi yake.
Tume inaendelea kuwashukuru wananchi na wadau wote waliotoa ushirikiano kwa Tume wakati wa kufanya uchunguzi, ikiwemo wale waliofika mbele ya Tume kutoa ushahidi, taarifa na maoni, waliopiga simu na kutuma ujumbe, waliotuma ushahidi, taarifa na maoni kwa maandishi na waliowasiliana na Tume kwa njia za mitandao ya kijamii.
POLISI TANGA WAOKOA VIJANA 87 WALIOINGIZWA KWENYE MTEGO WA UTAJIRI WA HARAKA MTANDAONI
Na Hadija Bagasha - Tanga
Jeshi la Polisi Mkoa wa Tanga kupitia Kikosi cha Upelelezi wa Makosa ya Jinai (CID), limefanikiwa kuwaokoa vijana wapatao 87 waliokuwa wametapeliwa fedha zao kupitia mtandao baada ya kushawishiwa kujiunga na kampuni inayojinasibisha kufanya biashara ya mtandao inayofahamika kwa jina la Champions E-Commerce Education ambapo katika tukio hilo vijana hao walihamasishwa kujiunga na kampuni hiyo kwa ahadi ya kupata utajiri wa haraka kupitia biashara za mtandaoni.
Kwa mujibu wa Taarifa za awali zinaeleza kuwa vijana hao ni kutokea Mikoay a Mtwara, Iringa, Daresalaa na Morogoro ambao walishawishiwa kujiunga na Kampuni hiyo kwa ahadi ya kupata utajiri wa haraka kupitia biashara za mtandaoni, ambapo walielezwa kuwa wangeanza kupata faida kubwa ndani ya muda mfupi mara baada ya kukamilisha mafunzo.
Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo Kamanda wa polisi Mkoa Tanga Almachius Mchunguzi ameeleza kuwa kila kijana alitakiwa kuchangia kiasi cha fedha kuanzia shilingi laki sita (600,000) hadi kufikia shilingi milioni nne (4,000,000) kama mtaji wa awali pamoja na gharama za mafunzo, fedha ambazo walidaiwa kuambiwa ndizo zingewapa fursa ya kuanza biashara na kupata faida kwa haraka.
Hata hivyo, baada ya kujiunga na mfumo huo, vijana hao walikutwa wakiishi katika mazingira yasiyoridhisha huku wakiendelea kupatiwa mafunzo yanayodaiwa kuwajengea uwezo, wakisubiri kupata utajiri waliokuwa wameahidiwa.
Katika operesheni hiyo, Jeshi la Polisi limekamata na kuwashikilia kwa mahojiano zaidi watu wawili waliokuwa wakisimamia kundi hilo ambao ni Mohammed Hamis Idrisa (24) mkazi wa Masiwani Jijini Tanga, na Fidolini Hamisi Rashidi (21) mkazi wa Mbugani.
Jeshi la Polisi Mkoa wa Tanga limetoa wito kwa wananchi kuwa makini na aina ya uwekezaji unaohusisha ahadi za kupata faida kubwa kwa muda mfupi bila kuwa na taarifa sahihi, pamoja na kufanya uhakiki kama kampuni husika imesajiliwa na mamlaka halali.
Polisi imewataka wananchi kufanya uchunguzi wa kina kabla ya kujiunga na taasisi au kampuni yoyote inayojihusisha na uwekezaji hususan kupitia mitandao, ili kuepuka kuingia kwenye mitego ya utapeli.
Uchunguzi wa tukio hilo unaendelea huku Jeshi la Polisi likisisitiza kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi ya wote watakaobainika kuhusika na utapeli wa aina hiyo.













