Sunday, 28 June 2026

RAIS DKT. SAMIA KUFUNGUA MKUTANO MKUBWA WA MADINI NOVEMBA 2026

▪️Ni Mkutano mkubwa wa Madini na Uwekezaji

▪️Washiriki 2000 kutoka mataifa 50 Duniani kushiriki

▪️Kauli Mbiu ya Mkutano inalenga kuongeza thamani madini kwa maendelezo ya Viwanda

▪️Serikali na Sekta Binafsi kushirikiana kuandaa mkutano huo


▪️Waziri Mavunde azindua rasmi maandalizi ya mkutano huo

📍 DAR ES SALAAM. 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. Dkt. Samia S. Hassan anatarajiwa kufungua rasmi Mkutano wa Saba wa Madini na Uwekezaji Tanzania (TMIC 2026) utakaofanyika Novemba 19 hadi 21, 2026 katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC), Dar es Salaam.

Akizungumza leo Juni 27, 2026 wakati wa uzinduzi wa TMIC 2026, Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, amesema serikali imeamua kujenga uchumi wa viwanda unaotokana na madini kwa kuwekeza katika uchakataji na uyeyushaji wa madini badala ya kuendelea kuuza malighafi.

Amesema kaulimbiu ya mkutano huo, "Madini Yaliyoongezwa Thamani: Chachu ya Ukuaji wa Viwanda na Uchumi," inaakisi dira ya serikali ya kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha uchakataji wa madini barani Afrika.

Kwa mujibu wa Mhe. Mavunde, amesema Tanzania tayari ina viwanda vinane vya kusafisha dhahabu, huku Mkoa wa Dodoma ukiwa na viwanda tisa vinavyojengwa na vinavyoendelea na uzalishaji pamoja na kiwanda kikubwa cha kuyeyusha madini ya nikeli na shaba.

"Zaidi ya Sh bilioni 600 zinawekezwa katika ujenzi wa kiwanda cha chuma kitakachotumia asilimia 100 ya malighafi za ndani, huku uwekezaji mwingine ukiendelea Kigamboni na Tanga kwa ajili ya uchakataji wa madini ya 'Heavy Mineral Sands' na mradi wa madini ya niobium wa Panda Hill, Mbeya," amesema Mhe. Mavunde

Amesema, katika kuongeza ushiriki wa Watanzania kwenye sekta hiyo,  thamani ya manunuzi kupitia mpango wa 'Local Content' imefikia Sh trilioni 5.1, huku bidhaa 20 zikitakiwa kuzalishwa na wazawa kwa ajili ya kuhudumia migodi mikubwa.

 Amesisitiza wafanyabiashara kuzingatia uaminifu na viwango vya kimataifa ili kunufaika zaidi na fursa hizo.

Amesema sekta ya madini imeendelea kuimarisha mchango wake katika uchumi kwa kuingiza Sh trilioni 1.374 katika Mfuko Mkuu wa Serikali, kiwango kilichovuka lengo la Sh trilioni 1.2 kwa mwaka huu wa fedha.

Mhe. Mavunde, amesema Serikali imeidhinisha asilimia 10 ya mapato yote ya sekta ya madini kuelekezwa kwenye utafiti wa kina wa jiofizikia ili kuongeza maeneo yanayofahamika kuwa na madini kutoka asilimia 16 ya sasa hadi asilimia 50 ifikapo mwaka 2030.

Aidha, amesema Serikali inaandaa mfuko maalumu wa mikopo kwa wachimbaji wadogo, ambao licha ya changamoto za mitaji na teknolojia, wanachangia takribani asilimia 40 ya mapato ya sekta ya madini.

Katika hatua nyingine, amesema Serikali inaanza operesheni ya kufuta kidijitali leseni zote za madini zisizotumika. Wamiliki watakaoshindwa kuwasilisha taarifa ndani ya muda uliowekwa watapewa notisi ya siku 30 kabla ya leseni hizo kujifuta moja kwa moja.

Nae, Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Mhandisi Yahya Samamba, amesema Serikali imejipanga kuhakikisha utajiri wa madini unakuwa chachu ya kukuza viwanda vya ndani, kuongeza ajira na kuimarisha uchumi kupitia uongezaji thamani badala ya kuishia kwenye uchimbaji pekee.

Amesema TMIC 2026 utawakutanisha viongozi wa Serikali, taasisi za fedha, kampuni za madini, wataalamu wa teknolojia, watafiti na wadau wengine kutoka duniani kote kujadili fursa za uwekezaji na maendeleo ya sekta hiyo.

 "Huu ni wakati wa kuingia katika awamu mpya ya uwekezaji, ubunifu na ukuaji wa sekta ya madini nchini," amesema.

Kwa upande wa Katibu Mtendaji wa Chemba ya Migodi Tanzania, Mhandisi Benjamin Mchwampaka, amesema mkutano huo unatarajiwa kuwakutanisha washiriki zaidi ya 2,000 na watoa mada zaidi ya 100 kutoka mataifa zaidi ya 50, huku zaidi ya mada 20 zikijadiliwa zikiwemo sera, kodi, uwekezaji, teknolojia, nishati safi, madini ya kimkakati, uongezaji thamani na masuala ya mazingira, jamii na utawala bora (ESG).

Mchwampaka amesema TMIC 2026 pia utaweka mkazo katika maendeleo ya wachimbaji wadogo pamoja na ushirikishwaji wa wanawake na watu wenye ulemavu katika mnyororo mzima wa uongezaji thamani wa madini. Mkutano huo unatarajiwa kufungwa rasmi na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi.

.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUNE 28,2026


Share:

Friday, 26 June 2026

ORYX, KIDOTI FOUNDATION KUWATUMIA WASUSI KUSAMBAZA ELIMU YA NISHATI SAFI


Na Mwandishi Wetu 

KAMPUNI ya Oryx Gas Tanzania kwa kushirikana na taasisi ya Kidodi Foundation wameingia makubaliano ya kuendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi nchini kwa kulifiki kundi la watoa huduma za Saluni nchini.

Kwa mujibu wa Oryx na Kidodi Foundation watoa huduma za Saluni nchini ni kundi lenye uwezo mkubwa wa kuharakisha matumizi ya nishati safi ya kupikia kutokana na mwingiliano wao wa karibu na jamii, hali inayowafanya kuwa mabalozi muhimu wa mabadiliko ya tabia na mtazamo kuhusu matumizi ya nishati hiyo.

Akizungumza leo Juni 26,2026 Jijini Dar es Salaam wakakati wa hafla ya kusaini makubaliano hayo Mkurugenzi wa Kidoti Foundation, Jokate Mwegelo, ambaye pia ni mlezi wa Chama cha Salunisti Tanzania (CCST) amesema lengo la kuwawezesha watoa huduma za saluni kutumia nishati safi na kuwa mabalozi wa kuhamasisha matumizi yake katika jamii.

Amesema kundi la wasusi na watoa huduma za saluni lina nafasi ya kipekee kwa kuwa hukutana na mamia ya wananchi kila siku, jambo linaloweza kutumiwa kueneza elimu kuhusu manufaa ya nishati safi ya kupikia kwa urahisi kuliko kutegemea kampeni za kawaida pekee.

Amefafanua watoa huduma za saluni wanazungumza na watu wa makundi mbalimbali kila siku. Wanajenga mahusiano ya karibu na wateja wao, hivyo wana nafasi kubwa ya kubadilisha mitazamo kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia. 

“Tunataka wawe mabalozi wa mabadiliko hayo na kupitia makubaliano haya tumeyaingia Kati ya Kidoti Foundation na Oryx Gas Tanzania matarajio yetu tutawafikia watoa huduma wote wa saluni kupitia chama chao ambapo tutawapatia mitungi ya gesi na tutaanza na mitungi 2000 ambayo itatolewa kwa awamu.

“Juhudi za kuhakikisha Watanzania wengi wanatumia nishati safi haziwezi kuachiwa Serikali pekee, bali zinahitaji ushiriki wa makundi yenye ushawishi wa moja kwa moja katika jamii.

Kundi la watoa huduma za saluni limesahaulika kwa muda mrefu lakini Kidoti Foundation tumeona iko haja ya kulishika kundi hili kwa kuliwezesha kutumia nishati safi ya kupikia.”

Jokate amesema saluni zimekuwa sehemu ambazo mbali na huduma za urembo, wananchi hubadilishana uzoefu kuhusu afya, biashara, malezi na masuala mbalimbali ya maendeleo, hivyo zinaweza pia kuwa majukwaa ya utoaji wa elimu kuhusu nishati safi.

Pia amesema kupitia ushirikiano huo, watoa huduma za saluni watanufaika kwa kutumia nishati safi katika shughuli zao za kila siku, huku wakipata nafasi ya kuwahamasisha wateja wao kuachana na matumizi ya nishati zinazochafua mazingira na kuhatarisha afya.

"Nishati safi si suala la kupikia pekee. Ni suala la afya, mazingira, uchumi wa familia na maendeleo ya taifa. Tukiwafikia wasusi, tutakuwa tumefikia maelfu ya familia kupitia wateja wao," amesema.

Kwa upande wake Meneja Mauzo wa Oryx Tanzania Shaban Fundi amesema kampuni hiyo imeamua kushirikiana na Kidoti Foundation kwa kutambua kuwa makundi ya kijamii yenye ushawishi yanaweza kuongeza kasi ya matumizi ya nishati safi nchini.

“Mbali  na kutoa suluhisho la nishati safi, kampuni yetu itaendelea kujenga uelewa wa wananchi kuhusu faida za matumizi ya gesi na teknolojia nyingine za kisasa zinazochangia kulinda afya na mazingira,”amesema na kusisitiza Oryx Gas na Kidoti Foundation kupitia makubaliano yanakwenda kuongeza watumiaji wa nishati safi nchini.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa CCST Ntuli Mwakatobe amesema amesema ushirikiano huo ni hatua muhimu ya kuwawezesha wanachama wa chama hicho kuwa sehemu ya utekelezaji wa ajenda ya nishati safi nchini.

Amesema wasusi na wamiliki wa saluni wamekuwa wakitafuta njia za kupunguza gharama za uendeshaji wa biashara zao huku wakihakikisha mazingira ya kazi yanakuwa salama zaidi.

"Leo tunapata nafasi ya kutumia nishati safi lakini pia kuwa sauti ya kuelimisha jamii. Hii ni fursa ambayo tutaenda kuitumia kuwafikia wateja wetu kila siku," amesema.

Matumizi ya nishati safi ya kupikia yanatajwa kuchangia kupunguza uzalishaji wa hewa ukaa unaochochea mabadiliko ya tabianchi, sambamba na kuboresha maisha ya wanawake ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakibeba mzigo mkubwa wa shughuli za kupikia.

Share:

VIONGOZI WAJENGEWA UWEZO KUHUSU MRADI WA INUA II IRINGA


WATENDAJI wa vijiji, viongozi wa serikali za mitaa na wadau mbalimbali wa maendeleo mkoani Iringa wamepatiwa mafunzo na uelewa kuhusu utekelezaji wa Mradi wa INUA II unaotekelezwa na Hand in Hand Eastern Africa Tanzania (HIHEA), wenye lengo la kuimarisha uchumi wa wananchi kupitia shughuli za uzalishaji na biashara.

Akizungumza katika semina hiyo, Mkurugenzi wa HIHEA, Jane Richard Sabuni, alisema taasisi hiyo imefungua rasmi ofisi yake mkoani Iringa na kuanza utekelezaji wa mradi huo unaolenga kuwawezesha wananchi kujiongezea kipato kupitia vikundi vya ujasiriamali na biashara mbalimbali.

Alisema Hand in Hand imejikita katika kusaidia wananchi kuanzisha na kukuza biashara halali zitakazochangia kuimarisha uchumi wa kaya na kuboresha maisha ya familia. Aidha, alieleza kuwa taasisi hiyo tayari imewafikia zaidi ya wananchi 87,000, kusaidia kuanzishwa kwa biashara zaidi ya 50,000, kupitia vikundi zaidi ya 4,000 vya kiuchumi vilivyoundwa na kuimarishwa, na kuchangia kuzalishwa kwa ajira zaidi ya 74,000 nchini.

Sabuni alisema semina hiyo imelenga kuwajengea uwezo viongozi wa serikali za vijiji na kata ili waweze kuelewa malengo ya mradi na kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wake, huku akisisitiza kuwa ushirikiano wa viongozi wa serikali za mitaa ni muhimu katika kuhakikisha Mradi wa INUA II unafanikisha malengo yake ya kuimarisha uchumi wa wananchi.

Aidha, alieleza kuwa Hand in Hand imefungua rasmi ofisi yake mkoani Iringa Juni 24, 2026, hatua inayofanya taasisi hiyo kuwa na matawi katika mikoa saba nchini Tanzania, ikiwemo Arusha (makao makuu), Kilimanjaro, Manyara, Singida, Dodoma na Simiyu.

Share:

KUELEKEA TUZO ZA RAIS KWA WALIPAKODI, TRA KARIAKOO YAWAPONGEZA WALIPAKODI


Kariakoo, 25 Juni, 2026

Kuelekea maadhimisho ya Tuzo za Rais kwa Walipakodi Bora, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Kariakoo imewapongeza walipakodi kwa mchango wao mkubwa katika ulipaji wa kodi na uzingatiaji wa sheria za kodi, hali iliyowezesha baadhi yao kutambuliwa kama walipakodi bora wa mwaka.

Akizungumza alipotembelea walipakodi meneja wa uzingatiaji wa sheria na ufuatiliaji Bw. Lihami Haule aliwashukuru walipakodi kwa kuendelea kutimiza wajibu wao kwa uaminifu na kuwataka kuendeleza utamaduni huo ili kuchangia maendeleo ya taifa na kukuza uchumi.

Nae, Meneja wa kituo cha TRA Gerezani Bi. Mercy Sijaona aliwakaribisha walipakodi kushiriki katika mbio za burudani (Fun Run) zitakazofanyika Gymkhana tarehe 27 Juni 2026 saa 12: 00 asubuhi.

Kwa upande wao, walipakodi walieleza kufurahishwa na huduma zinazotolewa na TRA, hususani utoaji wa elimu ya kodi na mwitikio wa maafisa wa mamlaka katika kutatua changamoto mbalimbali.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO IJUMAA JUNI 26, 2026


Magazetini Leo


Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger