Wednesday, 15 July 2026

MAANDAMANO SAHIHI YANAPASWA KUZINGATIA SHERIA NA HAKI ZA WENGINE- BALOZI SEFUE




Na Mwandishi wetu, Dar

Katibu Mkuu Kiongozi mstaafu, Balozi Ombeni Sefue amesema maandamano ni haki ya msingi inayotambuliwa na Katiba ya Tanzania, sheria za nchi pamoja na makubaliano ya kikanda na kimataifa, akisisitiza kuwa yanapaswa kufanyika kwa kuzingatia sheria na bila kuathiri haki za watu wengine.

Sefue Ametoa kauli hiyo alipokuwa akizungumza na Mtandao wa Mwananchi Digital, akisema kwamba maandamano yanaangukia katika haki ya kujieleza akieleza kwamba maandamano yanayostahili kulindwa kisheria ni yale yanayotekelezwa kwa amani na kufuata masharti yaliyowekwa na sheria.

"Unajua maandamano ni haki ya msingi kwenye Katiba yetu, sheria yetu, makubaliano ya kikanda na kimataifa na maandamano yanaingia kwenye kundi la kujieleza. Tofauti ambayo inaonekana kwenye nchi zetu, watu wanashindwa kutofautisha maandamano yenye sifa ya kujieleza na maandamano ya vurugu," amesema Sefue.

Ameongeza kuwa uhuru wa mtu mmoja haupaswi kukiuka haki za wengine, akitolea mfano maandamano yanayosababisha biashara kufungwa au yanayohusisha vitisho kwa wananchi. "Ukisema mimi naandamana kwa namna ambayo duka langu lifungwe hayo si halali. Hata ukibeba jiwe kwa namna ambayo utamfanya mtu aogope hayo si halali," amesema.

Sefue pia amesisitiza umuhimu wa waandaaji wa maandamano kutoa taarifa kwa Jeshi la Polisi kabla ya kuyafanya ili mamlaka ziweze kutoa ushauri kuhusu njia zitakazotumika na kuhakikisha usalama wa washiriki pamoja na wananchi wengine, akisema utaratibu huo unalenga kuwezesha matumizi ya haki ya kuandamana kwa njia inayozingatia sheria na kulinda maslahi ya jamii kwa ujumla.
Share:

JUMUIYA YA MADOLA YAPONGEZWA, MKWAMO WA KISIASA NI MEZA YA MAZUNGUMZO



Mawaziri wa Jumuiya ya Madola wameipongeza Tanzania kwa juhudi zake za kuendeleza mazungumzo kama njia ya kujenga maridhiano, kuimarisha demokrasia na kudumisha amani. Aidha, Jumuiya imeendelea kuhimiza wadau kuzingatia mazungumzo ya maridhiano kama nyenzo muhimu ya kutatua tofauti na kuimarisha mshikamano wa kitaifa.

Kutokana na umuhimu wa ujumbe huo, inapendekezwa kufanyika mkutano na waandishi wa habari ili kuufafanua na kuuhabarisha umma kuhusu utayari wa Jumuiya ya Madola kushirikiana na Serikali na wadau kuhakikisha mazungumzo tofauti na propaganda ambazo zinaenezwa na wanaharakati ambayo inaonesha kana kwamba serikali imeshinikizwa

Kwa hiyo pendekezo ni kwamba kwenye press conference msisitizo utakuwa ni namna gani Jumuiya ya Madola inasukuma roho ya mazungumzo na maridhiano na jinsi gani Jumuiya inatambua juhudi mfano za Tume ya Uchunguzi ya Jaji CHANDE...kuhusu uchunguzi wa masuala ya jinai na hivyo kuondoa propaganda kwamba hakuna juhudi zozote zile
Share:

SPIKA ZUNGU : TANZANIA IKO TAYARI KUWAKARIBISHA WABUNGE WA DUNIA OKTOBA HII

Na Prosper Makene  

New York, Marekani – Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Musa Azzan Zungu, Mbunge, ameuhakikishia Umoja wa Mabunge Duniani (IPU) kuwa Tanzania imejipanga kikamilifu kuwakaribisha wabunge kutoka duniani kote katika Mkutano wa 153 wa IPU utakaofanyika Oktoba 2026 jijini Arusha.

Mhe. Zungu ametoa hakikisho hilo wakati wa kikao na Rais wa IPU, Mhe. Dkt. Tulia Ackson, Mbunge, pamoja na Katibu Mkuu wa IPU, Balozi Anda Filip jijini New York, Marekani.

Kikao hicho kililenga kupitia hali ya maandalizi, mipango ya kilojisti na uhakika wa utayari kabla ya mkutano huo mkubwa wa kibunge duniani.

Spika ameeleza kuridhishwa na kazi ya Kamati ya Kitaifa ya Maandalizi inayoratibu tukio hilo. Amesema mipango yote ya kilojisti, kiprotocol na usalama inaendelea kama ilivyopangwa, na Tanzania imejitolea kutoa ukaribisho wa kiwango cha kimataifa.

Mhe. Zungu amesisitiza kuwa kuandaa mkutano huo ni jambo la fahari kwa Taifa na ni fursa muhimu ya kuimarisha nafasi ya Tanzania katika diplomasia ya kibunge duniani.

Ameongeza kuwa Mkutano huo utakuwa jukwaa muhimu la majadiliano, ushirikiano na utafutaji wa masuluhisho ya changamoto zinazolikabili dunia leo. Tanzania inajivunia kuwakaribisha Maspika, Wabunge na wajumbe kutoka pande mbalimbali za dunia jijini Arusha, mji unaojulikana kwa amani na diplomasia.

Katibu Mkuu wa IPU, Balozi Anda Filip, naye amepongeza Tanzania kwa maendeleo yaliyopatikana katika maandalizi. Amethibitisha kuendelea kwa ushirikiano na msaada wa Sekretarieti ya IPU kwa Bunge la Tanzania ili kuhakikisha mafanikio ya Mkutano huo 

Mkutano wa 153 wa IPU unatarajiwa kuhudhuriwa na washiriki zaidi ya 1,500 wakiwemo Waspika wa Bunge, Wabunge na wajumbe kutoka mabunge 180 wanachama wa IPU na wanachama 15 washirika.

Ajenda ya Mkutano itagusa masuala mbalimbali ya kimataifa. Miongoni mwa masuala hayo ni pamoja na mabadiliko ya tabianchi, amani na usalama, utawala wa teknolojia, haki za binadamu, usawa wa kijinsia, na jukumu la mabunge katika kuharakisha utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu. Mpango wa mkutano utajumuisha mijadala ya wazi, vikao vya kamati na mikutano ya pande mbili baina ya ujumbe.

Arusha, inayofahamika kama 'Geneva ya Afrika' imechaguliwa kuwa mwenyeji kutokana na sifa yake ya kimataifa kama kituo cha diplomasia, amani na mikutano ya kimataifa.

Mji huo una historia ya kuandaa mikutano mikubwa ya kimataifa ikiwemo vikao vya Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu wa Rwanda na mikutano mbalimbali ya Umoja wa Mataifa na Umoja wa Afrika.

Serikali ya Tanzania imesema Mkutano huo utaleta manufaa makubwa kwa mji wa Arusha na kwa Taifa kwa ujumla. Manufaa yanayotarajiwa ni pamoja na kukuza utalii, huduma za ukaribishaji na ubadilishanaji wa kitamaduni. Pia tukio hili litaonesha miundombinu ya Tanzania na uwezo wake wa kuandaa mikutano mikubwa ya kimataifa.


Share:

Tuesday, 14 July 2026

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMATANO JULAI 15, 2026

Share:

PROF. SHEMDOE AMPONGEZA MBUNGE JACQUELINE MZINDAKAYA KURATIBU MAFUNZO YA UWEZESHAJI WANANCHI KIUCHUMI

Na OWM–TAMISEMI, Sumbawanga

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amempongeza Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Rukwa, Mhe. Jacqueline Mzindakaya, kwa juhudi zake za kuwaunganisha wadau mbalimbali, ikiwemo Ofisi ya Waziri Mkuu, Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi, uongozi wa mkoa wa Rukwa na halmashauri zake, hatua iliyowezesha kufanyika kwa mafunzo ya utoaji elimu kuhusu fursa za mitaji na huduma za uwezeshaji wa wananchi kiuchumi mkoani Rukwa.

Prof. Shemdoe ametoa pongezi hizo Julai 13, 2026 katika Ukumbi wa Country Hotel mjini Sumbawanga wakati akifungua mafunzo ya utoaji elimu kuhusu fursa za mitaji na huduma za uwezeshaji wa wananchi kiuchumi kwa niaba ya Waziri Mkuu Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, mafunzo ambayo yameratibiwa na Mbunge huyo kwa kushirikiana na Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC).

Prof. Shemdoe amesema kuwa, anaamini mafunzo hayo yatafungua ukurasa mpya wa maendeleo kwa wananchi wa mkoa wa Rukwa, akiwataka washiriki kutumia elimu watakayopata kuanzisha biashara mpya, kuimarisha biashara walizonazo, kuongeza uzalishaji na kuongeza thamani ya bidhaa na mazao wanayozalisha, na kuongeza kwamba mafunzo hayo yameandaliwa kwa lengo la kuwafikia wananchi wa makundi yote, wakiwemo watu wenye ulemavu.

Aidha, Prof. Shemdoe amezielekeza ofisi za mikoa na halmashauri nchini kutenga nafasi za ofisi kwa ajili ya vituo vya uwezeshaji kiuchumi vitakavyohudumia vijana, wanawake, watu wenye ulemavu na makundi mengine maalum yanayojishughulisha na kilimo, ufugaji, uvuvi, umachinga, bodaboda, ufundi na ujasiriamali, ili kujenga taifa lenye uchumi imara, shindani na jumuishi.

"Ninazielekeza ofisi zote za mikoa na halmashauri nchini kuiga mfano wa mkoa wa Rukwa kwa kutenga ofisi za vituo vya uwezeshaji kiuchumi, vitakavyowawezesha wananchi kupata taarifa, ushauri na kuunganishwa na fursa za mitaji na huduma za uwezeshaji ili wananchi wajikwamue kiuchumi," amesema Prof. Shemdoe.

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Mhe. Makongoro Nyerere, amemshukuru Prof. Shemdoe kwa kukubali kumwakilisha Waziri Mkuu Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba katika ufunguzi wa mafunzo hayo, akisema uwepo wake unaonesha dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kuwawezesha kiuchumi vijana, wanawake, watu wenye ulemavu na makundi mengine maalum.

Kwa upande wake, Mhe. Mzindakaya amesema uwepo wa Prof. Shemdoe akimuwakilisha Waziri Mkuu Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba katika ufunguzi wa mafunzo hayo, ni ishara ya namna Serikali inavyothamini jitihada za kuwawezesha wananchi kiuchumi. 

Naye Kaimu Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC), Bw. Gwakisa Bapala, amesema mafunzo hayo yatawawezesha wananchi kunufaika na huduma za mifuko na programu mbalimbali za uwezeshaji kwa ajili ya kuanzisha miradi mipya, kukuza biashara zilizopo, kuongeza thamani ya mazao na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Mkoa wa Rukwa na Taifa kwa ujumla.

Mafunzo hayo yanayofanyika katika halmashauri zote nne za mkoa wa Rukwa kuanzia Julai 13 hadi 16, 2026, yamelenga kuwafikia wananchi zaidi ya 1,000 na kuwapa maarifa yatakayowawezesha kutumia kikamilifu fursa za mitaji na huduma za uwezeshaji kwa maendeleo yao na ya Taifa, fursa ambazo zinatoka katika mifuko na taasisi 15 ikijumuisha NMB, CRDB, Azania Bank, TADB, AGITF, Self MF, BOT, Machinga Fund, YDF, SIDO, Pass Trust, Pass Leasing, EFTA, TaFF na Mfuko wa Utamaduni na Sanaa.
Share:

TRA KUWAZAWADIA VIJANA 1020 WENYE MAWAZO BUNIFU






Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imekuletea mashindano ya Wazo Bunifu yanayolenga kupata suluhisho za kibunifu zitakazochangia kuboresha mfumo wa kodi nchini. Hii ni fursa yako ya kuwasilisha wazo lenye tija na kushindania zawadi ya hadi Shilingi Milioni 50.
Share:

KAPINGA AMKABIDHI MLEMAVU MASHINE YA KUSAGIA VIUNGO



Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga (Mb), amemkabidhi mfanyabiashara mwenye ulemavu, Bi.Esther Mashaka Msengi, mashine ya kusagia viungo ili kuongeza uzalishaji, kupunguza gharama za biashara na kuboresha kipato chake.

Akikabidhi mashine hiyo Julai 13, 2026 katika Viwanja vya Maonyesho ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), amesema aliguswa na changamoto za Esther aliyekuwa akitumia muda na fedha nyingi kusafirisha viungo kwenda kusagwa kabla ya kuvifungasha na kuviuza.

Amesema Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi zake kuhakikisha anaimarisha biashara yake, huku akiitaka BRELA kukamilisha usajili wa nembo ya bidhaa zake, TBS kumsaidia kupata ithibati ya ubora na SIDO kuendelea kumjengea uwezo.

Aidha, amelishukuru Shirika la Uhandisi na Usanifu Mitambo Tanzania TEMDO kwa kuwezesha upatikanaji wa mashine hiyo na kueleza kuwa hatua hiyo inaunga mkono maono ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwawezesha wajasiriamali kuongeza tija.

Kwa upande wake, Bi. Esther Msengi amesema mashine hiyo itapunguza gharama za uzalishaji na kumwezesha kupanua biashara yake.

Mwakilishi wa Shirika la Uhandisi na Usanifu Mitambo Tanzania (TEMDO), Mhandisi. Elisante Mjema, amesema mashine hiyo inaweza kusaga kilo 10 za viungo kwa saa moja na kuongeza uzalishaji hadi kufikia mauzo ya takribani shilingi milioni 1.5 kwa siku endapo kutakuwa na malighafi za kutosha.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMANNE JULAI 14, 2026


Magazetini Leo







Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger