Wednesday, 19 August 2026

MAAFISA BIASHARA WAFUNZWA NAMNA YA KUDHIBITI BIDHAA BANDIA




Na Mwandishi Wetu

Tume ya Ushindani (FCC) imetoa elimu kwa Maafisa Biashara kwa lengo la kuwaongezea uelewa kuhusu masuala ya ushindani katika biashara, udhibiti wa bidhaa bandia pamoja na umuhimu wa kumlinda mlaji dhidi ya bidhaa na huduma zisizokidhi viwango.

Semina hiyo imelenga kuwajengea uwezo Maafisa Biashara ambao wana nafasi muhimu katika kusimamia shughuli za biashara katika maeneo yao, ili waweze kutambua changamoto zinazohusiana na ushindani usio wa haki, bidhaa bandia na vitendo vinavyoweza kuwaathiri walaji.

Akitoa mada kuhusu udhibiti wa bidhaa bandia, wakati wa Mkutano wa Maafisa Biashara nchini katika Kikao cha Tatu cha Wizara ya Viwanda na Biashara na Maafisa Biashara, kilichofanyika kwa siku mbili jijini Dodoma.

Kaimu Mkurugenzi wa Udhibiti wa Bidhaa Bandia wa FCC, Bw. Salvatory Chuwa, ameeleza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya FCC na Maafisa Biashara katika kukabiliana na biashara ya bidhaa bandia.

"Bidhaa bandia zina madhara makubwa kwa uchumi, wafanyabiashara wanaofuata sheria na walaji, hivyo ni muhimu kwa Maafisa Biashara kuwa na uelewa wa kutosha kuhusu namna ya kubaini na kutoa taarifa kuhusu bidhaa zinazodhaniwa kuwa bandia."amesema Bw.Chuwa

Amesisitiza kuwa udhibiti wa bidhaa bandia unahitaji ushirikiano wa karibu kati ya taasisi za Serikali, wafanyabiashara na wananchi, huku akiwataka Maafisa Biashara kutumia nafasi zao kuelimisha wafanyabiashara na walaji kuhusu madhara ya bidhaa bandia.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Tafiti, Miungano ya Makampuni na Uraghibishi wa FCC, Bi. Zaytun Kikula, ametoa mada kuhusu masuala ya ushindani, akieleza umuhimu wa kuwepo kwa mazingira ya biashara yenye ushindani wa haki kwa ajili ya kukuza uchumi na kuwapa wafanyabiashara fursa sawa katika soko.

Bi.Kikula amebainisha kuwa ushindani wenye tija husaidia kuongeza ubunifu, kuboresha ubora wa bidhaa na huduma pamoja na kuwapa walaji fursa ya kupata bidhaa bora kwa bei shindani.

Aidha, amewataka Maafisa Biashara kushirikiana na FCC katika kutoa elimu kwa wafanyabiashara kuhusu sheria za ushindani na kuhakikisha kuwa vitendo vinavyoweza kuzuia au kupotosha ushindani vinatambuliwa na kuchukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria.

Semina hiyo ni sehemu ya jitihada za FCC za kuimarisha uelewa wa wadau kuhusu wajibu wa kulinda ushindani katika soko, kudhibiti bidhaa bandia na kuhakikisha haki za walaji zinalindwa.

FCC imeendelea kusisitiza kuwa ushirikiano wa wadau mbalimbali, hususan Maafisa Biashara, ni muhimu katika kujenga soko lenye ushindani wa haki, bidhaa salama na mazingira bora ya biashara kwa manufaa ya wafanyabiashara, walaji na uchumi kwa ujumla.


Share:

TANZANITE ROYAL GIN YAZIDI KUPAMBA MANYARA TANZANITE MARATHON 2026





Na Mwandishi Wetu, Manyara


Manyara Tanzanite Marathon 2026 inatarajiwa kuwa na burudani ya aina yake baada ya wasanii maarufu nchini, Dully Sykes, Banana Zoro na Mr Blue, kuthibitisha kushiriki na kutumbuiza katika tukio hilo litakalofanyika Agosti 22, 2026 mjini Babati, mkoani Manyara.


Ushiriki wa wasanii hao umewezeshwa na kampuni ya Mati Super Brands Ltd kupitia kinywaji chake cha Tanzanite Royal Gin, hatua inayoongeza ushiriki wa sekta binafsi katika kufanikisha mbio hizo zinazolenga kuunganisha michezo, burudani na shughuli za kijamii.



Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Queen Sendiga, amekabidhi wasanii hao T-shirt rasmi za Manyara Tanzanite Marathon, ikiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea tukio hilo ambalo limeendelea kupata mwitikio kutoka kwa wadau mbalimbali.


Manyara Tanzanite Marathon 2026 imebeba kaulimbiu “Hatua Moja Okoa Maisha”, ikiwa na lengo la kukusanya Shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa wodi maalumu ya kuwahudumia watoto njiti wanaozaliwa kabla ya wakati.



Ujio wa Dully Sykes, Banana Zoro na Mr Blue unatarajiwa kuongeza hamasa kwa wanariadha, vikundi vya jogging na wananchi watakaoshiriki au kujitokeza kushuhudia mbio hizo. Burudani hiyo pia inalenga kuwapa washiriki na watazamaji uzoefu wa kipekee huku ikihamasisha jamii kuunga mkono kampeni ya kuokoa maisha ya watoto njiti..



Mchango wa Mati Super Brands Ltd kupitia Tanzanite Royal Gin unaendelea kuonesha nafasi ya sekta binafsi katika kusaidia shughuli zenye manufaa kwa jamii. Ushiriki huo unatarajiwa kuongeza mvuto wa marathon na kuwafikia watu wengi zaidi kupitia michezo na burudani.


Kwa ujumla, Manyara Tanzanite Marathon 2026 inatarajiwa kuwa jukwaa linalounganisha michezo, burudani, utalii na uwajibikaji kwa jamii, huku kila hatua ya washiriki ikilenga kuchangia upatikanaji wa huduma bora kwa watoto njiti mkoani Manyara.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMATANO AGOSTI 19,2026


Magazeti



Share:

EADB YAMWAGA UFADHILI WA MIL 240 MICHEZO YA FEASSA, TANZANIA YAKAMIA KUFANYA VIZURI



Mashindano ya 23 ya Shirikisho la Michezo ya Shule za Sekondari Afrika Mashariki (FEASSA) yamepata msukumo mkubwa baada ya Benki ya Maendeleo ya Afrika Mashariki (EADB) kutoa udhamini wa Dola za Marekani 90,000, (takribani mil 240) katika kuunga mkono maandalizi na uendeshaji wa mashindano ya shirikisho hilo yanayoendelea mkoani Morogoro.

Mashindano hayo makubwa zaidi ya michezo ya shule katika ukanda wa Afrika Mashariki yamezikutanisha timu 413 na washiriki 5,548 kutoka nchi mbalimbali za Afrika Mashariki, zinazoshindana katika aina 51 za michezo. Mashindano hayo yanatarajiwa kuhitimishwa Agosti 22, 2026.

Akizungumza katika hafla rasmi ya ufunguzi wa mashindano hayo, Meneja wa EADB nchini Tanzania, Bw. Stephen Wambura, alisema ushirikiano wa Benki hiyo na FEASSA unaakisi dhamira ya EADB ya kuwekeza kwa vijana na kuunga mkono mipango inayochangia maendeleo endelevu katika Afrika Mashariki.

“Ingawa jukumu letu kuu ni kufadhili miradi ya maendeleo katika sekta mbalimbali muhimu za uchumi, tunatambua kuwa maendeleo endelevu hayaishii kwenye miundombinu na shughuli za biashara. Pia yanahusisha kuwawezesha watu, hususan vijana, ambao ndio msingi wa mustakabali wa ukanda wetu,” alisema Bw. Wambura.

Alisema dhamira hiyo ndiyo iliyochochea uamuzi wa EADB kuwa mdhamini mkuu wa Mashindano ya 23 ya FEASSA, kwa kutoa mchango wa Dola za Marekani 90,000 kwa ajili ya kuwezesha mashindano hayo kufanyika kwa mafanikio.

“Udhamini wa michezo ni mojawapo ya nguzo muhimu katika ajenda yetu ya Mipango ya Uwajibikaji wa Kijamii wa Kampuni (CSI), kwa sababu tunaelewa uwezo mkubwa wa michezo katika kujenga tabia, kuhamasisha mtindo bora wa maisha na kufungua fursa kwa vijana katika ukanda wetu,” aliongeza.

“Kupitia udhamini huu, hatuwekezi tu katika mashindano haya, bali pia tunawekeza katika kuwaandaa kizazi kijacho cha viongozi wa Afrika Mashariki.”

Kwa mujibu wa makubaliano ya udhamini, EADB inasaidia utengenezaji wa medali na vikombe kwa ajili ya washindi, pamoja na upatikanaji wa sare za michezo kwa washiriki watakaoshiriki katika hatua za fainali.

Ikiwa mwenyeji wa mashindano ya mwaka huu, Tanzania imetuma moja ya vikosi vikubwa zaidi, ikiwa na timu 127 na washiriki 1,704 wanaoshiriki katika michezo mbalimbali.

Katika mpira wa miguu kwa wavulana, Tanzania inawakilishwa na Shule za Sekondari Nsumba, Mbeya Day, Morogoro na Urambo Day, ambazo zitakuwa na jukumu la kutetea heshima ya nchi katika mashindano hayo.

Kwa upande wa mpira wa miguu kwa wasichana, Tanzania inawakilishwa na Shule za Sekondari Ziba, Fountain Gate na Kilombero, ambazo zinatarajiwa kutumia vyema fursa ya kucheza mbele ya mashabiki wa nyumbani katika kuwania nafasi za juu.

Tanzania pia inalenga kufanya vizuri katika mpira wa wavu. Katika upande wa wavulana, Shule za Sekondari Lumala, Kaliua na Kajunjumele ndizo zinazobeba matumaini ya Tanzania, huku Mengele, Lumala na Mwanhuzi zikiiwakilisha nchi katika mashindano ya wasichana.

Mpira wa kikapu ni miongoni mwa michezo ambayo Tanzania inalenga kutumia vizuri fursa ya kucheza nyumbani. Katika mashindano ya wavulana ya 5x5, Tanzania inawakilishwa na Shule za Sekondari Nsumba, St Jude na Juhudi.

Kwa upande wa wasichana wa 5x5, Shule za Sekondari Orkeeswa, Uru Community na Rungwa ndizo zitakazobeba matumaini ya Tanzania.

Tanzania pia inatarajia kupata matokeo mazuri katika netiboli, mchezo ambao kwa muda mrefu umekuwa miongoni mwa michezo ambayo Tanzania imekuwa ikitoa timu zenye ushindani mkubwa. Shule za Sekondari Mkolani, Vwawa na Mbeya ni miongoni mwa timu zinazotarajiwa kuongoza kinyang’anyiro cha Tanzania katika mchezo huo.

Kwa kuwakutanisha maelfu ya vijana kutoka nchi mbalimbali za Afrika Mashariki, Michezo ya FEASSA haitoi tu jukwaa la ushindani wa kimichezo, bali pia inawapa vijana fursa ya kukuza vipaji, nidhamu, mshikamano, uwezo wa kufanya kazi kwa pamoja na uongozi, huku ikichangia kuimarisha mshikamano na ushirikiano wa kikanda kupitia michezo.

Kadiri mashindano yanavyoelekea kileleni kuelekea tarehe 22 Agosti, Tanzania inalenga kutumia vyema faida ya kuwa mwenyeji ili kujinyakulia medali katika michezo mbalimbali. Kwa upande wake, udhamini wa EADB unaendelea kusisitiza dhamira ya Benki hiyo ya kuunga mkono mipango inayowekeza katika vijana na kuchangia maendeleo ya muda mrefu ya Afrika Mashariki.

Meneja wa Benki ya Maendeleo ya Afrika Mashariki (EADB), Bw. Stephen Wambura (kulia), akikabidhi rasmi sare za michezo kwa Rais wa Shirikisho la Michezo ya Shule za Sekondari Afrika Mashariki (FEASSA), Bw. Justus Mugisha, kwa ajili ya kutumiwa na timu zinazoshiriki katika hatua za fainali za Michezo ya FEASSA zinazoendelea Morogoro, Tanzania. Sare hizo ni sehemu ya udhamini wa Dola za Marekani 90,000 ( takribani mil 240) kutoka EADB kwa ajili ya kufanikisha toleo la 23 la mashindano hayo ya michezo ya shule katika ukanda wa Afrika Mashariki, ambayo yamewakutanisha timu 413 na washiriki 5,548 kutoka nchi mbalimbali za Afrika Mashariki.
Share:

Tuesday, 18 August 2026

MWENGE WA UHURU WAZINDUA TAWI LA CRDB MAGANZO, SHINYANGA, WANANCHI WASOGEZEWA HUDUMA NA FURSA ZA MIKOPO

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2026, Wazo Michael Mwang’onda (kulia) baada ya kufungua rasmi Tawi la Benki ya CRDB Maganzo, Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga, Agosti 18, 2026.
Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2026, Wazo Michael Mwang’onda akikata keki wakati akifungua rasmi Tawi la Benki ya CRDB Maganzo, Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga, Agosti 18, 2026.
Mkurugenzi wa Mikopo wa Benki ya CRDB, Xavery Makwi, akitoa taarifa kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dkt. Abdulmajid Mussa Nsekela, wakati wa uzinduzi wa Tawi la CRDB Maganzo, Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga, Agosti 18, 2026.
Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2026 ukiwa katika Benki ya CRDB Maganzo, Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga, wakati wa uzinduzi wa tawi hilo, Agosti 18, 2026.
Wafanyakazi wa Benki ya CRDB wakifurahia wakati wa uzinduzi wa Tawi la CRDB Maganzo, Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga.
Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2026 ukiondoka katika Tawi la Benki ya CRDB Maganzo, Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga, baada ya uzinduzi wa tawi hilo, Agosti 18, 2026.

Na Kadama Malunde & Elizabeth Cosmas Shinyanga

Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2026 umezindua rasmi Tawi la Benki ya CRDB Maganzo, Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga, huku benki hiyo ikiahidi kuongeza fursa za huduma za kifedha kwa wakulima, wafugaji, wafanyabiashara, wastaafu, vijana na wananchi wengine katika eneo hilo.

Tawi hilo limezinduliwa leo Jumanne, Agosti 18, 2026, na Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2026, Wazo Michael Mwang’onda, ambaye ameridhishwa na uwekezaji huo akieleza kuwa utaongeza upatikanaji wa huduma za kibenki kwa wananchi wa Maganzo na maeneo jirani.

Mwang’onda ameishukuru Serikali inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuweka mazingira rafiki kwa uwekezaji na kufanya taasisi za fedha, ikiwemo CRDB, kuendelea kupanua huduma zake nchini.

Amesema mazingira hayo yameiwezesha CRDB kuendelea kuwafikia wananchi katika maeneo mbalimbali na kutoa huduma zinazolenga kuchochea shughuli za kiuchumi, huku akisisitiza umuhimu wa wananchi kutumia fursa zinazotolewa na benki hiyo.

“Awali ya yote nipende kuishukuru Serikali yetu chini ya kiongozi wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuweka mazingira rafiki katika Benki yetu ya CRDB, kwani kupitia uwekezaji huo benki hii haina mikwamo tena katika kuwahudumia Watanzania kwa ujumla na wananchi wa Maganzo hii leo,” amesema Mwang’onda.
Aidha, Mwang’onda ameipongeza CRDB kwa kuona fursa ya biashara na kufungua tawi hilo Maganzo, akisema benki hiyo imekuwa ikipanua huduma zake katika maeneo mbalimbali nchini pale inapobaini mahitaji ya wananchi.

Ameeleza kuwa uwepo wa tawi hilo ni fursa muhimu kwa wakulima, wafanyabiashara na wananchi wengine kupata huduma za kifedha karibu na maeneo yao, ikiwemo mikopo na huduma nyingine zitakazosaidia kukuza shughuli zao za kiuchumi.

Mwang’onda pia amewataka wananchi kuendelea kutumia huduma za CRDB, akieleza kuwa benki hiyo imekuwa ikitoa fursa mbalimbali kwa wananchi, ikiwemo mikopo ya kilimo na uwezeshaji wa shughuli za uzalishaji.

“Niendelee kumpongeza Mkurugenzi wa Mikopo kwa kuendelea kutoa mikopo rafiki kwa wateja, lengo kuu ni kuhakikisha wateja wake wanapata huduma zenye ubora wa hali ya juu,” amesema.

Amesema Serikali pia imeendelea kuweka fedha kwa ajili ya kuwawezesha vijana kiuchumi, huku CRDB ikiwa miongoni mwa taasisi zinazoshiriki katika kuwawezesha wananchi kupitia huduma za kifedha.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Mikopo wa Benki ya CRDB, Xavery Makwi, akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dkt. Abdulmajid Mussa Nsekela, amesema uzinduzi wa tawi hilo utafungua fursa mbalimbali za huduma za kifedha kwa wananchi wa Maganzo na maeneo jirani.
Makwi amesema kupitia tawi hilo huduma za CRDB zitapatikana kwa urahisi zaidi na kwa kasi, huku wakulima na wafugaji wakipata fursa ya kupata mikopo kwa ajili ya kuendeleza shughuli zao za uzalishaji.

“Kupitia tawi hili fursa mbalimbali zitapatikana hapa, huduma zetu zimemulikwa, zitakuwa na kasi zaidi. Kutakuwa na fursa kwa wakulima na wafugaji ambapo mikopo itapatikana,” amesema Makwi.

Amesema pia tawi hilo litawahudumia wastaafu kwa kuwawezesha kuhifadhi fedha zao kwa usalama na kutumia huduma mbalimbali za benki, hivyo kupunguza changamoto zinazoweza kujitokeza endapo fedha zitahifadhiwa bila kutumia mfumo rasmi wa kibenki.

Makwi amewaalika wananchi wa Maganzo na maeneo jirani kufungua akaunti CRDB na kutumia huduma zinazotolewa na benki hiyo ili kunufaika na fursa mbalimbali za kifedha.

“Tunawashukuru sana wananchi kwa kuendelea kutumia huduma zetu,” amesema.

Tawi la CRDB Maganzo limejengwa kwa lengo la kuimarisha huduma za kibenki na kuboresha mazingira ya utoaji wa huduma kwa wateja wanaojihusisha na shughuli mbalimbali za kiuchumi katika eneo hilo.
Shughuli hizo ni pamoja na uchimbaji na uuzaji wa madini, kilimo cha zao la pamba, nyanya na mazao mengine ya chakula, ufugaji wa ng’ombe na mbuzi, pamoja na shughuli zinazohusiana na biashara na usafirishaji wa bidhaa na abiria.

Ujenzi wa Tawi la CRDB Maganzo umegharimu takribani Shilingi milioni 700, fedha zilizotumika kwa ajili ya ununuzi wa ardhi, ujenzi wa jengo na vifaa.

Wananchi wa Maganzo wameishukuru Benki ya CRDB kwa kufungua tawi hilo katika eneo lao, wakisema kusogezewa huduma za kibenki karibu kutawarahisishia kupata huduma bila kusafiri umbali mrefu.

Wamesema uwepo wa tawi hilo utaongeza fursa za kiuchumi kwa wakulima, wafugaji na wafanyabiashara, ikiwemo kupata mikopo na huduma nyingine za kifedha, huku wakiahidi kutumia fursa hizo kukuza shughuli zao za kiuchumi.
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger