Saturday, 22 August 2026

NEMC NA JNHPP: USIMAMIZI WA MAZINGIRA KATIKA MIRADI YA KIMKAKATI


Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limeshiriki kikamilifu katika uzinduzi wa Mradi wa Kufua Umeme wa Julius Nyerere (JNHPP), unaofanywa leo na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa jukumu la lake la kusimamia na kudhibiti masuala ya mazingira katika miradi ya maendeleo nchini.

Ushiriki wa NEMC katika uzinduzi wa mradi huu wa kimkakati unaakisi dhamira ya Serikali ya kuhakikisha kuwa maendeleo ya sekta ya nishati yanaenda sambamba na ulinzi na uhifadhi wa mazingira.

Akieleza ushiriki wa NEMC katika hafla hiyo, Mkurugenzi Mkuu Dkt. Immaculate Sware Semesi amesema NEMC inaendelea kuhakikisha kuwa utekelezaji wa mradi wa JNHPP unazingatia Sheria, Kanuni, miongozo na masharti ya mazingira yaliyowekwa.

Amesema katika kutekeleza majukumu yake, NEMC imeendelea kufuatilia uzingatiaji wa masharti ya Tathmini ya Athari kwa Mazingira na Jamii (TAM), ikiwemo ufuatiliaji wa ubora wa maji, hewa na udongo, usimamizi wa taka, udhibiti wa uchafuzi pamoja na utekelezaji wa hatua za kupunguza athari za kimazingira.

Aidha, NEMC inaendelea kusimamia masuala ya uhifadhi wa bioanuwai, ulinzi wa Mto Rufiji na mifumo yake ya ikolojia, kuhakikisha shughuli za mradi zinafanyika kwa kuzingatia wajibu wa kulinda mazingira na rasilimali za asili kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

NEMC itaendelea kushirikiana na Serikali, taasisi na wadau mbalimbali katika kuhakikisha JNHPP, kama mradi muhimu wa kimkakati kwa Taifa, unatekelezwa kwa kuzingatia misingi ya maendeleo endelevu, huku ulinzi wa mazingira ukipewa kipaumbele. NEMC: Mazingira Salama, Maendeleo Endelevu.


Share:

TFS YATUMIA JOGGING KAMA SEHEMU YA KUJIIMARISHA KIAFYA


WAFANYAKAZI wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Kanda ya Mashariki wamefanya mazoezi ya kukimbia umbali wa takribani kilomita saba katika eneo la Coco Beach jijini Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya kujiweka katika hali nzuri ya kiafya na utayari wa kutekeleza majukumu yao.

Akizungumza baada ya zoezi hilo leo Agosti 22, 2026 Jijini Dar es Salaam, Mhifadhi Mwandamizi wa TFS, Sunday Nachule, kwa niaba ya Kamanda wa Kanda ya Mashariki, amesema mazoezi hayo ni sehemu ya juhudi za kuhakikisha askari wanakuwa timamu muda wote kwa ajili ya kutekeleza majukumu yao.

Amesema TFS itaendelea kuhamasisha watumishi wake kushiriki katika mazoezi ya mwili mara kwa mara ili kujenga afya na utayari wa kiutendaji.

Katika zoezi hilo, wanafamilia wa TFS wamepata pia fursa ya kufanya mazoezi pamoja na Mbunge wa Jimbo la Buchosa, Eric Shigongo, ambaye amewapongeza kwa juhudi hizo na kuwataka kuendelea na mazoezi.

Shigongo amesema misitu ni muhimu kwa uhai wa binadamu kutokana na mchango wake katika upatikanaji wa hewa safi na maji, hivyo wananchi wanapaswa kushirikiana na Serikali katika kuilinda.

Ametaja maeneo ya Buhindi na Lubondo yaliyopo katika Jimbo la Buchosa kuwa miongoni mwa maeneo yenye misitu inayosimamiwa na TFS, akisisitiza umuhimu wa wananchi kutunza rasilimali hiyo.

“Bila misitu hakuna uhai. Kwa hiyo nawaomba Watanzania waendelee kutunza misitu kwa sababu ni chanzo cha hewa na maji,” amesema Shigongo.

Aidha, ameipongeza TFS kwa kazi inayofanya katika kulinda na kuhifadhi misitu nchini, akieleza kuwa wananchi wanapaswa kuwa wadau wa uhifadhi kwa kuhakikisha rasilimali hiyo inalindwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Share:

DKT. YONAZI AWAKUMBUSHA VIJANA KULINDA AFYA ZAO KATIKA MAPAMBANO DHIDI YA UKIMWI



Na. Mwandishi Wetu ,Kazuramimba Kigoma

Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dkt. Jim Yonazi, Amewaasa vijana kulinda afya zao na kuepuka tabia hatarishi ili kupunguza maambukizi mapya ya VVU, kwa kuzingatia kuwa ni kundi linaloongoza kuwa hatarini zaidi nchini Tanzania.

Dkt. Yonazi ameyasema hayo mwishoni mwa wiki wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa Afua za UKIMWI Wilaya ya Uvinza Mkoa wa Kigoma alipoambatana na Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania, Dkt. Adam Mrisho, timu ya wataalam kutoka Ofisi yake, Wizara ya Afya, TAMISEMI na Ofisi ya Mkoa huo.

Aidha amepata wasaa kutembelea Kituo cha Maarifa Kata ya Kazuramimba mkoani humo kinachotoa huduma za masuala ya VVU na UKIMWI, na kukutana na vijana wanaotekeleza afua za UKIMWI kupitia vikundi vya uzalishaji mali kwa lengo la kujiinua kiuchumi na kujiletea maendeleo yao.

Akiwa katika kituo hicho, Dkt. Yonazi amepokea taarifa kutoka kwa mwenyekiti wa kikundi, Billy Sekibaha, kuhusu shughuli zinazofanywa na kikundi hicho ikiwemo za biashara ndogondogo za kuuza dagaa pamoja na shunguli za ushonaji wa nguo kwa lengo la kujikwamua kiuchumi na kuondokana na dhana ya utegemezi.

Amesisitiza kuwa, kundi la vijana linategemewa na Taifa katika shughuli za uzalishaji mali na kujiletea maendeleo yao na Taifa kwa ujumla hivyo ni vyema vijana wakaendelea kujilinda na kulinda wengine kwa kutambua hali zao na endapo wakagundulika kuwa na maambukizi ya VVU inashauriwa kuanza kutumia dawa mapema.

"Mnafanya kazi nzuri sana, endeleeni kuchangamkia uwepo wa mitandao ya kijamii kutangaza bidhaa zenu ili kuwafikia wateja wengi zaidi na kujitangaza kitaifa na kimataifa," alisisitiza Dkt. Yonazi

Kwa upande wake Mtendaji wa TACAIDS, Dkt. Adam Mrisho amewapongeza vijana hao kwa kazi nzuri wanazofanya na kusisitiza kuwa Tume itaendelea kuwawezesha vijana kiuchumi na kuwajengea uwezo ili kuendeleza mapambano dhidi ya maambukizi mapya ya VVU na kufikia lengo la kutokomeza UKIMWI ifikapo mwaka 2030.











Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMAMOSI AGOSTI 22,2026




magazeti


Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger