Monday, 20 July 2026

WAZIRI SANGU: UANAGENZI UTAWATOA VIJANA KIMAISHA




Serikali ya Awamu ya Sita imeendelea kuimarisha programu ya mafunzo ya uanagenzi kama mkakati madhubuti wa kuwajengea vijana stadi za kazi zitakazowawezesha kujiajiri na kuajiri wengine, hatua inayolenga kuongeza fursa za ajira na kukuza uchumi wa Taifa.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mheshimiwa Deus Sangu, amesema hayo Julai 18, 2026, wakati alipokagua utekelezaji wa mafunzo hayo katika Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST), Kampasi ya Rukwa.
Waziri Sangu alibainisha kuwa katika mwaka wa fedha 2025/26, Serikali chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, imewezesha vijana 5,746 kupata mafunzo ya uanagenzi katika vyuo 46 nchini kwa kugharamia ada, bima ya afya, na nauli za mafunzo kwa vitendo.


Uwekezaji huu unaonesha dhamira ya Serikali ya kuwawezesha vijana kupata ujuzi unaokidhi soko la ajira, huku Waziri Sangu akiahidi kuwa kuanzia mwaka 2026, wahitimu wataanza kupatiwa vifaa vya kuanzia kazi ili kuwawezesha kujiajiri mara moja.


Akizungumzia utekelezaji wa programu hiyo mkoani Rukwa, Mkurugenzi wa Ajira na Ukuzaji Ujuzi, Alana Nchimbi, alieleza kuwa mkoa una vyuo viwili vinavyoshiriki, ambavyo ni MUST Kampasi ya Rukwa yenye wanagenzi 154 na Chuo cha Kilimo na Mifugo Laela chenye wanagenzi 120.


Mkuu wa Kampasi ya MUST Rukwa, Prof. Asheri Mwidege, aliongeza kuwa mafunzo hayo yamewawezesha wanagenzi kupata umahiri wa vitendo, ikiwemo ujenzi wa mageti na ukarabati wa hosteli ndani ya chuo, huku akishukuru Serikali kwa kugharamia bima ya afya na nauli kwa asilimia 100, hatua iliyoongeza ari ya vijana.


Mkuu wa Wilaya ya Sumbawanga, Mheshimiwa Nyakia Ally Chirukie, alipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu kwa uratibu huo ambao umekuwa chachu ya uwezeshaji kwa vijana wa wilaya hiyo.


Wanagenzi wenyewe wameeleza kufurahishwa na mafunzo hayo ambayo yamekuwa suluhisho la changamoto ya ukosefu wa ajira. Digna Sebastian John, mhitimu wa chuo kikuu aliyebadili mwelekeo na kuanza kujifunza ufundi bomba, alibainisha kuwa ujuzi huo unampa uhakika wa kujiajiri.


Kwa upande wake, Ismail William Mbogo, ambaye awali alikuwa akijishughulikia na kilimo cha mpunga katika Bonde la Ziwa Rukwa, alitoa ushuhuda kuwa ndani ya miezi sita pekee amejenga uwezo mkubwa wa ufundi unaomfanya sasa kupata ajira za muda katika vijiji vinavyozunguka chuo hicho.


Ujumbe huu unadhihirisha kuwa programu ya uanagenzi si tu inatoa ujuzi, bali inabadilisha maisha ya vijana kutoka kwenye shughuli za kawaida na kuwaweka kwenye mkondo wa wataalamu wanaochangia moja kwa moja katika maendeleo ya jamii na uchumi wa nchi.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMATATU JULAI 20, 2026

Share:

Sunday, 19 July 2026

MASAUNI: UHIFADHI WA UDONGO NI MSINGI WA MAENDELEO ENDELEVU

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni, akizungumza na wadau mbalimbali wa mazingira kabla ya kushiriki matembezi yaliyolenga kuhamashisha jamii katika Uhifadhi na Utunzaji wa Mazingira yaliyofanyika Julai 19, 2026 jijini Dar es Salaam.

*************

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, chini ya uongozi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, inaendelea kuimarisha juhudi za kuhakikisha kuwa masuala ya uendelevu wa mazingira yanapewa kipaumbele katika ajenda ya maendeleo ya Taifa.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni, aliposhiriki matembezi yaliyolenga kuhamashisha jamii katika Uhifadhi na Utunzaji wa Mazingira ‘Save Soil Walkathon’ yaliyofanyika Julai 19, 2026 jijini Dar es Salaam.

Mhe Masauni amesema, ahadi hii inaonyeshwa wazi katika Dira ya Maendeleo ya Tanzania ya 2050, haswa nguzo yake ya Tatu, ambayo inatambua uendelevu wa mazingira na ustahimilivu wa hali ya hewa kama misingi muhimu wa kufikia mabadiliko ya kiuchumi jumuishi ya kijani kibichi na endelevu.

Ameongeza kuwa afya ya udongo ni msingi wa usalama wa chakula, uhifadhi wa mazingira na ustawi wa uchumi wa taifa, hivyo kuna umuhimu wa kila Mtanzania kushiriki katika juhudi za kuutunza.

"Udongo ni rasilimali muhimu inayobeba maisha yetu ya kila siku. Bila udongo wenye afya hatuwezi kuwa na usalama wa chakula, mazingira bora wala maendeleo endelevu. Ni wajibu wa kila Mtanzania kushiriki katika juhudi za kulinda mazingira na kutumia ardhi kwa njia zinazohifadhi uhai wake kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho," amesema Mhe. Masauni.

“Tunapoanza kutekeleza Mpango huu wenye kuleta mabadiliko makubwa, tunaona fursa nyingi za kuimarisha ushirikiano wetu na Jamhuri ya India. Tunatarajia kuendeleza ushirikiano katika nyanja mbalimbali kama vile uhamishaji wa teknolojia, utafiti na uvumbuzi, ujenzi wa uwezo, urejeshaji endelevu wa ardhi, ufuatiliaji wa mazingira, uwekezaji rafiki kwa mazingira na suluhisho zinazozingatia kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.” Amesisitiza Mhe. Masauni.

Kwa upande wake, Rais wa Lions Club of Dar es Salaam Mazingira, Bi. Lion Ramadevi, amesema ‘Save Soil Walkathon’ ni sehemu ya kampeni pana inayolenga kuhamasisha jamii kutambua mchango mkubwa wa udongo katika maendeleo ya kiuchumi, kijamii na kimazingira.

"Save Soil Walkathon si matembezi pekee, bali ni harakati ya kuhamasisha mabadiliko ya tabia na kuwajengea wananchi uelewa wa umuhimu wa kulinda udongo. Tunataka kuona jamii, taasisi na sekta binafsi zikichukua hatua za pamoja katika kuhifadhi mazingira kwa mustakabali wa taifa letu," alisema Lion Ramadevi.

Naye Balozi wa India nchini Tanzania Mhe. Lakshay Anand amesema ni jambo jema kuona jamii inatambua umuhimu wa kulinda mazingira na huo ndio msingi wa Maisha ya binadamu ya kuhakikisha kila mmoja anakua sehemu ya kutunza mazingira.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni, akizungumza na wadau mbalimbali wa mazingira alipowasili eneo la Swami Vivekananda Culture Centre jijini Dar es Salaam kushiriki matembezi yaliyolenga kuhamashisha jamii katika Uhifadhi na Utunzaji wa Mazingira yaliyofanyika Julai 19, 2026.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni, akimwakilia maji mti mara baada ya kuupanda ikiwa ni ishara ya kuunga mkono juhudi za utunzaji wa mazingira, wakati aliposhiriki matembezi yaliyolenga kuhamashisha jamii katika Uhifadhi na Utunzaji wa Mazingira yaliyofanyika Julai 19, 2026 jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni, akipanda mti ikiwa ni ishara ya kuunga mkono juhudi za utunzaji wa mazingira, wakati aliposhiriki matembezi yaliyolenga kuhamashisha jamii katika Uhifadhi na Utunzaji wa Mazingira iliyofanyika Julai 19, 2026 jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni (katikati), akishiriki matembezi yaliyolenga kuhamashisha jamii katika Uhifadhi na Utunzaji wa Mazingira yaliyofanyika Julai 19, 2026 jijini Dar es Salaam.
Share:

KATAMBI: SERIKALI HAITAVUMILIA WANAOTUMIA HAKI ZA BINADAMU KAMA KIVULI CHA KUVURUGA AMANI



Na Mwandishi Wetu, Shinyanga

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Patrobas Katambi, amesema Serikali haitaruhusu kundi la watu wachache kutumia hoja za haki za binadamu na demokrasia kama kivuli cha kuvuruga amani na utulivu wa Tanzania, akisisitiza kuwa yuko tayari kufika mahakamani wakati wowote endapo ataitwa.

Katambi amesema kauli na vitendo vinavyochochea chuki, vurugu na machafuko haviwezi kuvumiliwa, huku akieleza kuwa dhamira ya Serikali ni kuhakikisha wananchi wanaendelea kuishi katika mazingira ya amani na usalama.

Akizungumza nyakati tofauti na makundi ya walinzi wa amani katika jamii, Polisi Jamii, Sungusungu, wazee, wenyeviti wa mitaa, mabalozi na viongozi wa vitongoji mjini Shinyanga, Waziri huyo alisema wanaomtishia kumpeleka mahakamani wanafanya hivyo kutokana na kushindwa kufanikisha ajenda zao za kuhamasisha maandamano.

Katambi alisema kupotea kwa amani kuna madhara makubwa kwa uchumi wa nchi, ikiwemo kupungua kwa watalii, kukimbia kwa wawekezaji, kusimama kwa miradi ya maendeleo na kudhoofika kwa mahusiano ya kidiplomasia.

"Wanajua wakiichafua Tanzania yetu na amani ikapotea tutapoteza mvuto kwa watalii, nchi inaweza kuwekewa vikwazo, miradi mikubwa ya maendeleo itasimama, wawekezaji wataondoka na mapato muhimu ya taifa yataathirika," alisema Katambi.

Aidha, alihoji kwa nini wanaojinasibu kutetea haki za binadamu hawajawahi kukemea hadharani vitendo vya uchomaji wa shule, vituo vya mafuta, ofisi za Serikali, biashara za watu binafsi pamoja na mashambulizi dhidi ya vituo vya polisi.

Kwa mujibu wa Waziri huyo, machafuko yanapoibuka waathirika wakubwa huwa ni wananchi wa kawaida, hususan wanawake, watoto, wazee na watu wenye ulemavu.

"Watoto wao na familia zao wako nje ya nchi, lakini machafuko yakitokea ni wananchi wa kawaida watakaobeba mzigo wake. Tanzania ndiyo nchi yetu pekee na hatuwezi kukubali ifikie hatua ya wananchi wake kuwa wakimbizi," alisema.

Katambi alitolea mfano baadhi ya nchi za ukanda wa Afrika zilizowahi kukumbwa na migogoro, akisema Tanzania imekuwa ikiwahifadhi wakimbizi kwa miaka mingi, hivyo hakuna sababu ya kuruhusu mazingira yanayoweza kuisukuma nchi katika hali kama hiyo.

Kuhusu madai ya kuvunja Katiba, Waziri huyo alisema Mahakama ndiyo chombo pekee chenye mamlaka ya kutoa uamuzi kuhusu tafsiri na uvunjifu wa Katiba, na si watu binafsi au taasisi nyingine.

Alisema hadi sasa hajapokea wito wowote wa kwenda mahakamani, lakini akisisitiza kuwa yuko tayari kuitikia wito huo wakati wowote, hata usiku wa manane, kwa kuwa anaamini katika utawala wa sheria na kuheshimu mamlaka ya Mahakama.

Katambi alihitimisha kwa kuwataka Watanzania kuendelea kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama kulinda amani, akisisitiza kuwa utulivu wa nchi ndiyo msingi wa maendeleo, uwekezaji na ustawi wa wananchi.
Share:

Saturday, 18 July 2026

SERIKALI IMEWEKEZA BILIONI 2.8 KUBORESHA AFYA, BARABARA, ELIMU YA AMALI GAIRO - PROF. SHEMDOE


Uwekezaji huo ni sehemu ya zaidi ya Shilingi Bilioni 100 zilizotolewa na Serikali ya Awamu ya Sita katika wilaya hiyo

Na. OWM–TAMISEMI, Gairo

Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imewekeza Shilingi bilioni 2.8 katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya Kituo cha Afya Chanjale, Barabara ya Confort Pub–Magoweko na Shule ya Amali Kwipipa, hatua iliyoboresha upatikanaji wa huduma za afya, kurahisisha usafiri na usafirishaji pamoja na kupanua fursa za elimu ya amali kwa wananchi wa wilaya ya Gairo.

Hayo yameelezwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, Julai 17, 2026 katika kijiji cha Kwipipa, kata ya Rubeho, wilaya ya Gairo, baada ya kukagua na kuweka mawe ya msingi katika miradi hiyo ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuhimiza uwajibikaji kwa watumishi wa umma.

Prof. Shemdoe amesema miradi hiyo inaonesha dhamira ya Serikali ya kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora karibu na maeneo wanayoishi kupitia uwekezaji unaogusa maisha yao ya kila siku.

"Leo nimekagua miradi mitatu muhimu. Mradi wa Kituo cha Afya Chanjale wenye thamani ya Shilingi Milioni 680, Barabara ya Confort Pub–Magoweko yenye thamani ya Shilingi Milioni 470 na Shule ya Amali Kwipipa yenye thamani ya Shilingi Bilioni 1.6.  Miradi hii ni matokeo ya fedha zinazotolewa na Serikali kwa ajili ya kuboresha maisha ya wananchi," amesema Prof. Shemdoe.

Akizungumzia Shule ya Amali Kwipipa, Prof. Shemdoe amesema shule hiyo imebobea katika mafunzo ya uhandisi na itakuwa chachu ya kuandaa wataalamu wenye ujuzi watakaoshiriki katika ujenzi wa taifa na maendeleo ya sekta mbalimbali za uzalishaji na amewataka wanafunzi wa shule hiyo kuitunza miundombinu yake ili idumu kwa muda mrefu na kuendelea kunufaisha vizazi vya sasa na vijavyo.

Prof. Shemdoe ameainisha kuwa, uwekezaji huo ni sehemu ya jitihada kubwa zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita, akieleza kuwa tangu Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan aingie madarakani, Halmashauri ya Wilaya ya Gairo imepokea zaidi ya Shilingi Bilioni 100 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo.

Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Gairo, Mhe. Ahmed Shabiby, amewapongeza wananchi wa kijiji cha Kwipipa kwa kujitolea eneo lililowezesha ujenzi wa shule ya Amali, yenye manufaa kwa wananchi wa Gairo na taifa kwa ujumla, Aidha ameipongeza TAMISEMI kwa kutenga bajeti ya chakula kwa wanafunzi wa shule hiyo, hatua itakayochangia kuboresha mazingira bora ya kujifunzia na kufundishia.

Naye, Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Josephine Kapoma, amesema Shule ya Amali Kwipipa itasaidia taifa kupata wahandisi wazawa wenye ujuzi na tija kwa taifa, hivyo amemuomba Prof. Shemdoe amfikishie salamu Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kuwa wananchi wa Kwipipa wameipokea shule hiyo kwa furaha kutokana na mchango wake katika kuinua elimu ya ufundi nchini.











Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMAMOSI JULAI 18,2026 Friday, July 17, 2026


Magazetini Leo





















Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger