Sunday, 17 May 2026
Saturday, 16 May 2026
DIWANI MABAO AWASHUKURU WANANCHI NGOGWA KWA KUMPA IMANI YA UONGOZI, CCM YASISITIZA AMANI NA USHIRIKIANO
Diwani wa Kata ya Ngogwa katika Manispaa ya Kahama, Abel Mabao, akiwashukuru wananchi wa kata hiyo kwa imani waliomuonesha katika uchaguzi mkuu wa madiwani, wabunge na Rais uliofanyika Oktoba mwaka 2025
Na Neema Nkumbi, Kahama
Diwani wa Kata ya Ngogwa katika Manispaa ya Kahama, Abel Mabao, amewashukuru wananchi wa kata hiyo kwa imani waliomuonesha katika uchaguzi mkuu wa madiwani, wabunge na Rais uliofanyika Oktoba mwaka 2025, huku akiahidi kutowavunja moyo wananchi waliompa dhamana ya kuwa mwakilishi wao.
Mabao amesema ataendelea kusimamia maslahi ya wananchi na kuhakikisha maendeleo yanapatikana katika maeneo mbalimbali ya kata hiyo.
Akizungumza mbele ya wananchi wa Ngogwa, Mabao amesema jukumu lake kubwa ni kufuatilia na kusimamia utekelezaji wa miradi ya maendeleo ndani ya kata hiyo, akisisitiza kuwa ataendelea kupigania upatikanaji wa huduma muhimu ikiwemo maji, barabara na umeme ili kuboresha maisha ya wananchi.
Amesema tayari ameanza kushirikiana na madiwani pamoja na viongozi wa serikali kuhakikisha miradi ya maendeleo inatekelezwa kwa vitendo huku akibainisha kuwa baadhi ya maeneo tayari yameingizwa katika mipango ya bajeti kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali kuanzia mwezi Julai mwaka huu.
Katika hatua nyingine, Mabao ameipongeza Serikali ya Chama Cha Mapinduzi chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kupeleka huduma za maendeleo kwa wananchi akitaja miradi ya maji, umeme pamoja na miundombinu kuwa ni miongoni mwa mafanikio yanayoonekana katika maeneo mbalimbali ya Kata ya Ngogwa.
Diwani huyo pia amewataka wananchi kuendelea kudumisha amani, mshikamano na ushirikiano ili kuharakisha maendeleo ya kata hiyo, amesema amani ndiyo msingi wa maendeleo na kwamba wananchi wanapaswa kushirikiana kwa karibu na viongozi wao ili kujenga jamii yenye ustawi na maendeleo endelevu.
Kwa upande wake, Katibu wa itikadi na uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Kahama, Joachim Simbila, amewataka wananchi kuendelea kulinda amani baada ya uchaguzi mkuu, akieleza kuwa amani ndiyo msingi wa maendeleo ya taifa na ustawi wa jamii, amesema wananchi wa Kahama wameonyesha ukomavu wa kisiasa kwa kushiriki uchaguzi kwa utulivu na kufanya maamuzi yao kwa amani.
Simbila amesema bila amani hakuna maendeleo, kwani hata biashara, uwekezaji na utekelezaji wa miradi ya maendeleo haviwezi kufanikiwa katika mazingira ya migogoro na vurugu.
Aidha, amegusia changamoto zinazoendelea kujitokeza duniani ikiwemo vita katika baadhi ya mataifa, akisema hali hiyo inaonesha umuhimu mkubwa wa kuendelea kuilinda amani iliyopo nchini Tanzania.
Naye Kaimu Katibu wa CCM Wilaya ya Kahama, Elia Wikunge, amewapongeza wananchi wa Kata ya Ngogwa kwa kuendelea kuonyesha ushirikiano na mshikamano katika shughuli mbalimbali za maendeleo ambapo amesema ushirikiano kati ya wananchi na viongozi wao ni msingi muhimu wa mafanikio ya maendeleo, huku akisisitiza kuwa CCM itaendelea kuwa karibu na wananchi katika kusikiliza changamoto zao na kushirikiana nao kutafuta suluhisho la maendeleo endelevu.
DKT.MIGIRO AIMARISHA USHIRIKIANO KIMATAIFA NA MABALOZI WA CUBA, VIETNAM, NA UN
Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi, Dkt. Asha-Rose Migiro, kwa nyakati tofauti amekutana na kufanya mazungumzo na mabalozi wawili wanaoziwakilisha nchi zao katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Mazungumzo hayo yamefanyika katika ofisi ndogo ya makao makuu CCM, Lumumba, jijini Dar es salaam.
Mabalozi hao ni Mheshimiwa Yordenis Despaigne Vera, Balozi wa Jamhuri ya Cuba na Mheshimiwa Vu Thanh Huyen, Balozi wa Jamhuri ya Kisoshalisti ya Viet Nam, wote wenye makaazi yao nchini Tanzania.
Mazungumzo hayo yalijikita katika kuendeleza na kuimarisha ushirikiano wa kihistoria kati ya CCM na vyama rafiki vya CPC–Cuba na CPV–Viet Nam, hususan katika maeneo ya uongozi, mshikamano wa vyama vya siasa na maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa manufaa ya wananchi wa nchi hizi mbili.
Katika hatua nyingine, Katibu Mkuu wa CCM, Dkt Migiro, alifanya mazungumzo na Mheshimiwa Susan Ngongi Namondo, Mwakilishi Mkaazi wa Umoja wa Mataifa nchini Tanzania, ambapo walijadiliana vipaumbele vya maendeleo ya jamii katika utekelezaji wa baadhi ya maeneo yaliyomo katika Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2025–2030 ambayo yanawiana na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, na Malengo ya Maendeleo ya Kimataifa (SDGs).
BODI YA TVLA YARIDHISHWA NA KASI YA UJENZI WA MAABARA YA KISASA DODOMA
Daudi Nyingo – DODOMA
Bodi ya Ushauri ya Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) imeeleza kuridhishwa kwake na maendeleo ya mradi mkubwa wa ujenzi wa jengo la ofisi na maabara ya kisasa unaotekelezwa katika Kituo cha Kanda ya Kati jijini Dodoma ambapo Mradi huo wenye ghorofa nne unategemewa kuwa mradi kielelezo nchini utakapokamilika.
Akizungumza wakati wa ziara ya ukaguzi katika eneo la ujenzi Mei 15, 2026, Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri ya TVLA, Prof. Amandus P. Muhairwa, alipongeza kasi ya mkandarasi na ubora wa kazi inayofanyika kwa kuwa awamu ya kwanza ya mradi huo ulioanza mwezi Oktoba 2025 na unatarajiwa kukamilika Oktoba 2026, tayari umefikia takriban asilimia 60% ya ujenzi.
"Kwa nilivyoangalia hali ya majengo waliyoyajenga na vifaa vilivyotumika, ubora wake ni wa juu, hilo naweza kuwapongeza sana wajenzi pamoja na wasimamizi wa ujenzi na mamlaka ya TVLA kwa kusimamia na kutoa mahitaji yanayotakiwa kwa wakati," alisema Prof. Muhairwa.
Aidha, alibainisha kuwa vifaa vinavyotumika kama nondo na zege ni vya hali ya juu, jambo linaloonyesha thamani halisi ya fedha (Value for Money) zinazowekezwa na alipongeza hali ya usalama wa wafanyakazi saiti, akisema kuwa wote wana vitendea kazi na vifaa vya kujikinga (PPE).
Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa TVLA, Dkt. Stella Bitanyi, alieleza kuwa mradi huo unagharimu takriban Shilingi Bilioni 6 na unatekelezwa kwa kutumia fedha za makusanyo ya ndani ya wakala. Alibainisha kuwa ujenzi huo unatekelezwa na Mkandarasi ambaye ni Kikosi cha Ujenzi na umefikia hatua ya nguzo baada ya msingi kukamilika.
"Tunashukuru serikali kwa kutuwezesha kibajeti na kupata fedha za mapato ya ndani zinazotumika kwenye mradi huu. Tutakuwa na maabara ya kisasa kabisa itakayohudumia wafugaji wa Kanda ya Kati na mikoa jirani," alisema Dkt. Bitanyi.
Dkt. Bitanyi aliongeza kuwa uamuzi wa kujenga maabara hiyo Dodoma ni wa kimkakati kufuatia shughuli nyingi za serikali kuhamia jijini humo. Lengo ni kuwa na maabara yenye hadhi ya makao makuu yenye uwezo wa kutoa huduma bora kwa jamii, taasisi za umma, na wafugaji binafsi.
Uongozi wa TVLA uliishukuru Wizara ya Mifugo na Uvuvi kupitia kwa Waziri na Katibu Mkuu kwa ushirikiano mkubwa unaohakikisha mradi unakamilika kwa wakati uliopangwa.
























Magazeti
Magazeti ya leo