Wednesday, 16 September 2026

SOMALIA, FCC ZAKUBALIANA KUIMARISHA USHIRIKIANO WA KIBIASHARA





Na.Mwandishi Wetu

Tume ya Ushindani ya Somali imefanya ziara ya siku moja nchini Tanzania kwa lengo la kujifunza uzoefu na mbinu zinazotumiwa na Tume ya Ushindani Tanzania (FCC) katika kusimamia ushindani wa kibiashara, kudhibiti bidhaa bandia na kulinda maslahi ya walaji.

Ziara hiyo imefanywa na Mkurugenzi wa Masuala ya Uchumi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa ya Jamhuri ya Shirikisho la Somalia na Kamishna wa Mamlaka ya Ushindani ya Afrika Mashariki (EACA), Bw. Ahmed Warsame pamoja na Mkurugenzi wa Biashara na Upatikanaji wa Masoko wa Wizara ya Biashara na Viwanda ya Jamhuri ya Shirikisho la Somalia, Bw. Abdihalim Osman.

Katika ziara hiyo, ujumbe huo umekutana na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Bi. Khadija Ngasongwa, pamoja na uongozi wa Tume, ambapo walipata fursa ya kujifunza namna FCC inavyotekeleza majukumu yake ya kukuza na kulinda ushindani, kumlinda mlaji na udhibiti wa bidhaa bandia.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, uongozi wa ujumbe wa Somalia umepongeza utendaji wa FCC, ukieleza kuwa uzoefu wa Tanzania katika kusimamia ushindani na kulinda mlaji ni muhimu kwa Somalia katika kuimarisha mifumo yake ya usimamizi wa soko na kukuza mazingira bora ya biashara.

Ujumbe huo umeeleza kuwa kujifunza kutoka FCC kutasaidia kuongeza uelewa na uwezo wa taasisi za Somalia katika kukabiliana na changamoto zinazohusu ushindani usio wa haki, bidhaa bandia na vitendo vinavyoweza kuwadhuru walaji.

Kwa upande wake,Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Bi. Khadija Ngasongwa, amesema kuwa Tanzania ipo tayari kuendelea kushirikiana na taasisi za Somalia na nchi nyingine katika kubadilishana uzoefu, maarifa na mbinu bora za usimamizi wa ushindani na ulinzi wa walaji.

Ziara hiyo ya siku moja imekuwa fursa muhimu kwa Somalia kujifunza uzoefu wa Tanzania katika eneo la ushindani wa kibiashara, udhibiti wa bidhaa bandia na ulinzi wa mlaji, hatua inayotarajiwa kuimarisha ushirikiano wa kitaasisi na kuchangia katika ujenzi wa masoko yenye ushindani wa haki na biashara endelevu.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMATANO SEPTEMBA 16,2026



Magazeti



Share:

Tuesday, 15 September 2026

MAKANDARASI WATAKIWA KUFANYIA KAZI MAAGIZO WANAYOPEWA KABLA MVUA ZA EL NINO

Dar es Salaam

Makandarasi wanaotekeleza miradi ya ujenzi wa miundombinu ya barabara za kuingia viwanja vya mazoezi na uendelezaji wa barabara ya uwanja wa Taifa ambayo itatumika wakati wa michuano ya AFCON wametakiwa kufanyia kazi maelekezo yote wanayopatiwa na Wakala ya Barabara za Vijini na Mijini (TARURA) kabla ya kuanza kwa mvua za El Nino.

Msisitizo huo umetolewa na Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri ya TARURA Mhandisi Florian Kabaka wakati wa ziara ya ukaguzi wa ujenzi wa barabara hizo jijini Dar es Salaam.

Mhandisi Kabaka amesema kwamba Makandarasi hawapaswi kuzungumza tu bali kutekeleza kwa kufanyia kazi yale yote wanayoshauriwa na kuelekezwa na Wakala huo ili mvua zitakavyoanza kunyesha iwakute wamemaliza ujenzi wa mitaro ya maji na hivyo kuepusha maeneo muhimu kutokupata changamoto za maji na kuathiri miundombinu mingine.

Aidha, Mwenyekiti huyo amesema ameridhishwa na maendeleo ya ujenzi unaoendelea na kuwapongeza kwa kufanya kazi usiku na mchana, pia kuwepo kwa wataalam, mitambo na vifaa vingine inatoa matumaini ya kufikia hatua nzuri hadi kufikia mwisho wa mwezi huu.

Amesema miradi yote inayotekelewa Dar es Salaam imefikia 50% na kuwasisitiza kuongeza kasi zaidi.

Pamoja na hayo, Mhandisi Kabaka aliwatoa hofu wananchi kwamba TARURA watahakikisha wanaboresha barabara zote muhimu wakati wa El Nino ili wananchi wasikwame katika kupata huduma muhimu.

Naye, Mtendaji Mkuu wa TARURA Mhandisi Victor Seff amesema miradi hiyo inaendelea vizuri na wao kama wasimamizi wataendelea kuwafuatilia kwa karibu ili kuhakikisha kazi zinamalizika kwa wakati ifikapo Desemba mwaka huu.

Pia amesema kwa hatua iliyofikiwa ana uhakika barabara zote zitakamilika kwa viwango na kufikiwa masharti yaliyowekwa.



Share:

PROF. SHEMDOE AWEKA JIWE LA MSINGI UJENZI WA MADARASA LINDI



Na: OWM – TAMISEMI, Mchinga – Lindi

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, ameweka jiwe la msingi katika mradi wa ujenzi wa madarasa manne na ofisi moja ya Mkuu wa Shule ya Msingi Mkwajuni, Kata ya Kitomanga, Manispaa ya Lindi, ikiwa ni utekelezaji wa maelekezo yake ya kuhakikisha shule hiyo inarejeshewa miundombinu iliyoharibiwa na maafa.

Shule hiyo ilikumbwa na maafa Januari 29, 2026, ambapo madarasa mawili, ofisi ya Mwalimu Mkuu, nyumba mbili za walimu na vyoo vya wanafunzi viliezuliwa, huku darasa moja likiangukiwa na mkorosho.

Prof. Shemdoe ameweka jiwe la msingi katika mradi huo Septemba 14, 2026, alipofika shuleni hapo kukagua maendeleo ya ujenzi wa madarasa hayo na ofisi ya Mkuu wa Shule, unaogharimu Shilingi Milioni 96. Ujenzi huo ulianza baada ya hoja iliyowasilishwa Bungeni na Mbunge wa Jimbo la Mchinga, Mhe. Salma Rashid Kikwete, akiomba Serikali kutoa usaidizi wa haraka kufuatia maafa yaliyolikumba shule hiyo. 

Kufuatia hoja hiyo, Prof. Shemdoe alimuagiza Mkurugenzi wa Manispaa ya Lindi kuhakikisha fedha zinapatikana kwa haraka kwa ajili ya ujenzi wa madarasa hayo manne, agizo ambalo lilitekelezwa.

Akizungumza baada ya kukagua mradi huo, Prof. Shemdoe amesema Serikali imeonesha utayari wa kuchukua hatua za haraka pale wananchi wanapokabiliwa na changamoto zinazohitaji suluhisho la dharura.

“Mhe. Mkuu wa Mkoa, tuliomba ridhaa kwa Mhe. Rais ya kuomba fedha za kujenga madarasa haya manne ziletwe mara moja, na leo hii wote tumeshuhudia madarasa manne mazuri pamoja na ofisi ya Mkuu wa Shule hii ya Mkwajuni yaliyotokana na juhudi za Mbunge Mhe. Salma Rashid Kikwete za kuomba usaidizi wa haraka,” amesema Prof. Shemdoe.

Aidha, Prof. Shemdoe amewahakikishia wananchi wa Kata ya Kitomanga kuwa OWM–TAMISEMI italeta fedha nyingine kwa ajili ya kujenga madarasa zaidi katika shule hiyo, ili hatimaye shule hiyo iwe na madarasa mapya na kuondokana na matumizi ya madarasa ya zamani yaliyopo katika hifadhi ya barabara.

Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Mchinga, Mhe. Salma Rashid Kikwete, amemshukuru Prof. Shemdoe kwa kuweka jiwe la msingi katika katika Shule ya Msingi Mkwajuni, huku akimuomba kuendelea kusaidia upatikanaji wa majengo mengine ya madarasa na ofisi ili walimu wapate mazingira bora zaidi ya kufanyia kazi na wanafunzi kujifunza katika mazingira salama na rafiki.

Naye, Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mhe. Adam Kighoma Malima, amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kumuamini na kumpa jukumu la kusimamia upatikanaji wa maendeleo kwa wananchi wa Mkoa wa Lindi.

Mhe. Malima pia amemshukuru Mhe. Rais kwa utayari wake wa kuendelea kutoa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo, akiahidi kuendelea kuwatumikia wananchi wa Lindi kwa bidii na moyo wa uzalendo.

Katika ziara yake mkoani Lindi Septemba 14, 2026, Prof. Shemdoe pia ametembelea na kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo, ikiwemo Mradi wa Bandari ya Uvuvi ya Kilwa Masoko; Mradi wa ujenzi wa Jengo la Wazazi (Maternity Ward) na Jengo la Wodi ya Matibabu ya Watoto Wachanga (NCU) katika Hospitali ya Wilaya ya Kinyonga; Mradi wa ujenzi wa Shule ya Msingi katika eneo la Sekondari Mkunyule, Kata ya Mandawa; pamoja na Mradi wa ujenzi wa Shule ya Msingi Kitomanga ‘B’.












Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger