Tuesday, 1 September 2026

PROF. SHEMDOE AELEKEZA WAFANYABIASHA 30 SOKO LA NDIZI MABIBO KUREJESHWA SOKONI



Na: OWM – TAMISEMI, Dar es Salaam

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, ameelekeza waliokuwa wafanyabiashara 30 wa soko la ndizi Mabibo (Mahakama ya Ndizi) kurejea kufanya biashara kwa udhamini wa maandishi kutoka ofisi za Serikali za Mitaa.

Prof. Shemdoe ametoa maelekezo hayo Agosti 31, 2026 katika Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi Ndogo ya OWM- TAMISEMI jijini Dar es Salaam, mara baada ya kupokea taarifa ya timu ya ufuatiliaji wa malalamiko ya wafanyabiashara hao wa soko la ndizi Mabibo, wakati wa kikao kazi chake na wafanyabiashara hao.

Aidha, Prof. Shemdoe ameilekeza Halmashauri ya Manispaa ya Ubungo kufanya tathmini ya mali ya Bw. Frego Njovu aliyewasilisha madai ya kuomba kurejeshewa fedha alizotumia kukarabati choo kilichopo sokoni hapo ambacho alikuwa akikisimamia.

Katika kuhakikisha haki inatendeka, Prof. Shemdoe ameelekeza bidhaa za mfanyabiashara Bw. Enock Kimwayeya aliyekuwa Mwenyekiti wa Wafanyabiashara waliowasilisha malalamiko kwa Prof. Shemdoe, arejeshewe bidhaa zake alizoziacha kwenye kibanda cha biashara pindi alipoondolewa, kwani taarifa ya timu ya ufuatiliaji imeainisha kuwa Halmashauri imekiri kwamba bidhaa za mfanyabiashara huyo zipo. 

Ili kuimarisha usimamizi wa soko, Prof. Shemdoe amemuelekeza Mkurugenzi wa Manispaa ya Ubungo kumpeleka meneja wa soko mwingine kulisimamia soko hilo na aliyepo kupangiwa majukumu mengine.

Maelekezo hayo ya Prof. Shemdoe yametokana na maafikiano baina ya pande zote katika kikao kazi cha Waziri huyo na walalamikaji (wafanyabiashara) na walalamikiwa ambao ni Halmashauri ya Manispaa ya Ubungo. 

Malalamiko ya wafanyabiashara hao 30 yaliwasilishwa kwa Prof. Shemdoe kupitia andiko lao la tarehe 15/01/2026 lililohusu Sakata la soko la Ndizi Mabibo wakilalamikia kupigwa marufuku kuingia sokoni, kutaifishwa na kuuzwa kwa maeneo yao ya biashara, aidha Manispaa ya Ubungo iliwaondoka sokoni wafanyabiashara hao kwa tuhuma za kuhamasisha vurugu na kutoitambua manispaa hiyo kama msimamizi wa soko.












Share:

LALJI NA BARAKA FOUNDATION WAENDESHA KAMBI YA MATIBABU YA MACHO BURE KOROGWE


Taasisi za LALJI FOUNDATION na BARAKA FOUNDATION kwa kushirikiana na VISION 4 ALL EYE CENTER imeendesha Kambi ya Matibabu ya Macho Bure katika Halmashauri ya Mji wa Korogwe, Mkoa wa Tanga, kwa lengo la kuwasaidia wananchi kupata huduma za uchunguzi, matibabu na upasuaji wa macho bila gharama.

Kambi hiyo iliyofanyika kwa muda wa siku tatu imewafikia jumla ya wananchi 3,259, ambao walihudhuria na kupata huduma mbalimbali za afya ya macho.

Akizungumza baada ya kutamatika kwa kambi hiyo mwenyekiti wa LALJI FOUNDATION Imtiaz Lalji amesema kwa siku zote tatu, jumla ya wagonjwa 333 walifanyiwa upasuaji wa macho, Kati yao, 291 walibainika kuwa na tatizo la mtoto wa jicho (cataract), huku 39 wakiwa na matatizo madogo ya macho yaliyohitaji huduma za upasuaji.

Aidha, jumla ya wananchi 1,723 walipewa dawa kulingana na mahitaji yao ya kiafya, huku wananchi 1,706 wakipatiwa miwani ya kusomea (reading glasses).

Imtiaz Lalji, amesema taasisi hiyo itaendelea kushirikiana na Serikali kuwasaidia Watanzania kupata matibabu ya macho bila malipo, kutokana na changamoto ya magonjwa ya macho ambayo imeendelea kuwaathiri wananchi wengi.

“Takwimu zilizopatikana katika kambi hiyo zinaonesha ukubwa wa changamoto ya magonjwa ya macho katika jamii, akibainisha kuwa wananchi wa maeneo ya vijijini ni miongoni mwa wanaokumbwa zaidi na changamoto ya upatikanaji wa huduma za macho kwa wakati" ameongeza

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Korogwe, Bi. Zahara Msangi, ameishukuru LALJI FOUNDATION na Baraka FOUNDATION kwa kuguswa na changamoto zinazowakabili wananchi na kuamua kufikisha huduma za matibabu ya macho katika Halmashauri hiyo.

Amesema huduma hiyo imekuwa na umuhimu mkubwa kwa wananchi, hususan wale ambao wamepata fursa ya kufanyiwa uchunguzi, kupata dawa, miwani pamoja na upasuaji bila kulipia gharama.

Naye Mratibu wa Huduma za Macho Mkoa wa Tanga, Dkt. Husein Abassy, amesema kuletwa kwa huduma hiyo mkoani Tanga ni hatua muhimu inayolenga kuwafikia wananchi wenye uhitaji, hususan wale ambao wanakabiliwa na changamoto ya kupata huduma za macho kwa wakati.

Nao baadhi ya wananchi walionufaika na kambi hiyo wameeleza namna huduma hizo zilivyowasaidia kupata matibabu ambayo huenda wasingeweza kuyapata kwa urahisi kutokana na gharama.

Wameishukuru LALJI FOUNDATION kwa huduma hiyo na kutoa wito kwa taasisi nyingine, mashirika na wadau mbalimbali kuendelea kujitokeza na kushirikiana na Serikali katika kuboresha afya na ustawi wa wananchi.

Huduma hiyo ya matibabu ya macho bila malipo ni sehemu ya juhudi za LALJI FOUNDATION katika kusaidia jamii na kupunguza changamoto ya upatikanaji wa huduma za afya kwa wananchi.

Taasisi hiyo imeahidi kuendelea kushirikiana na Serikali na wadau wengine katika kuwafikia wananchi wenye uhitaji katika maeneo mbalimbali nchini.
Share:

Monday, 31 August 2026

UVCCM YAWATAKA VIJANA KUHESHIMU MAMLAKA ZA UTEUZI


Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) umewataka vijana nchini kuwa na nidhamu, heshima kwa mamlaka za uteuzi, na kulinda misingi ya chama wanapotekeleza majukumu yao ya kikazi na kichama.

Wito huo ulitolewa na Mwenyekiti wa UVCCM Taifa, Mohammed Kawaida, alipozungumza na waandishi wa habari Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma baada ya kuapishwa kwa Makamu wa Rais, Deogratius Ndejembi, huku akisema kuwa nafasi aliyopewa kiongozi huyo ni mfano thabiti unaoonyesha vijana wanapaswa kuwa tayari kutumikia taifa kwa uadilifu, bidhi, na kujituma wanapopewa dhamana.

Kawaida alisisitiza kuwa viongozi vijana wanapopata nafasi za kuaminika wanapaswa kufanya kazi kwa weledi huku wakiepuka kiburi na majivuno, na badala yake wazingatie sheria, kanuni, na taratibu zilizowekwa na chama katika kutekeleza majukumu yao.

Aidha, aliwakumbusha vijana kuheshimu viongozi wazee na viongozi wastaafu kutokana na mchango wao mkubwa walioutoa katika kujenga taifa, akisisitiza kuwa kizazi cha sasa kinapaswa kujifunza kutoka kwa waliowatangulia bila kupoteza heshima kwa misingi ya kulinda maslahi ya chama na taifa.
Share:

NMB YAFUNGUA NJIA MPYA YA MIKOPO KWA WAFANYABIASHARA, WABUNGE WAIJIVIA





Na Dotto Kwilasa, Dodoma

BENKI ya NMB imepanua wigo wa huduma za mikopo kwa kuanzisha mfumo wa kidijitali unaowawezesha wateja kukopa hadi Sh milioni tano bila kuweka dhamana, hatua inayolenga kuwafungulia fursa zaidi wafanyabiashara wadogo na wajasiriamali.

Hatua hiyo imekuja wakati benki hiyo ikiendelea kuboresha huduma zake za kifedha kupitia teknolojia, huku tathmini ya uwezo wa mteja kukopa ikifanyika kwa kuangalia historia ya miamala yake badala ya kutegemea zaidi dhamana za mali.

Akizungumza katika Bonanza la Bunge lililowakutanisha wabunge, wizara na taasisi mbalimbali jijini Dodoma, Afisa Mkuu wa Kitengo cha Biashara na Wateja Binafsi wa NMB, Filbert Mponzi, alisema maboresho hayo yanalenga kufanya huduma za mikopo kuwa rahisi, haraka na kupatikana kwa watu wengi zaidi.

Alisema kupitia huduma ya NMB Mkononi, mteja anaweza kutumia huduma ya mkopo wa kidijitali ya MshikoFasta bila kulazimika kufika katika tawi la benki au kupitia taratibu ndefu za maombi.

Kwa mujibu wa Mponzi, mteja wa kawaida anaweza kukopa hadi Sh milioni mbili bila kujaza fomu wala kuweka dhamana, huku mfumo ukitumia historia ya miamala katika kutathmini uwezo wa mteja kurejesha mkopo.

“Mkopo huu ni suluhisho kwa wananchi wetu, wakiwemo wabunge, mamalishe, bodaboda na wafanyabiashara wengine. Hakuna dhamana inayohitajika, tunaangalia miamala yako,” alisema.

Alisema mfumo huo unalenga pia kuwasaidia wananchi ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakishindwa kupata mikopo kutokana na masharti yanayohitaji dhamana, pamoja na taratibu nyingi za kifedha.
WAJASIRIAMALI KUFIKIA SH MILIONI 5

Mponzi alisema NMB imeboresha pia huduma zake kwa wajasiriamali, ambapo wafanyabiashara wanaweza kupata mikopo ya hadi Sh milioni tano bila kuweka dhamana.

Alisema katika huduma hiyo, uwezo wa biashara kukopa unatathminiwa kwa kuangalia mwenendo na taarifa za miamala ya biashara, hatua inayolenga kuifanya historia ya biashara kuwa sehemu muhimu ya kupata huduma za kifedha.
NMB YABADILI MFUMO WA KIBENKI

Mbali na maboresho ya huduma za mikopo, Mponzi alisema NMB imeingia katika mfumo mpya wa kibenki baada ya kutumia mfumo wa awali kwa takribani miaka 15.

Alisema mabadiliko hayo yanatarajiwa kuongeza ufanisi wa huduma na kuiwezesha benki kutoa huduma za kisasa zaidi, hususan katika eneo la huduma za kidijitali.

“NMB tumeingia kwenye mfumo mpya. Tunatarajia kuona mambo mazuri zaidi katika huduma zote kutokana na kuingia kwenye mfumo huu mkubwa,” alisema.
MBUNGE AIPONGEZA NMB

Kwa upande wake, Mbunge wa Bunge la Afrika Mashariki, Machano Ali Machano, aliipongeza NMB kwa mchango wake katika shughuli za Bunge, akisema wabunge wanatambua na kuthamini ushirikiano unaotolewa na benki hiyo.

Alisema ushirikiano huo umeonekana pia katika shughuli za michezo, ikiwemo bonanza lililowakutanisha wabunge, wizara na taasisi mbalimbali jijini Dodoma.

Machano alisema mashindano ya Mabunge ya Afrika Mashariki yanatarajiwa kufanyika jijini Arusha mwezi Desemba mwaka huu, yakishirikisha wabunge kutoka nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).

Alisema Tanzania na wadau wake, ikiwemo NMB, wanapaswa kutumia mashindano hayo kama fursa ya kuimarisha ushirikiano na nchi nyingine wanachama wa jumuiya hiyo.
SILLO: MICHEZO NI SEHEMU YA AFYA YA WABUNGE

Naye Naibu Spika wa Bunge, Daniel Sillo, alisema Bunge lipo tayari kushirikiana na Serikali katika kufanikisha mashindano ya AFCON, akisisitiza umuhimu wa michezo katika kujenga afya, umoja, udugu na nidhamu.

Sillo alisema michezo ni muhimu pia katika kupunguza msongo wa mawazo, jambo alilosema ni muhimu kwa wabunge kutokana na majukumu yao ya kutunga sheria, kusimamia Serikali na kufanya maamuzi.

“Nimefurahishwa kuona idadi kubwa ya washiriki katika michezo ya leo. Michezo hupunguza msongo wa mawazo na mwili wenye afya ni suluhisho muhimu katika kufanya maamuzi mazuri,” alisema.

Aliwapongeza washindi na washiriki wote wa bonanza hilo, huku akiishukuru NMB kwa kufanikisha shughuli hiyo.

Alisema ushirikiano huo umewezesha wabunge kupata muda wa kushiriki michezo na kurejea katika majukumu yao wakiwa na afya bora na nguvu mpya.



Share:

Sunday, 30 August 2026

MKURANGA WATAKIWA KULINDA MIUNDOMBINU YA GESI ASILIA

Mkuu wa Wilaya ya Mkuranga, Khadija Nassir Ali, amewataka wananchi wa Mkuranga kuhakikisha wanalinda miundombinu ya gesi asilia iliyojengwa katika maeneo yao ili iweze kudumu na kuwanufaisha wananchi pamoja na taifa kwa ujumla.

Amesema ulinzi wa miundombinu hiyo ni jukumu la pamoja, huku akisisitiza wananchi kuendelea kuiunga mkono serikali na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) katika utekelezaji wa miradi ya nishati safi.

Akizungumza katika bonanza la michezo na upimaji wa afya bure lililoandaliwa na TPDC Kisemvule , Mkuranga, Khadija amesema mradi wa usambazaji wa gesi asilia tayari umewezesha zaidi ya nyumba 500 kuunganishwa na huduma hiyo.

Amesema bonanza hilo pia linalenga kuwakutanisha na kuwaunganisha wananchi wa Kisambule na Mkuranga kwa ujumla, sambamba na kuwaelimisha kuhusu umuhimu wa matumizi ya nishati safi na ulinzi wa miundombinu.

Aidha, Mkuu huyo wa Wilaya amesema Mkuranga inajivunia kuwa miongoni mwa maeneo yanayonufaika na uwekezaji mkubwa katika nishati safi, akieleza kuwa matumizi ya gesi asilia yana mchango katika kutunza mazingira, kuokoa maisha ya wananchi na kurahisisha shughuli za kila siku majumbani.

Ameipongeza TPDC kwa kuichagua Mkuranga kutekeleza mradi huo na kuahidi kuwa serikali ya Wilaya itaendelea kushirikiana na shirika hilo kuhakikisha miundombinu hiyo inalindwa na inatumika ipasavyo.

Khadija amesema matumizi ya nishati safi ni miongoni mwa vipaumbele vinavyoendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, hivyo wananchi wanapaswa kutumia fursa hiyo kwa manufaa yao na maendeleo ya taifa.

Amesema kuwa serikali inalenga kuona uwekezaji mkubwa unaofanywa katika miundombinu ya nishati ukitoa matokeo chanya kwa wananchi, huku akiwataka wananchi wengi zaidi kujitokeza kutumia huduma hiyo kadri inavyofikishwa katika maeneo yao.

Kwa upande wake Oscar Mwakasege Afisa Maendeleo ya Jamii Mwandamizi Kutoka Shirika la Petroli Tanzania (TPDC) amesema bonanza hilo na upimaji wa afya bure unalenga kuhamasisha ajenda ya matumizi ya nishati safi ya kupikia na ulinzi na usalama wa miundombinu ya bomba la gesi asilia huku akisema katika wilaya ya Mkuranga wameshawafungia wananchi gesi asilia nyumba 530 huku kwa mwaka huu wa Fedha 2026/27 wanatarajia kuwafungia huduma hiyo Wananchi zaidi ya 500 pia.

Kwa Upande wao Wananchi wa Kisemvule mkoani Pwani Ally Rajabu na Sharifa Hassan wamelishukukuru Shirika la Petroli Tanzania (TPDC) kwa bonanza hilo na upimaji wa afya bure huku wakisema wamenufaika na gesi asilia wanayoitumia majumbani hivyo kutumia nishati safi ukilinganisha na kipindi cha nyuma walikuwa wanatumia chafu.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA JUMAPILI AGOSTI 30,2026



Magazetini Leo








Share:

Saturday, 29 August 2026

WANANCHI MATONGO NA NYANGOTO KUELIMISHWA KUHUSU UTHAMINI WA FIDIA NORTH MARA


NYAMONGO, MARA

Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, kupitia wataalamu kutoka Ofisi ya Mthamini Mkuu wa Serikali, imefanya kikao na Kampuni ya Barrick North Mara Gold Mine pamoja na viongozi wa Vijiji vya Matongo na Nyangoto, kwa lengo la kujadili maandalizi ya utoaji elimu kwa wananchi kuhusu zoezi la uthamini wa fidia linalohusishwa na upanuzi wa shughuli za Mgodi wa North Mara.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao hicho, Diwani wa Kata ya Matongo, Mhe. Godfrey Mwita, amewataka viongozi wa Vijiji vya Matongo na Nyangoto kushirikiana kwa karibu na wataalamu pamoja na wadau wote wanaohusika katika mchakato huo, akieleza kuwa wananchi wa maeneo hayo wanatarajiwa kuguswa na upanuzi wa shughuli za mgodi.

Kwa upande wake, Meneja wa Mahusiano wa Kampuni ya Barrick, Bw. Francis Uhadi, amesema kampuni hiyo iko tayari kuanza mchakato huo kwa haraka, huku akisisitiza dhamira ya kampuni kuhakikisha haki na maslahi ya wananchi yanazingatiwa na kulindwa kwa mujibu wa sheria na taratibu za nchi.

Akifafanua hatua zinazofuata, Mthamini Kiongozi kutoka Ofisi ya Mthamini Mkuu wa Serikali, FRV. Baraka D. Mollel, amesema kikao hicho ni sehemu ya hatua muhimu kuelekea kuanza mchakato wa uthamini, baada ya hatua za awali zilizofanyika kwa kushirikisha Wizara ya Madini, ikiwemo tafiti na maandalizi mbalimbali.

Amesema hatua hizo zinalenga kuhakikisha zoezi la uthamini linafanyika kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu, pamoja na kuwezesha wananchi kupata taarifa sahihi kuhusu mchakato huo.

Naye Mtunzaji wa Bwawa la Mgodi, Bw. Majuto Kipande, ameeleza kuwa, tafiti za awali zilizofanyika wakati wa uanzishwaji wa mgodi zilionesha kuwa shughuli za uzalishaji zingefikia ukomo mwaka 2027. Hata hivyo, amesema tafiti zinazoendelea hivi sasa zinaonesha uwezekano wa uzalishaji kuendelea hadi kati ya mwaka 2031 na 2040.

Kwa mujibu wa Kipande, hali hiyo imeongeza umuhimu wa upanuzi wa bwawa la kutunza mabaki ya uchenjuaji wa dhahabu kutokana na bwawa linalotumika sasa kutaraji kufikia ukomo wa matumizi mwaka 2031.

Ameongeza kuwa, ujenzi wa bwawa jipya la kutunza mabaki ya uchenjuaji wa dhahabu unapaswa kukamilika kabla ya mwaka 2031, ili kuwezesha shughuli za mgodi kuendelea bila kuathiriwa na ukomo wa uwezo wa bwawa linalotumika sasa.

Mchakato wa uthamini unalenga kuhakikisha wananchi watakaoguswa na eneo la upanuzi wanapatiwa elimu na taarifa sahihi kuhusu hatua zinazochukuliwa, huku zoezi la uthamini wa fidia likitekelezwa kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za nchi.



















Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger