Wednesday, 5 August 2026

SERIKALI KUSHIRIKIANA NA SEKTA BINAFSI KUDHIBITI TAKA ZA PLASTIKI.


Serikali itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha kunakuwa na uwiano kati ya udhibiti wa taka za plastiki, ulinzi wa mazingira na ukuaji wa sekta ya viwanda ili uchumi wa nchi uendelee kuimarika.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Viwanda Biashara, Mhe. Judith Kapinga (Mb) wakati wa mkutano wa wadau wa udhibiti wa taka za plastiki Agosti 04, 2026 jijini Dar es Salaam .

Kapinga amesema suala la taka za plastiki lina pande mbili muhimu kwani kwa upande mmoja linahusu uhifadhi wa mazingira na kwa upande mwingine linagusa shughuli za uzalishaji wa viwanda vinavyochangia ajira, mapato ya Serikali na maendeleo ya uchumi.

Aidha, kuna wazalishaji wa plastiki zinazotumika kama vibebeo na vifungashio vya matumizi ya kila siku pamoja na viwanda vikubwa vinavyotumia vifungashio vya plastiki katika bidhaa zao, hivyo ni muhimu kujenga mazingira yatakayowezesha sekta hizo kuendelea kufanya biashara huku zikizingatia sheria na kulinda mazingira.

Kapinga ameongeza kuwa Serikali inalenga kujenga mazingira yanayowiana kwa pande zote, ambapo wawekezaji watimize wajibu wao wa kulinda mazingira na mamlaka za udhibiti zitekeleze wajibu wake kwa njia wezeshi ili wadau wote waweze kufanya kazi kwa ushirikiano.

Hata hivyo Kapinga amevipongeza viwanda vinavyozingatia Sheria na taratibu za mazingira, akisema hatua hiyo imeviwezesha kudumu kwenye biashara kwa muda mrefu, amesema Serikali itaendelea kuviunga mkono na kuvipatia mazingira bora yatakayovichochea kukua zaidi na kuongeza mchango wake katika Uchumi wa Taifa.

Vilevile amesema Viwanda vinavyokiuka Sheria vinapaswa kutumia vikao vya wadau kama fursa ya kujikumbusha misingi ya sheria na kuelekezwa namna ya kutumia teknolojia rafiki kwa mazingira ili viendelee kufanya biashara kwa ufanisi na kuongeza tija.

Sambamba na hayo, Serikali kwa sasa inatekeleza udhibiti wezeshi unaolenga kunufaisha wadau na Serikali kwa wakati mmoja, huku akimshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuimarisha ushirikiano kati ya sekta ya umma na sekta binafsi.

Kapinga amesema mkutano huo umeandaliwa kwa ushirikiano kati ya Wizara ya Viwanda na Biashara na Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), akibainisha kuwa sekta hizo zinategemeana katika kuhakikisha uwekezaji na maendeleo ya viwanda vinaenda sambamba na uhifadhi wa mazingira. Ameongeza kuwa Wizara ya Viwanda na Biashara ina taasisi 13 za udhibiti zinazoshirikiana katika kusimamia shughuli hizo.

Naye Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Mhe. Hamad Masauni (Mb), amesema mkutano huo umefanyika kwa mujibu wa maelekezo na maono ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuimarisha ushirikiano kati ya serikali na sekta binafsi.

Amesema hatua hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, ambapo takribani asilimia 70 ya utekelezaji wa dira hiyo unatarajiwa kuchangiwa na sekta binafsi, hivyo ushiriki wa wadau katika masuala ya mazingira na uwekezaji ni muhimu kwa maendeleo endelevu ya nchi.
Share:

TBA YAFUNGUA FURSA MPYA ZA UWEKEZAJI KATIKA MAKAZI NA MAJENGO YA BIASHARA



Na.Mwandishi Wetu

Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) umefungua fursa mpya za uwekezaji katika sekta ya makazi, majengo ya biashara na maendeleo ya miji, hatua inayolenga kuboresha huduma kwa wananchi, kuvutia mitaji na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Meneja wa TBA Mkoa wa Dodoma, Qs. Emmanuel Wambura, amesema hayo katika Maonesho ya Kimataifa ya Kilimo ya Nanenane yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Samuel Malecela, Nzuguni, jijini Dodoma.

Amesema TBA imeendelea kutekeleza kwa ufanisi miradi mbalimbali ya Serikali katika sekta tofauti, ikiwemo ujenzi wa majengo ya Wizara ya Kilimo na taasisi zake, ofisi za Tume ya Taifa ya Umwagiliaji, Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA), vituo vya afya pamoja na taasisi nyingine za umma.

Kwa mujibu wa Qs. Wambura, utekelezaji wa miradi hiyo unalenga kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma kwa wananchi na kuboresha mazingira ya kazi katika taasisi za Serikali.

“TBA inaendelea kutekeleza dhamana yake ya kuhakikisha Serikali inapata majengo bora, salama na ya kisasa. Miradi mingi ipo katika hatua mbalimbali za utekelezaji, huku mingine ikiwa katika hatua za mwisho kukamilika ili wananchi waanze kunufaika na huduma zinazotolewa kupitia miundombinu hiyo,” amesema Qs. Wambura.

Amesema mbali na miradi ya Serikali, TBA imeweka mkazo katika kuendeleza miradi ya makazi na miji ya kisasa, ikiwemo mradi wa ujenzi wa nyumba 3,500 katika eneo la Nzuguni jijini Dodoma, ambao unaendelea kutekelezwa.

Amebainisha kuwa wakala huo umefungua fursa za uwekezaji kupitia mfumo wa ubia kati ya sekta ya umma na sekta binafsi (PPP), ambapo tayari baadhi ya wawekezaji, ikiwemo kampuni ya Fit Group kutoka Nigeria, wameonyesha nia ya kuwekeza katika mradi huo wa makazi.

Aidha, amesema TBA imeandaa maeneo yenye fursa kubwa za uwekezaji katika mikoa mbalimbali, ikiwemo Dodoma, Dar es Salaam, Mwanza na Arusha, ambapo wawekezaji wanakaribishwa kuwekeza katika nyumba za makazi, majengo ya biashara, hoteli, ofisi na maghala ya kisasa ya kuhifadhi mazao.

Qs. Wambura amefafanua kuwa Mkoa wa Dodoma pekee una eneo la takribani hekta 630 lililoandaliwa kwa ajili ya uwekezaji, likiwa na miundombinu muhimu na mazingira rafiki kwa shughuli za biashara.

“Taratibu za uwekezaji ni wazi na rahisi. Tunawakaribisha Watanzania na wawekezaji kutoka nje ya nchi kushirikiana nasi katika kuendeleza miradi yenye tija kwa uchumi wa Taifa. Tunahitaji wawekezaji wenye uwezo na wanaozingatia sheria za nchi ili kuhakikisha miradi inatekelezwa kwa viwango vinavyotakiwa,” amesema.

Katika hatua nyingine, amesema TBA imepanua wigo wa shughuli zake hadi kusimamia miradi ya ujenzi na ukarabati wa majengo ya ubalozi wa Tanzania nje ya nchi kwa kushirikiana na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Amesema hatua hiyo inaonesha kuendelea kuaminiwa kwa uwezo wa kitaalamu wa wakala huo katika utekelezaji wa miradi ya ujenzi ndani na nje ya Tanzania.

Akizungumzia mchango wa TBA katika sekta ya kilimo, Qs. Wambura amesema wakala huo umeendelea kubuni na kusimamia ujenzi wa maghala ya kisasa ya kuhifadhi mazao, maabara za utafiti wa kilimo na miundombinu mingine muhimu inayosaidia kuongeza thamani ya mazao, kuimarisha usalama wa chakula na kukuza ushindani wa sekta hiyo.

Amewakaribisha wananchi, taasisi na wawekezaji kutembelea banda la TBA katika Maonesho ya Nanenane ili kupata taarifa kuhusu huduma zinazotolewa na wakala huo, ikiwemo usanifu wa majengo, ukadiriaji wa gharama za ujenzi, usimamizi wa miradi na fursa mbalimbali za uwekezaji.

“TBA ipo katika mikoa yote 26 ya Tanzania na itaendelea kushirikiana na sekta binafsi katika kujenga miundombinu ya kisasa, kuvutia uwekezaji na kuchangia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050,” amesema Qs. Wambura.
Share:

Tuesday, 4 August 2026

VIJANA JITOKEZENI KUITETEA SERIKALI DHIDI YA UCHOCHEZI MITANDAONI: ENG MARYPRISCA MAHUNDI



Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jinsia,Wanawake na Makundi Maalumu Eng. Maryprisca Mahundi amewataka vijana kusimama kusimama imara kukemea Uchochezi na upotoshwaji unaoenezwa mitandaoni dhidi ya Serikali na kusimama imara kuitetea Serikali kwa hoja zenye nguvu.

Eng.Mahundi ameyasema hayo alipokuwa akizungumza na vijana wa UVCCM Tawi la Chuo Cha ADEM Kampusi ya Mbeya katika mkutano maalumu wa Tawi la UVCCM chuoni hapo.

"Tujitokeze kukemea Uchochezi dhidi ya serikali yetu unaoenezwa mitandaoni,tueleze mazuri ya serikali yetu kwa hoja" alisema Eng Mahundi.

Aidha Naibu Waziri Mahundi ambaye pia ni Mbunge Viti Maalumu anayewakilisha Wanawake UWT Mkoa wa Mbeya kuwa mstari wa mbele kulinda amani na utulivu wa nchi jambo ambalo litachangia kuwa na fursa ya kufanya shughuli za kujiongezea kipato na kujiinua kiuchumi.

Amesema Vijana wanapaswa kutumia vyema nguvu na Elimu yao kwa kujiendeleza kiuchumi kwa kuwa Maendeleo ya nchi yanategemea zaidi Elimu na nguvu walizonazo.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMANNE AGOSTI 4,2026




 
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger