Monday, 7 September 2026

PROGRAMU YA KUENDELEZA KILIMO NA UVUVI (AFDP) YAWAFIKIA WAKULIMA,WAVUVI NA JAMII YA WAFUGAJI MKOANI TANGA




Na; Mwandishi wetu-Tanga.

Ujumbe kutoka Mfuko wa Kimataifa la Kuendeleza Kilimo (IFAD) na wataalamu kutoka katika sekta zinazotekeleza Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) wamekutana Mkoani Tanga Tarehe 7 Septemba 2026 kwa lengo la kufanya mapitio ya Utekelezaji wa Programu hiyo.

Sambamba na hilo timu hiyo itatembelea maeneo yanayotekeleza Programu kwa Mkoa wa Tanga, ambapo kwa upande wa sekta ya kilimo timu hiyo itatembelea kata ya Msomela iliyopo katika Halmashauri ya Handeni Vijijini ambako programu imehamasisha na kutoa elimu ya kilimo bora kwa jamii ya kimasai ambao kiasili ni wafugaji ambapo wameweza kujishughulisha na kilimo cha mahindi chenye tija.


Programu imewezesha kuwepo kwa eneo la mashamba darasa (FFS) kwa mazao ya Alizeti, Mahindi na Maharage, na shamba Darasa hilo limeonesha mafanikio kwa kiasi kikubwa, ambapo hekta moja inaweza kuzalisha takribani magunia 20 ya kilo mia moja kila moja, na jamii ya wafugaji sasa inajishulisha na shughuli za Kilimo na kunufaika na upatikanaji wa mazao yanayolimwa.


Kwa upande wa Sekta ya Uvuvi, Programu inaendelea na ujenzi wa soko la kimataifa la Samaki Kipumbwi lililloko katika halmashauri ya Pangani ambapo mpaka sasa ujenzi umefikia asilimia 68% na linategemewa kukamilika ifikapo Oktoba 2026.

Aidha, programu pia inaendelea na ujenzi wa vichanja 40 vya kukaushia dagaa ambavyo vinaweza kukausha takribani tani tano kwa za dagaa kwa wakati mmoja.


Kwa upande mwingine pia Programu ya AFDP inaendelea na ujenzi wa Ghala la baridi na mtambo wa barafu katika soko hilo kwa ajili ya kuhifadhi na kusafirisha samaki.




Awali Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la kimataifa la maendeleo ya Kilimo nchini (IFAD) Bw. Seth Meng alikutana na Kaimu Katibu tawala wa Mkoa wa Tanga Bw.Emmanuel Kisongo na kufanya mazungumzo kuhusiana na utekelezaji wa Programu katika Mkoa sambamba na mafanikio tarajiwa kwa wanachi wa maeneo husika ambapo Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa alieleza kuwa Programu hiyo ni muhimu sana katika kuhamasisha maendeleo ya kilimo na uvuvi katika mkoa huo.

 Aliishukuru IFAD kwa kuweza kuwafikia wananchi wa mkoa huo na kuwataka ikiwezekana kuongeza uwekezaji mkoani hapo.
Share:

MUME WA RAIS SAMIA, HAFIDH AMEIR AFARIKI DUNIA




Na Mwandishi wetu,ZANZIBAR.

Mume wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Daktari Samia Suluhu Hassan, Hafidh Ameir Hassan, amefariki dunia leo Jumatatu, Septemba 7, 2026.

Taarifa ya msiba huo imetolewa leo na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Deogratius Ndejembi, akisema Hafidh Ameir Hassan amefariki dunia majira ya saa mbili asubuhi katika Hospitali ya Kumbukumbu ya Mzee Ali Hassan Mwinyi, Zanzibar, alipokuwa akipatiwa matibabu ya ugonjwa wa moyo.

“Ndugu wananchi, kwa masikitiko makubwa, ninawajulisha taarifa ya kifo cha Mheshimiwa Hafidh Ameir Hassan, mume wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Daktari Samia Suluhu Hassan,” amesema Ndejembi.

Makamu wa Rais ametoa pole kwa Rais Samia, familia, ndugu, jamaa na marafiki wa marehemu, pamoja na Watanzania wote kutokana na msiba huo.

Amesema mipango ya mazishi ya marehemu Hafidh Ameir Hassan inaendelea kufanyika Kizimkazi, Zanzibar, ambako familia inatarajiwa kuandaa taratibu za mwisho za mazishi.

Kifo cha Hafidh Ameir Hassan kimekuja wakati Rais Samia Suluhu Hassan akiendelea kutekeleza majukumu yake ya kitaifa, huku taarifa hiyo ikisababisha simanzi miongoni mwa Watanzania na viongozi mbalimbali.

Malunde.com inaungana na familia ya Rais Samia Suluhu Hassan katika kipindi hiki kigumu cha maombolezo.


Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMATATU SEPTEMBA 7,2026

Magazeti





Share:

Sunday, 6 September 2026

NAIBU WAZIRI AVUTIWA NA USAJILI WANACHAMA KIDIGITALI: AITAKA NHIF KUONGEZA KASI YA BIMA YA AFYA KWA WOTE ‎



NAIBU Waziri wa Afya, Mhe Dkt. Florence George Samizi (Mb), amelipongeza Baraza la Wafanyakazi la Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) kwa kuwa moja ya mabaraza bora nchini. Amelitaka baraza kuhakikisha ajenda ya Bima ya Afya kwa wote inawafikia wananchi wengi zaidi.

Nimefurahi kusikia kwamba katika kipindi cha mwaka wa fedha 2025/2026 Mfuko umeweza kufikia 10.7% ya Wananchi toka 8% ya wananchi iliyodumu kwa takriban miaka 10.

Pamoja na pongezi hizo Mh. NAIBU WAZIRI ameutaka Mfuko kutumia TEHAMA na kusajili wanachama wengi zaidi ili kutimiza ahadi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwafikishia wananchi wote huduma za bima ya afya. Hii itasaidia wananchi kuondokana na umaskini pale wanapopata maradhi.

‎Dkt. Samizi ametoa maelekezo Hayo wakati wa mkutano wa nne wa wa Baraza la 4 wafanyakazi NHIF, Jijini Arusha, na kusisistiza menejimenti ya wafanyakazi wa NHIF kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia uadilifu, weledi na uwajibikaji, huku wakisikiliza na kutatua kwa wakati kero za wananchi.

‎Aidha, amesisitiza umuhimu wa kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kuwa na bima ya afya. Kutoa huduma bora na kuwa na mfumo wa kupokea mrejesho toka kwa wananchi.

‎Katika kuelekea maadhimisho ya miaka 25 tangu kuanzishwa kwa NHIF, Dkt. Samizi amesema ni muhimu mfuko huo kuonesha mafanikio yaliyopatikana. Kuwepo kwa NHIF kumesaidia kuboresha huduma za Afya kwa kulipa madai na kutoa mikopo kwa vituo vya afya. Ni vema wanachi wakajulishwa hatua kubwa iliyofikiwa katika huduma za Afya na mchango wa NHIFkatika Sekta hii muhimu. Mlianza na vituo vichache sana mwaka 2001 hivi sasa yaani mwaka wa Fedha 2025/26 mmesajili zaidi ya vituo 10,600 nchi nzima.

Ni vema kuonesha namna mlivyokabiliana na changamoto za wakati ule na namna zilivyowasaidia kuboresha Mfuko katika utoaji wa huduma.

‎Amesema mafanikio hayo yanadhihirishwa na kujituma, ushirikiano, umoja na mshikamano miongoni mwa watumishi wa NHIF ili kufikia malengo ya mfuko kwa lengo la kutekeleza jitihada za Serikali za kuhakikisha wananchi wanapata bima ya Afya.

‎Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa NHIF, Dkt. Irene Isaka, ameeleza mafanikio yaliyopatikana ikiwa ni pamoja na kupunguza muda wa kilipa madai toka zaidi ya siku 90 hadi wastan wa siku 50 kwa mwaka wa Fedha 2025/2026. Vile vile alieleza kwamba Mfuko umeendelea kuimarika ambapo ziada imeongezeka kwa 57% Mfuko umepunguza matumizi kwa asilimia13% na uwekezaji umeongezeka kwa 106%.

Hii imewezesha Mfuko kuendeleza kifurushi cha wanafunzi, Toto Afya. Mfuko kusajili kifurushi cha tarangire, Mikumi, Ngorongoro, Serengeti Tanzanite na kifurushi cha vikundi yaani Umoja Afya ambacho ni sh. 60, 000 kwa matibabu ya mwaka mzima.

Vile vile alielezea mikakati inayotekelezwa na mfuko huo katika kufikia malengo yake ikiwa ni pamoja na matumizi ya TEHAMA kwenye usajili, uchakataji madai na kupambana na udanganyifu. Mfuko pia unashirikisha Sekta Binafsi katika usajili wa wanachama na katika huduma za matibabu.

‎Mwakilishi wa chama Cha wafanyakazi TUGHE, Bw.Paul wamepongeza baraza Hilo kuzingati misingi ya Kazi stahiki za wafanyakazi kwenye taasisi hiyo.

‎Baadhi ya wafanyakazi walioshiriki semina elekezi ya siku mbili wamesema wamepata maarifa na mwelekeo mpya ambao utawasaidia kuboresha utendaji wao wa kazi na utoaji wa huduma kwa wananchi.







Share:

WATANZANIA 16 KWENDA JAPAN KUONGEZA UJUZI

 


 ******

Watanzania 274 tayari wamenufaika na programu za masomo ya muda mrefu nchini Japan, huku wanataaluma 16 wakielekea nchini humo kwa masomo ya uzamili na mafunzo ya vitendo katika kampuni za Kijapani.

Tanzania na Japan zimeendelea kuimarisha ushirikiano katika elimu, kupitia fursa zinazolenga kuongeza ujuzi na weledi wa watumishi na wataalamu wa Tanzania.

Hayo yamesemwa leo jijini Dar es Salaam na Mwakilishi wa JICA nchini Tanzania, Dk. Kuge Katsuya, wakati wa hafla ya kuwaaga wanataaluma hao 16.

Amesema programu hiyo ya ABE Initiative inawapa Watanzania nafasi ya kusoma fani mbalimbali, ikiwemo sera za umma, madini na uhandisi.

Dk. Katsuya amesema masomo ya uzamili huchukua takribani miaka miwili, huku ya uzamivu (PhD) yakichukua karibu miaka mitatu.

Balozi wa Japan nchini Tanzania, Yoichi Mikami, amesema vijana hao ni sehemu muhimu ya kuimarisha uhusiano wa nchi hizo na kuwataka kutumia elimu watakayoipata kwa maendeleo ya Tanzania.

Ofisa Rasilimali Watu Mwandamizi, Margareth Ngondya, amesema mafunzo hayo yanaongeza ujuzi na weledi wa watumishi wa umma, jambo linalosaidia kuboresha huduma kwa wananchi.

Miongoni mwa wanufaika hao ni Lucy Michael wa BMT, anayekwenda kusoma Global Education na kusema atatumia elimu hiyo kusaidia kuendeleza michezo nchini.








MWISHO.


Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger