Monday 27 February 2023

TMDA YATOA ELIMU YA UTOAJI TAARIFA MADHARA NA MATUKIO YATOKANAYO NA MATUMIZI YA VIFAA TIBA NA VITENDANISHI KWA WATOA HUDUMA ZA AFYA SHINYANGA

 


Meneja wa TMDA Kanda ya Ziwa Magharibi Geita Dkt. Edgar Mahundi akizungumza katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga

Na Kadama Malunde – Malunde 1 blog

Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba - TMDA imetoa elimu ya uhamasishaji juu ya utoaji wa taarifa za madhara na matukio yatokanayo na matumizi ya vifaa tiba na vitendanishi kwa watoa huduma za afya mkoa wa Shinyanga.

Elimu hiyo imetolewa leo Jumatatu Februari 27,2023 katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga yakishirikisha Madaktari, Wafamasia, Wataalamu wa maabara, watunza vifaa tiba na mafundi sanifu wa vifaa tiba na vitendanishi.

Akitoa elimu hiyo, Meneja wa TMDA Kanda ya Ziwa Magharibi Geita Dkt. Edgar Mahundi amesema TMDA inaendelea kutoa elimu ya uhamasishaji kuhusu utoaji taarifa za madhara na matukio ya vifaa tiba na vitendanishi kwa watoa huduma za afya ili wataalamu hao wa afya wanapobaini vifaa tiba vinaleta madhara kwa wagonjwa watoa taarifa TMDA.

“Tunataka watoa huduma za afya wanapobaini vifaa tiba vinaleta madhara kwa wagonjwa watoe taarifa TMDA lakini pia watoa huduma wa afya wanapobaini vifaa tiba havifanyi kazi inayotakiwa watoe taarifa ili TMDA tufanye ufuatiliaji”,ameeleza Dkt. Mahundi.

Amezitaja njia za utoaji wa taarifa za madhara na matukio yatokanayo na matumizi ya vifaa tiba na vitendanishi ni kupitia Fomu maalumu ya rangi ya machungwa, kutumia simu ya kiganjani/mkononi kwa kubonyeza *152*00# kisha unafuata maelekezo pamoja kutoa taarifa kwa kupiga simu bure namba 0800110084

“TMDA tumetoa elimu hii kwa watoa huduma za afya katika Manispaa ya Shinyanga lakini pia tutatoa elimu katika Manispaa ya Kahama na maeneo mbalimbali nchini kwenye hospitali, zahanati na vituo vya afya vya serikali na watu binafsi ikiwa ni sehemu ya kazi za TMDA kuhakikisha vifaa tiba na vitendanishi vinapozunguka katika Soko la Tanzania vinakuwa na ubora, usalama na ufanisi unaokidhi vigezo”, ameeleza Dkt. Mahundi.

Kwa upande wake, Afisa Usajili Dawa Daraja la kwanza kutoka TMDA, Bw. Haninu Salum Nakuchema amesema TMDA inatoa elimu kuhusu utoaji taarifa za madhara na matukio yatokanayo na matumizi ya vifaa tiba na vitendanishi ili kuhakikisha jamii inatumia vifaa tiba na vitendanishi vyenye ubora, usalama na ufanisi.


Nakuchema amewataka Madaktari, Wafamasia, Wataalamu wa maabara, watunza vifaa tiba na mafundi sanifu wa vifaa tiba na vitendanishi kushirikiana na TMDA kwa kutoa taarifa za madhara na matukio yatokanayo na matumizi ya vifaa tiba na vitendanishi ili kuhakikisha jamii inakuwa salama muda wote.

Nao watoa huduma za afya waliopatiwa elimu hiyo wameishukuru TMDA kwa kutoa elimu hiyo na kuahidi kuwa watashirikiana na TMDA kuifanya jamii kuwa salama kwa kutoa taarifa endapo watabaini vifaa tiba vinaleta madhara kwa wagonjwa ama havifanyi kazi kwa ufanisi unaotakiwa.
Meneja wa TMDA Kanda ya Ziwa Magharibi Geita Dkt. Edgar Mahundi akizungumza katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga
Afisa Usajili Dawa Daraja la kwanza kutoka TMDA, Bw. Haninu Salum Nakuchema akizungumza katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga
Mratibu wa Pharmacovigillance mkoa wa Shinyanga, Clementina Salutari akizungumza katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga
Maafisa kutoka TMDA wakipiga picha ya kumbukumbu na watoa huduma za afya katika Manispaa ya Shinyanga
Maafisa kutoka TMDA wakipiga picha ya kumbukumbu na watoa huduma za afya katika Manispaa ya Shinyanga
Maafisa kutoka TMDA wakipiga picha ya kumbukumbu na watoa huduma za afya katika Manispaa ya Shinyanga


Share:

POLISI SHINYANGA WAKAMATA WAGANGA WA RAMLI ZA MAUAJI.. RPC MAGOMI AONYA ASKARI WANAOSHIRIKI KUFANYA UHALIFU


Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga ACP Janeth Magomi akionesha vifaa vya uganga vilivyokamatwa wakati akizungumza na waandishi wa habari leo Jumatatu Februari 27,2023 - Picha na Kadama Malunde

Na Kadama Malunde - Malunde 1 blog

Jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga limewakamata waganga wa jadi watatu wakiwa na vifaa vinavyotumika katika kupiga ramli chonganishi ambayo husababisha mauaji ya kikatili yakiwemo ya kuua kwa mapanga huku likikemea vikali tabia ya baadhi ya askari polisi wasio waadilifu ambao wanavujisha siri na wanaoshirikiana na wahalifu.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumatatu Februari 27,2023 Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga ACP Janeth Magomi amesema vifaa hivyo na watuhumiwa hao wamekamatwa kufuatia misako na doria za jeshi la polisi kwa kipindi cha Februari 5 hadi 27,2023.

“Tumekamata waganga wa jadi wakiwa na vifaa vya kufanyia ramli chonganishi zinazopelekea mauaji ya kikatili yakiwemo mauaji ya mapanga. Pia tumefanikiwa kukamata watuhumiwa watatu wakiwa na vifaa tiba vya hospitali ambavyo haviruhusiwi kumilikiwa na mtu pasipo na idhini ya serikali”,ameeleza Kamanda Magomi.


“Pia tumekamata jumla ya lita 780 za mafuta ya diesel katika maeneo tofauti ya mradi wa Reli ya Kisasa (SGR) pamoja na pikipiki tatu zilizokuwa zinatumika katika uhalifu ikiwemo kubeba mafuta ya wizi katika mradi wa SGR. Hali kadhalika tumeokota pikipiki 2”,amesema.

Amevitaja vitu vingine vilivyokamatwa kuwa ni pamoja na milango 9 ya chuma,mabomba matatu ya chuma,bomba moja la alama za barabarani, milango mitano ya mbao, mzani wa kupimia uzito, mashine ya kutobolea miamba, godoro moja,viti vinne vya plastiki, bangi kete 31, ngoma moja ya shule na magitaa mawili,mashine mbili za kuchezea kamali, subwoofer 2,feni 1,mtungi mmoja wa gesi.

“Jeshi la Polisi mkoa wa Shinyanga linakemea vikali tabia ya baadhi ya askari polisi wasio waadilifu ambao wanavujisha siri na ambao wanashirikiana na wahalifu na kusababisha kudhoofika kwa upatikanaji wa taarifa za kihalifu kutoka kwa wananchi. Hatua kali za kinidhamu zitachukuliwa dhidi yao”, ameongeza Kamanda Magomi
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga ACP Janeth Magomi akizungumza na waandishi wa habari leo Jumatatu Februari 27,2023. Picha na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga ACP Janeth Magomi akizungumza na waandishi wa habari leo Jumatatu Februari 27,2023
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga ACP Janeth Magomi akizungumza na waandishi wa habari leo Jumatatu Februari 27,2023.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga ACP Janeth Magomi akionesha vifaa vya uganga vilivyokamatwa na Jeshi la polisi kufuatia misako na doria zilizofanyika
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga ACP Janeth Magomi akionesha vifaa vya uganga vilivyokamatwa na Jeshi la polisi
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga ACP Janeth Magomi akionesha vitu  mbalimbali vilivyokamatwa na Jeshi la polisi Shinyanga
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga ACP Janeth Magomi akionesha vitu  mbalimbali vilivyokamatwa na Jeshi la polisi Shinyanga

Vitu  mbalimbali vilivyokamatwa na Jeshi la polisi Shinyanga.

Picha zote na Kadama Malunde - Malunde 1 blog



Share:

WAFANYAKAZI WA BARRICK NORTH MARA WASHIRIKI MBIO ZA KILI MARATHON 2023


Baadhi ya wafanyakazi wa Barrick wakishiriki kukimbia mbio za masafa marefu
***

Wafanyakazi wa Mgodi wa Barrick North Mara, uliopo wilayani Tarime Mkoa wa Mara, wameshiriki katika mbio za kimataifa za Kilimanjaro Marathon zilizofanyika Mkoani Kilimanjaro ambapo baadhi yao wamemudu kukimbia mbio za masafa marefu.

Kampuni ya Barrick imekuwa na program za mazoezi kwa ajili ya kuhakikisha wafanyakazi wake wanakuwa na nguvu na afya bora.

Kila mwaka kampuni imekuwa ikiwezesha wafanyakazi wake kushiriki mashindano mbalimbali ya michezo ikiwemo mashindano ya mbio za kilomita 42 ya Bulyanhulu Healthy Lifestyle Marathon yanayofanyika kila mwaka.
Baadhi ya wafanyakazi wa Barrick North wakifurahia kumaliza kukimbia mbio za Kili Marathon zilizofanyika mkoani Kilimanjaro.
Baadhi ya wafanyakazi wa Barrick North wakifurahia kumaliza kukimbia mbio za Kili Marathon zilizofanyika mkoani Kilimanjaro.
Baadhi ya wafanyakazi wa Barrick North wakifurahia kumaliza kukimbia mbio za Kili Marathon zilizofanyika mkoani Kilimanjaro.
Baadhi ya wafanyakazi wa Barrick North wakifurahia kumaliza kukimbia mbio za Kili Marathon zilizofanyika mkoani Kilimanjaro.
Baadhi ya wafanyakazi wa Barrick North wakifurahia kumaliza kukimbia mbio za Kili Marathon zilizofanyika mkoani Kilimanjaro.
Share:

GGML YANG’ARA TUZO ZA ATE, MAJALIWA AAHIDI MAKUBWA


Meneja Mwandamizi (Rasilimaliwatu) kutoka GGML, Charles Masubi akipokea tuzo kutoka kwa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa (kulia). GGML iliibuka mshindi wa pili katika tuzo zilizoandaliwa na Chama cha Waajiri Tanzania (ATE) na Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET) kwa lengo la kutambua mchango wa uzalishaji wa rasilimaliwatu wenye ubora kwa soko la ajira.

 Na Mwandishi wetu 
JITIHADA za Kampuni ya Geita Gold Mining Limited (GGML) kuwajengea uwezo wahitimu wa vyuo vikuu kwa kuwapatia mafunzo kazini zimeendelea kuonekana baada ya kampuni hiyo kuibuka mshindi wa pili katika tuzo zilizoandaliwa na Chama cha Waajiri Tanzania (ATE) na Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET).


GGML ilibeba tuzo katika kundi la waajiri wakubwa kutokana na mchango wake wa uzalishaji wa rasilimaliwatu wenye ubora kwa soko la ajira.


Hatua hiyo inakuja siku chache baada ya kampuni hiyo kupokea wahitimu 50 kutoka vyuo vikuu mbalimbali nchini ambao wameanza kupatiwa mafunzo kazini mwaka huu. Kati yao 30 ni wanawake na 20 wanaume. Mwaka jana jumla ya vijana 26 walihitimu mafunzi hayo ndani ya GGML.


Akizungumza baada ya kupokea tuzo hiyo, katika hafla iliyofanyika mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam, Meneja Mwandamizi (Rasilimaliwatu) kutoka GGML, Charles Masubi aliishukuru Serikali kwa kutambua mchango wa kampuni hiyo katika uzalishaji wa vijana bora wanaokubalika katika soko la ajira.


Awali Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ambaye alikuwa mgeni rasmi katika hafla hiyo, alisema Serikali itaendelea kushirikiana kikamilifu na sekta binafsi katika utoaji elimu ya ufundi na mafunzo ya ufundi stadi ili kuzalisha wataalamu wenye ujuzi wa kutosha unaohitajika katika sekta mbalimbali.


Pia aliwapongeza waajiri kwa kutoa nafasi za mafunzo kwa vitendo, uanagenzi, utarajali pamoja na namna wanavyoshiriki katika kuandaa mitaala inayotumika kwenye vyuo na taasisi za elimu ya ufundi na mafunzo ya ufundi stadi.


Alitoa wito kwa waajiri wote nchini kuendelea kushirikiana na Serikali katika kuhakikisha malengo ya kukuza ujuzi na kuongeza soko la ajira yanafanikiwa kwa mustakabali wa maendeleo ya Taifa.


“Maendeleo ya uchumi wa nchi yoyote yanategemea sana ngazi ya ujuzi wa nguvukazi uliyokuwa nayo. Hivyo, mchango wa wadau ni muhimu,” alisema.


Alisema ushirikiano huo ni muhimu katika kuendeleza ujuzi kwa ajili ya kujenga uchumi wa viwanda. “Nataka nitumie fursa hii kuwapongeza lakini Serikali inatambua na inathamini juhudi mnazozifanya katika utoaji wa ajira kwa wahitimu wetu, tunawapongeza sana.”


Akizungumzia kuhusu kauli mbiu ya mwaka huu inayosema “Kuimarisha Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi kwa Uzalishaji wa Wafanyakazi Wenye Ujuzi Nchini Tanzania”, Waziri Mkuu alisema kauli hiyo ni thabiti kwani inaweka msisitizo katika ujenzi wa rasilimali watu yenye ujuzi.


Naye, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Adolf Mkenda alisema Serikali itaendelea kusimamia utekelezaji wa Makakati wa Taifa wa Uendelezaji wa Ujuzi wa Mwaka 2016/17-2025/26 ambao moja ya malengo yake ni kuwa na ushirikiano kati ya waajiri, wadau na vyuo au taasisi za elimu.


Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa Chama cha Waajiri Tanzania (ATE), Suzanne Ndomba-Doran alisema ili Tanzania iweze kushiriki kikamilifu katika soko shindani la Afrika Mashariki na dunia ni lazima hatua za makusudi zichukuliwe katika kukuza ujuzi hususani kwa vijana.


Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMATATU FEBRUARI 27,2023






















Share:

Sunday 26 February 2023

VIJANA WA ULINZI SHIRIKISHI WAONYWA KUJIHUSISHA NA VITENDO VYA KIHALIFU





Jeshi la Polisi Mkoa wa Kipolisi Ilala liwewaonya baadhi ya vijana wa ulinzi shirikishi kuacha tabia ya kujihusisha na vitendo vya kihalifu wakati wakitekeleza majukumu yao ya ulinzi katika mitaa yao.



Rai hiyo imetolewa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi Ilala Dr. Debora Magiligimba ACP katika bwalo la Polisi Buguruni alipokutana na vijana wa ulinzi shirikishi katika Wilaya ya Kipolisi Buguruni kwa lengo la kuwapa maelekezo na mwongozo wa utakaosaidia kuboresha utendaji wa kazi za ulinzi shirikishi katika maeneo yao.


 "Baadhi ya vijana wa ulinzi shirikishi mmekuwa mkishirikiana na wahalifu kwani mnatoa taarifa ya doria zenu kwa wahalifu mkiwajulisha sehemu mlipo jambo ambalo linawasaidia wahalifu hao kujipanga na kubadili sehemu ya kwenda kufanya matukio ya uhalifu",amesema.


Pia Kamanda Dr. Debora Magiligimba ametaka kila kikundi cha ulinzi shirikishi kuhakikisha kunakuwa na sare kwa ajili ya kuvaa wakati wa utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku ya ulinzi katika mitaa yao.


" Sare zinasaidia kuwatofautisha na vibaka pindi uhalifu unapotokea jambo ambalo litawasaidia wananchi kuwatofautisha na wahalifu", ameongeza.


Aidha Kamanda Dr. Debora Magiligimba amewataka vijana hao wa ulinzi shirikishi kuepuka vitendo vya ukatili katika familia zao na kutoa rai kwao kama kuna kijana wa ulinzi shirikishi ametendewa matendo ya ukatili wawezekufika katika madawati ya kijinsia na watoto yaliyopo katika vituo vya Polisi kutoa malalamiko yao.




Kikao hicho cha ulinzi shirikishi kiliudhuriwa Wakaguzi Kata 08 na vijana wa ulinzi shirikishi wapatao 139 kutoka katika Kata 08 zinazopatikana katika Wilaya ya Kipolisi Buguruni.
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger