Friday 30 September 2022

GGML WAZINDUA MASHINDANO YA SOKA KWA WATOTO WANAOZUNGUKA MGODI

Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Geita Gold Mining Limited, Terry Strong akisalimiana na timu ya soka ya watoto wanaozunguka kampuni hiyo kutoka Kata za Mtakuja na Nyankumbu zilizopo mkoani Geita. GGML jana imezindua mashindano ya mpira wa miguu kwa watoto hao ili kukabiliana na changamoto ya watoto wanaokwepa kwenda shule na kuingia kwenye eneo la mgodi na kufanya shughuli za uchimbaji bila ruhusa.
Waliosimama kutoka kulia ni Mratibu wa Miradi inayofadhiliwa na GGML kupitia mpango wa Wajibu wa Kampuni kwa Jamii (CSR), Moses Rusasa; Makamu Rais wa AngloGold Ashant-GGML anayeshughulikia miradi endelevu kwa upande wa Ghana na Tanzania, Simon Shayo; Mkurugenzi Mtendaji wa GGML, Terry Strong; Afisa Tawala wa mkoa wa Geita, Janeth Jonathan na wageni wengine wakiwa katika picha ya pamoja na timu ya soka ya watoto wanaozunguka mgodi wa GGML.
Waliosimama kutoka kulia ni Mratibu wa Miradi inayofadhiliwa na GGML kupitia mpango wa Wajibu wa Kampuni kwa Jamii (CSR), Moses Rusasa; Makamu Rais wa AngloGold Ashant-GGML anayeshughulikia miradi endelevu kwa upande wa Ghana na Tanzania, Simon Shayo; Mkurugenzi Mtendaji wa GGML, Terry Strong; Afisa Tawala wa mkoa wa Geita, Janeth Jonathan na wageni wengine wakiwa katika picha ya pamoja na timu ya soka ya watoto wanaozunguka mgodi wa GGML.


Na Mwandishi Wetu - Geita

KAMPUNI ya Uchimbaji Madini ya Dhahabu Geita (GGML) imezindua mashindano ya mpira wa miguu kwa watoto wanaozunguka mgodi huo ili kukabiliana na changamoto ya watoto kuingia kwenye eneo la mgodi na kufanya shughuli za uchimbaji bila ruhusa.

Mashindano hayo yanayohusisha kata za Mtakuja na Nyankumbu za Geita Mjini, yanalenga kuwapatia elimu watoto, walezi na wazazi wao madhara ya kuwatumikisha watoto wadogo katika shughuli za uchimbaji na kuwanyima fursa za kupata elimu.

Katika mashindano hayo, watoto kutoka mtaa wa Nyamalembo na Compound walimenyana na watoto kutoka mtaa wa Elimu na Nyankumbu.

Aidha, akizungumza katika uzinduzi huo uliofanyika katika uwanja wa General Tyre mjini Geita jana, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Geita Gold Mining Limited, Terry Strong alisema watoto ni sehemu muhimu katika biashara ya kampuni hiyo.

Alisema GGML imewekeza kwenye shule, hospitali na maeneo mengine ambayo watu wanaweza kupata huduma... ikiwa ni sehemu ya Wajibu wa Kampuni kuisadia Jamii inayozunguka mgodi ambapo kupitia mpango huo, GGML ilijenga zaidi ya madarasa 600 mwaka wa 2018.

“Watoto wadogo ndiyo kizazi cha baadaye na ndiyo wa kwanza kunufaika na uwekezaji wetu. Kampuni yetu inafuata kanuni Elekezi za Umoja wa Mataifa kuhusu Biashara na Haki za Kibinadamu na Kanuni za Hiari za Usalama na Haki za Kibinadamu (VPSHR) (UNGP).

“Kwa hivyo, tumekubali kuwalinda watoto dhidi ya hatari zozote zinazotokana na jinsi tunavyofanya biashara,” alisema.

Alisema idadi ya watoto wanaoingia kwenye shughuli za uchimbaji bila ruhusa imekuwa ya kutisha.

“Kwa kawaida sisi hutumia neno "kuwaokoa watoto" badala ya "kuvamia mgodi " kwa sababu watoto wapo chini ya umri wa watu wazima na wanalindwa na sheria za kitaifa na kimataifa.

“Hata hivyo, kutokana na ufuatiliaji wetu ni kwamba watoto wengi waliookolewa baada ya kuingia kwenye eneo la machimbo bila ruhusa, wengi wao tumekuwa tukiwakuta ndani au nje ya leseni yetu ya uchimbaji,” alisema.

Alisema kwa mujibu wa takwimu walizonazo ni kwamba watoto 680 waliokolewa ndani na nje ya eneo la shughuli za mgodi katika mgodi wa GGML kati ya mwaka 2019 na 2020.

Alisema ili kukabiliana na hili, GGML imekuwa ikishirikiana na serikali za mitaa kuzindua mfululizo wa kampeni za uhamasishaji, ikijumuisha ushirikiano wa moja kwa moja na shule za sekondari na msingi.

Aliongeza kuwa katika juhudi za kuwachangamsha watoto, kuwahusisha na michezo na kuwajengea mtindo bora maisha kwa manufaa ya afya zao, tumeamua kuandaa mashindano ya watoto katika kipindi cha likizo katika hali ya uchangamfu na kwenye kipindi chao cha likizo,

“Tunatarajia kuwa vijana wenye vipaji wataibuka kila mwisho wa shindano, na kwamba wataajiriwa na vilabu vikubwa kama Geita Gold Football Club (inayodhaminiwa na GGML) ili kuzidi kuonesha uwezo wao katika uwanja wa Magogo (pia unaodhaminiwa na GGML). Mpango ni kuwaokoa watoto hawa na kuwasaidia kukuza vipaji vyao,” alisema.

Awali, Makamu wa Rais wa AngloGold- GGML anayeshughulikia miradi endelevu kwa Ghana na Tanzania, Simon Shayo alisema moja ya tunu muhimu za kampuni hiyo ni kuhakikisha jamii inayozunguka mgodi huo inanufaika.

Alisema mipango ya kampuni hiyo inalenga kuboresha sekta ya afya, elimu, michezo na utamaduni ili kukuza vipaji vya watoto hao.

Aidha, Afisa utawala wa mkoa wa Geita, Janeth Jonathan akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Geita, Wilson Shimo, alisema wazo la kuanzisha mashindano hayo lilitokana na kamati iliyoundwa ili kukabiliana na wimbi la watoto wanaofanya kazi hatarishi katika eneo la Nyamatagata lenye mlipuko wa madini.

Alisema licha ya kwamba GGML imejenga uwanja, michezo kwa watoto inatakiwa kuzingatiwa ili kuwaondoa katika wimbi hilo la ajira hatarishi hasa ikizingatiwa watoto wanahusishwa zaidi kuchenjua madini kazi ambayo inahusisha kushika kemikali hatari za mercury.

Naye Afisa Kazi kutoka idara ya kazi mkoani humo, Jofrey Oled alitoa wito kwa wazazi kuacha watoto wapate muda wa kusoma badala ya kuwatumikisha kwenye kazi hatari kwani ni kosa kisheria.

Alisem kwa mujibu wa sheria ya ajira na mahusiano kazini, mzazi atakayepatikana na kosa hilo atapata adhabu ya kulipa faini Sh milioni tani au kwenda kutumia adhabu ya kifungo cha mwaka mmoja jela au vyote viwili.


Share:

HII NDIO DAWA YA MATAPELI WA VIWANJA

Share:

PAKUA APP YA MALUNDE 1 BLOG TUWE TUNAKUTUMIA HABARI NA MATUKIO BURE

Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO IJUMAA SEPTEMBA 30,2022













Share:

Thursday 29 September 2022

KIVULINI YATOA TUZO ZA UJASIRI NA UBUNIFU KWA VIONGOZI VINARA WA KUHAMASISHA JAMII KUTOKOMEZA UKATILI WA KIJINSIA MWANZA


Mkurugenzi Mtendaji Shirika la KIVULINI, Yassin Ally (kulia) akimkabidhi tuzo Sheikh wa Mkoa Mwanza, Hassan Kabeke
Mkurugenzi Mtendaji Shirika la KIVULINI, Yassin Ally (kulia) akimkabidhi tuzo Afisa Maendeleo ya Jamii Mkoa Mwanza, Isack Ndassa.
Mkurugenzi Mtendaji Shirika la KIVULINI, Yassin Ally (kulia) akimkabidhi tuzo Mwenyekiti Mwenza wa Kamati ya Amani ya viongozi wa dini mkoani Mwanza.

 ***
Shirika la kutetea haki za wanawake na watoto (KIVULINI) limetoa tuzo za ujasiri na ubunifu wa kuhamasisha jamii kutokomeza ukatili wa kijinsia dhidi ya wanawake na watoto kwa viongozi mbalimbali mkoani Mwanza.


Tuzo hizo zimekabidhiwa na Mkurugenzi wa shirika hilo, Yassin Ally Alhamsi Septemba 29, 2022 kwenye kikao kazi cha Kamati ya kutokomeza ukatili wa kijinsia kwa wanawake na watoto (MTAKUWWA) Mkoa Mwanza.


Miongoni mwa viongozi waliokabidhiwa tuzo hizo ni pamoja na Afisa Maendeleo ya Jamii Mkoa Mwanza Isack Ndassa, Sheikh wa Mkoa Mwanza Hassan Kabeke, Kamati ya MTAKUWWA Mkoa Mwanza pamoja na Kamati ya Amani ya Viongozi wa Dini Mkoa Mwanza.
Akizungumza wakati wa kikao hicho, Mkurugenzi huyo wa shirika la Kivulini Yassin Ally alisema kumekuwa na uelewa wa kutosha kwa wajamii kutonyamazia vitendo vya ukatili wa kijinsia ambapo wamekuwa wakifichua vitendo hivyo katika madawati ya jinsia, ustawi wa jamii na hata kwenye vyombo vya habari.


“Sasa tunashuhudia matokeo ya MTAKUWWA yametoa elimu na wanajamii na viongozi mbalimbali wakiwemo viongozi wa dini hawanyamazii tena vitendo vya ukatili wa kijinsia hususani kwa wanawake na watoto tofauti na ilivyokuwa hapo awali ambapo ilionekana ni jukumu la wadau kama KIVULINI”, alibainisha Yassin.


Naye Sheikh wa Mkoa Mwanza Hassan Kabeke alisema katika kukabiliana na vitendo vya ukatili wa kijinsia katika ndoa, BAKWATA imeanza kutoa mafunzo ya misingi ya ndoa kwa wanaume wa kiislamu kabla ya kufunga ndoa ambapo hapo awali mafunzo ya aina hiyo yalikuwa wakitolewa kwa wanawake pekee.


“Hatua hii itasaidia ndoa kudumu tofauti na sasa ambapo ndoa nyingi huvunjika kutokana na wanaume wengi kutokuwa na ujuzi wa namna bora ya kulea ndoa” ,alisema Sheikh Kabeke.

Na George Binagi-GB Pazzo, BMG
Share:

TBS YATOA MAFUNZO KWA WAFANYABIASHARA WANAOAGIZA NA KUUZA BIDHAA ZA CHAKULA NA VIPODOZI JIJINI MWANZA


Shirika la Viwango Tanzania (TBS) limetoa mafunzo kwa wafanyabiashara wanaoagiza na kuuza bidhaa mbalimbali za chakula na vipodozi jijini Mwanza ili kuwajengea uwezo kutekeleza shughuli zao kwa kuzingatia Sheria. 

Mafunzo hayo yamefanyika Alhamisi Septemba 29, 2022 yakiwashirikisha wafanyabishara mbalimbali wakiwemo waagizaji wa bidhaa kutoka nje ya nchi, wamiliki wa maghala ya kuhifadhia bidhaa na wamiliki wa maduka makubwa ya bidhaa za jumla. 

Akifungua mafunzo hayo, Mkuu wa Wilaya Nyamagana mkoani Mwanza Amina Makilagi amewataka wafanyabishara kuwa wazalendo kwa kuhakikisha wanaingiza nchini bidhaa zenye ubora zisizo na madhara kwa watumiaji 

Amesema Mwanza ni jiji la pili kiuchumi nchini na pia kitovu cha biashara katika nchi za ukanda wa Afrika Mashariki hivyo ni vyema wafanyabishara wakatumia fursa hiyo vizuri kwa kuhakikisha wanaagiza bidhaa zenye viwango na kuzihifadhi katika mazingira salama ili zisiharibike kabla ya kumfikia mtumiaji. 

"Serikalini inayoongozwa na Rais wetu Mhe. Samia Suluhu Hassan inaendelea kuboresha miundombi ya usafiri na usafirishaki ikiwemo ujenzi wa meli mpya katika Ziwa Victoria, bandari kavu ya Fela, reli ya kisasa (SGR) hadi jijini Mwanza na uboreshaji wa uwanja wa ndege wa Mwanza ili kurahisisha shughuli za kibiashara" amesema DC Makilagi. 

Katika hatua nyingine, Makilagi ameonya kuwa wafanyabishara wanaouza bidhaa zenye viambata sumu wanaliangamiza taifa na wanaenda kinyume na lengo la Serikali ya kuhakikisha afya ya wananchi iko salama akisema tafiti mbalimbali zinazoendelea kufanyika zinaonyesha magonjwa kama kansa yanasabanishwa na ulaji wa vyakula pamoja na utumiaji wa vipodozi vyenye viambata sumu. 

Pia Makilagi ameipongeza TBS kwa kuendelea kutoa elimu na semina kwa wadau mbalimbali ili kutambua bidhaa zenye ubora na zile zenye viambata sumu zilizopigwa marufuku akisema kila mdau anapaswa kutimiza wajibu ili jamii iwe salama. 

Naye Meneja wa TBS Kanda ya Ziwa, Mhandisi Joseph Mwaipaja amesema Shirika hilo litaendelea kuchukua hatua kali za kisheria kwa wafanyabishara wanaoingiza sokoni bidhaa zilizopigwa marufuku ingawa kabla ya kuchukua hatua hizo TBS inawaelimishwa kwanza. 

Kwa upande wake mmoja wa wafanyabiashara walioshiriki mafunzo hayo, Mohamed Muhan amesema watazingatia elimu waliyoipata ikiwemo kuagiza na kuuza bidhaa zilizosajiliwa kusajiliwa kisheria ili kwa pamoja kwa kushirikiana na TBS wafanikishe jitihada za kuondoa sokoni bidhaa zenye viambata sumu. 

Share:

NHC YATANGAZA MRADI WA “SAMIA HOUSING SCHEME” KWENYE MAONESHO YA MADINI GEITA


Bi. Domina Rwemanyila Afisa habari Shirika la Nyumba la Taifa NHC akitoa maelezo kuhusu mradi wa Samia Housing Scheme unaojengwa Kawe katika jiji la Dar es Salaam kwenye maonesho ya tano ya Teknolojia ya Madini yanayofanyika EPZA Bombambili mkoani Geita.

…………………………………….

Shirika la Nyumba la Taifa limejipanga kutekeleza mradi wa SAMIA Housing Scheme unaotarajia kujenga nyumba zaidi ya 5000 na kuzalisha ajira zaidi ya Elfu Ishirini na Sita.

Hayo yameelezwa na Daniel Kure Afisa Mauzo na Masoko Mwandamizi kutoka Shirika la Nyumba la Taifa wakati akizungumzia ushiriki wao katika Maonyesho ya Madini yanayoendelea Mkoani Geita ambapo amesema kuwa wataanza na awamu ya kwanza katika Mkoa wa Dar es salaam na kisha Dodoma.

Afisa huyo amesema kuwa wameshiriki katika maonyesho hayo ili kutoa taarifa kwa wananchi kuhusu mradi huo na hivyo kurahisisha upatikanaji wa taarifa na kwa wale wote wenye mahitaji ya nyumba waweze kupata kwa wakati.

Amesema kuwa mradi huo umeangalia vipato vya watanzania wote kwa kuangalia madaraja mbalimbali wakiwemo watumishi wa serikali,sekta binafsi pamoja na wafanyabiashara.

‘Mradi huu hadi utakapokamilika katika awamu zote utagharibu Bill 466 na utekelezaji wake utaanzia eneo la Kawe Tanganyika Packers baada ya hapo ndipo utasambaa kwa nchi nzima na tunatarajia tutajenga Nyumba 5000’amesema Daniel

Daniel amewataka wananchi wote wanaohitaji nyumba wahakikishe wanatumia fursa hiyo mapema kwani wataanza kuutekeleza kuanzia mwezi wa kumi na baada ya miezi kumi na mbili watakuwa wameukamilisha.

Aidha Daniel amewataka wananchi kujitokeza kwa wingi katika Maonyesho hayo ili waweze kupata taarifa kamili kuhusiana na mradi huo.

‘Nyumba zetu zinakuwa ghali kwa sababu tunapewa eneo na Halmashauri eneo ambalo hakuna miundombinu ,barabara,maji na umeme hivyo mara nyingi sisi ndiyo tunagharamia na hivyo kufanya gharama kuongezaka na kuwa kubwa na watanzania wanaona kama gharama kubwa lakini ukizingatia gharama zote hizo unaona kabisa ubora wa nyumba zanyewe na huduma tunayoitia ’amesema Daniel

Hata hivyo amesema Shirika la Nyumba la Taifa NHC katika kutekeleza hiyo miradi linaingia katika mchakato wa kununua Ardhi pamoja na kuweka miundombinu mbalimbali ili kurahisisha huduma zote.
Afisa Mauzo na Masoko Shirika la Nyumba la Taifa NHC Bw. Daniel Kure akitoa maelezo kuhusu mradi wa Samia Housing Scheme unaojengwa Kawe katika jiji la Dar es Salaam kwenye maonesho ya tano ya Teknolojia ya Madini yanayofanyika EPZA Bombambili mkoani Geita.
Afisa Mauzo na Masoko Shirika la Nyumba la Taifa NHC Bw. Daniel Kure na Bi. Domina Rwemanyila Afisa habari Shirika la Nyumba la Taifa NHC wakiwa katika picha ya pamoja kwenye banda la shirika hilo.
Bi. Domina Rwemanyila Afisa habari Shirika la Nyumba la Taifa NHC akioneshwa na Bw. Andrew Mwinuka mnufaika wa myumba za mradi wa Bombabili mjini Geita muamala aliolipa kwa ajili ya kununua nyumba yake katika mradi huo.
Bi. Domina Rwemanyila Afisa habari Shirika la Nyumba la Taifa NHC akimfafanulia jambo Bw. Andrew Mwinuka mnufaika wa mradi wa nyumba za NHC Bombambili mjini Geita aliyetembelea katika banda la shirika hilo kwenye maonesho ya madini mjini Geita.
Bi. Domina Rwemanyila Afisa habari Shirika la Nyumba la Taifa NHC akizungumza na mmoja wa raia wa kigeni waliotembelea katika banda la shirika hlo kwenye maonesho ya madini mjini Geita leo.
Muonekano wa nyumba mbalimbali katika picha zitakazojengwa kwenye mradi wa Samia Housing Scheme Kawe jijini Dar es Salaam.
Share:

GGML MDHAMINI MKUU WA MAONESHO YA TANO YA KITAIFA YA TEKNOLOJIA YA MADINI -GEITA


Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Msafiri Mbibo (kushoto) akimsikiliza Ofisa wa masuala ya usalama kutoka Kampuni ya Geita Gold Mining Ltd. (GGML), Israel Isaka (kulia) aliyekuwa akitoa maelezo namna kampuni hiyo inavyozingatia masuala ya afya na usalama katika shughuli za uchimbaji wa madini. Jana Mbibo alitembelea banda la GGML ambao ni wadhamini wakuu wa Maonesho ya kitaifa ya Teknolojia ya Madini yanayoendelea katika viwanja vya Bombambili Geita.
Mratibu wa Miradi inayofadhiliwa na Geita Gold Mining Limited (GGML) fedha za Wajibu wa Kampuni kwa Jamii (CSR), Moses Rusasa (kushoto) akifafanua namna kampuni hiyo inavyoshirikiana na serikali ya mkoa wa Geita kufadhili miradi mbalimbali kupitia Mpango wa Uwajibikaji wa Kampuni kwa Jamii (CSR).
Mratibu wa Miradi inayofadhiliwa na Geita Gold Mining Limited (GGML) fedha za Wajibu wa Kampuni kwa Jamii (CSR), Moses Rusasa  akifafanua namna kampuni hiyo inavyoshirikiana na serikali ya mkoa wa Geita kufadhili miradi mbalimbali kupitia Mpango wa Uwajibikaji wa Kampuni kwa Jamii (CSR).



Na Mwandishi Wetu - Geita

KAMPUNI ya Geita Gold Mining Limited (GGM) kwa mwaka wa tano mfululizo imejitosa kuwa mdhamini mkuu wa Maonesho ya Kitaifa ya Teknolojia ya Madini ambayo mwaka huu yanafanyika katika viwanja vya Ukanda wa Uwekezaji (EPZ) Bombambili mkoani Geita.


Mwaka huu, GGML imekuwa mdhamini mkuu tena katika maonesho hayo yanayotumika kuonesha teknolojia zinazotumika katika sekta ya uchimbaji pamoja na kuwezesha kliniki za biashara kwa wajasiriamali na kampuni zenye uhitaji na fursa zinazopatikana katika mgodi wa GGML.


Maonesho hayo yaliyoanza tarehe 27 Septemba 2022 na kufikia tamati tarehe 8 Oktoba 2022, yatatoa fursa kubwa kwa washiriki kujifunza teknolojia mbalimbali za kisasa katika uchimbaji wa madini.

Kampuni ya GGML inaungana na kampuni 600 zinazoshiriki maonesho ya mwaka huu ikiwa na mifumo na teknolojia za kisasa kwa ajili ya kuwaonesha wadau hususani wachimbaji wadogo.


Akizungumzia udhamini wa GGML katika maonesho hayo, Makamu Rais wa Kampuni Anglo Gold Ashanti – GGML anayeshughulikia miradi endelevu kwa nchi za Ghana na Tanzania, Simon Shayo amesema kampuni hiyo inafarijika kuwa mdhamini mkuu wa maonesho hayo.


Alisema maonesho hayo ya teknolojia ya madini ambayo yalianza kidogo kidogo miaka mitano iliyopita, ni wazo zuri ambalo Serikali ya mkoa wa Geita na wadau wengine walikuja nalo.


“Tunafarijika kwamba tulihusishwa kama mmoja wa wadhamini wakubwa kuanzia mwanzoni lakini pia tunatambua kwamba wadau wengine ambao hawapo hata kwenye sekta ya madini kama mabenki na wadau wengine waliona umuhimu wa kushiriki si tu kudhamini lakini pia kuleta bidhaa zao kwenye maonesho haya na kuzionesha.


“Wito wetu kwa wadau wote hata wale ambao hawapo kwenye sekta ya madini, tunawaalika waungane na serikali ya mkoa wa Geita na sisi kama GGML tutaendelea kuwepo wakati wote kuhakikisha maonesho haya yanakuwa makubwa, yanakuwa na tija na yanakuwa ya kimataifa,” alisema Bw. Shayo.


Aidha, akizungumzia udhamini huo wa GGML, Naibu Katibu Mkuu wa Madini, Msafiri Mbibo amesema GGML wanafanya vizuri sio tu kwa namna wanavyoonesha utayari wa kufadhili bali mwaka hata mwaka kwa ufadhili wao umewezesha maonesho hayo kukua.


“GGML wanatuwezesha ili tujenge uwezo kwa washiriki wengi zaidi wa maonesho ambapo sio GGML peke yake bali na hata watu wengine washiriki kwa manufaa ya nchi nzima na watu wote,” alisema.


Aidha, Meneja wa Kampuni ya Blue Coast Investment Limited ambayo ni mmoja wa wakandarasi wa kampuni ya GGML, Jeremiah Musa, alisema wamefanikiwa kupata zabuni mbili kutoka GGML ambazo ni kusambaza mafuta pamoja na kusafirisha wafanyakazi wa kampuni hiyo.


“Mbali na kusafirisha asilimia 30 ya mafuta ndani ya GGML pia wametupatia mafunzo mbalimbali jambo ambalo limetusaidia kampuni yetu kukua kwa haraka na kupata fursa ya kujitanua na kutoa fursa za ajira kwa Watanzania kwani mpaka sasa tuna wafanyakazi 400 walioajiriwa,” amesema.


Naye Msimamizi wa shughuli za kihandisi African Underground Mining Services (AUMS), Redempta Samky amesema kampuni hiyo ambayo inahusika na kutoa huduma za uchimbaji na uendeshaji wa migodi hasa chini ya ardhi (underground), imezidi kukua kutokana na GGML kuwaongezea miradi mbalimbali.


“GGML wametusaidia kukua kama kampuni kwa sababu tulianza na mradi mmoja wa Star and Comet ambao walitupatia, tukaendesha vizuri tukapata mradi mwingine wa Nyankanga ambao ndani yake kulikuwa na miradi mitatu zaidi. Sasa hivi tumeanzisha mradi mpya wa Geita hill ... kwa hiyo huu wote ni ukuaji kwamba GGML wanatuamini ndio maana tunaendelea kutoa huduma.


“Mpaka sasa tuna wafanyakazi zaidi ya 200, tulianza mwaka 2016 kufanya kazi hapa GGML, kwa hiyo sisi ni watoa huduma wa GGML,” alisema.


Maonesho hayo ya tano ya kitaifa ya teknolojia ya madini kwa mwaka huu yamebeba kauli mbiu ya “Madini na fursa za uchumi ajira kwa maendeleo endelevu”.


GGML imekuwa kinara wa uwekezaji kwenye jamii tangu kuanzishwa kwake mwaka 2000 ambapo vipaumbele vikuu vimekuwa ni miradi ya afya, elimu, maji, barabara, miradi ya kukuza kipato na miradi mingine mingi ya kijamii ili kuhakikisha jamii mwenyeji inapata maisha bora.


Mapema mwaka huu, kampuni ya GGML iliibuka mshindi wa jumla katika kampuni zinazofanya vizuri kwenye sekta ya madini nchini Tanzania kwa mwaka wa fedha 2020/2021 baada ya kunyakua tuzo katika vipengele vya uwajibikaji wa kampuni kwa jamii, mazingira, usalama, mlipaji bora wa mapato (kodi) na uendelezaji wazawa.

Share:

MLINDOKO ACHAGULIWA MWENYEKITI WA WAZAZI SHINYANGA MJINI..."SITAPENDA KUSIKIA UONGO UONGO"


Mwenyekiti wa jumuia ya wazazi CCM wilaya Fue Mlindoko akitangaza matokeo ya wagombea.

 Na Suzy Luhende , Shinyanga blog

Mwenyekiti wa jumuia ya wazazi wilaya ya Shinyanga mjini  Fue Mlindoko amesema katika uongozi wake hatapenda kuona watu wachonganishi ,waongo wanaorudisha nyuma maendeleo ya jumuia hiyo,endapo wakionekana watu wa  namna hiyo atapambana nao kwa kufuata sheria na kanuni na watatolewa mara moja ndani ya jumuia hiyo.

Hayo ameyasema jana kwenye kikao cha baraza la jumuia ya wazazi  lililofanyika katika ukumbi wa CCM wilaya ya Shinyanga la kuwachagua viongozi ambao walikuwa hawajachaguliwa, ambao ni katibu elimu malezi na mazingira na wajumbe wa kamati ya utekelezaji.

Mlindoko alisema hatapenda kusikia mambo ya uongo uongo katika jumuia yake, atawapenda watu wenye kutoa ushauri mzuri wa kujenga chama na kuleta maendeleo ndani ya chama na jumuia ya wazazi.

"Nawaombeni sana viongozi wenzangu uchaguzi umeisha tufanye kazi kwa pamoja tushirikiane, ili jumuia yetu iweze kusonga mbele, pia tutunze siri zetu za ndani za kimaendeleo na tufanye mabadiliko, ni vizuri tuweke alama nzuri katika jumuia yetu  na kuitendea haki," amesema Mlindoko.

" Inatakiwa tuwe wazazi kweli tusimame katika eneo letu, kwa sababu sisi ndio wazazi walezi, tabia yangu ni kuleta mshikamano, tuwe na upendo wa hali ya juu tupendane zaidi na dhumuni letu ni kujenga timu yetu imara"aliongeza. 

Kwa upande wake katibu wa jumuia ya wazazi wilaya ya Shinyanga Doris Kibabi amewaomba viongozi wote waliochaguliwa wawe viongozi wa mfano waonyeshe alama kuwa wamefanya maendeleo furani wasiache madoa ambayo yatakuwa hayana faida kwa kizazi kijacho, pia aliwaomba wakemee masuala ya ukatili wanayofanyiwa watoto.

"Nina imani na viongozi mlionichagulia tutaanza kwa mchaka mchaka, pia  viongozi wa kata nawaombeni muwe mnafanya vikao ndani ya miezi mitatu, kwani sisi wenyewe ndiyo tunaitengeneza jumuia yetu,  mnatakiwa muonyeshe alama tusiache madoa ambayo yatakuwa hayana faida kwa kizazi chetu tufanye kitu chenye faida kwa kizazi chetu,pia tukemee matukio mbalimbali ya ukatili kwa watoto wetu na tusimamie masuala ya elimu ili watoto wetu watimize ndoto zao", alisema Kibabi.

Aidha katika uchaguzi huo Richard Chacha Mseti alichaguliwa kuwa katibu elimu malezi na mazingira ambaye alishinda kwa kura 51, ambapo wapiga kura walikuwa 56, pia walichaguliwa wajumbe wa kamati ya utekelezaji, ambao ni Zulfa Dali, Daniel Kapaya, Josephate Msozi, na Giti Mliga Boniface, ikiwa msimamizi wa uchaguzi huo alikuwa Kudely Sokoine ambaye alikuwa katibu elimu malezi na mazingira hakugombea tena nafasi.
Wajumbe wa jumuia ya wazazi wakitumbukiza kura zao kwenye sanduku la kupigia kura.
Wajumbe wa jumuia ya wazazi wakidumbukiza kura zao kwenye sanduku la kupigia kura
Aliyekuwa katibu elimu malezi na mazingira Kudely Sokoine akihesabu kura kwa uwazi kwenye baraza la wazazi wilaya shinyanga.
Katibu elimu malezi na mazingira Richard Chacha Mseti akiwashukuru wajumbe baada ya kumchagua.
Katibu elimu malezi na mazingira Richard Chacha Mseti akiwashukuru wajumbe baada ya kumchagua.
Wajumbe wa jumuia ya wazazi wilaya ya Shinyanga mjini wakisikiliza maelekezo.
wajumbe wa jumuia ya wazazi wilaya ya Shinyanga mjini wakipiga kura.
Wenyekiti wa jumuiya ya wazazi Fue Mlindoko akitangaza matokeo.
Doris Kibabi,Katibu wa jumuiya ya wazazi wilaya ya Shinyanga mjini
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger