Monday 3 January 2022

BENKI YA CRDB YAZINDUA KAMPENI KUHAMASISHA WATANZANIA KUTUMIA HUDUMA NA BIDHAA BUNIFU CRDB



Benki ya CRDB imewataka Watanzania kutumia huduma na bidhaa bunifu zinazotolewa na benki hiyo kwa makundi mbalimbali ya wateja kufanikisha malengo waliyojiwekea katika mwaka huu mpya wa 2022. Hayo yamesemwa wakati wa uzinduzi wa kampeni ya “Unachostahili ni CRDB Bank” inayolenga katika kutoa elimu na kuwaonyesha Watanzania fursa mbalimbali zinazotolewa na Benki yao ya CRDB


Akizungumza katika uzinduzi wa kampeni hiyo Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela alisema Benki ya CRDB ikiwa benki ya kizalendo inatambua kuwa inawajibu wa kuwasaidia Watanzania na wadau wengine wa maendeleo nchini kutimiza malengo katika mwaka huu mpya 2022. Nsekela alisema kupitia kauli mbiu yake ya “Benki inayomsikiliza mteja”, Benki ya CRDB imekuwa ikisikiliza na kufanyia kazi mahitaji ya wateja ili kuwapa wanachostahili.
“Mwaka jana tulifanya utafiti maalum kufahamu mahitaji halisi ya wateja ambayo yamekuwa yakibadilika kila uchwao, utafiti ule ulienda sambamba na kupokea maoni ya namna bora ya kuwahudumia wateja. Ninajivunia kusema tumeweza kufanyia kazi maoni ya wateja na kuboresha sehemu kubwa ya huduma na bidhaa zetu ili kuweza kuwapa wanachostahili,” amesema Nsekela.


Nsekela alisema moja ya maeneo ambayo Benki hiyo imeyafanyia maboresho ni katika mtandao wa ufikishaji huduma za kibenki ambao unajumuisha mifumo ya kidijitali ikiwamo SimBanking, CRDB Wakala, TemboCard, na Internet banking ambayo inawawezesha wateja kupata huduma popote pale walipo. Hivi sasa wateja wa Benki ya CRDB wanaweza kupata zaidi ya asilimia 90 ya huduma kupitia njia hizo mbadala za upatikanaji wa huduma.
“Tunatambua wateja wanahitaji muda mwingi zaidi katika kufanya shughuli zao za kiuchumi, hivyo uboreshaji wa mifumo hii utawawezesha kufanya miamala yao kwa wakati na hivyo kuongeza ufanisi katika biashara na maeneo yao ya kazi hivyo kuongeza ufanisi,” amesema Nsekela huku akibainisha maboresho hayo yamesaidia kuongeza urahisi na unafuu wa kwa wateja.


Katika kampeni hiyo Benki ya CRDB pia imejipanga kuwaelimisha wateja juu ya huduma za uwezeshaji zinazotolewa na benki hiyo kupitia mikopo kwa makundi mbalimbali ya wateja ikiwamo wanafunzi, wafanyakazi, wajasiriamali, wakulima, wafanyabishara, makampuni na taasisi. “Niwahakikishie kuwa Benki yetu ina uwezo mkubwa kimtaji unaowezesha kutoa mikopo kwa makundi mbalimbali kwa gharama nafuu, hivyo niwasihi Watanzania kuchangamkia fursa zilizopo kufikia malengo yao.”
Nsekela alisema benki hiyo pia imejipanga kuendelea kushiriki kikamilifu katika miradi ya kimkakati ya Serikali huku akimpongeza Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuendeleza utekelezaji wa miradi hiyo. “Ukubwa wa mizania yetu unatufanya tuwe na uwezo mkubwa wa kushiriki katika kuwezesha wadau wote wanaoshiriki katika miradi hii ikiwamo Serikali yenyewe, pamoja na wakandarasi na wazabuni,” amesema Nsekela.


Aidha, Nsekela alieleza kuwa katika kipindi cha kampeni hiyo wateja pia watakuwa wakielimishwa juu ya umuhimu wa kujiwekea akiba ili kufikia malengo kwa kutumia akaunti mbalimbali za benki hiyo. Benki ya CRDB ina akaunti zinazoongoza makundi mbalimbali ya wateja kuanzia akaunti za Junior Jumbo maalum ya watoto, wanafunzi - Scholar, wafanyakazi - Salary, wajasiriamali - Hodari, wafanyabiashara - Current, wakulima – FahariKilimo, Wanawake - Malkia na hata Wastaafu – Pension Account.


“Hizi ni baadhi tu ya fursa nyingi ambazo wateja na wadau wetu wanastahili ili kufikia malengo yao kwa mwaka huu 2022. Katika kipindi hiki cha kampeni tumejipanga kuhakikisha tunatoa huduma za daraja la kwanza kwa wateja wetu ili wawaeze kunufaika na fursa hizi zinazotolewa na benki yao.,” amesema Nsekela.
Naye Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Benki ya CRDB, Tully Mwambapa amesema benki hiyo itaendelea kutekeleza ahadi yake ya kumuweka kwanza mteja na kuwakaribisha Watanzania wote, wateja binafsi, makampuni, na taasisi kuchangamkia fursa hizo kufikia malengo yao. “Benki yetu ni imara na yenye kuaminika kwa ubunifu hapa nyumbani na nje ya nchi.


Nafikiri wote tumeona tulivyopokelewa vizuri hata nchi za jirani za Burundi na Congo, na inavyoaminika na Serikali kwa kuwa na mchango mkubwa kwenye kusaidia kujenga uchumi,” alisema Tully huku akiwataka wafanyabiashara wanaofanya biashara nan chi za jirani pia kutumia fursa zinazotolewa na benki hiyo.
Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha Masoko, Benki ya CRDB, Joseline Kamuhanda aliwashukuru Watanzania kwa kuendelea kuichagua benki hiyo kuwa mtoa huduma wao na kuwaahidi benki hiyo itaendelea kuwapa wanachostahili kupitia bidhaa na huduma bunifu.


--
Share:

MASELE AMPONGEZA SPIKA NDUGAI KUMUOMBA RADHI RAIS SAMIA...."HUU NDIYO UUNGWANA


Aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Shinyanga Mjini na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Bunge la Afrika Stephen Masele amempongeza Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Job Ndugai kumuomba Radhi Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan.

Kupitia Ukurasa wake wa Twitter Stephen Masele andika ujumbe huu: 
"Hongera mhe Spika kwa kumuomba radhi Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan na kuwaomba radhi watanzania. Huo ndio uungwana"

Mapema leo Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai amemuomba radhi Rais Samia Suluhu Hassan na Watanzania wote ambao waliupokea ujumbe wake kitofauti kuwa yeye ni miongoni mwa watu wanaopinga jitihada zinazofanywa na Rais katika kuliletea Taifa maendeleo.

Pia amewahakikishia watanzania yeye ni yule yule ni uimara wake upo palepale na wale waliomrushia matusi amewasamehe bure na wengine hawajui wayatendayo na ndio maana amebeba matusi yote hivyo amekosa na asamehewe.

“Kwa hiyo binafsi yangu popote pale ambapo nilihisiwa kwamba nimetoa neno la kumvunja moyo Rais wetu na akavunjika moyo, ninatumia fursa hii kupitia kwenu kumuomba radhi sana mheshimiwa Rais na kwa Watanzania wote,”amesema.

Share:

SPIKA NDUGAI AMUOMBA RADHI RAIS SAMIA,ASIKITISHWA NA KAULI YAKE YA KUMVUNJA MOYO


Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai,akisisitiza jambo kwa akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) leo Januari 3,2022 jijini Dodoma .

Na Dotto Kwilasa,Malunde 1 blog-DODOMA.

SPIKA wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Job Ndugai amemomba radhi Rais Samia Suluhu Hassan na watanzania kwa ujumla kwa namna yoyote ambayo alihisiwa kutoa maneno ya kumvuja moyo na kusababisha Rais kuvunjika moyo.

Ndugai amesema hayo mapema leo Bungeni Jijini Dodoma katika Mkutano wake na waandishi wa habari uliolenga mambo kadhaa ikiwemo kuomba radhi kwa kauli yake aliyoitoa mwishoni mwa mwaka 2021 ikieleza kukerwa na madeni ambayo Tanzania inakopa kwenye Benki ya IMF.

Amesema kauli aliyoitoa ni tofauti na baadhi ya vyombo vya habari vilivyo mnukuu na kudai kwamba amechezewa
 na mitandao ya kijamii na hakuwa na nia mbaya kama ambavyo imeeleweka na kusababisha taharuki kwa jamii.

Hatua hiyo imekuja kufuatia  video ambayo Spika Ndugai anaonekana akipinga utaratibu wa Serikali wa uchukuaji mikopo kutoka taasisi za fedha na kwamba kwa mwendo huo nchi itakuja kupigwa mnada.

Video hiyo iliyozua mjadala mkubwa kwenye mitandao ya kijamii na kupewa uzito mkubwa na vyombo vya habari nchini imepelekea  Spika Ndugai kukiri wazi kwamba amekosea na amaomba msamaha Kwa Rais,wananchi na Kwa Mwenyezi Mungu.

'Kwa wale wote waliokwazwa na kauli yangu naomba sana mnisamehe,nimekosea sana , kwani natambua kazi kubwa iliyofanywa na Rais Samia katika kipindi kifupi cha uongozi wake,mengi ameyafanya kwenye Wilaya yangu ,

Mfano  mkopo wa sh. trilioni 1.3 ambazo Tanzania imepata kutoka IMF, fedha hizo zimefanya mambo makubwa hasa katika Wilaya ya Kongwa ambayo imepata mgawo wa sh. bilioni 3 sawa na mapato yake ya ndani ya mwaka mmoja kwa ajili ya ujenzi wa madarasa,"Amesema 


Share:

SPIKA NDUGAI:'NIMEKOSA MIMI,NIMEKOSA SANA,NISAMEHENI'


Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai,akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) leo Januari 3,2022 jijini Dodoma pamoja na kumuomba radhi Rais Samia na watanzania wote ambao waliupokea ujumbe wake kitofauti.

Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai,akisisitiza jambo kwa akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) leo Januari 3,2022 jijini Dodoma pamoja na kumuomba radhi Rais Samia na watanzania wote ambao waliupokea ujumbe wake kitofauti.


Waandishi wa habari wakimsikiliza Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai,wakati akizungumza nao leo Januari 3,2022 jijini Dodoma pamoja na kumuomba radhi Rais Samia na watanzania wote ambao waliupokea ujumbe wake kitofauti.

.........................................................

Na.Alex Sonna,Dodoma

Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai amemuomba radhi Rais Samia Suluhu Hassan na Watanzania wote ambao waliupokea ujumbe wake kitofauti kuwa yeye ni miongoni mwa watu wanaopinga jitihada zinazofanywa na Rais katika kuliletea Taifa maendeleo.

Pia amewahakikishia watanzania yeye ni yule yule ni uimara wake upo palepale na wale waliomrushia matusi amewasamehe bure na wengine hawajui wayatendayo na ndio maana amebeba matusi yote hivyo amekosa na asamehewe.

Spika Ndugai ameomba radhi hiyo leo Januari 3,2022 jijini Dodoma wakati akizungumza na Waandishi wa habari ambapo amesema amesema kuwa hotuba yake haikuwa na jambo la kukashifu wala kudharau juhudi za Serikali bali alikuwa anasisitiza ulipaji wa kodi na tozo mbalimbali.

“Kwa hiyo binafsi yangu popote pale ambapo nilihisiwa kwamba nimetoa neno la kumvunja moyo Rais wetu na akavunjika moyo, ninatumia fursa hii kupitia kwenu kumuomba radhi sana mheshimiwa Rais na kwa Watanzania wote,”amesema.

Amesema anaunga mkono jitihada zote za Serikali ikiwa ni pamoja na kukopa fedha kwa ajili ya kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo, na wanaomuona yuko kinyume basi wamemuelewa vibaya.

Spika Ndugai amesema wao ni kitu kimoja na katu haitatokea wakatengana na wataendelea kumsaidia Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan.

“Katika hali kama hii haiwezi kutokea na haitatokea na si rahisi jambo kama hili kutokea peke yake hataweza, tumsaidie kwa sababu kwa pamoja ndio tutaweza.Mtawasikia Wabunge wapo na Rais na sisi wote tunatekeleza sera ya ilani ya CCM hatugombani hata siku moja hao washindwe na walegee,”amesema.

Pia,amesema nchi nzima inafurahia kwa jinsi mpango wa fedha za Uviko 19 zilivyotumika ambapo ametoa wito matumizi ya fedha hizo yaendelee kutumika hivyo hivyo kwani itakuwa ni faida kwa nchi.

“Mfano kwangu Kongwa nimefuatilia kila chumba cha madarasa kinachojengwa hakuna jengo zuri kama majengo hayo.Tumepiga tiles madarasa yetu yote,tumejenga vyumba 150 wastani wa bilioni 3 Kongwa,makusanyo yetu halmashauri ya Kongwa ni bilioni 3.

“Nitakuwa mtu wa kubeba dhambi kubwa sana kwa mafanikio makubwa haya kumpinga Rais,tusimvunje moyo Rais wetu mtamsikia kila mbunge na fedha hizi ziliidhinishwa,”amesema.

Spika Ndugai ameyasema hayo kufuatia kauli yake aliyoitoa tarehe 26 mwezi Desemba mwaka 2021 kuzua mijadala katika mitandao ya kijamii na baadhi ya vyombo vya habari hapa nchini, huku yeye akishutumiwa na baadhi ya watu kuwa anaenda kinyume na mipango ya Serikali.
Share:

Sunday 2 January 2022

MWILI WA MWANASHERIA MKUU WA KWANZA KENYA WACHOMWA MOTO SAA 3 BAADA YA KUFARIKI...HAKUWAHI KULA UGALI UTOTONI


Mwanasheria mkuu wa kwanza wa Kenya bwana Charles Njonjo amefariki dunia akiwa na miaka 101.

Rais Uhuru Kenyatta ametangaza leo Jumapili, Januari 2,2022 taarifa ya kifo cha mwanasiasa huyo mkongwe Charles Mugane Njonjo.


"Ni kwa masikitiko makubwa kwamba asubuhi ya leo, Jumapili tarehe 2 Januari 2022, nimepokea taarifa za kuhuzunisha na za kufariki kwa Charles Mugane Njonjo," Rais Kenyatta amenukuliwa na magazeti ya Kenya.


Taarifa kutoka kwa familia zinasema, maiti ya aliyekuwa Mwanasheria Mkuu Charles Njonjo tayari imechomwa katika mji wa Kariokor jijini Nairobi.

Familia na marafiki wa marehemu Charles Njonjo walikusanyika kwenye Tanuru ya Kihindi eneo la Kariakor jijini Nairobi.


Mwanasheria huyo mkuu wa zamani aliyehudumu baada ya Kenya kujinyakulia uhuru wake, aliaga kwa amani nyumbani kwake Muthaiga, saa kumi na moja asubuhi Jumapili Januari 2,2022.

 Kulingana na mkaza mwanawe Carey Ngini, mwili wa mwendazake ulianza kuchomwa saa nne kamili siku hiyo hiyo, kulingana na mapenzi yake na kuongeza kusema kwamba alikuwa mtu aliyeweka masharti yake wazi.

"Alikuwa wazi kuhusu kile alichotaka maishani na kile alichotaka hata baada ya kufariki dunia. Sehemu ya masharti hayo ni kuchomwa mara tu atakapoaga dunia. Hakutaka mbwembwe wala sherehe nyingi zinzoandaliwa wakati mtu mwenye staha kama yake hufanyiwa. Kama familia yake tumeheshimu uamuzi na masharti yake," aliwaambia wanahabari.

Njonjo, alikuwa mjumbe pekee aliyebaki katika Baraza la Mawaziri la uhuru wa Kenya.


Kufariki kwa Mhe. Njonjo ni pigo kubwa sio tu kwa familia yake bali kwa Wakenya wote na kwa hakika, bara zima la Afrika kwa sababu ya jukumu lake kuu katika kuanzishwa kwa taifa la Kenya wakati wa uhuru," Rais alisema.


Charles Njonjo ni nani?


Charles Njonjo alizaliwa na kukulia katika familia ya viongozi huku akiwa mtoto wa chifu wa ukoloni Josiah Njonjo maisha ambayo yalikuwa ndoto kwa watoto wengine wa Kiambu kuishi wakati wa ukoloni. 

Alizaliwa Januari 23, 1920, Njonjo alijiunga na shule za kifahari kanda ya Afrika Mashariki pamoja na kaka yake James.


Mwaka 1939, alijiunga na King's College Budo, na kisha baadaye alijiunga na Shule ya Upili ya Wavulana ya Alliance. Inaripotiwa kwamba alikula ugali mara yake ya kwanza maishani alipojiunga na Shule ya Upili ya Wavulana ya Alliance akidhihirisha namna aliishi maisha ya kifahari.

Baada ya elimu yake ya sekondari, alijiunga na Chuo Kikuu cha Fort Hare nchini Afrika Kusini na kusomea Shahada ya Kingereza na Sheria ya Afrika Kusini.


Akiwa mwingi wa maono, Njonjo alikuwa na hamu ya kusomea sheria ya Kenya lakini Waafrika hawakuwa wanaruhusiwa kusomea sheria wakati wa ukoloni.

Baada ya kufuzu katika masomo yake Afrika Kusini, Njonjo alikabidhiwa udhamini na serikali ya kikoloni kusomea Utawala wa Umma katika Chuo Kikuu cha Kusini Magharibi mwa Uingereza huko Exeter. 

Ni wakati alipokuwa nchini Uingereza, ndipo alikumbatia utamaduni wa Waingereza na kubandikwa jina "Duke of Kabeteshire" kutokana na upendo wake kwa maisha ya Ulaya.


Akiwa Uingereza, pia alisomea sheria na kurejea Kenya mwaka 1954. Aliteuliwa kuwa Mwanasheria Mkuu wa kwanza mwaka 1963 wakati Kenya ilipata uhuru chini ya utawala wa hayati Jomo Kenyatta.

Taaluma yake kisiasa Baada ya kutimia umri wa miaka 60, alistaafu kama Mwanasheria Mkuu na kujitosa kwenye nyanja ya kisiasa.
Alichaguliwa, bila kupingwa kama Mbunge wa Kikuyu mwaka 1980, baada ya mbunge aliyekuwepo Amos Ng'ang'a kujiuzulu.

Kulingana na mwandishi Charles Hornsby, wa kitabu Kenya: A History Since Independence, Ng’ang’a alilipwa KSh 160,000 pesa taslimu kama fidia ya kujiuzulu kwake ili kumupa Njonjo nafasi.


Baada ya kuchaguliwa kuwa Mbunge, Rais wa pili marehemu Daniel Moi alimteua Njonjo kushikilia wadhifa wa Waziri wa Masuala ya Kikatiba. Hata hivyo, alipoteza cheo mwaka 1982, kwa tuhuma za kuhusika katika jaribio la mapinduzi ya serikali ili amnyanganye Moi mamlaka. Japo aliishi maisha ya kimya, wakati mmoja alidokeza kurejea kwenye siasa baada ya kutangaza hadharani kuunga mkono azma ya Raila Odinga kuwania urais.


Aoa akiwa na miaka 52 Njonjo alioa mwanamke Muingereza, Margaret Bryson mwaka 1972. Hadithi hiyo iliyosimuliwa na Duncan Ndegwa, mkuu wa kwanza wa utumishi wa umma nchini Kenya, katika wasifu kuhusu jinsi Jomo Kenyatta alivyoingiwa na wasiwasi kwamba mshauri wake bado alikuwa na umri wa miaka 50.
Hii ni licha ya kuwepo na wanawake Wakenya ambao walikuwa wanmumeea mate Duke of Kabeteshire, ikidaiwa kwamba Mkuu wa Manesi Kenya, Margaret Wanjiku Koinange alikuwa amezama katika penzi la Njonjo.
Lakini Njonjo hakuzinguliwa naye kimapenzi kwani hakuwa na mpango wa kumuoa mwanamke Mwafrika na kuvunja uhusiano wake na Koinange. Hivyo alimuoa Margaret mwaka 1972 na kujaliwa watoto watatu pamoja na wajukuu. Njonjo aliaga dunia akiwa na umri wa miaka 101, wiki chache kabla ya bathdei yake ya 102.


Charles Mugane Njonjo alikuwa Mwanasheria Mkuu wa kwanza mzaliwa wa Kenya kati ya 1963 na 1979.


Alistaafu kama mwanasheria mkuu akiwa na umri wa miaka 60.


Baadaye Njonjo alichaguliwa bila kupingwa katika Bunge la Kitaifa Aprili 1980 kama Mbunge wa Jimbo la Kikuyu.


Aliyekuwa rais Hayati Daniel Moi alimteua katika Baraza la Mawaziri mnamo Juni 1980 kuhudumu kama Waziri wa masuala ya ndani na Kikatiba.

Share:

Waziri Mkuu Avutiwa Kasi Ya Utekelezaji Miradi Ya Maendeleo


WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewapongeza Wakuu wote wa Mikoa na Wakuu wote wa Wilaya nchini kwa kazi nzuri waliyofanya ya kusimamia miradi ya maendeleo na hasa ujenzi wa madarasa.

“Kupitia kwako Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa na Wakuu wa Wilaya waliopo hapa, nitoe pongezi kwa Wakuu wengine wa Mikoa na Wilaya kwa kazi nzuri ya kusimamia miradi ya maendeleo. Hii ni pamoja na usimamizi wa fedha, uratibu wa matumizi ya fedha hizo na usimamizi wa kuhakikisha miradi inakuwa ya viwango,” amesema.

Ametoa pongezi hizo leo mchana (Jumapili, Januari 02, 2022) wakati akizungumza na viongozi wa Chama na Serikali wa mkoa wa Ruvuma kwenye uwanja wa ndege wa Ruhuwiko, wilayani Songea mara baada ya kupokea taarifa ya mkoa huo.

Waziri Mkuu amesema amefanya ziara kwenye mikoa ya Mbeya, Lindi, Dodoma, Dar es Salaam na sasa yuko Ruvuma na amejionea kazi nzuri iliyofanyika. Amesema ifikapo Januari 5, usafi ufanyike kwenye madarasa yaliyojengwa ili yakabidhiwe kwa Wakuu wa Shule.

“Ari ya usimamizi wa ujenzi iliyooneshwa katika miradi hii, ikifanyika kwenye miradi mingine yote, ni lazima nchi hii itafika mbali. Tunatambua katika miradi mikubwa kama hii hapakosi changamoto, lakini kuna wengine ambao wamefanya kazi nzuri hadi kubakiza fedha.”

Amewataka wasimamie miradi iliyosalia ya afya, maji na ujenzi wa barabara (TARURA) kwa mtindo huohuo. Ametumia fursa hiyo kumwahidi Mwenyekiti wa CCM wa mkoa huo, Bw. Oddo Mwisho kwa niaba ya wenzake, kwamba Serikali itasimamia vizuri miradi mingine kama ilivyosimamia miradi hii ya maendeleo.

Wakati huohuo, Waziri Mkuu amesema siyo sahihi kuiita miradi inayotekelezwa hivi sasa kuwa ni ya UVIKO 19 bali ni miradi ya Maendeleo ya Kitaifa ambayo inatokana na utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM.

“Hii miradi ni ya maendeleo ya Kitaifa lakini imetokana na Ilani ya Uchaguzi ya CCM ambayo ilielekeza madarasa yajengwe kwa haraka ili kukabiliana na uhaba wa madarasa wa kila mwaka. Kupatikana kwa hizi fedha za mkopo wenye masharti nafuu ni ubunifu wa Mheshimiwa Rais wetu ili ziweze kukamilisha na miradi mingine kwenye elimu, afya, maji na barabara za vijijini.”

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amewataka Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya nchini wawahimize wananchi kwenye maeneo yao watunze akiba ya chakula walichonacho na wapunguze kukiuza.

“Wakuu wa Mikoa na Wilaya kaeni na wananchi na kuwasisitiza wahifadhi chakula na wapunguze kuuza ili kujiwekea akiba. Kama kuna mbegu za muda mfupi ni vema wahimizwe kuzitumia ili waweze kuzalisha chakula kingine ndani ya muda mfupi. Tuendelee kuwatia moyo wananchi wetu, tushirikiane pia na viongozi wa dini ili tumuombe Mungu atushushie mvua za kutusaidia tupate mazao,” amesema.

Ili kurejesha uoto wa asili ndani ya miaka mitatu hadi minne ijayo, amewataka wawahimize wananchi kupanda miti pindi mvua zikianza. “Tukirejesha misitu midogo midogo, hali ya unyevu na uchepechepe itarejea haraka. Tunapaswa pia kukemea tabia ya kukata miti hovyo,” amesisitiza.

“Tumeanza kushuhudia ukame uliopitiliza kwenye mikoa hii ya Kusini. Kwa kawaida mikoa ya Kusini na Nyanda za Juu Kusini imekuwa ikitumika kutoa akiba ya chakula kwa mikoa mingine, kwa hiyo tunapaswa tukabiliane na mabadiliko ya tabianchi kwa kuwahamasisha wananchi wapande miti kila mahali.”

Mapema, Mkuu wa Mkoa huo, Brig. Jenerali (Balozi) Wilbert Ibuge alimweleza Waziri Mkuu kuwa mkoa huo ulipokea sh. bilioni 10.24 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa 500 na mabweni matatu kwa ajili ya shule zenye mahitaji maalum.

“Kwa sasa, ujenzi wa madarasa yote 500 umekamilika kwa asilimia 100 na ujenzi wa mabweni haya matatu unaendelea vizuri isipokuwa wamefikia hatua ya maboma. Tunaahidi kuwa yatakamilika kabla shule hazijafunguliwa,” alisema.

Alisema kwenye sekta ya afya, walipokea sh. bilioni 22.75 kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya kwenye tarafa 11 ambazo hazikuwa na vituo vya afya kabisa.


Share:

Wazimamoto Afrika Kusini wadhibiti moto uliounguza majengo ya Bunge


Ripoti kutoka Afrika Kusini zinasema kuwa kikosi cha zimamoto kimefanikiwa kudhibiti kwa kiasi fulani moto mkubwa uliokuwa ukiunguza jengo la Bunge la nchi hiyo jijini Cape Town.

Kwa mujibu wa vyombo vya habari vya kimataifa, moto huo ulianza lalfajiri ya leo Jumapili Januari 2, 2022.

Kikosi cha zimamoto kilikuwa bado kinaendelea kupambana na moto huo ambao chanzo chake bado hakijajulikana.

Hadi asubuhi ya leo, moshi ulikuwa bado ukifuka kutoka kwenye moja ya majengo kadhaa ya Bunge katika mji wa Cape Town.

Waziri wa Kazi za Umma na Miundombinu Patricia De Lille amewaambia waandishi wa habari kwamba hakuna ripoti za majeraha yoyote.

Vilevile Jean-Pierre Smith, mjumbe wa kamati ya Meya wa Cape Town inayohusika na ulinzi na usalama, amewaambia waandishi wa habari kuwa wazima moto wamegundua nyufa kwenye ukuta na paa moja lililoporomoka
.

Share:

CHUO CHA ARDHI MOROGORO KURASIMISHA MAKAZI 35,000 MBALIZI

Wataalamu kutoka chuo cha Ardhi Morogoro (ARIMO) wakiwa katika matayarisho ya awali ya kazi ya urasimishaji makazi holela katika mji mdogo wa Mbalizi mkoani Mbeya mwishoni mwa wiki.

Mkuu wa Cho cha Ardhi Morogoro (ARIMO) Huruma Lugalla (Kushoto) akipata maelezo kutoka kwa mmoja wa wataalam wakati wa maandalizi ya awali ya urasimishaji makazi holela kwenye mji mdogo wa Mbalizi mkoani Mbeya mwishoni mwa wiki.

Mkuu wa Chuo cha Ardhi Morogoro (ARIMO) Huruma Lugalla (wa pili kulia) akikagua sehemu ya vigingi vitakavyotumika kwenye zoezi la urasimishaji makazi holela katika mji mdogo wa Mbalizi mkoani Mbeya mwishoni mwa wiki.

Mkuu wa Cho cha Ardhi Morogoro (ARIMO) Huruma Lugalla (wa pili kulia) akitoa maelekezo wakati wa kutafuta alama eneo la Lumbila kata ya Luanda wilaya ya mbozi mkoani Mbeya kabla ya kuanza zoezi la urasimishaji makazi kwenye mji mdogo wa Mbalizi mwishoni mwa wiki. (PICHA ZOTE NA MUNIR SHEMWETA WIZARA YA ARDHI)

******************

Na Munir Shemweta, WANMM MBEYA

Chuo cha Ardhi Morogoro (ARIMO) kinatarajiwa kuanza kazi ya kurasimisha makazi holela katika mji mdogo wa Mbalizi mkoani Mbeya.

Kazi hiyo ni utekelezaji wa program ya Kupanga, Kupima na kumilikisha ardhi ambapo Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan iliipatia Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi shilingi bilioni 50 kwa ajili ya kuzikopesha halmashauri 55 nchini.

Akizungumza jijini Mbeya mwishoni mwa wiki, Mkuu wa Chuo cha Ardhi Morogoro Huruma Lugalla alisema kiasi cha shilingi bilioni 1.2 zitatumika kwenye kazi hiyo na malengo ya chuo chake ni kukamalisha kazi hiyo kufikia katikati ya mwezi April 2022.

‘’Malengo yetu kazi hii ikamilike katikati ya mwezi April 2022 kwa kukamilisha kupanga na kupima viwanja vyote 35000 pengine nusu ya ya viwanja hivyo viwe vimefanyiwa utaratibu wa kumilikishwa’ alisema Lugalla.

Kwa mujibu wa Mkuu huyo wa Chuo cha Ardhi Morogoro, iwapo kazi hiyo itakamilika kwa wakati watakuwa wameisadia serikali na wananchi wa Mbalizi kupata maeneo yaliyopangwa na kupimwa sambamba na kuwa na umiliki wa uhakika.

Lugalla aliongeza kuwa, mikakati ya chuo chake cha ARIMO ni kukamilisha miradi yake yote ya urasimishaji kwa wakati sambamba na kuwasaidia wananchi kupata hati ili wazitumie kwa shughuli za maendeleo huku serikali nayo ikipata mapato kupitia kodi ya pango la ardhi.

‘’Pamoja na kazi ya hapa Mbalizi lakini tumefanya kazi pia katika jiji la Arusha kata ya Muriet ambako tumepima viwanja 20,222 na pia tumefanya Dar es Salaam kata ya Kivule tulikopima viwanja 30140 na zoezi linaloendelea ni kupata uidhinishaji kwa baadhi ya viwanja kutoka ofisi ya ardhi mkoa’’ alisema Lugala

Kwa upande wake Mratibu wa mradi huo wa Urasimishaji Makazi Holela eneo la Mbalizi Manyama Majogolo alisema, tayari timu ya wataalam tayari imefika Mbalizi mkoani Mbeya kwa matayarisho ya awali kabla ya kuanza rasmi kazi katika eneo la mji mdogo wa Mbalizi.

‘’Kazi hizi za awali zikikamilika tunatarajia kuingia uwandani Januari 10, 2022 na kwa hivi sasa pamoja na maandalizi mengine pia tumeanza kuandaa vigingi na timu imesambaa kila eneo kuhakikisha tunaratibu vizuri maana nina imani tukianza vizuri tutamaliza vizuri ‘’ alisema Majogolo

Akielezea namna walivyojipanga kuhakikisha zoezi linakuwa na mafanikio, Majogolo alisema kuwa, wameanza kwa kuhamasisha wananchi kushiriki katika mradi huo ambapo katika uhamasishaji huo wameshirikisha pia viongozi wa serikali za mitaa, kata, mabalozi na ofsi ya halmashauri ili elimu iweze kuwafikia wananchi kwa ujumla wake.
Share:

AFARIKI BAADA YA KUNYWA CHANJO TABORA

Picha ya mfano wa bomba la sindano
 *****
Mtoto mmoja  mkazi wa Imalamakoye wilaya ya Urambo mkoani Tabora amefariki dunia baada ya kunywa chanjo ya ng'ombe huku mtoto mwingine akiwa katika hali mbaya kwa kunywa chanjo hiyo.

Mwenyekiti wa kitongoji cha Imalamakoye D Michael Philipo amesema watoto hao wa familia moja katika kitongoji chake waliokota chupa ya sindano za ng'ombe wakidhani kuwa ni dawa ya kifua ambapo mtoto mkubwa anayesoma darasa la pili mwenye umri wa miaka 7 alimnywesha mdogo wake aliyekuwa na kikohozi hali iliyopelekea kifo chake.


 Chanzo- CG FM Radio
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMAPILI JANUARI 2,2022









 



Share:

Saturday 1 January 2022

SIMBA SC YAFUNGUA MWAKA MPYA 2022 KIBABE... YAIBAMIZA AZAM FC MABAO 2-1

Beki wa kulia wa Azam Fc Nicolas Wadada akijaribu kumtoroka kiungo mkabaji Raia wa Mali, Sadio Kanoute aliyefunga bao la kwanza katika mchezo wa Ligi kuu ya NBC Simba imeibuka na ushindi wa mabao 2-1.

************************

Na.Alex Sonna,Dar es Salaam

Mabingwa watetezi Simba wameanza vyema mwaka mpya kwa kusepa na pointi tatu dhidi ya matajiri wa Chamazi timu ya Azam FC baada ya kupata ushindi wa mabao 2-1 katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC uliopigwa uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam.

Mnamo dakika ya 13 Simba walikosa Mkwaju wa Penalti iliyochezwa na Rally Bwalya baada ya Frank Domayo kumchezea rafu ndani ya 18 winga Pape Sakho Penalti iliyondakwa na golikipa wa Azam Ahmed Salula.

Baada ya kukosa Penalti Simba waliendelea kulisakama lango la Azam FC kama nyuki mpaka zinaenda mapumziko hakuna timu iliyokuwa inamtambia mwenzie.

Kipindi cha pili kilianza kwa kila timu kufanya mabadiliko mnamo dakika ya 67 kiungo Mkabaji Raia wa Mali, Sadio Kanoute alifunga bao la kwanza kwa kichwa na kuwanyanyua mashabiki wa Simba waliojitokeza katika uwanja wa Mkapa.

Licha ya kupata bao Simba waliendelea kulisakama lango la Azam na mnamo dakika ya 72 winga hatari kutoka Senegal Pape Sakho alipigilia msumari wa pili kwa bao safi la shuti kali lililomshinda mlinda mlango Salula.

Azam FC walipata bao la kufutia machozi kupitia kwa mshambuliaji wao raia wa Zambia Rodgers Kola,akimalizia pasi ya Tepsi Evance.

Hadi mwamuzi Herry Sasii akipuliza kipyenga cha mwisho Simba wameibuka na ushindi wa mabao 2-1 na kuondoka na Pointi 3 na kuendelea kuifukuzia Yanga kileleni Mwa Msimamo.

Kwa ushindi huo Simba wamefikisha Pointi 24 wakiwa nafasi ya pili wakiwa wamecheza mechi 10,Azam FC wanabaki nafasi ya tano kwa Pointi 15 huku Nafasi ya kwanza ikiendelea kushikiliwa na Yanga wenye pointi 29 wakiwa wamecheza mechi 11.

Simba na Azam FC wataelekea visiwani Zanzibar kushiriki Michuano ya Kombe la Mapinduzi linalotarajia kuanza kesho kwa mechi moja ya ufunguzi itakayowakutanisha Namungo FC.
Share:

Tanzia : DIWANI WA KATA YA MWAMALILI PAUL MACHELA AFARIKI DUNIA


Paul Machela  enzi za uhai wake

**
Diwani wa Kata ya Mwamalili Manispaa ya Shinyanga Paul Machela (CCM) amefariki dunia leo Januari 1,2021 wakati akiendelea kupatiwa matibabu katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga kutokana na maradhi yaliyokuwa yanamsumbua.

Mstahiki Meya wa Manispaa ya Shinyanga Mhe. Elias Ramadhani Masumbuko amesema Paul Machela amefariki dunia leo majira ya saa 11 alfajiri wakati akiendelea kupatiwa matibabu katika hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga kutokana na maradhi yaliyokuwa yanamsumbua kwa zaidi ya wiki moja.

“Nimepokea kwa masikitiko taarifa za kifo cha diwani mwenzetu Paul Machela.Ameacha pengo kubwa kwani alikuwa na mchango mkubwa katika mipango ya maendeleo ya Manispaa ya Shinyanga. Alikuwa mshiriki mkubwa katika mipango mikubwa tuliyokuwa tumejiwekea katika Manispaa ya Shinyanga”,amesema Masumbuko.

“Mpendwa wetu Paul Machela alikuwa anaendelea kupatiwa matibabu katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga kwa zaidi ya wiki moja kutokana na ugonjwa wa Kifua Kikuu na Moyo kuzungukwa maji.Desemba 29,2021 hali yake ilibadilika akapelekwa katika chumba maalumu cha uangalizi (ICU),taarifa za madaktari jana usiku alikuwa anaendelea vizuri lakini saa 11 alfajiri hali ilibadilika akafariki dunia. Mwenyezi Mungu ailaze mahali pema peponi roho ya marehemu Paul Machela. Amina.”,amesema.

Paul Machela amekuwa diwani wa kata ya Mwamalili kwa zaidi ya miaka 15. 

Share:

Hotuba ya Rais Samia ya kuuaga mwaka 2021, kuukaribisha 2022


RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan  Ijumaa tarehe 31 Desemba 2021, ametoa hotuba ya kuufunga mwaka 2021 na kuukaribisha mwaka mpya 2022.

Rais Samia amezungumzia changamoto zilizotokea mwaka huu, mafanikio na kile ambacho Serikali anayoiongoza itakwenda kukifanya ikiwemo kuboresha maisha ya wananchi.

==>>Hii hapa ndiyo hotuba yote ya Rais Samia


Ndugu Wananchi na Watanzania wenzangu;
Nawasalimu kwa jina la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Kwanza kabisa hatuna budi kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa Rehema na Huruma, kwa kutujaalia uhai na afya, na kutuwezesha kuumaliza Mwaka 2021 kwa amani na kuushuhudia Mwaka Mpya wa 2022 ukiingia. Wapo wapendwa wetu wengi ambao tungelipenda kuwa nao katika kipindi hiki cha furaha, lakini hatupo nao. Tuwaombee wapendwa wetu hawa Mungu aendelee kuwalaza mahali pema peponi. Amina.

Kwa wale ambao tumeendelea kubarikiwa tunu hii ya uhai basi hatuna budi kumshukuru Mwenyezi Mungu. Ni wazi kuwa katika kipindi hiki cha sikukuu za mwisho wa mwaka wengi wetu hupenda kutumia muda huu kufanya tathmini ya malengo yetu tuliyojipangia katika kipindi cha mwaka wa kalenda uliopita, ikiwa ni pamoja na kusherehekea mafanikio tuliyoyapata. Hivyo, ni katika msingi huo, nimeona ni vyema nami nikaongea nanyi ili kwa pamoja tuweze kufanya mapitio ya mwaka 2021 na kutathmini milima na mabonde tuliyopitia kama Nchi na Taifa, katika mwaka huo.
Ndugu Wananchi na Watanzania wenzangu;
Safari yetu ya Mwaka 2021 haikuwa tambarare; ilikuwa na milima na mabonde, furaha na majonzi, na mafanikio na vikwazo kadhaa. Huu ni mwenendo wa Maisha, huwezi kupata na kufurahia mafanikio bila kukutana na vikwazo vya hapa na pale. Msemo huu ulisadifu safari yetu ya 2021 kama Taifa. Pamoja na kupiga hatua kimaendeleo katika maeneo mbalimbali, tulikumbana pia na vikwazo na vipindi vya majonzi.

Mwaka 2021 Taifa letu lilipitia katika kipindi kigumu kwa kumpoteza Kiongozi Mkuu wa Nchi, mpendwa wetu Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, wakati akiwa madarakani; na aliyekuwa Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad. Hakika ilikuwa ni misiba mikubwa kwa Taifa na Bara la Afrika kwa ujumla. Tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwamba tuliweza kuwapumzisha wazee wetu hawa kwa amani. Tuendelee kumuomba Mwenyezi Mungu aendelee kuwalaza mahali pema peponi. Amina.

Mwaka 2021, tuliendelea kukabiliana na janga la UVIKO – 19, ambalo linaendelea kuisumbua dunia hadi hii leo. Janga hili lilisababisha kuzorota kwa kasi ya ukuaji wa uchumi, kutoka ukuaji wa asilimia 7 mwaka 2019/2020 hadi asilimia 4.8 mwaka 2020/2021. Kupungua kwa kasi ya ukuaji uchumi kulitokana na mambo mawili makubwa. La kwanza, ni athari za kufungwa mipaka, kusitishwa safari za ndege za kimataifa na kusitishwa baadhi ya shughuli za uzalishaji na kiuchumi. Hatua hizi zilichukuliwa na mataifa ambayo kati yao, ni washirika wakubwa wa biashara na Tanzania, kwa lengo la kukabiliana na janga la UVIKO – 19. La pili, ni mvua zilizozidi wastani ambazo zilisababisha uharibifu wa miundombinu ya usafirishaji nchini na kuchelewesha utekelezaji wa baadhi ya miradi.

Aidha, kuelekea mwishoni mwa mwaka 2021, tulishuhudia mfumuko wa bei uliofikia asilimia 4.1, kiwango ambacho kipo ndani ya malengo ya Taifa ambacho ni asilimia 3hadi 5. Mfumuko huo wa bei ulisababishwa na kupanda kwa bei ya mafuta duniani; na mlipuko wa UVIKO-19 ambapo viwanda vingi vilisimamisha uzalishaji na hivyo kusababisha uhaba na ongezeko kubwa la uhitaji wa bidhaa. Kwa hapa nchini mfumuko huo wa bei ulichagizwa zaidi na utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano dhidi ya UVIKO-19 uliotoa kiasi cha Shilingi trilioni 1.3, kwa ajili ya ujenzi wa miundo mbinu ya afya, elimu, maji safi na salama ambao ulisababisha upandaji wa bei za vifaa vya ujenzi kama Saruji, Nondo, Mabati.

Ndugu Wananchi na Watanzania Wenzangu;
Pamoja na vikwazo nilivyovitaja hapo juu ambavyo tulikumbana navyo katika Mwaka wa 2021, Watanzania tulipata mafanikio katika nyanja mbali mbali. Miongoni mwa maeneo ambayo tunapaswa kujivunia na ambayo nimeona ni muhimu niyataje ni pamoja na; kuweza kudumisha amani na utulivu wa nchi yetu; kulikoendana na kuendeleza umoja, mshikamano na upendo miongoni mwetu. Mtakumbuka kwamba kwenye hotuba yangu ya kwanza niliyoitoa baada ya kuapishwa, niliwaomba na kuwasihi sana Watanzania, tuwe watulivu, na tudumishe umoja na mshikamano. Nitumie fursa hii kuwashukuru sana Watanzania kwa kudumisha Amani na Utulivu nchini na hatimaye, Taifa letu likibaki kuwa salama na imara.

Eneo jingine ambalo tuliweza kupata mafanikio katika Mwaka 2021 ni kuwa, pamoja na athari za UVIKO-19 tulikuwa na ukuaji chanya wa uchumi, tukiwa ni miongoni mwa nchi 11 zilizokuwa kiuchumi kati ya nchi 54 za Afrika. Hali hii ilisababishwa na kuruhusu wananchi kuendelea na shughuli zao za uzalishaji kiuchumi badala ya hatua za kuwafungia kama ilivyokuwa kwa nchi nyengine.

Aidha, katika kuhakikisha uchumi haupati athari hasi, tulichukua hatua za kudhibiti Mfumuko wa bei, ambapo umeendelea kuwa kati ya asilimia 3 hadi 5; na kuhakikisha kwamba tunakuwa na akiba ya kutosheleza ya fedha za kigeni ambapo kwa sasa nchi yetu ina kiwango cha kiasi cha Dola za Kimarekani bilioni 6,253 zitakazotosheleza kuagiza chakula na huduma kwa kipindi cha miezi 7.

Vilevile, katika kuvutia uwekezaji na kurudisha fedha kwenye mzunguko, tulifanya marekebisho mbalimbali ya Kisera, kisheria, kikodi na kiutendaji. Matokeo yake tumeweza kuvutia uwekezaji kutoka miradi 186 yenye thamani ya Dola za Kimarekani bilioni 1.013 mwaka 2020 hadi miradi 237 yenye thamani ya Dola za Kimarekani bilioni 4.144 mwaka 2021.

Ndugu Wananchi;
Kwa upande wa kilimo, tulifanikiwa kuiongezea uwezo Benki ya Maendeleo ya Kilimo (TADB) kwa kuipatia mtaji wa Shilingi bilioni 208 ili iweze kuwafikia wakulima zaidi na kufanya kazi kwa ufanisi. Aidha, tuliweza kuondoa vikwazo vya biashara vilivyokuwepo na kuanzisha masoko na kufungua vituo vya kuuza mazao katika nchi za Kenya, Sudan Kusini, China, India, Ukraine, Umoja wa Ulaya, nchi za ukanda wa SADC na Saudi Arabia. Vilevile, Serikali iliziwezesha Ghala la Taifa la Chakula (NFRA) na Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko (CBP) kununua tani 950,000 za mahindi zilizokuwa mikononi mwa wakulima.

Pamoja na mafanikio hayo katika sekta ya Kilimo, tunatambua uwepo wa changamoto ya upungufu wa mbolea, ambayo kwa kiasi kikubwa imesababishwa na kushuka kwa uzalishaji wa bidhaa hiyo duniani kwa sababu ya UVIKO-19. Lakini habari njema ni kwamba, mapema mwakani 2022 tunatarajia kupata mbolea ya kukuzia mazao itakayouzwa kwa bei ambayo wakulima wameizoea. Pamoja na jitihada hizo, Kampuni ya ITRACOM Fertilizers Ltd, inajenga kiwanda kikubwa cha mbolea Jijini Dodoma, ambacho kitazalisha tani 500,000 sawa na takriban asilimia 70 ya mahitaji yetu kwa mwaka. Aidha, Kampuni ya Dangote nayo imeonesha nia ya kuanzisha Kiwanda cha Mbolea ya UREA kule Mtwara.

Ndugu Wananchi;
Sekta ya Utalii nayo iliathiriwa sana na UVIKO-19, hatua mbalimbali za kuinusuru sekta hii kutodidimia zilichukuliwa na kuhakikisha sekta inarudi kwenye nafasi yake ya kuchangia uchumi wetu. Hadi mwezi Desemba mwaka huu 2021, sekta hii imeweza kujikongoja na kuingiza nchini Watalii 1,400,000 ikilinganishwa na watalii 620,867 kwa kipindi cha mwaka 2020, sawa na ongezeko la watalii 779,133. Matarajio yetu ni kushuhudia kukua zaidi kwa sekta hii kuanzia msimu wa 2022, na kuendelea.

Aidha, mwaka 2021 tuliendelea na utekelezaji wa miradi yetu mikubwa ya kimkakati, ikiwemo mradi wa ufuaji umeme wa Nyerere kule Rufiji; upanuzi wa bandari ya Dar es Salaam; ujenzi wa daraja la Kigongo – Busisi kule Mwanza, daraja la Tanzanite Dar es Salaam; upanuzi wa barabara za viwanja vya ndege yaani Run ways, na Barabara kadhaa zinazounganisha Mikoa na Wilaya ya nchi yetu. Lakini vilevile ujenzi wa reli ya kisasa ya SGR, ambapo tarehe 28 mwezi huu tumesaini mkataba wa ujenzi wa kipande cha tatu cha kutoka Makutupora hadi Tabora chenye kilometa 368.Pia, tumefanikiwa kuongeza ndege nyingine tatu (03), ambazo ni Dash 8 Q-400 ndege moja na Airbus 200dege mbili, na kulifanya Shirika letu la ATCL kuwa na ndege 12.

Vile vile, tumeendelea na ujenzi wa Makao Makuu ya Nchi yetu Dodoma, ambao unahusisha ujenzi wa Ikulu ya Chamwino uliokamilika kwa asilimia 90, na tumeanza awamu ya pili ya ujenzi wa Mji wa Serikali pale Mtumba. Kwa ujumla Makao Makuu Dodoma yanaendelea kujengwa na Serikali na Sekta binafsi kwa kasi ya kuridhisha.

Halikadhalika, katika kuhakikisha kwamba kunakuwa na mazingira mazuri ya kisiasa, Baraza la vyama vya Siasa Tanzania limekutana na wadau mbalimbali wa siasa na demokrasia na kujadili kwa pamoja mustakabali na namna bora ya uendeshaji wa siasa za vyama vingi nchini kwetu. Matumaini yangu ni kwamba kikosi kazi kilichoundwa na Msajili wa Vyama vya Siasa, kitafanyia kazi maazimio ya mkutano huo kwa weledi. Serikali itapokea mapendekezo yatakayoletwa na tuone hatua za kuchukua ili tuweze kusonga mbele kwa pamoja, kama Taifa.

Ndugu Wananchi;
Kwenye Uhusiano wa Kimataifa tumeweza kuifungua nchi yetu kwenye uwanda mpana wa ushirikiano na uhusiano, na kutuwezesha kuimarisha sauti yetu na ushawishi wetu kimataifa.

Aidha, mwaka 2021 Nchi yetu ilipata heshima kwa Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu na Sayansi (UNESCO) kuitangaza tarehe 7 Julai ya kila mwaka kuwa Siku ya Kiswahili Duniani. Hii ni hatua nzuri ya kufikia lengo la kukifanya Kiswahili kuwa miongoni mwa lugha zitakazotumika na Umoja wa Mataifa.

Kwa upande wa Sanaa, Michezo na Utamaduni, tunajivunia vijana wetu wa Tembo Warriors kwa kufuzu kushiriki katika Kombe la Dunia la mpira wa miguu kwa watu wenye ulemavu litakalofanyika mwezi Oktoba mwakani 2022 kule nchini Uturuki. Vile vile Timu ya mpira wa miguu ya wanawake chini ya miaka 20 (Tanzanite) tunawapongeza kwa kubakiza hatua moja ya kushiriki kombe la Dunia kule nchini Costa Rica na Mungu awasaidie wapate sifa ya kwenda huko; na Warembo na watanashati wetu viziwi ambao watashiriki mashindano ya Dunia kule Brazil nao pia tunawapongeza. Haya ni mafanikio makubwa kwetu katika medani ya michezo. Ni fakhari kwetu pia kuona vijana wetu wa tasnia ya muziki wameweza kushiriki na kupata tuzo mbalimbali katika ngazi za kimataifa. Kwa ujumla tumeshuhudia ukuaji katika sekta ya Sanaa, Utamaduni na Michezo.

Ndugu Wananchi;
Baada ya kuelezea kwa uchache changamoto na mafanikio yetu kwa mwaka 2021, sasa nizungumzie kwa kifupi masuala mtambuka wakati tukiuelekea Mwaka 2022. Serikali inautizama mwaka 2022 kuwa ni mwaka wa kukabiliana na changamoto zinazopunguza uwezo wa Wananchi katika kukabiliana na Maisha ya kila siku. Kama ilivyotamkwa kwenye Mpango wa Tatu wa Serikali wa Miaka Mitano wa 2021/2026, kwamba lengo kuu ni kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na uchumi wa Taifa kwa ujumla.

Aidha, kama nilivyosema hapo awali, dunia bado inakabiliwa na UVIKO – 19 na kwa sasa tupo katika wimbi la nne la ugonjwa huo. Kirusi kipya cha Omicron kinaenea kwa kasi kubwa, na tayari kipo na kimeshaingia nchini kwetu. Niwakumbushe kuchukua tahadhari kwa kufuata ushauri wa wataalamu wa afya. Pia, nitumie fursa hii kuwahimiza wananchi kupata chanjo dhidi ya UVIKO – 19. Natambua kuwa chanjo haizuii mtu kupata maambukizi, ila inapunguza makali ya ugonjwa huo. Hivyo niwahimize wananchi kwenda kuchanja. Chanjo zipo na zinapatikana bila malipo.

Vile vile, mwaka 2022 ni mwaka wa Sensa ya Watu na Makazi, hivyo naendelea kuwahimiza Watanzania kujitokeza kuhesabiwa ili tuweze kupata Takwimu zitakazotusaidia katika kupanga kwa usahihi masuala yetu ya maendeleo.

Halikadhalika, kwa watumishi wote wa umma na sekta binafsi, nitoe rai kuwa ni vyema tukauanza mwaka mpya wa 2022 na lengo la kuongeza ufanisi katika uzalishaji na ubora katika utoaji wa huduma. Tuazimie kuinua uchumi na kustawisha hali zetu, na tuendelee kulipa kodi stahiki kwa ajili ya maendeleo ya nchi.

Kwa wazazi wenzangu, nawasihi msijisahau na tafrija na sherehe za Sikukuu; ni vyema mkatumia muda huu kuwaandaa watoto wetu kukabiliana na changamoto mpya za kimasomo, na kuhakikisha kwamba hawaikosi fursa adhimu ya elimu bila malipo inayotolewa na Serikali yao.

Ndugu Wananchi;
Ni utamaduni na desturi kuwa kipindi hiki cha Sikukuu za mwisho wa mwaka huwa tunatumia muda huu kuwatembelea wazazi, ndugu, jamaa na marafiki katika maeneo mbalimbali. Hivyo basi, nitumie fursa hii kuwakumbusha wale watakaokuwa safarini kurudi kutoka maeneo mbalimbali ambayo walikwenda kwa ajili ya mapumziko ya mwisho wa mwaka, kuzingatia na kuheshimu sheria za barabarani ili kupunguza ajali zinazoepukika ambazo mara nying humaliza nguvu kazi ya Taifa.

Kwa kumalizia, napenda kuwatakia Watanzania wote kheri, fanaka na mafanikio katika Mwaka wa 2022. Tuombe Mwenyezi Mungu atushushie Neema na Baraka na atunusuru na kila aina ya majanga ndani ya nchi yetu. Tumuombe Mwenyezi Mungu atujaalie Afya, Siha na Nguvu, na atujaze hekima, busara na uadilifu katika kuliendeleza Taifa letu. Aamiin, Aamiin.

Kwa mara nyingine tena, nawasalimu kwa jina la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kuwatakia Kheri ya Mwaka Mpya wa 2022.

Ahsanteni sana.




Share:

Majaliwa Awajulia Hali Wagonjwa Katika Kituo Cha Afya Cha Nandagala Wilayani Ruangwa, Mkoani Lindi

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akimpongeza Rehema Hamisi ambaye amejifungua mtoto wa kike katika Kituo cha Afya cha Nandagala wilayani Ruangwa, mkoani Lindi katika wodi ya Mama na Mtoto kwenye kituo hicho, Desemba 31, 2021. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu) 


Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akimsalimia mtoto, Sarah Abubakar (1.5) na mama yake Loveness Njinjo wakati alipotembelea wodi ya Mama na Mtoto katika Kituo cha Afya cha Nandagala wilayani Ruangwa, mkoani Lindi, Desemba 31, 2021. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).


Share:

RAIS SAMIA AANZA 2022 KWA KUPONGEZA MAFANIKIO YA TANZANIA KATIKA MICHEZO YA KIMATAIFA


********************

Na. John Mapepele

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mhe, Samia Suluhu Hassan ameukaribisha mwaka 2022 kwa kupongeza mafanikio makubwa ya Michezo na Sanaa yaliyofikiwa na Tanzania kwenye medani za kimataifa.

Mhe. Samia ameyasema haya kwenye hotuba yake ya kufunga mwaka 2021 na kuukaribisha mwaka 2022 ambapo amesema kwa ujumla nchi yetu imepata mafanikio makubwa kwenye sekta za michezo na sanaa.

"Kwa upande wa Sanaa, michezo na utamaduni tunajivunia vijana wetu wa Tembo Warriors kwa kufuzu kushiriki katika kombe la dunia la mpira wa miguu kwa watu wenye ulemavu". Ameeleza Mhe. Rais

Timu ya Tembo Warriors inashiriki kombe la Dunia la watu wenye ulemavu nchini Uturuki, Oktoba mwaka huu.

Pia ameipongeza timu ya mpira wa miguu ya taifa ya wanawake chini ya miaka 20 ya Tanzanite kwa kubakiza hatua mmoja kufuzu kushiriki kwenye kombe la dunia nchini Costa Rica.

Tanzanite inatarajia hivi karibuni kuvaana na Ethiopia kwenye mchezo wa kufuzu mashindano hayo baada ya kuishinda kishujaa timu ya Burundi 1-1 ikicheza pungufu uwanjani ikiwa na wachezaji nane tu nchini kwao.

Pia amepongeza washindi wa Afrika wa mashindano ya urembo na utanashati ya viziwi watakaoiwakilisha Tanzania kwenye mashindano ya Dunia mwaka huu nchini Brazil. "Haya ni mafanikio makubwa katika medani za michezo. Ni fahari kwetu pia kuona vijana wetu wa tasnia ya muziki wameweza kushiriki na kupata tuzo Mali Bali katika ngazi za kimataifa". Amezisitiza Mhe. Rais

Naye, Waziri mwenye dhamana ya michezo nchini. Mhe, Innocent Lugha Bashungwa amesema Wizara yake kwa kushirikiana na wadau mbalimbali itahakikisha Tanzania inafanya vizuri katika mashindano yote ya kimatafa yanayofanyika kuanzia mwaka huu.

"Kipekee namshukuru sana, Mhe. Rais kwa maelekezo na kutoa kipaombele kwenye sekta za michezo hali ambayo imetuwezesha kufanya vizuri katika mashindano ya kimataifa, tunamwahidi kuendelea kusimamia vizuri zaidi ili kupeperusha bendera ya nchi yetu kimataifa katika michezo". Amesisitiza Mhe. Bashungwa

Aidha, amefafanua kuwa tayari Wizara imejiweka mikakati kabambe ya kushinda kwenye michuano ya kimataifa ikiwa ni pamoja na michezo ya jumuiya ya madola ya mwaka huu nchini Uingereza na Olympic.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo Dk. Hassan Abbasi ameongeza kuyataja mafanikio mengine makubwa kwenye michezo katika Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mhe, Rais. Samia Suluhu Hassan ni pamoja na kurejesha kwa Mashindano ya Michezo kwa Shule za Msingi ( UMITASHUMTA) na Sekondari (UMISSETA) na mashindano ya Taifa CUP yaliyoshirikisha zaidi ya mchezo mmoja tofauti na awali.

Pia amesema kwa mara kwanza nchini kumeanzishwa tamasha maalum la wanawake kwa ajili ya Michezo ya wanawake (Tanzania Women Festival) lililotoa mahasa kubwa na kuibua vipaji vya wachezaji wanawake hapa nchini.

Ameongeza kuwa Serikali imeratibu Tamasha la utoaji wa Tuzo mbalimbali kwa wasanii ili kuthamini na kutambua mchango wao pia kuwapa ali wasanii ya kufanya vizuri katika viwango vya kimataifa na hivyo kujipatia kipato.

Amesema sambamba na hayo Wizara iliandaa tamasha la kimataifa la Utamaduni na Sanaa la Bagamoyo ambalo lilitumika katika kutangaza utalii wa kiutamaduni kwa wageni kutoka sehemu mbalimbali za dunia ambalo lilipata mafanikio makubwa.
Share:

Majaliwa: Tanzania Iko Mikononi Mwa Mungu


WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Tanzania iko mikononi mwa Mungu na ndiyo maana imeendelea kuwa nchi yenye amani na utulivu na kimbilio la mataifa yaliyopoteza tumaini.

“Nchi hii imeshikwa na Mwenyezi Mungu na ni kwa sababu viongozi wa dini wanaendelea kuliombea Taifa hili, kwa hiyo na sisi tunalo jukumu la kuhakikisha kwamba nchi hii inabaki kwa salama,” amesema.

Ametoa kauli hiyo  Ijumaa, Desemba 31, 2021 wakati akizungumza na waumini baada ya kushiriki ibada ya Ijumaa na kuzindua msikiti wa Nkowe, ulioko kata ya Nkowe, wilayani Ruangwa, mkoani Lindi.

Amesema Serikali zote tangu awamu ya kwanza hadi ya sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, zimeendeela kuheshimu uwepo wa dini nchini kwani miongozo na mafundisho yanayotolewa na viongozi wa dini mbalimbali yanawafanya waumini wao kuwa rai wema.

“Mheshimiwa Rais alipoingia madarakani alikutana na Mababa Askofu wote wa nchi hii, lakini pia alikutana na masheikh wote kupitia BAKWATA ili kupata miongozo na baraka za kuongoza nchi hii.”

Waziri Mkuu amewataka Watanzania wampe nafasi Rais Samia ya kufanya kazi kwa sababu amekuwa Serikalini kwa muda mrefu na anajua ni nini Watanzania wanatamani Serikali yao iwafanyie.

 Wakati huohuo, Waziri Mkuu amesema madaraka yote yanatoka kwa Mwenyezi Mungu na yeye ndiye hupanga nani awe nani na kwa wakati gani. “Tuache tabia ya kuwafanya viongozi washindwe kufanya kazi zao kwa kuwatengenezea migogoro ya kila siku, tena mengine ya kusingizia tu.”

“Kila nafasi imetengenezwa na Mwenyezi Mungu na kila anayekwenda kuongoza Mwenyezi ndiye amesema wewe utakuwa pale. Na kama hajasema, hutokuwa; utatumia hela nyingi na zitapotea bure. Utakwenda na mambo mengine ya giza, lakini hutomudu. Mwenyezi Mungu keshasema huyu ni huyu, tuwaheshimu walioko kwenye nafasi za kuwatumikia Watanzania wafanye kazi zao kwa weledi.”

Akizungumzia juhudi zinazofanywa na Serikali, Waziri Mkuu amesema hivi karibuni Serikali imetoa sh. bilioni 2.3 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa na vituo vya afya wilayani Ruangwa. Amesema wilaya hiyo ina uhakika wa kuwapeleka shule kwa wakati watoto wote waliofaulu kuingia kidato cha kwanza kwani madarasa yapo ya kutosha.

Waziri Mkuu yuko jimboni kwake Ruangwa kwa mapumziko ya mwisho wa mwaka.


Share:

Friday 31 December 2021

YANGA YAINYESHEA MVUA YA MAGOLI DODOMA JIJI, YAICHAPA 4-0



*************

NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

Klabu ya Yanga imeichapa mvua ya magoli timu ya Dodoma Jiji mabao 4-0 katika mchezo wa NBC Premier league uliochezwa kwenye dimba la Benjamini Mkapa Jijini Dar es Salaam.

Yanga imecheza kandanda safi ambapo mshambuliaji wao mahiri Fiston Mayele alipachika bao la kuongoza dakika ya 42 kipindi cha kwanza .

Kipindi cha pili Yanga iliendelea kutawala mchezo kwani mpaka dakika ya 54 ya mchezo Yanga ilikuwa inatawala mchezo kwa asilimia 80% kwa 20%.

Yanga ilifanikiwakupata bao la pili kupitia kwa winga wao Jesus Muloko na baadae Dodoma Jiji kujifunga.

Aucho alifunga ubao wa magoli kwa kupachika bao tamu akipokea pasi kutoka kwa Jesus Muloko.
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger