Tuesday 16 May 2017

BODI YA MIKOPO ELIMU YA JUU ZANZIBAR: ANGAZO LA MAOMBI YA MIKOPO MWAKA WA MASOMO 2017/18

...

Image result for BODI YA MIKOPO ZANZIBAR

TANGAZO

Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu Zanzibar inawatangazia wanafunzi wote wanaohitaji kujiendeleza katika fani mbalimbali za Elimu ya Juu kuwa fomu za maombi ya mikopo ya elimu ya juu kwa mwaka wa masomo 2017/18 zitaanza kutolewa kwa miezi mitatu kuanzia tarehe 02/05/2017 hadi tarehe 31/07/2017.

Mikopo itatolewa kwa waombaji waliotimiza sifa za kujiunga na masomo ya juu katika ngazi za:
  • Shahada ya Kwanza (Bachelor Degree),
  • Shahada ya Pili (Master Degree)
  • Shahada ya Tatu (PhD).
Walengwa wa maombi ya mikopo ni:
  • Wahitimu wa Kidato cha Sita wenye sifa za kujiunga na masomo ya Shahada ya Kwanza.
  • Wahitimu wa Diploma wenye sifa za kujiunga na masomo ya Shahada ya Kwanza.
  • Wahitimu wa Shahada ya Kwanza wenye sifa za kujiunga na masomo ya Shahada ya Pili.
  • Wahitimu wa Shahada ya Pili wenye sifa za kujiunga na Shahada ya Tatu.
Kuanzia mwaka wa masomo 2017/18 Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu Zanzibar haitatoa mikopo kwa waombaji ambao ni watumishi wa Taasisi za Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (SMT). Mkazo umewekwa kwa vijana wapya waliomaliza masomo na ambao hawajapata ajira.

Waombaji wa mikopo wanapaswa kuzingatia Fani za Vipaumbele vya Serikali ambazo zinapatikana katika tovuti za Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu Zanzibar (www.zhelb.go.tz) na tovuti ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar (www.moez.go.tz).

Fomu za maombi zitalipiwa shilingi 10,000 ambazo zitalipwa moja kwa moja na muombaji kwenye akaunti namba 021108001357 ya Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu iliyopo katika Benki ya Watu wa Zanzibar (PBZ).

Wanaohitaji fomu za maombi wanaombwa kufika katika ofisi za Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu zilizopo Vuga kwa Unguja na jengo la Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali, Chakechake Pemba na wanatakiwa kuchukua:
  • Kitambulisho cha Mzanzibari
  • Fomu ya malipo (Pay Slip) kutoka Benki ya Watu wa Zanzibar (PBZ)
  • Vivuli vya vyeti na matokeo ya masomo kwa ngazi aliyohitimu.

SIFA ZA KUPATA MKOPO

Sifa za waombaji wa mikopo ambao maombi yao yanaweza kuzingatiwa wakati wa uteuzi zimetajwa kwenye kifungu cha 20 zikiwemo:
  • Mwombaji awe Mzanzibari
  • Awe ameomba mkopo kwa kujaza Fomu Namba 1 au kupitia njia nyengine yoyote ile ambayo BMEJZ itaona inafaa. Maombi yawe yamewasilishwa ndani ya muda maalum uliowekwa na BMEJZ unaoanzia Mei 2 hadi Julai 31 ya kila mwaka.
  • Awe amepata udahili kwenye chuo cha elimu ya juu kinachotambuliwa na mamlaka husika nchini.
  • Awe amepata alama nzuri za ufaulu.
  • Mwombaji wa shahada ya kwanza (Bachelor/First Degree) aliyehitimu kidato cha sita anapaswa awe amefaulu angalau masomo mawili (Principal subjects) kwa alama za ufaulu zinazoanzia:
  • alama 4.0 kwa wahitimu wa masomo ya sayansi au ufundi;
  • alama 5.0 kwa wahitimu wa masomo ya biashara;
  • alama 5.0 kwa wahitimu wa masomo ya sanaa au sayansi jamii.
  • Mwombaji wa shahada ya kwanza aliyehitimu stashahada ya kawaida (Ordinary Diploma) katika masomo ya sayansi au ufundi anatakiwa awe na ufaulu wa alama (GPA) 3.0 au B; wahitimu wa stashahada za masomo ya biashara, sayansi jamii au Sanaa wapate alama kuanzia 3.5 au B+.
  • Mwombaji wa shahada ya uzamili (Master/Second Degree) katika masomo ya sanaa au sayansi jamii awe amehitimu shahada ya kwanza na kupata alama za ufaulu kuanzia daraja la pili la juu (upper second class). Waombaji wa shahada ya uzamili katika nasomo ya sayansi, ufundi, tiba, uchumi, mipango na biashara wawe na alama za ufaulu za kuanzia daraja la pili la chini (lower second class). Wahitimu wa stashahada ya uzamili wanapaswa kupata alama za ufaulu kuanzia daraja la pili la chini (lower second class)
  • Mwombaji wa shahada ya uzamivu (Doctor of Philosophy - PhD) awe amehitimu shahada ya uzamili na kupata alama za kuanzia daraja la pili la juu kwa waombaji wa masomo ya sanaa na sayansi jamii. Waombaji wa shahada ya uzamivu katika masomo ya sayansi, ufundi, udaktari na uchumi, mipango na takwimu wapate alama za ufaulu kuanzia daraja la pili la chini.
  • Waombaji wanaoendelea na masomo vyuoni pia wanaweza kuomba kwa kuzingatia sifa za kitaaluma zilizotajwa hapo juu [d(i) –(iv)]. Aidha mwombaji awe amefaulu mitihani yake ya chuo kwa kiwango kitakachomwezesha kuendelea na masomo kwa mwaka unaofuatia katika ngazi ya masomo anayoombea mkopo.
  • Awe ameomba fani inayolingana na vipaumbele vya SMZ katika mwaka husika.
  • Asiwe na mkopo au udhamini wa masomo kutoka taasisi nyengine.
  • Mwombaji wa shahada ya kwanza asizidi umri wa miaka 40 kuanzia tarehe ya kutuma maombi na mwombaji wa shahada ya uzamili asizidi miaka 45 kuanzia tarehe ya kutuma maombi. Ukomo wa umri wa mwombaji wa shahada ya uzamivu ni miaka 47 kuanzia tarehe ya kutuma maombi.
  • Mwombaji aliyeajiriwa kwenye utumishi wa umma awasilishe barua ya ruhusa kutoka kwa mwajiri wake.
  • Mwombaji anayedaiwa na Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu Zanzibar awe ameshaanza kulipa deni lake kwa angalau asilimia 25 ya deni lote bila ya kusita kwa malipo ya deni ya kila mwezi.
  • Mwombaji aliyesoma kwa mkopo kutoka BMEJZ awe ameshafanya kazi kwa angalau miaka miwili baada ya kuhitimu masomo yake ya awali kabla ya kuomba mkopo mwengine kutoka BMEJZ.

Angalizo:

  • Waombaji wanaotumia sifa za masomo ya kidato cha nne kuomba udahili katika vyuo vikuu vya nje ya nchi ili kujiunga na masomo ya Shahada ya Kwanza, maombi yao ya mkopo hayatozingatiwa.
  • Waombaji wa mikopo waliohitimu masomo ya Diploma pasi na kuwa na elimu ya kidato cha sita au sifa za kujiunga na kidato cha sita, wanatakiwa wawe wamefaulu angalau masomo matano ya Kidato cha Nne kwa kiwango cha alama D na kuhitimu ngazi ya cheti (Certificate) kabla ya kujiunga na masomo ya Diploma.
  • Waajiriwa hawahusiki na utaratibu wa maombi ya mikopo ya elimu ya juu kwa mwaka huu wa masomo

FANI ZA VIPAUMBELE WA KIPINDI CHA 2016 - 2020

Tume ya Mipango ya SMZ imetoa taarifa kuhusu utafiti uliofanywa juu ya hali ya utumishi nchini ambayo imeonesha uwepo wa mahitaji makubwa ya wataalamu. Taarifa hiyo imeibua maeneo ya Vipaumbele vya SMZ juu ya mahitaji ya wataalamu na imeagizwa kuwa taarifa hiyo itumike kama kigezo muhimu kwa utoaji wa mafunzo ya elimu ya juu nchini ili kufikia utekelezaji wa mipango na maendeleo ya rasilimali watu iliyo bora na itakayowaandaa watu wenye ujuzi sahihi, taaluma, tabia na silka zenye tija zinazoendana na mabadiliko ya mfumo wa ushindani wa soko la ajira na kufikia viwango vya juu vya uzalishaji na utoaji huduma.

Ili kurahisisha utekelezaji wa Vipaumbele vya SMZ katika utoaji wa mafunzo ya elimu ya juu kuanzia mwaka wa masomo 2016/17 hadi 2019/20, Tume ya Mipango imevigawa vipaumbele hivyo katika madaraja matatu tofauti kulingana na umuhimu wa kila kada kama inavyoonekana katika jedwali la hapo chini.

Hivyo, kwa mwaka huu wa masomo, BMEJZ itazingatia kikamilifu taarifa ya Tume ya Mipango wakati wa upokeaji wa maombi ya mikopo na uteuzi wa waombaji katika mwaka wa masomo 2017/18. 

TAARIFA ZAIDI <<BOFYA HAPA>>
Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger