Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) mkoa wa Shinyanga imeokoa Shilingi milioni 30, laki tano na elfu tatu miasita na hamsini kutoka kwa Viongozi wa Vyama vya ushirika (AMCOS) waliofanya ubadhirifu wa Fedha za Wakulima wa Pamba msimu wa Mwaka 2018/2019.
Akizungumza na waandishi wa habari januari 14 mwaka huu Kaimu Mkuu wa (TAKUKURU) Mkoa wa Shinyanga, Hussein Mussa alisema kuwa ofisi yake ilifuatilia kwa kina madeni ya Wakulima wa Pamba wanaodai fedha zao kutokana na pamba waliyouza kupitia AMCOS na kubaini kuwepo ubadhilifu wa fedha za wakulima.
Alisema kuwa Baada ya uchunguzi TAKUKURU ilibaini kuwa AMCOS saba za Lugana, Mwakipoya, Ng'washinong'hela, Nyenze, Kalitu, Kweli Balimi na Ibadakuli ndizo zinadaiwa fedha na wakulima wa pamba shilingi 109,497,130 licha kuwa fedha hizo zimekwisha kutolewa na Kampuni za Ununuzi.
“TAKUKURU ilibaini kuwa mpaka kufikia mwezi Desemba 2019 makampuni yaliyonunua pamba mkoani Shinyanga yalikuwa hayadaiwi Fedha za Wakulima bali walikuwa yanadaiwa ushuru wa AMCOS jumla ya Shilingi 890,105,580 alisema Mussa.
Amefafanua kuwa kuwa baada ya kubaini ubadhirifu huo Takukuru iliweza kuwakamata baadhi ya Viongozi wa AMCOS waliofanya ubadhilifu wa fedha za Wakulima na waliweza kurejesha kiasi cha Shilingi 30,503,650 fedha ambazo zinatarajiwa kugaiwa kwa Wakulima hivi Karibuni.
“ Viongozi wa AMCOS ya Kweli Balimi ya Wilaya ya Shinyanga ambao walirejesha Fedha walizokuwa wanadaiwa kiasi cha Shilingi 6,362,400 walikuwa wamezifanyia ubadhilifu na tayari fedha hizo zimeshatolewa kwa Wakulima” alisema Mussa.
Aliwataka wananchi wa Mkoa wa Shinyanga wametakiwa kuendelea kutoa ushirikiano kwa TAKUKURU ili Kuhakikisha wanatokomeza rushwa katika mkoa wa Shinyanga.
Mwisho.
0 comments:
Post a Comment