Thursday, 22 May 2025

DKT.SERERA: SEKTA BINAFSI TUMIENI FURSA ZA AFREXIM BANK KANDA YA AFRIKA


Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara Dkt. Suleiman Serera,akizungumza wakati akifungua Kongamano la Afreximbank Roadshow lililoandaliwa na Benki Kuu ya Tanzania lililofanyika jijini Dar es Salaam.

.....

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara Dkt Suleiman Serera ameishauri sekta binafsi ya Tanzania kuhakikisha inatumia fursa ya uwepo wa Benki ya Kanda ya Afrika ya Afrexim kupata mitaji itakayowezesha kuongeza thamani mazao na bidhaa za viwandani kwa kiwango cha kimataifa ili kuiwezesha nchi kushindana ndani ya soko la Afrika.

Dkt. Serera ameyasema hayo jijini Dar es Salaam wakati akiongea na Waandishi wa Habari baada ya kufungua Kongamano la Afreximbank Roadshow lililoandaliwa na Benki Kuu ya Tanzania pamoja na Benki hiyo likilenga kutambua changamoto za wafanyabiashara ili benki hiyo iweze kuzitatua kupitia fursa za mitaji, fursa za masoko na teknolojia

Aidha, Dkt. Serera aliwahimiza Wajasiliamali wa Tanzania, Wawekezaji wa viwanda, na biashara zinazoongozwa na vijana kushirikiana na Afreximbank na kutumia fedha zinazopatikana kwa usindikaji wa kilimo, maendeleo ya mauzo ya nje, ujenzi wa viwanda vya kijani, na biashara ya kikanda.

"Tuwekeze Dodoma, Mbeya, na Kigoma," alihimiza. "Tujenge Maeneo ya Usindikaji wa Mauzo ya Nje, tuimarishe korido za vifaa, na tujenge miundombinu ya kidijitali kwa mfumo wa biashara unaostawi."

Kwa upande wake Rais wa Chemba ya Biashara, Viwanda na Kilimo Tanzania (TCCIA) Bw. Vincent Minja amesema jukwaa hilo ni muhimu katika uwezeshaji wa biashara barani Afrika akiweka bayana kuwa biashara kati ya nchi za Afrika bado ni kidogo ikilinganishwa na biashara kati ya nchi za Bara hilo na mabara mengine duniani

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Uhusiano wa Wateja wa benki hiyo Bw. Eric Monchu ameihakikishia sekta binafsi ya Tanzania kuwa wako tayari kukuza uchumi endelevu wa Tanzania

Aidha Bw Monchu amebainisha kuwa hadi sasa, Benki hiyo imetoa takriban dola bilioni 2 kuwezesha utekelezaji wa Miradi ya Kimkakati nchini ikiwemo Dola milioni 800 kwa kwa ajili ya Mradi wa Umeme wa Maji wa Julius Nyerere, Dola milioni 290 kwa Reli ya Kati (SGR), Dola milioni 200 kwa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP) pamoja na Nyongeza ya fedha kwa benki za ndani na wadau wa sekta binafsi

Naye Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade) Bi Lulu Mkude amewaalika wadau na mabenki mbalimbali waliohudhuria kongamano hilo kushiriki Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es salaam yatakayoanza tarehe 28 Juni hadi 13 Julai 2025 kwani ni jukwaa zuri la kutangaza biashara na huduma wanazotoa.


Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara Dkt. Suleiman Serera,akizungumza wakati akifungua Kongamano la Afreximbank Roadshow lililoandaliwa na Benki Kuu ya Tanzania lililofanyika jijini Dar es Salaam.





Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara Dkt. Suleiman Serera (katikati ) akizungumza na Viongozi mbalimbali wakiwemo Kaimu Mkurugenzi wa Uhusiano wa wa Wawateja wa Areximbank Bw. Eric Monchu Intong, Rais wa Chemba ya Biashara, Viwanda na Kilimo Tanzania (TCCIA) Bw. Vincent Minja na Kaimu Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Bi lulu Mkude kabla ya ufunguzi wa Kowngamano la Afreximbank Roadshow lililofanyika Mei 2025 jijini Dar es Salaam


Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara Dkt. Suleiman Serera,akiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kufungua Kongamano la Afreximbank Roadshow lililoandaliwa na Benki Kuu ya Tanzania lililofanyika jijini Dar es Salaam.
Share:

MHE. MBEKI ASHIRIKI MHADHARA WA SIKU YA AFRIKA UDSM


Rais wa zamani wa Jamhuri ya Afrika Kusini Mheshimiwa Thabo Mbeki ameshiriki mhadhara wa Siku ya Afrika uliofanyika katika Ukumbi wa Nkrumah wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM).

Akizungumza katika mjadala huo Mhe.Thabo Mbeki amesema mjadala huo umewakutanisha wasomi, vijana na Taasisi ya Thabo Mbeki ili kuangalia kwa pamoja juu ya nini kifanyike ili kuiletea maendeleo Afrika.


Mhe. Mbeki alielezea hali ya sasa ya Afrika kwa kutumia muktadha wa kihistoria wa ukoloni, udhaifu wa taasisi za ndani, utegemezi mkubwa wa mataifa ya nje na haja ya Umoja wa Afrika na Taasisi zake kufikia malengo ya kuanzishwa kwake..


“Kesho ya bara la Afrika haiwezi kuendelea kuamuliwa na watu wengine bali utatokana na uamuzi, juhudi na mshikamano wa Waafrika wenyewe na sio watu wengine”, alisema.


Alisema kuwa licha ya mafanikio ya kisiasa yaliyopatikana baada ya uhuru, bado Afrika inakumbwa na changamoto za kiuchumi, usalama, na ukosefu wa mshikamano


Ametoa wito kwa Nchi za Afrika kuhakikisha umoja na mshikamano unaendelea kuwepo na kuongeza kuwa taasisi za Umoja wa Afrika na Tume ya AU lazima zihakikishe zinasimamia misingi ya kuanzishwa kwao na kutimiza malengo yao


Ameongeza kuwa vyama vya siasa katika bara la Afrika vinahitaji viongozi kama Mwalimu Nyerere watakao iwezesha Afrika kufikia matarajio yake ya kiuchumi na kisiasa.


Ametoa rai kwa vijana wa vyuo vikuu kushirikiana na vijana wenzao barani Afrika na kutumia nafasi zao kutoa muelekeo wa nini kifanyike ili kufufua matumaini na mwelekeo wa bara la Afrika.


Nao Wasomi wa UDSM wakichangia mjadala huo, wamesema ni wakati wa kuchukua hatua na kuacha kulalamika na kushirikiana kwa ajili ya kuleta maendeleo ya kweli kwa bara la Afrika


Akitoa salamu za shukurani baada ya mhadhara huo Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Rais wa Awamu ya Nne Mheshimiwa Dkt. Jakaya Kikwete ameishukuru Taasisi ya Thabo Mbeki kwa kukichagua Chuo hicho kuwa mwenyeji wa mhadhara wa Siku ya Afrika kwani unaonesha imani ya Taasisi hiyo kwa Chuo hicho.


Amesema kauli mbiu ya mhadhara wa Siku ya Afrika usemao “Hali ya Bara la Afrika:Ufufuo mpya wa Mwamko wa Kiafrika“ unaakisi mahitaji ya kweli ili kuifanya Afrika iendelee.


Mhadhara huo uliwakutanisha wasomi kutoka UDSM na Taasisi ya Thabo Mbeki kwa lengo la kujadili na kujenga uelewa wa pamoja, huku wakitafakari makosa yaliyopita na kutathmini hatua stahiki zinazopaswa kuchukuliwa ili kuleta maendeleo ya kweli barani Afrika.


Mhadhara huo uliwaleta pamoja wasomi, wanafunzi, viongozi wa serikali, na wanadiplomasia ni sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Afrika ambayo huadhimishwa kila mwaka ifikapo tarehe 25 Mei.


Washiriki wa mhadhara kwa pamoja walitafakari hatma ya bara la Afrika katika muktadha wa changamoto na fursa zinazolikabili bara la Afrika.
Share:

Wednesday, 21 May 2025

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO ALHAMISI MEI 23, 2025






















Share:

WIZARA YA KILIMO YAOMBA BAJETI YA SHILINGI TRILIONI 1.24



Na Dotto Kwilasa, Dodoma

Serikali kupitia Wizara ya Kilimo imewasilisha mpango wake wa makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka wa fedha 2025/2026, ukilenga kuimarisha ajira staha kwa vijana na wanawake kupitia Programu ya Building a Better Tomorrow (BBT) pamoja na utekelezaji wa miradi mikubwa ya kilimo na miundombinu ya umwagiliaji.

Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe amesema Wizara yake imepanga kukusanya jumla ya Shilingi 12.26 bilioni kupitia vyanzo mbalimbali vya mapato ambapo Shilingi 8.66 bilioni zitatokana na ukaguzi wa mazao, kodi za majengo na uuzaji wa nyaraka za zabuni, huku Shilingi 3.6 bilioni zikipatikana kupitia ada za umwagiliaji na ukodishaji wa mitambo.

Akizungumza Bungeni leo Mei 21,2025 Jijini Dodoma, Waziri Bashe ameomba Bunge liidhinishe matumizi ya jumla ya Shilingi trilioni 1.24 kwa mwaka huo wa fedha.

Kuhusu miradi ya Maendeleo na Matumizi ya Kawaida, Wizara imeomba Shilingi bilioni 838.26, ambapo Shilingi bilioni 702.28 zitatumika kutekeleza miradi ya maendeleo, zikiwemo Shilingi bilioni 424.33 kutoka vyanzo vya ndani na Shilingi bilioni 277.95 kutoka nje.

Fedha nyingine ni Shilingi bilioni 135.98 zitatumika kwa matumizi ya kawaida, ikiwa ni pamoja na Shilingi bilioni 81.45 kwa mishahara ya watumishi na Shilingi bilioni 54.54 kwa matumizi mengine ya wizara, bodi na taasisi zake.

Waziri Bashe amesema Tume ya Taifa ya Umwagiliaji inaomba kuidhinishiwa Shilingi bilioni 382.14, kati ya hizo Shilingi bilioni 308.72 ni kwa ajili ya miradi ya maendeleo (zikiwemo Shilingi bilioni 259.62 kutoka ndani na Shilingi bilioni 49.10 kutoka nje), na Shilingi bilioni 73.42 kwa matumizi ya kawaida ambapo Shilingi bilioni 8.27 ni kwa ajili ya mishahara na Shilingi bilioni 65.15 kwa matumizi mengineyo.

Kuhusu Tume ya Maendeleo ya Ushirika, jumla ya Shilingi bilioni 22.58 zinaombwa, ambapo Shilingi bilioni 21.88 ni kwa matumizi ya kawaida (mishahara Shilingi bilioni 12.85, matumizi mengineyo Shilingi bilioni 9.03) na Shilingi milioni 697.18 kwa utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa fedha za ndani.

Kwa upande mwingine Waziri huyo mwenye dhamana ya Kilimo amesema Ajira kwa Vijana na Wanawake Kwenye Mashamba Makubwa

Mbali na makadirio ya fedha, Serikali imeeleza maendeleo ya utekelezaji wa Programu ya BBT inayolenga kuimarisha ajira za vijana na wanawake kupitia miradi mitano.

Ameitaja miradi hiyo kuwa ni pamoja na mashamba ya pamoja, mitaji, huduma za ugani, uongezaji thamani wa mazao, na umwagiliaji,Shamba la Chinangali (ekari 1,772) limekabidhiwa kwa vijana 261 na linaendelea kuzalisha mazao mbalimbali.

Aidha, shamba la Ndogowe (ekari 11,453) limekabidhiwa kwa vijana 342, huku miundombinu muhimu ikiwa tayari imejengwa.

Aidha ameutaja mradi mwingine mkubwa ni Shamba la Mapogoro mkoani Mbeya ambalo litafadhiliwa kwa Dola milioni 129 kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika, ikiwa ni hatua ya kukuza kilimo kikubwa chenye tija nchini.





Share:

MAKAMANDA WA POLISI WAFANYA UKAGUZI WA MIUNDOMBINU YA GESI ASILIA MTWARA

Kamishna wa Operesheni na Mafunzo ya polisi CP Awadhi Juma Haji
Fred Mfikwa Mkuu wa kitengo cha usalama GASCO

Kamishna wa Operesheni na Mafunzo wa Jeshi la Polisi Tanzania, CP Awadhi Juma Haji, ameongoza Makamanda wa Polisi wa Mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, Lindi na Mtwara—mikoa inayopitiwa na miundombinu ya gesi asilia na kufanya ziara ya ukaguzi wa miundombinu hiyo inayotoka Msimbati, Madimba hadi Kinyerezi kupitia Somanga.

,Ziara hii ni sehemu ya utekelezaji wa makubaliano ya ushirikiano kati ya Jeshi la Polisi na Kampuni ya GASCO inayosimamiwa na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC).

Akizungumza wakati wa ukaguzi huo, CP Awadhi amebainisha kuwa Jeshi la Polisi lina wajibu wa kuhakikisha miundombinu ya gesi asilia inakuwa katika hali ya usalama wa kutosha, kwa kuwa rasilimali hiyo ni muhimu kwa maendeleo ya taifa.

“Jeshi la Polisi lina makubaliano ya ushirikiano na Kampuni ya GASCO kupitia TPDC kwa ajili ya kutoa ulinzi kwenye miundombinu ya gesi asilia. Ziara hii ni utekelezaji wa takwa la makubaliano hayo, ambapo kila mwaka tunatakiwa kufanya ukaguzi ili kutathmini hali ya kiusalama,” amesema CP Awadhi.

Amesema ukaguzi huo unaangazia tathmini ya hali ya usalama katika kipindi kilichopita, kutambua changamoto zilizojitokeza na namna zilivyoshughulikiwa, pamoja na kupanga mikakati ya kuimarisha zaidi ulinzi wa miundombinu hiyo.

“Nichukue fursa hii kuwashukuru wenzetu wa GASCO na TPDC kwa ushirikiano mkubwa walioutoa katika kuandaa ziara hii. Ushirikiano huu unatupa nafasi ya kufanya tathmini ya pamoja ya hali ya kiusalama kwenye maeneo yote ya miundombinu ya gesi asilia,” ameongeza.

Naye Mkuu wa Kitengo cha Usalama GASCO,Fred Mfikwa ameeleza kuwa mbali na vyombo vya dola, GASCO pia imeingia mikataba na vijiji vinavyopitiwa na miundombinu hiyo, ambapo wananchi hushiriki katika shughuli za ulinzi na usafi wa maeneo yanayopitiwa na miundombinu ya gesi asilia. 

Mfikwa amesema hatua hii imeongeza urafiki kati ya TPDC na jamii, hali inayowasaidia kupokea taarifa muhimu za kiusalama na kutambua mapema hitilafu zinazoweza kutokea.

Aidha, ametoa pongezi kwa Jeshi la Polisi kwa namna lilivyo mstari wa mbele katika kushughulikia changamoto za kiusalama.

 “Kwa kipindi chote tangu tuingie makubaliano na Jeshi la Polisi, hatujakumbwa na changamoto yoyote kubwa. Polisi wamekuwa wakijitokeza haraka tunapohitaji msaada, na hatua za kisheria huchukuliwa kwa wanaoharibu au kuingilia miundombinu yetu,” amesema.


Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger