Wednesday 31 July 2024

TCB BENKI YATOA VIFAA VYA UJENZI VYENYE THAMANI YA MILIONI 50 SUMBAWANGA


*Sumbawanga, 30 Julai 2024* — TCB Benki inajivunia kutangaza mchango mkubwa wa vifaa vya ujenzi vyenye thamani ya milioni 50 za Kitanzania (TZS) kusaidia maendeleo ya sekta ya elimu na afya katika Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga. Mchango huu wa hali ya juu unalenga kuboresha miundombinu muhimu kwa ajili ya kuongeza upatikanaji wa elimu bora na huduma za afya katika eneo hilo.

Mchango huu, uliokabidhiwa rasmi katika hafla iliyofanyika katika makao makuu ya Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga, unajumuisha aina mbalimbali za vifaa vya ujenzi kama vile mifuko ya saruji, mabati, na vitu vingine muhimu. Vifaa hivi vitatumiwa katika ujenzi na ukarabati wa madarasa ya shule, kliniki za afya, na vituo vingine muhimu, hivyo kuwa na athari moja kwa moja kwa ustawi na matarajio ya baadaye ya jamii ya eneo hilo.

*Kujitolea kwa TCB Benki kwa Maendeleo ya Jamii*

Mpango wa TCB Benki ni uthibitisho wa kujitolea kwake kwa dhati kwa majukumu ya kijamii na maendeleo ya jamii. Kwa kuwekeza katika sekta muhimu kama vile elimu na afya, TCB Benki inalenga kukuza ukuaji endelevu na kuboresha viwango vya maisha katika maeneo yasiyo na huduma za kutosha.

"Utoaji wa vifaa hivi vya ujenzi unaonyesha kujitolea kwetu kusaidia jamii tunazohudumia," alisema, Bi. Chichi Banda, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Mahusiano ya Umma wa TCB Benki. "Elimu na huduma za afya ni nguzo muhimu kwa jamii inayostawi, na tunajivunia kuchangia katika kuboresha Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga. Tunaamini msaada huu utaweza kuboresha mazingira ya kujifunzia na huduma za afya."

*Athari kwa Jamii ya Mitaa*

Vifaa vya ujenzi vilivyotolewa na TCB Benki vinatarajiwa kuwa na athari kubwa katika Wilaya ya Sumbawanga. Shule zitakazonufaika na mchango huu zitakuwa na uwezo wa kupanua miundombinu yao na kutoa mazingira bora ya kujifunzia kwa wanafunzi. Kliniki za afya zitakuwa na vifaa bora zaidi vya kuwahudumia wananchi, kuhakikisha kuwa wakazi wanapata huduma za matibabu muhimu.

Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga ilieleza shukrani zake kwa msaada huo. KALOLOLWANGA GERALD NTILLA

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Sumbawanga DC, alisema, "Tunashukuru sana kwa mchango wa TCB Benki. Vifaa hivi vitaboresha sana juhudi zetu za kuboresha miundombinu ya elimu na afya katika wilaya yetu. Ushirikiano huu unaonyesha dhamira ya pamoja kwa maendeleo ya jamii yetu."

*Kuangalia Mbele*

TCB Benki inaendelea kujitolea kwa kuunga mkono mipango inayohimiza maendeleo endelevu na kuboresha ubora wa maisha nchini Tanzania. Mchango huu kwa Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga ni hatua moja ya mchakato mrefu kuelekea kufanikisha malengo haya.

Kwa maelezo zaidi kuhusu mipango ya kijamii ya TCB Benki na shughuli nyingine za majukumu ya kijamii, tafadhali tembelea www.tcbbank.co.tz au wasiliana na Idara ya Mawasiliano ya Benki.

*Kuhusu TCB Benki*

TCB Benki ni taasisi ya kifedha inayongoza nchini Tanzania, inayojulikana kwa suluhisho zake za ubunifu katika benki na kujitolea kwa huduma kwa wateja. Kwa msisitizo mkubwa katika majukumu ya kijamii, TCB Benki inasaidia kwa dhati mipango inayosababisha mabadiliko chanya na kukuza maendeleo endelevu katika jamii inazohudumia.
Share:

BIL 3 ZIMETOLEWA MATENGENEZO BARABARA ZILIZOATHIRIWA NA EL-NINO MKOANI NJOMBE-ENG RUTH


Na Mathias Canal, Njombe

Serikali inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt Samia Suluhu Hassan imetoa kiasi cha shilingi bilioni 3 kwa ajili ya kushughulikia Barabara zilizoathiriwa na mafuriko/Mvua za El-Nino kwa mkoa wa Njombe.

Fedha hizo zimetumika kuhakikisha kuwa miundombinu yote ya Barabara iliyoathiriwa na wananchi kushindwa kutoka eneo moja Kwenda jingine inapitika kwa haraka kama ambavyo serikali imekusudia.

Akizungumza mara baada ya kukagua miundombinu ya miradi ya Barabara inayoendelea na matengenzo mbalimbali Meneja wa Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS) mkoa wa Njombe Mhandisi Ruth Shaluwa amesema kuwa Maeneo ya miundombinu ya barabara na madaraja yaliyoathiriwa na Mvua za El Nino mwezi Januari – Mei, 2024 ni Itoni – Ludewa – Manda Km 211.4; Sehemu ya Lusitu – Mawengi Km 50 (Maporomoko ya Udongo, Gangitoroli Km 62 – Km 64 na Jongojongo Km 82 – Km 85), ambapo kiasi cha shilingi Milioni 350 zimetumika.

Maeneo mengine ni Pamoja na Barabara ya Njombe – Makete Km 107.4 katika Maporomoko ya Udongo eneo la Mang’oto, Barabara ya Ikonda – Lupila – Mlangali Km 78.84 katika eneo lililokatika kwenye barabara na Maporomoko ya Udongo ambapo shilingi Milioni 383 zimetumika.

Pia Milioni 250 zimetumika kwa ajili ya ukarabati wa tuta la Barabara eneo la Ikowo katika Barabara ya Ndulamo – Nkenja – Kitulo I Km 42.28 ambao ujenzi umefikia asilimia 58 kwa gharama ya shilingi Milioni 150, Matengenezo ya eneo lililofurika kwenye Mto Rumakali na Maporomoko ya Udongo eneo la Utanziwa katika Barabara ya Kikondo – Bulongwa – Makete Km 74.2

Mhandisi Ruth amesema kuwa Milioni 359.76 zimetumika kwa ajili ya matengenezo kwenye Barabara ya Nkenja – Ikuwo – Usalimwani Km 42.70, huku Milioni 257.24 zikitumika kwa ajili ya matengenezo kwenye Barabara ya Kitulo II – Matamba – Mfumbi.
Mhandisi Ruth amesema kuwa Pamoja na Barabara hizo pia serikali imetoa shilingi milioni 150 kwa ajili ya kukabiliana na uharibifu wa Barabara uliotokana na mvua za El-Nino katika Barabara ya Mkoa ya Kipengele – Wangama – Kidugala – Mambegu, Pamoja na Milioni 150 zilizotolewa kwa ajili ya Barabara ya Mkoa ya Makoga – Kinenulo – Imalinyi – Mdandu pamoja na Milioni 750 zilizotumika kwa ajili ya Barabara kuu ya Makambako-Lukumburu yenye urefu wa Kilomita 139.5 eneo la Lukumburu.

Meneja huyo amesema kuwa kutokana na Athari hizo za Mvua za El Nino, barabara nyingi zilikuwa zikipitika kwa taabu na hivyo kupelekea kuidhinishiwa fedha kiasi cha shilingi billioni 3 ili kuboresha miundombinu ya barabara na madaraja.

Mhandisi Ruth amesema kuwa katika mwaka wa fedha 2024/25 kwa ujumla Mkoa umepangiwa kiasi cha Shilingi bilioni 11.58 ili kutekeleza kazi za Matengenezo na Shilingi bilioni 3.079 kutekeleza miradi ya maendeleo. Taa zaidi ya 90 zitafungwa katika maeneo mbali mbali ya mtandao wa barabara zinazohudumiwa na TANROADS.

Share:

Tuesday 30 July 2024

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMATANO JULAI 31,2024

Share:

MBUNGE MTATURU AITAKA RUWASA KUKAMILISHA MRADI MAPEMA


MBUNGE wa Singida Mashariki Miraji Mtaturu,akizungumza kwenye ziara katika Kata ya Kikio kwa ajili ya kutoa mrejesho wa Bunge la Bajeti 2024/2025,kuhamasisha uchaguzi wa serikali za mitaa,vijiji na vitongoji 2024 na kusikiliza kero za wananchi.

.......

MBUNGE wa Singida Mashariki Miraji Mtaturu amefanya ziara katika Kata ya Kikio na kukagua mradi wa maji wa kijiji cha Mkunguwakihendo na kumshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutenga fedha kiasi cha Shilingi Bilioni 1.9 kwa ajili ya miradi ya maji kwenye jimbo hilo.

Ili jitihada za Rais Dkt Samia za kumtua mama ndoo ya maji kichwani zifanikiwe amemtaka Meneja wa RUWASA wilaya ya Ikungi kuongeza nguvu kazi ili mradi wa maji wa Mkunguwakihendo ukamilike ndani ya miezi miwili kuanzia sasa na Septemba 2024 wananchi waanze kunywa maji waliyoyasubiri kwa muda mrefu.

Mtaturu ametoa shukrani hizo Julai 29,2024,akiwa kwenye ziara katika Kata ya Kikio kwa ajili ya kutoa mrejesho wa Bunge la Bajeti 2024/2025,kuhamasisha uchaguzi wa serikali za mitaa,vijiji na vitongoji 2024 na kusikiliza kero za wananchi.

"Mradi huu umechelewa kukamilika kwa sababu mbalimbali mojawapo ikiwa ni Mkandarasi aliyepewa kazi alisuasua akaondolewa na kuamuliwa ujenzi usimamiwe na Ruwasa kwa kutumia mfumo wa Force Account, kwa sasa kazi za kujenga Pump house imekamilika,utandazaji wa mabomba kwenye DPs umekamilika ikiwemo bomba kutoka chanzo cha maji hadi kwenye tanki,".amesema.

Amesema ujenzi wa tanki unaendelea upo asilimia 25 na matarajio ni mradi ukamilike disemba 2024 ambapo kukamilika kwake kutaondoa adha ya wananchi kwenda kutafuta maji umbali mrefu.

"Tunamshukuru sana Rais Samia kwa kutenga fedha kwa ajili ya miradi ya maji kwenye jimbo la Singida Mashariki inayofikia Shilingi Bilioni 1.9,"amesema.

Meneja wa RUWASA Ikungi akisoma taarifa ya mradi huo amesema ni mradi mmojawapo kati ya miradi mingi inayotekelezwa kwenye jimbo la Singida Mashariki ambapo serikali ilitenga Shilingi Milioni 312 ili kutekeleza mradi huo.

Diwani Wa Kikio Kalebi Nkhondeya amempongeaza Mbunge Mtaturu kwa kupaza sauti bungeni na serikali kuleta fedha za miradi mingi kwenye Kata yao hususan katika sekta ya Elimu,Umeme,Maji na Miundombinu ya barabara.

Share:

WAGOMBEA URAIS WAELEZA WATAKAVYOIFANYA TLS KUWA NA NGUVU

 

Wagombea wa nafasi ya Urais katika Chama Cha Mawakili Tanganyika (TLS) wakiwa kwenye mdahalo.

Na Mwandishi Wetu

WAKATI uchaguzi wa Chama cha Mawakili Tanganyika (TLS) ukitarajiwa kufanyika Agosti 2, mwaka huu jijini Dodoma, wagombea nafasi ya Urais wamejinadi namna ya kujenga chama hicho kwenye misingi yenye nguvu ikiwamo kuondokana na vishoka katika taaluma hiyo.

Wagombea wanaowania nafasi hiyo ni Wakili Sweetbert Nkuba, Paul Kaunda, Revocatus Kuuli, Emmanuel Muga, Ibrahim Bendera na Boniface Mwabukusi.

Akizungumza juzi kwenye mdahalo wa wagombea hao jijini Dar es salaam, Mgombea wa Urais TLS, Wakili Revocatus Kuuli, alisema “Wako Mawakili vishoka ambao ni matapeli tu na kwanza huwezi kuwaita Mawakili. Matapeli wa kisheria hawatakuwepo nikiwa Rais wa TLS.”

Alisema kuwa Wakili kishoka ni kosa la jinai na vyombo vinavyoshughulika na jinai kama polisi vina wajibu wa kushughulika na watu hao.

“Kuna baadhi ya watu wanakiona chama hicho kupoteza ubora, lakini wagombea ambao tunagombea sasa tumeweka mikakati ya kukirudisha chama kuwa na nguvu na kutekeleza misingi iliyowekwa ya chama,”alisema.

Mgombea Wakili Boniface Mwabukusi alisema atarudisha taaluma ya uwakili katika misingi kwa kuwa TLS ni taasisi kongwe.

“Mimi ni simba nitakayeongoza kundi la simba na watanzania wataanza kuona uwepo wa chama hiki kwa kuwa TLS ina wajibu kwa wananchi, serikali, wanachama na utawala wa sheria na mgawanyo wa madaraka katika mhimili ya dola,”alisema.

Alisema TLS ndio kiungo wa kuifanya nchi ishamiri kiuchumi, kisiasa na kidemokrasia.

“Nataka kuleta umoja kwenye uwakili kwasasa umegawanyika, tunapokuwa na TLS yenye kuwajibika nchi zinavamiwa kiuchumi ni wajibu wa TLS kuongoza watanzania kujua ukweli wa kisheria wa mikataba ya kimataifa na sera tunazoingia, nikipewa nafasi anakwenda kubadili mfumo wa watu kufikiri TLS ni jukwaa la kutafuta mambo fulani.”

“Hatutaruhusu mawakili kunyanyasika katika taifa hili, kanuni zinazoongoza malipo kwa mawakili zinakatisha tamaa, tusipokuwa na ulinzi katika taaluma yetu hakuna aliye salama,”alisema.

Mgombea Wakili Emmanuel Muga, alisema akichaguliwa ataimarisha utawala kwa kutengeneza kamati zenye uwezo wa kufanya kazi na kuifanya TLS kufuata taratibu za kisheria na sio kuendesha mambo yake kiholela.

“Nitasimamia wajibu wa TLS kwa wanachama, serikali na kwa wananchi, na mimi sitakuwa Rais wa TLS wa kufoka foka kwa kuwa sina mamlaka yangu peke yangu ya kutoa tamko ambalo halijatokana na kamati ya uongozi wa TLS,”anasema.

Naye, Mgombea Wakili Sweetbert Nkuba alisema kama atachaguliwa kuwa Rais wa TLS atahakikisha taasisi hiyo inalinda heshima yake na kuwasambaratisha vishoka walioko kwenye kada hiyo ambao hawajasomea sheria.

Alisema atahakikisha mawakili wote wanasajiliwa na ofisi zao zitambulike kisheria ili kuwabaini mawakili wababaishaji.

“Nitaimarisha TLS tunatakiwa kuwa na nguvu na sauti moja ambayo itasaidia uimara wa chama, hivyo ni muhimu kupata viongozi makini wenye dhamira thabiti ya kusimamia chama na si ujanja ujanja,”alisema.

MAWAKILI VIJANA

Wakili Nkuba alisema akipata nafasi hiyo atahakikisha mawakili vijana chipukizi hawatozwi ada nyingi kuwa mawakili, kuwajengea weledi kwa kuwa wengi wao wanashindwa kufanya kazi zao kwa kukosa mitaji na maeneo ya kufanyia kazi.

Aidha, Mgombea Wakili Paul Kaunda alisema anataka kuwalinda na kuwatetea mawakili wachanga kwa kuwaongezea thamani na heshima ikiwamo kuanzisha Wakili APP ambayo watajisajili na itarahisisha wao kupata wateja.

Kadhalika, Mgombea Wakili Ibrahim Bendera alisema amedhamiria kuwaunganisha mawakili vijana na wale wenye uzoefu ili kuwasaidia kujijenga kitaaluma kutokana na wengi wao kushindwa kuanzisha ofisi zao kwa kukosa mitaji huku Wakili Muga akisema ataanzisha utaratibu wa kuwasaidia mawakili wachanga kwa kusimamiwa na mawakili wazoefu.

Share:

Monday 29 July 2024

NCHIMBI AWAPONGEZA MTWARA VIJIJINI UTEKELEZAJI ILANI YA CCM


Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akiambatana na Wajumbe wa Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, ameendelea na ziara yake ya mikoa miwili ya Kusini, Lindi na Mtwara leo tarehe 29 Julai 2024 amepata fursa ya kuzungumza na Wananchi wa Jimbo la Mtwara Vijijini, Kata ya Mpapura.

Akiwa hapo Mpapura, Balozi Nchimbi amesema pamoja na kwamba jimbo hilo linaongozwa na mbunge asiyekuwa wa CCM, lakini Ilani ya Uchaguzi inayotekelezwa ni ya CCM, ambapo aliwapongeza wanachama na viongozi wa CCM na wananchi, kwa kushirikiana na Serikali ya CCM, kuhakikisha ilani hiyo inatekelezwa kwa kiwango cha juu.

Ameongeza kusema kuwa hilo limefanikiwa kwa sababu Mbunge wa CCM Jimbo la Nanyamba, Mhe Abdallah Chikota anafanya kazi pia ya kuwa kaimu mbunge kuwawakilisha na kuwasemea wananchi wa Mtwara Vijijini.

“Hapa hakika kazi Imefanyika nafikiri mmeona sasa kazi kwenu wakati ukifika inadili mbadilike kwani pamoja na yote CCM inawafanyia mambo makubwa tumeyasikia hapa wenyewe sasa wakati ukifika pigeni chini wasiobadilika kichagueni Chama cha Mapinduzi.”

Mwisho amewaasa wananchi kuendelea kutunza na kulinda amani na utulivu na wasikubali kadanganywa na mtu yeyote kuhusu kuharibu tunu hiyo adhimu.

Balozi Nchimbi pia amechangia Shilingi 10 milioni kwa ajili ya kumalizia ujenzi wa Ofisi ya CCM Wilaya ya Mtwara Vijijini.

Mapema kabla, Katibu Mkuu wa CCM Balozi Nchimbi alikutana na Kamati ya Siasa ya CCM ya Mkoa wa Mtwara kwa ajili ya kikao na kupokea taarifa ya utendaji wa kazi wa CCM na utekelezaji wa Ilani ya CCM ya Uchaguzi ya Mwaka 2020 - 2025, kutoka kwa uongozi wa Chama na Serikali mkoani humo.
Share:

SERIKALI KUFADHILI MASOMO YA TEKNOLOJIA YA NYUKILIA



Na Dotto Kwilasa,Dodoma

WIZARA ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imesema Serikali imetenga bilioni 1.6 kuwekeza kwenye Sayansi na Teknolojia ya Nyuklia ili kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Hayo yameelezwa jijini hapa na Waziri wa Wizara hiyo Prof.Adolf Mkenda wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu ufadhili wa masomo ya Chuo Kikuu nje ya nchi kwa asilimia 100 kwa shahada za umahiri(MSc)katika fani za Sayansi na teknolojia ya nyukilia ambapo kiasi hicho cha fedha kimetengwa kwa jili ya ufadhili huo.

Prof.Mkenda amesema kuwa Wizara hiyo kupitia Tume ya nguvu za Atomu Tanzania (TAEC)imetangaza kutoa ufadhili kwa mwaka huu wa fedha 2024/25 wa Samia Scholarship Extended ambapo itasaidia kukidhi mahitaji makubwa ya huduma zitokanazo na Teknolojia ya nyukilia na upungufu wa wataalamu nchini.

"Wizara imebaini ongozeko kubwa la matumizi haya hasa kwenye miradi mikubwa ya madini kama vile Urani,Madini adimu na maeneo mengine ambayo yanahitaji nchi kuwa na wataalamu wa ndani na wabobezi kwelikweli,

"Tangu mwaka wa fedha 2022/23 serikali kupitia Wizaracya Elimu ilianza programu ya kutoa ufadhili kwa asilimia 100 kwa wanafunzi bora katika masomo ya sayansi kuanzia ngazi ya kidato cha sita,"amesema.

Amesema kuwa ufadhili unawalenga wanafunzi walichagua kusoma shahada ya kwanza katika masomo ya Sayansi,TEHAMA na Teknolojia, Uhandisi wa uhasibu,hisabati na elimu tiba.

"Mpaka sasa Tanzania inawataalamu sita tu wa Medical Physics pamoja na Nuclear Medical Doctors ambapo mtaalamu mmoja ni wa Radiochemistry na madaktari wawili tu wa Radio Pharmacist.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa TAEC Prof.Najat Mohamed ametaja lengo la ufadhili huo kuwa unalenga eneo la Sayansi na Teknolojia ya Nyuklia katika ,matibabu ya saratani,utafiti viwandani na mazao,nishati ya Nyuklia na utafiti wa vinu vya Nyuklia pamoja na uzalishaji wa dawa za mimea.

Ametaja sifa za waombaji wa ufadhili huo kuwa utatolewa kwa waombaji wenye sifa katika Vyuo Vikuu vinavyotambuliwa na Tume ya Vyuo Vikuu Tanazania(TCU)kwenye nchi za Australia,Austria,Ubelgiji,Canada,China,Jamhuri ya Czech,Sweden,Ufaransa,India,Korea ya Kusini,Uturuki,Urusi,Finland,Uingereza na Marekani.

Pamoja na hayo Prof.Najat alisema kuwa dirisha la maombi lipo wazi na waombaji wote wapitie tovuti ya Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia.




Share:

Sunday 28 July 2024

WANAFUNZI NAMNA PEKEE YA KUMLIPA RAIS SAMIA NI KUSOMA KWA BIDII-KATIMBA


Na Angela Msimbira, GEITA

NAIBU WAZIRI Ofisi ya Rais TAMISEMI (Elimu), Mhe. Zainab Katimba ametoa rai kwa wanafunzi wote nchini kuhakikisha wanasoma kwa bidii na kufaulu kwa viwango vya juu ili badae walitumikie taifa.

Mhe.Katimba ametoa rai hiyo alipotembelea shule mpya maalum ya wasichana ya sayansi ya Mkoa wa Geita kwa lengo la kukagua miundombinu iliyojengwa na kujionea maboresho yaliyofanywa na serikali katika ujifunzaji na ufundishaji kwenye sekta ya elimu nchini.

Amesema kuwa dhamira ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha watanzania wanapata elimu iliyobora katika mazingira mazuri hivyo ni wajibu wa wanafunzi kusoma kwa bidii ili kutimiza malengo yao.

“Namna pekee ya kumlipa Dkt, Samia Suluhu Hassan kwa kuwawezesha na kujenga miundombinu iliyobora na kuhakikisha mnapata elimu bila ada ni kuhakikisha na ninyi mnasoma kwa bidii, mfaulu vizuri na kupata elimu bora ili baadaye muweze kulitumikia taifa.”

Katimba amesema wanafunzi wanapaswa kutambua kuwa Taifa linawategemea, hivyo amewataka kuhakikisha hawafanyi mchezo wakiwa shuleni bali watumie fursa hiyo kujenga kesho yao.

Akitoa taarifa ya elimu Mkoa wa Geita, Katibu Tawala Mkoa huo, Mohamed Gombati amesema kwa upande wa shule ya sekondari ya wasichana imepokea Sh bilioni 3 katika awamu ya kwanza na Juni mwaka huu zimepokelewa Sh bilioni 1.1 kwa ajili ya kukamilisha baadhi ya majengo na tayari imeshaanza kuchukua wanafunzi.

Amesema kwa mwaka 2021/22 Mkoa wa Geita ilipokea Sh bilioni 17, mwaka 2022/23 zilipokelewa Sh bilioni 31 na kwa mwaka 2023/24 zilipokelewa Sh bilioni 32 bila kujumuisha fedha zinazotolewa kugharamia elimu bila ada.

Amesema kuwa katika fedha za ndani zinazoelekezwa kwenye miradi ya maendeleo za asilimia 60 au 40 kiwango kikubwa kinaelekezwa kwenye sekta ya elimu.

Awali, Mkuu wa Shule ya Sekondari ya wasichana ya sayansi ya Mkoa wa Geita, Mwamin Kagoma amesema shule hiyo imegharimu Sh bilioni 4 na mpaka sasa wanafunzi 172 kati ya 211 waliopangiwa kujiunga na kidato cha tano wameripoti shuleni.
Share:

Saturday 27 July 2024

SIKU YA BAHARI AFRIKA; WANAWAKE SEKTA YA BAHARI WAASWA KULINDA MAZINGIRA

Na Grace Semfuko, Maelezo.

Wanawake wanaofanya kazi katika sekta ya bahari nchini, wameungana na wanawake wenzao Duniani kuadhimisha siku ya bahari Afrika ambapo katika maadhimisho hayo wamesema ni muhimu kulinda mazingira ili kuwe na uchumi endelevu wa mazao katika sekta hiyo.

Wanawake hao leo Julai 27, 2024 wameadhimisha siku hiyo kwa kufanya usafi katika fukwe za Coco Jijini Dar es Salaam.

Mwenyekiti wa Taasisi ya Wanawake wanaofanya kazi katika sekta ya bahari (WOMESA) Bi. Fortunata Kakwaya amesema wanaunga mkono juhudu za serikali za kulinda na kuendeleza gukwe za bahari ili kuweza kuwa na uchumi wa buluu imara na endelevu.

“Kama mjuavyo, kama bahari itachafuliwa hatutakuwa na mazingira safi ya bahari, kwa maana hiyo hatutakuwa na uchumi wa buluu endelevu, na ndio maana tumekuja kusafisha hii fukwe na kutoa elimu ili jamii ione umuhimu wa kulinda mazingira ya bahari, zoezi hili pia linalenga kuunga mkono juhudi za serikali za kuhifadhi mazingira” amesema Bi Kakwaya. 

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) Bw. Nelson Mlali amesema Tanzania kama taifa la lililozungukwa na neema ya maji linafanikisha kufanya biashara ya usafirishaji na nchi zingine, hivyo kuongeza pato la taifa. 

“Tunapoadhimisha tulio hili tunafanya kumbukumbu ya utajiri tuliopewa na Mwenyezi Mungu kama Bara la Afrika, kwa hapa Tanzania tumejaaliwa kuwa na maji na fukwe ndefu, yenye kilomita Zaidi ya 1,400, kupitia maji tunapata chakula na kufanikisha shughuli zetu za kiuchumi, sasa Tanzania kama taifa la maji tunafanikisha biashara sio tu ya nchi yetu lakini pia ya nchi zingine, katika Afrika nchi kama 32 zina ukanda wa pwani, zinapakana na bahari na theluthi ya nchi hizo hazihusiani na bahari, hasara wanazopata ni pamoja na kutumia mapato yao mengi ya nchi zaidi ya asilimia 40 kwa ajili ya kufanya biashara za kimataifa kupitia njia ya maji, kwa hiyo sisi kama nchi tumejaaliwa kuziepuka gharama hizo na badala yake pesa hiyo inatumika katika mambo mengine ya kijamii” amesema Bw. Mlali.

Nae Katibu Mkuu wa Chama cha Mabaharia Tanzania (TASU), Bw.Josiah Mwakibuja, amewataka mabaharia nchini kutoa taarifa pindi wanapokutana na viashiria vya uhalifu wawapo kwenye majukumu yao.

“Baharia ni mtu ambaye ana nidhamu na welezi, ni mtu ambaye amesoma, kuna baadhi ya masomo ambayo tunafundishwa mtu aweje katika meli au kwenye jamii, hao wanaoshiriki kufanya uhalifu ni wahalifu kama wahalifu wengine, na hao hawana weledi wa kibaharia, baharia ni mtu wa heshima, natoa wito tuwe na ushirikiano na vyombo vinavyohusika na usalama wa nchi , tuwe wepesi wa kutoa taarifa kwenye vyombo vya ulinzi na usalama pale tunapoona matukio ya uhalifu” amesema Bw. Mwakibuja.

Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger