Monday, 27 April 2026

WENZA WA MAJAJI WAWAFARIJI WAGONJWA WA SARATANI DAR


NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

Kikundi cha We Are Family kinachowahusisha wenza wa majaji nchini, kimetembelea wagonjwa wa saratani katika Ocean Road Cancer Institute jijini Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa dhamira yao ya kufanya matendo ya huruma kwa jamii.

Kikundi hicho chenye wanachama 59 waliosajiliwa, kimeeleza kuwa pamoja na shughuli nyingine, pia kinalenga kuwafikia wenza wa majaji wastaafu na waliopo kazini kwa lengo la kuimarisha mshikamano na kusaidiana katika masuala ya kijamii.

Akizungumza Aprili 26, 2026, Makamu Mwenyekiti wa kikundi hicho, Edivije Nangela, amesema uamuzi wa kutembelea wagonjwa wa saratani ulifikiwa baada ya kufanya tathmini na kufuata taratibu zote muhimu zilizowezesha kuwafikia wahitaji hao.

Amebainisha kuwa, licha ya kulenga kuwafikia wagonjwa 100, wamefanikiwa kuwafikia wagonjwa 39 pekee, hali inayodhihirisha ukubwa wa uhitaji uliopo pamoja na changamoto ya gharama kubwa za matibabu.

“Uhitaji ni mkubwa sana na gharama za matibabu ni kubwa, hivyo kuna umuhimu wa kuendelea kuweka mikakati ya kuwafikia watu wengi zaidi,” amesema Nangela.

Ameongeza kuwa kikundi hicho kinatarajia kufanya kikao maalum kitakacholenga kuweka mikakati endelevu ya kusaidia makundi mbalimbali yenye uhitaji katika jamii.

Kwa upande wake, Mratibu wa Matukio wa kikundi hicho, Beatrice Mdemu, amesema zoezi hilo litakuwa endelevu na kuwahimiza wenza wengine wa majaji kujiunga na kikundi hicho ili kuongeza nguvu katika kufanikisha malengo yao ya kijamii.

Naye Afisa wa Ocean Road Cancer Institute, Karafuu Ally, kwa niaba ya uongozi wa taasisi hiyo, amekishukuru kikundi hicho kwa kutembelea wagonjwa na kutoa faraja, akisisitiza umuhimu wa kuendeleza moyo wa kujitolea kwa jamii.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMATATU APRILI 27,2026

Magazeti


















Share:

Sunday, 26 April 2026

WATANZANIA WATAKIWA KUENZI MISINGI YA MUUNGANO


Katika kuadhimisha miaka 62 ya Muungano wa Tanzania, Mkurugenzi Mkuu wa Kituo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Binafsi (PPPC), David Kafulila, amesema mafanikio ya Muungano huo yanatokana zaidi na mshikamano wa watu kuliko mifumo ya kiserikali.

Ameeleza kuwa Muungano wa Tanzania ni wa kipekee barani Afrika kwa kudumu kwa zaidi ya miongo sita, tofauti na miungano mingine iliyoshindwa kuhimili misukosuko ya kisiasa na kijamii ndani ya muda mfupi.

“Wetu ni muungano wa watu zaidi ya serikali. Ni miaka 62 sasa, na huu ndio Muungano pekee wa mataifa mawili huru barani Afrika uliofanikiwa kudumu kwa muda mrefu kiasi hiki,” amesema Kafulila.

Alifafanua kuwa mifano ya miungano iliyovunjika ni pamoja na ule wa Ethiopia na Eritrea uliodumu kati ya mwaka 1952 hadi 1962, pamoja na muungano wa Ghana, Guinea na Mali (1958–1963), na ule wa Senegambia (1982–1989), ambayo yote ilidumu kwa muda mfupi kabla ya kuvunjika.

Kwa mujibu wa Kafulila, siri ya uimara wa Muungano wa Tanzania ipo katika misingi yake ya kijamii na kitamaduni, ikiwemo udugu wa kihistoria, matumizi ya lugha ya Kiswahili na mshikamano wa watu wake.

Aidha, aliwataka Watanzania kuendelea kuthamini na kuuenzi Muungano huo kwa kuzingatia misingi iliyoasisiwa na viongozi wa awali, akiwemo Julius Nyerere na Abeid Karume.

Kauli hiyo imekuja wakati Watanzania wakiendelea kuadhimisha miaka 62 ya Muungano, wakitafakari mafanikio, changamoto na mustakabali wa ushirikiano huo wa kihistoria.
Share:

TAIFA GESI YATOA ELIMU YA MATUMIZI SALAMA YA GESI NJOMBE






Na Mwandishi Wetu

Kampuni ya Taifa Gesi imeendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi sahihi na salama ya gesi, sambamba na kuhamasisha usalama mahali pa kazi katika maadhimisho ya Wiki ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi Duniani.

Akizungumza katika viwanja vya Shule ya Msingi Mji Mwema, Njombe, Mtaalamu wa Masuala ya Afya, Mazingira, Usalama na Ulinzi Mahali pa Kazi kutoka Taifa Gesi, Aurelius Marcus Mdemu, alisema kampuni hiyo imeshiriki maadhimisho hayo yanayoanza Aprili 24 hadi 29, 2026 kwa lengo la kutoa elimu kwa wateja na jamii kwa ujumla.




Alisema kupitia banda lao, wanaonesha vifaa mbalimbali vinavyotumika kazini ili kuimarisha usalama wa wafanyakazi, pamoja na kutoa elimu kuhusu matumizi sahihi ya gesi na faida zake. Aidha, alieleza kuwa wanajitahidi kuondoa hofu na dhana potofu zilizopo miongoni mwa watumiaji wa gesi.

“Tunawaonesha wananchi namna Taifa Gesi inavyoweka kipaumbele kwenye usalama wa wafanyakazi, ikiwa ni pamoja na matumizi ya vifaa kinga vinavyotakiwa kutumika muda wote wakiwa kazini,” alisema Mdemu.








Kwa upande wake, Afisa Masoko wa Chapa wa Taifa Gesi, Santina Ngaponda, alisema maonyesho hayo yameandaliwa na OSHA, yalianza Aprili 24 na yanatarajiwa kufikia kilele chake Aprili 29 mwaka huu.

Ngaponda aliwahimiza wakazi wa Njombe na maeneo ya jirani kutembelea banda la Taifa Gesi ili kupata elimu kutoka kwa wataalamu wa usalama, kujifunza matumizi sahihi ya gesi, pamoja na kuona vifaa vya usalama vinavyotumika kazini na umuhimu wake.


Aidha, aliongeza kuwa kampuni hiyo inatoa punguzo maalum la bei ya gesi na vifaa vyake, pamoja na zawadi mbalimbali kwa wateja watakaotembelea banda hilo.


Naye Meneja Mauzo wa Kanda ya Nyasa wa Taifa Gesi, Arnold Salewa, alisema wanaendelea kutumia maonyesho hayo kutoa elimu kuhusu matumizi sahihi ya nishati safi pamoja na kuuza bidhaa zao kwa bei ya promosheni.

Alisema kanda hiyo inajumuisha mikoa ya Njombe, Iringa na Ruvuma, na kwamba pia wanatoa fursa kwa wananchi wanaotaka kuwa mawakala wao, kwa kuwapatia elimu ya biashara na usimamizi salama wa mitungi ya gesi.

Salewa alisisitiza kuwa Taifa Gesi ipo mstari wa mbele kuhakikisha kaya, migahawa na taasisi mbalimbali zinaanza kutumia nishati safi ya kupikia kwa gharama nafuu, ili kupunguza athari za matumizi ya mkaa na kuni kwa mazingira na afya za Watanzania.

Aliongeza kuwa mwitikio wa wananchi umekuwa mkubwa, huku Taifa Gesi ikiendelea kuwa chaguo sahihi kwa watumiaji wengi nchini.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMAPILI APRILI 26,2026

Magazeti






 
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger