Monday, 6 July 2026

FCC YATUMIA MAONESHO SABASABA KUKUZA ELIMU YA BIASHARA


NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

WAFANYABIASHARA na wananchi kwa ujumla wametakiwa kutumia Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) kutembelea banda la Tume ya Ushindani (FCC) ili kupata huduma mbalimbali za papo kwa papo pamoja na elimu kuhusu ulinzi wa mlaji, ushindani wa biashara na udhibiti wa bidhaa bandia.

Wito huo umetolewa leo Julai 6, 2026 na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Mahusiano kwa Umma wa FCC, Roberta Feruzi, ambapo ameongeza kuwa maonesho hayo yameipa tume hiyo fursa ya kuwafikia wananchi wengi zaidi na kuwaelimisha kuhusu haki zao pamoja na huduma zinazotolewa na taasisi hiyo.

Amesema mbali na kutoa elimu, FCC pia inatoa huduma za moja kwa moja kwa wananchi wanaotembelea banda lake, ikiwemo kupokea na kushughulikia malalamiko, usajili wa mikataba na huduma nyingine zinazotolewa na tume hiyo.

"Tunawaalika wananchi wote kufika katika banda la Wizara ya Viwanda na Biashara, ambalo ni banda jumuishi lenye taasisi zote zilizo chini ya wizara hiyo, ikiwemo FCC, ili wapate huduma na elimu kuhusu masuala ya ushindani, ulinzi wa mlaji na udhibiti wa bidhaa bandia," amesema.

Amebainisha kuwa FCC haijajikita kutoa huduma ndani ya banda pekee, bali imeandaa programu ya kuwafuata wafanyabiashara na wajasiriamali katika maeneo mbalimbali ndani ya viwanja vya Sabasaba kwa lengo la kuhakikisha elimu inawafikia wadau wengi zaidi.

Amesemakuwa FCC imekuwa ikiendesha semina kwa makundi mbalimbali ya wafanyabiashara, ikiwapa mafunzo kuhusu sheria za ushindani, namna ya kufanya biashara kwa kuzingatia misingi ya ushindani wa haki pamoja na wajibu wao katika kulinda maslahi ya walaji.

Amesema tangu kuanza kwa maonesho hayo, FCC imefanikiwa kuwafikia zaidi ya wajasiriamali 700, wakiwemo wazalishaji wadogo na wa kati, ambao wamepatiwa elimu kuhusu namna ya kulinda alama na nembo za biashara zao, kuendeleza ubunifu na kuongeza ushindani katika soko.

Aidha, amesema taasisi hiyo inaendelea kuwalea vijana wabunifu wanaoshiriki maoneshoni kwa kuwapatia mwongozo wa namna ya kukuza biashara zao katika mazingira ya ushindani wa haki.

Amesisitiza kuwa kampeni ya utoaji elimu haitakoma baada ya kumalizika kwa maonesho ya Sabasaba, bali itaendelea kupitia ofisi za FCC zilizopo Dar es Salaam na ofisi za kanda za Mwanza, Arusha, Mbeya na Dodoma.

Ameongeza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayolenga kujenga uchumi jumuishi kwa kuweka mazingira bora ya biashara, huku FCC ikiendelea kuwa mlezi, mwezeshaji na mdhibiti wa ushindani wa haki nchini.

Amewahimiza wafanyabiashara, wabunifu na wananchi ambao hawajapata nafasi ya kushiriki maonesho hayo kufika katika ofisi za FCC zilizo karibu nao ili kupata elimu, ushauri na huduma mbalimbali zinazotolewa na tume hiyo kwa maendeleo ya biashara zao.
Share:

Breaking : HAYA HAPA MATOKEO YA MTIHANI WA KIDATO CHA SITA (ACSEE) 2026, UALIMU 2026



Baraza la Mitihani la Tanzania (NECTA) limetangaza matokeo ya Mtihani wa Kidato cha Sita 2026, yakionyesha ongezeko la ufaulu ambapo asilimia 99.92 ya watahiniwa wa shule wamefaulu.

Katibu Mtendaji wa NECTA, Profesa Said Ally Mohamed, amesema watahiniwa 125,056 kati ya 125,320 waliopata matokeo wamefaulu kwa madaraja ya Kwanza hadi Nne. Idadi ya waliopata Daraja la Kwanza imeongezeka kutoka 61,020 mwaka 2025 hadi 67,606 mwaka 2026.

Aidha, zaidi ya asilimia 99.6 ya watahiniwa walipata madaraja ya Kwanza, Pili na Tatu, huku karibu masomo yote yakirekodi ufaulu wa zaidi ya asilimia 93. Pia, hakuna shule iliyopata wastani wa Daraja F mwaka huu.










Share:

Video Mpya : LIMBU LUCHAGULA Ft. SUZY NDATULU - NG'WANIKUMBULA


Msanii wa muziki wa asili Limbu Luchagula ameachia rasmi video ya wimbo wake mpya "Ng'wanikumbula", akimshirikisha Suzy Ndatulu.

Video hiyo ya ubora wa 4K imeongozwa na Director Migera na sasa inapatikana kupitia YouTube pamoja na majukwaa mengine ya kidijitali. 

Limbu amewaomba mashabiki kuendelea kuisapoti kazi hiyo kwa kuitazama, kuishirikisha na kutoa maoni yao.
Share:

RAIS MWINYI ATOA MILIONI 200 KUSAIDIA KITUO CHA IRSHAAD LUSHOTO, ARIDHIA OMBI LA PROF. SHEMDOE



Na OWM - TAMISEMI, Lushoto

Mhe. Alhaji Dkt. Hussein Mwinyi, Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar,  amekubali ombi la Mbunge wa Jimbo la Lushoto Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kwa kutoa mchango wa Shilingi Milioni 200 kwa ajili ya kuendeleza Kituo cha Elimu ya Kiislamu Irshaad (Irshaad Islamic Centre) kilichopo Lushoto, mkoani Tanga.

Fedha hizo zinatarajiwa kuwezesha utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo katika kituo hicho, ikiwemo kuboresha Chuo cha Ufundi, kuanzisha bustani ya kisasa, kujenga madrasa yenye kukidhi mahitaji ya wanafunzi, kujenga nyumba za walimu, jengo la kupokelea wageni, hospitali pamoja na ukumbi wa kisasa wa kufanyia shughuli mbalimbali za kielimu na kijamii.

Prof. Shemdoe alitoa ombi hilo Julai 5, 2026 wakati wa Sherehe ya Maulidi ya Kumswalia Mtume Muhammad S.A.W iliyoandaliwa na Sheikh Sharrif Hussein Ahmad Badawiyy wa Kituo cha Irshaad Islamic Centre Lushoto, ambapo Mgeni Rasmi alikuwa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi.

Katika hatua nyingine, Mhe. Rais Dkt. Hussein Mwinyi amekubali ombi la Rais wa Kituo cha Irshaad Islamic Centre Lushoto Sheikh Sharrif Hussein Ahmad Badawiyy la kumwomba awe mlezi wa kituo hicho, ambapo Mhe. Dkt. Dkt. Hussein Mwinyi ameahidi kuendelea kushirikiana na viongozi pamoja na wadau mbalimbali katika kukiendeleza ili kiwe kitovu cha utoaji wa elimu bora na maadili mema.

Sanjari na hilo, Mhe. Rais Dkt.  Mwinyi ameridhia pia ombi la Rais wa Kituo hicho cha Irshaad Islamic Centre la kumtaka kuridhia jina la Hayati Alhaji Ali Hassan Mwinyi, litumike katika eneo la bustani linalotarajiwa kujengwa katika Chuo cha Ufundi kilichopo ndani ya kituo hicho, ikiwa ni sehemu ya kumuenzi na kutambua mchango wa maendeleo alioutoa Hayati Alhaji Ali Hassan Mwinyi akiwa ni mlezi wa kituo hicho. 

Mhe. Prof. Shemdoe alimuunga mkono Mhe. Rais Dkt. Hussein Mwinyi kwa kuchangia Shilingi Milioni 20, Mkuu wa Mkoa wa Tanga Dkt. Batilda Burian  Milioni 5, Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Adam Malima Milioni 5, Mbunge wa Bumbuli Mhe. Mhandisi Ramadhani Hamza Milioni 5, Mwenyekiti wa CCM Mkoa Bw. Rajab Abdallah Milioni 3 na Mbunge wa Afrika Mashariki Mhe. Dkt. Abdullah Makame amechanga Milioni 5 na kufanya jumla ya fedha zilichangwa kuwa Milioni 248, hatua iliyoonyesha mshikamano wa viongozi hao katika kuunga mkono maendeleo ya elimu na ustawi wa jamii. 

Akizungumza mara baada ya hafla hiyo, Mhe. Prof. Shemdoe amemshukuru Mhe. Rais Dkt. Mwinyi kwa kukubali ombi hilo, akieleza kuwa msaada huo utakuwa chachu ya kuinua viwango vya elimu, ustawi wa jamii na huduma zinazotolewa katika kituo hicho, ambacho kimeendelea kuwa nguzo muhimu ya malezi na elimu kwa vijana wa Lushoto na maeneo jirani.

Aidha, Wananchi na viongozi waliohudhuria hafla hiyo wamempongeza Mhe. Rais Dkt. Mwinyi kwa kukubali maombi yaliyowasilishwa na Mhe. Prof. Shemdoe, wakieleza kuwa uamuzi huo utaacha alama ya kudumu katika maendeleo ya Kituo cha Elimu ya Kiislamu Irshad Lushoto na kuongeza fursa za elimu, ujuzi na huduma za kijamii kwa vizazi vya sasa na vijavyo.












Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMATATU JULAI 6,2026

Magazeti


 




Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger