Saturday, 9 May 2026

VIJANA IRINGA WAHIMIZWA KUTUMIA TEKNOLOJIA NA UBUNIFU KUJIKWAMUA KIUCHUMI


Mkuu wa Mkoa wa Iringa mheshimiwa Khery James wa kwanza kutoka kushoto akikata utepe kabla ya kuzungumza na wafanyabiashara na wajasiriamali katika ukumbi wa Gentle Hills Hotel uliopo Manispaa ya Iringa Mkoani Iringa
Mkuu wa Mkoa wa Iringa mheshimiwa Khery James akisalimiana na meneja wa taasisi ya Zidiup Mentorship John Waryuba wakati alipowasili katika ukumbi wa Gentle Hills Hotel Manispaa ya Iringa 
Meneja wa taasisi ya Zidiup Mentorship John Waryuba Akizungumza na wafanyabiashara na wajasiriamali kutoka maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Iringa wakati wa kongamano hilo kubwa la wafanyabiashara na wajasiriamali ukumbi wa Gentle Hills Hotel 

 Regina Ndumbaro-Iringa 


Kongamano kubwa la
wafanyabiashara na wajasiriamali kutoka maeneo mbalimbali ya mkoa wa Iringa na wilaya zake limefanyika kwa mafanikio makubwa katikq ukumbi wa Gentle Hills Hotel tarehe 8 april 2026 chini ya uratibu wa programu ya Zidiup Mentorship, likiongozwa na Meneja wake, John Waryuba, huku mgeni rasmi akiwa Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Khery James. 


Kongamano hilo limewakutanisha wafanyabiashara wakubwa, wajasiriamali wadogo pamoja na vijana waliopata nafasi ya kuuliza maswali kuhusu biashara, mikopo, teknolojia na maendeleo ya kiuchumi, ambapo viongozi na wataalamu walitoa majibu papo kwa papo mbele ya washiriki waliojitokeza kwa wingi.


Akizungumza katika kongamano hilo Mkuu wa  Mkoa wa Iringa mheshimiwa Khery James ameipongeza Zidiup Mentorship kwa juhudi zake za kulea vipaji na kuwawezesha vijana kujitambua kupitia ubunifu na matumizi ya teknolojia. 


Amesema vijana wa Tanzania wana uwezo mkubwa wa kufanya mambo makubwa ikiwa watapata majukwaa sahihi ya kuonesha vipaji vyao. 


Mkuu huyo wa mkoa amefananisha maisha na maji yenye ladha inayotegemea maamuzi ya mtu mwenyewe, akisisitiza kuwa vijana wanapaswa kuwa na mtazamo chanya na kuamini kuwa changamoto zinaweza kuwa fursa za mafanikio iwapo wataamua kuzitazama kwa mtazamo wa maendeleo.


Katika hotuba yake Mkuu wa Mkoa Khery James amewahamasisha vijana kutumia teknolojia na mitandao ya kijamii kama nyenzo ya kujiletea maendeleo badala ya kuikimbia. 


Amesema dunia ya sasa imebadilika na teknolojia imegusa kila sekta ikiwemo biashara, elimu, mawasiliano na uzalishaji, hivyo vijana wanapaswa kuitumia kimkakati ili kujitangaza na kuongeza kipato chao. 


Ametoa mifano ya wafanyabiashara wanaouza bidhaa kupitia mitandao na kuwafikia watu wengi zaidi kwa muda mfupi, huku akieleza kuwa viongozi wa kisasa hutumia mitandao ya kijamii kusikiliza na kufahamu changamoto za wananchi. 


Aidha amempongeza kijana Kelvin anayejishughulisha na ushonaji wa mabegi aliyegunduliwa kupitia Zidiup Mentorship, akisema hiyo ni ishara kuwa teknolojia inaweza kuwa daraja la mafanikio kwa vijana wengi.


Mbali na hilo, Mkuu huyo wa Mkoa amewataka vijana wa Iringa kutumia rasilimali zilizopo mkoani humo kuongeza thamani ya bidhaa na kukuza uchumi wa mkoa. 


Amesema Iringa ina fursa kubwa katika utalii kupitia Hifadhi ya Taifa ya Ruaha, biashara ya mazao, usafirishaji na bidhaa za misitu, hivyo vijana wanapaswa kuwekeza katika ubunifu badala ya kuuza malighafi pekee. 


Amesisitiza umuhimu wa kuongeza thamani ya mazao na mbao kwa kutengeneza bidhaa kama fenicha bora zitakazoongeza ajira na mapato kwa vijana wengi zaidi. 


Pia ameahidi kuendelea kuwaunga mkono vijana kupitia mikopo, ubunifu, sayansi na teknolojia ili kuhakikisha wanapata nafasi ya kufikia ndoto zao za maendeleo.


Kwa upande wake, Meneja wa Zidiup Mentorship John Waryuba amemshukuru Mkuu wa Mkoa kwa kukubali kushiriki katika kongamano hilo na kwa namna anavyoendelea kuwa karibu na vijana wa Iringa. 


Waryuba amewahamasisha vijana na wajasiriamali wadogo kuanza biashara kwa kutumia mtaji mdogo walionao badala ya kusubiri mazingira makubwa, akisema mafanikio huanza na hatua ndogo. 


Amesema kongamano hilo limekuwa jukwaa muhimu la kuwaunganisha vijana, wafanyabiashara na viongozi wa serikali kwa lengo la kujenga uchumi imara wa mkoa wa Iringa na kuwapa vijana matumaini mapya ya kujitegemea kupitia biashara, ubunifu na teknolojia



Share:

Friday, 8 May 2026

WAZIRI KAPINGA AKABIDHI MAGARI 11 TBS, KUIMARISHA UTEKELEZAJI WA MAJUKUMU


NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga, amelielekeza Shirika la Viwango Tanzania (TBS) kuhakikisha linalinda na kuthamini rasilimali za taasisi ili kuongeza ubora na ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wananchi.

Waziri Kapinga ametoa kauli hiyo Mei 8, 2026 jijini Dar es Salaam wakati akikabidhi magari mapya 11 kwa TBS, ambapo alisisitiza umuhimu wa kuyatumia kwa shughuli rasmi za ofisi ili kuimarisha utekelezaji wa majukumu ya shirika hilo.

Alisema ubora wa huduma unaotolewa na taasisi yoyote unategemea mazingira bora ya kazi pamoja na ufanisi wa watumishi katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku.

“Ubora tunaouzungumzia unajengwa na ufanisi katika kazi. Ili kufikia ufanisi huo ni lazima kujenga mazingira yanayowezesha watumishi kufanya kazi kwa weledi na tija, hatimaye kufanikisha lengo kuu la taasisi ambalo ni kuhakikisha ubora,” amesema Waziri Kapinga.

Aidha, alimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kuiwezesha wizara na taasisi zake kupitia utoaji wa bajeti na fedha zinazowasaidia kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa TBS, Dk. Ashura Katunzi, amesema magari hayo yataongeza ufanisi wa kazi na kurahisisha utekelezaji wa majukumu ya shirika hilo katika kusimamia viwango nchini.

Dk. Katunzi amesema awamu ya kwanza taasisi hiyo ilipokea magari matano, huku awamu ya pili ikihusisha magari 11 yaliyokabidhiwa sasa, hatua ambayo itaongeza uwezo wa TBS kuwafikia wadau na kutoa huduma kwa ufanisi zaidi.

Share:

WAZIRI MKUU ATAKA WATENDAJI SERIKALINI KUTUMIA USHAWISHI KUVUTIA WAWEKEZAJI


Waziri Mkuu Dkt Mwigulu Nchemba amewataka watendaji katika taasisi na mamlaka za Serikali wawe tayari kuwawezesha wawekezaji badala ya kuwadhibiti ili wavutiwe kuwekeza zaidi na zaidi.



“Nitoe wito kwa taasisi na mamlaka za Serikali, tumieni muda mwingi kuwawezesha wawekezaji badala ya kuwadhibiti. Washawishini waongeze uwekezaji badala ya kuwafanya waonekane wanaomba. Tumieni vivutio zaidi ili washawishike zaidi na zaidi,” amesema.


Ametoa wito huo leo (Ijumaa, Mei 8, 2026) wakati akizungumza na wadau waliohudhuria uzinduzi wa hoteli ya Mikumi Wildlife katika Hifadhi ya Taifa ya Mikumi, wilayani Kilosa, mkoani Morogoro.


Amesema hoteli hiyo ambayo zamani ilikuwa inamilikiwa na serikali lakini ikapata janga la kuungua moto, ina historia ya miaka mingi; na ana imani na uwekezaji uliofanyika kwani umesaidia kuongeza ajira na kipato kwa wananchi.


“Sina shaka uwekezaji huu utaongeza mvuto kutokana na viwango vilivyopo kwenye hoteli hii. Viwango vya hoteli hii ni vya juu sana, ninaamini vitasaidia kuongeza muda wa watalii kukaa ndani ya hifadhi na uwepo wa malazi mazuri pia utaongeza idadi ya watalii,” amesema.


Akielezea juhudi za serikali kuboresha hifadhi ya Mikumi, Waziri Mkuu amesema Serikali imetoa sh. bilioni 35 za kuboresha uwanja wa ndege wa Kikoboga na ifikapo Oktoba mwaka huu, utakuwa umekamilika.


Amezitaka Wizara ya Maliasili na Utalii, TANAPA washirikiane na mamlaka nyingine za Serikali na kutumia fursa ya stesheni ya Kilosa ili kufungua njia na kuboresha miundombinu itakayorahisisha watalii kuingia katika Hifadhi ya Mikumi na hivyo kuongeza idadi ya watalii.


Ameitaka Wizara ya Maliasili na Utalii iendelee kubuni mikakati ya kwa kuhamasisha sekta binafsi iwekeza katika maeneo ya utalii huku akizitaka taasisi zote za umma ikiwa ni pamoja na mikoa yenye maeneo yaliyo na fursa za utalii ziendelee kuboresha mazingira ya uwekezaji ili kuvutia wawekezaji wengi zaidi. “Suala hili litekelezwe sambamba na kutangaza vivutio vilivyopo.”


Waziri Mkuu amewataka wadau wa utalii waweke mipango ya kuendeleza mazao mapya ya utalii yatakayochochea ongezeko la watalii na kuwahamasisha kuchagua kutembelea vivutio vilivyopo katika Kanda ya Utalii Kusini.


Ametumia fursa hiyo kumwelekeza Waziri wa Maliasili na Utalii aangalie namna ya kuongeza programu za utalii kwenye Chuo cha Ufundi (VETA) kilichopo Mikumi. “Waziri wa Utalii tuongeze programu nyingi za utalii ili vijana wa hapa wanufaike na rasilimali zilizopo katika eneo lao. Kwa maono ya Mheshimiwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, alitaka hivi vyuo vinapojengwa viweke programu kulingana na shughuli za kiuchumi za eneo husika kama vile utalii, uvuvi ili viwasaidie vijana wa maeneo husika.”


Mapema, akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na washiriki wa hafla hiyo, Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji alisema miaka ya nyuma hifadhi ya Mikumi ilikuwa ikipokea watalii 60,000 kwa mwaka lakini mwaka jana idadi ya watalii iliongezeka sana kufikia 174,808.


“Mapato yanayotokana na utalii yalikuwa sh. milioni 2.5 lakini nayo kwa mwaka jana yaliongezeka na kufikia sh.milioni 9.81. Hadi kufikia tarehe 31 Machi, 2026 idadi ya watalii waliofika kwenye hifadhi ya Taifa ya Mikumi walikuwa 151,275 na mapato yaliyokusanywa yalikuwa yamefikia sh. milioni 10.12,” alisema.


Alisema tayari sh. bilioni nne za kujenga geti upande wa Kilosa zimeshatolewa na ziko hifadhini tayari kuanza kazi hiyo ambapo mtu akishuka Kilosa kwa treni ya SGR atatumia dk.20 tu kuingia hifadhini.


Naye Bw. Simon Nguka, akisoma taarifa kuhusu mradi huo, alisema ujenzi na ukarabati wa hoteli hiyo yenye vyumba 48 na ambayo inamilikiwa na Watanzania kwa asilimia 100, umetumia sh. bilioni 26.8.


Alisema mradi huo ni miongoni mwa miradi 24 waliyonayo. Wellworth Group inamiliki mahoteli, loji, resorts na kambi za kitalii zenye uwekezaji wa thamani ya sh. bilioni 640.




Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO IJUMAA MEI 8,2026



magazeti






















Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger