


Meli hiyo, ambayo sasa ndiyo mfalme wa maji katika Ukanda wa Maziwa Makuu, si chombo cha usafiri tu, bali ni kiunganishi kikuu cha biashara kati ya mikoa ya Kanda ya Ziwa na nchi jirani za Uganda na Kenya.
Uwezo wa Kipekee
Kwa mara ya kwanza baada ya kipindi kirefu cha "ukame" wa vyombo vikubwa, MV New Mwanza inakuja na uwezo mkubwa wa kubeba abiria na mizigo. Ikiwa na uwezo wa kubeba abiria 1,200 inapunguza msongamano na gharama kubwa za usafiri wa barabara.
Kwenye suala la mizigo ambapo ndipo penye moyo wa biashara, meli hii ina uwezo wa kubeba tani 400 za bidhaa kwa wakati mmoja, jambo ambalo litaleta mapinduzi ya bei za bidhaa sokoni. Aidha ina uwezo wa kubeba magari madogo 20 na makubwa (malori) 3 .
Manufaa ya Kiuchumi
Kukosekana kwa meli ya uhakika kwa miaka mingi kuliathiri vibaya mabadilishano ya bidhaa. Sasa, kwa safari ya saa 6 hadi 7 pekee wakulima wa kahawa, ndizi, na mazao mengine ya chakula kutoka mkoani Kagera sasa wanakuwa na soko la uhakika jijini Mwanza na mikoa mingine. Bidhaa hizi zitafika zikiwa bado mbichi na kwa gharama nafuu ya usafirishaji.Wakati huo huo wafanyabiashara wa Mwanza sasa wanaweza kusafirisha bidhaa za viwandani, vifaa vya ujenzi, na samaki kwenda Bukoba na maeneo ya pembezoni mwa ziwa kwa urahisi zaidi.
Ongezeko la uwezo wa kubeba mizigo mikubwa kutaondoa gharama za ziada za usafirishaji zinazosababishwa na malori, hivyo kupelekea bei za bidhaa kupungua kwa mlaji wa mwisho.
Usalama na Utimamu wa Biashara
Mkurugenzi Mtendaji wa TASHICO, Eric Hamisi, amebainisha kuwa meli hiyo imetengenezwa kwa teknolojia ya kisasa inayohakikisha usalama wa watu na mali zao. Uwepo wa madaraja mbalimbali, ikiwemo daraja la biashara na VIP, unatoa fursa kwa wafanyabiashara kufanya safari zao kwa faraja huku wakiratibu mipango yao ya kibiashara.
Kwa wakazi wa kandoni mwa Ziwa Victoria, MV New Mwanza si tu fahari ya kitaifa, bali ni injini ya kukuza kipato, kutoa ajira, na kufungua fursa za kitalii ambazo zilikuwa zimefifia. Huu ni mwanzo wa zama mpya ambapo biashara itashamiri na uchumi wa kaya utaimarika kupitia maji ya ziwa hilo kuu.



Katika ulimwengu wa sasa unaotawaliwa na ushindani mkali wa kidiplomasia na kiuchumi, Tanzania na mataifa mengine ya Afrika yanapita katika kipindi cha kihistoria kinachohitaji mabadiliko makubwa ya kifikra ili kulinda rasilimali na mustakabali wa vizazi vijavyo. Kupitia mjadala mzito uliofanyika hivi karibuni, wasomi na viongozi wabobezi nchini wakiongozwa na Profesa wa Uchumi, Samuel Wangwe, Kanali Mstaafu Joseph Simbakalia na mwanasiasa mkongwe Hamad Rashid Mohammed, wametoa msisitizo ambao unapaswa kuwa dira ya maendeleo ya taifa letu.
Hoja kuu inayopaswa kueleweka kwa kila mwananchi ni kuwa maslahi ya kitaifa ni kitu kitakatifu ambacho hakipaswi kuchezewa au kuamuliwa kwa misingi ya itikadi za vyama vya siasa, ukabila wala dini, bali kwa kuangalia faida ya muda mrefu ya taifa zima.
Profesa Samuel Wangwe ameweka wazi kuwa taifa linalolenga maendeleo ya kweli ni lile ambalo wananchi wake wanaunganishwa na msimamo mmoja wa kizalendo, hususan katika usimamizi wa rasilimali.
Ili kufikia hatua hii, kuna haja kubwa ya kuongeza thamani ya rasilimali zetu badala ya kuziuza kama malighafi pekee, jambo ambalo linawezekana tu kwa kuwekeza kwa vijana kupitia teknolojia. Profesa Wangwe anazitaja nchi za India, China na Malaysia kama mifano ya kuigwa kwani zimepiga hatua kwa kuwapeleka vijana wao kujifunza nje ya nchi na kurudi kukuza uchumi wa viwanda wa ndani. Hii ina maana kuwa ufunguo wa utajiri wa Tanzania haupo tu kwenye madini au ardhi, bali upo kwenye akili za vijana walioandaliwa kiteknolojia kuongoza mageuzi ya kiuchumi.
Ukombozi wa kifikra ni nguzo nyingine muhimu iliyosisitizwa na Kanali Mstaafu Joseph Simbakalia, ambaye amewataka Waafrika kuacha kutegemea mataifa ya Magharibi kuamua mustakabali wao.
Simbakalia anafafanua kuwa kudhani kuwa mataifa ya nje yana mamlaka ya mwisho juu ya matumizi ya rasilimali zetu ni aina ya utumwa wa kifikra unaorudisha nyuma maendeleo. Ili Afrika iweze kujenga uchumi imara, viongozi wanapaswa kutanguliza uadilifu na kuwajibika kwa wananchi bila kuathiriwa na shinikizo za nje au migogoro ya kikanda inayochelewesha umoja.
Hoja ya utambulisho na utamaduni imeguswa kwa uzito na Hamad Rashid Mohammed, ambaye anakumbusha kuwa ukoloni haukuishia tu kwenye utumwa wa kimwili bali uliingia kwenye mioyo ya Waafrika kwa kuwafanya wadharau tamaduni zao. Siasa za kimataifa kwa sasa zinatumia taasisi za kifedha kama mbinu mpya ya utawala, jambo ambalo linaweza kupingwa tu ikiwa tutaimarisha utamaduni wetu wa kupendana, kusikilizana na kudhibiti rasilimali zetu wenyewe.
Mkakati wa kuelimishana juu ya umuhimu wa kujitambua kama Waafrika ndio utakaotuwezesha kusimamia maendeleo yetu bila kuyumbishwa na misaada yenye masharti magumu yanayominya uhuru wetu wa kiuchumi.
Ujumbe huu wa pamoja kutoka kwa wabobezi hawa unatoa funzo kubwa kwa vijana, wafanyakazi na wafanyabiashara nchini Tanzania kuwa maendeleo ya nchi ni jukumu la pamoja. Serikali ya Awamu ya Sita tayari imeanza kutekeleza misingi hii kwa kufungua fursa za kibiashara na mataifa makubwa kama Marekani huku ikisisitiza tija na ajira kwa wazawa. Ni wajibu wa kila mwananchi kuelewa kuwa tunapozungumzia uwekezaji katika madini ya kimkakati au mikopo ya halmashauri kwa vijana, tunazungumzia utekelezaji wa maslahi ya taifa kwa vitendo. Maamuzi yoyote tunayoyafanya leo katika ngazi ya familia, halmashauri au serikali kuu lazima yapimwe kwa mizani ya kama yanajenga au yanabomoa umoja na utajiri wetu wa pamoja kama taifa.