Monday, 11 May 2026

JANI LA “SALE” LINAVYOTAJWA KUCHOCHEA UKATILI WA KIJINSIA KILIMANJARO

 

Na Deogratius Temba

Matumizi ya jani la “sale” katika jamii ya Wachaga mkoani Kilimanjaro yameendelea kutajwa kuwa moja ya mila zinazochochea na kuficha vitendo vya ukatili wa kijinsia, huku baadhi ya wananchi wakidai kuwa utaratibu huo wa kuombana msamaha umegeuka kinga ya watuhumiwa wa ubakaji na unyanyasaji wa watoto.

Tuhuma hizo zimeibuliwa na wananchi pamoja na wadau wa kupinga ukatili wa kijinsia wakati wa mafunzo yaliyoandaliwa na Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) kupitia mradi wa kuimarisha mifumo ya jamii katika kupambana na ukatili wa kijinsia na kulinda haki za wanawake na watoto, yaliyofanyika katika maeneo ya Mabogini (Moshi DC), Kalenga (Iringa DC) na Mgagao (Mwanga DC).

Washiriki wa mafunzo hayo walieleza kuwa mila ya kutumia jani la “sale” pamoja na “ngiambii”  jani dogo linalotambaa ardhini kuashiria kuombana msamaha katika jamii ya Kichaga, imekuwa ikitumika vibaya kumaliza kesi za ukatili wa kijinsia nje ya mfumo wa sheria.

Mchungaji wa kanisa la TAG, Mabogini, Lidyia Materu alisema mila hiyo awali ilikuwa sehemu ya maridhiano ya kifamilia katika migogoro ya kawaida, lakini sasa imeanza kutumiwa hata kwenye makosa ya jinai ikiwemo ubakaji na ukatili dhidi ya watoto.

“Mila hii imekuwa hatari sana kwa sababu watu wanaamini wataomba msamaha na suala litakwisha. Unakuta mtuhumiwa ameshakamatwa lakini kesho yake familia zote zimekaa pamoja zinakunywa mbege, jani la sale linawekwa pembeni, halafu wanaambiwa ‘tumeshapatana’,” alisema Mchungaji Materu.

Kwa mujibu wa Jamii ya wachaga, matumizi ya mila hiyo yamechangia familia nyingi kushindwa kufikisha kesi kwenye vyombo vya sheria kwa kuhofia kuvunja mshikamano wa kifamilia au kijamii.

Mila na ukimya wa jamii

Katika mjadala huo, wananchi walikiri kuwa jamii imekuwa sehemu ya tatizo kwa kufumbia macho vitendo vya ukatili wa kijinsia na kuhalalisha baadhi ya tabia kandamizi kupitia mila na desturi.

Mjumbe wa Kamati ya MTAKUWWA Kata ya Mabogini, Elizabeth Chuwa, alisema jamii imefikia hatua ya kuona udhalilishaji wa wanawake kama jambo la kawaida.

“Unaweza kuona vijana wakimdhalilisha mwanamke barabarani na watu wote wanakaa kimya. Hakuna anayekemea kwa sababu jamii imezoea,” 

Anakazia zaidi kwa kusema  hali hiyo imejenga mazingira ya ukimya hata kwa makosa makubwa kama ubakaji wa watoto.

“Mtoto anabakwa lakini jamii inanyamaza. Watu wanaona ni jambo la kifamilia badala ya kosa la jinai,” 
Uchambuzi wa wadau unaonesha kuwa baadhi ya mila ambazo hapo zamani zilikuwa na lengo la kuleta maridhiano ndani ya jamii, sasa zimekuwa zikikinzana na sheria za kisasa na haki za binadamu, hasa pale zinapotumiwa kuficha uhalifu.

Kwa mujibu wa Sheria ya Kanuni ya Adhabu, Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009 na Sheria ya Makosa ya Kujamiiana (SOSPA), makosa ya ukatili wa kijinsia ni makosa ya jinai yasiyoweza kumalizwa kwa maridhiano ya kifamilia au kimila.
Aidha, Tanzania ni mwanachama wa mikataba ya kimataifa ikiwemo Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Kutokomeza Aina Zote za Ubaguzi dhidi ya Wanawake (CEDAW) na Mkataba wa Haki za Mtoto, ambayo inaitaka jamii kuhakikisha wanawake na watoto wanalindwa dhidi ya ukatili na kunyimwa haki.

Maridhiano yanayotajwa kuficha uhalifu

Mwanasheria kutoka Ofisi ya Taifa ya Mashtaka Mkoa wa Kilimanjaro, Wakili Bora Mfinanga, anasema kwamba baadhi ya maridhiano ya kimila yanaambatana na vitendo vya rushwa.

“Haiwezekani mtu apewe pombe, fedha au mifugo halafu ikaelezwa kuwa ni msamaha wa kimila. Huo ni mchakato unaozuia haki,” 
Anasisitiza kuwa sheria za Tanzania haziruhusu kesi za ubakaji au ukatili dhidi ya watoto kumalizwa kwa makubaliano ya kifamilia.

Kwa upande wake, Mratibu wa Dawati la Jinsia Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, SP Asia Matauka, anasema amii ina wajibu wa kutoa taarifa mapema badala ya kuficha matukio kwa kisingizio cha mila.

“Kesi za ukatili wa kijinsia hazipaswi kunyamaziwa wala kumaliziwa nyumbani. Manusura wanapaswa kulindwa na kupewa haki zao,” anasema.

Watoto na Wasichana wazidi kuwa hatarini

Katika majadiliano na jamii ya kata ya mabogini, walieleza kuwa ukimya wa jamii umechangia watoto wengi kubaki kwenye mazingira hatarishi, huku baadhi ya wazazi wakihofia aibu na hivyo kushindwa kutoa taarifa.

Katika Kata ya Mabogini na Tarafa ya Kibosho kwa ujumla matukio mbalimbali ya ubakaji na unyanyasaji wa watoto yalitajwa kuhusisha watu wanaofahamika ndani ya jamii, lakini hatua zikidaiwa kutokuchukuliwa ipasavyo.  

Huku wakitolea mifano ya kesi za ubakaji kadhaa katika kata ya mabogini na Kibosho kati ambazo hazikufanyiwa kazi ipasavyo na watuhumiwa waliokamatwa kuachiwa huru.

Aidha, viongozi wa jamii walikosoa kuongezeka kwa vilabu vya pombe za kienyeji na baa holela, hali inayotajwa kuongeza mazingira ya ukatili dhidi ya wanawake na watoto.

Kiongozi mmoja wa kijiji cha Chekereni ambaye hakutaka kutajwa jina alisema watoto wengi wameanza kuathirika kutokana na kuishi karibu na mazingira ya ulevi na biashara ya ngono.

“Watoto wanaona kila kitu hadharani. Wapo vilabuni hadi usiku na jamii imekaa kimya kana kwamba ni kawaida,” alisema.

Afisa ustawi wa jamii wa Kata ya Mabogini, Kunti Hutta, analazea suala la ulinzi wa Watoto kwa kusema kwamba jamii inapaswa kuweka mifumo madhubuti ya ulinzi kwa watoto wa kike, hasa wanafunzi wa sekondari.

“Wasichana wengi wanabaki mitaani hadi usiku baada ya masomo. Lazima wazazi, shule na jamii kwa ujumla wawajibike kuhakikisha wanakuwa salama,” 

Wito wa kubadili mila zinazoumiza jamii

Mwezeshaji wa mafunzo kutoka TGNP, Deogratius Koyanga, alisema jamii ina wajibu wa kuchambua mila zake na kuona zipi zinafaa kuendelea na zipi zinapaswa kubadilishwa kwa maslahi ya haki na usalama wa wanawake na watoto.

“Mila ni sehemu ya utamaduni wetu, lakini hazipaswi kutumika kuzuia haki. Jamii lazima ikubali kujadili kwa uwazi mila zinazochochea ukatili wa kijinsia,” anasisistiza Koyanga.

Kauli za wadau wanaotekeleza mnyororo wa kutokomeza Ukatili wa Kijinsia zinaonesha kuwa vita dhidi ya ukatili wa kijinsia haviwezi kufanikiwa bila jamii yenyewe kukubali kubadilika. 

Wadau wanaamini kuwa kuendelea kutumia mila kama jani la “sale” kuficha makosa ya jinai kunadhoofisha sheria, kunyamazisha manusura, na kuendeleza mzunguko wa ukatili katika jamii.
Share:

CultivAid YATOA MAFUNZO YA AFYA YA MIMEA KWA WAKULIMA



Na Sifa Lubasi

WAKULIMA mkoani Dodoma wametoa shime kwa Serikali na wadau wa kilimo kutoa mafunzo kwa wakulima hasa walio vijijini ili waweze kwenda sambamba na mabadiliko ya teknolojia ikiwemo umwagiliaji na kupatiwa elimu juu ya afya ya mimea ili kilimo kiwe na tija.

Wamesema hayo Jijini Dodoma wakati wa mafunzo ya wakulima juu ya afya ya mimea yaliyofanyika shamba darasa linalojulikana kama Agricultural Motivation and Technology Centre (AITEC).lililopo Don Bosco Dodoma

Mafunzo hayo yaliandaliwa na CultivAid ambalo ni shirika la kimataifa linalokuza usalama wa chakula, ustahimilivu wa hali ya hewa, na maendeleo ya kiuchumi yanayoongozwa na kilimo.

Mmoja wa wakulima kutoka Kijiji cha Mpunguzi Dk Fabian Matonya ambaye ni daktari mstaafu alisema kuwa mafunzo hayo yana manufaa makubwa kwa wakulima.

Alisema kulingana na kuwepo kwa tenolojia mbalimbali kwenye kilimo ikiwemo mfumo wa umwagiliaji, matumizi ya viuatilifu wakulima hasa wa vijijini wanahitaji elimu zaidi ya kilimo bora ili uzalishaji uwe na tija.

" Mimi ni mkulima wa zabibu elimu niliyoipata itanisaidia sana kwani zabibu inakuwa na matoleo mengi ambayo mengine hayahitajiki na yanatakiwa kutolewa ili mimea uwe na afya," alisema.

Mkulima mwingine wa kijiji cha Matumbulu, Caroline Manyungu alisema kuwa amejifunza juu ya matumizi salama ya viuatilufu bila kuathiri mimea.

Kwa upande wake,Mkurugenzi Mkazi wa CultivAid Tanzania, Eldad Barbar amesema ushirikiano wa Serikali na wadau umesaidia wakulima wakiwemo wa vijijini kuendesha kilimo cha umwagiliaji chenye sura ya uzalishaji wenye malengo.

Alisema kuwa kuna haja kwa Serikali kushirikiana na wadau ili kuunga mkono wakulima hasa wa vijijini ili kuendeleza kilimo cha umwagiliaji ambacho kimekuwa kikifanya vizuri kwenye maeneo mengi.

Alisema kuwa kilimo cha umwagiliaji kimekuwa na tija kubwa hasa kwenye kilimo cha mazao mbalimbali ikiwemo matunda , mbogamboga na parachichi ambazo zinalimwa kwenye shamba la AITEC.

"Kwenye shamba hili kuna uzalishaji mkubwa wa parachichi na limekuwa likifanya vizuri, ni zao linahitaji maji na ubaridi, tunatumia mfumo wa umwagiliaji wa matone," alisema.

Alisema kuwa, wakulima nchini wanatakiwa kuzingatia mbinu bora za kilimo, na matumizi ya teknolojia na kilimo cha umwagiliaji ili kuwa na matokeo makubwa.

Kwa upande wake mtaalam wa kilimo katika shamba hilo, Jackline Ihungo alisema kuwa wamekuwa wakitoa elimu ya kilimo bora, mbinu bora za kilimo ili kukuza sekta ya kilimo.

Alisema kuwa serikali imekuwa ikihakikisha wakulima wanapata mbinu bora za kilimo na matumizi ya viuatilufu ili kutunza usalama wa viumbe hai na mazingira.

Alitaja,mambo muhimu yanayosaidia afya ya mimea pamoja na udongo wenye rutuba , ambao unatakiwa uwe na virutubisho vya kutosha kama nitrojeni, fosforasi, na potasiamu.

Pia maji ya kutosha ikiwemo umwagiliaji sahihi husaidia ukuaji bila kuzidisha maji pamoja na mwanga wa jua kwani mimea mingi huhitaji mwanga wa kutosha kwa ajili ya kutengeneza chakula.

Aidha katika kudhibiti wadudu na magonjwa, wakulima wanapaswa kutumia mbegu bora, usafi wa shamba, na dawa salama

Hivi karibuni kulitolewa ripoti ya Maendeleo ya mwaka 2025 ya Programu ya AgriCluster ya CultivAid Tanzania ambayo ilisema iliwafikia zaidi ya wakulima 600, na kusambaza zaidi ya miche bora ya mbegu chotara 170,000, na ilikabidhi maeneo matatu kwa umiliki kamili wa jamii katika mikoa ya Dodoma na Singida.

Kulingana na ripoti hiyo, maendeleo ya programu ya pamoja na Innovation Africa na Water4Mercy katika mikoa ya Dodoma na Singida nchini Tanzania, Mwaka 2025, kazi ilifanyika katika maeneo 11 ya maonesho yanayofanya kazi,

"Programu iliwafikia zaidi ya wakulima 600, ilisambaza zaidi ya miche bora ya mbegu chotara 170,000, na ilikabidhi maeneo matatu kwa umiliki kamili wa jamii lkiwa ni ishara wazi kwamba mfumo huo unajenga uwezo wa kudumu na unaojiendesha wenyewe," ilisema sehemu ya ripoti hiyo.


Share:

BARRICK YAWEZESHA WANAFUNZI VYUO VIKUU MBEYA KUTAMBUA FURSA KUPITIA KONGAMANO LA AIESEC 2026


Naibu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Mbeya University of Science and Technology ( MUST) Prof. Said Wai akifungua kongamano la AIESEC 2026 lililofanyika katika chuo hicho.
Afisa Mwandamizi wa AIESEC Tanzania, Joshua Samwel akiongea na wanafunzi katika kongamano hilo.
Mhandisi Kiugu James wa Barrick North Mara akitoa mada kwenye kongamano hilo.
Baadhi ya wafanyakazi wa Barrick walioshiriki katika kongamano hilo wakijitambulisha
Picha ya viongozi wa AIESEC na wadhamini.

***
Kampuni ya Barrick nchini yenye ubia na serikali kupitia kampuni ya Twiga, imeungana na wadau wengine kudhamini na kushiriki katika kongamano la kuwajengea uwezo wanafunzi wa vyuo vya elimu ya juu mkoani Mbeya lililoandaliwa na taasisi ya AIESEC na kufanyika katika katika chuo Kikuu cha Mbeya University of Science and Technology (MUST).

Kupitia kongamano hilo ambalo kufanyika kila mwaka, wanafunzi wa vyuo vya elimu ya juu na kati huweza kufahamu taasisi mbalimbali na makampuni nchini yanavyoendesha shughuli zake na kujengewa uwezo wa kujiamini na kujiandaa kikamilifu kuchangamkia fursa zinazojitokeza na jinsi ya kutafuta fursa za ajira katika makampuni makubwa,ubunifu sambamba na jinsi ya kujiajiri na kupata mafanikio kupitia katika taaluma zao.

Wafanyakazi wa Barrick waliobobea katika fani mbalimbali walishiriki kutoa mada za kuwajengea uwezo wanafunzi na kuwaeleza shughuli zinazoendeshwa na Barrick-Twiga nchini ikiwemo mkakati wa kampuni wa kuibua na kuendeleza vipaji vya vijana wa kitanzania na wafanyakazi wake kwa ujumla.

Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMATATU MEI 11,2026



Magazeti leo





Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger