Sunday, 10 May 2026

SALOME: NYUMBA 2,512 ZIMEUNGANISHWA NA MIUNDOMBINU YA GESI ASILIA


Na Mwandishi Wetu

Naibu Waziri wa Nishati, Salome Makamba amesema hadi Aprili 2026, jumla ya nyumba 2,512 zimeunganishwa na miundombinu ya gesi asilia katika mikoa ya Mtwara, Lindi, Pwani na Dar es Salaam.

Mhe. Salome ametoa taarifa hiyo Mei 8, 2026 bungeni jijini Dodoma alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Asha Omar Rashid, aliyetaka kujua mpango wa Serikali wa kuboresha upatikanaji wa nishati ya gesi vijijini.

Akijibu swali hilo, Mhe.Salome amesema Serikali kupitia Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) inaendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya usambazaji wa gesi asilia, ambapo hadi Aprili 2026 nyumba 425 zimeunganishwa katika Mkoa wa Mtwara, 677 Mkoa wa Lindi, 530 Mkoa wa Pwani na 880 Mkoa wa Dar es Salaam.

Aidha, amesema katika kuhakikisha nishati ya gesi inawafikia Watanzania wengi zaidi, Wakala wa Nishati Vijijini (REA) unaendelea kutekeleza mradi wa kusambaza mitungi 452,445 ya Gesi Oevu ya Petroli (LPG) yenye ujazo wa kilogramu sita kwa ruzuku ya asilimia 50 ili kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia katika maeneo ya vijijini na vijiji-miji.

Vilevile, Serikali inaendelea kuhamasisha sekta binafsi kuwekeza katika miundombinu ya usambazaji wa gesi ya LPG katika maeneo ya vijijini na vijiji-miji.

Mhe. Salome amesema Serikali pia inaendelea kufanya tafiti katika maeneo ya mijini na vijijini ili kubaini aina sahihi ya miundombinu inayohitajika kwa ajili ya kufikisha na kusambaza gesi asilia kwa ufanisi zaidi.

Amefafanua kuwa matokeo ya tafiti hizo yatawezesha kubainisha njia bora za usambazaji wa gesi asilia kulingana na mahitaji ya maeneo husika, sambamba na kuibua fursa za kuanzishwa kwa miradi mingine ya usambazaji wa gesi asilia itakayotekelezwa kwa ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi ili kuhakikisha wananchi wengi zaidi mijini na vijijini wananufaika na nishati hiyo safi.




Share:

COOP BANK YAZINDUA TAWI MTWARA MJINI KUCHOCHEA UCHUMI JUMUISHI


Na Mwandishi Wetu

Benki ya Ushirika (Coop Bank) mwishoni mwa wiki ilizindua rasmi tawi lake jipya Mtwara mjini ikiwa ni hatua muhimu katika utekelezaji wa mkakati wa benki hiyo wa kupanua huduma za kifedha na kuimarisha uchumi jumuishi.

Kwa uzinduzi huo, mtandao wa matawi ya Coop Bank umeongezeka na kufikia matawi matano ambapo ni Dodoma, Moshi, Tabora, Tandahimba na Mtwara.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi huo chini ya kauli mbiu “Ustawi Jumuishi, Uwezo kwa memba”, Mgeni Rasmi ambaye ni Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Mhe. Kanali Donald Msengi aliishukuru benki hiyo kwa kuendelea kuwa na Imani na mkoa wake huku akisisitiza kuwa Serikali inaendelea kuweka mazingira wezeshi ilikuvujia uwekezaji zaidi mkoani humo.

“Uzinduzi wa Tawi hili hapa Mtwara mjini ishara tosha ya imani kubwa ambayo Coop Bank inaendelea kuiweka katika mkoa wetu kwa kuwa tayari wana tawi wilayani Tandahimba.” alisema.

Aliongeza, “Serikali itaendelea kushirikiana na sekta binafsi kuhakikisha huduma za kifedha zinawafikia wananchi wengi zaidi, hasa vijijini,” alisema.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi Coop Bank Dr. Joseph Witts kupitia hotuba yake iliyosomwa na mjumbe wa Bodi wa Benki hiyo Mohamed Mwinguku alisema uzinduzi wa tawi hilo ni sehemu ya utekelezaji wa mkakati mpana wa benki hiyo wa kusogeza huduma karibu na wananchi, kwa lengo la kuongeza ujumuishwaji wa kifedha na ustawi kwa wote.

“Mkoa wa Mtwara ni miongoni mwa mikoa yenye mchango mkubwa katika uchumi wa taifa, hasa kupitia zao la korosho. Kama Bodi, tulifanya uamuzi wa makusudi kuwekeza hapa kwa sababu tunaamini katika uwezo wa wananchi wa Mtwara na fursa zilizopo katika mkoa huu,” alisema.

Dkt. Witts alisema kupitia tawi hilo, Coop Bank itaendelea kutoa masuluhisho ya kifedha yatakayokidhi mahitaji ya wananchi yakiwemo mikopo nafuu, huduma za kidijitali, na ushauri wa kifedha.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Coop Bank Godfrey Ngu’urah alisema benki yake baada ya uzinduzi wa tawi hilo imejipanga kuzindua matawi mengine matatu kabla ya mwisho wa robo ya tatu ya mwaka huu mikoani Dar es Salaam, Kagera na Mwanza.

Ng’urah alibainisha kuwa benki yake imepata mafanikio makubwa ndani ya mwaka mmoja baada ya kuzinduliwa kwake akatumia fursa hiyo kuwashukuru wadau mbalimbali kwa kuendelea kuwa na Imani na benki yake.

Alibainisha kuwa Kitabu cha mikopo cha benki hiyo kimeongezeka hadi kufikia shilingi bilioni 101.02 kutoka shilingi bilioni 16.6, ikiwa ni ukuaji wa asilimia 506, huku amana za wateja zikifikia shilingi bilioni 101.5 kutoka shilingi bilioni 12.5, sawa na ukuaji wa asilimia 709.

“Fedha za wanahisa zimeongezeka hadi kufikia shilingi bilioni 42.1 katika robo ya kwanza ya mwaka huu kutoka shilingi bilioni 27.4 ya robo ya kwanza ya mwaka 2025 ikiwa ni ukuaji wa asilimia 54,” alisema.

Ng’urah aliongeza kuwa ndani ya mwaka mmoja, benki imeongeza wateja wake hadi kufikia zaidi ya 37,000 kutoka wateja 5,000 katika robo ya kwanza ya mwaka 2025, hatua inayodhihirisha kukua kwa imani ya wateja na kupanuka kwa wigo wa huduma.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMAPILI MEI 10,2026



Magazeti




Share:

Saturday, 9 May 2026

VIJANA IRINGA WAHIMIZWA KUTUMIA TEKNOLOJIA NA UBUNIFU KUJIKWAMUA KIUCHUMI


Mkuu wa Mkoa wa Iringa mheshimiwa Khery James wa kwanza kutoka kushoto akikata utepe kabla ya kuzungumza na wafanyabiashara na wajasiriamali katika ukumbi wa Gentle Hills Hotel uliopo Manispaa ya Iringa Mkoani Iringa
Mkuu wa Mkoa wa Iringa mheshimiwa Khery James akisalimiana na meneja wa taasisi ya Zidiup Mentorship John Waryuba wakati alipowasili katika ukumbi wa Gentle Hills Hotel Manispaa ya Iringa 
Meneja wa taasisi ya Zidiup Mentorship John Waryuba Akizungumza na wafanyabiashara na wajasiriamali kutoka maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Iringa wakati wa kongamano hilo kubwa la wafanyabiashara na wajasiriamali ukumbi wa Gentle Hills Hotel 

 Regina Ndumbaro-Iringa 


Kongamano kubwa la
wafanyabiashara na wajasiriamali kutoka maeneo mbalimbali ya mkoa wa Iringa na wilaya zake limefanyika kwa mafanikio makubwa katikq ukumbi wa Gentle Hills Hotel tarehe 8 april 2026 chini ya uratibu wa programu ya Zidiup Mentorship, likiongozwa na Meneja wake, John Waryuba, huku mgeni rasmi akiwa Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Khery James. 


Kongamano hilo limewakutanisha wafanyabiashara wakubwa, wajasiriamali wadogo pamoja na vijana waliopata nafasi ya kuuliza maswali kuhusu biashara, mikopo, teknolojia na maendeleo ya kiuchumi, ambapo viongozi na wataalamu walitoa majibu papo kwa papo mbele ya washiriki waliojitokeza kwa wingi.


Akizungumza katika kongamano hilo Mkuu wa  Mkoa wa Iringa mheshimiwa Khery James ameipongeza Zidiup Mentorship kwa juhudi zake za kulea vipaji na kuwawezesha vijana kujitambua kupitia ubunifu na matumizi ya teknolojia. 


Amesema vijana wa Tanzania wana uwezo mkubwa wa kufanya mambo makubwa ikiwa watapata majukwaa sahihi ya kuonesha vipaji vyao. 


Mkuu huyo wa mkoa amefananisha maisha na maji yenye ladha inayotegemea maamuzi ya mtu mwenyewe, akisisitiza kuwa vijana wanapaswa kuwa na mtazamo chanya na kuamini kuwa changamoto zinaweza kuwa fursa za mafanikio iwapo wataamua kuzitazama kwa mtazamo wa maendeleo.


Katika hotuba yake Mkuu wa Mkoa Khery James amewahamasisha vijana kutumia teknolojia na mitandao ya kijamii kama nyenzo ya kujiletea maendeleo badala ya kuikimbia. 


Amesema dunia ya sasa imebadilika na teknolojia imegusa kila sekta ikiwemo biashara, elimu, mawasiliano na uzalishaji, hivyo vijana wanapaswa kuitumia kimkakati ili kujitangaza na kuongeza kipato chao. 


Ametoa mifano ya wafanyabiashara wanaouza bidhaa kupitia mitandao na kuwafikia watu wengi zaidi kwa muda mfupi, huku akieleza kuwa viongozi wa kisasa hutumia mitandao ya kijamii kusikiliza na kufahamu changamoto za wananchi. 


Aidha amempongeza kijana Kelvin anayejishughulisha na ushonaji wa mabegi aliyegunduliwa kupitia Zidiup Mentorship, akisema hiyo ni ishara kuwa teknolojia inaweza kuwa daraja la mafanikio kwa vijana wengi.


Mbali na hilo, Mkuu huyo wa Mkoa amewataka vijana wa Iringa kutumia rasilimali zilizopo mkoani humo kuongeza thamani ya bidhaa na kukuza uchumi wa mkoa. 


Amesema Iringa ina fursa kubwa katika utalii kupitia Hifadhi ya Taifa ya Ruaha, biashara ya mazao, usafirishaji na bidhaa za misitu, hivyo vijana wanapaswa kuwekeza katika ubunifu badala ya kuuza malighafi pekee. 


Amesisitiza umuhimu wa kuongeza thamani ya mazao na mbao kwa kutengeneza bidhaa kama fenicha bora zitakazoongeza ajira na mapato kwa vijana wengi zaidi. 


Pia ameahidi kuendelea kuwaunga mkono vijana kupitia mikopo, ubunifu, sayansi na teknolojia ili kuhakikisha wanapata nafasi ya kufikia ndoto zao za maendeleo.


Kwa upande wake, Meneja wa Zidiup Mentorship John Waryuba amemshukuru Mkuu wa Mkoa kwa kukubali kushiriki katika kongamano hilo na kwa namna anavyoendelea kuwa karibu na vijana wa Iringa. 


Waryuba amewahamasisha vijana na wajasiriamali wadogo kuanza biashara kwa kutumia mtaji mdogo walionao badala ya kusubiri mazingira makubwa, akisema mafanikio huanza na hatua ndogo. 


Amesema kongamano hilo limekuwa jukwaa muhimu la kuwaunganisha vijana, wafanyabiashara na viongozi wa serikali kwa lengo la kujenga uchumi imara wa mkoa wa Iringa na kuwapa vijana matumaini mapya ya kujitegemea kupitia biashara, ubunifu na teknolojia



Share:

Friday, 8 May 2026

WAZIRI KAPINGA AKABIDHI MAGARI 11 TBS, KUIMARISHA UTEKELEZAJI WA MAJUKUMU


NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga, amelielekeza Shirika la Viwango Tanzania (TBS) kuhakikisha linalinda na kuthamini rasilimali za taasisi ili kuongeza ubora na ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wananchi.

Waziri Kapinga ametoa kauli hiyo Mei 8, 2026 jijini Dar es Salaam wakati akikabidhi magari mapya 11 kwa TBS, ambapo alisisitiza umuhimu wa kuyatumia kwa shughuli rasmi za ofisi ili kuimarisha utekelezaji wa majukumu ya shirika hilo.

Alisema ubora wa huduma unaotolewa na taasisi yoyote unategemea mazingira bora ya kazi pamoja na ufanisi wa watumishi katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku.

“Ubora tunaouzungumzia unajengwa na ufanisi katika kazi. Ili kufikia ufanisi huo ni lazima kujenga mazingira yanayowezesha watumishi kufanya kazi kwa weledi na tija, hatimaye kufanikisha lengo kuu la taasisi ambalo ni kuhakikisha ubora,” amesema Waziri Kapinga.

Aidha, alimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kuiwezesha wizara na taasisi zake kupitia utoaji wa bajeti na fedha zinazowasaidia kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa TBS, Dk. Ashura Katunzi, amesema magari hayo yataongeza ufanisi wa kazi na kurahisisha utekelezaji wa majukumu ya shirika hilo katika kusimamia viwango nchini.

Dk. Katunzi amesema awamu ya kwanza taasisi hiyo ilipokea magari matano, huku awamu ya pili ikihusisha magari 11 yaliyokabidhiwa sasa, hatua ambayo itaongeza uwezo wa TBS kuwafikia wadau na kutoa huduma kwa ufanisi zaidi.

Share:

WAZIRI MKUU ATAKA WATENDAJI SERIKALINI KUTUMIA USHAWISHI KUVUTIA WAWEKEZAJI


Waziri Mkuu Dkt Mwigulu Nchemba amewataka watendaji katika taasisi na mamlaka za Serikali wawe tayari kuwawezesha wawekezaji badala ya kuwadhibiti ili wavutiwe kuwekeza zaidi na zaidi.



“Nitoe wito kwa taasisi na mamlaka za Serikali, tumieni muda mwingi kuwawezesha wawekezaji badala ya kuwadhibiti. Washawishini waongeze uwekezaji badala ya kuwafanya waonekane wanaomba. Tumieni vivutio zaidi ili washawishike zaidi na zaidi,” amesema.


Ametoa wito huo leo (Ijumaa, Mei 8, 2026) wakati akizungumza na wadau waliohudhuria uzinduzi wa hoteli ya Mikumi Wildlife katika Hifadhi ya Taifa ya Mikumi, wilayani Kilosa, mkoani Morogoro.


Amesema hoteli hiyo ambayo zamani ilikuwa inamilikiwa na serikali lakini ikapata janga la kuungua moto, ina historia ya miaka mingi; na ana imani na uwekezaji uliofanyika kwani umesaidia kuongeza ajira na kipato kwa wananchi.


“Sina shaka uwekezaji huu utaongeza mvuto kutokana na viwango vilivyopo kwenye hoteli hii. Viwango vya hoteli hii ni vya juu sana, ninaamini vitasaidia kuongeza muda wa watalii kukaa ndani ya hifadhi na uwepo wa malazi mazuri pia utaongeza idadi ya watalii,” amesema.


Akielezea juhudi za serikali kuboresha hifadhi ya Mikumi, Waziri Mkuu amesema Serikali imetoa sh. bilioni 35 za kuboresha uwanja wa ndege wa Kikoboga na ifikapo Oktoba mwaka huu, utakuwa umekamilika.


Amezitaka Wizara ya Maliasili na Utalii, TANAPA washirikiane na mamlaka nyingine za Serikali na kutumia fursa ya stesheni ya Kilosa ili kufungua njia na kuboresha miundombinu itakayorahisisha watalii kuingia katika Hifadhi ya Mikumi na hivyo kuongeza idadi ya watalii.


Ameitaka Wizara ya Maliasili na Utalii iendelee kubuni mikakati ya kwa kuhamasisha sekta binafsi iwekeza katika maeneo ya utalii huku akizitaka taasisi zote za umma ikiwa ni pamoja na mikoa yenye maeneo yaliyo na fursa za utalii ziendelee kuboresha mazingira ya uwekezaji ili kuvutia wawekezaji wengi zaidi. “Suala hili litekelezwe sambamba na kutangaza vivutio vilivyopo.”


Waziri Mkuu amewataka wadau wa utalii waweke mipango ya kuendeleza mazao mapya ya utalii yatakayochochea ongezeko la watalii na kuwahamasisha kuchagua kutembelea vivutio vilivyopo katika Kanda ya Utalii Kusini.


Ametumia fursa hiyo kumwelekeza Waziri wa Maliasili na Utalii aangalie namna ya kuongeza programu za utalii kwenye Chuo cha Ufundi (VETA) kilichopo Mikumi. “Waziri wa Utalii tuongeze programu nyingi za utalii ili vijana wa hapa wanufaike na rasilimali zilizopo katika eneo lao. Kwa maono ya Mheshimiwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, alitaka hivi vyuo vinapojengwa viweke programu kulingana na shughuli za kiuchumi za eneo husika kama vile utalii, uvuvi ili viwasaidie vijana wa maeneo husika.”


Mapema, akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na washiriki wa hafla hiyo, Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji alisema miaka ya nyuma hifadhi ya Mikumi ilikuwa ikipokea watalii 60,000 kwa mwaka lakini mwaka jana idadi ya watalii iliongezeka sana kufikia 174,808.


“Mapato yanayotokana na utalii yalikuwa sh. milioni 2.5 lakini nayo kwa mwaka jana yaliongezeka na kufikia sh.milioni 9.81. Hadi kufikia tarehe 31 Machi, 2026 idadi ya watalii waliofika kwenye hifadhi ya Taifa ya Mikumi walikuwa 151,275 na mapato yaliyokusanywa yalikuwa yamefikia sh. milioni 10.12,” alisema.


Alisema tayari sh. bilioni nne za kujenga geti upande wa Kilosa zimeshatolewa na ziko hifadhini tayari kuanza kazi hiyo ambapo mtu akishuka Kilosa kwa treni ya SGR atatumia dk.20 tu kuingia hifadhini.


Naye Bw. Simon Nguka, akisoma taarifa kuhusu mradi huo, alisema ujenzi na ukarabati wa hoteli hiyo yenye vyumba 48 na ambayo inamilikiwa na Watanzania kwa asilimia 100, umetumia sh. bilioni 26.8.


Alisema mradi huo ni miongoni mwa miradi 24 waliyonayo. Wellworth Group inamiliki mahoteli, loji, resorts na kambi za kitalii zenye uwekezaji wa thamani ya sh. bilioni 640.




Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger