Monday, 29 June 2026

WAZIRI SANGU: MAHUSIANO, AMANI NA UMOJA NI MSINGI WA MAENDELEO YA TAIFA

 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu amesema kuwa uamuzi wa Serikali ya Awamu ya Sita wa kuanzisha Wizara maalum yenye dhamana ya kushughulikia masuala ya Mahusiano inaakisi maono ya Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuimarisha Umoja, Mshikamano na Amani nchini.

“Dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha Tanzania inaendelea kuwa taifa lenye amani, mshikamano na maendeleo kupitia mazungumzo, maridhiano na ushirikiano wa wadau wote,” amesema.

Mhe. Sangu amesema hayo Juni 28, 2026 katika Ibada maalumu ya kilele cha harambee iliyofanyika kwenye ushirika wa Amani wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Kati, mjini Singida ambapo alieleza kuwa Serikali imeendelea kujenga mazingira ya mazungumzo na ushirikiano kati yake na taasisi za dini ili kuimarisha mshikamano wa kitaifa.

Alisema Ofisi ya Waziri Mkuu kuratibu Mahusiano ni utekelezaji wa maelekezo ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na kutimiza wito wa kibiblia wa kuwaleta watu pamoja bila kujali tofauti za kisiasa, kidini au kikabila.

Vile vile, Waziri Sangu amempongeza Waziri Mkuu Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba kwa kusimamia karibu agenda ya mahusiano nchini, jambo ambalo limewezesha viongozi wa dini kupata fursa ya kuwasilisha hoja zao serikalini kupitia wizara hiyo, hatua ambayo imeongeza ushirikiano na kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili wananchi.

Aidha, alisema jukumu la kuwasikiliza wananchi, hususan wanyonge na wenye mahitaji, ni sehemu ya wajibu wa Serikali na linaendana na mafundisho ya dini yanayohimiza kuwajali wahitaji na kujenga jamii yenye haki na mshikamano.

Kwa upande mwengine, Waziri Sangu aliwashukuru viongozi wa dini kwa kuendelea kuliombea Taifa na viongozi wake, na kusema maombi yao yamekuwa nguzo muhimu katika kudumisha amani, utulivu na maendeleo ya nchini.

Kadhalika, Mhe. Sangu amesema Serikali itaendelea kushirikiana kwa karibu na taasisi za dini pamoja na wadau wengine katika kuimarisha mahusiano ya kijamii na kisiasa, ikiwa ni pamoja na kuendelea kufanya mazungumzo na vyama vya siasa kwa lengo la kuimarisha umoja wa Watanzania.

Share:

PROF. SHEMDOE AWAASA WANAFUNZI KUENDELEZA VIPAJI VYAO VYA MICHEZO, SANAA


•Awataka kuwa na nidhamu na kusoma kwa bidii

Na OWM - TAMISEMI, Iringa

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amewaasa wanafunzi walioshiriki mashindano ya UMISSETA mwaka 2026 kuendeleza vipaji vya michezo na Sanaa walivyonavyo kwani vitawasaidia katika maisha yao ya baadaye, huku akiwataka kuzingatia nidhamu na kusoma kwa bidii ili  kufikia ndoto zao na kutoa mchango katika maendeleo ya taifa.

Prof. Shemdoe ametoa wito huo kwa wanafunzi leo Juni 28, 2026 mjini Iringa katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Lugalo, wakati akifunga mashindano ya UMISSETA kwa mwaka wa 2026.

“Nina wasihi muendelee kuwa na nidhamu, kujituma katika masomo yenu na kuendeleza vipaji vyenu vya michezo na sanaa, msiviache vipaji vyenu kwani hata mimi juzi tulipokuwa tunapokea Mwenge wa Uhuru Lushoto nilijikuta nikikumbushia kipaji changu cha kupiga ngoma za utamaduni na kuimba kwa umahiri,” amesisitiza Prof. Shemdoe.

Prof. Shemdoe amewahakikishia wanafunzi hao kuwa, Serikali itaendelea kuweka mazingira bora ya kuhakikisha vipaji vya wanafunzi vinaibuliwa, vinatambuliwa, vinakuzwa ili kuwanufaisha na kulinufaisha taifa kupitia ushiriki wao katika kuliwakilisha taifa kwenye mashindano ya michezo na Sanaa ndani na nje ya nchi.

Aidha, Prof. Shemdoe ametumia fursa hiyo kumpongeza Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuipa kipaumbele sekta ya elimu, michezo, sanaa na maendeleo ya vijana kwenye ajenda kuu ya taifa na kuongeza kuwa, uwekezaji huo unaendelea kuweka msingi imara wa kuibua na kuendeleza vipaji vya watoto na vijana wa Tanzania.

 Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI anayeshughulikia Elimu Bw. Atupele Mwambene amesema kuwa, ushiriki wa wanafunzi katika michezo mbalimbali ya UMITASHUMTA na UMISSETA umeendelea kuwa jukwaa muhimu la kitaifa la kuibua vipaji, kuimarisha afya, kujenga urafiki na kuendeleza umoja wa kitaifa miongoni mwa wanafunzi. 

Naye Mwakilishi wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Bi. Leah Kihimbi amemuhakikishia Prof. Shemdoe kuwa wizara yake itatekeleza ipasavyo jukumu la kuibua kuendeleza vipaji na vipawa vinavyotokana na mashindano hayo ya sanaa na michezo shuleni. 

Mwakilishi wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar ambaye ni Afisa Mdhamini Bw. Mohamed Nassoro Salimu amesema Zanzibar inakwenda kujipanga ili kuleta ushindani mkubwa katika mashindano ya mwakani, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi ya kufanya mageuzi katika sekta ya michezo.

Akitoa neno la shukrani, Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI Bw. Adolf Ndunguru amewashukuru maafisa elimu, wakuu wa shule, walimu, waratibu wa michezo na walezi wa wanafunzi, kwa kazi kubwa walioifanya ya kuwaandaa na kuwaleta wanafunzi katika mashindano ambayo yamewawezesha kujifunza thamani ya nidhamu, ushindani wa haki, uvumilivu, uzalendo na mshikamano wa kitaifa.











Share:

Sunday, 28 June 2026

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMATATU JUNI 29, 2026

Share:

RAIS DKT. SAMIA KUFUNGUA MKUTANO MKUBWA WA MADINI NOVEMBA 2026

▪️Ni Mkutano mkubwa wa Madini na Uwekezaji

▪️Washiriki 2000 kutoka mataifa 50 Duniani kushiriki

▪️Kauli Mbiu ya Mkutano inalenga kuongeza thamani madini kwa maendelezo ya Viwanda

▪️Serikali na Sekta Binafsi kushirikiana kuandaa mkutano huo


▪️Waziri Mavunde azindua rasmi maandalizi ya mkutano huo

📍 DAR ES SALAAM. 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. Dkt. Samia S. Hassan anatarajiwa kufungua rasmi Mkutano wa Saba wa Madini na Uwekezaji Tanzania (TMIC 2026) utakaofanyika Novemba 19 hadi 21, 2026 katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC), Dar es Salaam.

Akizungumza leo Juni 27, 2026 wakati wa uzinduzi wa TMIC 2026, Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, amesema serikali imeamua kujenga uchumi wa viwanda unaotokana na madini kwa kuwekeza katika uchakataji na uyeyushaji wa madini badala ya kuendelea kuuza malighafi.

Amesema kaulimbiu ya mkutano huo, "Madini Yaliyoongezwa Thamani: Chachu ya Ukuaji wa Viwanda na Uchumi," inaakisi dira ya serikali ya kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha uchakataji wa madini barani Afrika.

Kwa mujibu wa Mhe. Mavunde, amesema Tanzania tayari ina viwanda vinane vya kusafisha dhahabu, huku Mkoa wa Dodoma ukiwa na viwanda tisa vinavyojengwa na vinavyoendelea na uzalishaji pamoja na kiwanda kikubwa cha kuyeyusha madini ya nikeli na shaba.

"Zaidi ya Sh bilioni 600 zinawekezwa katika ujenzi wa kiwanda cha chuma kitakachotumia asilimia 100 ya malighafi za ndani, huku uwekezaji mwingine ukiendelea Kigamboni na Tanga kwa ajili ya uchakataji wa madini ya 'Heavy Mineral Sands' na mradi wa madini ya niobium wa Panda Hill, Mbeya," amesema Mhe. Mavunde

Amesema, katika kuongeza ushiriki wa Watanzania kwenye sekta hiyo,  thamani ya manunuzi kupitia mpango wa 'Local Content' imefikia Sh trilioni 5.1, huku bidhaa 20 zikitakiwa kuzalishwa na wazawa kwa ajili ya kuhudumia migodi mikubwa.

 Amesisitiza wafanyabiashara kuzingatia uaminifu na viwango vya kimataifa ili kunufaika zaidi na fursa hizo.

Amesema sekta ya madini imeendelea kuimarisha mchango wake katika uchumi kwa kuingiza Sh trilioni 1.374 katika Mfuko Mkuu wa Serikali, kiwango kilichovuka lengo la Sh trilioni 1.2 kwa mwaka huu wa fedha.

Mhe. Mavunde, amesema Serikali imeidhinisha asilimia 10 ya mapato yote ya sekta ya madini kuelekezwa kwenye utafiti wa kina wa jiofizikia ili kuongeza maeneo yanayofahamika kuwa na madini kutoka asilimia 16 ya sasa hadi asilimia 50 ifikapo mwaka 2030.

Aidha, amesema Serikali inaandaa mfuko maalumu wa mikopo kwa wachimbaji wadogo, ambao licha ya changamoto za mitaji na teknolojia, wanachangia takribani asilimia 40 ya mapato ya sekta ya madini.

Katika hatua nyingine, amesema Serikali inaanza operesheni ya kufuta kidijitali leseni zote za madini zisizotumika. Wamiliki watakaoshindwa kuwasilisha taarifa ndani ya muda uliowekwa watapewa notisi ya siku 30 kabla ya leseni hizo kujifuta moja kwa moja.

Nae, Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Mhandisi Yahya Samamba, amesema Serikali imejipanga kuhakikisha utajiri wa madini unakuwa chachu ya kukuza viwanda vya ndani, kuongeza ajira na kuimarisha uchumi kupitia uongezaji thamani badala ya kuishia kwenye uchimbaji pekee.

Amesema TMIC 2026 utawakutanisha viongozi wa Serikali, taasisi za fedha, kampuni za madini, wataalamu wa teknolojia, watafiti na wadau wengine kutoka duniani kote kujadili fursa za uwekezaji na maendeleo ya sekta hiyo.

 "Huu ni wakati wa kuingia katika awamu mpya ya uwekezaji, ubunifu na ukuaji wa sekta ya madini nchini," amesema.

Kwa upande wa Katibu Mtendaji wa Chemba ya Migodi Tanzania, Mhandisi Benjamin Mchwampaka, amesema mkutano huo unatarajiwa kuwakutanisha washiriki zaidi ya 2,000 na watoa mada zaidi ya 100 kutoka mataifa zaidi ya 50, huku zaidi ya mada 20 zikijadiliwa zikiwemo sera, kodi, uwekezaji, teknolojia, nishati safi, madini ya kimkakati, uongezaji thamani na masuala ya mazingira, jamii na utawala bora (ESG).

Mchwampaka amesema TMIC 2026 pia utaweka mkazo katika maendeleo ya wachimbaji wadogo pamoja na ushirikishwaji wa wanawake na watu wenye ulemavu katika mnyororo mzima wa uongezaji thamani wa madini. Mkutano huo unatarajiwa kufungwa rasmi na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi.

.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUNE 28,2026


Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger