Tuesday, 7 April 2026

BARRICK NORTH MARA YAWEZESHA VIJANA TARIME KUANZISHA MIRADI YA KIUCHUMI


Vijana wakiwezeshwa kuendesha miradi mbalimbali ikiwemo ya kilimo wataweza kujikwamua kiuchumi kama wanavyoonekana vijana wakiwa shambani kwenye mradi wa kilimo cha mboga wa Matongo unaofadhiliwa na Barrick North Mara (Picha kutoka maktaba)
Mgodi wa Barrick North Mara uliopo wilayani Tarime katika mkoa wa Mara umeendelea kutekeleza moja ya sera ya mkakati endelevu wa kampuni ya kuwezesha wananchi wanaoishi jirani na migodi yake kuwa na maisha bora ambapo kupitia fedha za uwajibikaji kwa jamii (CSR) umetoa shilingi milioni 220 kwa vikundi 13 vya vijana ili kuanzisha miradi ya kiuchumi katika vijiji vyote 11 vinavyozunguka mgodi huo.

Hatua hii ni mwendelezo wa mgodi wa Barrick North Mara kuwezesha kiuchumi makundi mbalimbali katika jamii hususani vijana ambapo mwaka jana iliunga mkono jitihada za Serikali za kuwapatia leseni za uchimbaji ambapo mgodi ulitoa leseni zake na kufadhili mafunzo ya vijana hao zaidi ya 1700 wanaojiandaa kuingia katika uchimbaji wa madini chini ya programu ya Mining For a Brighter Tomorrow (MBT) inayolenga kuboresha usalama, kuongeza tija na kuondoa uvamizi wa mgodi kwa kuwapatia rasmi maeneo ya uchimbaji.

Tayari vikundi hivyo vimepokea fedha hizo, ikiwa ni ruzuku ya (CSR) ya mwaka uliopita kutoka kwa mgodi huo ambao unaendeshwa kwa ubia na serikali kupitia kampuni ya Twiga Minerals.

Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jami wa Halmashauri hiyo, Anthony George Nyange amesema kuwa fedha hizo zimesaidia vijana takriban 100 wanachama wa vikundi hiyo kuanzisha miradi ya mbalimbali ya kiuchumi.
Anthony George Nyange

“Nawashukuru sana Barrick North Mara hususan idara ya mahusiano ya jamii kwa ushirikiano ambao wamekuwa wakitoa katika kufanikisha mpango huu wa ruzuku ya uwajibikaji kwa jamii kwa vijana,” amesema Nyange.

Nyange amesema miradi hiyo imesaidia kutatua changamoto mbalimbali zilizokuwa katika vijiji hivyo kwa ajili ya ustawi wa jamii vinavyouzunguka mgodi huo.

“Wanufaika wengi ni vijana na wamejielekeza kwenye miradi ambayo siyo tu kwa ajili ya kujipatia kipato bali pia kutatua changamoto zilizokuwepo,” amesema.

Ametaja vikundi ambavyo vimenufaika na mpango huo kuwa ni Mokarambe Agribusiness, Hope and Revolution of Economy for Youth, Tunza Mazingira Nyamongo, Amshana Nyamongo na REMHOCHI.

Vingine ni Kazi ni Moyo, Konna Nne, Kiumanya, Ibuka Umoja, Tunaweza Kerende, Nyasa Group, Mtazamo Youth na Kikundi cha Keryoba.

Amesema baadhi ya vikundi hivyo vimeanzisha miradi ya usafi wa mazingira jambo ambalo limesaidia kuweka mji mdogo wa Nyamongo katika hali nzuri ya usafi na mazingira.

“Kwa mfano, kulikuwa na changomoto ya usafi katika mji wa Nyamongo, sasa hali ya usafi ni nzuri kwa sababu kuna kikundi cha mazingira ambacho kinafanya vizuri sana kwenye usafi wa mazingira,” amesema Nyange.

Nyange amesema Halmashauri ya Wilaya ya Tarime itaendelea kutenga sehemu ya fedha za Uwajibikaji kwa Jamii (CSR) zinazotolewa na mgodi wa Barrick North Mara kwa ajili ya kuwawezesha vijana kuanzisha na kuendeleza miradi ya kiuchumi.

“Tunategemea na mwaka huu pia tutatenga sehemu ya CSR kwenda kuwezesha vijana kwenye miradi ya kiuchumi. Sasa hivi, vijana wengi kule Nyamongo wana shughuli za kufanya kujipatia kipato na hata vitendo vya kihalifu vimepungua,” amesema Nyange.

Amesema mbali na mpango wa Uwajibikaji kwa Jamii (CSR), vijana hao pia wamenufaika na mikopo kupitia asilimia 10 ya mapato ya ndani inayotolewa na halmshauri hiyo kuwezesha wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.

“Wanufaika wakubwa ni vijana, na mbali ya kunufaika na mikopo yetu ya halmashauri ya asilimia 10, pia wamenufaika na mpango wa ruzuku ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR) kwa vijana,” amefafanua Nyange.

Taarifa zinaonesha Halmashauri ya Wilaya ya Tarime inaongoza kwa kutoa kiasi kikubwa cha mikopo ya asilimia 10 kwa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu katika Mkoa wa Mara.

Mgodi wa Barrick North Mara pamoja na kutekeleza sera ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR) pia utoaji wa leseni za uchimbaji kwa vijana uliwezesha na mafunzo ya siku 14 yaliyofanywa kwa kushirikiana na serikali.

Lengo la mafunzo hayo ni kuhakikisha sekta ya madini iankuwa na tija zaidi kwa kuzingatia usalama mahali pa kazi na utunzaji wa mazingira , usimamizi wa biashara za madini na kufuata sheria za nchini na usimamizi wa vikundi pamoja na elimu ya masuala ya fedha.

Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMANNE APRILI 7,2026

Magazeti



 













Share:

Monday, 6 April 2026

TUME YA UCHUNGUZI YAONGEZEWA MUDA TENA HADI APRILI 24,2026


Na Mwandishi Wetu Dodoma

MAMLAKA ya Uteuzi imeridhia maombi ya muda wa ziada kwa Tume ya Kuchunguza Matukio ya Uvunjifu wa Amani Wakati na Baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025 hivyo imeiongezea tena muda wa siku ishirini na moja (21) na kuitaka ikamilishe kazi kabla au ifikapo Aprili 24, 2026.

Mamlaka hiyo imeeleza sababu za kuongeza muda huo kwa Tume ni pamoja na kuiwezesha Tume kukamilisha uchambuzi wa ushahidi, taarifa na maoni yaliyopokelewa, kutoa fursa kwa wataalamu wa uchunguzi wa kisayansi kufanyia kazi baadhi ya vielelezo vipya vilivyowasilishwa.
Sababu nyingine ni kuiwezesha Tume kukamilisha maandalizi ya Ripoti itakayowasilishwa kwa Rais na kutoa fursa kwa Tume kuandaa tafsiri ya Ripoti hiyo.

Tume hiyo ilianza kutekeleza majukumu yake Novemba 20, 2025 na kutarajiwa kukamilisha kazi yake ndani ya kipindi cha siku 90. Hata hivyo, kutokana na sababu mbalimbali, Tume iliongezewa muda wa kukamilisha kazi na kutakiwa kuwasilisha Ripoti kwa Rais kabla au ifikapo April 3, 2026.

Hivyo, kufuatia nyongeza ya muda, wananchi waliendelea kujitokeza kwa wingi tofauti na matarajio ya Tume. Hivyo, Tume iliendelea kupokea ushahidi, taarifa na maoni zaidi. Kwa sababu hiyo, Tume haikuweza kukamilisha kazi yake ndani ya muda wa nyongeza uliotolewa na hivyo kulazimika kuomba muda wa ziada ili kukamilisha kazi yake.

Tume inaendelea kuwashukuru wananchi na wadau wote waliotoa ushirikiano kwa Tume wakati wa kufanya uchunguzi, ikiwemo wale waliofika mbele ya Tume kutoa ushahidi, taarifa na maoni, waliopiga simu na kutuma ujumbe, waliotuma ushahidi, taarifa na maoni kwa maandishi na waliowasiliana na Tume kwa njia za mitandao ya kijamii.
Share:

POLISI TANGA WAOKOA VIJANA 87 WALIOINGIZWA KWENYE MTEGO WA UTAJIRI WA HARAKA MTANDAONI


Na Hadija Bagasha - Tanga

Jeshi la Polisi Mkoa wa Tanga kupitia Kikosi cha Upelelezi wa Makosa ya Jinai (CID), limefanikiwa kuwaokoa vijana wapatao 87 waliokuwa wametapeliwa fedha zao kupitia mtandao  baada ya kushawishiwa kujiunga na kampuni inayojinasibisha kufanya biashara ya mtandao inayofahamika kwa jina la Champions E-Commerce Education ambapo katika tukio hilo vijana hao walihamasishwa kujiunga na kampuni hiyo kwa ahadi ya kupata utajiri wa haraka kupitia biashara za mtandaoni. 

Kwa mujibu wa Taarifa za awali zinaeleza kuwa vijana hao ni kutokea Mikoay a Mtwara, Iringa, Daresalaa na Morogoro ambao walishawishiwa kujiunga na Kampuni hiyo kwa ahadi ya kupata utajiri wa haraka kupitia biashara za mtandaoni, ambapo walielezwa kuwa wangeanza kupata faida kubwa ndani ya muda mfupi mara baada ya kukamilisha mafunzo.

Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo Kamanda wa polisi Mkoa Tanga Almachius Mchunguzi ameeleza kuwa kila kijana alitakiwa kuchangia kiasi cha fedha kuanzia shilingi laki sita (600,000) hadi kufikia shilingi milioni nne (4,000,000) kama mtaji wa awali pamoja na gharama za mafunzo, fedha ambazo walidaiwa kuambiwa ndizo zingewapa fursa ya kuanza biashara na kupata faida  kwa haraka.

Hata hivyo, baada ya kujiunga na mfumo huo, vijana hao walikutwa wakiishi katika mazingira yasiyoridhisha huku wakiendelea kupatiwa mafunzo yanayodaiwa kuwajengea uwezo, wakisubiri kupata utajiri waliokuwa wameahidiwa.

Katika operesheni hiyo, Jeshi la Polisi limekamata na kuwashikilia kwa mahojiano zaidi watu wawili waliokuwa wakisimamia kundi hilo ambao ni Mohammed Hamis Idrisa (24) mkazi wa Masiwani Jijini Tanga, na Fidolini Hamisi Rashidi (21) mkazi wa Mbugani.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Tanga limetoa wito kwa wananchi kuwa makini na aina ya uwekezaji unaohusisha ahadi za kupata faida kubwa kwa muda mfupi bila kuwa na taarifa sahihi, pamoja na kufanya uhakiki kama kampuni husika imesajiliwa na mamlaka halali.

Polisi imewataka wananchi kufanya uchunguzi wa kina kabla ya kujiunga na taasisi au kampuni yoyote inayojihusisha na uwekezaji hususan kupitia mitandao, ili kuepuka kuingia kwenye mitego ya utapeli.

Uchunguzi wa tukio hilo unaendelea huku Jeshi la Polisi likisisitiza kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi ya wote watakaobainika kuhusika na utapeli wa aina hiyo.




Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMATATU APRILI 6,2026

         
 Magazeti
   


Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger