Sunday, 12 July 2026
Saturday, 11 July 2026
JAB YAZINDUA MWONGOZO WA ITHIBATI YA MAISHA KWA WAANDISHI WA HABARI WAKONGWE


Na Mwandishi Wetu.
Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imezindua rasmi Mwongozo wa Kisheria wa Utoaji wa Ithibati ya Maisha kwa Waandishi wa Habari Wakongwe, hatua inayolenga kutambua na kuthamini mchango wa waandishi wa habari waliolitumikia Taifa kwa muda mrefu na kwa utumishi uliotukuka katika maendeleo ya sekta ya habari nchini.
Uzinduzi huo umefanyika leo, Julai 11, 2026, wakati wa maadhimisho ya JAB Day yaliyofanyika katika Banda la Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwenye Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba).
Kupitia hotuba yake iliyosomwa na Dkt. Egbert Mkoko, Mwenyekiti wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari, Bw. Tido Mhando, alisema mwongozo huo umeandaliwa kwa kuzingatia mamlaka iliyopewa Bodi chini ya Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229 pamoja na Kanuni zake, ili kuweka utaratibu wa utoaji wa Ithibati ya Maisha kwa waandishi wa habari wakongwe waliotoa mchango wa kipekee katika maendeleo ya taaluma hiyo.
Alisema mwongozo huo unawahusu waandishi wa habari ambao wakati Sheria ya Huduma za Habari ilipoanza kutumika mwaka 2016 walikuwa na umri wa miaka 50 au zaidi na walikuwa tayari wametoa mchango mkubwa katika sekta ya habari, lakini hawakupata fursa ya kujiendeleza hadi kufikia sifa za kitaaluma zinazohitajika kwa mujibu wa sheria.
"Mwongozo huu unalenga kuhifadhi historia ya tasnia ya habari, kuthamini mchango wa waandishi wa habari wakongwe na kuhakikisha uzoefu wao unaendelea kuwa sehemu ya urithi wa taaluma ya uandishi wa habari nchini," ilieleza sehemu ya hotuba ya Mwenyekiti.


Bw. Mhando alisisitiza kuwa mwongozo huo hauondoi wala haupunguzi masharti ya msingi yaliyowekwa na Sheria ya Huduma za Habari kuhusu sifa za kupata ithibati kwa waandishi wa habari, bali unaweka utaratibu wa kutekeleza mamlaka ambayo sheria imeipa Bodi kuhusu utoaji wa Ithibati ya Maisha kwa watu wenye utumishi uliotukuka na waliotoa mchango wa kipekee katika maendeleo ya sekta ya habari.
Aidha, aliipongeza Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kuendelea kuiwezesha Bodi kutekeleza majukumu yake na kuimarisha ushirikiano unaolenga kukuza weledi, uwajibikaji na maadili katika taaluma ya uandishi wa habari.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari, Wakili Patrick Kipangula, alisema uzinduzi wa mwongozo huo ni hatua muhimu katika utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari na unaonesha dhamira ya Bodi ya kuimarisha viwango vya taaluma huku ikitambua na kuthamini mchango wa waandishi wa habari wakongwe waliolitumikia Taifa kwa uaminifu, uzalendo na weledi.
Sambamba na uzinduzi huo, JAB iliendesha mdahalo uliowakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya habari kujadili maendeleo ya sekta ya habari nchini, utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari pamoja na mafanikio na changamoto zilizojitokeza katika mwaka mmoja wa utekelezaji wa mfumo wa utoaji wa ithibati kwa waandishi wa habari waliokidhi vigezo vya sheria.
UWEKEZAJI WA SERIKALI WAFUNGUA FURSA ZA UCHUMI RUVUMA
Waziri wa Uchukuzi Mheshimiwa Profesa Makame Mbarawa wa pili kutoka kulia akiwa pamoja na mwenyeji wake mkuu wa mkoa wa Ruvuma Brigedia Jenerali Ahmed Abbas Ahmed baada ya kuzindua jengo la mapumziko ya muda mfupi kwa abiria katika uwanja wa ndege wa Songea unatarajiwa kuwa chachu ya maendeleo ya kiuchumi katika ukanda wa kusini Na Regina Ndumbaro
Songea-Ruvuma
Uwekezaji wa Serikali wa shilingi milioni 842 katika upanuzi wa jengo la mapumziko ya muda mfupi kwa abiria katika uwanja wa ndege wa Songea unatarajiwa kuwa chachu ya ukuaji wa biashara, uwekezaji na utalii, baada ya kuongeza uwezo wa uwanja huo kuhudumia abiria 300 kwa wakati mmoja.
Friday, 10 July 2026
CHANJO ZA TVLA NI BORA NA ZINA MATOKEO CHANYA – RAS TANGA
Katibu Tawala wa Mkoa wa Tanga, Bw. Rashid Kassim Mchatta, amesema chanjo zinazozalishwa na Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) zimeendelea kuthibitisha ubora wake kwa kusaidia kudhibiti magonjwa mbalimbali ya mifugo na kuongeza tija kwa wafugaji nchini.
Bw. Mchatta alitoa kauli hiyo tarehe 9 Julai 2026 alipotembelea banda la TVLA katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) yanayoendelea katika Viwanja vya Julius Nyerere, Dar es Salaam, ambapo alipata maelezo kuhusu huduma mbalimbali zinazotolewa na TVLA pamoja na kuona aina za chanjo zinazozalishwa kwa ajili ya kuboresha afya ya mifugo.
"TVLA inaendelea kufanya kazi kubwa ya kulinda afya ya mifugo. Chanjo zake ni bora na zimeonyesha matokeo mazuri kwa wafugaji wengi, hivyo ni muhimu wananchi waendelee kuzitumia ili kuongeza uzalishaji na kuchangia maendeleo ya sekta ya mifugo."
“Serikali itaendelea kuhamasisha wafugaji kutumia chanjo zetu za mifugo kwa kuwa zimefanyiwa tafiti za kisayansi, zina ubora unaokidhi viwango na zimekuwa na mchango mkubwa katika kupunguza milipuko ya magonjwa ya mifugo nchini” amesema Bw. Mchatta.
Akimkaribisha Katibu Tawala katika banda la TVLA, Mtaalamu wa Maabara wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania, Bw. Henry Mlundachuma, alisema TVLA ina jukumu la kufanya uchunguzi wa magonjwa ya mifugo, kuzalisha na kusambaza chanjo, kufanya tafiti za mifugo, kusajili na kuhakiki ubora wa viuatilifu vya mifugo pamoja na kutoa huduma za ushauri na mafunzo kwa wadau wa sekta hiyo.
Alieleza kuwa katika maonesho hayo, TVLA imekuwa ikitoa elimu kwa wafugaji na wananchi kuhusu matumizi sahihi ya chanjo, umuhimu wa uchunguzi wa magonjwa kabla ya tiba, pamoja na huduma za maabara zinazosaidia kubaini magonjwa mbalimbali ya mifugo kwa wakati.
Bw. Mlundachuma aliongeza kuwa matumizi ya chanjo bora na huduma za kitaalamu za TVLA ni nguzo muhimu katika kuimarisha afya ya mifugo, kuongeza uzalishaji wa nyama, maziwa na mayai, pamoja na kuimarisha usalama wa chakula na uchumi wa wafugaji.
Banda la TVLA limeendelea kuvutia idadi kubwa ya wageni wanaotembelea Maonesho ya Sabasaba, ambapo wamekuwa wakipata elimu kuhusu huduma mbalimbali za Wakala na namna zinavyochangia maendeleo ya sekta ya mifugo nchini.
Matukio mbalimbali katika picha: Katibu Tawala wa Mkoa wa Tanga, Bw. Rashid Kassim Mchatta, akitembelea banda la Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) yanayoendelea katika Viwanja vya Julius Nyerere, Dar es Salaam, tarehe 9 Julai, 2026. Katika ziara hiyo alipokea maelezo kuhusu huduma mbalimbali zinazotolewa na TVLA, ikiwemo uzalishaji wa chanjo za mifugo, uchunguzi wa magonjwa ya mifugo, huduma za maabara, uhakiki wa ubora na usajili wa viuatilifu vya mifugo, pamoja na tafiti zinazolenga kuboresha afya za mifugo nchini.
SERIKALI KUENDELEA KUWAUNGA MKONO WAZALISHAJI WA NDANI
Na.Mwandishi Wetu
Serikali imeahidi kuendelea kuwaunga mkono wazalishaji wa ndani ili kuongeza uwezo wa uzalishaji na kukuza mauzo ya bidhaa nje ya nchi hatua inayolenga
kuimarisha uchumi wa viwanda na kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika masoko ya kimataifa.
Hayo yamesemwa na Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Judith Kapinga(Mb), Julai 09, 2026 wakati akizungumza na Waandishi wa Habari baada ya ziara yake katika Kiwanda cha Kamal Refinery kilichopo Bagamoyo mkoani Pwani kinachojihusisha na uchakataji wa mafuta machafu ya mitambo na magari (Waste/Used Lube Oil) ili kuyasafisha na kuzalisha mafuta mapya ya vilainishi (lubricants) na mafuta mazito ya viwandani (heavy fuel oil).
Aidha, amesema Sekta ya Viwanda na Biashara imeweka kipaumbele cha juu katika kuongeza minyororo ya thamani ya uzalishaji hapa nchini mkakati unaolenga kupunguza utegemezi na uingizaji wa bidhaa kutoka nje ambazo zina uwezo na sifa ya kuzalishwa kikamilifu na viwanda vya ndani.
Amesema uwekezaji huo umebainika kuwa na manufaa makubwa kimazingira, kwani unachangia kuweka mazingira katika hali ya usafi na usalama katika wakati ambao Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, akiwa kinara na “Champion” wa utunzaji wa mazingira.
Aidha, amesema ili kufanikisha azma hiyo, Sekta ya Viwanda na Biashara itashirikiana kwa karibu na Wizara yenye dhamana ya Mazingira, ambayo tayari ina uhusiano wa kikazi na kiwanda hicho ili kuhakikisha kiwanda hicho kinaongeza uzalishaji na kukuza biashara huku kikizingatia kikamilifu utunzaji endelevu wa ikolojia.
Vilevile, Amewasihi wadau mbalimbali kuunga mkono kiwanda hicho, kinachosaidia kulinda mazingira ya taifa kwa vizazi vijavyo huku akiwataka Watanzania kuendelea kuchangamkia fursa za kiuchumi zinazojitokeza.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Kiwanda hicho Bw. Sameer Santosh ametoa shukrani za dhati kwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuweka mazingira wezeshi ya biashara na kuwaunga mkono wazalishaji wa ndani.
Amesema kiwanda hocho kitaendelea kuongeza zaidi uwezo wa uzalishaji ili kupunguza uingizaji wa bidhaa hizo kutoka nje ya nchi.
Magazetini Leo





























