Thursday, 16 July 2026

SIMAMMIENI MIRADI YA MAENDELEO, PINGENI UKATILI DHIDI YA WATOTO: NAIBU WAZIRI MAHUNDI



Na Jackline Minja, WMJJWM - Kakonko

Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi, amewataka wananchi wa Wilaya ya Kakonko mkoani Kigoma kuendelea kushirikiana na Maafisa Maendeleo ya Jamii, kusimamia na kuendeleza miradi ya kiuchumi inayotekelezwa katika maeneo yao ili kuongeza kipato, kuinua ustawi wa familia na maendeleo ya jamii kwa ujumla.

Mahundi metoa rai hiyo Julai 15, 2026, wakati wa ziara yake ya kukagua shughuli mbalimbali za maendeleo wilayani humo, ikiwemo shughuli za Kikundi cha Wanawake Ubihumwe Kata ya Gwarama, kikundi cha vijana Tuinuane na Shule ya Msingi Itumbike yenye kitengo cha watoto wenye mahitaji maalum.

Amekutana pia na kikundi cha watu wenye ulemavu Kakonko pamoja na kuzindua jengo la kivuli cha Soko la Kijiji cha Kanyonza.

Amesema, Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuweka mazingira wezeshi kwa makundi mbalimbali ya wananchi kupitia mikopo, mafunzo na miradi ya maendeleo, hivyo ni wajibu wa wananchi kuitunza na kuisimamia miradi hiyo ili iwe na tija ya kudumu kwa vizazi vya sasa na vijavyo.

Aidha, amewataka wazazi na walezi kutimiza wajibu wao wa malezi kwa kuwajenga watoto katika maadili mema na kuhakikisha wanakuwa mstari wa mbele kupinga vitendo vya ukatili wa kijinsia vinavyoathiri watoto na wanawake katika jamii.

"Tupige kelele kukataa ukatili wa kijinsia na tuwalinde watoto wetu ili wakue katika mazingira salama yatakayowafanya kuwa raia wema na wenye mchango kwa Taifa," alisema Naibu Waziri Mahundi.

Akizungumza kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Kakonko, Mbunge wa Jimbo hilo, Mhe. Allan Mvano amesema ataendelea kuwa sauti ya wananchi wake kwa kusimamia utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuhakikisha ahadi alizozitoa kwa wananchi zinaendelea kutekelezwa kwa kushirikiana na Serikali, wadau wa maendeleo na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, kuhakikisha kunapatikana matunda katika sekta mbalimbali ya elimu, uwezeshaji wa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu pamoja na kuboresha miundombinu ya huduma za kijamii.








Share:

MRADI WA BARABARA YA LUTUKIRA-SONGEA WABUNGE WATAKA HAKI NA USALAMA KWA WAFANYAKAZI

barabara ya Lutukira-Songea yenye urefu wa kilomita 100 pamoja na barabara ya mchepuko yenye kilomita 16 iliyotembelewa na wabunge wa mkoa wa Ruvuma yenye thamani ya shilingi bilioni 150
Meneja wa TANROADS mkoa wa Ruvuma mhandisi Saleh Juma wa kwanza kutoka kulia akiwa na wabunge wa mkoa wa Ruvuma walipotembelea na kukagua maendeleo ya mradi huo wa barabara ya Songea-lutukira yenye kilomita 100 na barabara ya mchepuko yenye kilomita 16

Na Regina Ndumbaro Songea-Ruvuma.

Wabunge wa mkoa wa Ruvuma wamezitaka taasisi zinazosimamia ujenzi wa barabara ya Lutukira–Songea yenye urefu wa kilomita 100 pamoja na barabara ya mchepuko ya kilomita 16, kuhakikisha haki za wafanyakazi zinalindwa kwa kuzingatia sheria, kanuni na miongozo ya kazi.

Share:

Wednesday, 15 July 2026

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO ALHAMISI JULAI 16, 2026

Share:

MAANDAMANO SAHIHI YANAPASWA KUZINGATIA SHERIA NA HAKI ZA WENGINE- BALOZI SEFUE




Na Mwandishi wetu, Dar

Katibu Mkuu Kiongozi mstaafu, Balozi Ombeni Sefue amesema maandamano ni haki ya msingi inayotambuliwa na Katiba ya Tanzania, sheria za nchi pamoja na makubaliano ya kikanda na kimataifa, akisisitiza kuwa yanapaswa kufanyika kwa kuzingatia sheria na bila kuathiri haki za watu wengine.

Sefue Ametoa kauli hiyo alipokuwa akizungumza na Mtandao wa Mwananchi Digital, akisema kwamba maandamano yanaangukia katika haki ya kujieleza akieleza kwamba maandamano yanayostahili kulindwa kisheria ni yale yanayotekelezwa kwa amani na kufuata masharti yaliyowekwa na sheria.

"Unajua maandamano ni haki ya msingi kwenye Katiba yetu, sheria yetu, makubaliano ya kikanda na kimataifa na maandamano yanaingia kwenye kundi la kujieleza. Tofauti ambayo inaonekana kwenye nchi zetu, watu wanashindwa kutofautisha maandamano yenye sifa ya kujieleza na maandamano ya vurugu," amesema Sefue.

Ameongeza kuwa uhuru wa mtu mmoja haupaswi kukiuka haki za wengine, akitolea mfano maandamano yanayosababisha biashara kufungwa au yanayohusisha vitisho kwa wananchi. "Ukisema mimi naandamana kwa namna ambayo duka langu lifungwe hayo si halali. Hata ukibeba jiwe kwa namna ambayo utamfanya mtu aogope hayo si halali," amesema.

Sefue pia amesisitiza umuhimu wa waandaaji wa maandamano kutoa taarifa kwa Jeshi la Polisi kabla ya kuyafanya ili mamlaka ziweze kutoa ushauri kuhusu njia zitakazotumika na kuhakikisha usalama wa washiriki pamoja na wananchi wengine, akisema utaratibu huo unalenga kuwezesha matumizi ya haki ya kuandamana kwa njia inayozingatia sheria na kulinda maslahi ya jamii kwa ujumla.
Share:

JUMUIYA YA MADOLA YAPONGEZWA, MKWAMO WA KISIASA NI MEZA YA MAZUNGUMZO



Mawaziri wa Jumuiya ya Madola wameipongeza Tanzania kwa juhudi zake za kuendeleza mazungumzo kama njia ya kujenga maridhiano, kuimarisha demokrasia na kudumisha amani. Aidha, Jumuiya imeendelea kuhimiza wadau kuzingatia mazungumzo ya maridhiano kama nyenzo muhimu ya kutatua tofauti na kuimarisha mshikamano wa kitaifa.

Kutokana na umuhimu wa ujumbe huo, inapendekezwa kufanyika mkutano na waandishi wa habari ili kuufafanua na kuuhabarisha umma kuhusu utayari wa Jumuiya ya Madola kushirikiana na Serikali na wadau kuhakikisha mazungumzo tofauti na propaganda ambazo zinaenezwa na wanaharakati ambayo inaonesha kana kwamba serikali imeshinikizwa

Kwa hiyo pendekezo ni kwamba kwenye press conference msisitizo utakuwa ni namna gani Jumuiya ya Madola inasukuma roho ya mazungumzo na maridhiano na jinsi gani Jumuiya inatambua juhudi mfano za Tume ya Uchunguzi ya Jaji CHANDE...kuhusu uchunguzi wa masuala ya jinai na hivyo kuondoa propaganda kwamba hakuna juhudi zozote zile
Share:

SPIKA ZUNGU : TANZANIA IKO TAYARI KUWAKARIBISHA WABUNGE WA DUNIA OKTOBA HII

Na Prosper Makene  

New York, Marekani – Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Musa Azzan Zungu, Mbunge, ameuhakikishia Umoja wa Mabunge Duniani (IPU) kuwa Tanzania imejipanga kikamilifu kuwakaribisha wabunge kutoka duniani kote katika Mkutano wa 153 wa IPU utakaofanyika Oktoba 2026 jijini Arusha.

Mhe. Zungu ametoa hakikisho hilo wakati wa kikao na Rais wa IPU, Mhe. Dkt. Tulia Ackson, Mbunge, pamoja na Katibu Mkuu wa IPU, Balozi Anda Filip jijini New York, Marekani.

Kikao hicho kililenga kupitia hali ya maandalizi, mipango ya kilojisti na uhakika wa utayari kabla ya mkutano huo mkubwa wa kibunge duniani.

Spika ameeleza kuridhishwa na kazi ya Kamati ya Kitaifa ya Maandalizi inayoratibu tukio hilo. Amesema mipango yote ya kilojisti, kiprotocol na usalama inaendelea kama ilivyopangwa, na Tanzania imejitolea kutoa ukaribisho wa kiwango cha kimataifa.

Mhe. Zungu amesisitiza kuwa kuandaa mkutano huo ni jambo la fahari kwa Taifa na ni fursa muhimu ya kuimarisha nafasi ya Tanzania katika diplomasia ya kibunge duniani.

Ameongeza kuwa Mkutano huo utakuwa jukwaa muhimu la majadiliano, ushirikiano na utafutaji wa masuluhisho ya changamoto zinazolikabili dunia leo. Tanzania inajivunia kuwakaribisha Maspika, Wabunge na wajumbe kutoka pande mbalimbali za dunia jijini Arusha, mji unaojulikana kwa amani na diplomasia.

Katibu Mkuu wa IPU, Balozi Anda Filip, naye amepongeza Tanzania kwa maendeleo yaliyopatikana katika maandalizi. Amethibitisha kuendelea kwa ushirikiano na msaada wa Sekretarieti ya IPU kwa Bunge la Tanzania ili kuhakikisha mafanikio ya Mkutano huo 

Mkutano wa 153 wa IPU unatarajiwa kuhudhuriwa na washiriki zaidi ya 1,500 wakiwemo Waspika wa Bunge, Wabunge na wajumbe kutoka mabunge 180 wanachama wa IPU na wanachama 15 washirika.

Ajenda ya Mkutano itagusa masuala mbalimbali ya kimataifa. Miongoni mwa masuala hayo ni pamoja na mabadiliko ya tabianchi, amani na usalama, utawala wa teknolojia, haki za binadamu, usawa wa kijinsia, na jukumu la mabunge katika kuharakisha utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu. Mpango wa mkutano utajumuisha mijadala ya wazi, vikao vya kamati na mikutano ya pande mbili baina ya ujumbe.

Arusha, inayofahamika kama 'Geneva ya Afrika' imechaguliwa kuwa mwenyeji kutokana na sifa yake ya kimataifa kama kituo cha diplomasia, amani na mikutano ya kimataifa.

Mji huo una historia ya kuandaa mikutano mikubwa ya kimataifa ikiwemo vikao vya Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu wa Rwanda na mikutano mbalimbali ya Umoja wa Mataifa na Umoja wa Afrika.

Serikali ya Tanzania imesema Mkutano huo utaleta manufaa makubwa kwa mji wa Arusha na kwa Taifa kwa ujumla. Manufaa yanayotarajiwa ni pamoja na kukuza utalii, huduma za ukaribishaji na ubadilishanaji wa kitamaduni. Pia tukio hili litaonesha miundombinu ya Tanzania na uwezo wake wa kuandaa mikutano mikubwa ya kimataifa.


Share:

Tuesday, 14 July 2026

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMATANO JULAI 15, 2026

Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger