Wednesday, 10 June 2026

TANZANIA YAIELEZEA DUNIA HATUA ZILIZOPIGWA KATIKA KULINDA HAKI ZA WATU WENYE ULEMAVU


Na Mwandishi wetu-New York, Marekani.


Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi, ameieleza Jumuiya ya Kimataifa hatua kubwa zinazochukuliwa na Serikali ya Tanzania katika kulinda na kuendeleza haki za watu wenye ulemavu, wakati aliposhiriki Mkutano wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (COSP19) unaofanyika katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, Jijini New York, Marekani.

Mhe. Mahundi, ambaye amemuwakilisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Sera, Bunge na Uratibu na Wenye Ulemavu, Mhe. Profesa Palamagamba John Kabudi, amesema Tanzania imeendelea kuimarisha mifumo ya kisheria, kisera na kiutendaji ili kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata haki, fursa na huduma stahiki kama wananchi wengine.

Akiwasilisha taarifa ya nchi, Mhe. Mahundi amesema Tanzania imepiga hatua kubwa kupitia Sheria ya Watu Wenye Ulemavu Na. 9 ya mwaka 2010 kwa Tanzania Bara pamoja na Sheria Na. 8 ya mwaka 2022 ya Zanzibar, ambazo zimeweka msingi imara wa kulinda haki na ustawi wa watu wenye ulemavu.

“Masuala ya ulemavu yamejumuishwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na mipango mbalimbali ya maendeleo ili kuhakikisha hakuna anayebaki nyuma katika safari ya maendeleo ya taifa na kusema kuwa Serikali imeendelea kupanua upatikanaji wa elimu jumuishi, huduma za afya, huduma za urekebishaji na tiba, teknolojia saidizi, programu za uwezeshaji kiuchumi pamoja na huduma za hifadhi ya jamii kwa watu wenye ulemavu” amesema Mhe. Mahundi.

Aidha Mhe. Mahundi amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa uongozi wake madhubuti na dhamira ya dhati ya kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata huduma bora na fursa zinazowawezesha kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya nchi.

“Serikali ya Tanzania itaendelea kushirikiana na nchi wanachama, Umoja wa Mataifa, asasi za kiraia na watu wenye ulemavu wenyewe katika kuharakisha utekelezaji wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu na kujenga jamii jumuishi inayoheshimu usawa, utu na haki za kila mtu,” amesema Mhe. Mahundi.

Mkutano huo wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu umebeba kaulimbiu inayosema “CRPD at 20: Celebrating and Consolidating Achievements and Shaping the Next Phase of Implementation in a Changing World,” ukilenga kutathmini mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha miaka 20 tangu kuanzishwa kwa mkataba huo na kuweka mikakati ya kuendeleza utekelezaji wake duniani.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMATANO JUNI 10, 2026

magazerini Leo



Share:

Tuesday, 9 June 2026

RAIS SAMIA: TANZANIA INATAFUTA WASHIRIKA WA KIUCHUMI, HAIEGEMEI UPANDE WOWOTE


Na Beda Msimbe, TBN, Petersburg, Urusi - Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, amezitaka nchi za Magharibi na wachambuzi wa mambo ya kisiasa kuondoa hofu yoyote ile kuhusu ushirikiano wa nchi yake na Urusi, akisisitiza kuwa Tanzania ni nchi isiyofungamana na upande wowote na inaongozwa na diplomasia ya kiuchumi yenye kulinda maslahi ya taifa kwanza.


Kauli hiyo imekuja kufuatia maswali na hisia zilizoibuka kuhusu ziara yake nchini Urusi, ambapo baadhi ya waandishi wa habari walieleza uwepo wa dhana kwamba Tanzania huenda inaikabili mgongo nchi za Magharibi na kugeukia upande wa Mashariki kiitikadi.


Akizungumza pembezoni mwa Jukwaa la Uchumi la Kimataifa la St. Petersburg (SPIEF), Rais Samia alifafanua kuwa Tanzania haihamishi nguvu zake kutoka upande mmoja kwenda mwingine, bali inatanua wigo wa washirika ili kukuza uchumi na kuinua maisha ya wananchi wake.


Rais alieleza kuwa msimamo huu una mizizi mirefu ya kihistoria tangu enzi za Muasisi wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, ambaye miaka 57 iliyopita alipotembelea Urusi alisisitiza falsafa hiyohiyo ya kutofungamana na upande wowote.


Aliongeza kuwa Watanzania wa sasa wanachotaka ni diplomasia ya uchumi inayofungua fursa za biashara na uwekezaji, na serikali inakaribisha taifa lolote lililo tayari kushirikiana nayo bila kujali tofauti zao za kijiografia.


Akitolea mfano uwiano wa washirika wa Tanzania, Kiongozi mkuu huyo wa nchi alitaja kuwa nchi yetu ina uhusiano imara sana na Marekani, ambayo inaongoza kwa uwekezaji mkubwa nchini kukiwa na zaidi ya kampuni 500 za Kimarekani zilizowekeza katika sekta za utalii na migodi.


Vilevile alitaja ushirikiano mzuri na China katika sekta ya miundombinu na uchukuzi, India katika biashara, Japan katika nishati na elimu, pamoja na mataifa ya Ulaya, Australia, Uingereza, na Ufaransa yanayochangia maendeleo kupitia programu mbalimbali za uwezeshaji wa kifedha.


Rais Samia alihitimisha kwa kusema kuwa kuelekea utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa ya Mwaka 2050 inayolenga kukuza uchumi kufikia thamani ya dola trilioni moja, Tanzania haitasita kushirikiana na nchi yoyote inayoweza kuwa mshirika mzuri wa kibiashara, kwani lengo kuu si ushindani wa kisiasa bali ni ustawi wa wananchi wa Tanzania.
Share:

KAULI YA UMMY MWALIMU BAADA YA UTEUZI MPYA

Uteuzi wa Ummy ulitangazwa Juni 2, 2026 na Katibu Mkuu Kiongozi, Moses Kusiluka kupitia Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, Bakari Machumu ukimrejesha katika eneo la afya ambalo amekuwa akilihudumia kwa miaka kadhaa akiwa serikalini.


Waziri wa zamani wa Afya, Ummy Mwalimu amemshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa imani aliyompa huku akiahidi kutekeleza majukumu yake kwa weledi, bidii na uaminifu.


Ummy ametoa shukurani hizo ikiwa ni siku sita baada ya kuteuliwa kuwa Mshauri wa Rais wa masuala ya afya ya uzazi, mama na mtoto.


Kupitia ujumbe aliouchapisha kwenye mtandao wa Instagram leo Juni 8, 2026 na kuweka taarifa ya Ikulu ya uteuzi wake, Ummy amesema anashukuru kwa baraka za Mwenyezi Mungu na kwa heshima kubwa aliyopewa na Rais Samia kupitia uteuzi huo.


“Kwa heshima na unyenyekevu mkubwa namshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk Samia Suluhu Hassan kwa kuniamini na kuniteua kuwa Mshauri wake wa masuala ya afya ya uzazi, mama na mtoto,” ameandika Ummy.



Mbunge huyo wa zamani wa Tanga Mjini amesema atatumia nafasi hiyo kutekeleza wajibu wake kwa kuzingatia dhamana kubwa aliyopewa Rais Samia, ambaye pia ametambuliwa na viongozi wa Afrika kama kinara wa afya ya mama na mtoto wa Umoja wa Afrika (African Union Champion for Maternal and Child Health).


Katika ujumbe huo, Ummy pia amewashukuru watu mbalimbali waliomtumia salamu za pongezi na kumuombea mafanikio baada ya uteuzi wake.


Uteuzi wa Ummy ulitangazwa Juni 2, 2026 na Katibu Mkuu Kiongozi, Moses Kusiluka kupitia Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Bakari Machumu ukimrejesha katika eneo la afya ambalo amekuwa akilihudumia kwa miaka kadhaa akiwa serikalini.


Kabla ya uteuzi huo, Ummy aliwahi kuwa Mbunge wa Viti Maalumu kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM) na aliwahi kushika nyadhifa mbalimbali za uwaziri katika Serikali ya awamu ya tano na ya sita.


Mwaka 2015 aliteuliwa kuwa Naibu Waziri katika Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira kabla ya kuhamishiwa Wizara ya Afya mwaka 2017 ambako alihudumu kama Waziri wa Afya hadi mwaka 2024.

Na Mwananchi Digital
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMANNE JUNI 9,2026

Magazeti
 


Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger