Wednesday, 20 May 2026

TANZANIA KUJIFUNZA KUTOKA CHINA KUHUSU MAGEUZI YA MASHIRIKA YA UMMA

Na Mwandishi wa OMH

Dar es Salaam. Tanzania imeonesha nia ya kutumia uzoefu wa China katika mageuzi ya mashirika ya umma, ikiwa ni sehemu ya mkakati mpana wa serikali wa kuongeza ufanisi, faida na uwajibikaji katika uwekezaji wa umma.

Nia hiyo ilibainishwa Jumatatu, Mei 18, 2026, wakati Balozi wa China nchini Tanzania, Chen Mingjian, pamoja na ujumbe wake, walipotembelea Ofisi ya Msajili wa Hazina jijini Dar es Salaam na kufanya mazungumzo na menejimenti ikiongozwa na Msajili wa Hazina, Nehemiah Mchechu, kuhusu uwekezaji, maendeleo ya miundombinu na uhamishaji wa teknolojia.

Akizungumza katika kikao hicho, Bw. Mchechu alisema Tanzania inalenga kujifunza kutoka China katika kusimamia na kuleta mageuzi ya mashirika ya umma kupitia mfumo wa Tume ya Usimamizi na Uendeshaji wa Mali za Serikali ya China (SASAC), akibainisha kuwa Ofisi ya Msajili wa Hazina ni taasisi ya kimkakati yenye dhamana ya kusimamia uwekezaji wa Serikali.

Alisema kutokana na jukumu hilo, Ofisi ya Msajili wa Hazina inaona umuhimu wa kuwa na ushirikiano wa karibu na taasisi za China, hususan katika maeneo ya uwekezaji, usimamizi wa mashirika ya umma na utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

“Tunapofanya mageuzi ya taasisi zetu, tunataka kujifunza kutoka kwa nchi ambazo zimefanikiwa kupitia njia hii. China ni mojawapo ya mifano bora duniani katika kufanya mageuzi kwenye mashirika ya umma,” alisema.

Bw. Mchechu alisema baadhi ya mashirika yanayosimamiwa na Ofisi ya Msajili wa Hazina tayari yana ushirikiano mzuri na taasisi mbalimbali za China, hali ambayo imeongeza umuhimu wa kuimarisha zaidi ushirikiano kati ya pande hizo mbili.

Pande hizo mbili pia zilijadili umuhimu wa kubadilishana uzoefu katika usimamizi wa mashirika ya umma, utekelezaji wa mageuzi ya taasisi pamoja na maendeleo ya miundombinu na uhamishaji wa teknolojia.

Bw. Mchechu alisema Ofisi ya Msajili wa Hazina kwa sasa inasimamia taasisi na kampuni 308 ambazo serikali ina uwekezaji, zikiwemo 252 ambazo Serikali ina hisa nyingi.

Alieleza kuwa uwekezaji huo umefanywa katika sekta mbalimbali muhimu ikiwemo usafiri wa anga, nishati, mafuta na gesi pamoja na madini.

Aidha, alisema serikali inaendelea na mageuzi ya kupunguza utegemezi wa ruzuku, kuongeza mchango wa gawio serikalini, kuimarisha uwajibikaji wa taasisi na kutoa uhuru zaidi wa kiutendaji kwa mashirika ya umma.

“Hata kama tunataka uchumi uongozwe na sekta binafsi, sekta ya umma isiyo na ufanisi itaendelea kuwa kikwazo kwa sekta binafsi kustawi,” alisisitiza.

Katika mazungumzo hayo, Bw. Mchechu pia aligusia ushirikiano unaoendelea kati ya Tanzania na China katika miradi ya kimkakati ikiwemo usafiri wa majini, madini na uendeshaji wa bandari.

Pia aliishukuru China kwa kuendelea kutoa fursa za mafunzo kwa watumishi wa Ofisi ya Msajili wa Hazina, akieleza kuwa watumishi sita walinufaika na mafunzo mwaka jana huku wengine watatu wakitarajiwa kupata mafunzo mwaka huu.

“Mafunzo haya yamekuja wakati muafaka na yana mchango mkubwa katika kujenga uwezo wa watumishi wetu,” alisema.

Akizungumza katika kikao hicho, Balozi Mingjian alisema China iko tayari kushirikiana na Tanzania katika kubadilishana uzoefu wa mageuzi ya kiuchumi na mabadiliko ya taasisi.

Alisema sera ya Mageuzi na Ufunguaji Uchumi ya China iliyoanza mwaka 1978 ilisaidia kuibadilisha nchi hiyo kiuchumi licha ya changamoto kubwa katika miaka ya awali ya utekelezaji.

“Tuko tayari kabisa kushirikiana na ndugu zetu wa Tanzania katika uzoefu huu wa kitaasisi,” alisema.

Aliongeza kuwa China itaendelea kuunga mkono ajenda ya Tanzania ya viwanda kupitia biashara, miundombinu, teknolojia na mafunzo ya watumishi.

Pia alibainisha kuwa serikali ya China itaendelea kutoa nafasi za mafunzo kwa watumishi wa umma wa Tanzania katika maeneo ya mabadiliko ya kidijitali, utawala na usimamizi wa uchumi.


Balozi mingjian alisema Tanzania na China zimekuwa na uhusiano wa muda mrefu wenye kuaminiana, akitaja ziara ya Rais Samia Suluhu Hassan nchini China mwaka 2022 kuwa sehemu ya juhudi za kuimarisha ushirikiano wa kimkakati kati ya mataifa hayo mawili.

Kikao hicho pia kilijadili namna ya kuimarisha ushirikiano katika uongezaji thamani wa madini, ambapo Tanzania inalenga kuanzisha viwanda vya ndani vya kusafisha na kuchakata madini ya kimkakati.

Vilevile, pande hizo mbili zilijadili mustakabali wa Mamlaka ya Reli ya Tanzania na Zambia (TAZARA), ambayo mwaka huu inatimiza miaka 50 ya uendeshaji wa kibiashara.







Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMATANO MEI 20, 2026

 Magazeti leo






 

        
 


Share:

WAGONJWA 15 WA MIFUPA WANUSURIKA KUFA KWA MOTO WAKIPATA MATIBABU NYUMBANI KWA MGANGA WA KIENYEJI KAHAMA

Na William Bundala, Kahama – Shinyanga.

Zaidi ya wagonjwa 15 wa mifupa wamenusurika kufa kufuatia nyumba ya mganga wa tiba asili anayeunga mifupa kwa njia ya kienyeji kuteketea kwa moto wakati wakiendelea kupatiwa matibabu katika mtaa wa Mbulu Misheni manispaa ya Kahama mkoani Shinyanga.

Wakizungumza na Jambo Fm baadhi ya wagonjwa wamesema kuwa walisikia kelele za watu wakivunja milango na ndipo wakapata msaada wa kubebwa na kutolewa nje wakati moto huo ukielekea kwenye vyumba vyao.

“Ilikuwa hali ya taharuki sana kwani tulisikia kelele za wananchi na wengine walikuja kwenye milango ya vyumba vyetu na kuingia ndani kisha wakaanza kututoa nje wakati moto ukizidi kuja kwenye vyumba vyetu” Amesema Hamis Simon na John Makoye wagonjwa wa mifupa ya miguu walionusurika.

Katika hatua nyingine wamesema kuwa walitumia nguvu kujivuta kwenda nje ili kujiokoa licha ya kwamba wengine walijitonesha majeraha yao wakati wa purukushani za kujiokoa huku wakilalamika kuibiwa mali zao na baadhi ya vijana waliokuwa wanaowakoa.

“Tunashukuru Mungu tumetoka salama changamoto ni wakati wa purukushani za kujiokoa tumejitonesha majeraha yetu yaliyoaza kupona na baadhi yetu tumeibiwa vitu vyetu na vijana ambao walikuwa wanaingia vyumbani kutupa msaada” amesema Hassan Ahmed na Tumaini Duru walionusurika.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa serikali ya mtaa wa Misheni Solomoni Ruta amesema kuwa alipata taarifa majira ya saa kumi jioni ndipo akatoa taarifa kwa mamlaka husika na kupata ushirikiano mkubwa toka kwa wananchi ambao katika hatua za awali walijitaidi kuuzima moto huo na kutoa nje vitu vilivyowezekana.

“Nilipata taarifa toka kwa wananchi majia ya saa kumi jioni na tukawataarifu zima moto,na waipokuja wafanya jitihada kwa kushirikiana na wananchi hatimaye kufanikiwa kuuzima moto huu,niwashukuru sana wananchi wa mtaa wa Mbulu Misheni kwa kujitoa kusaidia uzimaji wamoto huu katika hatua za awali na kufanikiwa kutoa nje baadhi ya vitu,” amesema Ruta Mwenyekiti wa mtaa wa Mbulu Misheni.

Akielezea Chanzo cha moto huo Mkaguzi msaidizi wa jeshi la Zima moto na uokoaji Wilaya ya Kahama Hafidhi Omary amesema chanzo cha moto huo ni mmmoja wa wajukuu wa familia hiyo mwenye umri wa miaka 5 kuchezea kiberiti cha gesi kwenye chumba cha bibi yake kwa kukiwasha na kukielekeza kwenye godoro na kusababisha moto huo.

“Tulifika hapa na kuanza kuzima moto huu,tumefanikiwa kuokoa vyumba vinane na vyumba vinne vimeungua kabisa,na baada ya uchunguzi tumebaini chanzo cha moto huu ni mtoto ambaye ni mjukuu wa familia hii kuchezea kiberiti cha gesi kwa kukiwasha na kukielekeza kwenye godoro ndipo moto huo ukawaka.“ Amesema Hafidhi.

Katika hatua nyingine Jeshi la zima moto na uokoaji wilayani Kahama limewataka wananchi kutoa taarfa mara tu moshi unapoanza kutoka kwa kupiga namba ya bure ya 114 badala ya kusubiri uwashide ndiopo watoe taarifa.

“Tuwaombe wananchi toeni taarifa mara tu moto unapoanza kwa kutupigia simu namba 114,msianze kuzima moto ukiwashida ndipo mtoe taarifa,wengine wakati wanazima basi wengine wapige simu kwetu ili tufike haraka eneo la tukio,” amesisitiza Omary.

Wagonjwa walionusurika katika ajali hiyo ni Joseph Mashauzi,George Joseph,Yunge Mnduka,Elius Ephrahim,Rose Raiza,Samson Deus,Roda Tobotobo na Juma Jumanne.

Wengine ni Magembe Magire,Hassan Ahmed,Tumaini Duru,Zephania Silas,Salum Peter,Hamis Simoni na John Makoye.



CHANZO - JAMBO FM
Share:

Tuesday, 19 May 2026

SERIKALI YASISITIZA UHURU WA KUKOSOA SI MATUSI

WAZIRI wa Katiba na Sheria, Dk Juma Homera amesema watu wanaoitukana Serikali, kufanya uchochezi na vitendo visivyo vya maadili mitandaoni, majina yao yameshakabidhiwa kwa Wizara ya Mambo ya Ndani ili Jeshi la Polisi ili wachukuliwe hatua za kisheria.

Aliyasema hayo jana wakati akifungua mkutano wa siku wa mafunzo kwa mawakili wa serikali yaliyoandaliwa na Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali jijini Arusha.

Dk. Homera alitoa kauli hiyo akijibu ombi la Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Dk. Damas Ndumbaro aliyetaka mawakili wa serikali kuisaidia Serikali dhidi mashambulizi na upotoshaji unaofanywa mitandaoni.

Dk. Homera alisema majina ya wahusika wa uhalifu huo tayari yamekabidhiwa Wizara ya Mambo ya Ndani kwa hatua za kisheria.

Alisema kuna Sheria ya Mitandao, sheria za Jeshi la Polisi na sheria ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) ambazo zinadhibiti upotoshaji, uchochezi na uvunjifu wa maadili, hivyo serikali itahakikisha inazisimamia ili kukomesha uhali huo nchini.

"Serikali haikatai kukosolewa, lakini ikoselewa kwa jambo la haki na kweli na si jambo la uongo, na kutumia lugha ya matusi au uchochezi, hivyo wahusika watachukuliwa hatua za kisheria ili kuimarisha amani na usalama,"alisisitiza Dk Homera.

Aliongeza"Jeshi la Polisi limeanza kuchukua hatua dhidi ya wanaoitukana serikali, kufanya uchochezi na vitendo visivyo vya maadili mitandaoni."

Kuhusu mafunzo hayo, alisema yatawasaidia mawakili wa serikali kuishauri serikali ipasavyo na kwa weledi, kuwa na uelewa mpana wa masuala mbalimbali, kujengewa uelewa kuhusu miradi ya ubia kati ya sekta ya umma na sekta binafsi (PPP) na masuala mengine mbalimbali.

Alisema Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali inafanya kazi nzuri ya kuitetea serikali katika mashauri mbalimbali na kufanikiwa kuisadia serikali kuokoa zaidi ya shilingi trilioni moja kwa kushinda kesi hizo.

Naye Wakili Mkuu wa Serikali, Dk Ally Possi alisema katika kipindi cha Julai 2025 hadi Machi 2026, kati ya mashauri 641, serikali ilishinda mashauri 595 sawa na asilimia 88.1 na kuokoa Sh bilioni 316.3 ambayo serikali ingelipa kama ingeshindwa mashauri hayo.

Kuhusu mashauri ya usuluhishi, alisema mashauri 18 yamekamilika na serikali kuokoa Sh bilioni 6.8 katika kipindi hicho.

"Kwa hiyo katika mashauri yote ya madai na usuluhishi kuanziaJulai 2025 hadi Aprili 2026, Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali tumeisadia Serikali kuokoa shilingi trilioni 1.35,"alisema Dk Possi.

Aliongeza"Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali ilianzishwa mwaka 2018, na moja ya mafanikio makubwa tuliyoyapata ni kuitetea serikali katika kesi ya kukamatwa kwa ndege yetu na kushinda."

Pia alisema mafunzo hayo kwa mawakili wa serikali yanalenga kulinda kila senti ya mlipakodi, kutetea rasilimali za serikali, kuongeza uwezo wa mawakili katika nyanja mbalimbali, kujinoa kitaaluma, na kuendesha mashauri kwa weledi na umahiri.

Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Dk. Damas Ndumbaro alisema kuna haja kwa mawakili wa serikali kuja na mpango wa namna ya kuitetea serikali dhidi ya mashambulizi na upotoshaji mkubwa dhidi ya serikali.

"Nini nafasi ya mawakili wa Serikali katika jambo hili? Nashauri kupitia mafunzo haya jadilianeni nini cha kufanya ili kuihudumia nchi na jamii yetu kwa weledi,"alisema Dk. Ndumbaro

Pia alisema kwa kuwa asilimia 36 ya migogoro yote iliyoibuliwa na timu ya Msaada wa Kisheria ya Samia imetokana na ardhi, hivyo alimuomba Wizara ya Katiba na Sheria kulifanyia utafiti jambo hilo ili kujua chanzo na kuja na suluhu ya kuikomesha migogoro hiyo.

Dk Ndumbaro aliwataka mawakili hao wa serikali kujifunza kwa vitendo kupitia mashauri mbalimbali wanayoshinda na kushindwa ili kufanya mabadiliko ya kisheria yanayohitajika kwa maslshi ya taifa na kuleta ufanisi katika sekta ya sheria.

Kwa mujibu wake, Februari 2018, Tanzania ilifanya mageuzi makubwa katika sekta ya sheria nchini kwa kupangilia upya nafasi tatu ikiwemo Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali na Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP).

Alisema mageuzi hayo yamesaidia kuleta ufanisi katika sekta ya sheria nchini.

Naye Naibu Wakili Mkuu wa Serikali, Alice Mtulo alisema mafunzo hayo yanalenga kuwajengea uwezo Mawakili wa serikali kuhusu uendedhaji wa mashauri ya madai na usuluhishi.

Alisema jumla ya washiriki 600 wanahudhuria mafunzo hayo wakiwemo mawakili kutoka Wizara ya Katiba na Sheria, taasisi za serikali na Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali.

Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Samwel Maneno alisema mawakili wa serikali wanawajibu wa kuisaidia serikali kwa kutoa ushauri mzuri wa kisheria pale serikali inapoingia mikataba na sekta binafsi ambayo ni injini ya uchumi wa taifa.

Maneno alisema Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali imeshasajili mawakili zaidi ya 30 katika kitengo cha ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi (PPP) katika kutekeleza miradi ya ubia.

Naye Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali Zanzibar, Shaaban Abdalla aliwataka mawakili hao wa serikali kusimamia mashauri ya madai na usuluhishi kwa weledi na uzalendo kupitia mafunzo wanayopewa.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama Tanzania, Profesa Elisante Ole Gabriel alisema kwa kuwa Mahakama ni chombo cha juu na cha mwisho katika kutoa haki, hivyo Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali ni mdau muhimu katika jambo hilo.
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger