Friday, 24 April 2026

MKUTANO WA KIKANDA WAJADILI USALAMA NA BIASHARA YA SILAHA HARAMU



Na Mwandishi Wetu,DAR ES SALAAM

Makamu Mwenyekiti wa RECSA na ‎Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhe. Paschal Katambi Patrobass (Mb), ameshiriki Mkutano kwa njia ya Mtandao wa Kamati Ndogo ya Mawaziri ya Kikanda, unaoshughulikia Udhibiti wa Silaha ndogo na nyepesi katika Ukanda wa Maziwa Makuu na Pembe ya Afrika (RESCA).

‎Kikao hicho, kimewakutanisha Mawaziri wa Usalama kutoka nchi wanachama, kikiwa na lengo la kujadili Hali ya Usalama katika ukanda huo pamoja na changamoto zinazoendelea kujitokeza, hususani Usambazaji na Matumizi Haramu ya Silaha ndogo na nyepesi.

Ametoa kauli hiyo baada ya Kikao cha Saba cha nchi wanachama wa Kituo cha Kikanda Kinachoshughulika na Udhibiti wa Silaha katika Nchi za Maziwa Makuu na Pembe ya Afrika (RECSA),ngazi ya mawaziri kinachojumuisha nchi ya Tanzania,Burundi,Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo(DRC), Rwanda,Uganda,Kenya,Somalia,Sudan,Sudan Kusini, Ethiopia, Eritrea, Djibouti, Jamhuri ya Kongo na Jamhuri ya Kati, kilichofanyika kwa njia ya mtandao ambapo masuala mbalimbali yalijadiliwa ikiwemo udhibiti wa silaha na kupambana na biashara haramu ya silaha.

Amesema sambamba na hilo, Serikali kupitia Wizara ya mambo ya ndani ya Nchi imejipanga kimkakati kuimarisha ulinzi na usalama wa Mifumo ya Uthibiti katika Uingizaji Silaha,Kuangalia Dhana nzima ya Umiliki na Wajibu wa Mmiliki, Tathmini ya Matumizi sahihi ya Silaha,Ukaguliwaji wa Silaha,Lengo na Dhamira ya Muombaji na Mmiliki wa Silaha, Tabia na mienendo hatarishi ya mmiliki wa Silaha na kuimarisha mifumo ya kiteknolojia na Kidigitali katika kudhibiti Silaha.

“Nchi yetu ni nchi ya Muungano Kikatiba, yenye misingi ya kisheria, sera madhubuti, zinazochochea Amani, Mshikamano na Utulivu,Tanzania ni Nchi mwanachama wa RECSA, tumeendelea kuwahakikishia wanachama wenzetu kuwa nguzo ya amani na utulivu ndani na nje ya mipaka yetu.

 Tunashirikiana pamoja katika doria ili kudhibiti na kupunguza silaha ndogondogo na nyepesi zinazozunguka kinyume na sheria. Katika dhana nzima ya udhibiti wa silaha, serikali tumedhamiria kuimarisha mifumo ya uingizaji wa silaha,utambuzi wa mifumo ya uingizaji,umiliki na wajibu wa mmiliki,ukaguliwaji wa silaha,pamoja na tathmini ya matumizi sahihi ya silaha kuondoa matishio ya amani ndani na nje ya kanda ya pembe ya Afrika.” Amesema Mheshimiwa Katambi

Mhe. Katambi pia amewataka wamiliki wa silaha hapa nchini, kuzingatia kikamilifu masharti ya umiliki wa silaha zao pamoja na kulipia leseni za silaha wanazomiliki ikiwa ni takwa la kisheria ambapo kwa mujibu wa kifungu cha 20 cha Kanuni za Udhibiti wa Silaha na Risasi za mwaka 2016 linalomtaka kila mmiliki wa silaha nchini kulipia Leseni za Bastola, Shotgun na Rifle na ada hiyo ya Leseni hulipwa kuanzia tarehe 1 Julai hadi 30 Septemba kila mwaka.

Ametoa agizo kwa wale wanaomiliki au kukaa na Silaha kinyume cha Sheria iwe kwa kupewa, kuokota, kurithishwa, kupora au kwa namna yoyote isivyo kisheria kuzisalimisha haraka katika Kituo cha Polisi au kutoa taarifa za siri kufichua umiliki wa kinyemera kwa ajili ya Usalama wa Raia na Mali zao pia Amani ya Nchi yetu.


Share:

Video Mpya : SHINJE ORIGINAL - YA MOTO BALAA

 

Share:

TAMCU YAIMARISHA UCHUMI WA WAKULIMA TUNDURU KWA UNUNUZI WA MALORI MAPYA MATANO

Mkuu wa Wilaya ya Tunduru Mhe.  Denis Masanja watatu kutoka kulia akiwa anakata utepe wakati wa kukabidhi magari hayo mapya matano ya chama cha Ushirika Tunduru (TAMCU) limited Mwenyekiti wa Chama kikuu cha ushirika wilaya ya Tunduru (Tamcu) Musa Manjaule kushoto na meneja masoko wa Benki ya Crdb kanda ya kusini  Emanuel Bigailo wakisaini hati ya makabidhiano ya malori matano mapya yaliyonunuliwa na Tamcu baada ya kupata mkopo kutoka Crdb,nayeshuhudia katikati Mkuu wa Wilaya ya Tunduru Deni Masanja.

Na Regina Ndumbaro Tunduru-Ruvuma 

Chama Kikuu cha Ushirika Wilaya ya Tunduru (TAMCU) kimechukua hatua kubwa ya kuongeza ufanisi katika sekta ya kilimo kwa kununua malori matano mapya ya kubebea mazao, hatua inayolenga kurahisisha usafirishaji na kuongeza mapato ya chama pamoja na wanachama wake. 

Uamuzi huo umepokelewa kwa furaha na wakulima wa wilaya hiyo ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakikumbwa na changamoto ya ucheleweshaji wa mazao kufika sokoni kutokana na uhaba wa vyombo vya usafiri.

Akizungumza kwa niaba ya wakulima, Rashid Chibwana amesema kuwa malori hayo yatasaidia kuwafikia wakulima mashambani na kusafirisha mazao yao kwa wakati hadi maghala na hatimaye kwenye minada. 

Amebainisha kuwa hapo awali walitegemea chanzo kimoja cha mapato, lakini uwekezaji huo mpya utaongeza mapato ya chama huku ukipunguza gharama na usumbufu wa usafirishaji.

Mwenyekiti wa TAMCU, Mussa Manjaule, amesema ununuzi wa malori hayo umetokana na maombi ya wanachama waliotaka kuboreshwa kwa huduma za usafirishaji pamoja na kuongeza vyanzo vya mapato. 

Ameeleza kuwa awali walikuwa wanapata changamoto hata katika kusafirisha pembejeo kama viuatilifu kutoka mikoa jirani, lakini sasa hali hiyo itaboreshwa kwa kiasi kikubwa.

Kwa upande wake, Meneja wa Benki ya CRDB Tawi la Tunduru, Emanuel Mwasuka, amesema benki hiyo imechangia sehemu kubwa ya fedha zilizotumika kununua malori hayo yenye thamani ya shilingi bilioni 1.5. 

Ameahidi kuendelea kushirikiana na vyama vya ushirika kwa kutoa mikopo, huku akisisitiza umuhimu wa kuyatunza malori hayo ili yadumu na kuleta tija inayokusudiwa.

Mkuu wa Wilaya ya Tunduru, Denis Masanja, ameipongeza TAMCU kwa hatua hiyo akieleza kuwa ni mfano bora wa maendeleo katika sekta ya ushirika. 

Amesema uwekezaji huo utachochea biashara ya mazao kama korosho, ufuta na mbaazi, kupunguza gharama za usafirishaji na kuongeza kipato kwa wakulima, huku akitoa wito kwa wanachama kushirikiana na viongozi wao ili kufanikisha malengo ya chama.


Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO IJUMAA APRILI 24,2026


Magazeti
 
Share:

Thursday, 23 April 2026

HAMU YA MARIDHIANO: VIONGOZI WA DINI NA WANASIASA WAHIMIZA AMANI BAADA YA RIPOTI

 

Viongozi wa dini na wanasiasa nchini wametoa mwito wa dhati kwa Watanzania kudumisha amani, utulivu, na mshikamano kufuatia kukamilika na kuwasilishwa kwa ripoti ya Tume ya Kuchunguza Matukio Wakati na Baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025. Ripoti hiyo inawasilishwa leo Aprili 23,2026.

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maridhiano na Amani Tanzania (JMAT), Alhad Mussa Salum, amesisitiza kuwa huu ni wakati wa kujenga imani miongoni mwa wananchi na kuamini uwezo wa ndani katika kutatua changamoto za kitaifa bila kutegemea msaada wa nje. 

Salum amebainisha kuwa tume hiyo iliyoongozwa na Jaji Mkuu mstaafu, Mohamed Chande Othman, ina wajumbe wenye weledi mkubwa, hivyo ni muhimu ripoti hiyo ipokewe, ichambuliwe, na iwapo kutakuwa na upungufu, mifumo iliyopo itumike kurekebisha badala ya kujenga chuki.

Kiongozi huyo wa JMAT ameongeza kuwa kutokuaminiana kati ya wananchi na viongozi wao kunaweza kukwamisha juhudi za kujitawala, akionya kuwa matukio ya Oktoba 29 ya mwaka jana yanapaswa kuwa chachu ya kujenga taifa imara zaidi badala ya kurudia makosa yaliyopita. 

Kwa upande wake, Kiongozi wa Kanisa la Evangelical Fellowship Church Tanzania (EFCT), Askofu Charles Howard, ameeleza hamu yake ya kuiona Tanzania inayojenga misingi ya kusikilizana na kuridhiana hata pale kunapokuwa na tofauti za kifikra. Amesema misingi ya dini zote inahimiza amani na kuheshimiana, hivyo Watanzania hawana budi kutumia maadili hayo kuimarisha umoja wa kitaifa.

Naye Askofu Godfrey Songambele wa Kanisa la Tumaini la Mataifa Yote (HOFAN), amekumbusha kuwa amani ya kweli inapaswa kwenda sambamba na utekelezaji wa haki kwa wananchi, akisisitiza kuwa "amani ni wimbo, lakini haki ni matendo." 

Mtazamo huu wa hitaji la haki na maridhiano umeungwa mkono na Katibu Mkuu wa Chama cha National League for Democracy (NLD), Hassan Doyo, ambaye amesema mustakabali wa Tanzania unategemea wanasiasa wanaoweza kukaa pamoja na kujadili maendeleo, uchumi, na usalama wa nchi. Doyo ametoa mwito kwa wananchi kutokubali kushawishiwa kufanya vurugu na viongozi wa kisiasa, badala yake walinde tunu ya amani iliyopo.

Katika kutoa mwelekeo wa kisiasa, Kiongozi wa Chama cha ACT-Wazalendo, Dorothy Semu, amebainisha matarajio yake kuwa ripoti hiyo itasema ukweli mtupu kuhusu nini hasa kilisababisha uvunjifu wa amani uliotokea wakati wa mchakato wa uchaguzi. Maoni haya ya viongozi mbalimbali yanadhihirisha kiu ya Watanzania kuona taifa linasonga mbele kwa masikilizano na kurejea katika hali ya utulivu wa kudumu baada ya taarifa hiyo ya tume ya uchunguzi kuwekwa wazi kwa umma.

Share:

AMANI YATAJWA KAMA MTAJI WA MAENDELEO NA USTAWI WA JAMII



Katika kile kinachoonekana kama mwendelezo wa kusisitiza misingi ya Taifa, watanzania wamekumbushwa kuwa amani ndiyo nguzo kuu inayotoa uhuru wa kweli kwa mwananchi yoyote yule kuweza kufanya shughuli zake za kila siku kwani bila amani na utulivu hakuna uhuru wa Kijamii wala fursa za kiuchumi zinazoweza kuwepo kwenye jamii na Taifa kwa ujumla.

Akizungumza na mwandishi wetu wa habari leo Jumatano Aprili 22, 2026 Wilayani Ilala Jijini Dar Es Salaam, Bi. Lucy Mgecha, mjasiriamali katika soko la Ilala anasema kwamba amani si tu hali ya kutokuwa na vita bali pia ni mazingira yanayomfanya kila mwananchi kujihisi salama kukuza kipato chake na kushiriki katika ujenzi wa jamii na uchumi wake.

"Amani ni kuwa na uhuru wa kufanya lolote linalokubalika kisheria na kwenda popote unapotaka kwenda, uwe na uwezo huo wa kutoka sehemu moja kwenda nyingine na ninakumbuka kilichotokea Oktoba mwaka jana tulikosa uhuru kabisa wa kutembea kuanzia sisi watu wazima hadi watoto na hapa ndipo tuliposema amani sasa imevurugika na kwasasa tunamshukuru Mungu amani ipo na tunaendelea na biashara zetu." Amesema Bi. Lucy Mgecha.

Mgecha anaungana na wadau wengine wa maendeleo nchini ambao wanabainisha kuwa amani ni mtaji usioonekana, wakieleza kwamba katika maeneo yenye utulivu, wafanyabiashara, wakulima na wawekezaji hupata uhuru wa kupanga mipango ya muda mrefu na mfupi, uhuru pia ukichochea mzunguko wa fedha na kuongeza fursa za ajira na masoko.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO ALHAMISI APRILI 23,2026



Magazeti



Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger