Thursday, 28 May 2026

KUTOKA MSIKITI WA GADDAFI: WAUMINI WATAKIWA KUTII MAMLAKA NA KULINDA AMANI YA TAIFA




Shehe wa Mkoa wa Dodoma, Mustapha Rajabu Shaaban, amewataka waumini wa dini ya Kiislamu na jamii kwa ujumla kudumisha amani na mshikamano kwa kuwa wasikivu na wenye kutii mamlaka.

Akizungumza katika ibada ya Idd al-Adha kwenye Msikiti wa Gaddafi jijini Dodoma, Shehe Shaaban alisisitiza kuwa kukosekana kwa utiifu na usikivu ndiko kunakosababisha migogoro na umwagaji wa damu katika jamii.


Katika kuelezea umuhimu wa ibada ya kuchinja iliyohitimisha mwezi wa Dhulhijjah, kiongozi huyo alikumbusha kuwa ibada hiyo chimbuko lake ni historia ya Nabii Ibrahim na mwanawe Nabii Ismail.


Alieleza kuwa kisa hicho si hadithi tu ya kawaida, bali ni fundisho kubwa la jinsi Nabii Ibrahim alivyomshirikisha mwanawe kuhusu ndoto ya kumchinja, jambo linalofundisha umuhimu wa kuheshimiana, kusikilizana na kutii amri za Mwenyezi Mungu na mamlaka husika.

Mwisho, Shehe Shaaban aliwasihi wananchi kuendeleza utamaduni wa kuheshimiana ndani ya familia na kitaifa, huku akiwataka kuheshimu viongozi, taasisi, na vyombo mbalimbali vya kijamii na kidini.

Alitolea mfano kamati na tume zinazoundwa ndani ya Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA), akisisitiza kuwa kuheshimu mifumo hiyo ndiko kunakojenga ustawi wa jamii.
Share:

WENYE MAHITAJI MAALUM KUPEWA KIPAUMBELE MAFUNZO YA JKT



Na Dotto Kwilasa, Dodoma 

Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) limesema vijana wenye mahitaji maalum, hususan wenye ulemavu wa viungo, wamewekewa mazingira rafiki yatakayowawezesha kushiriki kikamilifu mafunzo ya uzalendo na stadi za maisha yanayoanza rasmi Juni mwaka huu.

Hatua hiyo imekuja sambamba na maandalizi ya kupokea jumla ya vijana 60,000 wa kidato cha sita kutoka shule mbalimbali Tanzania Bara na Zanzibar watakaoripoti katika makambi ya JKT kuanzia Juni 1 hadi Juni 7, 2026.

Akizungumza jijini Dodoma leo Mei 28, 2026 kwa niaba ya Mkuu wa JKT, Meja Jenerali Rajabu Mabele, Mkuu wa Utawala wa JKT, Brigedia Jenerali Hassan Mabena amesema vijana wenye mahitaji maalum watapangiwa katika Kambi ya Ruvu mkoani Pwani kutokana na uwepo wa miundombinu na huduma zinazokidhi mahitaji yao.

Amesema Serikali imeendelea kuboresha mfumo wa mafunzo hayo kwa kuongeza idadi ya vijana wanaopokelewa kutoka 40,000 hadi 60,000 mwaka huu ikiwa ni sehemu ya kuimarisha uzalendo, nidhamu na uwezo wa kujitegemea kwa vijana.

“Lengo ni kuwajenga vijana kuwa na maadili mema, uzalendo na stadi zitakazowasaidia katika maisha yao ya baadaye na katika kulitumikia taifa,” amesema Mabena.

Kwa mujibu wa Mabena, vijana hao watapangiwa katika makambi mbalimbali nchini ikiwemo Rwamkoma Mara, Msange Tabora, Mpwapwa na Makutupora Dodoma, Mafinga Iringa pamoja na Oljoro Arusha.

Makambi mengine yaliyotajwa ni Bulombora Kagera, Kanembwa na Mtabila Kigoma, Itaka Songwe, Luwa na Milundikwa Rukwa pamoja na Nachingwea mkoani Lindi.

Aidha, JKT limewataka vijana wote waliochaguliwa kuzingatia maelekezo ya kuripoti kwa wakati pamoja na kubeba vifaa muhimu vitakavyotumika wakati wa mafunzo, ikiwemo mavazi ya michezo, shuka, soksi na nyaraka muhimu za masomo na utambulisho.

Amesema mafunzo hayo hayalengi kuwapa vijana maarifa ya kijeshi pekee, bali pia kuwaandaa kuwa raia wenye nidhamu, uwezo wa kufanya kazi na kujitegemea hata kwa wale watakaokosa nafasi za kuendelea na elimu ya juu.

Programu ya mafunzo ya lazima ya JKT ilirejeshwa rasmi mwaka 2013 ikiwa na dhamira ya kuwajengea vijana moyo wa uzalendo na kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo ya taifa.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO ALHAMISI MEI 28, 2026

Magazeti Leo


















Share:

Wednesday, 27 May 2026

JUMUIYA ZA KIRAIA 126 ZIMESAJILIWA NCHINI 2025/26- WAZIRI KATAMBI



Na mwandishi wetu,Dodoma

Katika kipindi cha Julai 2025 hadi Aprili 2026, Jumla ya Jumuiya za Kiraia 126 zimesajiliwa Nchini, 12 kati yake zikiwa ni Jumuiya za kidini na 114 zisizo sa kidini.

Takwimu hizo zimebainishwa leo Jumatatu Mei 25, 2026 Bungeni Mjini Dodoma na Waziri wa mambo ya ndani ya Nchi Mhe. Patrobas Katambi wakati akisoma hotuba ya bajeti ya Wizara hiyo kwa mwaka 2026/27, akibainisha kwamba ukaguzi wa jumuiya 350 ulifanyika na Wizara yake katika kipindi kama hicho cha Julai 2025 hadi Aprili, 2026, lengo likiwa ni kufuatilia utekelezaji wa masharti ya usajili pamoja na kubaini mchango wa Jumuiya hizo katika maendeleo.

"Mhe. Spika, pia Wizara imeanzisha programu za ushirikishwaji ili kuimarisha uelewa na uwajibikaji wa viongozi wa jumuiya za kiraia katika uendeshaji wa jumuiya zao. Kupitia programu hiyo, jumla ya viongozi wa jumuiya za kidini na zisizo za kidini 2,500 walipatiwa mafunzo kuhusu uendeshaji wa jumuiya unaozingatia sheria na kuimarisha amani, utulivu na mshikamano wa kitaifa. 

Katika mwaka 2026/27, Wizara imetenga Shilingi bilioni 1.57 kwa ajili ya shughuli za usimamizi na uratibu wa Jumuiya za Kiraia nchini." Amesema Waziri Katambi.
Share:

Tuesday, 26 May 2026

WAZIRI SANGU AZINDUA BODI YA SABA YA USHAURI YA OSHA.


-Asisitiza Utekelezaji wa Viwango vya Kimataifa vya Usalama na Afya katika Maeneo ya Kazi

Na, OWM-KAM

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mheshimiwa Deus Sangu, amezindua Bodi ya Saba ya Ushauri ya Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA), iliyoanzishwa kwa mujibu wa Sheria ya Wakala za Serikali, Sura ya 245 Toleo la mwaka 2023 chini ya Kifungu cha 6 cha sheria hiyo.

Amezungumza hayo tarehe 25 Mei, 2026 wakati wa uzinduzi huo, Waziri Sangu amesema bodi hiyo ina jukumu la kutoa ushauri wa kitaalamu kwa OSHA ili kuimarisha utendaji wa taasisi hiyo na kuhakikisha mikakati inaendelea kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi, kwa kuzingatia dira, dhima na malengo ya Serikali.

Amesema kuwa miongoni mwa majukumu ya bodi hiyo ni kushauri kuhusu uandaaji na utekelezaji wa mpango mkakati wa OSHA, kufanya tathmini ya utendaji wa taasisi kupitia taarifa za mwaka na hesabu za wakala, pamoja na kutoa ushauri kuhusu maslahi na stahili za watumishi kwa lengo la kuongeza motisha, uwajibikaji na tija mahali pa kazi.

Katika hatua nyingine, Waziri Sangu ameielekeza bodi hiyo kusimamia utekelezaji wa mikataba ya kimataifa ya Shirika la Kazi Duniani (ILO) Na. 155 na 187 ili kuhakikisha viwango vya kimataifa vya usalama na afya mahali pa kazi vinaendelea kuzingatiwa nchini.

Aidha, ameitaka bodi hiyo kuimarisha mifumo ya utoaji huduma kwa njia ya kidijitali, ikiwemo mfumo wa Workplace Information Management System (WIMS), kwa lengo la kuongeza uwazi, ufanisi na kurahisisha utoaji wa huduma kwa wananchi na wadau mbalimbali.

"Majukumu haya yatekelezwe kwa kuzingatia sera, sheria, kanuni, taratibu na miongozo inayotolewa na Serikali pamoja na misingi ya uwajibikaji, uadilifu, ubunifu, ushirikiano kazini na uwazi" amesema Waziri Sangu.

Sambamba na hilo, amesema bodi hiyo inaanza majukumu yake katika kipindi muhimu ambapo Serikali inaendelea na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 pamoja na Mpango wa Nne wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano, huku uzinduzi wa Mpango Mkakati wa OSHA ukiwa chachu ya utekelezaji wa majukumu ya bodi hiyo.

Waziri Sangu pia ameisisitiza bodi hiyo kutekeleza wajibu wake kwa kuzingatia sera, sheria na miongozo iliyowekwa, huku akiitaka kutoa nafasi kwa menejimenti ya OSHA kusimamia shughuli za kila siku bila kuingiliwa. Amesema jukumu kuu la bodi ni kutoa ushauri na usimamizi wa kimkakati ili kuhakikisha kila upande unatekeleza wajibu wake ipasavyo.

Akizungumza Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri OSHA, Makwaia Makani, ameishukuru Serikali kwa imani iliyowaonesha na kuahidi kuwa bodi hiyo itatekeleza maelekezo yote yaliyotolewa kwa kuzingatia sheria, kanuni na miongozo iliyowekwa.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo, Bi. Zuhura Yunus, amewapongeza wajumbe wa bodi kwa kuaminiwa na kuteuliwa, akiwataka kutumia weledi na umahiri wao katika kuisimamia OSHA kwa manufaa ya taasisi na taifa kwa ujumla.

Naye Mtendaji Mkuu wa OSHA, Bi. Khadija Mwenda, amesema bodi zimekuwa na mchango mkubwa katika maendeleo ya taasisi hiyo na kwamba menejimenti ya OSHA ipo tayari kushirikiana na bodi mpya ili kuendelea kuimarisha utendaji na utoaji wa huduma.
Share:

MTWARA YAFUNGUA FURSA MPYA KATIKA SEKTA YA CHUMVIMTWARA YAFUNGUA FURSA MPYA KATIKA SEKTA YA CHUMVI

- Serikali yapunguza gharama za leseni ya Madini Chumvi, wachimbaji wanufaika

📍Mtwara

Mkoa wa Mtwara umeendelea kujidhihirisha kuwa kitovu muhimu cha uwekezaji katika sekta ya chumvi kutokana na uwepo wa fukwe zinazofaa kwa uzalishaji, maboresho ya mazingira ya biashara na ongezeko la uzalishaji linalofikia takribani tani 90 kwa majaruba manne katika baadhi ya maeneo ya uzalishaji.

Kutokana na hatua hiyo, wachimbaji na wazalishaji wa chumvi wameanza kunufaika na fursa mpya za kiuchumi kupitia kuongezeka kwa uzalishaji, ajira na upanuzi wa maeneo ya uzalishaji.

Akizungumza katika mahojiano maalum, Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Mtwara, Winnifrida Mrema, amesema sekta ya chumvi mkoani humo inaendelea kukua kwa kasi kutokana na kuimarika kwa shughuli za uzalishaji pamoja na matumizi ya teknolojia za kisasa katika uchakataji wa chumvi.

Amesema maboresho hayo yanalenga kuongeza ubora wa chumvi kwa matumizi ya majumbani, viwandani na mifugo, huku yakichochea ajira kwa wananchi wa maeneo yanayozunguka mashamba ya chumvi.

“Mtwara ina mazingira rafiki kwa uzalishaji wa chumvi na Serikali inaendelea kuhamasisha uwekezaji katika sekta hii ili kuongeza mapato kwa wananchi na taifa kwa ujumla,” amesema Mrema.

Katika Kijiji cha Mnete, Kata ya Nalingu Halmashauri ya Mtwara Vijijini, msimamizi wa mashamba ya chumvi, Salum Amani, amesema mashamba hayo yanamilikiwa na Zamda Khatibu na yana leseni mbili za uvunaji chumvi pamoja na majaruba 24 yanayotumika kwa uzalishaji.

Amesema kwa sasa wanaendelea na shughuli za usafishaji wa majaruba baada ya msimu wa mvua ili kuruhusu maji ya chumvi kuingia tayari kwa uzalishaji mpya.

Kwa mujibu wa Salum, uzalishaji wa chumvi hutegemea hali ya hewa, ambapo jua kali huwezesha chumvi kukauka ndani ya siku 30, huku hali ya baridi ikifanya mchakato huo kuchukua hadi siku 40.

“Kwa kawaida majaruba manne huzalisha takribani tani 90 za chumvi kwa msimu mmoja, huku shughuli hizi zikitoa ajira kwa wafanyakazi tisa katika eneo hili,” amesema.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama cha Wazalishaji Chumvi Mkoa wa Mtwara na  Mwenyekiti wa Kamati ya Chumvi kupitia  FEMATA, Khalfan Nassoro, amesema kupunguzwa kwa gharama ya ada ya pango ya leseni za chumvi  kutoka Shilingi 45,000 hadi Shilingi 20,000 kumeongeza uwezo wa wazalishaji kupanua maeneo ya uzalishaji.

Amesema hatua hiyo imeongeza matumaini kwa wawekezaji na wachimbaji wadogo, huku akisisitiza kuwa mazingira bora ya uwekezaji yataifanya Mtwara kuwa kitovu kikuu cha uzalishaji wa chumvi nchini.

Nassoro amesema pia ukuaji wa sekta hiyo unaweza kuchochea ujenzi wa viwanda vya kuongeza thamani ya chumvi na hivyo kuongeza mchango wa sekta hiyo katika uchumi wa taifa.






Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMANNE MEI 26,2026


Magazeti





Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger