Friday, 14 August 2026

ORYX GAS ZANZIBAR YANOGESHA TAMASHA LA KIZIMKAZI,YAKABIDHI MITUNGI YA GESI 200


Na Mwandishi Wetu ,Zanzibar

ORYX Gas Zanzibar imeeleza hatua mbalimbali inazochukua kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia na katika Tamasha la Kizimkazi kampuni hiyo imetoa mitungi ya gesi 200 huku mkakati kwasasa ni kutoa majenerata yanatotumia gesi ya LPG katika hoteli na viwanda visiwani Zanzibar.

Imesema Zanzibar imepiga hatua kubwa katika matumizi ya LPG na kwamba katika kipindi cha miaka sita matumizi ya nishati safi ilikuwa asilimia sita mwaka 2020 lakini mwaka 2025 ni zaidi ya asilimia 30 ya watumiaji wa nishati safi ya kupikia ya gesi na muamko huo umechangiwa na sekta binafsi,Serikali na wadau wengine.

Akizungumza katika kongamano la nishati safi lililofanyika wakati wa Tamasha la Kizimkazi Zanzibar lililoanza Agosti 12 na kuhitimiswa leo Agosti 14,2026, Meneja Mkuu wa Oryx Gas Zanzibar Shuwekha Khamis amesema kampuni hiyo Oryx wanamchango mkubwa katika matumizi ya nishati safi ya kupikia.

“Hii kazi tumeianza muda mrefu na tumekuwa tukizisaidia taasisi katika mabadiliko na hapa Zanzibar oryx tumeshapiga hatua kuzibadilisha baadhi ya taasisi zikiwemo shule shule 25,Jeshi la Kujenga Uchumi, JKU kuna kambi sita Unguja na Pemba

“Pia kwa kushirikiana na Mwanamke Initiative Foundation tumebadilisha gereza la Kiinua Mguu , vituo vya polisi viwili, vituo vya afya 12 pamoja na baadhi ya ofisi za Serikali na ofisi nyingine.Kwahiyo tunaona kuna hatua kubwa ambayo tumeifanya katika kuzibadilisha taasisi.”

Awali katika tamasha hilo la Kizimkazi Oryx Gas imetoa mitungi ya gesi ya kupikia 250 bure kwa wananchi lengo likiwa kuendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia hasa kwa kutambua mkakati wa Serikali ni kuhakikisha ifikapo mwaka 2034 asilimia 80 ya Watanzania wawe wanatumia nishati safi ya kupikia.
Share:

WATUMISHI WA WIZARA WATEMBELEA OFISI ZA UBALOZI WA TANZANIA NCHINI INDIA


Watumishi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wanaohudhuria mafunzo maalum ya diplomasia nchini India wametembelea Ofisi za Ubalozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania jijini New Delhi.

Katika ziara hiyo, watumishi hao walikutana na wafanyakazi wa Ubalozi na kupata fursa ya kuzungumza na Balozi wa Tanzania nchini India, Mheshimiwa Anisa Mbega, pamoja na watumishi wengine wa Ubalozi.

Akizungumza wakati wa kuwakaribisha watumishi hao Ubalozini, Mheshimiwa Balozi Anisa Mbega alisema Ubalozi umefurahi kuwapokea watumishi wenzao kutoka Wizara na kuwapongeza kwa kupata fursa ya kushiriki mafunzo hayo maalum ya diplomasia.

Balozi Mbega alisema ana imani kuwa mafunzo waliyoyapata yamewaongezea maarifa na hivyo yatachangia kuboresha utendaji wao wa kazi na hivyo kuleta tija na ufanisi kwa Wizara.

Aliishukuru Serikali ya India kwa kuitikia ombi la Wizara la kuwajengea watumishi uwezo ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa tija na ufanisi na kuongeza kuwa Ubalozi utaendelea kushirikiana na Serikali ya India ili kuimarisha uhusiano kati ya Tanzania na India

Watumishi hao wa Wizara walikuwa nchini India kwa mafunzo maalum ya muda mfupi yaliyofadhiliwa na Serikali ya India na kutolewa na Chuo cha Sushma Swaraj (Sushma Swaraj Institute of Foreign Service - SSIFS), yakilenga kuwajengea uwezo watumishi wa Wizara katika maeneo ya diplomasia ya kisasa, masuala ya kimataifa na kikanda, historia, mabadiliko ya kidigitali,utamaduni na sera ya mambo ya nje ya India.
Share:

ALAT YAJIFUNZA KILIMO CHA PARACHICHI NJOMBE



Na Mwandishi Wetu, NJOMBE


KAMATI Tendaji ya Jumuiya ya Tawala za Serikali za Mitaa Tanzania (ALAT) Taifa imehitimisha kikao kazi chake kwa kufanya ziara ya mafunzo katika shamba la Mkulima Bora wa Zao la Parachichi kitaifa, Abishae Hairun Mwalongo, lililopo Kijiji cha Igosi, Wilaya ya Wanging’ombe, mkoani Njombe.

Ziara hiyo, iliyoongozwa na Mwenyekiti wa ALAT Taifa, Mhe. Agnetha Mpangile, imelenga kuwawezesha wajumbe wa kamati hiyo kujifunza kwa vitendo kuhusu kilimo cha parachichi na namna wakulima wanavyoweza kuongeza uzalishaji na ubora wa mazao.

Mwalongo, ambaye ni mmiliki wa MWIDIS Green Garden, aliwaeleza wajumbe hao hatua mbalimbali za kilimo cha parachichi, kuanzia uchaguzi wa mbegu bora, maandalizi ya shamba, upandaji hadi namna ya kulitunza shamba katika vipindi tofauti vya mwaka.

Alisema matumizi ya mbegu bora pamoja na maandalizi sahihi ya shamba ni miongoni mwa mambo muhimu yanayomwezesha mkulima kupata mavuno yenye tija na mazao yenye ubora unaokidhi mahitaji ya soko.

Katika ziara hiyo, Mwalongo pia alitoa maelekezo kuhusu aina mbalimbali za mbegu bora za parachichi na namna ya kuzitumia kulingana na mazingira ya eneo husika.

Alisema wakulima wanapaswa kuzingatia utaalamu katika kila hatua ya uzalishaji ili kuongeza tija na kuhakikisha zao hilo linakuwa na ushindani katika masoko ya ndani na nje ya nchi.

Akizungumza baada ya ziara hiyo, Mwalongo aliwashukuru viongozi wa ALAT Taifa kwa kutenga muda na kufika katika shamba lake kwa lengo la kujifunza na kuona kwa vitendo namna kilimo cha parachichi kinavyofanyika.

Alisema ziara hiyo ni muhimu kwa kuwa inatoa fursa kwa viongozi kujionea shughuli za kilimo na kupata uelewa wa changamoto na fursa zinazowakabili wakulima.

Kwa upande wake, ziara hiyo imekuwa sehemu ya shughuli za Kamati Tendaji ya ALAT Taifa mkoani Njombe, ikiwa ni hatua ya kuunganisha masuala ya utawala wa Serikali za Mitaa na shughuli za kiuchumi zinazofanywa na wananchi katika maeneo yao.

Njombe ni miongoni mwa mikoa inayofanya vizuri katika uzalishaji wa parachichi nchini, hivyo ziara hiyo imeongeza fursa ya kubadilishana uzoefu kuhusu namna ya kuimarisha kilimo na kuongeza tija kwa wakulima.





Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO IJUMAA AGOSTI 14,2026


Magazeti







Share:

Wednesday, 12 August 2026

KATIBU WA BARAZA LA VYAMA VYA SIASA: MARIDHIANO NA MAZUNGUMZO NDIYO NJIA SAHIHI YA KATIBA MPYA


Mwenyekiti wa Baraza la Vyama vya Siasa, Juma Ali Khatib, amesema kuwa Rais Samia Suluhu Hassan ameendelea kuonesha dhamira ya dhati katika mchakato wa kupatikana kwa katiba mpya kupitia maridhiano, mazungumzo, na ushirikishwaji mpana wa wadau mbalimbali wa kitaifa.

Kauli hiyo imetolewa kufuatia mkutano uliozikutanisha jumla ya vyama vya siasa 19 vilivyohudhuria Ikulu jijini Dar es Salaam, huku Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kikikosekana baada ya kususia mazungumzo hayo.


Khatib amesisitiza kuwa mchakato wa kupata katiba mpya hauwezi kufikiwa kwa misimamo mikali au kugomea mikutano ya mashauriano, bali unahitaji nia njema na utayari wa kusikiliza mawazo ya wengine kupitia utekelezaji wa falsafa ya 4R inayosisitiza umoja, mshikamano, na ustahimilivu.


Amemuunga mkono Rais Samia kufuatia mipango ya kuunda tume maalumu ya kuchunguza na kutatua masuala ya vurugu za kisiasa zilizopita kwa kuzingatia mapendekezo ya Tume ya Jaji Chande, sambamba na kuimarisha misingi ya Serikali ya Umoja wa Kitaifa kupitia makubaliano ya hivi karibuni kati ya CCM na ACT Wazalendo huko Zanzibar. Vilevile, serikali imeweka mikakati thabiti kupitia sera za ajira, ujasiriamali, na sekta ya kilimo ili kuwaondoa vijana katika hatari ya kutumiwa kwenye migogoro ya kisiasa na kuwashirikisha kikamilifu katika ujenzi wa uchumi wa taifa.


Viongozi wengine mbalimbali wakiwemo Katibu wa Chama cha Demokrasia Makini, Ameir Hassan Ameir, mgombea wa zamani wa urais wa Zanzibar kupitia NCCR-Mageuzi, Lela Rajab Khamis, na Makamu Mwenyekiti wa UWT, Zainab Shomari, wamempongeza Rais Samia kwa uongozi wake unaojumuisha makundi yote katika ujenzi wa taifa na kuimarisha misingi ya demokrasia na maridhiano nchini
Share:

SERIKALI YAWEKA MKAKATI WA HIFADHI YA BIONUAI

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni akiwasilisha taarifa kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira kuhusu mkakati na mpango kazi wa Taifa wa hifadhi ya bioanuai, taarifa hiyo ameiwasilisha Bungeni Agosti 11, 2026.

***************

NA; MWANDISHI WETU, DODOMA

Serikali, kwa kushirikiana na wadau mbalimbali, imeendelea kuimarisha uwezo wa kitaalamu na utafiti katika masuala yanayohusu bioanuai, pamoja na kujenga na kuimarisha mfumo thabiti wa kisheria na utawala ili kuwezesha uhifadhi na matumizi ya rasilimali za bioanuaii nchini kwa manufaa ya sasa na ya kizazi kijacho.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni ameyasema hayo wakati akiwasilisha taarifa kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira kuhusu mkakati na mpango kazi wa Taifa wa hifadhi ya bioanuai, taarifa aliyoiwasilisha Bungeni Agosti 11, 2026.

Amesema, wadau mbalimbali zikiwemo Wizara za Kisekta, Taasisi za serikali na zisizo za serikali, makampuni binafsi, wadau wa Maendeleo na makundi ya Kijamii, huhitajika kuutekeleza mkakati huu.

“Mkakati huu hutekelezwa kwa kuhuisha masuala ya bioanuai kwenye mipango ya kisekta, ikiwemo Kuandaa programu maalumu ya hifadhi ya bioanuai kwa sekta husika, pamoja na kuandaa na kutekeleza miradi mbalimbali inayohusu hifadhi ya bioanuai.”

Utekelezaji wa Mkakati huu unachangia utekelezaji wa mikakati mingine ya Mazingira ikiwemo; Mpango Kabambe wa Taifa wa Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (2022-2032), Sera naMkakati wa Uchumi wa Buluu (2024).

“Matokeo ya utekelezaji wa Mkakati huu utachangia katika kuimiarisha hali ya uhifadhi wa mazingira nchini kufikia asilimia 25 na kufanya jumla ya asilimia 65 ya uhifadhi nchini ifikapo mwaka 2030.

“Kiasi hicho kitachangia nguzo ya tatu ya Dira 2050 katika eneo la hifadhi ya bioanuai ambapo tunatarajia kwamba ifikapo mwaka 2050 Tanzania itakuwa miongoni mwa nchi kumi (10) bora Afrika katika kuhifadhi mazingira.”

Mkakati wa Taifa wa bioanuai (2025-2030) umeshirikisha wadau mbalimbali katika mchakato wa uaandaji wake. Wadau hao ni pamoja na Wizara za kisekta; Taasisi za serikali na zisizo za serikali; na Makundi ya jamii.

Mkakati na Mpango kazi wa Kitaifa wa Bioanuwai (2025 2030) ni mwongozo wa kitaifa unaotoa mwelekeo na umeainisha mikakati ya inayopaswa kutekeleza ili kuwezesha uhifadhi na  matumizi ya rasilimali za bioanuaii nchini kwa manufaa ya sasa na ya kizazi kijacho.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Jackson Kiswaga amesema kwa kutambua kuwa suala la mazingira ni mtambuka, Ofisi ya Makamu wa Rais iendelee kushirikiana na wadau mbalimbali ili kuhakikisha programu ya elimu kwa umma kuhusu mazingira inawafikia wadau wengi zaidi.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. MhandisiHamad Yussuf Masauni akiwasilisha taarifa kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira kuhusu mkakati na mpango kazi wa Taifa wa hifadhi ya bioanuai, taarifahiyo ameiwasilisha Bungeni Agosti 11, 2026.

PICHA NA OFISI YA MAKAMU WA RAIS
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger