Wednesday, 19 August 2026

ELIMU YA MABADILIKO YA KODI YAWAFIKIA WAFANYABIASHARA SHINYANGA KUPITIA TRA

Meneja Msaidizi Huduma kwa Mlipa Kodi Mkoa wa Shinyanga Ramadhan Sengo



Na Stella Herman,Shinyanga

Wafanyabiashara Mkoa wa Shinyanga wametakiwa kuongeza uelewa kuhusu mabadiliko ya sheria za kodi ili waweze kutekeleza ipasavyo wajibu wao wa kikodi na kuepuka makosa yanayoweza kusababisha migogoro au adhabu.
Wito huo umetolewa wakati wa mafunzo yaliyotolewa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Shinyanga kwa wafanyabiashara kutoka maeneo mbalimbali ya mkoa huo, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa marekebisho ya sheria za kodi yaliyoanza kutumika Juni 30, 2026.

Mafunzo hayo yamelenga kuwawezesha wafanyabiashara kufahamu mabadiliko yaliyofanyika, kupata ufafanuzi kutoka kwa wataalamu wa kodi pamoja na kujenga uelewa wa pamoja kuhusu wajibu wa walipa kodi na namna ya kushirikiana na TRA katika kuongeza ufanisi wa ukusanyaji wa mapato ya Serikali.

Akizungumza wakati wa mafunzo hayo yaliyofanyika leo Agost 19, 2026, Meneja Msaidizi Huduma kwa Mlipa Kodi Mkoa wa Shinyanga Ramadhan Sengo, amesema TRA imeamua kuwashirikisha wafanyabiashara moja kwa moja ili kuwapa nafasi ya kuelewa mabadiliko hayo na kupata majibu ya maswali yanayohusu shughuli zao.

Sengo amesema ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi ni muhimu katika kuhakikisha mfumo wa ulipaji na ukusanyaji wa kodi unakuwa na ufanisi.

“Kwa pamoja, mafunzo haya ni muhimu katika kuongeza jitihada za wafanyabiashara na taasisi kwa pamoja ili kusaidia Taifa letu kuwa na uwezo wa kukusanya kodi kwa ajili ya maendeleo. Tumieni fursa hii kuuliza maswali yatakayotupa uelewa na kutusaidia kujua mambo mbalimbali kupitia wataalamu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania,” amesema Sengo.


Katika mafunzo hayo, Afisa Mkuu Msimamizi wa Kodi kutoka TRA Mkoa wa Dar es Salaam, Abdalah Seif, alitoa ufafanuzi kuhusu maeneo mbalimbali yaliyofanyiwa marekebisho katika sheria za kodi.

Kwa upande wake, Makamu Mwenyekiti wa Chemba ya Taifa ya Biashara Tanzania (TNCC) Mkoa wa Shinyanga, Hatibu Mgeja, amesema sekta binafsi ni sehemu muhimu katika kukuza uchumi na hivyo Serikali na wafanyabiashara wanapaswa kuendelea kushirikiana.

Mgeja alisema Serikali ya Awamu ya Sita imeendelea kutoa elimu kuhusu mabadiliko ya mfumo wa kodi, hatua ambayo amesema itasaidia wafanyabiashara kutekeleza wajibu wao kwa uelewa zaidi.

“Tunashukuru Serikali ya Awamu ya Sita kwa kuendelea kuleta mabadiliko chanya katika mfumo wa kodi kwa wafanyabiashara, hatua ambayo inalenga kusaidia ukusanyaji wa fedha kwa ajili ya maendeleo ya Taifa,” amesema Mgeja.

Wafanyabiashara walitumia pia fursa hiyo kuiomba TRA kuendelea kushirikiana na taasisi nyingine zinazohusiana na shughuli zao, ikiwemo TANROADS, Wakala wa Misitu Tanzania (TFS), TARURA na Halmashauri, katika kutoa elimu ya pamoja kuhusu kodi na majukumu mbalimbali yanayowahusu.

Wamesema ushirikishwaji wa taasisi hizo utasaidia kupunguza mkanganyiko unaoweza kujitokeza wakati wafanyabiashara wanapotekeleza majukumu yao ya kikodi na majukumu mengine yanayohusiana na uendeshaji wa biashara.

Mkurugenzi wa Lyakale Civil Engineering, Christopher Ringo, ameomba TRA Mkoa wa Shinyanga kuendelea kutoa elimu ya kodi kwa watumishi wa TANROADS na TARURA, akisema hatua hiyo itasaidia kuongeza uelewa na kupunguza changamoto zinazoweza kujitokeza katika utekelezaji wa majukumu ya kikodi kwa wakandarasi, hususan kutokana na kuchelewa kwa malipo.

Mabadiliko ya sheria za kodi yaliyofafanuliwa katika mafunzo hayo yanahusu maeneo mbalimbali, yakiwemo uuzaji wa mali, mazao ya misitu, ushuru wa uagizaji wa bidhaa kutoka nje ya nchi, uendeshaji wa kampuni za madini, viwango vya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT), wajibu wa waajiri kuzingatia Namba ya Utambulisho wa Mlipa Kodi (TIN), mirahaba ya malipo kwa timu za mpira wa miguu, biashara zinazofanyika kupitia mitandao, kodi kwa vyombo vya usafiri wa abiria, wajibu wa kulipa kodi pamoja na kodi zinazohusiana na michezo ya bahati nasibu.

Meneja Msaidizi Huduma kwa Mlipa Kodi Mkoa wa Shinyanga Ramadhan Sengo



Share:

MAAFISA BIASHARA WAFUNZWA NAMNA YA KUDHIBITI BIDHAA BANDIA




Na Mwandishi Wetu

Tume ya Ushindani (FCC) imetoa elimu kwa Maafisa Biashara kwa lengo la kuwaongezea uelewa kuhusu masuala ya ushindani katika biashara, udhibiti wa bidhaa bandia pamoja na umuhimu wa kumlinda mlaji dhidi ya bidhaa na huduma zisizokidhi viwango.

Semina hiyo imelenga kuwajengea uwezo Maafisa Biashara ambao wana nafasi muhimu katika kusimamia shughuli za biashara katika maeneo yao, ili waweze kutambua changamoto zinazohusiana na ushindani usio wa haki, bidhaa bandia na vitendo vinavyoweza kuwaathiri walaji.

Akitoa mada kuhusu udhibiti wa bidhaa bandia, wakati wa Mkutano wa Maafisa Biashara nchini katika Kikao cha Tatu cha Wizara ya Viwanda na Biashara na Maafisa Biashara, kilichofanyika kwa siku mbili jijini Dodoma.

Kaimu Mkurugenzi wa Udhibiti wa Bidhaa Bandia wa FCC, Bw. Salvatory Chuwa, ameeleza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya FCC na Maafisa Biashara katika kukabiliana na biashara ya bidhaa bandia.

"Bidhaa bandia zina madhara makubwa kwa uchumi, wafanyabiashara wanaofuata sheria na walaji, hivyo ni muhimu kwa Maafisa Biashara kuwa na uelewa wa kutosha kuhusu namna ya kubaini na kutoa taarifa kuhusu bidhaa zinazodhaniwa kuwa bandia."amesema Bw.Chuwa

Amesisitiza kuwa udhibiti wa bidhaa bandia unahitaji ushirikiano wa karibu kati ya taasisi za Serikali, wafanyabiashara na wananchi, huku akiwataka Maafisa Biashara kutumia nafasi zao kuelimisha wafanyabiashara na walaji kuhusu madhara ya bidhaa bandia.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Tafiti, Miungano ya Makampuni na Uraghibishi wa FCC, Bi. Zaytun Kikula, ametoa mada kuhusu masuala ya ushindani, akieleza umuhimu wa kuwepo kwa mazingira ya biashara yenye ushindani wa haki kwa ajili ya kukuza uchumi na kuwapa wafanyabiashara fursa sawa katika soko.

Bi.Kikula amebainisha kuwa ushindani wenye tija husaidia kuongeza ubunifu, kuboresha ubora wa bidhaa na huduma pamoja na kuwapa walaji fursa ya kupata bidhaa bora kwa bei shindani.

Aidha, amewataka Maafisa Biashara kushirikiana na FCC katika kutoa elimu kwa wafanyabiashara kuhusu sheria za ushindani na kuhakikisha kuwa vitendo vinavyoweza kuzuia au kupotosha ushindani vinatambuliwa na kuchukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria.

Semina hiyo ni sehemu ya jitihada za FCC za kuimarisha uelewa wa wadau kuhusu wajibu wa kulinda ushindani katika soko, kudhibiti bidhaa bandia na kuhakikisha haki za walaji zinalindwa.

FCC imeendelea kusisitiza kuwa ushirikiano wa wadau mbalimbali, hususan Maafisa Biashara, ni muhimu katika kujenga soko lenye ushindani wa haki, bidhaa salama na mazingira bora ya biashara kwa manufaa ya wafanyabiashara, walaji na uchumi kwa ujumla.


Share:

TANZANITE ROYAL GIN YAZIDI KUPAMBA MANYARA TANZANITE MARATHON 2026





Na Mwandishi Wetu, Manyara


Manyara Tanzanite Marathon 2026 inatarajiwa kuwa na burudani ya aina yake baada ya wasanii maarufu nchini, Dully Sykes, Banana Zoro na Mr Blue, kuthibitisha kushiriki na kutumbuiza katika tukio hilo litakalofanyika Agosti 22, 2026 mjini Babati, mkoani Manyara.


Ushiriki wa wasanii hao umewezeshwa na kampuni ya Mati Super Brands Ltd kupitia kinywaji chake cha Tanzanite Royal Gin, hatua inayoongeza ushiriki wa sekta binafsi katika kufanikisha mbio hizo zinazolenga kuunganisha michezo, burudani na shughuli za kijamii.



Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Queen Sendiga, amekabidhi wasanii hao T-shirt rasmi za Manyara Tanzanite Marathon, ikiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea tukio hilo ambalo limeendelea kupata mwitikio kutoka kwa wadau mbalimbali.


Manyara Tanzanite Marathon 2026 imebeba kaulimbiu “Hatua Moja Okoa Maisha”, ikiwa na lengo la kukusanya Shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa wodi maalumu ya kuwahudumia watoto njiti wanaozaliwa kabla ya wakati.



Ujio wa Dully Sykes, Banana Zoro na Mr Blue unatarajiwa kuongeza hamasa kwa wanariadha, vikundi vya jogging na wananchi watakaoshiriki au kujitokeza kushuhudia mbio hizo. Burudani hiyo pia inalenga kuwapa washiriki na watazamaji uzoefu wa kipekee huku ikihamasisha jamii kuunga mkono kampeni ya kuokoa maisha ya watoto njiti..



Mchango wa Mati Super Brands Ltd kupitia Tanzanite Royal Gin unaendelea kuonesha nafasi ya sekta binafsi katika kusaidia shughuli zenye manufaa kwa jamii. Ushiriki huo unatarajiwa kuongeza mvuto wa marathon na kuwafikia watu wengi zaidi kupitia michezo na burudani.


Kwa ujumla, Manyara Tanzanite Marathon 2026 inatarajiwa kuwa jukwaa linalounganisha michezo, burudani, utalii na uwajibikaji kwa jamii, huku kila hatua ya washiriki ikilenga kuchangia upatikanaji wa huduma bora kwa watoto njiti mkoani Manyara.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMATANO AGOSTI 19,2026


Magazeti



Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger