Thursday, 20 August 2026

KONGAMANO LA UCHUMI WA BLUU KUFUNGUA FURSA ZA KUKUZA KIPATO NA UCHUMI PROF- GURUMO



Na Sheila Ahmadi, Dar es Salaam

Kongamano la Tano la Uchumi wa Bluu linatarajiwa kuwakutanisha wadau kutoka ndani na nje ya Tanzania kujadili namna ya kutumia fursa za uchumi wa bluu kuongeza kipato cha wananchi na kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa.

Akizungumza Jijini Dar e s salaam na wanahabari kuhusu kongamano hilo, Mkuu wa Chuo cha Bahari Dar es Salaam (DMI) Profesa Tumaini Gurumo amesema kuwa uchumi wa bluu ni miongoni mwa sekta zinazolenga kuchangia katika kukuza uchumi wa Tanzania, hivyo ni muhimu kwa wadau kukutana na kujadili namna bora ya kutumia rasilimali zilizopo katika sekta hiyo.

lengo la kongamano hilo ni kuwaunganisha wadau mbalimbali ili kubadilishana uzoefu, kujadili changamoto na kutafuta suluhisho litakalowezesha uchumi wa bluu kuwa na tija zaidi kwa wananchi na taifa kwa ujumla.

“Lengo hasa la kongamano hili ni kuwakutanisha wadau wa uchumi wa bluu waweze kutafakari namna gani tunaweza kuwezesha uchumi wa bluu, ili tutoke katika kiwango tulichopo sasa na kufikia hatua ambayo inaweza kuongeza kipato cha mtu mmoja mmoja, lakini pia kukuza uchumi wa taifa,” amesema.

Amesema kongamano hilo pia litatoa fursa kwa watafiti kuwasilisha tafiti mbalimbali walizofanya, huku washiriki wakijadili matokeo ya tafiti hizo na kutoa maoni yatakayosaidia kuboresha shughuli zinazohusiana na uchumi wa buluu

pamoja na kukuza uchumi wa taifa, ni muhimu kuhakikisha wananchi wanapata elimu na uelewa wa kutosha kuhusu fursa zinazopatikana katika uchumi wa bluu ili waweze kuzitumia kuboresha maisha yao.

“Tunataka kuwapa Watanzania uelewa wa shughuli za uchumi wa bluu na namna wanavyoweza kufanya vizuri zaidi katika shughuli ambazo tayari wamekuwa wakizifanya kwa miaka mingi. Tukipata Watanzania wenye uelewa, elimu na ujuzi, ndipo tutakapoweza kupata ubunifu na maendeleo ya sayansi na teknolojia,” amesema Profesa Gurumo.

Chuo cha Bahari Dar es Salaam, ni taasisi ambayo imejikita katika kutoa elimu na mafunzo yanayohusiana na masuala ya bahari, kufanya tafiti na kutoa ushauri kwa Serikali pamoja na taasisi binafsi.

Katika hatua nyingine chuo hicho kinaendelea kutoa elimu kwa jamii kuhusu uchumi wa bluu ili kuongeza uelewa wa fursa zilizopo, kuimarisha mifumo na sera, pamoja na kuwahamasisha wawekezaji kutumia fursa hizo.

Hivyo kongamano hilo litawakutanisha washiriki kutoka taasisi za serikali na binafsi, watafiti, wanataaluma, wawekezaji na wadau wa maendeleo kutoka Tanzania na mataifa mbalimbali.

Sanjari na hayo Baadhi ya nchi za Afrika ambazo zimethibitisha kushiriki ni pamoja na Comoro, Kenya, Uganda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, huku nchi nyingine nje ya Afrika zikiwemo China, Sweden na Canada pia zikitarajiwa kushiriki.

Kupitia washiriki hao watapata fursa ya kujadili tafiti na kuonesha ubunifu mbalimbali unaohusiana na matumizi ya rasilimali za bahari na maendeleo ya uchumi wa bluu.

Aidha baada ya kukamilika kwa kongamano hilo, wanatarajia kupata maarifa mapya yatakayowanufaisha Watanzania na washiriki wengine, pamoja na mapendekezo ya kisera yatakayosaidia kuboresha mazingira ya kufanya shughuli za uchumi wa bluu.

“Tunatarajia kupata mapendekezo ya kisera. Zipo sera ambazo zinatumika, lakini kutokana na mabadiliko yanayotokea, kuna umuhimu wa kuangalia kama zinahitaji marekebisho au kama kuna maeneo yanahitaji sera mpya,” amesema Profesa Gurumo.




Share:

HII NDIO TOFAUTI KATI YA WAONGOZAJI WA NDEGE NA WAEGESHAJI WA NDEGE



Katika sekta ya usafiri wa anga, kuna wataalamu mbalimbali wanaoshiriki kuhakikisha ndege zinafanya safari kwa usalama na ufanisi. Miongoni mwa wataalamu ambao mara nyingi huchanganywa ni Waongozaji wa Ndege, wanaojulikana kama Air Traffic Controllers, na Waegeshaji wa Ndege, wanaojulikana kitaalamu kama Aircraft Marshallers.

Waegeshaji wa ndege ni wataalamu wanaofanya kazi katika maeneo ya maegesho ya ndege viwanjani. Mara nyingi huonekana wakiwa wamevaa mavazi maalum ya usalama na kutumia vijiti vya mwanga au ishara za mikono kumwelekeza rubani wakati ndege inapokaribia sehemu ya maegesho au inapojiandaa kuondoka.

Jukumu lao ni kuhakikisha ndege inaelekezwa kwa usahihi katika eneo lililotengwa bila kuhatarisha usalama wa ndege, vifaa vya uwanja, majengo au watu waliopo katika mazingira ya karibu. Ishara wanazotumia hutambulika kimataifa na humsaidia rubani kufanya maamuzi sahihi hasa katika maeneo ambayo mwonekano kutoka ndani ya ndege unaweza kuwa na mipaka.

Historia ya kazi ya uegeshaji wa ndege inaanzia katika miaka ya mwanzo ya maendeleo ya usafiri wa anga, ambapo mawasiliano kati ya marubani na wahudumu wa ardhini yalitegemea zaidi ishara za mikono. Pamoja na maendeleo ya teknolojia katika viwanja vya ndege, kazi ya Aircraft Marshaller bado inaendelea kuwa sehemu muhimu ya shughuli salama za ndege ardhini.

Kwa upande mwingine, Waongozaji wa Ndege, au Air Traffic Controllers, wana jukumu la kusimamia na kuratibu mwendo wa ndege angani na katika maeneo maalum ya viwanja vya ndege. Hutumia mifumo ya mawasiliano, ufuatiliaji na taratibu za uongozaji wa ndege kuhakikisha ndege zinatenganishwa kwa umbali salama na kupewa maelekezo wakati wa kuruka, kutua na kujiendesha katika maeneo wanayoyasimamia.

Tofauti kubwa kati ya wataalamu hawa ni kwamba Air Traffic Controllers huongoza na kuratibu mwendo wa ndege kupitia mawasiliano ya redio na mifumo ya uongozaji, wakati Aircraft Marshallers humwelekeza rubani kwa ishara za kuona katika eneo la maegesho ya ndege.

Pamoja na tofauti hiyo ya majukumu, wataalamu hawa wote ni sehemu muhimu ya mfumo wa usalama wa usafiri wa anga na huchangia kuhakikisha shughuli za ndege zinafanyika kwa mpangilio, usalama na ufanisi.


Nchini Tanzania, Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) ina jukumu la kusimamia na kudhibiti usalama wa usafiri wa anga kwa kuzingatia sheria, kanuni na viwango vinavyotambuliwa kitaifa na kimataifa, ikiwemo miongozo ya Shirika la Kimataifa la Usafiri wa Anga, ICAO.

 

Share:

RUWASA KWA KUSHIRIKIANA NA WADAU WAJA NA MKAKATI WA KUSHUGHULIKIA SUALA LA USAFI WA MAZINGIRA VIJIJINI


Morogoro

Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA), kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa Sekta ya Maji, Afya na Usafi wa Mazingira, umeanza rasmi mchakato wa kuandaa Mkakati wa RUWASA wa Menejimenti ya Tope Kinyesi (Faecal Sludge Management Strategy), unaolenga kuweka mfumo madhubuti, salama na endelevu wa menejimenti ya tope kinyesi katika maeneo ya vijijini.

Akifungua Kikao Kazi cha National Task Force kinachofanyika mjini Morogoro, Mkurugenzi Mkuu wa RUWASA, Eng. Wolta S. Kirita, amesema maandalizi ya Mkakati huo ni hatua muhimu katika kuimarisha huduma za usafi wa mazingira vijijini na kupunguza athari za kiafya na kimazingira zinazoweza kusababishwa na menejimenti isiyo salama ya tope kinyesi.

Eng. Kirita amesisitiza umuhimu wa ushirikiano wa wadau katika kuhakikisha Mkakati utakaoandaliwa unazingatia mazingira halisi ya vijijini, unaweka bayana majukumu ya wadau mbalimbali na, muhimu zaidi, unatekelezeka na kuwa endelevu.

“Pamoja na jukumu letu kubwa la kuhakikisha wananchi wa vijijini wanapata huduma endelevu za maji, RUWASA pia ina wajibu katika masuala ya usafi wa mazingira. Tupo tayari kushirikiana na wadau wote kuhakikisha tunakuwa na mfumo bora na endelevu wa menejimenti ya tope kinyesi katika maeneo ya vijijini,” amesema Eng. Kirita.

Awali, akimkaribisha Mkurugenzi Mkuu, Mkurugenzi wa Usambazaji Maji na Usafi wa Mazingira, Eng. Mariam Majala, amesema menejimenti salama ya tope kinyesi bado ni changamoto inayohitaji juhudi za pamoja za kitaalamu na kitaasisi.

Eng. Majala amesema maandalizi ya Mkakati huo yatawezesha kuweka mwelekeo wa pamoja kuhusu namna bora ya kukusanya, kusafirisha, kutibu na kutupa au kutumia tena tope kinyesi kwa njia salama, sambamba na kuweka mpango na mwongozo wa utekelezaji unaozingatia mazingira na mahitaji ya maeneo ya vijijini.

Kikao Kazi hicho cha siku nne kinawaleta pamoja wajumbe wa National Task Force kutoka RUWASA, Wizara na Taasisi za Serikali, Vyuo Vikuu, Wadau wa Maendeleo pamoja na wataalamu wenye uzoefu katika Sekta ya Maji na Usafi wa Mazingira.

Miongoni mwa taasisi zinazoshiriki katika Kikao Kazi hicho ni Wizara ya Maji, Wizara ya Afya, Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Chuo Kikuu Ardhi, EWURA, SNV na WaterAid, pamoja na wadau wengine wa Sekta ya Maji na Usafi wa Mazingira.

Kikao hicho ni sehemu ya hatua za awali za maandalizi ya Mkakati na kinatarajiwa kujenga uelewa wa pamoja kuhusu msingi wa kisera na kisheria, hali ya sasa ya menejimenti ya tope kinyesi vijijini, majukumu ya wadau, mbinu za maandalizi ya Mkakati pamoja na mpango wa utekelezaji wa kazi ya National Task Force.

Kupitia mchakato huo, RUWASA inalenga kuhakikisha kuwa Mkakati utakaoandaliwa unatoa mwelekeo wa kitaifa na mfumo unaotekelezeka wa menejimenti salama na endelevu ya tope kinyesi katika maeneo ya vijijini, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuboresha huduma za maji na usafi wa mazingira na kulinda afya ya jamii na mazingira.

Share:

NEMC YAKUTANA NA WAANDAAJI WA TANZANIA GREEN SUMMIT 2026


Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limekutana na ujumbe wa waandaaji wa Tanzania Green Summit (TGS), inayotarajiwa kufanyika Septemba 15–16, 2026 Ukumbi wa Mlimani City, Jijini Dar es Salaam, kwa lengo la kuimarisha ushirikiano na kujadili mikakati ya kuhakikisha unaleta tija katika ajenda ya mazingira na mabadiliko ya tabianchi.

Akizungumza katika kikao hicho, Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt. Immaculate Sware Semesi, amesema ushirikiano kati ya NEMC na TGS ni muhimu katika kuongeza uelewa, ubunifu na ushiriki wa wadau, hususan vijana, katika kutafuta suluhisho la changamoto za mazingira na mabadiliko ya tabianchi.

"NEMC, kama mlezi wa Tanzania Green Summit, ataendelea kuunga mkono majukwaa yanayochochea uendelevu wa mazingira, hatua za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi pamoja na ushiriki wa vijana katika ajenda ya mazingira na maendeleo endelevu" amesisitiza Dkt.Sware Semesi

Ushirikiano kati ya NEMC na TGS unaendana na Mpango Mkakati wa NEMC pamoja na malengo ya Dira ya Tanzania ya 2050, hususan katika kujenga uchumi endelevu, thabiti, wa kibunifu na jumuishi unaozingatia fursa zinazotokana na hatua za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Tanzania Green Summit 2026 yenye kaulimbiu “Kugeuza Hatua za Tabianchi Kuwa Fursa” inatarajiwa kuwakutanisha washiriki takribani 1,000 kutoka sekta mbalimbali kujadili na kuibua fursa za ubunifu, uwekezaji, ajira, ushirikiano na maendeleo endelevu zinazotokana na juhudi za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi
Share:

JAB YAWAWEZESHA WAANDISHI CROWN MEDIA KUZINGATIA SHERIA NA MAADILI








Na Mwandishi Wetu.

Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imewataka Waandishi wa Habari wa Crown Media kulinda imani ya umma kwa kuzingatia weledi, maadili, uadilifu na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao.

Wito huo umetolewa wakati wa mafunzo ya siku mbili yaliyotolewa na JAB kwa Waandishi wa Habari wa Crown Media, kuanzia Agosti 18 hadi 19, 2026, jijini Dar es Salaam yakilenga kuwaongezea maarifa na kuwajengea uwezo wa kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia sheria, maadili na viwango vya taaluma ya uandishi wa habari.

Akiwasilisha Mada kuhusu Msingi na Mfumo wa Kisheria unaosimamia Sekta ya Habari nchini Tanzania katika mafunzo hayo, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, amewasihi Waandishi wa Habari kuthamini na kulinda taaluma yao kwa kuzingatia misingi inayowaongoza katika utekelezaji wa majukumu yao.




“Waandishi wa Habari tunapaswa kuthamini na kulinda taaluma yetu wenyewe. Weledi, maadili na uadilifu ndiyo msingi wa kuaminika kwa mwandishi na sekta ya habari kwa ujumla,” amesema Wakili Kipangula.

Kwa upande wake, Dkt. Egbert Mkoko amewataka Waandishi wa Habari kuzingatia maadili katika kila hatua ya kazi zao, akieleza kuwa maadili ndiyo msingi wa uandishi wa habari unaowajibika na wenye tija kwa jamii.

“Mwandishi wa Habari anapaswa kuzingatia maadili ya kazi katika kila hatua ya utekelezaji wa majukumu yake, kwa kuwa uadilifu na uwajibikaji ndiyo msingi wa taaluma hii,” amesema Dkt. Mkoko alipokuwa akifafanua mada Kuhusu Maadili ya Utangazaji na makosa ya kimaadili yanayofanywa mara kwa mara.

Naye Mjumbe wa JAB na Kaimu Meneja wa Huduma za Kiswahili wa Shirika la Magazeti ya Serikali (TSN), Bw. Mgaya Kingoba, akiwasilisha mada kuhusu uzalendo, amewataka Waandishi wa Habari kutumia taarifa kwa usahihi na kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia maslahi ya umma.








Wakizungumza wakati wa tathmini ya mafunzo hayo, baadhi ya Waandishi wa Habari wa Crown Media wamesema wamepata uelewa mpana kuhusu Sheria ya Huduma za Habari, hali iliyowasaidia kuondokana na fikra potofu zilizotokana na tafsiri zisizo sahihi zinazotolewa katika jamii kuhusu Sheria hiyo. Pia wameomba mafunzo kama hayo kutolewa mara kwa mara ili kuwajengea uwezo Waandishi wa Habari.



“Kwa kweli, changamoto tuliyonayo katika vyombo vyetu vya habari ni kushindwa kutofautisha maoni binafsi na uchambuzi wa kitaaluma, pamoja na kushindwa kutenganisha nafasi ya mtu binafsi na wajibu wake kama mwanataaluma. 

Pia kumekuwa na dhana kwamba Bodi ipo kwa ajili ya kuwadhibiti Waandishi wa Habari, pamoja na uelewa mdogo kuhusu ithibati, umuhimu wake na nafasi yake katika kulinda heshima ya taaluma,” amesema Imani Luvanga mmoja wa washiriki.

Mafunzo hayo ni sehemu ya utekelezaji wa majukumu ya JAB kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, yanayolenga kuimarisha weledi, uadilifu, uwajibikaji na tija katika taaluma ya uandishi wa habari.
Share:

Wednesday, 19 August 2026

ELIMU YA MABADILIKO YA KODI YAWAFIKIA WAFANYABIASHARA SHINYANGA KUPITIA TRA

Meneja Msaidizi Huduma kwa Mlipa Kodi Mkoa wa Shinyanga Ramadhan Sengo



Na Stella Herman,Shinyanga

Wafanyabiashara Mkoa wa Shinyanga wametakiwa kuongeza uelewa kuhusu mabadiliko ya sheria za kodi ili waweze kutekeleza ipasavyo wajibu wao wa kikodi na kuepuka makosa yanayoweza kusababisha migogoro au adhabu.
Wito huo umetolewa wakati wa mafunzo yaliyotolewa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Shinyanga kwa wafanyabiashara kutoka maeneo mbalimbali ya mkoa huo, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa marekebisho ya sheria za kodi yaliyoanza kutumika Juni 30, 2026.

Mafunzo hayo yamelenga kuwawezesha wafanyabiashara kufahamu mabadiliko yaliyofanyika, kupata ufafanuzi kutoka kwa wataalamu wa kodi pamoja na kujenga uelewa wa pamoja kuhusu wajibu wa walipa kodi na namna ya kushirikiana na TRA katika kuongeza ufanisi wa ukusanyaji wa mapato ya Serikali.

Akizungumza wakati wa mafunzo hayo yaliyofanyika leo Agost 19, 2026, Meneja Msaidizi Huduma kwa Mlipa Kodi Mkoa wa Shinyanga Ramadhan Sengo, amesema TRA imeamua kuwashirikisha wafanyabiashara moja kwa moja ili kuwapa nafasi ya kuelewa mabadiliko hayo na kupata majibu ya maswali yanayohusu shughuli zao.

Sengo amesema ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi ni muhimu katika kuhakikisha mfumo wa ulipaji na ukusanyaji wa kodi unakuwa na ufanisi.

“Kwa pamoja, mafunzo haya ni muhimu katika kuongeza jitihada za wafanyabiashara na taasisi kwa pamoja ili kusaidia Taifa letu kuwa na uwezo wa kukusanya kodi kwa ajili ya maendeleo. Tumieni fursa hii kuuliza maswali yatakayotupa uelewa na kutusaidia kujua mambo mbalimbali kupitia wataalamu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania,” amesema Sengo.


Katika mafunzo hayo, Afisa Mkuu Msimamizi wa Kodi kutoka TRA Mkoa wa Dar es Salaam, Abdalah Seif, alitoa ufafanuzi kuhusu maeneo mbalimbali yaliyofanyiwa marekebisho katika sheria za kodi.

Kwa upande wake, Makamu Mwenyekiti wa Chemba ya Taifa ya Biashara Tanzania (TNCC) Mkoa wa Shinyanga, Hatibu Mgeja, amesema sekta binafsi ni sehemu muhimu katika kukuza uchumi na hivyo Serikali na wafanyabiashara wanapaswa kuendelea kushirikiana.

Mgeja alisema Serikali ya Awamu ya Sita imeendelea kutoa elimu kuhusu mabadiliko ya mfumo wa kodi, hatua ambayo amesema itasaidia wafanyabiashara kutekeleza wajibu wao kwa uelewa zaidi.

“Tunashukuru Serikali ya Awamu ya Sita kwa kuendelea kuleta mabadiliko chanya katika mfumo wa kodi kwa wafanyabiashara, hatua ambayo inalenga kusaidia ukusanyaji wa fedha kwa ajili ya maendeleo ya Taifa,” amesema Mgeja.

Wafanyabiashara walitumia pia fursa hiyo kuiomba TRA kuendelea kushirikiana na taasisi nyingine zinazohusiana na shughuli zao, ikiwemo TANROADS, Wakala wa Misitu Tanzania (TFS), TARURA na Halmashauri, katika kutoa elimu ya pamoja kuhusu kodi na majukumu mbalimbali yanayowahusu.

Wamesema ushirikishwaji wa taasisi hizo utasaidia kupunguza mkanganyiko unaoweza kujitokeza wakati wafanyabiashara wanapotekeleza majukumu yao ya kikodi na majukumu mengine yanayohusiana na uendeshaji wa biashara.

Mkurugenzi wa Lyakale Civil Engineering, Christopher Ringo, ameomba TRA Mkoa wa Shinyanga kuendelea kutoa elimu ya kodi kwa watumishi wa TANROADS na TARURA, akisema hatua hiyo itasaidia kuongeza uelewa na kupunguza changamoto zinazoweza kujitokeza katika utekelezaji wa majukumu ya kikodi kwa wakandarasi, hususan kutokana na kuchelewa kwa malipo.

Mabadiliko ya sheria za kodi yaliyofafanuliwa katika mafunzo hayo yanahusu maeneo mbalimbali, yakiwemo uuzaji wa mali, mazao ya misitu, ushuru wa uagizaji wa bidhaa kutoka nje ya nchi, uendeshaji wa kampuni za madini, viwango vya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT), wajibu wa waajiri kuzingatia Namba ya Utambulisho wa Mlipa Kodi (TIN), mirahaba ya malipo kwa timu za mpira wa miguu, biashara zinazofanyika kupitia mitandao, kodi kwa vyombo vya usafiri wa abiria, wajibu wa kulipa kodi pamoja na kodi zinazohusiana na michezo ya bahati nasibu.

Meneja Msaidizi Huduma kwa Mlipa Kodi Mkoa wa Shinyanga Ramadhan Sengo



Share:

MAAFISA BIASHARA WAFUNZWA NAMNA YA KUDHIBITI BIDHAA BANDIA




Na Mwandishi Wetu

Tume ya Ushindani (FCC) imetoa elimu kwa Maafisa Biashara kwa lengo la kuwaongezea uelewa kuhusu masuala ya ushindani katika biashara, udhibiti wa bidhaa bandia pamoja na umuhimu wa kumlinda mlaji dhidi ya bidhaa na huduma zisizokidhi viwango.

Semina hiyo imelenga kuwajengea uwezo Maafisa Biashara ambao wana nafasi muhimu katika kusimamia shughuli za biashara katika maeneo yao, ili waweze kutambua changamoto zinazohusiana na ushindani usio wa haki, bidhaa bandia na vitendo vinavyoweza kuwaathiri walaji.

Akitoa mada kuhusu udhibiti wa bidhaa bandia, wakati wa Mkutano wa Maafisa Biashara nchini katika Kikao cha Tatu cha Wizara ya Viwanda na Biashara na Maafisa Biashara, kilichofanyika kwa siku mbili jijini Dodoma.

Kaimu Mkurugenzi wa Udhibiti wa Bidhaa Bandia wa FCC, Bw. Salvatory Chuwa, ameeleza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya FCC na Maafisa Biashara katika kukabiliana na biashara ya bidhaa bandia.

"Bidhaa bandia zina madhara makubwa kwa uchumi, wafanyabiashara wanaofuata sheria na walaji, hivyo ni muhimu kwa Maafisa Biashara kuwa na uelewa wa kutosha kuhusu namna ya kubaini na kutoa taarifa kuhusu bidhaa zinazodhaniwa kuwa bandia."amesema Bw.Chuwa

Amesisitiza kuwa udhibiti wa bidhaa bandia unahitaji ushirikiano wa karibu kati ya taasisi za Serikali, wafanyabiashara na wananchi, huku akiwataka Maafisa Biashara kutumia nafasi zao kuelimisha wafanyabiashara na walaji kuhusu madhara ya bidhaa bandia.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Tafiti, Miungano ya Makampuni na Uraghibishi wa FCC, Bi. Zaytun Kikula, ametoa mada kuhusu masuala ya ushindani, akieleza umuhimu wa kuwepo kwa mazingira ya biashara yenye ushindani wa haki kwa ajili ya kukuza uchumi na kuwapa wafanyabiashara fursa sawa katika soko.

Bi.Kikula amebainisha kuwa ushindani wenye tija husaidia kuongeza ubunifu, kuboresha ubora wa bidhaa na huduma pamoja na kuwapa walaji fursa ya kupata bidhaa bora kwa bei shindani.

Aidha, amewataka Maafisa Biashara kushirikiana na FCC katika kutoa elimu kwa wafanyabiashara kuhusu sheria za ushindani na kuhakikisha kuwa vitendo vinavyoweza kuzuia au kupotosha ushindani vinatambuliwa na kuchukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria.

Semina hiyo ni sehemu ya jitihada za FCC za kuimarisha uelewa wa wadau kuhusu wajibu wa kulinda ushindani katika soko, kudhibiti bidhaa bandia na kuhakikisha haki za walaji zinalindwa.

FCC imeendelea kusisitiza kuwa ushirikiano wa wadau mbalimbali, hususan Maafisa Biashara, ni muhimu katika kujenga soko lenye ushindani wa haki, bidhaa salama na mazingira bora ya biashara kwa manufaa ya wafanyabiashara, walaji na uchumi kwa ujumla.


Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger