Sunday, 25 January 2026

RAIS SAMIA AMEIMARISHA UCHUMI GEITA KUPITIA UJENZI WA BARABARA YA KASAMWA-GAMASHI - PROF. SHEMDOE

Na OWM - TAMISEMI, Geita

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu -TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amemshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuidhinisha Shilingi 1,035,047,200/= za ujenzi wa dharura wa barabara ya Kasamwa- Gamashi yenye urefu wa kilomita 18, iliyoimarisha shughuli za kiuchumi kupitia Sekta ya Usafiri na Usafirishaji kati ya Wilaya ya Nyang’hwale na Makao Makuu ya Mkoa wa Geita.

Prof. Shemdoe amesema barabara hiyo ina umuhimu kiuchumi kwa wananchi wa Nyang’hwale na Geita ambao wanategemea shughuli za kilimo na  ufugaji, hivyo uzalishaji unaofanyika Nyang’hwale ulikuwa hauwezi kufika makao makuu ya mkoa kutokana na changamoto iliyokuwepo ya ubovu wa miundombinu ya barabara ya  Kasamwa- Gamashi.

“Ujenzi wa barabara hii ni muhimu sana kiuchumi, hivyo tunapaswa kumshukuru Mhe. Rais kwa kuidhinisha fedha zilizowezesha barabara kujengwa ili kuendeleza shughuli za wananchi kiuchumi,” amesisitiza Prof. Shemdoe.

Sanjari na hilo, Prof. Shemdoe amempongeza Mshauri Elekezi kampuni ya Norplan Tanzania Ltd kwa usimamizi mzuri wa mradi huo  akiwa ni mwakilishi wa mshitiri, na kuongeza kuwa Washauri Elekezi wote wangetekeleza wajibu wao kama alivyotekeleza Norplan Tanzania Limited, kusingekuwa na malalamiko wala changamoto ya miradi kusuasua.

Aidha, Prof. Shemdoe amempongeza Mkandarasi wa mradi huo kampuni ya Madata Investment Ltd kwa utekelezaji mzuri wa mradi huo uliofikia asilimia 82 kwa kutumia fedha yake mwenyewe, na kuanisha kwamba wakandarasi wa aina ya Madata Investment wakipatikana kutakuwa hakuna miradi mingi inayosuasua.  

“Nakupongeza sana mkandarasi kwa kazi nzuri uliyoifanya katika mradi huu, na ninakuhakikishia kuwa fedha ya kukulipa ipo, wewe lete maombi ulipwe lakini nakuomba uzingatie Februari 27, 2026 unapaswa kukabidhi mradi huu,” ameeleza Prof. Shemdoe.

Akitoa taarifa ya utekelezaji wa mradi huo, Meneja wa TARURA Wilaya ya Geita, Mhandisi Bahati Subeya amesema mradi huo wa ujenzi wa dharura katika barabara ya Kasamwa- Gamashi ulianza rasmi Agosti 25, 2025 na unatarajiwa kukamilika Februari 27, 2026.

Mhandisi Subeya amefafanua kuwa, kukamilika kwa mradi huo kutaboresha sekta ya usafiri na usafirishaji pamoja na shughuli za kiuchumi, ikiwa ni pamoja na kurahisisha upatikanaji wa huduma za kijamii zikiwemo za afya na elimu.

Naye, Mkuu wa Wilaya ya Nyang’hwale Mhe. Grace Kingalame amemshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwezesha ujenzi wa barabara ya Kasamwa- Gamashi ambayo itaondoa changamoto ya mawasiliano kati ya wilaya yake na makao makuu ya mkoa, na kuongeza kuwa wananchi wa Nyang’wale na Geita wanafurahishwa na dhamira ya dhati ya Mheshimiwa Rais ya kuwaletea maendeleo kupitia ujenzi wa miundombinu ya barabara.

Mradi huo wa Barabara ya Kasamwa- Gamashi, ni miongoni mwa miradi tisa (9) yenye thamani ya Shilingi 4,015,469,549/= inayotekelezwa na TARURA mkoa wa Geita kupitia Mradi wa CERC (Contingency Emergency Response Component) - DMDP II unaofadhiliwa na Benki ya Dunia, ambao unatokana na barabara  zilizoathiriwa na mvua za Elnino mwaka 2023.

Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMAPILI JANUARI 25,2026

Magazeti



 
Share:

Saturday, 24 January 2026

MV NEW MWANZA: MKOMBOZI WA UCHUMI NA BIASHARA KANDA YA ZIWA

Kukamilika na kuzinduliwa kwa meli ya kisasa ya MV New Mwanza, kumeleta matumaini mapya ya kiuchumi kwa mamilioni ya wakazi wa mikoa ya Kanda ya Ziwa, ambao kwa muda mrefu walikuwa wakikabiliwa na changamoto kubwa ya usafirishaji wa bidhaa na abiria kati ya majiji ya Mwanza na Bukoba.

Meli hiyo, ambayo sasa ndiyo mfalme wa maji katika Ukanda wa Maziwa Makuu, si chombo cha usafiri tu, bali ni kiunganishi kikuu cha biashara kati ya mikoa ya Kanda ya Ziwa na nchi jirani za Uganda na Kenya.

Uwezo wa Kipekee

Kwa mara ya kwanza baada ya kipindi kirefu cha "ukame" wa vyombo vikubwa, MV New Mwanza inakuja na uwezo mkubwa wa kubeba abiria na mizigo. Ikiwa na uwezo wa kubeba abiria 1,200 inapunguza msongamano na gharama kubwa za usafiri wa barabara.

Kwenye suala la mizigo ambapo ndipo penye moyo wa biashara, meli hii ina uwezo wa kubeba tani 400 za bidhaa kwa wakati mmoja, jambo ambalo litaleta mapinduzi ya bei za bidhaa sokoni. Aidha ina uwezo wa kubeba magari madogo 20 na makubwa (malori) 3 .

Manufaa ya Kiuchumi

Kukosekana kwa meli ya uhakika kwa miaka mingi kuliathiri vibaya mabadilishano ya bidhaa. Sasa, kwa safari ya saa 6 hadi 7 pekee wakulima wa kahawa, ndizi, na mazao mengine ya chakula kutoka mkoani Kagera sasa wanakuwa na soko la uhakika jijini Mwanza na mikoa mingine. Bidhaa hizi zitafika zikiwa bado mbichi na kwa gharama nafuu ya usafirishaji.Wakati huo huo wafanyabiashara wa Mwanza sasa wanaweza kusafirisha bidhaa za viwandani, vifaa vya ujenzi, na samaki kwenda Bukoba na maeneo ya pembezoni mwa ziwa kwa urahisi zaidi.

Ongezeko la uwezo wa kubeba mizigo mikubwa kutaondoa gharama za ziada za usafirishaji zinazosababishwa na malori, hivyo kupelekea bei za bidhaa kupungua kwa mlaji wa mwisho.

Usalama na Utimamu wa Biashara 

Mkurugenzi Mtendaji wa TASHICO, Eric Hamisi, amebainisha kuwa meli hiyo imetengenezwa kwa teknolojia ya kisasa inayohakikisha usalama wa watu na mali zao. Uwepo wa madaraja mbalimbali, ikiwemo daraja la biashara na VIP, unatoa fursa kwa wafanyabiashara kufanya safari zao kwa faraja huku wakiratibu mipango yao ya kibiashara.

Kwa wakazi wa kandoni mwa Ziwa Victoria, MV New Mwanza si tu fahari ya kitaifa, bali ni injini ya kukuza kipato, kutoa ajira, na kufungua fursa za kitalii ambazo zilikuwa zimefifia. Huu ni mwanzo wa zama mpya ambapo biashara itashamiri na uchumi wa kaya utaimarika kupitia maji ya ziwa hilo kuu.

Share:

BILIONI 67 ZIMETUMIKA KUJENGA BARABARA NA MASOKO MWANZA - PROF. SHEMDOE



Na OWM – TAMISEMI, Mwanza

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amesema Serikali kupitia Mradi wa Uendelezaji Miundombinu ya Miji Tanzania (TACTIC) imetumia kiasi cha bilioni 67 kujenga Barabara na Masoko ili kuwahudumia wananchi wa Mwanza.

Prof. Shemdoe ametoa taarifa hiyo leo jijini Mwanza wakati alipopewa nafasi na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba ya kuzungumza na wananchi wa mwanza waliojitokeza kumsikiliza Waziri Mkuu mara baada ya Waziri Mkuu kuhitimisha ziara yake ya kikazi ya kukagua miradi ya maendeleo na kuzindua meri ya New MV Mwanza.

Prof. Shemdoe amefafanua kuwa, fedha hizo zinatumika kujenga barabara ya Nyamaghani yenye urefu wa kilomita 14 yenye thamani ya bilioni 22, barabara ya Ilemela yenye urefu wa kilomita 12 yenye thamani ya bilioni 24, Soko la Samaki Mkuyuni Nyamaghana lenye thamani ya bilioni 7 pamoja na soko la mazao mchanganyiko Ilemela lenye thamani ya bilioni 14.

Akizungumzia hatua ya ujenzi wa barabara hizo, Prof. Shemdoe amesema zimekamilika na ziko kwenye hatua ya kuweka taa za barabarani ili wananchi waweze kuzitumia nyakati za usiku huku wakiwa salama. 

“Mhe. Waziri Mkuu ikikupendeza pindi barabara zikikamilika, tutakuomba uje kuzizindua rasmi kwa ajili ya kuanza kutumiwa na wananchi wa Mwanza na watanzania wote watakao kuja jijini Mwanza kwa shughuli mbalimbali,” Prof. Shemdoe amewasilisha ombi.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu -TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amemhakikishia Waziri Mkuu Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba kuwa, ofisi yake itaisimamia vema TARURA ili miradi yote ya Barabara, Soko la Samaki na Soko la Mazao mchanganyiko ikaamilike kwa wakati, na hatimaye wanachi waanze kunufaika na uwepo wa miradi hiyo.




Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMAMOSI JANUARI 24, 2026




magazetini








Share:

Friday, 23 January 2026

TUTACHUKUA HATUA KALI KWA WATAKAOTUMIA TAARIFA BINAFSI ZA WATU KINYEMELA- PDPC



Tume ya taarifa ya ulinzi wa Taarifa binafsi Tanzania PDPC imetangaza kuanza mara moja kwa ukaguzi wa uzingatiaji wa sheria kwa Taasisi za umma na za binafsi, zinazokusanya na kuchakata taarifa binafsi.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Alhamisi Januari 22, 2026, Mkurugenzi Mkuu wa Tume hiyo Dkt. Emmanuel Mkilia amesema zoezi hilo linafanyika mara baada ya muda wa hiari kuisha kulingana na tangazo la Tume hiyo lililoweka ukomo wa Aprili 8, 2026 kwa Taasisi husika kukamilisha usajili wao.

"Ukaguzi huu utahusisha kubaini Taasisi za umma na za binafsi zinazokusanya, kuhifadhi kuchakata na kusafirisha taarifa binafsi nje ya nchi bila kuzingatia matakwa ya sheria ya ulinzi wa taarifa binafsi sura ya 44 na kanuni zake na PDPC tutachukua hatua kali za kisheria dhidi ya yeyote, taasisi ama kampuni itakayokiuka sheria hii ikiwa ni pamoja na faini, kifungo, fidia kwa waathirika ama vyote kwa pamoja." Amesema Dkt. Mkilia.

Aidha PDPC imesema mtu ama Taasisi itakayobainika kutumia taarifa ya mtu binafsi bila ridhaa yake au kinyume na taratibu zilizowekwa kisheria, Taasisi hiyo itawajibishwa Ipasavyo bila ya kujali hadhi ama ukubwa wa Taasisi itakayokiuka misingi ya sheria katika ulinzi wa taarifa binafsi.

Pamoja na mafanikio yanayotokana na ukuaji wa TEHAMA duniani, kumekuwepo na changamoto mbalimbali ikiwemo ulinzi wa taarifa binafsi ambazo zimekuwa zikikusanywa, zikichakatwa na wakati mwingine kusafirishwa kutoka nchi moja kwenda nyingine bila kuzingatia utaratibu na misingi ya ulinzi wa taarifa binafsi iliyokubalika kisheria.


Share:

Thursday, 22 January 2026

MASLAHI YA TAIFA KWANZA: MAPINDUZI YA KIFIKRA NA KIUCHUMI KATIKA KULINDA RASILIMALI

Katika ulimwengu wa sasa unaotawaliwa na ushindani mkali wa kidiplomasia na kiuchumi, Tanzania na mataifa mengine ya Afrika yanapita katika kipindi cha kihistoria kinachohitaji mabadiliko makubwa ya kifikra ili kulinda rasilimali na mustakabali wa vizazi vijavyo. 

Kupitia mjadala mzito uliofanyika hivi karibuni, wasomi na viongozi wabobezi nchini wakiongozwa na Profesa wa Uchumi, Samuel Wangwe, Kanali Mstaafu Joseph Simbakalia na mwanasiasa mkongwe Hamad Rashid Mohammed, wametoa msisitizo ambao unapaswa kuwa dira ya maendeleo ya taifa letu. 

Hoja kuu inayopaswa kueleweka kwa kila mwananchi ni kuwa maslahi ya kitaifa ni kitu kitakatifu ambacho hakipaswi kuchezewa au kuamuliwa kwa misingi ya itikadi za vyama vya siasa, ukabila wala dini, bali kwa kuangalia faida ya muda mrefu ya taifa zima.

Profesa Samuel Wangwe ameweka wazi kuwa taifa linalolenga maendeleo ya kweli ni lile ambalo wananchi wake wanaunganishwa na msimamo mmoja wa kizalendo, hususan katika usimamizi wa rasilimali. 

Ili kufikia hatua hii, kuna haja kubwa ya kuongeza thamani ya rasilimali zetu badala ya kuziuza kama malighafi pekee, jambo ambalo linawezekana tu kwa kuwekeza kwa vijana kupitia teknolojia. Profesa Wangwe anazitaja nchi za India, China na Malaysia kama mifano ya kuigwa kwani zimepiga hatua kwa kuwapeleka vijana wao kujifunza nje ya nchi na kurudi kukuza uchumi wa viwanda wa ndani. Hii ina maana kuwa ufunguo wa utajiri wa Tanzania haupo tu kwenye madini au ardhi, bali upo kwenye akili za vijana walioandaliwa kiteknolojia kuongoza mageuzi ya kiuchumi.

Ukombozi wa kifikra ni nguzo nyingine muhimu iliyosisitizwa na Kanali Mstaafu Joseph Simbakalia, ambaye amewataka Waafrika kuacha kutegemea mataifa ya Magharibi kuamua mustakabali wao. 

Simbakalia anafafanua kuwa kudhani kuwa mataifa ya nje yana mamlaka ya mwisho juu ya matumizi ya rasilimali zetu ni aina ya utumwa wa kifikra unaorudisha nyuma maendeleo. Ili Afrika iweze kujenga uchumi imara, viongozi wanapaswa kutanguliza uadilifu na kuwajibika kwa wananchi bila kuathiriwa na shinikizo za nje au migogoro ya kikanda inayochelewesha umoja. 

Hoja ya utambulisho na utamaduni imeguswa kwa uzito na Hamad Rashid Mohammed, ambaye anakumbusha kuwa ukoloni haukuishia tu kwenye utumwa wa kimwili bali uliingia kwenye mioyo ya Waafrika kwa kuwafanya wadharau tamaduni zao. Siasa za kimataifa kwa sasa zinatumia taasisi za kifedha kama mbinu mpya ya utawala, jambo ambalo linaweza kupingwa tu ikiwa tutaimarisha utamaduni wetu wa kupendana, kusikilizana na kudhibiti rasilimali zetu wenyewe. 

Mkakati wa kuelimishana juu ya umuhimu wa kujitambua kama Waafrika ndio utakaotuwezesha kusimamia maendeleo yetu bila kuyumbishwa na misaada yenye masharti magumu yanayominya uhuru wetu wa kiuchumi.

Ujumbe huu wa pamoja kutoka kwa wabobezi hawa unatoa funzo kubwa kwa vijana, wafanyakazi na wafanyabiashara nchini Tanzania kuwa maendeleo ya nchi ni jukumu la pamoja. Serikali ya Awamu ya Sita tayari imeanza kutekeleza misingi hii kwa kufungua fursa za kibiashara na mataifa makubwa kama Marekani huku ikisisitiza tija na ajira kwa wazawa. Ni wajibu wa kila mwananchi kuelewa kuwa tunapozungumzia uwekezaji katika madini ya kimkakati au mikopo ya halmashauri kwa vijana, tunazungumzia utekelezaji wa maslahi ya taifa kwa vitendo. Maamuzi yoyote tunayoyafanya leo katika ngazi ya familia, halmashauri au serikali kuu lazima yapimwe kwa mizani ya kama yanajenga au yanabomoa umoja na utajiri wetu wa pamoja kama taifa.

Share:

ILALA TUNAJIVUNIA RAIS SAMIA, AMETULETEA MAENDELEO- MAMBO


Na Jonas Jovin, Dar

Wananchi wa Wilaya ya Ilala Jijini Dar Es Salaam wameeleza kufurahishwa na kazi kubwa inayotekelezwa na Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan hasa katika Ujenzi wa mundombinu ya barabara za ndani, Vyumba vya madarasa katika shule za msingi na Sekondari pamoja na ujenzi wa miundombinu katika sekta ya afya na maji Wilayani humo.

Kwa kuitaja, wananchi hao wameeleza kuhusu ujenzi wa barabara za ndani kupitia miradi mbalimbali ikiwa ni pamoja na mradi wa DMDP, ikiwemo barabara ya Nyeburu- Miti mirefu pamoja na barabara ya Kigezi- Njianne kuelekea Majohe, wakisema awali ilikuwa ni ngumu kuona barabara za ndani zikijengwa kwa kiwango cha lami nchini.

Bw. Othman Hassan Mambo, Mkazi wa Nyeburu, ameitaja miradi ya ujenzi wa madarasa katika shule za msingi na sekondari ikiwemo katika shule za Msingi Nyeburu na Kaliani pamoja na ujenzi wa shule mpya ya Sekondari Kigezi.

"Mama Samia hakuishia hapo kwenye elimu pia ameipandisha hadhi shule ya Sekondari Nyeburu, na sasa ina kidato cha kwanza mpaka cha sita. 

Haya ni matunda ambayo Mhe. Rais ameyafanya, sisi tumpongeze kwa kazi hii kubwa iliyotukuka na sisi tunamuombea dua Mungu aendelee kumuweka na kumjalia afya njema." Amesema Bw. Mambo.

Katika hatua nyingine, mwananchi huyo pia ameeleza kuhusu urahisi wa sasa wa wananchi kupata Vitambulisho vya Taifa (NIDA) kupitia programu maalumu iliyoanzishwa ngazi ya Kata pamoja na kasi ya ujenzi wa tenki kubwa la maji Bangulo, akisema yote hayo ni sehemu ya jitihada za serikali za kuondoa changamoto zote zinazowakwaza wananchi.

Ameeleza pia kuhusu fursa za uwezeshaji wananchi kiuchumi kupitia Mikopo ya Halmashauri inayotolewa kwa Vijana, wanawake na wenye ulemavu, akisisitiza wajibu wa kila mmoja kulinda amani ili kuruhusu utekelezaji wa miradi ya maendeleo na ustawi wa wananchi.
Share:

WANANCHI WA UKONGA WAMSHUKURU RAIS SAMIA KWA KUDUMISHA AMANI NA USALAMA





Na Mwandishi wetu, Dar

Wananchi wa Ukonga Mkoani Dar Es Salaam wametoa pongezi na Shukrani kwa Rais wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuimarisha amani, utulivu na usalama katika Jimbo lao la Ukonga, suala ambalo limewezesha shughuli za kiuchumi na kijamii kuendelea.

Kwaniaba ya wananchi wengine wa Jimbo hilo wakati akizungumza na Chombo chetu cha habari, Bw. Salum Issa Salum, Mkazi wa Kata ya Buyuni ameeleza kuwa licha ya kupitia baadhi ya changamoto mwishoni mwa mwaka jana, hali kwasasa ni shwari na hatua za maendeleo zimeendelea kushuhudiwa katika Kata hiyo na maeneo mengine kote Tanzania.

"Nisemee zaidi katika miundombinu, Mama amesikia kilio chetu na sasa barabara nyingi zimejengwa kwa kiwango cha lami kupitia miradi mbalimbali ikiwemo mradi wa DMDP kutoka hapa kwetu kwenda Kivule." Amesema Bw. Salum.

Katika maelezo yake, Mwananchi huyo amemuombea uhai zaidi na afya njema Rais Samia, akisisitiza pia umuhimu wa kila mwananchi kushiriki kikamilifu katika kuilinda amani ya Tanzania ili kutoa fursa ya Taifa na kila mwananchi kupiga hatua za kimaendeleo.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO ALHAMISI JANUARI 22,2026

Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger