Thursday, 27 August 2026

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO ALHAMISI AGOSTI 27,2026






Magazeti ya leo

 



Share:

Wednesday, 26 August 2026

NILE BLUES PROJECT KUWAFIKIA SHULE 10 ARUSHA KWA ELIMU YA MUZIKI, SANAA NA UTAMADUNI

Na Bora Mustafa, Arusha

 Mradi wa Nile Blues Project umeendelea kuwafikia wanafunzi wa shule mbalimbali jijini Arusha kupitia warsha za muziki, sanaa, ubunifu na utamaduni, ukiwa na lengo la kuwajengea vijana ujuzi na kuwapa nafasi ya kugundua na kukuza vipaji vyao.

Mradi huo ambao unalenga kufikia jumla ya shule 10 jijini Arusha, umeendelea na mafunzo yake katika Sekei Secondary School, ambapo wanafunzi wamepata nafasi ya kujifunza kwa vitendo pamoja na kushiriki katika shughuli za ubunifu.

Akizungumza Leo Agosti 26,2026 wakati wa programu hiyo, Lwanda Magere,Meneja wa Mradi wa Nile Blues Project, amesema mafunzo hayo yamekuwa na matokeo mazuri kutokana na mwitikio wa wanafunzi ambao wameweza kutumia maarifa waliyopata kutengeneza na kuonesha ubunifu wao wenyewe.

Pia amesema furaha kubwa kwa timu ya mradi huo ni kuona wanafunzi wakipata ujuzi ambao unaweza kuwasaidia kutambua uwezo wao na kuutumia katika maisha ya sasa na baadaye.

Kwa upande wake, Renalda Masawe, Mratibu wa Programu, amesema Sekei Secondary ni miongoni mwa shule ambazo mradi umefikia katika utekelezaji wa programu hiyo, baada ya awali kutembelea St. Patrick School.

Amesema baada ya Sekei, mpango huo utaendelea katika Kaloleni Primary School na baadaye Arusha Meru, huku lengo likiwa ni kufikisha mafunzo hayo katika shule 10 za Arusha.

Masawe amesema mpango huo utaendelea pia wiki ijayo katika shule nyingine, huku akieleza kuwa baadhi ya shule zimeonesha nia ya kushiriki katika programu hiyo kutokana na umuhimu wake kwa wanafunzi.

Amesema timu ya mradi iko tayari kushirikiana na shule zitakazohitaji programu hiyo ili kuhakikisha wanafunzi wengi zaidi wanapata fursa ya kujifunza na kukuza vipaji vyao.

Aidha, amesema lengo si kuwafundisha wanafunzi maarifa ya darasani pekee, bali pia kuwawezesha kutumia ubunifu, sanaa na utamaduni kama sehemu ya kujenga uwezo wao.

Kwa upande wake, Sir Patrick, Mwalimu wa Michezo wa Sekei Secondary School, amesema programu kama hiyo ina umuhimu mkubwa katika kuboresha elimu kwa wanafunzi kwa kuwa inawapa nafasi ya kujifunza kupitia michezo, sanaa na utamaduni.

Amesema ni muhimu shule kuendelea kutoa nafasi kwa shughuli za nje ya darasa ambazo zinaweza kuwasaidia wanafunzi kugundua vipaji na uwezo wao katika maeneo mbalimbali.

Amesema ushirikiano kati ya shule na programu zinazolenga kukuza vipaji unaweza kuwa chachu ya kuwajenga wanafunzi wenye uwezo mpana zaidi, sambamba na masomo yao ya kawaida.

Naye Rose Frank, mwanafunzi wa Kidato cha Tatu katika Sekei Secondary School, amesema mafunzo hayo yamewapa wanafunzi fursa ya kujifunza mambo mapya ambayo awali hawakuwa na uelewa nayo.

Pia amesema kupitia mafunzo hayo wanafunzi wameweza kupata maarifa mapya na kujifunza kwa vitendo, jambo ambalo limewapa hamasa ya kuendelea kutumia vipaji na ubunifu wao.

Nile Blues Project inaendelea na mpango huo katika shule mbalimbali za Arusha, huku ikilenga kuwafikia wanafunzi wengi zaidi na kuwapa ujuzi unaohusisha muziki, sanaa, ubunifu na utamaduni.

Programu hiyo pia inaendana na umuhimu wa kuwapa vijana nafasi ya kujifunza kuhusu sanaa na utamaduni wao, huku shughuli za vitendo zikiwasaidia kugeuza maarifa wanayopata kuwa ujuzi unaoweza kutumika katika maisha yao.
Share:

MICHEZO KWA WATUMISHI WA HALMASHAURI ITUMIKE KUIMARISHA AFYA, MSHIKAMANO, TIJA KIUTENDAJI - PRO. SHEMDOE

Na: OWM – TAMISEMI, Mbeya

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, amezitaka Halmashauri zote nchini kutumia michezo kama nyenzo ya kuimarisha afya, ustawi, mshikamano na tija kwa watumishi, ili kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi. 

Prof. Shemdoe ametoa wito huo Agosti 23, 2026 jijini Mbeya wakati akifungua rasmi Mashindano ya Michezo ya Watumishi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa Tanzania (SHIMISEMITA), kwa niaba ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba.

Akizungumza katika ufunguzi huo, Prof. Shemdoe amemshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuyarejesha tena mashindano ya SHIMISEMITA mwaka 2023 baada ya  kusitishwa, akitambua kwamba michezo ni sehemu muhimu ya kujenga afya ya mwili na akili, kuimarisha mahusiano kazini na kukuza ushirikiano miongoni mwa watumishi kutoka Halmashauri mbalimbali nchini.

 “Leo hii mmekutana watumishi zaidi ya 5,000 kutoka katika Halmashauri 177. Kila mmoja anao wajibu wa kujenga mahusiano mazuri na watumishi wa Halmashauri nyingine, kwani michezo ni afya, michezo ni kiunganishi. Hivyo, tumieni fursa hii kujenga afya zenu na kuimarisha ushirikiano miongoni mwenu,” amesema.

Aidha, Prof. Shemdoe amewataka Wakurugenzi wa Halmashauri kuhakikisha ushiriki wa michezo unawahusisha watumishi kutoka maeneo mbalimbali, badala ya watumishi wa Makao Makuu pekee. Amesema watumishi kutoka ngazi za kata, vijiji na vitongoji wanapaswa kupewa fursa ya kushiriki, kwa kuwa michezo itawajengea ari na morali ya kutekeleza majukumu yao, ikiwemo ukusanyaji wa mapato, ikizingatiwa kuwa mtumishi mwenye afya njema ya mwili na akili atatekeleza majukumu yake kwa ufanisi na kutoa huduma bora kwa wananchi.

Sanjari na hilo, Prof. Shemdoe amezitaka Halmashauri kuwaandaa na kuwajengea uwezo wananchi kutumia fursa zitakazotokana na Mashindano ya Soka kwa Timu za Taifa Barani Afrika (AFCON 2027). Amesema mashindano hayo si suala la michezo pekee, bali yatatoa fursa za kiuchumi, kijamii, kiutamaduni na hususan katika sekta ya utalii, ambayo ni miongoni mwa sekta muhimu katika kuiingizia Tanzania fedha za kigeni.

Kutokana na umuhimu wa michezo kwa afya na utendaji wa watumishi wa umma, Prof. Shemdoe amezitaka Halmashauri zote nchini kuhakikisha michezo ya SHIMISEMITA inawekewa kifungu katika bajeti zao na kutengewa fedha ili kuwawezesha watumishi kushiriki kikamilifu. Amesema uwekezaji katika michezo ni uwekezaji katika afya ya mwili na akili za watumishi, jambo litakalosaidia kuongeza morali, ufanisi na tija katika utekelezaji wa majukumu ya Serikali na utoaji wa huduma kwa wananchi.


Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Mhe. Beno Malisa, amemshukuru Prof. Shemdoe kwa Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI kuyaleta mashindano ya SHIMISEMITA mkoani Mbeya, na kuahidi kuwa uongozi wa mkoa umejipanga kuhakikisha usalama na ustawi wa wanamichezo wote wakati wa mashindano hayo. Aidha, Mhe. Malisa amemshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuridhia mashindano ya SHIMISEMITA kuendelea kufanyika nchini.

Naye, Katibu Mkuu wa SHIMISEMITA, Bw. Henry Kapella, ameiomba Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, ikiwa mlezi wa SHIMISEMITA, kuendelea kuzihimiza Halmashauri kutenga bajeti kwa ajili ya kuwawezesha watumishi kushiriki mashindano hayo kila mwaka. Ameshauri pia TAMISEMI kuweka kigezo cha uwepo wa fedha zilizotengwa kwa ajili ya michezo ya SHIMISEMITA katika mchakato wa kupitisha bajeti za Halmashauri, ili kuhakikisha watumishi wanapata fursa endelevu ya kushiriki michezo.

Mashindano ya SHIMISEMITA mwaka huu yamebeba kaulimbiu “Tuko Tayari kwa AFCON 2027,” ikiwa ni ujumbe unaosisitiza utayari wa Tanzania kutumia fursa za michezo, kuimarisha afya na mshikamano wa watumishi, pamoja na kunufaika na fursa za kiuchumi, kijamii, kiutamaduni na kiutalii zitakazotokana na AFCON 2027.
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger