Saturday, 19 September 2026
Friday, 18 September 2026
MAKAMU WA RAIS AZURU DAMPO LA PUGU KINYAMWEZI
-Atoa siku saba Kupatikana kwa Suluhisho la Mgogoro wa Udhibiti wa Taka
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Deogratius John Ndejembi, amefanya ziara katika Dampo la Pugu Kinyamwezi jijini Dar es Salaam, ambapo amekagua hali ya udhibiti na usimamizi wa taka.
Katika ziara hiyo, ameambatana na viongozi wa Halmashauri za Jiji la Dar es Salaam, viongozi wa Ofisi yake, Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Dkt. Immaculate Sware Semesi, pamoja na baadhi ya watumishi wa taasisi hiyo.
Mhe. Ndejembi amewaagiza viongozi wa Halmashauri za Jiji la Dar es Salaam, Wizara na taasisi husika kukutana na kujadili kwa kina njia bora na endelevu za kudhibiti taka katika dampo hilo.
Amesisitiza umuhimu wa ushirikiano wa karibu miongoni mwa wadau hao ili kupata ufumbuzi wa kudumu wa changamoto zinazolikabili eneo hilo.
Katika kutekeleza maagizo hayo, ameelekeza viongozi hao kufikia makubaliano kuhusu njia bora za udhibiti wa taka na kuwasilisha kwake ripoti yenye mapendekezo ndani ya siku saba.
Aidha, ameagiza kupuliziwa dawa maalum dhidi ya vimelea vya magonjwa katika maeneo yanayolizunguka dampo, hususan makazi ya wananchi walio jirani, ili kupunguza hatari ya kuenea kwa magonjwa yanayoweza kusababishwa na taka.
Sambamba na hilo, Makamu wa Rais amewataka viongozi na taasisi zinazohusika kushirikiana katika ukusanyaji na uwasilishaji wa takwimu sahihi za taka, ili taarifa zinazotolewa ziwe na uhalisia na kuendana.
RC TANGA : WASTAAFU TUMIENI MIFUMO YA KIDIJITALI KULINDA MAFAO YENU
Mkuu wa mkoa wa Tanga, Balozi Dkt. Batilda Burian akizungumza katika semina ya PSSSF kwa maafisa Rasilimaliwatu wa mkoa wa Tanga kilichofanyika mapema leo Septemba 17, 2026 ikiwa na lengo la kuwaelimisha huduma mbalimbali zitolewazo na Mfuko na hasa kuwahamasisha kuwasilisha madai ya wanachama kwa wakati na matumizi ya kidigitali.
Meneja wa PSSSF Kanda ya Kaskazini Mashariki, Bw. Kwame Temu akizungumza katika semina kwa maafisa Rasilimaliwatu na Utawala wa Mkoa wa Tanga.Afisa Mfawidhi wa Mkoa wa Tanga, Bi. Hanim Babika akizungumza katika semina ya PSSSF kwa maafisa Rasilimaliwatu na Utawala wa mkoa wa Tanga.
NA MWANDISHI WETU, TANGA
Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Balozi Dkt. Batilda Burian amewataka wastaafu kulinda mafao yao dhidi ya matapeli, huku akiupongeza Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) kwa kuhamasisha matumizi ya mifumo ya kidijitali inayorudisha heshima na tabasamu kwa wastaafu.
Akifungua semina ya PSSSF kwa waajiri iliyofanyika jijini Tanga iliyowakutanisha Maafisa Rasilimaliwatu na Utawala 120 kutoka taasisi mbalimbali za Serikali, Balozi Dkt. Batilda alieleza kuwa maboresho hayo yanaendana na maagizo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kutoa huduma bora, za haraka na bila vikwazo. "Niwapongeze sana PSSSF kwa hatua hii inaowezesha Mafao kulipwa kwa haraka," alisema.
Meneja wa PSSSF Kanda ya Kaskazini Mashariki, Kwame Temu, aliwahimiza waajiri kutoa taarifa za watumishi wapya ndani ya siku 30 ili wasajiliwe mapema na kuwahamasisha watumishi kutumia kikamilifu mifumo ya kielektroniki. Kwa upande wake, Afisa Mfawidhi wa Mkoa wa Tanga, Hanim Babika, alisisitiza waajiri kufanyia kazi changamoto ya kugongana kwa taarifa na kuhakikisha wafanyakazi wa mikataba kusajiliwa.
Akitoa ushuhuda, Katibu Tawala wa Mkoa wa Tanga, Rashid Mchatta alisema elimu inayotolewa na PSSSF imebadili kabisa maisha ya wastaafu wa sasa, kwani wanatoka utumishi wakiwa wanajiamini na wenye uelewa mpana wa uwekezaji. "Sekretari wangu alipostaafu, alikuja ofisini kwangu mwenye furaha, ananieleza habari za fursa za uwekezaji tu baada ya kupata mafunzo ya PSSSF," alisema Katibu Tawala.
PSSSF inaendelea kuwasihi wanachama na wastaafu nchini kutumia mifumo rasmi ya kielektroniki ili kupata huduma kwa haraka, uwazi na usalama zaidi ambayo ni PSSSF Member Portal na PSSSF Kiganjani, aidha wawawe na changamoto kutumia simu ya bure kuwasiliana na Mfuko ambazo ni 0800110055.
Magazeti


























