Saturday, 22 August 2026

TFS YATUMIA JOGGING KAMA SEHEMU YA KUJIIMARISHA KIAFYA


WAFANYAKAZI wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Kanda ya Mashariki wamefanya mazoezi ya kukimbia umbali wa takribani kilomita saba katika eneo la Coco Beach jijini Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya kujiweka katika hali nzuri ya kiafya na utayari wa kutekeleza majukumu yao.

Akizungumza baada ya zoezi hilo leo Agosti 22, 2026 Jijini Dar es Salaam, Mhifadhi Mwandamizi wa TFS, Sunday Nachule, kwa niaba ya Kamanda wa Kanda ya Mashariki, amesema mazoezi hayo ni sehemu ya juhudi za kuhakikisha askari wanakuwa timamu muda wote kwa ajili ya kutekeleza majukumu yao.

Amesema TFS itaendelea kuhamasisha watumishi wake kushiriki katika mazoezi ya mwili mara kwa mara ili kujenga afya na utayari wa kiutendaji.

Katika zoezi hilo, wanafamilia wa TFS wamepata pia fursa ya kufanya mazoezi pamoja na Mbunge wa Jimbo la Buchosa, Eric Shigongo, ambaye amewapongeza kwa juhudi hizo na kuwataka kuendelea na mazoezi.

Shigongo amesema misitu ni muhimu kwa uhai wa binadamu kutokana na mchango wake katika upatikanaji wa hewa safi na maji, hivyo wananchi wanapaswa kushirikiana na Serikali katika kuilinda.

Ametaja maeneo ya Buhindi na Lubondo yaliyopo katika Jimbo la Buchosa kuwa miongoni mwa maeneo yenye misitu inayosimamiwa na TFS, akisisitiza umuhimu wa wananchi kutunza rasilimali hiyo.

“Bila misitu hakuna uhai. Kwa hiyo nawaomba Watanzania waendelee kutunza misitu kwa sababu ni chanzo cha hewa na maji,” amesema Shigongo.

Aidha, ameipongeza TFS kwa kazi inayofanya katika kulinda na kuhifadhi misitu nchini, akieleza kuwa wananchi wanapaswa kuwa wadau wa uhifadhi kwa kuhakikisha rasilimali hiyo inalindwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Share:

DKT. YONAZI AWAKUMBUSHA VIJANA KULINDA AFYA ZAO KATIKA MAPAMBANO DHIDI YA UKIMWI



Na. Mwandishi Wetu ,Kazuramimba Kigoma

Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dkt. Jim Yonazi, Amewaasa vijana kulinda afya zao na kuepuka tabia hatarishi ili kupunguza maambukizi mapya ya VVU, kwa kuzingatia kuwa ni kundi linaloongoza kuwa hatarini zaidi nchini Tanzania.

Dkt. Yonazi ameyasema hayo mwishoni mwa wiki wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa Afua za UKIMWI Wilaya ya Uvinza Mkoa wa Kigoma alipoambatana na Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania, Dkt. Adam Mrisho, timu ya wataalam kutoka Ofisi yake, Wizara ya Afya, TAMISEMI na Ofisi ya Mkoa huo.

Aidha amepata wasaa kutembelea Kituo cha Maarifa Kata ya Kazuramimba mkoani humo kinachotoa huduma za masuala ya VVU na UKIMWI, na kukutana na vijana wanaotekeleza afua za UKIMWI kupitia vikundi vya uzalishaji mali kwa lengo la kujiinua kiuchumi na kujiletea maendeleo yao.

Akiwa katika kituo hicho, Dkt. Yonazi amepokea taarifa kutoka kwa mwenyekiti wa kikundi, Billy Sekibaha, kuhusu shughuli zinazofanywa na kikundi hicho ikiwemo za biashara ndogondogo za kuuza dagaa pamoja na shunguli za ushonaji wa nguo kwa lengo la kujikwamua kiuchumi na kuondokana na dhana ya utegemezi.

Amesisitiza kuwa, kundi la vijana linategemewa na Taifa katika shughuli za uzalishaji mali na kujiletea maendeleo yao na Taifa kwa ujumla hivyo ni vyema vijana wakaendelea kujilinda na kulinda wengine kwa kutambua hali zao na endapo wakagundulika kuwa na maambukizi ya VVU inashauriwa kuanza kutumia dawa mapema.

"Mnafanya kazi nzuri sana, endeleeni kuchangamkia uwepo wa mitandao ya kijamii kutangaza bidhaa zenu ili kuwafikia wateja wengi zaidi na kujitangaza kitaifa na kimataifa," alisisitiza Dkt. Yonazi

Kwa upande wake Mtendaji wa TACAIDS, Dkt. Adam Mrisho amewapongeza vijana hao kwa kazi nzuri wanazofanya na kusisitiza kuwa Tume itaendelea kuwawezesha vijana kiuchumi na kuwajengea uwezo ili kuendeleza mapambano dhidi ya maambukizi mapya ya VVU na kufikia lengo la kutokomeza UKIMWI ifikapo mwaka 2030.











Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMAMOSI AGOSTI 22,2026




magazeti


Share:

Thursday, 20 August 2026

KONGAMANO LA UCHUMI WA BLUU KUFUNGUA FURSA ZA KUKUZA KIPATO NA UCHUMI PROF- GURUMO



Na Sheila Ahmadi, Dar es Salaam

Kongamano la Tano la Uchumi wa Bluu linatarajiwa kuwakutanisha wadau kutoka ndani na nje ya Tanzania kujadili namna ya kutumia fursa za uchumi wa bluu kuongeza kipato cha wananchi na kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa.

Akizungumza Jijini Dar e s salaam na wanahabari kuhusu kongamano hilo, Mkuu wa Chuo cha Bahari Dar es Salaam (DMI) Profesa Tumaini Gurumo amesema kuwa uchumi wa bluu ni miongoni mwa sekta zinazolenga kuchangia katika kukuza uchumi wa Tanzania, hivyo ni muhimu kwa wadau kukutana na kujadili namna bora ya kutumia rasilimali zilizopo katika sekta hiyo.

lengo la kongamano hilo ni kuwaunganisha wadau mbalimbali ili kubadilishana uzoefu, kujadili changamoto na kutafuta suluhisho litakalowezesha uchumi wa bluu kuwa na tija zaidi kwa wananchi na taifa kwa ujumla.

“Lengo hasa la kongamano hili ni kuwakutanisha wadau wa uchumi wa bluu waweze kutafakari namna gani tunaweza kuwezesha uchumi wa bluu, ili tutoke katika kiwango tulichopo sasa na kufikia hatua ambayo inaweza kuongeza kipato cha mtu mmoja mmoja, lakini pia kukuza uchumi wa taifa,” amesema.

Amesema kongamano hilo pia litatoa fursa kwa watafiti kuwasilisha tafiti mbalimbali walizofanya, huku washiriki wakijadili matokeo ya tafiti hizo na kutoa maoni yatakayosaidia kuboresha shughuli zinazohusiana na uchumi wa buluu

pamoja na kukuza uchumi wa taifa, ni muhimu kuhakikisha wananchi wanapata elimu na uelewa wa kutosha kuhusu fursa zinazopatikana katika uchumi wa bluu ili waweze kuzitumia kuboresha maisha yao.

“Tunataka kuwapa Watanzania uelewa wa shughuli za uchumi wa bluu na namna wanavyoweza kufanya vizuri zaidi katika shughuli ambazo tayari wamekuwa wakizifanya kwa miaka mingi. Tukipata Watanzania wenye uelewa, elimu na ujuzi, ndipo tutakapoweza kupata ubunifu na maendeleo ya sayansi na teknolojia,” amesema Profesa Gurumo.

Chuo cha Bahari Dar es Salaam, ni taasisi ambayo imejikita katika kutoa elimu na mafunzo yanayohusiana na masuala ya bahari, kufanya tafiti na kutoa ushauri kwa Serikali pamoja na taasisi binafsi.

Katika hatua nyingine chuo hicho kinaendelea kutoa elimu kwa jamii kuhusu uchumi wa bluu ili kuongeza uelewa wa fursa zilizopo, kuimarisha mifumo na sera, pamoja na kuwahamasisha wawekezaji kutumia fursa hizo.

Hivyo kongamano hilo litawakutanisha washiriki kutoka taasisi za serikali na binafsi, watafiti, wanataaluma, wawekezaji na wadau wa maendeleo kutoka Tanzania na mataifa mbalimbali.

Sanjari na hayo Baadhi ya nchi za Afrika ambazo zimethibitisha kushiriki ni pamoja na Comoro, Kenya, Uganda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, huku nchi nyingine nje ya Afrika zikiwemo China, Sweden na Canada pia zikitarajiwa kushiriki.

Kupitia washiriki hao watapata fursa ya kujadili tafiti na kuonesha ubunifu mbalimbali unaohusiana na matumizi ya rasilimali za bahari na maendeleo ya uchumi wa bluu.

Aidha baada ya kukamilika kwa kongamano hilo, wanatarajia kupata maarifa mapya yatakayowanufaisha Watanzania na washiriki wengine, pamoja na mapendekezo ya kisera yatakayosaidia kuboresha mazingira ya kufanya shughuli za uchumi wa bluu.

“Tunatarajia kupata mapendekezo ya kisera. Zipo sera ambazo zinatumika, lakini kutokana na mabadiliko yanayotokea, kuna umuhimu wa kuangalia kama zinahitaji marekebisho au kama kuna maeneo yanahitaji sera mpya,” amesema Profesa Gurumo.




Share:

HII NDIO TOFAUTI KATI YA WAONGOZAJI WA NDEGE NA WAEGESHAJI WA NDEGE



Katika sekta ya usafiri wa anga, kuna wataalamu mbalimbali wanaoshiriki kuhakikisha ndege zinafanya safari kwa usalama na ufanisi. Miongoni mwa wataalamu ambao mara nyingi huchanganywa ni Waongozaji wa Ndege, wanaojulikana kama Air Traffic Controllers, na Waegeshaji wa Ndege, wanaojulikana kitaalamu kama Aircraft Marshallers.

Waegeshaji wa ndege ni wataalamu wanaofanya kazi katika maeneo ya maegesho ya ndege viwanjani. Mara nyingi huonekana wakiwa wamevaa mavazi maalum ya usalama na kutumia vijiti vya mwanga au ishara za mikono kumwelekeza rubani wakati ndege inapokaribia sehemu ya maegesho au inapojiandaa kuondoka.

Jukumu lao ni kuhakikisha ndege inaelekezwa kwa usahihi katika eneo lililotengwa bila kuhatarisha usalama wa ndege, vifaa vya uwanja, majengo au watu waliopo katika mazingira ya karibu. Ishara wanazotumia hutambulika kimataifa na humsaidia rubani kufanya maamuzi sahihi hasa katika maeneo ambayo mwonekano kutoka ndani ya ndege unaweza kuwa na mipaka.

Historia ya kazi ya uegeshaji wa ndege inaanzia katika miaka ya mwanzo ya maendeleo ya usafiri wa anga, ambapo mawasiliano kati ya marubani na wahudumu wa ardhini yalitegemea zaidi ishara za mikono. Pamoja na maendeleo ya teknolojia katika viwanja vya ndege, kazi ya Aircraft Marshaller bado inaendelea kuwa sehemu muhimu ya shughuli salama za ndege ardhini.

Kwa upande mwingine, Waongozaji wa Ndege, au Air Traffic Controllers, wana jukumu la kusimamia na kuratibu mwendo wa ndege angani na katika maeneo maalum ya viwanja vya ndege. Hutumia mifumo ya mawasiliano, ufuatiliaji na taratibu za uongozaji wa ndege kuhakikisha ndege zinatenganishwa kwa umbali salama na kupewa maelekezo wakati wa kuruka, kutua na kujiendesha katika maeneo wanayoyasimamia.

Tofauti kubwa kati ya wataalamu hawa ni kwamba Air Traffic Controllers huongoza na kuratibu mwendo wa ndege kupitia mawasiliano ya redio na mifumo ya uongozaji, wakati Aircraft Marshallers humwelekeza rubani kwa ishara za kuona katika eneo la maegesho ya ndege.

Pamoja na tofauti hiyo ya majukumu, wataalamu hawa wote ni sehemu muhimu ya mfumo wa usalama wa usafiri wa anga na huchangia kuhakikisha shughuli za ndege zinafanyika kwa mpangilio, usalama na ufanisi.


Nchini Tanzania, Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) ina jukumu la kusimamia na kudhibiti usalama wa usafiri wa anga kwa kuzingatia sheria, kanuni na viwango vinavyotambuliwa kitaifa na kimataifa, ikiwemo miongozo ya Shirika la Kimataifa la Usafiri wa Anga, ICAO.

 

Share:

RUWASA KWA KUSHIRIKIANA NA WADAU WAJA NA MKAKATI WA KUSHUGHULIKIA SUALA LA USAFI WA MAZINGIRA VIJIJINI


Morogoro

Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA), kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa Sekta ya Maji, Afya na Usafi wa Mazingira, umeanza rasmi mchakato wa kuandaa Mkakati wa RUWASA wa Menejimenti ya Tope Kinyesi (Faecal Sludge Management Strategy), unaolenga kuweka mfumo madhubuti, salama na endelevu wa menejimenti ya tope kinyesi katika maeneo ya vijijini.

Akifungua Kikao Kazi cha National Task Force kinachofanyika mjini Morogoro, Mkurugenzi Mkuu wa RUWASA, Eng. Wolta S. Kirita, amesema maandalizi ya Mkakati huo ni hatua muhimu katika kuimarisha huduma za usafi wa mazingira vijijini na kupunguza athari za kiafya na kimazingira zinazoweza kusababishwa na menejimenti isiyo salama ya tope kinyesi.

Eng. Kirita amesisitiza umuhimu wa ushirikiano wa wadau katika kuhakikisha Mkakati utakaoandaliwa unazingatia mazingira halisi ya vijijini, unaweka bayana majukumu ya wadau mbalimbali na, muhimu zaidi, unatekelezeka na kuwa endelevu.

“Pamoja na jukumu letu kubwa la kuhakikisha wananchi wa vijijini wanapata huduma endelevu za maji, RUWASA pia ina wajibu katika masuala ya usafi wa mazingira. Tupo tayari kushirikiana na wadau wote kuhakikisha tunakuwa na mfumo bora na endelevu wa menejimenti ya tope kinyesi katika maeneo ya vijijini,” amesema Eng. Kirita.

Awali, akimkaribisha Mkurugenzi Mkuu, Mkurugenzi wa Usambazaji Maji na Usafi wa Mazingira, Eng. Mariam Majala, amesema menejimenti salama ya tope kinyesi bado ni changamoto inayohitaji juhudi za pamoja za kitaalamu na kitaasisi.

Eng. Majala amesema maandalizi ya Mkakati huo yatawezesha kuweka mwelekeo wa pamoja kuhusu namna bora ya kukusanya, kusafirisha, kutibu na kutupa au kutumia tena tope kinyesi kwa njia salama, sambamba na kuweka mpango na mwongozo wa utekelezaji unaozingatia mazingira na mahitaji ya maeneo ya vijijini.

Kikao Kazi hicho cha siku nne kinawaleta pamoja wajumbe wa National Task Force kutoka RUWASA, Wizara na Taasisi za Serikali, Vyuo Vikuu, Wadau wa Maendeleo pamoja na wataalamu wenye uzoefu katika Sekta ya Maji na Usafi wa Mazingira.

Miongoni mwa taasisi zinazoshiriki katika Kikao Kazi hicho ni Wizara ya Maji, Wizara ya Afya, Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Chuo Kikuu Ardhi, EWURA, SNV na WaterAid, pamoja na wadau wengine wa Sekta ya Maji na Usafi wa Mazingira.

Kikao hicho ni sehemu ya hatua za awali za maandalizi ya Mkakati na kinatarajiwa kujenga uelewa wa pamoja kuhusu msingi wa kisera na kisheria, hali ya sasa ya menejimenti ya tope kinyesi vijijini, majukumu ya wadau, mbinu za maandalizi ya Mkakati pamoja na mpango wa utekelezaji wa kazi ya National Task Force.

Kupitia mchakato huo, RUWASA inalenga kuhakikisha kuwa Mkakati utakaoandaliwa unatoa mwelekeo wa kitaifa na mfumo unaotekelezeka wa menejimenti salama na endelevu ya tope kinyesi katika maeneo ya vijijini, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuboresha huduma za maji na usafi wa mazingira na kulinda afya ya jamii na mazingira.

Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger