Friday, 24 July 2026

BARAZA LA VYAMA VYA SIASA LAHIMIZA MARIDHIANO YA NDANI NA USHIRIKIANO WA KITAIFA



Vyama vya siasa nchini vimehimizwa kuzingatia maridhiano yanayosimamiwa na Watanzania wenyewe pasipo kutegemea msaada au ushawishi kutoka mataifa ya nje.

Mwenyekiti wa Baraza la Vyama vya Siasa Tanzania, Juma Ali Khatib, aliyasema hayo mjini Morogoro alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kumalizika kwa uchaguzi wa viongozi wa baraza hilo.

Khatib, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Taifa wa chama cha ADA-TADEA, alieleza kuwa maridhiano ya dhati hufanywa na viongozi wenye serikali kwa sababu ndio wenye mamlaka ya Bunge na dola, huku akimpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuleta fikra hiyo chanya inayojenga nchi kwa maslahi mapana ya wananchi.

Katika mazungumzo yake, Khatib aliwakumbusha wanasiasa kuachana na siasa za kuwagawa wananchi na badala yake wajikite katika kujenga umoja, huku akisisitiza kuwa hoja za maridhiano hazipaswi kutumika kama mtaji wa kisiasa.

Aliongeza kuwa baraza hilo limepanga kuishauri serikali kupitia upya suala la zuio la mikutano ya hadhara ili vyama ambavyo havina makosa visiadhibiwe kutokana na makosa ya chama kimoja. Mtazamo huu ulitolewa wakati serikali kupitia Msemaji Mkuu wake, Gerson Msigwa, ikieleza kuwa zuio hilo litaendelea hadi vyombo vya ulinzi na usalamaakapojiridhisha na hali ya amani.

Wakati huohuo, uchaguzi wa viongozi wa baraza hilo ulimrejesha Juma Ali Khatib kuwa mwenyekiti kwa miaka mingine miwili baada ya kujinyakulia kura 30 kati ya 31 zilizopigwa, huku nafasi ya makamu mwenyekiti ikichukuliwa na John Mongella ambaye ni Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Bara aliyetetea nafasi yake kwa idadi hiyo hiyo ya kura. Viongozi wengine kama Katibu Mkuu wa UDP, Saum Rashid, na Mwenyekiti wa AAFP, Said Sudi Said, walitumia fursa hiyo kuwakumbusha Watanzania umuhimu wa kulinda amani, kudumisha utulivu, na kutatua changamoto zote za kitaifa kupitia mazungumzo ya ndani bila kuhusisha nguvu za nje.
Share:

TNCM YAIDHINISHA OMBI LA TANZANIA LA UFADHILI WA MZUNGUKO WA NANE (GC8) WA MFUKO WA DUNIA KWA KIPINDI CHA 2027–2029



Na. Mwandishi wetu - Dar es Salaam

Kamati ya Kitaifa ya Kuratibu na Kusimamia Fedha za Mfuko wa Dunia nchini Tanzania (Tanzania National Coordinating Mechanism – TNCM), imeidhinisha rasmi Ombi la Tanzania la Ufadhili wa Mzunguko wa Nane wa Mfuko wa Dunia (Global Fund Grant Cycle 8 – GC8) kiasi cha dola za Marekani milioni 538.6 kwa ajili ya kuendeleza mapambano dhidi ya UKIMWI, Kifua Kikuu (TB) na Malaria, pamoja na kuimarisha Mifumo Thabiti na Endelevu ya Afya (RSSH), katika kipindi cha utekelezaji kuanzia Januari 2027 hadi Desemba 2029.

Uidhinishaji huo umefanyika jijini Dar es Salaam katika kikao maalum cha TNCM kilichoongozwa na Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge,Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. Jim Yonazi, ambaye pia ni Mwenyekiti wa TNCM.

Dkt. Yonazi amesema kuwa, mchakato wa maandalizi ya Ombi la GC8 ulianza rasmi tarehe 13 Machi, 2026 na umeendelea kwa zaidi ya miezi minne, ukihusisha mashauriano ya kina, majadiliano ya kitaifa, upangaji wa vipaumbele, uandishi wa andiko, mapitio ya kitaalamu na uhakiki wa nyaraka za maombi.

Aidha, alifafanua kuwa, mchakato huu umejengwa katika msingi wa ushirikishwaji mpana wa wadau, uwazi, uwajibikaji na umiliki wa kitaifa ambapo zaidi ya wadau 270 walishiriki kwa uwakilishi wa makundi mbalimbali, yakiwemo Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara, Idara na Taasisi zake; Washirika wa Maendeleo, Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mashirika ya Kimataifa, Asasi za Kiraia, Sekta Binafsi, Mashirika ya Dini, watu wanaoishi na VVU, jamii zilizo katika hatari kubwa ya maambukizi na zilizoathiriwa na magonjwa hayo; pamoja na wataalamu wa sekta ya afya.

Dkt. Yonazi ameeleza kuwa uwekezaji wa Mfuko wa Dunia umeendelea kutoa mchango mkubwa katika juhudi za Serikali za kuboresha afya na ustawi wa Watanzania, na kusema utekelezaji wa GC8 utatoa fursa kwa Nchi kuendela kuzuia maambukizi mapya ya VVU, kuongeza upatikanaji wa dawa za kufubaza makali ya VVU (ARV), kuimarisha kinga, uchunguzi na matibabu ya Malaria, pamoja na kuboresha ugunduzi wa mapema na matibabu ya Kifua Kikuu.

“Kuidhinishwa kwa Ombi hili la Ufadhili ni matokeo ya kazi kubwa na ushirikiano wa wadau wetu ambao wamewekeza muda, utaalamu na rasilimali kuhakikisha kuwa vipaumbele vilivyoainishwa vinazingatia mahitaji ya nchi pamoja na sauti za jamii na makundi yanayoathiriwa na magonjwa hayo”.Alisema Dkt. Yonazi.

Aliongezea kuwa,hatua hiyo ni mafanikio muhimu yanayoonesha dhamira ya Tanzania ya kuendeleza mapambano dhidi ya magonjwa hayo matatu, sambamba na kujenga mfumo wa afya ulio imara, jumuishi na endelevu.

Dkt. Yonazi ameshukuru Sekretarieti ya Mfuko wa Dunia iliyopo Geneva (Global Fund Country Team), wajumbe wa TNCM pamoja na wadau wote walioshiriki katika maandalizi na ukamilishaji wa maombi hayo, amepongeza jitihada zao akisema zimekuwa na mchango muhimu kuwezesha kufikia hatua

Kwa upande wake, Katibu Mtendaji wa TNCM, Bw. Kent Pius, ametoa shukrani maalum kwa Mwenyekiti wa TNCM, Mfuko wa Dunia, wajumbe na wadau wote kwa ushirikiano na uwajibikaji mkubwa katika kuhakikisha kuwa zoezi hili limefanyika kwa ufanisi na ubora uliokusudiwa na kusema kuwa, hatua hii ni matokeo ya dhamira ya dhati na juhudi za pamoja.

“TNCM itaendelea kuratibu ushirikiano kati ya Serikali, jamii, Asasi za Kiraia, Washirika wa Maendeleo, Sekta Binafsi na wadau wa kimataifa katika kuhakikisha uwekezaji wa Mfuko wa Dunia unachangia katika kufikia malengo ya Kitaifa na Kimataifa ya kutokomeza UKIMWI, Kifua Kikuu na Malaria kama vitisho vya afya ya jamii,” alisema Kent





Share:

WAZIRI KAIRUKI AANIKA MAFANIKIO MAKUBWA YA MAWASILIANO MPWAPWA, ATAJA MIKAKATI YA KUIMARISHA ELIMU KIDIGITALI



Na Dotto Kwilasa, Dodoma

Serikali imesema itaendelea kuwekeza kwa kiwango kikubwa katika sekta za elimu, mawasiliano na huduma za kijamii mkoani Dodoma, huku ikiahidi kuondoa changamoto za mawasiliano na kuimarisha miundombinu ya maendeleo ifikapo mwaka 2030.

Hayo yameelezwa Julai 23, 2026 na Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki, wakati wa ziara yake ya kikazi Wilaya ya Mpwapwa iliyolenga kukagua miradi ya maendeleo na kusikiliza kero za wananchi katika Kijiji cha Mlembule.

Akizungumza na wananchi Wilayani humo, Waziri Kairuki amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kutekeleza kwa vitendo Ilani ya CCM ya mwaka 2025–2030 kwa kuwekeza katika miradi inayogusa maisha ya wananchi, hususan elimu, afya, mawasiliano, maji na miundombinu.

Katika sekta ya elimu, amesema ndani ya kipindi cha miaka mitano Serikali imejenga shule mpya 12 katika Wilaya ya Mpwapwa kwa gharama ya shilingi bilioni 15.1. Aidha, madarasa 251, mabweni 11, matundu ya vyoo 265, maabara tano za sayansi, nyumba saba za walimu na mabwalo manne ya chakula kwa wanafunzi yamejengwa ili kuboresha mazingira ya kujifunzia.

Ameongeza kuwa katika mwaka wa fedha 2026/27, Serikali imetenga shilingi milioni 562.9 kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya ya sekondari pamoja na matundu ya vyoo, hatua inayolenga kuongeza fursa za elimu kwa watoto wa Mpwapwa.

Mbali na elimu, Waziri Kairuki amesema Serikali imepiga hatua kubwa katika sekta ya mawasiliano ambapo mkoani Dodoma tayari minara 488 ya mawasiliano imesimikwa, huku zaidi ya wananchi 150,000 wakinufaika na huduma bora za mawasiliano na matumizi ya mkongo wa taifa wa mawasiliano wenye urefu wa kilomita 942.5.

Amesema Serikali inaendelea na utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya mawasiliano, ikiwemo kukamilisha minara 636 ifikapo Machi 2027 pamoja na mradi mwingine wa minara 280, sambamba na kufanya tathmini ya maeneo yenye changamoto ili kuhakikisha huduma za mawasiliano zinawafikia wananchi wote.

Kairuki amesisitiza kuwa uboreshaji wa miundombinu ya TEHAMA ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kujenga uchumi wa kidijitali na kuongeza fursa za elimu, biashara na utoaji wa huduma za Serikali kwa njia ya mtandao.

Katika ziara hiyo, Waziri huyo pia aliweka jiwe la msingi la shule mpya ya msingi na awali katika Kijiji cha Mlembule pamoja na kukagua ujenzi wa chumba maalumu cha TEHAMA, ambapo alitangaza kuwa Serikali itapeleka kompyuta 22 kwa ajili ya kuwawezesha wanafunzi kujifunza kwa kutumia teknolojia.

Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Mpwapwa, Adam Malima, amesema pamoja na hatua kubwa iliyofikiwa katika ujenzi wa minara ya mawasiliano, bado yapo maeneo yanayokumbwa na changamoto ya mtandao, ikiwemo Kijiji cha Mlembule ambako wananchi hutegemea mawasiliano kutoka minara ya maeneo jirani.

Ameiomba Serikali kuharakisha utekelezaji wa miradi ya mawasiliano ili kuhakikisha wananchi wa maeneo yote ya jimbo hilo wanapata huduma bora za mawasiliano.


Share:

Thursday, 23 July 2026

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO IJUMAA JULAI 24,2026



Magazeti
















Share:

MAADILI ,UZALENDO NA MAENDELEO YA TAIFA



Serikali imesisitiza kuwa maendeleo ya kweli na ya kudumu ya Taifa yanategemea kwa kiasi kikubwa ujenzi wa wananchi wenye maadili, uzalendo, uwajibikaji na mshikamano thabiti.

Akizungumza jijini Dar es Salaam alipokutana na Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere, Joseph Butiku, Waziri Mkuu Dk. Mwigulu Nchemba alibainisha kuwa serikali itaendelea kuwekeza katika kuboresha tabia za wananchi na kuimarisha utendaji kazi wa taasisi za umma ili kulinda haki za wananchi na kuimarisha amani nchini.

Aidha, serikali imeahidi kuendelea kushirikiana kwa karibu na Taasisi ya Mwalimu Nyerere katika kukuza umoja wa kitaifa na kuunga mkono ujenzi wa Taasisi ya Kimataifa ya Uongozi ya Mwalimu Nyerere.

Kwa upande wake, Joseph Butiku alimpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa uongozi wake thabiti na kumpongeza Waziri Mkuu kwa jinsi anavyomsaidia katika kusimamia shughuli za serikali na kutatua changamoto za wananchi kupitia ziara zake mikoani.

Butiku alitumia fursa hiyo kukemea tabia ya baadhi ya watu kuwavunjia heshima viongozi, wazee, na viongozi wa dini, akisisitiza kuwa wananchi wanapaswa kukosoana kwa hoja na kwa kufuata sheria huku wakilinda amani na mshikamano wa Taifa.

Vilevile, aliishukuru serikali kwa ushirikiano wake unaoendelea na Taasisi ya Mwalimu Nyerere, pamoja na kuipongeza kwa kuchukua hatua za kuimarisha misingi ya demokrasia, haki za watu, utawala wa sheria, na kutoa kipaumbele suala la Katiba Mpya kupitia Ilani ya CCM ya mwaka 2025–2030.
Share:

Wednesday, 22 July 2026

MUUNGANO WA TANZANIA NI TUNU, KILA MMOJA AULINDE - MASAUNI



Chalinze - Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni amesema, kati ya jambo ambalo halipaswi kuchezewa ni Muungano ambao unatakiwa kulindwa na kila mmoja maana ndio alama kubwa ya
Tanzania.

Mhe. Masauni ameyasema hayo wilayani Bagamoyo mkoani Pwani katika ziara yake ya kikazi aliyoifanya Julai 22, 2026 akieleza kufurahishwa na shughuli za maendeleo katikaMkoa wa Pwani zinazofanyika ambazo zinaunganisha na Zanzibar ikiwemo bandari.

"Fursa ya Muungano inatakiwa kusaidia pande zote bara na Zanzibar na katika hili itakuwa inasaidia zaidi kwenye sekta ya utalii kwani mtalii anapokuja Zanzibar anaunganisha na Bagamoyo kwenye hifadhi ya Saadani",amesema.

Kadhalika amewataka vijana kuwa makini na matumizi ya mitandao ya kijamii katika kipindi hiki cha utandawazi kutokana na kuwepo kwa upotoshaji mkubwa unaofanywa na baadhi ya vijana.

Amewataka kutumia mitandao ya kijamii kwa mambo ambayo yatakuwa na faida kwao hususani kujifunza mbinu za kuboresha shughuli zao za kibiashara za kujikwamua kiuchumi.

Kwa upande wake Mbunge wa Chalinze ambaye ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais,Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete amesema Chalinzi inabadilika kwa kasi kutokana na kazi kubwa inayofanywa na Serikali pamoja na wananchi wa eneo hilo.

Ameongeza kuwa ushirikiano baina ya viongozi na wananchi imesaidia kufanya kimbilio kwa wawekezaji wengi kutokana na kuwepo kwa miundombinu Rafiki jambo ambalo limeifanya Chalinze kukua kukua kila siku.

Awali Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhe. Abubakar Kunenge alisema Wilaya ya Bagamoyo ni kati ya maeneo ya utalii ambayo kwasasa yanakuwa kwa kasi kwa kuwa na wawekezaji wengi wazawa na wageni wanaofika kuwekeza.

“Kuhusu suala la Muungano hapa Pwani watu wengi wanakutana na kufanya shighuli mbalimbali kutoka Zanzibar na Bagamoyo ni moja ya mji ambao wananchi wananufaika
na Muungano wa nchi yetu,”

Ameaema upo mpango wa ujenzi wa reli ya km 100 kutoka Bagamoyo kwenda bandari kavu ya Kwala ambayo itasaidia usafirishaji wa bidhaa mbalimbali kutoka katika mji huo.

Mhe. Kunenge amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa ujenzi wa barabara ya Afrika Mashariki ambayo itafungua wigo wa usafirishaji wa na Barabara ya Mlandizi Manerumango.


Amewataka wawekezaji kujenga hoteli kubwa za kitalii kwani uwekezaji huo unahitajika kwenye Wilaya hiyo ya kitalii ambayo kwasasa imekuwa na fursa nyingi za kimaendeleo.


Mkuu huyo wa Mkoa amemuomba Waziri Masauni kufikisha ombi la Halmashauri ya Chalinze kuwa Manispaa kutokana na kuwa na vigezo vingi kikiwemo cha ongezeko la kukua kwa mapato.
Share:

TAASISI ZA UMMA ZATAKIWA KUACHANA NA UTENDAJI WA MAZOEA ILI KUFANIKISHA DIRA 2050



Na Mwandishi Wetu - Pwani.

Serikali imezitaka Taasisi, Mashirika ya Umma na Wakala za Serikali kuachana na utendaji wa mazoea na kujielekeza katika uongozi unaozingatia matokeo, ubunifu, uwajibikaji na ushirikiano wa karibu na sekta binafsi ili kuharakisha utekelezaji wa DIRA ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Wito huo ulitolewa Jumanne jioni na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Mhe. Prof. Kitila Mkumbo, wakati akifungua Mafunzo Elekezi kwa Watendaji Wakuu wa Taasisi, Mashirika ya Umma na Wakala za Serikali yanayoratibiwa na Ofisi ya Msajili wa Hazina kwa kushirikiana na Taasisi ya UONGOZI katika Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere, Kibaha mkoani Pwani.

Mafunzo hayo ya siku nne yanafanyika chini ya kaulimbiu "Kutoka Maono mpaka Matokeo: Kufungamanisha Utendaji wa Mashirika ya Umma na DIRA 2050."

Akizungumza katika hafla hiyo, Prof. Mkumbo alisema Tanzania imeweka lengo la kufikia uchumi wa kati wa juu na kukuza Pato la Taifa (GDP) kutoka dola za Marekani bilioni 85 hadi dola trilioni 1 ifikapo mwaka 2050 kupitia DIRA 2050.

Alisema mafanikio ya DIRA hiyo hayatategemea ubora wa sera na mipango iliyoandaliwa pekee, bali uwezo wa viongozi wa Taasisi za Umma kutafsiri maono hayo kuwa matokeo yanayoonekana katika maisha ya wananchi.

“Jukumu mlilonalo ni kubwa. Tunahitaji viongozi wenye maono, uwajibikaji, ubunifu na uadilifu watakaoweza kutafsiri DIRA 2050 kuwa matokeo yanayopimika,” alisema.

Prof. Mkumbo alisema dunia ya sasa inabadilika kwa kasi kutokana na maendeleo ya teknolojia, ushindani wa kimataifa wa kuvutia uwekezaji, mabadiliko ya tabianchi na mabadiliko ya masoko ya dunia, hivyo Taasisi za Umma hazina budi kubadilika ili ziwe sehemu ya suluhisho la changamoto za maendeleo.

Alisisitiza kuwa Serikali haitapima mafanikio ya taasisi kwa idadi ya vikao vinavyofanyika au taarifa zinazoandaliwa, bali kwa matokeo yanayopatikana kupitia utoaji wa huduma bora, ongezeko la tija, uwekezaji, ajira na mapato ya Serikali.

Aidha, aliwataka Watendaji Wakuu kuhakikisha mipango ya kimkakati ya taasisi zao, bajeti, mipango ya mwaka, mikataba ya utendaji na viashiria vya utendaji vinaendana na DIRA 2050 ili kila taasisi iwe na mchango unaopimika katika utekelezaji wa malengo ya Taifa.

Alisema DIRA hiyo imebainisha sekta za kimageuzi zitakazochochea ukuaji wa uchumi, zikiwemo kilimo, viwanda, utalii, ujenzi, madini, uchumi wa buluu, michezo na ubunifu, huduma za kifedha pamoja na sekta ya huduma, huku Taasisi za Umma zikipewa jukumu la kuwezesha ukuaji wa sekta hizo.

Prof. Mkumbo alisema utekelezaji wa DIRA 2050 unahitaji ushirikiano wa karibu kati ya Serikali, sekta binafsi, wananchi na wadau wa maendeleo.

Alieleza kuwa sekta binafsi ndiyo injini ya uwekezaji, ubunifu, uzalishaji na uundaji wa ajira, hivyo Taasisi za Umma zinapaswa kujiona si wadhibiti wa maendeleo pekee, bali pia wawezeshaji wa uwekezaji kwa kuweka mazingira rafiki ya biashara na kuvutia mitaji.

“Tunapaswa kujenga mazingira yatakayowezesha sekta binafsi kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa DIRA 2050. Ushirikiano huo ndio utakaoharakisha ukuaji wa uchumi na kufikia malengo ya Taifa,” alisema huku akionya taasisi za umma kutokuwa kikwazo kwa wawekezaji.

Aliongeza: “Ninyi mmepewa dhamana ya kuongoza mageuzi ya Taasisi za Umma. Watanzania wanatarajia kuona matokeo kupitia uongozi wenu. Fanyeni kazi kwa bidii, uadilifu na ubunifu ili taasisi mnazoziongoza ziwe chachu ya kufanikisha DIRA ya Taifa ya Maendeleo 2050.”
Awali akizungumza katika hafla hiyo, Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, alisema kaulimbiu ya mwaka huu inaonesha dhamira ya Serikali ya kuhakikisha DIRA ya Taifa ya Maendeleo 2050 haitabaki kuwa maono ya muda mrefu, bali inageuzwa kuwa matokeo yanayopimika kupitia utendaji wa Taasisi za Umma.

“Hatutaifikia Tanzania tunayoitamani kwa kutegemea sera pekee. Tunahitaji taasisi zenye viongozi wanaoweza kutafsiri maono ya Taifa kuwa matokeo yanayopimika katika kila sekta,” alisema.
Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Uwekezaji, Dk. Fred Msemwa, alisema Watendaji Wakuu wana wajibu wa kuhakikisha taasisi wanazoongoza zinakuwa chachu ya kuvutia uwekezaji, kuongeza ushindani wa uchumi na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Alisisitiza kuwa uongozi wenye maono, unaozingatia uwajibikaji na matumizi bora ya rasilimali za umma ni nguzo muhimu katika kufanikisha utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na kuharakisha maendeleo endelevu ya nchi.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais – UTUMISHI, Bw. Juma Mkomi, alisema mafunzo hayo ya siku nne ni sehemu ya utekelezaji wa sera za maendeleo ya rasilimali watu na uongozi katika Utumishi wa Umma, yakilenga kuwawezesha Watendaji Wakuu kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi.

Alisema matarajio ya Serikali ni kwamba maarifa na ujuzi watakaoupata washiriki kupitia mafunzo hayo yataakisiwa katika utendaji wao wa kila siku, hivyo kuimarisha ufanisi wa taasisi wanazoongoza na kuchangia kwa kiwango kikubwa kufanikisha utekelezaji wa Dira 2050.

“Matarajio yetu ni kuwa maarifa na ujuzi mtakaoupata kupitia mafunzo haya vitaonekana katika utendaji wenu wa kila siku na hatimaye kuchangia kwa kiwango kikubwa kufanikisha utekelezaji wa Dira 2050,” alisisitiza Bw. Mkomi.

Akihitimisha, aliwataka washiriki kuwasilisha mapendekezo kuhusu mahitaji ya rasilimali watu yatakayowezesha taasisi wanazoongoza kuwa chachu ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Kwa mujibu wa Msajili wa Hazina, ndiyo sababu Ofisi ya Msajili wa Hazina, kwa kushirikiana na Taasisi ya UONGOZI, imeendelea kuwekeza katika maendeleo ya uongozi kupitia mafunzo elekezi kwa Watendaji Wakuu wa Taasisi, Mashirika ya Umma na Wakala za Serikali.

Alisema tangu programu hiyo ilipoanzishwa mwaka 2024, zaidi ya Watendaji Wakuu 187 wamepatiwa mafunzo hayo, huku viongozi wapatao 57 wakishiriki katika awamu ya mwaka huu.

Bw. Mchechu alisema mafunzo hayo yanawajengea viongozi uelewa wa matarajio ya Serikali, utawala bora, uwajibikaji, usimamizi wa uwekezaji wa umma, matumizi bora ya rasilimali na uongozi unaozingatia matokeo.

Alisema uwekezaji huo katika maendeleo ya viongozi tayari umeanza kuleta matokeo chanya, ambapo makusanyo ya gawio na michango yameongezeka kutoka Sh637 bilioni mwaka wa fedha 2020/21 hadi Sh1.327 trilioni mwaka 2025/26, sawa na ongezeko la asilimia 108.

“Matokeo haya yanaonesha kuwa uwekezaji katika uongozi ni uwekezaji katika uchumi wa Taifa. Kadiri tunavyojenga viongozi wenye uwezo, ndivyo tunavyojenga taasisi zenye tija na kuongeza mchango wake katika mapato ya Serikali,” alisema.

Alisema katika kipindi cha utekelezaji wa DIRA 2050, Ofisi ya Msajili wa Hazina imeainisha maeneo matano ya kimkakati yatakayoongoza mageuzi ya Taasisi za Umma.

Maeneo hayo ni kuimarisha utawala bora, kuendeleza uongozi na rasilimali watu, kuimarisha usimamizi wa utendaji unaotegemea viashiria na ushahidi, kuwezesha upatikanaji wa rasilimali kupitia ubia kati ya sekta ya umma na binafsi (PPP), masoko ya mitaji na mifuko ya uwekezaji, pamoja na kuongeza tija, faida na thamani ya uwekezaji wa Serikali.

Aliongeza kuwa mafanikio ya maeneo hayo yanategemea pia ushirikiano wa karibu kati ya Taasisi za Umma na sekta binafsi, ili kuongeza uwekezaji, matumizi ya teknolojia, ubunifu, ushindani wa uchumi na ajira.

Naye Bw. Kadari Singo, Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Uongozi, alisema kuwa mafanikio ya utekelezaji wa Dira 2050 yatategemea kwa kiasi kikubwa uwepo wa mfumo imara wa uongozi.

Alisema ni muhimu kujenga mifumo ya kutambua na kuendeleza vipaji vya uongozi, kuhakikisha viongozi wanawekwa katika nafasi zinazolingana na uwezo wao, kuweka mipaka ya wazi ya mamlaka na majukumu yao, pamoja na kuimarisha uwajibikaji katika ngazi zote za uongozi.

"Masuala haya yanapaswa kupewa kipaumbele na kuzingatiwa kikamilifu katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050," alisema.

Katika mafunzo hayo ya siku nne, washiriki watapata mada kuhusu afya na ustawi wa viongozi, kufungamanisha mipango ya taasisi na DIRA 2050, uongozi wa kimkakati, usimamizi wa migogoro, usimamizi wa uwekezaji wa Serikali, utawala bora, usimamizi wa vihatarishi, ESG, fedha, ukaguzi pamoja na zoezi la kuandaa ahadi binafsi za utekelezaji wa DIRA 2050.

Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO ALHAMISI JULAI 22,2026



Magazeti

































Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger