Saturday, 1 August 2026

WAZIRI MKUU AZINDUA BOTI MBILI ZA DORIA NA UOKOZI

 


*Atoa siku 14 Kituo cha Kitaifa cha Oparesheni kianze kufanya kazi

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba ametoa siku 14 kwa wizara na taasisi zinazohusika na Kituo cha Kitaifa cha pamoja cha Oparesheni zipeleke wawakilishi ili kianze kufanya kazi mara moja.

Dkt. Mwigulu ametoa wito huo leo (Ijumaa, Julai 31, 2026) wakati akizungumza na washiriki wa hafla ya makabidhiano na uzinduzi wa boti mbili za doria aina ya PB Sailfish 02 na PB Sailfish 03 iliyofanyika bandarini, jijini Dar es Salaam. Boti hizo zimenunuliwa kwa thamani ya dola za Marekani milioni 1.6.

"Wizara na taasisi zote zinazohusika na utekelezaji wa majukumu katika Kituo cha Kitaifa cha pamoja cha Oparesheni zipeleke wawakilishi wote wanaohitajika ndani ya siku 14 kuanzia leo. Kituo hiki kianze kazi mara moja ili kuleta tija inayokusudiwa," amesema Waziri Mkuu.

Amezitaka Wizara za Muungano zinazohusika na suala hilo zishirikiane ili kuziba chochoro zote ambazo zingetumiwa na wahalifu katika eneo hili tunalolilenga na hasa katika mipaka ya mwambao wa bahari.

Ili kuhakikisha boti hizo zinafanya kazi kama inavyotarajiwa, Waziri Mkuu ameziagiza wizara na taasisi zote za umma zinazohusika katika matumizi ya boti hizi za doria zitenge fedha kwa ajili ya kazi za boti hizi.

"Ninasisitiza suala la kutenga bajeti ili kazi za doria zisikwamishwe na ukosefu wa bajeti.  Nimekuwa nikikutana na kesi kama hizo mikoani ambapo Mheshimiwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan alinunua ambulance za kisasa na nyingine zina ICU lakini zinashindwa kuhudumia wagonjwa kwa wakati kwa kukosa mafuta. Hili linakinzana na dhamira njema ya Mheshimiwa Rais ya kutaka kuokoa maisha ya Watanzania pindi wanahitaji huduma hizo," amefafanua.

Akielezea umuhimu wa boti hizo za doria, Waziri Mkuu amesema makabidhiano ya boti hizo ni tukio muhimu kiuchumi kwa sababu zinaenda kulinda mazao yatokanayo na uchumi wa bluu. Amesema uhitaji wa boti hizo umekuwa ni kilio cha muda mrefu tangu yeye akiwa Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi.

Amesema upatikanaji wa boti hizo mbili, utaimarisha ulinzi hasa ikizingatiwa kwamba Tanzania ni lango la nchi nyingi zikiwemo za Afrika Mashariki na za SADC lakini usalama utakaokuwepo unahusu Tanzania na wananchi wa hizo nchi jirani. "Wananchi kutoka nchi hizo watakuwa na uhakika wa usalama watakapotumia lango la bandari ya Dar es Salaam," amesisitiza.

Mapema, akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na washiriki wa hafla hiyo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Prof. Palamagamba Kabudi alisema ununuzi wa boti mbili za doria aina ya PB Sailfish 02 na PB Sailfish 03 ulifanyika baada ya kukamilika kwa taratibu zote za manunuzi ambapo mkataba wa ununuzi ulisainiwa Julai 29, 2025 kati ya Chuo cha Mipango na Maendeleo Vijijini na Kampuni ya Yamaha Motors Co. Ltd.

“Ujenzi wa boti hizo ulifanyika nchini Japan kwa kuzingatia vipimo na viwango vya kimataifa vilivyokubaliwa na wataalamu wa Serikali. Hadi kukamilika kwake, ujumbe wa wataalamu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, TASAC, UNDP na Chuo cha Mipango ulifanya ziara za ukaguzi ili kujiridhisha na ubora wa kazi iliyotekelezwa,” alisema.

Naye, Balozi wa Japan nchini Tanzania, Mikami Yoichi alisema kijiografia Tanzania na Japan ziko mbali lakini zinaunganishwa na bahari za Hindi na Pasifiki na kwamba uwepo wa usalama kwenye mipaka ya baharini, kuwahakikishia wananchi wake usalama wa maisha yao.

Alisema ana imani kwamba Serikali ya Tanzania itahakikisha boti hizo zinatumika kwa miaka mingi kwa faida ya vizazi vijavyo.

Share:

Friday, 31 July 2026

WAKALA WA VIPIMO WAENDELEA KUTOA ELIMU YA MATUMIZI YA VIPIMO SAHIHI MKOANI NJOMBE


Njombe, Julai 31, 2026
 
Wakala wa Vipimo (WMA) wameendelea na kampeni ya utoaji elimu kuhusu matumizi ya vipimo sahihi kwa wafanyabiashara, wazalishaji na wadau mbalimbali wa biashara mkoani Njombe, ikiwa ni sehemu ya kuhakikisha biashara zinafanyika kwa uwazi, usawa na kwa kuzingatia sheria za vipimo.

Katika mwendelezo wa kampeni hiyo, leo Julai 31, 2026, timu ya WMA imefanya ziara katika maeneo mbalimbali ya shughuli za kiuchumi ikiwemo masoko, viwanda vya mbao, eneo la madalali wa viazi maarufu kama Chaugingi, pamoja na kiwanda cha kuchakata parachichi. Katika maeneo hayo, elimu ilitolewa kuhusu umuhimu wa kutumia vipimo sahihi ili kuhakikisha biashara inafanyika kwa usahihi na haki.

Wananchi na wafanyabiashara walipata fursa ya kufahamu kuwa matumizi ya vipimo sahihi huchangia kulinda maslahi ya mlaji na muuzaji, huongeza uaminifu katika biashara, hupunguza migogoro ya kibiashara na kuimarisha ushindani wa haki sokoni.

 Zoezi hilo liliongozwa na Kaimu Meneja wa Wakala wa Vipimo Mkoa wa Njombe, Bw. Shabani Ikingu, ambaye alisisitiza umuhimu wa kuendelea kuwafikia wadau wa biashara kwa elimu ili kuongeza uelewa kuhusu matumizi sahihi ya vipimo na wajibu wa kila mfanyabiashara kuzingatia matakwa ya sheria. Alibainisha kuwa utoaji wa elimu ni nyenzo muhimu katika kujenga utamaduni wa biashara unaozingatia uwazi, uadilifu na kulinda maslahi ya pande zote mbili katika biashara.

Hata hivyo  WMA imepanga kufanya semina maalumu kwa waheshimiwa madiwani, wakulima na wajasiriamali katika ukumbi wa Halmashauri ya Mji wa Njombe tarehe 2 Agosti 2026.

Semina hiyo inalenga kuongeza uelewa kuhusu sheria za vipimo, kuimarisha ushirikiano kati ya WMA, viongozi wa serikali za mitaa na wadau wa biashara, pia kuhamasisha matumizi ya vipimo sahihi ili kujenga mazingira ya biashara yenye haki, ushindani usawa na yanayomlinda mlaji pamoja na mfanyabiashara.

WMA itaendelea kufikisha elimu hii katika maeneo mbalimbali nchini ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa dhamira yake ya kuhakikisha vipimo vinavyotumika katika biashara vinakuwa sahihi kwa maendeleo ya biashara yenye uaminifu na ustawi wa uchumi.

#Vipimo Sahihi, Haki kwa Mlaji na Mfanyabiashara.







Share:

Thursday, 30 July 2026

RC MTAKA AIPONGEZA WMA KUENDELEA KUTOA ELIMU YA VIPIMO KWA WAKULIMA NA WAFANYABIASHARA

Njombe, Julai 30, 2026

Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Anthony Mtaka, ameipongeza Wakala wa Vipimo (WMA) kwa kuendesha kampeni ya kutoa elimu kuhusu matumizi sahihi ya vipimo kwa wakulima na wafanyabiashara wa mazao. 

Amesema kampeni hiyo itaimarisha biashara yenye haki, uwazi na uzingatiaji wa Sheria ya Vipimo, huku ikipunguza migogoro inayotokana na uelewa mdogo wa matumizi ya vipimo.

Akizungumza ofisini kwake baada ya kupokea ujumbe wa WMA, Mtaka amesema elimu hiyo itasaidia kuondoa mkanganyiko unaojitokeza katika biashara ya mazao, hususani kuhusu matumizi ya lumbesa.

Alieleza kuwa baadhi ya wafanyabiashara wamekuwa wakikamatwa kwa madai ya kubeba lumbesa kutokana na kutofahamu maana yake halisi. Alifafanua kuwa kujaza mzigo na kuweka kishungi juu yake hakumaanishi kuwa ni lumbesa.

Aidha, amesema mzigo hutambulika kama lumbesa pale unapokuwa na uzito unaozidi kilo 100 hadi kilo 105. Amesema uelewa huu utawasaidia wafanyabiashara na wakulima kuzingatia sheria, kuepuka migogoro na kuongeza uaminifu katika masoko.

Awali, Kaimu Meneja wa WMA Mkoa wa Njombe, Bw. Shabani Ikingu, akiwa na wataalamu kutoka Makao Makuu ya WMA, walimtembelea Mkuu wa Mkoa kwa lengo la kujitambulisha na kueleza dhamira ya kampeni hiyo.

WMA wanaendelea kutembelea wakulima na wafanyabiashara wa mazao, hususani parachichi na viazi, kuwajengea uelewa kuhusu matumizi sahihi ya vipimo na umuhimu wa kuzingatia Sheria ya Vipimo.

Katika kuendeleza kampeni hiyo, WMA imepanga kutoa semina maalumu kwa madiwani na wajasiriamali wa Halmashauri ya Mji wa Njombe tarehe 2 Agosti 2026. Semina hiyo inalenga kuongeza uelewa, kuimarisha ushirikiano kati ya WMA, viongozi na wadau wa biashara, pamoja na kujenga mazingira ya biashara yenye haki na ushindani wa usawa.

WMA inaendelea kusisitiza kuwa elimu ndiyo msingi wa matumizi sahihi ya vipimo na utekelezaji wa Sheria ya Vipimo, hatua itakayochochea ukuaji wa biashara na kulinda maslahi ya wakulima, wafanyabiashara na watumiaji.

#Vipimo Sahihi, Biashara ya Haki; Elimu Kwanza, Maendeleo Endelevu kwa Wote.
Share:

EWURA KANDA YA KASKAZINI YAWAJENGEA UWEZO MAAFISA HUDUMA KWA WATEJA NA MAHSUSI


Babati, Manyara

30 Julai 2026 – Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) Kanda ya Kaskazini imeendesha semina ya kuwajengea uwezo Maafisa wa Huduma kwa Wateja, Mahusiano na Sheria kutoka TANESCO na Mamlaka za Majisafi na Usafi wa Mazingira za Kanda ya Kaskazini kuhusu huduma kwa wateja na uzingatiaji wa matakwa ya kisheria.

Akifungua semina hiyo katika Hoteli ya White Rose, Babati, Meneja wa EWURA Kanda ya Kaskazini, Bw. George Mhina, aliwasisitiza washiriki kuyafahamu vyema majukumu yao ili waweze kutoa majibu sahihi, ya wakati na yanayozingatia sheria, hivyo kuboresha huduma kwa wateja.

Kwa niaba ya washiriki, Bi. Devotha Mayala kutoka Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira Tanga na Bw. Samwel Mandari kutoka TANESCO waliishukuru EWURA kwa mafunzo hayo, wakieleza kuwa yamewaongezea uelewa na uwezo wa kuwahudumia wateja kwa weledi zaidi.

Semina hiyo ni sehemu ya juhudi za EWURA za kuimarisha uwezo wa watoa huduma na kulinda haki za watumiaji wa huduma za nishati na maji kupitia Udhibiti wa Haki kwa Matokeo Chanya.







Share:

TADB YAFIKIA HATUA MPYA YA UKUAJI: MTAJI WAFIKIA SHILINGI BILIONI 452.16



Na Dotto Kwilasa, Dodoma

Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania, TADB, imeingia katika awamu mpya ya ukuaji baada ya mtaji wake kuongezeka kwa kiasi kikubwa kutoka Shilingi bilioni 60 hadi kufikia Shilingi bilioni 452.16.

Ongezeko hilo linaledwa na kuongezeka kwa uwekezaji wa Serikali ya Awamu ya Sita katika sekta ya fedha za kilimo. Kwa mujibu wa uongozi wa benki hiyo, mtaji mpya umeipa TADB nguvu zaidi ya kutoa mikopo na kufadhili miradi inayolenga kubadilisha kilimo cha asili na kuwa kilimo cha kibiashara.

Mkurugenzi Mwendeshaji wa TADB, Frank Nyabundege, amesema ongezeko la mtaji limekuja wakati sahihi ambapo nchi inahitaji kuongeza uzalishaji wa chakula na ajira kupitia kilimo.

Amesema asilimia 73.6 ya jumla ya mikopo yote iliyotolewa na benki hiyo tangu kuanzishwa kwake, imetolewa katika kipindi cha miaka mitatu kati ya 2022 na 2025. Hii inaonyesha kasi ya utoaji wa huduma za kifedha imeongezeka mara tatu.

“Kwa sasa tuna uwezo mkubwa zaidi wa kufikia wakulima wadogo, wafugaji na wavuvi katika mikoa yote. Pia tunaweza kuingia katika minyororo ya thamani kama usindikaji, uhifadhi na masoko,” amesema Nyabundege.

TADB imetangaza kuwa katika kipindi kijacho itaweka mkazo katika maeneo matano. Maeneo hayo ni pamoja na kuongeza upatikanaji wa mitaji yenye masharti nafuu, kuimarisha kilimo cha kibiashara, kukuza matumizi ya teknolojia shambani, kuwawezesha vijana na wanawake kiuchumi, na kusaidia miradi ya kuongeza thamani ya mazao.

Wataalamu wa uchumi wanasema hatua hii ni muhimu kwa kuwa sekta ya kilimo inachangia zaidi ya asilimia 26 ya Pato la Taifa na kuajiri zaidi ya asilimia 65 ya Watanzania. Kwa hiyo kuweka fedha zaidi katika benki maalumu ya kilimo ni njia ya moja kwa moja ya kukuza uchumi.

Benki hiyo pia imesema itashirikiana na taasisi za kifedha nyingine, makampuni ya bima na wadau wa teknolojia ya kilimo ili kuhakikisha mkulima anapata ufadhili kamili kuanzia pembejeo hadi soko.

Ongezeko hili la mtaji linakuja wakati Tanzania ikiijiandaa kwa Maonyesho ya Wakulima Nane Nane 2026, ambapo sekta ya kilimo inatarajiwa kuonyesha mafanikio mapya katika uzalishaji na uongezaji thamani.

Kwa wakulima wengi, taarifa hii inatoa matumaini mapya. Maana yake ni kwamba kupata mkopo wa kununua pembejeo, kununua matrekta au kujenga ghala kutakuwa rahisi zaidi kuliko miaka iliyopita.

TADB ilianzishwa na Serikali kwa lengo la kutoa ufadhili maalumu kwa sekta ya kilimo. Tangu kuanzishwa kwake imekuwa ikipitia mageuzi mbalimbali ili iweze kuwafikia wale wanaohitaji zaidi.

Kwa sasa, benki hiyo inasema mlango umefunguka zaidi. Na lengo ni moja: kuhakikisha kila shilingi inayowekezwa inarudi shambani na kubadilisha maisha ya mkulima.




Share:

ULINZI WAIMARISHWA MIPAKANI, SERIKALI YAZINDUA OFISI NA NYUMBA YA JESHI LA UHAMIAJI MPAKA NA MSUMBIJI

Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Brigedia Jenerali Ahmed Abbas Ahmed, ametoa wito kwa wananchi wanaoishi maeneo ya mipakani kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama kwa kutoa taarifa zinazohusu vitendo vya uvunjifu wa sheria za mipaka, viashiria vya uhalifu, na matukio mengine yanayoweza kuhatarisha usalama, kwa lengo la kulinda usalama wa taifa na maslahi mapana ya nchi.

Ametoa wito huo wakati wa hafla fupi ya uzinduzi wa Ofisi ya Uhamiaji Kituo cha Mkenda–Nakawale, kilichopo mpakani mwa Tanzania na Msumbiji, iliyojengwa kwa gharama ya shilingi milioni 240.8 fedha  kutoka Serikali Kuu  na nyumba ya mtumishi iliyogharimu kiasi cha shilingi 133.7 zilizofadhiliwa na Shirika la Kimataifa la Uhamiaji (IOM).

Akizungumza katika hafla hiyo, Brigedia Jenerali Ahmed amesema maendeleo ya taifa yanategemea uwepo wa usalama imara, amesema  kuwa ni wajibu wa kila mwananchi kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama ili kuhakikisha nchi inaendelea kuwa salama 

Naye Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Dkt. Franklin Rwezemula, akimwakilisha waziri wa mambo ya ndani  amesema Serikali inaendelea kutenga fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika vyombo vya ulinzi na usalama, ikiwemo Idara ya Uhamiaji, kwa lengo la kuboresha mazingira ya kazi, kuongeza ufanisi wa utendaji na kuimarisha usalama wa mipaka ya nchi

Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Peramiho, Dkt. Lazaro Komba, ameipongeza Serikali ya Awamu ya Sita kwa jitihada zake za kuwaletea wananchi maendeleo kupitia utekelezaji wa miradi mbalimbali, akibainisha kuwa katika mwaka wa fedha 2026/2027 Serikali imetenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa awamu ya kwanza wa barabara ya Likuyufusi–Mkenda yenye urefu wa kilomita 60 kwa kiwango cha lami.




Share:

RC SHINYANGA AFANYA ZIARA YA UKAGUZI MIRADI YA MAENDELEO KISHAPU

Na Sumai Salum – Kishapu
  • ARIDHISHWA NA HATUA YA MIRADI YA MAENDELEO KISHAPU

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita, Julai 29, 2026 amefanya ziara ya kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo wilayani Kishapu mkoani humo, ikiwa ni pamoja na mradi wa sekta za elimu, afya, maji, miundombinu ya barabara, miradi inayotekelezwa kwa ushirikiano na wadau wa maendeleo pamoja na unufaishaji wa mikopo ya asilimia 10 ya Halmashauri. 

Akiwa katika ziara hiyo, Mhita amesema maendeleo yanayoonekana ni matokeo ya amani, utulivu na demokrasia ya kiuchumi inayowavutia wadau wa maendeleo na wawekezaji kushirikiana na Serikali kuboresha maisha ya wananchi.


Mhita amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuwekeza katika sekta ya elimu kwa kujenga vyumba vya madarasa na kuboresha miundombinu ya shule ili kuhakikisha kila mtoto anapata haki ya elimu katika mazingira bora, ikiwa ni pamoja na kuongeza uwiano wa madarasa na matundu ya vyoo kulingana na idadi ya wanafunzi. Aidha, amepongeza vikundi vilivyonufaika na mikopo ya asilimia 10 ya Halmashauri, ikiwemo kikundi cha Wachapakazi kilichotumia mkopo huo kununua trekta kwa ajili ya kuongeza tija katika shughuli za uzalishaji.

Hata hivyo mmoja wa wananchi kutokea Kata ya Mwataga Patricia Nkana ameipongeza Serikali kwa kuendelea kuboresha huduma za afya na upatikanaji wa maji safi na salama, akisema ujenzi na uboreshaji wa zahanati na upanuzi wa upatikanaji wa maji safi na salama umeongeza usalama wa akina mama wajawazito wakati wa kujifungua na kuinua ustawi wa wananchi kwa ujumla na kuchochea kuimarisha afya ya ndoa zao.
Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Mboni Mhita akizungumza wakati wa ziara yake ya kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo wilayani Kishapu ikiwa ni pamoja na mradi wa sekta za elimu, afya, maji, miundombinu ya barabara, miradi inayotekelezwa kwa ushirikiano na wadau wa maendeleo pamoja na unufaishaji wa mikopo ya asilimia 10 ya Halmashauri Julai 29, 2026
Katibu Tawala mkoani Shinyanga Cp. Salum Hamduni akiwa kwenye ziara ya Mkuu wa Mkoa huo Mhe. Mboni Mhita Wilayani Kishapu Julai 29, 2026
Mkuu wa Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga Mhe Peter Masindi akizungumza wakati wa ziara ya Mkuu wa Mkoa huo Mhe. Mboni Mhita Wilayani humo ya kukagua miradi mbalimbali ikiwa ni pamoja na miradi ya sekta za elimu, afya, maji, miundombinu ya barabara, miradi inayotekelezwa kwa ushirikiano na wadau wa maendeleo pamoja na unufaishaji wa mikopo ya asilimia 10 ya Halmashauri Julai 29, 2026 Katibu Tawala wilayani Kishapu mkoani Shinyanga Fatma Mohamed akiwa kwenye ziara ya Mkuu wa Mkoa huo Mhe. Mboni Mhita Wilayani Kishapu Julai 29, 2026
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga Emmanuel Johnson
Mwananchi wa Kata ya Mwataga wilayani Kishapu mkoani Shinyanga Patricia Nkana akielezea namna wanavyonufaika na uboreshaji wa miundombinu hasa ya Elimu, Afya, Maji na Nishati ya Umeme hadi Vijijini Julai 29,2026 wakati wa ziara ya Mkuu wa Mkoa huo Mhe Mboni Mhita wilayani humo

Tazama picha za matukio mbalimbali👇👇👇























































































































































































Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger