Wednesday, 22 July 2026
Monday, 20 July 2026
RAIS SAMIA: AMANI NA USALAMA NI MSINGI MKUU WA MAENDELEO
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema amani na usalama ni msingi mkuu wa maendeleo ya Taifa, akiwataka wananchi kuendelea kulinda tunu hizo ili kuhakikisha nchi inaendelea kuwa na mazingira bora ya ukuaji wa uchumi na ustawi wa jamii.
Rais Samia amesema hayo leo Jumatatu Julai 20, 2026 mkoani Kigoma wakati akizungumza mara baada ya kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR) kipande cha Tabora hadi Kigoma na uzinduzi wa meli nne za mizigo katika Bandari ya Kigoma.
Amesema Serikali itaendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo miundombinu ya usafiri na usafirishaji, lakini mafanikio ya miradi hiyo yanategemea uwepo wa amani na usalama nchini huku akisisitiza kuwa suala hilo ni kipaumbele cha kwanza na halipaswi kupuuzwa kwani maendeleo hayatashamiri endapo amani itavurugwa.
Amewataka wananchi wa Kigoma na Watanzania kwa ujumla kuwa na utamaduni wa kuweka usalama mbele, akisisitiza kuwa maendeleo yanahitaji mazingira yenye utulivu na mshikamano.
Rais Samia pia amewataka wananchi kutokubali kushawishiwa au kutumiwa na watu wenye nia ya kuvuruga amani ya nchi, akieleza kuwa kulinda usalama ni jukumu la kila Mtanzania na kuwataka wote kuwa macho huku wakiepuka kuwa wasaliti na maadui wa nchi yao.
Ameongeza kuwa ulinzi wa amani na usalama utaendelea kuiwezesha Tanzania kutekeleza miradi mikubwa ya maendeleo, kuvutia uwekezaji na kukuza uchumi kwa manufaa ya wananchi wa sasa na vizazi vijavyo.
WAZIRI SANGU: UANAGENZI UTAWATOA VIJANA KIMAISHA
Serikali ya Awamu ya Sita imeendelea kuimarisha programu ya mafunzo ya uanagenzi kama mkakati madhubuti wa kuwajengea vijana stadi za kazi zitakazowawezesha kujiajiri na kuajiri wengine, hatua inayolenga kuongeza fursa za ajira na kukuza uchumi wa Taifa.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mheshimiwa Deus Sangu, amesema hayo Julai 18, 2026, wakati alipokagua utekelezaji wa mafunzo hayo katika Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST), Kampasi ya Rukwa.
Uwekezaji huu unaonesha dhamira ya Serikali ya kuwawezesha vijana kupata ujuzi unaokidhi soko la ajira, huku Waziri Sangu akiahidi kuwa kuanzia mwaka 2026, wahitimu wataanza kupatiwa vifaa vya kuanzia kazi ili kuwawezesha kujiajiri mara moja.
Akizungumzia utekelezaji wa programu hiyo mkoani Rukwa, Mkurugenzi wa Ajira na Ukuzaji Ujuzi, Alana Nchimbi, alieleza kuwa mkoa una vyuo viwili vinavyoshiriki, ambavyo ni MUST Kampasi ya Rukwa yenye wanagenzi 154 na Chuo cha Kilimo na Mifugo Laela chenye wanagenzi 120.
Mkuu wa Kampasi ya MUST Rukwa, Prof. Asheri Mwidege, aliongeza kuwa mafunzo hayo yamewawezesha wanagenzi kupata umahiri wa vitendo, ikiwemo ujenzi wa mageti na ukarabati wa hosteli ndani ya chuo, huku akishukuru Serikali kwa kugharamia bima ya afya na nauli kwa asilimia 100, hatua iliyoongeza ari ya vijana.
Mkuu wa Wilaya ya Sumbawanga, Mheshimiwa Nyakia Ally Chirukie, alipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu kwa uratibu huo ambao umekuwa chachu ya uwezeshaji kwa vijana wa wilaya hiyo.
Wanagenzi wenyewe wameeleza kufurahishwa na mafunzo hayo ambayo yamekuwa suluhisho la changamoto ya ukosefu wa ajira. Digna Sebastian John, mhitimu wa chuo kikuu aliyebadili mwelekeo na kuanza kujifunza ufundi bomba, alibainisha kuwa ujuzi huo unampa uhakika wa kujiajiri.
Kwa upande wake, Ismail William Mbogo, ambaye awali alikuwa akijishughulikia na kilimo cha mpunga katika Bonde la Ziwa Rukwa, alitoa ushuhuda kuwa ndani ya miezi sita pekee amejenga uwezo mkubwa wa ufundi unaomfanya sasa kupata ajira za muda katika vijiji vinavyozunguka chuo hicho.
Ujumbe huu unadhihirisha kuwa programu ya uanagenzi si tu inatoa ujuzi, bali inabadilisha maisha ya vijana kutoka kwenye shughuli za kawaida na kuwaweka kwenye mkondo wa wataalamu wanaochangia moja kwa moja katika maendeleo ya jamii na uchumi wa nchi.

















































