Friday, 19 December 2025

WAZIRI MCHENGERWA AUONGOZA UJUMBE WA TANZANIA KWENYE UZINDUZI WA MKUTANO WA PILI WA DUNIA WA TIBA ASILI


Na John Mapepele, New Delhi

Waziri wa Afya, Mhe. Mohamed Omary Mchengerwa leo ameuongoza ujumbe wa Serikali ya Tanzania katika uzinduzi wa Mkutano wa pili wa dunia wa Tiba Asili unaoratibiwa na Shirika la Afya Duniani (WHO) kwenye ukumbi wa kimataifa wa Bharat Mandapam jijini New Delhi India.

Mhe. Mchengerwa amepongeza juhudi zinazofanywa na WHO za kuileta dunia pamoja ili kujadili suala la Tiba Asili na kupata ufumbuzi katika masuala kadhaa ikiwa ni pamoja na utawala na udhibiti wa tiba asili, utafiti na ushahidi wa kisayansi, ujumuishaji wa tiba asili katika mifumo ya afya, matumizi endelevu ya raslimali za kiasili na uendelezaji wa raslimali watu kwenye eneo la Tiba Asili.

Mkutano huo umefunguliwa rasmi na Mheshimiwa Prataprao Ganpatrao Jadhav, Waziri wa Nchi (Independent Charge), Wizara ya Tiba Asili (AYUSH), na Waziri wa Nchi, Wizara ya Afya na Ustawi wa Familia ya Serikali ya India, mbele ya Mheshimiwa Jagat Prakash Nadda, Waziri wa Afya na Ustawi wa Familia wa Serikali ya India. Hafla hiyo imewakutanisha Mawaziri, watunga sera wakuu, na wadau wa sekta ya afya kutoka mataifa mbalimbali duniani.

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Dkt. Tedros Adhanom Ghebreyesus akitoa hotuba yake kwa njia ya video kwenye ufunguzi huo amewasihi wajumbe wa mkutano huo kujadili kwa kina mada mbalimbali ili kubadilishana uzoefu na kwamba kwa sasa Tiba Asili bado itaendelea kuwa na mchango mkubwa kwa wanadamu kwa kuzingatia kuwa tiba asili ni sehemu ya tamaduni za watu katika mataifa yao.

Pembezoni mwa mkutano huo, Tanzania inatarajia kusaini Hati mbili za Makubaliano (MoU) na Serikali ya India kuhusu ushirikiano katika sekta ya afya na tiba asilia (Ayurveda), hatua itakayosaidia kuimarisha ushirikiano wa kitaasisi, kuongeza uwezo wa rasilimali watu, na kuimarisha matumizi salama ya tiba asilia nchini.


Kusainiwa kwa hati hizi mbili za makubaliano ni hatua muhimu kwa Tanzania, kwani kutaimarisha ushirikiano wa kitaasisi na India katika maeneo ya kipaumbele ya sekta ya afya, kuongeza uwezo wa rasilimali watu wa sekta ya afya, kuimarisha udhibiti na matumizi salama ya tiba asilia, pamoja na kuchangia jitihada za Serikali katika kuimarisha mifumo ya huduma za afya na kufikia Bima ya Afya kwa Wote.

Ushiriki wa Tanzania katika mkutano huu unaakisi dhamira ya Serikali kupitia Wizara ya Afya katika kukuza tiba asilia salama, yenye ushahidi wa kisayansi na inayosimamiwa kwa misingi madhubuti ya udhibiti, sambamba na kuendeleza ushirikiano wa kimataifa kwa maendeleo endelevu ya afya kwa watu wote.

Mkutano huo wa siku tatu unatarajiwa kufungwa na Desemba 19, 2025 na Waziri Mkuu wa India, Mheshimiwa Narendra Modi, jambo linaloonesha uzito na umuhimu mkubwa wa mkutano huo katika ngazi ya juu ya kisera.





Share:

RC TANGA AMTAKA MKANDARASI KUFANYA KAZI USIKU NA MCHANA MRADI WA UJENZI BWAWA LA UMWAGILIAJI MKOMAZI





Na Oscar Assenga, KOROGWE.

MKUU wa Mkoa wa Tanga Balozi,Dkt Batilda Burian amemtaka Mkandarasi anayesimamia mradi wa Ujenzi wa Bwawa la Umwagiliaji la Mkomazi wilayani Korogwe unao gharimu kiasi cha Bilioni 18.6 kuongeza nguvu kazi ya kutosha ikiwemo kufanya kazi usiku na mchana ili kuhakikisha unakamilika kwa wakati uliopangwa.

Bwawa la Umwagiliaji la Mkomazi linajengwa katika Kijiji cha Manga Mtindilo wilayani ya Korogwe ambalo linatarajiwa kuwa mkombozi mkubwa kwa Kilimo cha Umwagiliaji mkoani Tanga na mradi huo unatekelezwa na Mkandarasi China Sichuan International Cooperation Co.LTD.

Maelekezo ya Mkuu huyo wa Mkoa aliyatoa wakati alipofanya ziara ya kutembelea mradi huo akiwa na kamati ya ulinzi na usalama kwa lengo la kujionea hali ya utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa Bwawa hilo kuhakikisha mradi huo wa kimkakati unatekelezwa kwa viwango na kwa kasi inayostahili.

Hatua hiyo ilitokana na kutokuridhishwa na kasi ya ujenzi wa mradi wa bwawa hilo kutokana na namna unavyotekelezwa hasa kwa kazi ambazo zingepaswa kutekelezwa kwa haraka zaidi .

Aidha alisema kwamba wamekuja kutembelea Bwawa hili ambalo ni muhimu kutokana na kwamba mkoa wa Tanga unatarajiakuwa kitovu cha uzalishaji wa chakula kwa mikoa ya Kilimanjaro,Manyara na Arusha kupitia mradi huo mkubwa pindi utakapokamilika

Mkuu huyo wa mkoa alimshukuru Rais Dkt Samia Suluhu kwa maono yake na kuamua kutenga zaidi ya Bilioni 18.2 kwa ajili ya mradi huo mkubwa na kuongeza tena Milioni 400 hivyo kufikia Bilioni 18.6 ikiwa ni dhamira ya kweli kuhakikisha kilimo cha umwagliaji kinakuwa nguvu ya usalama wa chakula.

Alisema kwamba mradi huo ni muhimu kutokana na kwamba mabadiliko ya tabia ya nchi mvua ambazo zilitarajiwa kunyesha mkoa wa Tanga hazikunyesha kwa wakati wala kwa kiwango kilichokusudiwa hivyo hiyo ni ishara kwamba hawawezi kutegemea kilimo cha mvua pekee ndio maana wanasisitiza kilimo cha uhakika ni cha umwagiliaji.

Awali akizungumza Mhandisi kutoka kwa Mkandarasi Andrew Magungu alisema kwamba wamepokea maelekezo ya kiongozi huyo na kuhaidi kuyafanyia kazi ili kuhakikisha malengo ya mradi huo yaliyowekwa ya kukamilisha mradi huo kwa wakati.
Naye kwa upande wake Meneja wa Mradi huo ,Mhandisi Leonard Someke maendeleo ya kazi mpaka sasa ipo asilimia 84.9 na mradi huo utakapokamilika unatarajiwa kuwanufaisha zaidi ya wananchi 20,000 kutoka Kata saba ambapo ni jumla ya vijiji 28 kutoka wilaya ya Korogwe kwa kuwawezesha kulima mara mbili hadi tatu kwa mwaka tofauti na awali .


Eneo ambalo litakapomwagiliwa litakuwa ni Hekta 9000 sawa na Ekari 22,500 huku faida za mradi huo zikielezw kupunguza athari ya mafuriko yanayokumba mashamba ya wakulima .
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO IJUMAA DESEMBA 19,2025


Magazeti ya leo
































Share:

Thursday, 18 December 2025

WAZIRI DKT. GWAJIMA - IBUENI CHANGAMOTO MCHAKATO WA KUOMBA MIKOPO YA SERIKALI ‎



‎Na Saidi Saidi WMJJWM - Dar Es Salaam

‎Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima, amewataka wanawake katika vikundi mbalimbali kueleza changamoto walizokumbana nazo katika mchakato wa kupata mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na Halmashauri, ili changamoto hizo ziweze kupatiwa ufumbuzi.

Dkt. Gwajima ametoa wito huo Desemba 17, 2025 wilayani Ubungo, jijini Dar Es Salaam, wakati wa ziara yake ya kutembelea na kufuatilia utekelezaji wa programu za uwezeshaji wanawake kiuchumi.

‎Katika ziara hiyo, Waziri Dkt. Gwajima ametembelea vikundi vya wanawake wanufaika wa mikopo ya asilimia 10 inayotolewa kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, pamoja na Majukwaa ya Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi.

Aidha, amefanya kikao na Jukwaa la Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi la Wilaya hiyo, ambapo amebaini kuwa baadhi ya wanawake wanakumbwa na changamoto mbalimbali, ikiwemo ukosefu wa ujuzi wa kuandaa maandiko ya miradi, kushindwa kutimiza baadhi ya vigezo kama vile kutokuwa na Kitambulisho cha Taifa (NIDA), pamoja na changamoto nyingine zinazowafanya washindwe kunufaika na mikopo hiyo.

Waziri‎ Dkt. Gwajima amesema kuwa Serikali, imeweka mikakati madhubuti ya kuwasaidia wanawake kukabiliana na changamoto wanazokutana nazo katika upatikanaji wa mikopo ya Serikali, ikiwa ni pamoja na kuimarisha utoaji wa elimu ya ujasiriamali na usimamizi wa miradi, kuwawezesha wanawake kujikwamua kiuchumi.

‎Amesisitiza kwamba, Serikali ina dhamira ya dhati ya kuhakikisha wanawake wengi zaidi wanashiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji mali kupitia programu za uwezeshaji kiuchumi.

Waziri Dkt. Gwajima ameongeza kuwa, ufuatiliaji wa karibu wa vikundi na majukwaa ya wanawake utasaidia kupata taarifa sahihi kuhusu mahitaji halisi ya wanawake na kuboresha mifumo ya utoaji wa mikopo ili iwe rafiki, jumuishi na inayowafikia wanawake wengi zaidi.


‎Naye Diwani wa Kata ya Mbezi, Mhe. Pius Nyantoli, amesema kuwa kupitia uongozi wake ataendelea kufuatilia changamoto zinazowakabili wanawake katika eneo lake, ili kushirikiana na mamlaka husika kuhakikisha wanawake wanapata fursa stahiki za mikopo na kunufaika na programu za uwezeshaji kiuchumi.

‎Wanawake wa Jukwaa walioshiriki katika kikao hicho wamemshukuru Waziri Dkt. Gwajima kwa kuwapa nafasi ya kusikilizwa na kueleza changamoto wanazokumbana nazo katika mchakato wa kupata mikopo ya Serikali.

Wamesema hatua hiyo imewapa matumaini mapya, na wameahidi kutoa ushirikiano kwa Serikali na viongozi husika ili kuhakikisha changamoto zilizobainishwa zinapatiwa ufumbuzi na wanawake wengi zaidi wanapata fursa za uwezeshaji wa kiuchumi.





Share:

WAZIRI NANAUKA ATOA MAAGIZO KWA MAAFISA MAENDELEO YA VIJANA NCHINI


-Ataka Maafisa hao kuwa na takwimu sahihi za vijana

-Kuunganisha vijana na programu na fursa za Ujuzi, Ajira na Uwezeshaji Kiuchumi

Na: Ofisi ya Rais, Maendeleo ya Vijana – Dodoma

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana, Mhe. Joel Nanauka ametoa maagizo manne (4) kwa Maafisa Maendeleo ya Vijana wa Mikoa na Halmashauri kwa lengo la kuboresha na kuimarisha ustawi wa vijana na Maendeleo yao nchini.

Aidha, Mhe. Nanauka amewataka maafisa hao, katika kutekeleza majukumu yao wahakikishe wanakuwa na takwimu sahihi za vijana waliopo katika maeneo yao na waweze kutambua changamoto zinazowakabili vijana na kutafuta ufumbuzi. Pili, kuwaunganisha vijana hao na programu na fursa zote za kitaifa zinazohusu ujuzi, ajira na uwezeshaji wa kiuchumi.

Vile vile, amewataka Maafisa Maendeleo ya Vijana kuimarisha ushirikiano na wadau waliopo katika Mikoa na halmashauri zenu ili kuleta matokeo ya haraka na endelevu kwa vijana pamoja na kuzingatia uwajibikaji, uadilifu na matumizi sahihi ya rasilimali zinazotolewa kwa ajili ya vijana.

Amesema hayo wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha maafisa Maendeleo ya vijana wa mikoa na halmashauri kilichofanyika ukumbi wa Hazina, leo Disemba 17, 2025, Jijini Dodoma.

Waziri Nanauka amesema kuwa, Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imechukua hatua za kimkakati za kuimarisha mifumo ya sera, sheria na utendaji kuhusu maendeleo ya vijana na hivyo kupelekea kuanzishwa Wizara yenye dhamana mahsusi ya Maendeleo ya Vijana chini ya Ofisi ya Rais.

Kwa upande mwengine, Waziri Nanauka ametoa rai kwa Maafisa Maendeleo ya vijana kuzingatia falsafa tatu (3) za wizara hiyo ambayo ni, Kasi ya kusikiliza na kutekeleza mawazo na ushauri wa vijana, Kuwafikia vijana walipo na kuwasikiliza na Kutumia teknolojia ili kwenda na kasi ya vijana.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO DESEMBA 18,2025

 Magazeti







Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger