Tuesday, 23 June 2026

SERIKALI YASISITIZA HAKI YA KUPANDA MADARAJA KWA WATUMISHI ,YATAMBUA VIPAJI VYA WENYE ULEMAVU



Na Dotto Kwilasa, Dodoma

Serikali imeagiza hatua za haraka zichukuliwe dhidi ya maafisa rasilimali watu wanaochelewesha watumishi wa umma kupanda madaraja licha ya kukidhi vigezo vinavyotakiwa, huku ikisisitiza uwajibikaji na haki katika usimamizi wa rasilimali watu serikalini.

Akizungumza wakati wa maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma jijini Dodoma, Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Profesa Riziki Shemdoe, alisema baadhi ya watumishi wamekuwa wakipata usumbufu mkubwa kufuatilia stahiki zao licha ya kutimiza masharti yote ya kupandishwa madaraja.

Amesema ni muhimu kwa maafisa rasilimali watu kutekeleza majukumu yao kwa wakati ili kuondoa malalamiko yasiyo ya lazima na kuongeza motisha kwa watumishi wa umma.

"Jaribuni kuvaa viatu vya watumishi hawa,Wapo wanaotoka maeneo ya mbali na kutumia muda na fedha nyingi kufuatilia stahiki zao hapa Dodoma ilhali wamekidhi masharti yote yanayotakiwa," amesema Prof. Shemdoe.

Kutokana na hali hiyo,ameagiza  kufanyika tathmini maalumu ya maafisa rasilimali watu waliosababisha ucheleweshaji wa madaraja katika mwaka wa fedha 2025/2026 ili hatua stahiki zichukuliwe.

Katika hatua nyingine,ameeleza kufurahishwa na mafanikio ya vijana wenye ulemavu wanaopata mafunzo ya ufundi stadi na kuibua vipaji vinavyoweza kuchangia maendeleo ya taifa.

Miongoni mwa waliovutia ni kijana Joseph ambaye ameonesha uwezo mkubwa katika usanifu wa majengo kwa kutumia mifumo ya kompyuta, jambo lililopelekea kuagizwa kutafutiwa ufadhili wa masomo pamoja na kuanza mchakato wa kupatiwa ajira ya kudumu serikalini.

Aidha, Serikali imeagiza kufanyika sensa ya mifumo yote ya TEHAMA inayotumika katika taasisi za umma ili kubaini kiwango cha matumizi yake na kuhakikisha mifumo hiyo inaunganishwa kwa lengo la kuongeza ufanisi, kupunguza urudufu na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Hatua hiyo ni sehemu ya mkakati mpana wa Serikali wa kuimarisha utawala bora, matumizi ya teknolojia na utoaji wa huduma bora kwa wananchi kupitia taasisi za umma.


Share:

MWENYEKITI MPYA WA BODI YA USHAURI ADEM AONGOZA KIKAO CHAKE CHA KWANZA


📍Bagamoyo, Tanzania

Mwenyekiti mpya wa Bodi ya Ushauri ya ADEM, Dkt. Hillary A. Dachi, amewasili rasmi chuoni hapo na kuongoza kikao chake cha kwanza tangu alipoteuliwa kushika nafasi hiyo, ambapo Bodi ilikutana kujadili masuala mbalimbali ya kimkakati yanayolenga kuimarisha utendaji wa taasisi na kuchangia maendeleo ya sekta ya elimu nchini.

Kikao hicho, ambacho ni Kikao cha 62 cha Bodi ya Ushauri ya ADEM, kilifanyika katika Kampasi ya Bagamoyo na kuhudhuriwa na wajumbe wa bodi pamoja na menejimenti ya taasisi wakiongozwa na Mtendaji Mkuu wa ADEM, Dkt. Maulid J. Maulid.

Akizungumza katika kikao hicho, Dkt. Dachi alieleza dhamira yake ya kushirikiana kwa karibu na wajumbe wa bodi pamoja na menejimenti ya ADEM ili kuhakikisha taasisi inaendelea kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi, ubunifu na weledi mkubwa katika kuandaa na kuendeleza viongozi wa elimu wenye uwezo wa kukabiliana na changamoto za wakati.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa ADEM, Dkt. Maulid J. Maulid, alimkaribisha rasmi Mwenyekiti huyo mpya na kumhakikishia ushirikiano wa karibu kutoka kwa menejimenti na watumishi wa taasisi katika kutekeleza maamuzi na maelekezo yatakayosaidia kuifikisha ADEM katika viwango vya juu zaidi vya utoaji huduma.

Katika kikao hicho, wajumbe wa bodi walipata fursa ya kujadili na kutoa maelekezo kuhusu masuala mbalimbali ya maendeleo ya taasisi, ikiwemo utekelezaji wa mipango ya kimkakati, ubora wa mafunzo, uendelevu wa programu za kitaaluma pamoja na fursa za kukuza mchango wa ADEM katika maendeleo ya sekta ya elimu na Taifa kwa ujumla.

Kikao cha 62 cha Bodi ya Ushauri ya ADEM kinaashiria mwanzo wa hatua mpya ya kuimarisha usimamizi na uongozi wa taasisi hiyo, huku kikidhihirisha dhamira ya viongozi wake kuendelea kuifanya ADEM kuwa kitovu cha ubora katika maendeleo ya uongozi na usimamizi wa elimu nchini Tanzania.

Share:

Monday, 22 June 2026

PROF. SHEMDOE AELEKEZA BILIONI 5.2 ZA MRADI WA LoCAL ZITUMIKE KWA MALENGO YALIYOKUSUDIWA


Na OWM - TAMISEMI, Dodoma

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amazielekeza Halmashauri za wilaya ya Mkinga, Mafia, Mpwapwa, Kondoa, Chamwino, Mtwara, Mtama na Manispaa ya Kigamboni kutumia Bilioni 5.2 za programu ya kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi (Local Climate Adaptive Facility-LoCAL) kwa malengo yaliyokusudiwa ili kuwanufaisha wananchi.

Prof. Shemdoe ametoa maelekezo hayo leo Juni 22, 2026 jijini Dodoma katika Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi ya Waziri Mkuu –TAMISEMI, mara baada ya kukabidhiwa hundi yenye thamani ya Bilioni 5.2 za kitanzania na Katibu Mtendaji wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo ya Mitaji (UNCDF) Bw. Pradeep Kurukulasuriya, ambalo linafadhili utelelezaji wa programu ya kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi (LoCAL).

“Katumieni fedha hizi kama zilivyoanishwa kwenye maelekezo ya mradi huu, kama ambavyo tumefanya vizuri katika utekelezaji wa awamu ya kwanza kwenye halmashauri za Chamwino, Kondoa na Mpwapwa,” amesisitiza Prof. Shemdoe.

Prof. Shemdoe ameeleza kuwa, utekelezaji mzuri wa awamu ya kwanza ya mradi wa LoCAL katika Halmashauri hizo umewezesha kupatikana kwa mradi mpya wa SCALE wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi ambao unaotekelezwa katika halmashauri 54 nchini.

Katika kuongeza ufanisi wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, Prof. Shemdoe ametoa wito kwa wadau mbalimbali wa maendeleo  kujitokeza ili kuunga mkono jitihada za Serikali za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, na kuongeza kuwa milango ya Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI ipo wazi kwa mdau yeyote mwenye nia ya kuwasaidia wananchi kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Prof. Shemdoe amefafanua kuwa, Diplomasia ya Uchumi ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ndio inayofungua milango ya wadau mbalimbali kuja kushirikiana na Serikali katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Mratibu wa Mradi wa LoCAL Wilaya ya Kondoa Bw. Laurence Robert Mogela amesema Halmashauri ya Kondoa imepokea dola za kimarekani 149,043 kwa ajili utekelezaji wa awamu ya pili ya mradi huo, utakaotekelezwa kwenye Kata ya Bumbuta kupitia kilimo cha kisasa kitakachoimarisha usalama wa chakula.

Kwa upande wake, Afisa Mazingira wa Wilaya ya Chamwino Bi. Elizabeth Solwa amesema wananchi wengi wa Wilaya ya Chamwino watanufaika na fedha za mradi wa LoCAL kwani wilaya itapokea milioni 500 kwa ajili ya kutekeleza awamu ya pili ya mradi huo katika kata mbili za Mtamalo na Mvumi Makulu.

Naye, Mratibu wa Mradi wa LoCAL Wilaya ya Mpwapwa Bw. Issa Abdallah Sepanja, amesema wilaya ya Mpwapwa imepokea Shilingi Milioni 491 kwa ajili ya kutekeleza awamu ya pili ya mradi wa LoCAL ambazo zitatumika katika vijiji vya Godegode na Kitati kuchimba visima vya umwagiliaji na kujenga mfereji wa umwagiliaji wenye urefu wa mita 1200.











Share:

Wimbo Mpya : PILI NZALIA - MAMA MKWE

 

Share:

TARURA WATOA ELIMU KWA WANANCHI 300 KUPITIA MAADHIMISHO YA UTUMISHI WA UMMA DODOMA.


Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) wametoa Elimu ya miundombinu ya barabara kwa wananchi 300 waliotembelea kwenye banda lao kupitia Maadhimisho ya Utumishi wa Umma Mkoani Dodoma ambapo wananchi hao wamepatiwa ufafanuzi wa miradi mbalimbali ya barabara katika maeneo yao

Hayo yamesemwa Mkoani  na Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano kwa Umma TARURA Catherine Sungura, amesema wananchi waliotembelea kwenye banda letu tumewahudumia na kusikiliza changamoto zao ambapo tunaenda kuzitatua kupitia mameneja waliopo maeneo husika.

Aidha sungura ameongeza kuwa Tarura inaendelea na ujenzi wa barabara ya zege kimara King'ong'o Dar es salaam hivyo unaendelea vizuri, na Meneja wa TARURA amewahakikishia wananchi kuwa kilomita 1.6 pekee ndizo zimebaki kukamilishwa, huku mita 800 zikitarajiwa kujengwa mwanzoni mwa mwaka mpya wa fedha kuanzia Julai na sehemu iliyobaki kukamilishwa katika awamu inayofuata.

"Nitoe wito kwa wananchi kuwa tarura itaendelea kuhakikisha miundombinu ya barabara inaboreshwa ili kurahisisha mawasiliano na usafiri kwa wananchi kwani barabara hizo zinachochea Upatikanaji wa Maendeleo ya uchumi nchini "Amesema Afisa sungura"

Hata hivyo sungura amewataka wananchi wote waendelee kutembelea kwenye banda la tarura waweze kujipatia elimu ya Miundombinu ya barabara zinazoendelea kujengwa nchini.







Share:

Wimbo Mpya : PILI NZALIA - MAMA MKWE

 

Share:

Sunday, 21 June 2026

WAZIRI SANGU: SERIKALI INATHAMINI MCHANGO WA TAASISI ZA DINI KATIKA KUJENGA AMANI NA MAENDELEO YA TAIFA


SERIKALI imeendelea kuthamini mchango mkubwa unaotolewa na taasisi za kidini nchini katika kuimarisha amani, mshikamano na maendeleo ya taifa.

Amesema hayo Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Sangu leo Juni 19,2026 alipomwakilisha Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, katika ibada maalum ya kuliombea Taifa la Tanzania katika kanisa la KKKT Dayosisi ya Mashariki ya Ziwa Victoria Jijini Mwanza.

Akizungumza katika ibada hiyo, Waziri Sangu amesema Serikali inatambua mchango muhimu wa taasisi za kidini katika kujenga jamii yenye maadili mema, umoja na mshikamano, mambo ambayo ni msingi wa maendeleo endelevu ya nchi.

Amesema kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wote ikiwemo makundi mbalimbali ya kijamii yenye nia njema ya kuijenga Tanzania yetu.

“Tunatambua kuwa maendeleo ya kweli hayawezi kupatikana bila amani, utulivu, umoja na mshikamano wa wananchi wake”

Katika hatua nyingine Waziri Sangu amewahasa viongozi wa dini kuendelea kuhubiri amani, upendo, uvumilivu na maadili mema kwa jamii yetu, hasa kwa vijana ambao ndio nguvu kazi ya Taifa letu.

Vilevile, amewapongeza Umoja wa Unity of Christian International (UCI) kwa kuweka malengo mazuri yanayoendana na Dira ya Taifa 2050 yenye lengo la kujenga jamii yenye mshikamano, upendo, utu na maendeleo.

Kwa upande wake, Askofu Profesa Wilson George Munguza, Askofu kiongozi Unity Christian International Dar es Salaam, ameipongeza Serikali kwa kuendelea kushirikiana na taasisi za kidini katika kuimarisha umoja na maendeleo ya Taifa.

Ibada hiyo maalum ya kuliombea Taifa viongozi wa dini, waumini na wadau mbalimbali wameshiriki ikiwa ni sehemu ya kuendelea kuhamasisha amani, umoja na maendeleo ya Tanzania.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMAPILI JUNI 21,2026

Magazetini Leo




Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger