Sunday, 31 May 2026
KAPINGA AITAKA TBPL KUONGEZA UZALISHAJI NA KUIMARISHA MIKAKATI YA MASOKO
Friday, 29 May 2026
SERIKALI YAPONGEZA UWEKEZAJI WA HALYAZ, ORXY YAZINDUA KITUO KIPYA CHA MAFUTA KARATU
Na Bora Mustafa, Karatu.
Serikali imesema itaendelea kuwalinda wawekezaji wa ndani pamoja na kuunga mkono uwekezaji unaofanywa na Watanzania kwa lengo la kuboresha huduma za kijamii na kukuza uchumi wa nchi.

Akizungumza leo Mei 29, 2026 na Mkuu wa Wilaya ya Karatu, Lameck Karanga, wakati wa uzinduzi wa kituo kipya cha mafuta cha Orxy kinachoendeshwa chini ya Kampuni ya Halyaz.
Karanga amesema ujenzi wa kituo hicho ni muendelezo wa maono ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha wawekezaji wa ndani wanapatiwa mazingira rafiki ya kufanya biashara na kuendelea kuchangia maendeleo ya taifa.
Amesema Wilaya ya Karatu ni lango muhimu la utalii nchini, hivyo uwepo wa kituo hicho utarahisisha upatikanaji wa nishati kwa wasafirishaji pamoja na wadau wa sekta ya utalii. Aidha, amesema bidhaa za kampuni ya Orxy zimeendelea kuaminika katika ukanda wa Afrika na duniani kwa ujumla.
"niwapongeze kwa uwekezaji huu. Mbali na kutuletea kituo bora cha mafuta, mmeanza kwa kutengeneza mazingira mazuri ya bustani mbele ya kituo chenu, jambo linaloonesha namna mlivyojipanga kuleta thamani kwa jamii," amesema Karanga.
Amesema usafi wa mazingira uliooneshwa na kampuni hiyo ni mfano wa kuigwa na taasisi nyingine pamoja na wadau wa biashara katika wilaya hiyo. Hata hivyo, amesisitiza kuwa mazingira safi ni sehemu ya kuimarisha utalii na kuvutia wageni wanaotembelea Karatu.
Aidha, Karanga amewataka wananchi pamoja na wafanyabiashara wa Karatu kuiga mfano wa Kampuni ya Halyaz kwa kuanzisha miradi ya uwekezaji itakayosaidia kuongeza ajira kwa vijana na kuchangia mapato ya Serikali kupitia kodi.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Kampuni ya Halyaz, Ally Abdulrazak, amesema ujenzi wa kituo hicho umetokana na maono ya kuhakikisha Karatu inapata huduma bora za nishati zinazokidhi mahitaji ya wananchi na wageni wanaofika katika eneo hilo.
Amesema kampuni hiyo iliamua kuingia ubia na Orxy kutokana na ubora wa mafuta yake pamoja na uaminifu ambao kampuni hiyo imeujenga kwa muda mrefu katika soko la nishati.
Abdulrazak amesema wateja watakaopata huduma katika kituo hicho watanufaika na huduma zenye viwango vya kimataifa kwa kuwa wafanyakazi wake wamepatiwa mafunzo ya kutosha na huduma zote zinaendeshwa kwa kuzingatia ubora.
"Nina kituo kingine katika mji wa Moshi. Wateja wetu, hususan wa sekta ya utalii, wamekuwa wakituuliza mara kwa mara wanapoweza kupata huduma za mafuta katika ukanda wa Karatu, jambo lililotusukuma kufungua kituo hiki," amesema.
Ameongeza kuwa malengo ya Kampuni ya Halyaz ni kuuza zaidi ya lita 10,000 za mafuta kwa siku pamoja na kuendelea kupanua huduma za vilainishi kwa wateja wake.
Kwa upande wake, Meneja wa Fedha wa Orxy Tanzania, Greyson Francis, aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa kampuni hiyo, amesema uzinduzi wa kituo hicho ni sehemu ya mkakati wa Orxy wa kuendelea kusogeza huduma zake karibu na wananchi.
Amesema Orxy kwa sasa inafanya shughuli zake katika nchi 19 barani Afrika pamoja na kuwa na mtandao mkubwa wa vituo vya mafuta nchini Tanzania. Aidha, amesema kampuni hiyo inatarajia kuzindua vituo vingine viwili vya mafuta katika Jiji la Dar es Salaam katika siku za karibuni.
Uzinduzi wa kituo hicho unatarajiwa kuongeza upatikanaji wa huduma za nishati katika Wilaya ya Karatu, pamoja na kuchochea ukuaji wa uchumi wa eneo hilo kupitia ajira na shughuli nyingine za kijamii na kiuchumi.
Thursday, 28 May 2026
𝐌𝐀𝐅𝐔𝐍𝐙𝐎 𝐘𝐀 𝐔𝐎𝐍𝐆𝐎𝐙𝐈 𝐊𝐖𝐀 𝐖𝐀𝐊𝐔𝐔 𝐖𝐀 𝐒𝐇𝐔𝐋𝐄 𝐘𝐀𝐙𝐈𝐍𝐃𝐔𝐋𝐈𝐖𝐀 𝐑𝐀𝐒𝐌𝐈
KUTOKA MSIKITI WA GADDAFI: WAUMINI WATAKIWA KUTII MAMLAKA NA KULINDA AMANI YA TAIFA

Shehe wa Mkoa wa Dodoma, Mustapha Rajabu Shaaban, amewataka waumini wa dini ya Kiislamu na jamii kwa ujumla kudumisha amani na mshikamano kwa kuwa wasikivu na wenye kutii mamlaka.
Akizungumza katika ibada ya Idd al-Adha kwenye Msikiti wa Gaddafi jijini Dodoma, Shehe Shaaban alisisitiza kuwa kukosekana kwa utiifu na usikivu ndiko kunakosababisha migogoro na umwagaji wa damu katika jamii.
Katika kuelezea umuhimu wa ibada ya kuchinja iliyohitimisha mwezi wa Dhulhijjah, kiongozi huyo alikumbusha kuwa ibada hiyo chimbuko lake ni historia ya Nabii Ibrahim na mwanawe Nabii Ismail.
Alieleza kuwa kisa hicho si hadithi tu ya kawaida, bali ni fundisho kubwa la jinsi Nabii Ibrahim alivyomshirikisha mwanawe kuhusu ndoto ya kumchinja, jambo linalofundisha umuhimu wa kuheshimiana, kusikilizana na kutii amri za Mwenyezi Mungu na mamlaka husika.
Mwisho, Shehe Shaaban aliwasihi wananchi kuendeleza utamaduni wa kuheshimiana ndani ya familia na kitaifa, huku akiwataka kuheshimu viongozi, taasisi, na vyombo mbalimbali vya kijamii na kidini.
Alitolea mfano kamati na tume zinazoundwa ndani ya Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA), akisisitiza kuwa kuheshimu mifumo hiyo ndiko kunakojenga ustawi wa jamii.





























































