Thursday, 18 June 2026

NBS YAAHIDI KUENDELEA KUTOA TAKWIMU SAHIHI KUSAIDIA UTEKELEZAJI WA DIRA YA TAIFA YA MAENDELEO 20250




Na Wellu Mtaki, Dodoma

OFISI ya Taifa ya Takwimu (NBS) imesema itaendelea kuhakikisha takwimu rasmi zinapatikana kwa wakati, kwa ubora unaohitajika na kwa kuzingatia viwango vya kitaifa na kimataifa ili kusaidia juhudi za maendeleo ya taifa katika kipindi chote cha utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Kauli hiyo imetolewa na Mkurugenzi wa Takwimu za Uchumi wa NBS, Daniel Masolwa, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma wakati wa maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika viwanja vya Chinangali.

Amesema NBS ni miongoni mwa taasisi za serikali zinazoshiriki maadhimisho hayo kwa kutoa elimu kwa wananchi kuhusu huduma zake, majukumu yake pamoja na umuhimu wa takwimu rasmi katika maendeleo ya taifa.

Masolwa alisema kuwa takwimu rasmi zitakuwa nyenzo muhimu katika kufuatilia, kutathmini na kupima utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, ambayo inalenga kuifikisha Tanzania katika uchumi wa dola trilioni moja na kuongeza ustawi pamoja na kipato cha wananchi.

Alieleza kuwa takwimu zenye ubora na zinazopatikana kwa wakati zinasaidia serikali, sekta binafsi, taasisi za utafiti na wadau mbalimbali kufanya maamuzi sahihi yanayochochea ukuaji wa uchumi na maendeleo endelevu.

Aidha, amesema kaulimbiu ya mwaka huu ya Wiki ya Utumishi wa Umma inayosema, “Kuchochea Uwajibikaji Jumuishi kwa Huduma Endelevu,” imeipa NBS fursa ya kuendelea kuhamasisha wananchi kuhusu nafasi ya takwimu rasmi katika upangaji wa maendeleo, ugawaji wa rasilimali na ufuatiliaji wa utekelezaji wa mipango ya taifa.

Amefafanua kuwa kwa mujibu wa Sheria ya Takwimu, Sura ya 351, NBS imepewa mamlaka ya kukusanya, kuchakata, kuchambua na kusambaza takwimu rasmi zinazotumika katika sekta mbalimbali za maendeleo nchini.

“Takwimu rasmi ni msingi wa upangaji wa maendeleo. Serikali, sekta binafsi, watafiti na wadau wengine hutegemea takwimu hizi katika kufanya maamuzi sahihi, kuandaa sera, kupanga bajeti na kupima matokeo ya mipango inayotekelezwa,” amesema.

Masolwa alitaja baadhi ya takwimu zinazozalishwa na NBS kuwa ni pamoja na takwimu za mfumuko wa bei zinazotolewa kila mwezi na kuonesha mwenendo wa bei za bidhaa na huduma nchini, hali inayosaidia kutathmini mazingira ya uchumi na gharama za maisha kwa wananchi.

Pia alisema ofisi hiyo huzalisha takwimu za Pato la Taifa (GDP) kwa vipindi vya robo mwaka ambazo huonesha thamani ya bidhaa na huduma zinazozalishwa nchini, kiwango cha ukuaji wa uchumi pamoja na mchango wa kila sekta katika maendeleo ya uchumi wa taifa.

Kwa upande wa ajira, alisema NBS hutoa takwimu zinazoonesha hali ya soko la ajira, kiwango cha ukosefu wa ajira, idadi ya watu walio katika ajira na wale walio nje ya nguvu kazi, jambo linalosaidia katika uandaaji wa sera na mikakati ya kukuza fursa za ajira.

“Tunaendelea pia kuzalisha takwimu za kilimo, uzalishaji viwandani, biashara ya nje pamoja na takwimu za kijamii zinazotokana na Sensa ya Watu na Makazi. Takwimu hizi zinaonesha mwenendo wa idadi ya watu, mgawanyo wa umri, hali ya makazi na rasilimali watu iliyopo nchini,” amesema.

Aliongeza kuwa takwimu hizo ni muhimu katika kukokotoa viashiria mbalimbali vya maendeleo ikiwemo wastani wa pato la mwananchi, viwango vya umaskini, maendeleo ya sekta mbalimbali na hali ya uchumi kwa ujumla.

Akizungumzia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Masolwa alisema mafanikio ya utekelezaji wake yatategemea kwa kiasi kikubwa uwezo wa nchi kutumia takwimu sahihi katika kupanga, kufuatilia na kutathmini hatua zinazopigwa kuelekea malengo yaliyowekwa.

Alisisitiza kuwa katika dunia ya sasa inayotegemea maarifa na teknolojia, matumizi ya takwimu yamekuwa nguzo muhimu katika kufanya maamuzi yenye tija na kuongeza ushindani wa uchumi.

“Lengo la Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ni kuwa na uchumi mkubwa zaidi unaotoa ustawi kwa wananchi. Ili kufikia malengo hayo tunahitaji jamii inayojifunza, inayozalisha maarifa, inayotumia ujuzi na inayofanya maamuzi kwa kuzingatia takwimu sahihi na zenye kuaminika,” amesema.


Amesema NBS itaendelea kuimarisha mifumo ya ukusanyaji na uchambuzi wa takwimu ili kuhakikisha wadau wote wanapata taarifa sahihi zitakazosaidia kuharakisha maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.
Share:

OWM YASHIRIKI MAONESHO YA WIKI YA UTUMISHI WA UMMA 2026


Na Mwandishi wetu - Dodoma


Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Bi. Stella Mwaiswaga pamoja na Watumishi wengine kutoka Ofisi hiyo wameshiriki ufunguzi wa Maonesho ya Wiki ya Utumishi tarehe 17 Juni, 2026 katika viwanja vya Chinangali Park Jijini Dodoma.


Maonesho ya Wiki ya Utumishi ni moja ya matukio katika kalenda ya Umoja wa Afrika (AU) ambapo nchi wanachama huadhimisha kwa kaulimbiu moja na kufanya maonesho ya kazi mbalimbali kuhusu masuala ya Utumishi wa Umma ambapo hufanyika kila mwaka kuanzia tarehe 16 hadi 23 Juni 2026.


Kwa mwaka huu Maadhimisho hayo yamebeba kaulimbiu isemayo; “Kuchochea Uwajibikaji Jumuishi wa Huduma Endelevu”.


SAmbamba na hilo Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu inashiriki maonesho hayo huku ikitoa elimu mbalimbali kwa umma kuhusiana na shughuli za Wakala Serikali wa uchapishaji Tanzania, elimu kuhusu masuala ya Menejimenti ya Maafa, Watu wenye Ulemavu, Ufuatiliaji na Tathimini pamoja na Masuala ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi.







Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO ALHAMISI JUNI 18, 2026


Magazetini Leo



Share:

Wednesday, 17 June 2026

JESHI LA MAGEREZA LASHIRIKI MAADHIMISHO YA KITAIFA YA WIKI YA UTUMISHI WA UMMA 2026



Na. Ssgt Mawazo Mtondo - Dodoma.

Jeshi la Magereza kwa mara nyingine tena linashiriki kikamilifu kwenye Maadhimisho ya Kitaifa ya Wiki ya Utumishi wa Umma kwa mwaka 2026 Maadhimisho ambayo ni moja ya Maazimio ya Umoja wa Afrika (AU).

Hivyo, Jeshi la Magereza linawakaribisha wananchi wote wa Tanzania kutembelea Banda la Magereza katika Maadhimisho ya Kitaifa ya Wiki ya Utumishi wa Umma 2026 yanayofanyika katika Viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma kuanzia Leo Juni 16 hadi 23, 2026.

Maonesho hayo yatawakutanisha Wananchi, Taasisi za Umma na Wadau mbalimbali kwa lengo la kuelezea Dhima, Dira, Mafanikio, Changamoto zilizopo katika suala zima la urekebishaji Wafungwa, kutoa huduma na taarifa mbalimbali muhimu kuhusu shughuli zinazotolewa na Serikali kwa Wananchi kupitia Jeshi la Magereza na kuueleza Umma juu ya Mageuzi ya kisayansi yanayofanywa sasa na Jeshi katika uendeshaji na urekebishaji Wafungwa.

Pamoja na kutoa huduma hizo, Jeshi la Magereza kupitia Maadhimisho haya linatoa elimu kwa umma kuhusu huduma zinazotolewa kwa wafungwa na mahabusu pamoja na shughuli mbalimbali za uzalishaji mali zinazofanywa Magerezani kama mbinu za urekebishaji wafungwa.

 Wananchi pia wanapata fursa ya kuuliza maswali, kutoa maoni na kupata ufafanuzi wa papo kwa papo kutoka kwa Maafisa Magereza waliopo katika Banda hilo.

Sambamba na utoaji wa huduma hizo, Jeshi la Magereza linaendelea kutoa elimu kuhusu shughuli za urekebishaji wa wafungwa, ikiwemo elimu ya maadili, stadi za maisha, mafunzo ya ufundi stadi, ushauri nasaha na programu nyingine zinazolenga kuwawezesha wafungwa kubadilika na kujiandaa kurejea katika jamii wakiwa raia wema na wenye tija kwa familia zao na Taifa kwa ujumla.

Kupitia elimu hiyo, wananchi wanahamasishwa kutambua mchango wa Programu za urekebishaji katika kupunguza uhalifu nchini, kuwajengea wafungwa uwezo wa kujitegemea na kuimarisha usalama wa jamii kwa ujumla.

Aidha, elimu hiyo inalenga kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu umuhimu wa kushirikiana na Jeshi la Magereza katika mchakato wa urekebishaji na urejeshwaji wa wafungwa katika jamii baada ya kutumikia vifungo vyao na kuondoa unyanyapaa hivyo kuwapokea na kuwashirikisha Wafungwa wanaorudi kutoka Magerezani katika shughuli mbalimbali za kijamii na kiuchumi.

Maadhimisho ya Kitaifa ya Wiki ya Utumishi kwa Umma 2026 yanaongozwa na kaulimbiu isemayo: “Kuchochea Uwajibikaji Jumuishi kwa Huduma Endelevu.”


Share:

Tuesday, 16 June 2026

DHAHABU YA DABALO YAFUNGUA FURSA MPYA



Na Dotto Kwilasa, Dodoma

Ugunduzi wa mgodi mpya wa dhahabu katika Kata ya Dabalo, Wilaya ya Chamwino mkoani Dodoma, unatajwa kuwa fursa kubwa ya kiuchumi inayoweza kubadilisha maisha ya wananchi na kuongeza mapato ya Taifa, huku Serikali ikisisitiza uzingatiaji wa sheria za madini na tahadhari za kiusalama ili kuhakikisha rasilimali hiyo inanufaisha Watanzania.

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule, ametoa wito huo alipokuwa akizungumza na wananchi wa Dabalo katika ziara ya kukagua miradi ya maendeleo na kusikiliza kero za wananchi, akiwataka wachimbaji wadogo kuhakikisha wanaendesha shughuli zao kwa kufuata taratibu zote zilizowekwa na Serikali.

Senyamule amesema uwepo wa madini hayo ni neema kwa eneo hilo, lakini mafanikio yake yatategemea namna wachimbaji watakavyofuata sheria, kulipa kodi stahiki na kuchukua tahadhari dhidi ya watu wenye nia ovu wanaoweza kuhatarisha usalama wa mgodi na nchi kwa ujumla.

“Kunapokuwa na madini ya namna hii, tufuate taratibu za Serikali ili tuyatumie kwa tija, lakini tuwe na tahadhari nyingi za kiusalama. Tupokee wageni ambao wana tija na tusipokee wageni wenye hila kwa nchi yetu, huku tukizingatia pia huduma za afya kutokana na mikusanyiko inayoweza kujitokeza,” amesema Senyamule.

Ameongeza kuwa utii wa sheria za madini utasaidia kukuza uchumi wa wananchi mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla, huku ukiibua fursa mpya za maendeleo katika Kata ya Dabalo.

Mbali na masuala ya madini, Mkuu huyo wa Mkoa alikagua mradi wa maji uliotekelezwa na Shirika la World Vision Tanzania kwa gharama ya Shilingi 355,795,952.01 ambao umekamilika na kunufaisha wananchi wapatao 525 wa Kitongoji cha Muungano.

Pia ametembelea mradi wa umaliziaji wa maabara ya sayansi katika Shule ya Sekondari Dabalo uliogharimu Shilingi milioni 50 kutoka Serikali Kuu, ukiwa na lengo la kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia masomo ya sayansi pamoja na kuongeza idadi ya wanafunzi wanaochagua mkondo huo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Chamwino, Janeth Mayanja, amesema utekelezaji wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala unaendelea vizuri, huku elimu kwa vitendo ikiendelea kutolewa kwa wakulima ili kuwahamasisha kupeleka zao la ufuta maghalani na kuuzwa kupitia mfumo rasmi unaowawezesha kupata bei yenye ushindani.

Amesema mwitikio wa wakulima umeendelea kuongezeka kutokana na uelewa wa faida za mfumo huo katika kuongeza kipato na kuimarisha tija kwenye sekta ya kilimo.






Share:

TUNAYAKUMBUKA YA OKTOBA 29, HATUSHIRIKI MAANDAMANO- W/BIASHARA WA MWENGE


Na mwandishi wetu, Dar

Wafanyabiashara ndogondogo maarufu kama Machinga pamoja na waendesha pikipiki za kubeba abiria maarufu kama bodaboda wa eneo la Mwenge jijini Dar es Salaam wameweka msimamo mkali wa kutoshiriki maandamano yaliyopangwa na kuhamasishwa kufanyika Julai 07, 2026, wakisema hawatashawishiwa na mtu yeyote kujiingiza kwenye fujo hizo zinazoweza kuvuruga usalama na amani ya nchi.

Maamuzi hayo yamekuja baada ya kufanya vikao vya ndani na kukubaliana kulinda usalama wa maeneo yao ya kazi, msimamo unaotokana pia na hofu ya kurejea kwa athari kubwa zilizojitokeza wakati wa machafuko ya Oktoba 29, 2025. Katika kipindi hicho kibaya, wengi wakisema kuwa walipoteza ndugu na jamaa zao wa karibu huku biashara zikiharibiwa vibaya. Maduka mengi yalivamiwa, kuibiwa bidhaa zote na mengine kuchomwa moto na kusababisha hasara kubwa sana ya mitaji.

"Sisi wafanyabiashara wa Mwenge kwa kauli moja tunapinga maandamano yanayohamasishwa ya Tarehe saba Julai kwasababu hakuna faida ya maandamano haya hasa kwa tulivyojifunza katika maandamano yaliyopita ikiwemo kupoteza ndugu, marafiki na wengine biashara zao kuathirika kabisa. Sisi hiyo tarehe saba tutakuwa kwenye biashara zetu kama kawaida na tuiombe serikali kuimarisha ulinzi na usalama siku hiyo ya tarehe saba mwezi ujao." Amesema Bi. Tumaini Ulotu, mfanyabiashara soko la Mwenge.

Wafanyabiashara hao wameeleza pia namna ambavyo wao na familia zao walitaabika kupata mahitaji muhimu ya kibinadamu baada ya serikali kuweka amri ya kutotoka nje, waendesha bodaboda wengi wakikosa kipato kwa sababu hawakuweza kubeba abiria barabarani. Hali hiyo ilisababisha uhaba mkubwa wa chakula majumbani mwao na kuwaletea ugumu mkubwa wa maisha.

Kundi hili limesisitiza kuwa halitakubali kutumika kisiasa kwa ajili ya maslahi ya watu wachache wenye nia mbaya, wakitoa wito kwa vijana wote nchini kutokubali kurubuniwa na wanasiasa wanaotafuta umaarufu kwa kutumia nguvu kazi zao.


Share:

Monday, 15 June 2026

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMANNE JUNI 16, 2026

Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger