Sunday, 31 May 2026

KAPINGA AITAKA TBPL KUONGEZA UZALISHAJI NA KUIMARISHA MIKAKATI YA MASOKO


Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, ameagiza Menejimenti ya Kiwanda cha Kuzalisha Bidhaa za Kibaolojia Tanzania (TBPL) kinachomilikiwa na Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC) kuongeza uzalishaji na kuimarisha mikakati ya masoko ili kunufaika na mahitaji makubwa yaliyopo sokoni, kuhakikisha kiwanda kinaendelea kujiendesha kwa ufanisi wa kibiashara

Vilvile amezitaka Taasisi zote hususani TFC, TARI, TFRA na TPHPA zilizoingia makubaliano na TBPL kuhakikisha yanatekelezwa kwa vitendo na kuleta matokeo yenye manufaa kwa wakulima, sekta ya viwanda na uchumi wa taifa kwa ujumla.

Ametoa maagizo hayo Mei 30, 2026 katika hafla ya utiaji saini wa makubaliano ya ushirikiano iliyofanyika katika Kiwanda cha TBPL kilichopo Kibaha mkoani Pwani, kwa lengo la kuimarisha uzalishaji, usambazaji na matumizi ya mbolea hai nchini.

Aidha, amesisitiza kuwa ushirikiano uliowekwa kati ya TBPL, na Taasisi hizo ni hatua muhimu katika kuimarisha minyororo ya thamani ya Mazao ya kilimo na viwanda pamoja na kukuza matumizi ya teknolojia na ubunifu.

Aidha, Waziri Kapinga amesema uzalishaji wa mbolea hai nchini utapunguza matumizi ya fedha za kigeni zinazotumika kuagiza pembejeo hizo kutoka nje ya nchi huku ukiwawezesha wakulima kupata bidhaa bora kwa wakati na kwa gharama nafuu.

Waziri Kapinga pia ameeleza kuwa matumizi ya mbolea hai kupitia TBPL ni hatua muhimu katika kuongeza tija ya kilimo, kuchochea ukuaji wa viwanda vinavyotegemea malighafi za ndani na kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha uzalishaji wa mbolea hai katika ukanda wa Afrika Mashariki..

Kapinga pia amempongeza Mkurugenzi Mwendeshaji wa Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC), Dkt. Nicolaus Herman Shombe, kwa usimamizi wake wa miradi ya maendeleo ya kimkakati na mchango wake katika kuendeleza shughuli za uzalishaji viwandani.
Share:

Friday, 29 May 2026

SERIKALI YAPONGEZA UWEKEZAJI WA HALYAZ, ORXY YAZINDUA KITUO KIPYA CHA MAFUTA KARATU

Na Bora Mustafa, Karatu.

Serikali imesema itaendelea kuwalinda wawekezaji wa ndani pamoja na kuunga mkono uwekezaji unaofanywa na Watanzania kwa lengo la kuboresha huduma za kijamii na kukuza uchumi wa nchi.

Akizungumza leo Mei 29, 2026 na Mkuu wa Wilaya ya Karatu, Lameck Karanga, wakati wa uzinduzi wa kituo kipya cha mafuta cha Orxy kinachoendeshwa chini ya Kampuni ya Halyaz.

Karanga amesema ujenzi wa kituo hicho ni muendelezo wa maono ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha wawekezaji wa ndani wanapatiwa mazingira rafiki ya kufanya biashara na kuendelea kuchangia maendeleo ya taifa.

Amesema Wilaya ya Karatu ni lango muhimu la utalii nchini, hivyo uwepo wa kituo hicho utarahisisha upatikanaji wa nishati kwa wasafirishaji pamoja na wadau wa sekta ya utalii. Aidha, amesema bidhaa za kampuni ya Orxy zimeendelea kuaminika katika ukanda wa Afrika na duniani kwa ujumla.

"niwapongeze kwa uwekezaji huu. Mbali na kutuletea kituo bora cha mafuta, mmeanza kwa kutengeneza mazingira mazuri ya bustani mbele ya kituo chenu, jambo linaloonesha namna mlivyojipanga kuleta thamani kwa jamii," amesema Karanga.

Amesema usafi wa mazingira uliooneshwa na kampuni hiyo ni mfano wa kuigwa na taasisi nyingine pamoja na wadau wa biashara katika wilaya hiyo. Hata hivyo, amesisitiza kuwa mazingira safi ni sehemu ya kuimarisha utalii na kuvutia wageni wanaotembelea Karatu.

Aidha, Karanga amewataka wananchi pamoja na wafanyabiashara wa Karatu kuiga mfano wa Kampuni ya Halyaz kwa kuanzisha miradi ya uwekezaji itakayosaidia kuongeza ajira kwa vijana na kuchangia mapato ya Serikali kupitia kodi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Kampuni ya Halyaz, Ally Abdulrazak, amesema ujenzi wa kituo hicho umetokana na maono ya kuhakikisha Karatu inapata huduma bora za nishati zinazokidhi mahitaji ya wananchi na wageni wanaofika katika eneo hilo.

Amesema kampuni hiyo iliamua kuingia ubia na Orxy kutokana na ubora wa mafuta yake pamoja na uaminifu ambao kampuni hiyo imeujenga kwa muda mrefu katika soko la nishati.

Abdulrazak amesema wateja watakaopata huduma katika kituo hicho watanufaika na huduma zenye viwango vya kimataifa kwa kuwa wafanyakazi wake wamepatiwa mafunzo ya kutosha na huduma zote zinaendeshwa kwa kuzingatia ubora.

"Nina kituo kingine katika mji wa Moshi. Wateja wetu, hususan wa sekta ya utalii, wamekuwa wakituuliza mara kwa mara wanapoweza kupata huduma za mafuta katika ukanda wa Karatu, jambo lililotusukuma kufungua kituo hiki," amesema.

Ameongeza kuwa malengo ya Kampuni ya Halyaz ni kuuza zaidi ya lita 10,000 za mafuta kwa siku pamoja na kuendelea kupanua huduma za vilainishi kwa wateja wake.

Kwa upande wake, Meneja wa Fedha wa Orxy Tanzania, Greyson Francis, aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa kampuni hiyo, amesema uzinduzi wa kituo hicho ni sehemu ya mkakati wa Orxy wa kuendelea kusogeza huduma zake karibu na wananchi.

Amesema Orxy kwa sasa inafanya shughuli zake katika nchi 19 barani Afrika pamoja na kuwa na mtandao mkubwa wa vituo vya mafuta nchini Tanzania. Aidha, amesema kampuni hiyo inatarajia kuzindua vituo vingine viwili vya mafuta katika Jiji la Dar es Salaam katika siku za karibuni.

Uzinduzi wa kituo hicho unatarajiwa kuongeza upatikanaji wa huduma za nishati katika Wilaya ya Karatu, pamoja na kuchochea ukuaji wa uchumi wa eneo hilo kupitia ajira na shughuli nyingine za kijamii na kiuchumi.

Share:

Thursday, 28 May 2026

𝐌𝐀𝐅𝐔𝐍𝐙𝐎 𝐘𝐀 𝐔𝐎𝐍𝐆𝐎𝐙𝐈 𝐊𝐖𝐀 𝐖𝐀𝐊𝐔𝐔 𝐖𝐀 𝐒𝐇𝐔𝐋𝐄 𝐘𝐀𝐙𝐈𝐍𝐃𝐔𝐋𝐈𝐖𝐀 𝐑𝐀𝐒𝐌𝐈


SERIKALI imezindua rasmi Mpango wa Mafunzo ya Uongozi na Usimamizi wa Elimu kwa Wakuu wa Shule za Sekondari na Maafisa Elimu Kata nchini, hatua inayolenga kuimarisha ufanisi wa uongozi wa shule, usimamizi wa ufundishaji na ujifunzaji pamoja na kuimarisha ubora wa elimu nchini.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo Mei 28, 2026 mkoani Mwanza Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo, amesema mpango huo ni hatua muhimu katika kujenga uwezo wa viongozi wa elimu hususan wakuu wa shule za sekondari ambao kwa muda mrefu hawajapata mafunzo ya uongozi na usimamizi wa elimu kwa kiwango kinacholingana na mahitaji ya sasa ya mfumo wa elimu.

Amesema tofauti na walimu wakuu wa shule za msingi ambao wamekuwa wakipata mafunzo ya uongozi, wakuu wa shule za sekondari wamekuwa wakikosa fursa hiyo kwa kipindi kirefu, hali iliyofanya Serikali kuona umuhimu wa kuanzisha mpango huo wa kitaifa ili kuongeza ufanisi wa utendaji kazi na kuboresha utoaji wa elimu.

“Mpango huu ni fursa muhimu kwa viongozi wa shule kupata maarifa ya kisasa ya uongozi, utawala bora na usimamizi wa elimu ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku,” alisema Prof. Nombo.

Prof. Nombo ameeleza kuwa mafunzo hayo hayatawahusu wakuu wa shule pekee, bali yatawajumuisha pia wakuu wasaidizi wa shule za sekondari pamoja na Maafisa Elimu Kata kutoka Tanzania Bara na Zanzibar ili kuhakikisha viongozi wote wa elimu wanakuwa na uelewa unaofanana katika kusimamia ubora wa elimu.

Aidha, amesema Maafisa Elimu wa Mikoa na Halmashauri watashiriki kama wasimamizi wa utekelezaji wa mpango huo katika maeneo yao, hatua itakayosaidia kuhakikisha maarifa yanayopatikana yanaenda sambamba na maboresho ya mifumo ya usimamizi wa elimu.

Pamoja na hayo ameipongeza ADEM pamoja na VVOB-Tanzania kwa kuandaa na kufadhili mpango huo, akieleza kuwa ndani ya kipindi cha miaka mitano kuanzia 2025 hadi 2030, jumla ya viongozi wa elimu 16,000 wanatarajiwa kufikiwa, wakiwemo wakuu wa shule na wasaidizi wao 12,000 pamoja na Maafisa Elimu Kata 4,000.

Amesema mbali na mafunzo ya uongozi, mpango huo utatoa fursa za ufadhili wa masomo kwa Watanzania kupitia scholarships, huku akiwataka viongozi wa elimu kuchangamkia nafasi hizo kwa kuwa elimu ni mchakato endelevu usio na kikomo.

Amesema mafunzo hayo yatafanyika kwa muda wa miezi mitano kwa mfumo wa elimu masafa na ana kwa ana (blended learning), ambapo washiriki wataendelea kutekeleza majukumu yao ya kawaida huku wakijifunza na kutekeleza shughuli za kimradi zinazohusiana na usimamizi wa shule.

Amewataka viongozi wa elimu ngazi ya mkoa na halmashauri kutoa ushirikiano wa karibu kwa washiriki wa mafunzo ili kuwajengea mazingira rafiki ya kujifunza na kuhakikisha wanatimiza wajibu wao wa kikazi sambamba na mafunzo.

Aidha, amefafanua kuwa utekelezaji wa awamu ya kwanza utaanza mwezi Juni 2026 ukihusisha washiriki kutoka halmashauri 12 katika mikoa sita ya Mwanza, Mara, Kagera, Geita, Simiyu na Shinyanga, huku kila mkoa ukianza na halmashauri mbili.

Katika mafunzo hayo, washiriki watajengewa uwezo katika maeneo mbalimbali ya kitaaluma yakiwemo uandaaji wa mipango mkakati, ufunzaji na uatamizi, uthibiti ubora wa ndani wa shule, uongozi wa ufundishaji na ujifunzaji, usimamizi wa mtaala ulioboreshwa wa mwaka 2023 pamoja na usimamizi wa mtaala unaojenga umahiri.

Wakati huo huo, Prof. Nombo amesema Serikali inaendelea kufanya mageuzi makubwa katika sekta ya elimu kupitia utekelezaji wa mtaala ulioboreshwa, ujenzi na ukarabati wa shule, upatikanaji wa vifaa vya kufundishia na kujifunzia pamoja na uwekezaji katika elimu ya amali ili kuandaa wahitimu wenye maarifa, ujuzi na ushindani ifikapo mwaka 2050.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa ADEM, Dkt. Maulid J. Maulid amesema mafunzo hayo yana umuhimu mkubwa kwa wakuu wa shule za sekondari, hasa kutokana na ukweli kwamba kwa muda mrefu kundi hilo halijapata mafunzo ya kina ya kiuongozi na kiutendaji.

Amesema kupitia mafunzo hayo, wakuu wa shule watapata maarifa na mbinu mpya zitakazowawezesha kusimamia shule kwa ufanisi zaidi, kujenga mazingira bora ya kujifunzia na hatimaye kuboresha matokeo ya wanafunzi.

Uzinduzi huo umehudhuriwa na viongozi mbalimbali kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Wathibiti Ubora wa Shule, Maafisa Elimu wa Mikoa na Wilaya pamoja na wadau wa elimu, jambo linalodhihirisha uzito na umuhimu unaowekwa katika kuimarisha uongozi wa elimu nchini.
Share:

KUTOKA MSIKITI WA GADDAFI: WAUMINI WATAKIWA KUTII MAMLAKA NA KULINDA AMANI YA TAIFA




Shehe wa Mkoa wa Dodoma, Mustapha Rajabu Shaaban, amewataka waumini wa dini ya Kiislamu na jamii kwa ujumla kudumisha amani na mshikamano kwa kuwa wasikivu na wenye kutii mamlaka.

Akizungumza katika ibada ya Idd al-Adha kwenye Msikiti wa Gaddafi jijini Dodoma, Shehe Shaaban alisisitiza kuwa kukosekana kwa utiifu na usikivu ndiko kunakosababisha migogoro na umwagaji wa damu katika jamii.


Katika kuelezea umuhimu wa ibada ya kuchinja iliyohitimisha mwezi wa Dhulhijjah, kiongozi huyo alikumbusha kuwa ibada hiyo chimbuko lake ni historia ya Nabii Ibrahim na mwanawe Nabii Ismail.


Alieleza kuwa kisa hicho si hadithi tu ya kawaida, bali ni fundisho kubwa la jinsi Nabii Ibrahim alivyomshirikisha mwanawe kuhusu ndoto ya kumchinja, jambo linalofundisha umuhimu wa kuheshimiana, kusikilizana na kutii amri za Mwenyezi Mungu na mamlaka husika.

Mwisho, Shehe Shaaban aliwasihi wananchi kuendeleza utamaduni wa kuheshimiana ndani ya familia na kitaifa, huku akiwataka kuheshimu viongozi, taasisi, na vyombo mbalimbali vya kijamii na kidini.

Alitolea mfano kamati na tume zinazoundwa ndani ya Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA), akisisitiza kuwa kuheshimu mifumo hiyo ndiko kunakojenga ustawi wa jamii.
Share:

WENYE MAHITAJI MAALUM KUPEWA KIPAUMBELE MAFUNZO YA JKT



Na Dotto Kwilasa, Dodoma 

Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) limesema vijana wenye mahitaji maalum, hususan wenye ulemavu wa viungo, wamewekewa mazingira rafiki yatakayowawezesha kushiriki kikamilifu mafunzo ya uzalendo na stadi za maisha yanayoanza rasmi Juni mwaka huu.

Hatua hiyo imekuja sambamba na maandalizi ya kupokea jumla ya vijana 60,000 wa kidato cha sita kutoka shule mbalimbali Tanzania Bara na Zanzibar watakaoripoti katika makambi ya JKT kuanzia Juni 1 hadi Juni 7, 2026.

Akizungumza jijini Dodoma leo Mei 28, 2026 kwa niaba ya Mkuu wa JKT, Meja Jenerali Rajabu Mabele, Mkuu wa Utawala wa JKT, Brigedia Jenerali Hassan Mabena amesema vijana wenye mahitaji maalum watapangiwa katika Kambi ya Ruvu mkoani Pwani kutokana na uwepo wa miundombinu na huduma zinazokidhi mahitaji yao.

Amesema Serikali imeendelea kuboresha mfumo wa mafunzo hayo kwa kuongeza idadi ya vijana wanaopokelewa kutoka 40,000 hadi 60,000 mwaka huu ikiwa ni sehemu ya kuimarisha uzalendo, nidhamu na uwezo wa kujitegemea kwa vijana.

“Lengo ni kuwajenga vijana kuwa na maadili mema, uzalendo na stadi zitakazowasaidia katika maisha yao ya baadaye na katika kulitumikia taifa,” amesema Mabena.

Kwa mujibu wa Mabena, vijana hao watapangiwa katika makambi mbalimbali nchini ikiwemo Rwamkoma Mara, Msange Tabora, Mpwapwa na Makutupora Dodoma, Mafinga Iringa pamoja na Oljoro Arusha.

Makambi mengine yaliyotajwa ni Bulombora Kagera, Kanembwa na Mtabila Kigoma, Itaka Songwe, Luwa na Milundikwa Rukwa pamoja na Nachingwea mkoani Lindi.

Aidha, JKT limewataka vijana wote waliochaguliwa kuzingatia maelekezo ya kuripoti kwa wakati pamoja na kubeba vifaa muhimu vitakavyotumika wakati wa mafunzo, ikiwemo mavazi ya michezo, shuka, soksi na nyaraka muhimu za masomo na utambulisho.

Amesema mafunzo hayo hayalengi kuwapa vijana maarifa ya kijeshi pekee, bali pia kuwaandaa kuwa raia wenye nidhamu, uwezo wa kufanya kazi na kujitegemea hata kwa wale watakaokosa nafasi za kuendelea na elimu ya juu.

Programu ya mafunzo ya lazima ya JKT ilirejeshwa rasmi mwaka 2013 ikiwa na dhamira ya kuwajengea vijana moyo wa uzalendo na kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo ya taifa.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO ALHAMISI MEI 28, 2026

Magazeti Leo


















Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger