Monday 30 October 2023

SHIGELA ANADI FURSA ZA GGML ZINAZOIPAISHA GEITA KATIKA KONGAMANO LA MADINI


Mkuu wa Mkoa wa Geita, Martin Shigela (katikati) ambaye alitembelea banda la GGML kwenye kongamano la Kimataifa la Madini na Uwekezaji Tanzania 2023 akipokea zawadi kutoka kwa Afisa Uhusiano wa Jamii wa GGML, Doreen Dennis akiwa katika picha ya pamoja na Meneja Mwandamizi Mahusiano ya Jamii -  GGML, Gilbert Mworia.
Akiwa katika banda la maonesho la GGML jijini Dar es Salaam, Mkuu wa Mkoa wa Geita, Martin Shigel pia kwa kutumia kifaa maalumu alipata wasaa wa kutembelea sehemu Mgodi wa GGML Geita, na kupata maelezo ya shughuli za uchimbaji wawazi na chini ya ardhi.


NA MWANDISHI WETU

WAKATI Kongamano la Kimataifa la Uwekezaji katika Sekta ya Madini Tanzania 2023 likifikia tamati tarehe 26 Oktoba mwaka huu, Mkuu wa mkoa wa Geita, Martin Shigela amebainisha fursa zinazotokana na uwepo wa kampuni kubwa ya Geita Gold Mining Limited (GGML) kuwa chanzo cha kupaisha mkoa huo kiuchumi.

Mbali na GGML, pia zipo kampuni za kati na wachimbaji wadogo ambao wametajwa kusisimua uchumi wa mkoa huo ambao unazalisha asilimia 60 ya dhahabu yote inayozalishwa nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam katika kongamano hilo lililofungwa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, Shigela alisema wamekuja kushiriki ili kuona mwelekeo wa sekta ya madini, teknolojia mpya inayotumika na namna wachimbaji wadogo wanavyowea kuitumia.

Alisema GGML ni miongoni mwa makampuni makubwa ambayo yanaongoza kwa kulipa kodi nchini lakini pia yanaongoza kwenye uzalishaji wa dhahabu.

Alisema jitihada za Rais Samia Suluhu Hassan kusimamia sheria, sera, miongozo ambayo inamtaka waziri wa madini kuhakikisha wachimbaji wadogo wanashiriki katika uchimbaji kwa kupewa leseni za umiliki, zimezidi kuipaisha sekta hiyo.

Alitoa mfano kuwa karibu asilimia 30 ya ya dhababu inayozalishwa mkoani Geita inatoka kwa wachimbaji wadogo huku asilimia 70 ikitoka kwa wachimbaji wakubwa.

“Maana yake ni kwamba rasilimali ya madini iliyopo katika mkoa wetu wa Geita inawafaidisha watanzania wote ikiwamo wenye mtaji na wasio na mtaji ambao pia wanataka kuingia kwenye sekta ya madini na mkoa pekee ambao wanaweza kuchimba kwa uhakika ni Geita.

Alisema katika kipindi cha miaka miwili ya Rais Samia wamezalisha dhahabu zaidi ya tani 47 zenye thamani ya Sh trilioni sita na katika hizo tani 11 zinatokana na wachimbaji wadogo na 36 ni kwa wachimbaji wakubwa. 

Aidha, alisema uzoefu ambao wameupata kwenye sekta ya madini, ni pamoja na kupata fedha za kigeni kwa sababu ya kuuza dhahabu,

“Kwenye suala la ajira, mathalani kwa GGML peke yake imetengeneza ajira kwa watanzania zaidi ya 6000.

“Wananchi wanafanya biashara, manunuzi peke yake ya GGML kwa mwaka yanafikia zaidi ya Sh trilioni moja. Wananunua chakula, mavazi kwa ajili ya shughuli za uchimbaji, wananunua mafuta, wanatumia magari kusafirisha bidhaa, wanatumia malori na mabasi kusafirisha wafanyakazi zote hizi ni huduma ambazo zinapatikana Geita kupitia GGML,” alisema  na kuongeza;

“Lakini wapo wafanyabiashara ambao wanafanya biashara za hoteli wapo wafanyakazi ambao wanakuja kwenye mgodi, wapo wafanyabiashara wanakuja kununua dhahabu,” alisema.

Alisema mbali na Geita kuwa na soko la dhahabu, pia eneo la tatu ni faida itokanayo na mahusiano kati ya migodi na wananchi ambapo mkoa huo unafaidika na mpango wa uwajibikaji wa kampuni kwa jamii (CSR) kutoka GGML peke yake wenye thamani ya Sh bilioni tisa kila mwaka. 

Alisema Halmashauri ya Mji wa Geita na wilaya ya Geita hupanga bajeti ili fedha hizo zirudishe huduma kwa jamii ikiwamo kugusa sekta ya maji, elimu, afya na sekta za uzalishaji.

Katika uzalishaji alitoa mfano shughuli za kilimo pamoja na wafanyabiashara ndogondogo ambao wanawezeshwa na GGML kupitia jitihada hizo za uzalishaji na kukuza sekta ya madini.

Aidha, alitoa wito kwa wananchi kutumia vema fursa wanazozipata kutokaja na uwepo wa rasilimali hizo kwa kuweka akiba na kufungua biashara mbalimbali.

Pia aliwataka wamiliki wa migodi ambao hawajanza kutekeleza mpango huo wa CSR kushirikiana na jamii inayowazunguka lakini pia kujenga uwezo wa wachimbaji wadogo.


Share:

TBS YAWAFUNDA WAJASIRIAMALI NJOMBE

Afisa Udhibiti Ubora (TBS), Bi.Doris Mchwampaka akitoa elimu kuhusu masuala ya Viwango kwa wananchi waliotembelea banda la TBS katika maonesho ya nne ya SIDO  yanayofanyika  katika viwanja vya Sabasaba mkoani Njombe.

******************

Na Mwandishi Wetu, Njombe

WAJASIRIAMALI wanaozalisha bidhaa za aina mbalimbali wameshauriwa kuthibitisha ubora wa bidhaa ili kupata masoko ya ndani na nje ya nchi.

Hatua hiyo itawawezesha kuongeza ubora wa bidhaa zao, kupata masoko ya uhakika ndani na nje ya nchi na kuzalisha bidhaa ambazo zina uwezo wa kushindana katika soko la Tanzania, Afrika Mashariki na Dunia kwa ujumla.

Ushauri huo umetolewa leo na afisa Uhusiano wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Neema Mtemvu, wakati wa akizungumza na wajasiriamali kwenye Maonesho ya Nne Kitaifa ya SIDO yaliyoanza Oktoba 21, mwaka huu na yatamalizika kesho (Oktoba 31) mkoani Njombe.

Mtemvu alisema wameshiriki maonesho hayo ili kueleza huduma ambazo zinatolewa na TBS, kwani wao ndiyo wanaohusika na kusajili na kuhakikisha bidhaa zote zinazozalishwa nchini na zile zinazotoka nje zinakidhi vigezo vyote vya ubora.

Kwa mujibu wa Mtemvu Serikali ina mpango wa kukuza viwanda vidogo na vya kati wa wajasiriamali, hivyo TBS kwa kushirikiana na SIDO wana programu ya kuhakikisha wajasiriamali wanazalisha bidhaa ambazo zina ubora na zinazoweza kushindana sokoni.

Alisema wajasiriamali wanatakiwa kupitia SIDO na kupatiwa mafunzo mbalimbali yanayohusiana na bidhaa wanazozalisha, kisha wataandikiwa barua ya utambulisho kwenda TBS.

"TBS tukishapata barua ya mjasiriamali, tutampatia huduma na leseni ya kutumia alama ya ubora ya TBS bure bila gharama yoyote. Atatumia miaka mitatu bila kulipia gharama yoyote na kuanzia mwaka wa nne kadri itakavyoonekana ataanza kulipa asilimia 25 ya ile ada ambayo alitakiwa ailipe," alisema na kuongeza.

"Huduma hii inawasaidia wajasiriamali wote kuhakikisha kwamba bidhaa zao zinakidhi vigezo vya ubora.

Kwa sababu hiyo, Mtemvu alisema wana jukumu kubwa la kuhakikisha bidhaa zote zinazozalishwa na wajasiriamali nazo zinakidhi ubora.

Alifafanua kuwa wanataka bidhaa hizo ziwe na uwezo wa kutumika hapa nchini na hata nje ya nchi, kwa sababu zikishathibitishwa zitakuwa na ubora unaokubalika.

Wajasiriamali waliotembelea banda la TBS kwenye maonesho hayo ili kufahamu ni kwa namna gani bidhaa zao zinaweza kuthibitishwa ili kuwezesha wateja wengi na kupata kilicho bora na kinachoaminiwa na Serikali, walipongeza utaratibu huo na kwamba baada ya maonesho hayo wanaenda kuanza safari ya kuthibitisha ubora wa bidhaa zao.

Walisema maofisa wa TBS wamewaelekeza namna ya kufanya, hivyo alishukuru uongozi wa shirika hilo na shirika hilo, SIDO na Serikali kwa kuwa na mpango wa kuwainua wajasiriamali.
Afisa Udhibiti Ubora (TBS), Bi.Doris Mchwampaka akitoa elimu kuhusu masuala ya Viwango   kwa wananchi waliotembelea banda la TBS katika maonesho ya nne ya SIDO  yanayofanyika  katika viwanja vya Sabasaba mkoani Njombe
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMATATU OKTOBA 30,2023





Share:

Sunday 29 October 2023

TaSUBa KITOVU CHA MAFUNZO TASNIA ZA SANAA NA UTAMADINI NCHINI-DKT. BITEKO

Jukwaa kuu likiongozwa na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dkt. Doto Biteko alipomwakilisha Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Kilele cha Tamasha la 42 la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni Bagamoyo lililoandaliwa na Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kushirikiana na Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa) mkoani Pwani Oktoba 28, 2023.

******************

--Amefunga tamasha la 42 la Kimataifa la Utamaduni Bagamoyo

--Aipongeza Wizara kwa kutangaza utamaduni wa nchi

--Sanaa iwe nyenzo kuunganisha wananchi

Imeelezwa kuwa, Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa) ni kitovu cha mafunzo katika tasnia za Sanaa na Utamaduni nchini na Serikali imeendelea kuiboresha taasisi hiyo kwa kutoa fedha za kuboresha miundombinu na vifaa vya kufundishia na kujifunzia.

Hayo yameelezwa na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dkt. Doto Biteko alipomwakilisha Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Kilele cha Tamasha la 42 la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni Bagamoyo lililoandaliwa na Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kushirikiana na TaSUBa mkoani Pwani Oktoba 28, 2023.

"Niwapongeze Wizara kwa kuitangaza nchi yetu kwa kupitia kazi mbalimbali za utamaduni, sanaa na michezo. Aidha nakupongeza Waziri na wafanyakazi wa Wizara yako kwa kazi kubwa mnayoifanya kila mwaka katika kuliandaa na kuliendesha Tamasha hili kwa kipindi cha miaka 42 sasa," amesema Dkt. Biteko.

Ameongeza kuwa, tamasha hilo lina hadhi kitaifa na kimataifa kwani limehusisha ushiriki wa vikundi vingi vya sanaa vya hapa nchini na vya kutoka nje ya nchi zikiwemo Zambia, Kenya, Burundi, Uganda, Botswana, Afrika Kusini, Canada na nyinginezo.

Katika hatua nyingine, Dkt. Biteko ameipongeza taasisi hiyo kwa kukuza utalii wa kiutamaduni (cultural tourism) hapa nchini jambo linalofanya kuendelea kuvutia utalii wa ndani na nje ya nchi.

"Nawakaribisha na kuwahimiza vijana wote wa kitanzania wenye vipaji vya sanaa kuchangamkia fursa hii kwani sanaa sasa ni ajira hivyo tuitumie vyema kupitia taasisi hii," amesisitiza Dkt. Biteko.

Vile vile, Dkt. Biteko ameitaka Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo kuwa na Mipango mikakati ya kuwasaidia wasanii nchini ili kupitia sanaa hiyo waweze kunufaika kiuchumi na kuitangaza nchi. Amesisitiza wapewe ushirikiano ili Sekta hiyo iwe na mchango mkubwa katika Pato la Taifa.

Kwa upande wake, Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Nape Nnauye amesema kuwa, tamasha hilo limekua na mafanikio makubwa kwa Bagamoyo na mkoa wa Pwani. Amesema wadau wamejitokeza kwa wingi na kulifanya liwe tamasha bora nchini.

Naye, Katibu Mkuu Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo, Gerson Msigwa amesema kuwa, tamasha hilo ni fursa ya kutangaza utalii uliopo nchini kwa kuwakutanisha wadau kutoka ndani na nje ya nchi. Amesisitiza kuwa mwaka 2024 tamasha litakuwa kubwa kwa kuwaleta wadau wengi zaidi nchini.

Wengine walioshiriki kilele cha tamasha hilo ni Mkuu wa Chuo TaSUBa, Dkt.Herbert Makoye, Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Abubakar Kunenge, Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Halima Okash na Watendaji wa Taasisi za Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo na Wadau wa Sanaa na Utamaduni. Maonyesho hayo ambayo hufanyika kila mwaka yalianza rasmi tarehe 26 mwezi huu na kilele chake ilikuwa Oktoba 28, 2023.
Jukwaa kuu likiongozwa na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dkt. Doto Biteko akizungumza na wananchi alipomwakilisha Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Kilele cha Tamasha la 42 la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni Bagamoyo lililoandaliwa na Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kushirikiana na Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa) mkoani Pwani Oktoba 28, 2023.
Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe.Nape Nnaye akizungumza katika Kilele cha Tamasha la 42 la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni Bagamoyo lililoandaliwa na Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kushirikiana na Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa) mkoani Pwani Oktoba 28, 2023.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe.Gerson Msigwa akizungumza katika Kilele cha Tamasha la 42 la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni Bagamoyo lililoandaliwa na Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kushirikiana na Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa) mkoani Pwani Oktoba 28, 2023.
Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhe.Aboubakar Kunenge akizungumza katika Kilele cha Tamasha la 42 la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni Bagamoyo lililoandaliwa na Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kushirikiana na Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa) mkoani Pwani Oktoba 28, 2023.
Baadhi ya Wasanii wakitoa burudani katika Kilele cha Tamasha la 42 la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni Bagamoyo lililoandaliwa na Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kushirikiana na Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa) mkoani Pwani Oktoba 28, 2023.
Wananchi wakifuatilia Tamasha la 42 la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni Bagamoyo lililoandaliwa na Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kushirikiana na Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa) mkoani Pwani Oktoba 28, 2023.

(PICHA ZOTE NA EMMANUEL MBATILO)
Share:

WATAALAMU WA UBONGO NA MISHIPA YA FAMAMU KUSINI MWA JANGWA LA SAHARA WAKUTANA MLOGANZILA


Serikali imesema itaendelea kuwajengea uwezo wataalamu namna ya kubaini na kumhudumia mgonjwa mwenye changamoto za magonjwa ya Ubongo, Mgongo na Mishipa ya Fahamu hapa nchini kwa kutambua kuwa magonjwa hayo yamekuwa tishio duniani.

Akizungumza kwa niaba ya Mganga Mkuu wa Serikali, Mkuu wa Idara ya Matibabu nje ya nchi Wizara ya Afya Dkt. Asha Mahita alipokuwa akifungua Kongamano la Mafunzo ya 14 ya Mishipa ya Fahamu na Ubongo Kusini mwa Jangwa la Sahara linalofanyika kwa siku nne Hospitali ya Taifa Muhimbili-Mloganzila.

Dkt. Asha amebainisha kuwa tatizo la Magonjwa ya Ubongo na Mishipa ya Fahamu hususani kiharusi ni kubwa ulimwenguni ambapo takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO) zinaonesha kuwa kila baada ya sekunde 40 mtu mmoja hupata ugonjwa wa kiharusi na kila baada ya sekunde 3.5 mtu hufariki dunia kwa ugonjwa huo duniani.

“Magonjwa haya yasiyo ya kuambukiza ni hatari sana na wataalamu wake ni wachache kwa hapa nchini tunao Madaktari Bingwa wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu wapo 14 tu ambapo kati yao, madaktari watu wazima ni 11 na kwa upande wa watoto ni watatu tu, ndio maana Serikali imeendelea kuweka msukumo wa kuwaendeleza watalaamu hususani wa mishipa ya fahamu na kuishauri jamii kufanya mazoezi na kula mlo kamili” ameongeza Dkt. Asha.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama cha Wataalamu wa Magonjwa ya Fahamu, Prof. William Matuja amesema kongamano hilo limehusisha wataalamu kutoka hospitali za hapa nchini pamoja na wataalamu kutoka zaidi ya nchi 15 Duniani ikiwemo kutoka Kusini mwa Jangwa la Sahara.

Prof. Matuja ameongeza kuwa kupitia kongamano hilo wataalamu hao watapata fursa ya kubadilisha ujuzi na uzoefu wa kuhudumia wagonjwa wa Ubongo, Mgongo na Mishipa ya Fahamu ambapo wanaamini kuwa maarifa hayo yatasaidia kuendelea kuboresha utendaji kazi wa wataalamu katika maeneo yao ya kutolea huduma.

Naye, Naibu Mkurugenzi Mtendaji MNH-Mloganzila, Dkt. Julieth Magandi ameishauri jamii kupima afya zao mara kwa mara kwakuwa magonjwa ya kiharusi hutokea ghafla hivyo mtu akipima afya yake mapema anaweza kujitambua na kuchukua hatua stahiki.

Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMAPILI OKTOBA 29,2023


Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger