Thursday 4 March 2021
ATUPWA JELA MIAKA 30 KWA KUBAKA MTOTO WA MPANGAJI WAKE SHINYANGA
Vijiji 52 kunufaika na mradi wa kutoa ajira za muda kwa walengwa wa Tasaf Simiyu
Itilima. Wananchi wa Wilaya ya itilima mkoani Simiyu wanatarajia kunufaika na Mradi wa kutoa ajira za muda kwa walengwa wa TASAF chini ya mpango wa kunusuru kaya masikini katika awamu ya tatu kipindi cha pili.
Mradi umelenga kuvifikia vijiji 55 kati ya vijiji 102 vya wilaya hiyo, ambao utatekelezwa kwa kipindi cha miezi sita katika kila kijiji hali itakayo sababisha walengwa wa eneo husika kupata ajira za muda kwa kipindi chote cha mradi.
Hayo yameelezwa na afisa ufuatiliaji TASAF Wilaya ya Itilima Paulo Tibabihilila wakati wa ufunguzi wa mafunzo kwa timu ya wawezeshaji ngazi ya mamlaka ya eneo la utekelezaji kuhusu maandalizi, utekelezaji na usimamizi wa mradi.
Amesema kuwa zoezi la kuibua miradi katika vijiji limeanza katika hatua ya awali ya mafunzo kwa wawezeshaji ili waweze kwenda kubaini miradi itakayokuwa na tija katika jamii na kuwa utekelezaji wake utatumia teknolojia rahisi pamoja na nguvu kazi ya wananchi.
"Miradi itaibuliwa na wananchi wenyewe, wataitekeleza katika hatua zote za utekelezaji na baada ya kukamilika wataisimamia...
Lengo likiwa ni kutengeneza miundo mbinu mizuri katika jamii pamoja na kuwapa wananchi ujuzi katika kuendesha miradi ili waondokane na umasikini".
Akielezea miradi ambayo itakwenda kutekelezwa katika vijiji mmoja wa wawezeshaji wa mafunzo hayo Skay Thomas amesema kuwa miradi itakayokwenda kutekelezwa ni pamoja na miradi ya upandaji miti, miradi ya maji, barabara, umwagiliaji pamoja na kuongeza rutuba ya udongo.
Huku baadhi ya washiriki wa mafunzo hayo Maiko Mhoja na Mary Boniphace wakieleza kuwa mradi huu umekuwa na mapokeo chanya kwa sababu umelenga kuinufaisha jamii.
"Muhimu ni kupeleka elimu katika jamii ili waweze kuwa tayari kuipokea na kuiendele za miradi kwa manufaa yao".
Aidha mkurugenzi mtendaji wa halshauri ya wilaya ya Itilima Elizabeth Gumbo Amewataka wawezeshaji kwenda kuibua miradi endelevu katika vijiji ili hata baada ya mradi kuisha wananchi waendelee kuwa na uwezo wa kuiendeleza miradi hiyo.
Halmashauri ya wilaya ya Itilima ni miongoni mwa halmashauri 51 nchini ambazo zinanufaika na mradi wa ajira kwa muda, mlengwa atapata nafasi ya kuajiriwa kwa kipindi cha miezi sita, katika siku 30 za mwezi atafanya kazi siku 10 kwa masaa manne kwa siku.
Mwisho.
WAZIRI WA NISHATI DKT MEDADI KALEMANI AWEKA JIWE LA MSINGI UJENZI WA NJIA YA KUSAFIRISHA UMEME BARIADI
Samirah Yusuph,
Bariadi. Waziri wa nishati Dkt Medadi Kalemani ameweka jiwe la msingi katika ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme msongo wa kilovolti 220 na kituo cha kupokea na kupoza umeme cha Imalilo wilayani Bariadi Mkoa wa Simiyu wenye gharama ya bilioni 75.
Katika uwekaji wa jiwe hilo Machi 03, Kalemani ameagiza kukamilika kwa mradi huo katika kipindi cha miezi tisa hadi kumi na mbili ili kuwawahishia wananchi huduma ya umeme wa uhakika ambayo ilikuwa haipatikani kwa muda mrefu.
Ambapo amelitaka shirika la umeme nchini Tanesco kuhakikisha kuwa litandaza mtandao wa nguzo za umeme katika maeneo yote vijijini ili kuhakikisha kuwa wananchi wote wanapata umeme majumbani.
"Zoezi la uwekaji wa umeme majumbani kwa sasa sio suala la hiali badala yake ni jambo la lazima ni kila mwananchi awe na umeme katika makazi yake...
Serikali imetumia gharama kubwa kujenga miradi hii hivyo yule atakayeshindwa kuvuta umeme nyumbani kwake tutamtafuta aseme ni kwa nini ameshindwa kuweka umeme".
Aidha aneagiza kuwa Kwa sasa mita zote za umeme katika mitaa na vijiji vitauzwa kwa bei moja bila kujali umbali wa kaya na nguzo hata walio nje ya mita 30 za nguzo watapata umeme kwa bei elekezi ambayo ni tsh 27,000.
Akitoa taarifa ya shirika la umeme mkurugenzi mtendaji wa Tanesco Tito Mwinuka, amesema kuwa ujenzi wa mradi huo umegharimu kiasi cha bilioni 75 pamoja na bilioni 46.7 kwa ajili ya fidia kwa wananchi waliopisha eneo la Mradi.
"Tayari wananchi wameanza kupewa stahiki zao kama fidia baada kupisha mradi huu".
Kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa, Mkuu wa Wilaya ya Bariadi Festo Kiswaga amesema kuwa ujenzi wa mradi huo katika Mkoa wa Simiyu utapelekea upatikanaji wa umeme kuwa wa uhakika tofauti na ilivyokuwa awali.
"Uwepo wa umeme wa uhakika katika Mkoa wetu inakwenda kuwa chachu ya kuinua uchumi wa wananchi kwa sababu wananchi wa mkoa huu ni wakulima, kupitia kulimo wataweza kulima kisasa kwa kutumia mashine ambazo zinahitaji Kumia umeme ikiwa ni pamoja na usindikaji wa mazao jambo ambalo litaongeza tija katika kilimo.
Aidha ameongeza kuwa ni wakati wa shirika la umeme kuboresha miundo mbinu ikiwamo nguzo za umeme zilizo choka ili kuhakikisha umeme haukati mara kwa mara na kuwapa adha wananchi.
Hapo awali Mkoa wa Simiyu haukuwa na kituo cha kupoza, kupokea na kusafirisha umeme badala yake ulipokea umeme kutoka katika vituo vya kupozea umeme kutoka Mwanza na Shinyanga kwa sasa kituo hiki kitakuwa na uwezo wa kufua kilowati 100 za umeme mara mbili ya hitaji la umeme kwa Mkoa.
Mwisho.
WAZIRI LUKUVI AAMURU KUFUTWA HATI YA ARDHI NA KUSHUSHA NEEMA KWA WAKAZI WA MHANDU NYAMAGANA
Na Munir Shemweta, NYAMAGANA
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi William Lukuvi ameshusha neema kwa wakazi wa kata ya Mhandu katika halmashauri ya manispaa ya Nyamagana mkoa wa Mwanza kwa kuamuru kuondolewa katika daftari Hati ya kitalu Na 153 eneo hilo na kupatiwa wananchi 74 waliokuwa katika mgogoro.
Akitoa uamuzi huo tarehe 3 Machi 2021 katika wilaya ya Nyamagana alipokwenda kutatua mgogoro wa eneo hilo uliodumu kwa takriban miaka 14, Waziri Lukuvi alisema, hati ya mtu anayedaiwa mmiliki wa eneo hilo anayetambulika kwa jina la abdallah maliki ilitakiwa kufutwa muda mrefu kwa kuwa hajalipia kodi ya pango la ardhi kwa miaka 15.
“Hati miliki ikaondolewe katika daftari la hati na jaji amethibitisha katika maamuzi yake kuwa wamiliki wa asili katika eneo hili hawakulipwa fidia” alisema Lukuvi.
Waziri wa Ardhi aliongeza kuwa, kutokana na maamuzi hayo sasa wananchi wa eneo hilo watatakiwa kupimiwa kulingana na ukubwa wa eneo wanalomiki na kila mmiliki atatakiwa kulipa tozo la mbele (Premium) asilimia 2.5 kufidia gharama ambayo mmiliki wa awali alishindwa kulipa kodi ya pango la ardhi.
“Huyu mtu ameshindwa kuendeleza kwa wakati na hajalipa kodi kwa miaka 15 sasa wananchi wapimiwe na kupatiwa eneo bila fidia. Huwezi kupewa eneo una hati watu sabini wanajenga miaka 15 wewe una hati umekaa nayo tu” alisema Lukuvi.
Kwa mujibu wa Lukuvi Serikali itahakikisha inalinda hati ya mmiliki wa ardhi huku mmiliki akitakiwa kulinda eneo lake na kusisitiza kuwa hati ya ardhi ni dhamana na ndiyo inayotoa usalama wa mmiliki.
‘Mtu hajaonekana halafu atoe kibali cha kuvunja nyumba. Sheria hairihusu umilikishaji juu ya hati nyingine ndiyo maana nimeamua kuifuta kwanza hati hii ndiyo hati nyingine isajiliwe” alisema Lukuvi.
Aidha, aliagiza eneo lingine kitalu 154 linalokaliwa na wananchi 40 na kumilikiwa na Abdulkarim Mbaga mmiliki wake apelekewe ilani ya siku 90 kabla ya hatua za kisheria hazijachukuliwa dhidi ya eneo lake.
Akiwasilisha mgogoro huo mbele ya Waziri wa Ardhi mwakilishi wa wananchi wa Kata ya Mhandu Sokoni Bw. Kazimiri Shimbi alisema kuwa, muda mrefu wananchi wa eneo hilo wamekuwa katika mgogoro wa ardhi wakishitakiwa na mtu wasiyemjua jambo lililosababisha kushindwa kurasimishiwa makazi katika eneo hilo kwa madai ya kuvamia eneo. Hata hivyo, kwa mujibu wa Shimbi wananchi hao wa Mhandu mara kadhaa wamekuwa wakishinda kesi mahakamani dhidi ya mdai.
DKT. ABBAS: WATENDAJI BMT BADILIKENI VINGINEVYO MTABADILISHWA
Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Hassan Abbasi, amewataka watendaji wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), kufanyakazi kwa bidii na wale watakaoonekana kushindwa kutekeleza majukumu yao Serikali itaawachukulia hatua ikiwa ni pamoja kuwaondoa.
Dkt Abbasi ameyasema hayo Machi 03,2021 jijini Dar es Salaam alipofanya vikao vya kukagua utekelezaji wa kazi na maagizo ya viongozi kwa Baraza hilo pamoja na pia Taasisi ya Hakimiliki Tanzania (COSOTA).
“Katika siri sita za mageuzi na mafanikio ambazo nimekuwa nikiwaeleza siku zote ni kuwa na timu yenye ari, maadili na inayojituma, hili kwa watendaji ni jambo la muhimu sana katika Serikali yetu ya kimageuzi kufanikiwa katika malengo ya kuivusha Tanzania, na hapa BMT wapo watu kama hawajaelewa hili,” alisema Dkt. Abbasi.
Katibu Mkuu Dkt. Abbasi ameongeza kuwa kuna baadhi ya hatua zimeanza kuchukuliwa kutokana na utendaji mbovu akiwemo aliyekuwa Kaimu Msajili wa Vyama vya Michezo.
“Mtendaji Mkuu pendekeza ndani ya siku saba mtu mwingine wa Kukaimu nafasi hiyo ulete wizarani, huyu Msajili aliyekuwepo hapa amesharejeshwa kwenye majukumu ya taaluma yake.”alisisitiza Dkt.Abbasi
Aidha, Dkt. Abbasi alitumia kikao hicho na BMT kuonya baadhi ya watendaji akiwemo mmoja wa watumishi wa Idara ya Utawala katika Baraza hilo kuwamua kubadilika la sivyo atabadilishwa.
“Wizara inapokea malalamiko mengi kuhusu utendaji wako sasa inawezekana ni majungu au kweli una tatizo. Kazi ya Idara ya utawala ni kufanikisha mambo sio kukwaza watumishi na kuwatengenezea jakamoyo. Sasa wewe nilikuwa niondoke na wewe leo, lakini ngoja tukupe muda kukuangalia zaidi.”Dkt. Abbasi
Hata hivyo, awali Dkt. Abbasi alizungumza na Menejimenti ya COSOTA ambapo alisisitiza watendaji hao kukamilisha maboresho ya mifumo yanayoendelea, ili wasanii na wabunifu wengine waanze kupata migao yao huku akisisitiza moja ya nguzo kuu za Wizara kwa sasa ni pamoja na kuona utawala na utendaji bora kuanzia Wizarani, taasisi hadi kwa wadau wa sekta zote.
“Wizara ikiongozwa na Mhe. Waziri wetu Innocent Bashungwa na Naibu wake Abdallah Ulega kwa sasa katika nguzo muhimu za mageuzi katika sekta zetu nne tumekubaliana hili la utawala bora kuanzia Wizarani, kwenye Taasisi na hadi kwenye asasi za wadau wetu ni muhimu na tutalisimamia ipasavyo. Zama za uzembe, majungu, mizungu na watu kuwekeza katika fitna na akadabraha zimekwisha. Tunanyoosha mambo, kila mtu alipo anyooke kabisa kabla hatujafika kumnyoosha.” Aliendelea kusisitiza Dkt. Abbasi.
Wednesday 3 March 2021
MBUNGE SANTIEL KIRUMBA ATEMBELEA KIWANDA CHA CHAKI SHINYANGA MJINI..ATOA PONGEZI KWA VIONGOZI
RAIS MWINYI ATEUA WANACHAMA WA ACT WAZALENDO KUWA MAWAZIRI
KAKA WAWILI WAUANA BAADA YA WAKE ZAKE ZAO KUCHAPANA MAKONDE
MWALIMU AMKATA PANGA MWALIMU MWENZAKE OFISINI WAKIGOMBANIA PENZI LA MWANAFUNZI WA 'FIELD'
Majaliwa: Tpa Imarisheni Usimamizi Wa ‘flow Meter’
WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa ameiagiza Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) ihakikishe inaendelea kuimarisha usimamizi wa mitambo ya mita za upimaji wa mafuta (Flow Meter) ili kudhibiti upotevu wa mapato ya Serikali.
Pia, Waziri Mkuu amesema Serikali inataka kuona makusanyo yote ya mapato kutoka katika bandari zote nchini yanayokusanywa na TPA yanaingia katika mfuko mkuu wa Serikali na kwamba haitakubali kubaki na mtu yeyote anayejihusisha na upotevu wake.
Waziri Mkuu ametoa maagizo hay leo (Jumatano, Machi 3, 2021) baada ya kukagua mitambo ya mita ya mafuta Kigamboni na Kurasini Oil Jety (KOJ) kwenye Bandari ya Dar es Salaam.
Hata hivyo, Waziri Mkuu amesema ameridhishwa na utekelezwaji wa maagizo na maelekezo mbalimbali aliyoyatoa katika vipindi tofauti kuanzia mwaka 2016 alipofanya ziara katika eneo la mitambo ya mita ya mafuta (Flow Meter) ya Kigamboni na KOJ.
Amesema kipindi hicho teknolojia iliyokuwa inatumika haikuwa nzuri sana na ilikuwa inaifanya Serikali kupoteza kiasi kikubwa cha mafuta na kusababisha mapato yaliyokuwa yakipatikana kuwa madogo, hivyo Serikali iliyopita ilifanya maamuzi ya kununua flow meter ya Kigamboni.
Waziri Mkuu amesema Serikali ya Awamu ya Tano imeendelea kuimarisha ununuzi wa mitambo hiyo kwa lengo la kuboresha bandari za Dar es Salaam, Tanga na Mtwara hasa kwenye sekta ya mafuta. ”Leo nimekuja kuona hatua sahihi tuliyofikia na nimeridhishwa na utekelezaji wake.”
Amesema baada ya kuona mifumo ya upimaji si sahihi sana Serikali ilipendekeza vinunuliwe viwanja Kigamboni ili kujenga matenki ambayo yatapokea mafuta kutoka bandarini, licha kupimwa katika ‘flow meter’ yanapopelekwa kwa mteja yatapimwa tena kuhakikisha mteja anapata kiwango sahihi cha mafuta anachokihitaji.
”Nimefurahi kupata taarifa kwamba viwanja vimenunuliwa na sasa zabuni ya ujenzi wa matenki mapya inafanywa, tukishafika hapo Taifa litanufaika sana kuwa na mafuta mengi yaliyopo kwenye akiba yetu. Pia hata wateja wanaotaka mafuta watakuwa wanaagiza wakati wowote kulingana na mauzo waliyoyafanya na kiwango wanachokihitaji kwa wakati huo.”
Waziri Mkuu amesema matanki hayo yatatoa fursa kwa nchi jirani ambazo zinatumia bandari hiyo kuagiza mafuta kwani wataweza kuhifadhi mafuta yao na kuiwezesha bandari hiyo kufanya biashara ya mafuta ndani na nje ya nchi. Ameagiza zabuni ya ujenzi wa matanki hayo iharakishwe ili ujenzi uanze mara moja.
Kadhalika, Waziri Mkuu ameitaka Mamlaka ya Bandari iimarishe usimamizi wa ‘flow meter’ na pia inatakiwa ianzishe idara maalumu ya kuzisimamia katika bandari zote. Amesema watendaji wa idara hiyo ndio watakaowajibika kwenye utunzaji na utoaji wa huduma katika eneo hilo.
Awali, Mhandisi wa Idara ya Mafuta wa TPA, Mhandisi Yona Malago alimueleza Waziri Mkuu hatua zilizochukuliwa na TPA ili kuhakikisha ufanisi wa kushusha mafuta kupitia mita ya Kigamboni unafikiwa. ”Hatua ya awali ni ile iliyowezesha mita kufanyakazi bila kusimama na hatua ya pili ni kufanya ukarabati mkubwa wa mita ikiwemo kurekebisha machujio.”
Alitaja hatua nyingine zilizochukuliwa kuwa ni pamoja na kuweka wafanyakazi wenye sifa, vigezo na uwezo wa kusimamia mita hizo ikiwa ni pamoja na wahandisi, mafundi sanifu na mafundi mchundo wa umeme, mitambo na tehama na kufanya mafunzo kwa wafanyakazi wa TPA ambao wanasimamia utendaji wa mita hiyo.
(Mwisho)
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU
Burundi Yaiomba Tanzania Kuisemea Kimataifa
Burundi imeiomba Tanzania kuendelea kuisemea nchi hiyo katika majukwaa ya Kimataifa ili iweze kuondolewa vikwazo vya kiuchumi ilivyowekewa na Jumuiya ya Ulaya jambo linalozorotesha maendeleo ya kiuchumi kwa nchi hiyo.
Ombi hilo limetolewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimaendeleo wa Burundi, Mhe. Isidore Ntirampeba wakati wa ufunguzi wa mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ya Kudumu kati ya Tanzania na Burundi unaofanyika kwa ngazi ya wataalam mjini Kigoma tarehe 3 na 4 Machi 2021.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mkutano huo, Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Brig. Gen. Wilbert Ibuge amesema Tanzania itaendelea kuisemea Burundi katika majukwaa ya Kimataifa ili Burundi iondolewe vikwazo vyote vya kiuchumi ilivyowekewa ili kuipa nafasi nchi hiyo kuendelea na jitihada za kuwaletea wananchi wake maendeleo.
Pamoja na hilo Balozi Ibuge ameihakikishia Burundi kuwa, Tanzania itaendelea na jitihada zake za kuisadia nchi hiyo kuingia katika Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) ili iweze kuungana na nchi za ukanda huo katika kuwaletea wananchi wake maendeleo.
“Tanzania na Burundi zimeendelea kushirikiana kwenye Nyanja za Kimataifa na Kikanda kupitia Jumuiya za EAC, ICGLR, AU na Umoja wa Mataifa (UN). Ni kupitia ushirikiano huu, Tanzania itaendelea kuisemea Burundi katika majukwaa ya kimataifa ili iondolewe vikwazo vyote vya kiuchumi ilivyowekewa. Na kwa mara nyingine na uhakikishia ujumbe wa Burundi kwamba Tanzania itaendelea kuunga mkono ombi la nchi hiyo la kuwa mwanachama wa SADC” alisema Balozi Ibuge.
Katika hatua nyingine, Balozi Ibuge alieleza kwamba Mkutano wa Sita wa Tume ya Pamoja ya Kudumu ni fursa nzuri ya kujadili masuala mbalimbali yenye manufaa kwa nchi zote mbili na kuwataka wajumbe wa mkutano huo kujipanga kutekeleza kikamilifu yale yote yatakayokubalika katika mkutano huo.
Mkutano huu umeanza kwa ngazi ya wataalam na utamalizika kwa ngazi ya Mawaziri tarehe 5 Machi 2021 ambapo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa AFrika Mashariki ataongoza ujumbe wa Tanzania kwenye mkutano huo.
Ujumbe Kutoka U.A.E Kukagua Viwanda Vya Nyama Nchini
Na. Edward Kondela
Balozi wa Falme za Nchi za Kiarabu (U.A.E) hapa nchini Mhe. Khalifa Almarzooqi Abdulrahman amesema ataandaa wajumbe kutoka U.A.E kuja hapa nchini kutembelea viwanda vya kuchakata nyama ili kujiridhisha na ubora wa nyama kwa ajili ya kupeleka katika nchi zao.
Akizungumza leo (03.03.2021) na Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki, mara baada ya kumtembelea katika ofisi ndogo za wizara hiyo zilizopo jijini Dar es Salaam, balozi huyo amesema ni muhimu kwa viwanda vya kuchakata nyama vilivyopo hapa nchini kupata soko la uhakika katika nchi za Falme za Kiarabu kwa kuzingatia Tanzania ni nchi ya pili kwa kuwa na idadi kubwa ya mifugo.
Aidha, amewaasa wamiliki wa viwanda hivyo kuketi pamoja na kuwa na umoja wao katika kukabiliana na changamoto mbalimbali ikiwemo ya kutafuta masoko ya bidhaa zao.
Kwa upande wake Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki amemweleza balozi huyo kuwa viwanda vingi vya kuchakata nyama vinakabiliwa na changamoto ya masoko kupeleka bidhaa zao nchi za nje kutokana na kudaiwa kukosa sifa kulingana na baadhi ya sheria na kanuni zilizopo katika nchi hizo za kuingiza nyama kutoka nchi za nje.
“Viwanda vyetu vya kuchakata nyama licha ya kuwa na uwezo mkubwa wa kuchinja idadi kubwa ya ng’ombe, mbuzi na kondoo lakini bado vinakabiliwa na changamoto ya kukosa masoko ya kupeleka bidhaa zao mara baada ya kuchakata nyama.” Amesema Mhe. Ndaki
Kuhusu ujumbe kutoka Falme za Nchi za Kiarabu (U.A.E) kuja nchini kutembelea viwanda vya kuchakata nyama na kujiridhisha na ubora wa bidhaa zinazozalishwa kama alivyoahidi balozi wa U.A.E hapa nchini Mhe. Khalifa Almarzooqi Abdulrahman, Waziri Ndaki amesema ujumbe huo utakuwa ni mwanzo mzuri wa viwanda hivyo kupata masoko ya bidhaa zao nchi za nje.
Pia, Waziri Ndaki kuhusu sekta ya uvuvi amemwambia balozi huyo kuwa serikali iko katika hatua mbalimbali za kuhakikisha uvuvi wa bahari kuu unaanza katika ukanda wa Bahari ya Hindi kwa kujenga bandari ya uvuvi pamoja na ununuzi wa meli za uvuvi.
WAZALISHAJI WA MAFUTA YA KULA NYANDA ZA JUU KUSINI WAPIGWA MSASA
Wadau wa mafuta ya kula Nyanda za Juu Kusini wakifuatilia kwa karibu mafunzo yaliyotolewa na TBS kwa kushirikiana na BRELA, SIDO na Wakala wa Vipimo.
Wazalishaji wa mafuta ya kula wametakiwa kufuata kanuni bora za kilimo, usindikaji na zile za afya ili kuongeza uzalishaji nanubora wa bidhaa hiyo nchini.
Wito huo ulitolewa na Shirika la Viwango Tanzania (TBS) wakati wa mafunzo kwa wasindikaji, wauzaji, wasambazaji na wenye maduka yanayouza mafuta wapatao 972 yaliyofanyika katika mikoa minne ya nyanda za juu kusini kuanzia February 19 hadi 29 mwaka huu.
Mafunzo hayo yalihusisha wadau hao kutoka mikoa ya Iringa, Njombe, Songwe na Mbeya ikiwa ni utekelezaji wa agizo la Serikali kupitia Wizara ya Viwanda na Biashara kutaka wazalishaji wa mafuta nchini kusaidiwa ili waweze kuongeza uzalishaji wa bidhaa hiyi.
Kwa sasa mafuta ya kula yanayozalishwa nchini ni tani 200, 000 kwa mwaka, wakati mahitaji halisi ni kati ya 400,000 hadi 600,000.
Mafunzo hayo yalihudhuriwa na BRELA, SIDO na Wakala wa Vipimo (WMA), ambapo kila mmoja alieleza wadau hao nafasi yake katika kufanikisha uzalishaji na ukuzaji biashara ya mafuta.
Akizungumza wakati wa mafunzo hayo Kaimu Mkuu wa Udhibiti Ubora wa Bidhaa TBS, Baraka Mbajije, aliwataka wazalishaji wa mafuta kufuata kanuni bora za kilimo, usindikaji pamoja na za afya.
Mbajije alisema kanuni bora za kilimo zinahusiha mbegu bora, kuvuna kwa wakati na mazao yanayovunwa kwa ajili ya uzalishaji mafuta yanatakiwa yawe yamekomaa.
Kwa upande wa kanuni bora za usindikaji kwa mujibu wa Mbajije ni pamoja na kuzingatia usafi hasa kwenye mazingira ya viwandani.Alisema mazingira ya uzalishaji viwandani yanatakiwa kuwa safi pamoja na mashine zinazotumika.
Akizungumzia kanuni bora za afya, Mbajije alisema wazalishaji wanatakiwa kuhakikisha vifaa vya kuhifadhi mafuta ni safi ikiwa ni pamoja na madumu yanayotumika kuhifashi mafuta hayo yawe yamesafishwa vizuri.
" Madumu wanayoweka mafuta wahakikishe wameyasafisha vizuri na waweke lebo zinazoeleza bidhaa hizo ni za aina gani," alisema na kuongeza kwamba haikubaliki kwenye vifungashio ambavyo wazalishaji wanaweka mafuta iwe lebo inayohusu bidhaa nyingine.
Aidha, alisema mafuta ya kula hayatakiwi kuwekwa juani, kwani yanapokuwa juani kuna kemikali zinazozalishwa na zinaweza kusababisha magonjwa ikiweno kansa.
Kwa upande wake Kaimu Mkuu wa Kanda ya Nyanda za Juu Kusini Abel Mwakasonda, alitoa mwito kwa wadau hao kusajili TBS majengi ya bidhaa za vyakula na vipodozi.
Alisema kwa kufanya hivyo Shirika hilo litaweza kuwafikia kwa urahisi.
" Tunatoa mwito kwa wadau kufika TBS, wasiogope kama kuna makosa tutawasaidia kuyarekebisha," alisema Mwakasonda.
Alisema ni muhimu kwa wafanyabishara kusajili bidhaa na majengo ya vyakula na vipodozi kwa mujibu wa sheria ambayo imetokana na mabadiliko ya Sheria ya fedha ya mwaka 2019.
Sheria hiyo ilirudisha majukumu ya usimamizi wa usalama na ubora wa vyakula na vipodozi kwa TBS kutoka kwa iliyokua Mamlaka ya Dawa na Chakula Tanzania (TFDA).
Alisema usajili wa bidhaa majengo ya vyakula na vipodozi ni takwa la kisheria ili kuwawezesha kufanya biashara zao urahisi.
Usajili majengi ya biashara unawapa wafanyabiashara uhakika wa kutunza bidhaa na wanasajili jengo kulingana na bidhaa zinazoenda kuhifadhiwa humo.
Kwa upande wa usajili wa bidhaa, eneo linalohusika ni bidhaa za chakula na vipodozi.Usajili wa vipodozi vilivyopigwa marufuku kwenye soko la Tanzania haviingizwi nchini kutokana na kuwa na viambata sumu.
Mafunzo hayo kwa wazalishaji wa mafuta ni mwendelezo wa mafunzo yaliyokwisha kutolewa katika mikoa Dodoma, Singida, Tabora na Kigoma.
UKARABATI WA MTO LUKOSI RUAHA MBUYUNI WAKAMILIKA
Mhandisi Mazingira kutoka Tume ya Taifa ya Umwagiliaji Daniel Manase akizungumzia kuhusu kazi ya kurejesha Mto Lukosi katika njia yake asili, Ruaha Mbuyuni Mkoani Iringa. |
Mtambo aina ya Excavator ukifanya kazi ya kuiinua tuta kwa kupanga mawe katika mto Lukosi, ili kuurejesha katika njia yake ya asili.
Picha ni Banio linalotumika kupitisha maji kutoka katika chanzo na kupeleka katika skimu ya kilimo cha umwagiliaji Ruaha Mbuyuni |
Picha inaonesha Muonekano wa Tuta, likiendelea kufanyiwa kazi katika mto Lukosi, Ruaha Mbuyuni |
Na Mwandishi Wetu,Ruaha Mbuyuni–Iringa
Ukarabati wa kingo za Mto Lukosi uliyopo katika Wilaya ya Kilolo Mkoani Iringa, unayopeleka Maji yake katika mto Ruaha mkuu na kutumika katika skimu ya kilimo cha Umwagiliaji Ruaha Mbuyuni, umekamilika baada yakusombwa na mafuriko makubwa yalitokea mwaka jana, yaliyosababishwa na mvua kubwa zilizonyesha katika ukanda wa nyada za nyanda za juukusini.
Akizungumza baada ya kukamilika kwa kazi hiyo Mhandishi Mazingira kutoka Tume ya Taifa ya Umwagiliaji, Daniel Manase alisema mafuriko hayo yaliyoharibu kingo yenye urefu wa takribani mita 180, yalisababisha kingo za mto kubomoka n ahivyo mto kuacha njia ya asili nakuanza kupita kwenye mkondo mpya uliojitokeza.
Aliongeza kwakusema kuwa Kuhama kwa mto kulipelekea banio la skimu ya Umwagiliaji Ruaha Mbuyuni kukosa maji na mazao yaliyokuwa shambani yalikauka, Mhandisi Manase Alisema, baada ya kufika katika eneo hilo nakuona hali halisi kazi kubwa ilikuwa nikutengeneza barabara ya muda kwanza ili kuweza kufika katika eneo liliko haribika kutokana na mazingira kutokuwa rafiki.
Alisema, Kazi ya ujenzi iliendelea kwa kujaza mawe na vifusi katika ujenzi wa tuta ili kulimmarisha.
“Pamoja na kwamba tulikuwa na vifaa vyetu, tulipata msaada wanyongeza ya eskaveta, kutoka kwa muwekezaji Kilimanjaro express anayefanya uwekezaji katika maeneo hayo, nakufanya kazi usiku na mchana karibia masaa 29, ili kuweza kuzunguka na kuziba gema maana maji yalikuwa yanakula gema.”Alibainisha.
“Tulizunguka kwa umbali wa kilometa 25 ili kuweza kubeba mawe na vifusi kuhakikisha kazi inakamilika, mwanzoni tulikuwa tunazunguka umbali wa kilomita tano kutokana na kwamba hali haikuwa nzuri ikabidi tuzunguke hizo kilomita 25.”Alisisitiza Mhandisi Manase.
Mhandisi Manase alisema, Kazi ya kupandisha tuta ilikuwa na changamoto ya mvua kutokana na kwamba vifaa vilikuwepo, magari yaliyokuwa yakikwama yalikwamuliwa.
Aliendelea kusema kuwa kwasasa kazi hiyo imekamilika na wananchi katika maeneo hayo wanaweza kuendelea na shughuli za kilimo katika skimu ya Ruaha mbuyuni kama kawaida kwani hali ya mazingira sasa imesharudi katika hali yake ya kawaida.