Saturday 17 April 2021

SIMBA SC : TUNAIJUA MWADUI, HATUWACHUKULII POA.....MWADUI NAYO YATAMBA KUINUKA KESHO

...
Mratibu wa Simba SC, Abbas Ally

Na Damian Masyenene, SHINYANGA
 
MABINGWA Watetezi wa Ligi Kuu Tanzania Bara (VPL), Wekundu wa Msimbazi Simba, wamesema kuwa hawatowadharau wapinzani wao katika mchezo wa kesho, Mwadui FC, bali wataingia uwanjani kwa lengo moja la kupata alama tatu ili kuwa na uhakika wa kuutetea ubingwa wao msimu huu.

Simba SC watakaribishwa kesho (Jumapili) katika uwanja wa CCM Kambarage mjini Shinyanga na wenyeji wao, Mwadui FC kwa ajili ya mchezo wa Ligi Kuu Tanzania bara, huku wenyeji wakiwa na kumbukumbu nzuri ya kushinda bao 1-0 timu hizo zilipokutana uwanjani hapo msimu uliopita.

Akizungumza leo uwanjani hapo katika maandalizi ya mchezo wa kesho, Mratibu wa Simba SC, Abbas Ally amesema kikosi chao takimekuja kikamilifu kupambana na Mwadui na wanafahamu vyema namna wapinzani wao walivyo wasumbufu wanapokuwa uwanja wa nyumbani.

“Tuna historia isiyo nzuri katika mchezo wa mwisho hapa, …Mwadui wamekuwa wasumbufu wakiwa hapa nyumbani kwao, naamini watatumia nguvu nyingi kupata matokeo ili kujinusuru hapo walipo, hivyo itakuwa mechi ngumu, lakini lengo letu ni kutafuta alama tatu ili tuwe katika mazingira mazuri ya kutetea ubingwa wetu,” amesema.

Mratibu huyo ameeleza kuwa, kutokana na upinzani mkubwa unaokuwepo baina ya timu hizo, tayari Kocha Mkuu wa Wekundu hao wa Msimbazi, Didier Gomez anazo taarifa ya kilichojiri katika mchezo wa mwisho uwanjani hapo, hivyo anauchukulia mchezo huo kwa umuhimu mkubwa na amezungumza na wachezaji kuupa umuhimu na kushinda.

Hata hivyo, Abbas ameeleza kuwa katika kuhakikisha wanapata ushindi kwenye michezo yao mitatu ya Kanda ya Ziwa baina ya Mwadui FC, Kagera Sugar na Gwambina FC, timu hiyo imekuja na nyota wote 28 wa kikosi hicho.
Kocha Mkuu wa Mwadui FC, Salhina Mjengwa

Kwa upande wake, Kocha Mkuu wa Mwadui FC, Salhina Mjengwa amekiri kuwa wanakutana na timu bora yenye mwendelezo mzuri ndani na nje ya nchi, lakini wamejiandaa vyema kuikabili Simba na kupata matokeo mazuri yatakayowapa matumaini ya kujinusuru na janga la kushuka daraja, huku akibainisha kuwa wachezaji wake wote wako kwenye hali nzuri na hakuna majeruhi.

“Wachezaji wako katika hali nzuri, kuelekea kesho asilimia 90 tumekamilisha maandalizi yote kuikabili Simba. Ni kweli tunacheza na timu bora, mabingwa watetezi na timu yenye mwendelezo mzuri, tunafahamu wanakuja kwenye uwanja usio rafiki, pamoja na kwamba mwenendo wetu siyo mzuri lakini hatuchezi vibaya, tunataka kuanzia kwao kupata alama tatu,” amesema. 
Nahodha wa Mwadui FC, Mussa Mbise

Naye Nahodha wa Mwadui FC, Mussa Mbise amesema kwa sasa morali ndani ya kikosi chao ni kubwa na kwa wiki nzima wamejiandaa vyema kwa ajili ya Simba, hivyo ana matumaini watashinda kesho.

“Timu yetu ni nzuri tunakosa tu mwendelezo mzuri tumekuwa na bahati mbaya tu ya kukosa matokeo, tunawaheshimu Simba lakini tutafanya vizuri. Wana Shinyanga watarajie matokeo mazuri,” ameeleza. 



Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger