Saturday 30 March 2019

KINDOKI AGEUKA SHUJAA!! APANGUA PENALTI MBILI KUIPELEKA YANGA NUSU FAINALI


Kipa Klaus Kindoki amepangua penalti mbili na kuiwezesha Yanga SC kwenda Nusu Fainali ya michuano ya Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), au Azam Sports Federation Cup (ASFC) kwa ushindi wa penalti 4-3 dhidi ya wenyeji, Alliance FC kufuatia sare ya 1-1 ndani ya dakika 90 jioni ya leo Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza.

Kindoki, mlinda mlango kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), alipangua penalti za Dickson Ambundo na Nahodha wa Alliance FC, Siraj Juma, wakati kinda Martin Kiggi aligongesha mwamba wa kushoto.

Waliofanikiwa kumfunga penalti zao upande wa Alliance FC ni Joseph James, Geofrey Luseke na Samir Vincent, wakati za Yanga zilifungwa na beki Paul Godfrey ‘Boxer’, viungo Mzimbabwe Thabani Kamusoko, Haruna Moshi ‘Boban’ na Deus Kaseke.

Vijana wazaliwa wa Mwanza na walioibukia mkoani hapa kisoka ndiyo waliokosa penalti zote za Yanga, beki Kelvin Patrick Yondan akigongesha mwamba na kiungo Mrisho Khalfan Ngassa mkwaju wake ukipanguliwa na kipa John Mwanda. 

Katika dakika 90 za mchezo huo, Yanga SC walitangulia kwa bao la mshambuliaji kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Heritier Ebenezer Makambo dakika ya 38 kwa shuti la kitaalamu baada ya pasi ya kiungo Pius Charles Buswita.

Alliance FC walisawazisha bao hilo dakika ya 62, kupitia kwa kiungo wake wa ulinzi, Joseph James aliyemalizia kwa kichwa mpira wa adhabu uliopigwa na Mapinduzi Balama kutoka upande wa kulia.

Sasa Yanga itasafiri kuwafuata Lipuli FC Uwanja wa Samora mjini Iringa mwishoni mwa mwezi Aprili katika mchezo wa Nusu wa Fainali.

Nusu Fainali nyingine itafanyika Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam ikiwakutanisha Azam FC walioitoa Kagera Sugar kwa kuichapa 1-0 jana Bukoba na KMC ya Kinondoni walioitupa nje African Lyon kwa kuipiga 2-0 Jumatano Mbweni. 

Kikosi cha Alliance FC leo kilikuwa; John Mwanda, Godlove Mdumule, Siraj Juma, Wema Sadoki, Geoffrey Luseke, Joseph James, Michael Chinedu/Samir Vincent dk58, Paul Maona/ Hussein Javu dk55, Bigirimana Blaise/Martin Kiggi dk90+3, Balama Mapinduzi na Dickson Ambundo.

Yanga SC; Klaus Kindoki, Paul Godfrey, Gustapha Simon, Said Juma ‘Makapu’, Kelvin Yondan, Feisal Salum ‘Fei Toto’/Thabani Kamusoko dk77, Mrisho Ngassa, Papy Kabamba Tshishimbi, Heritier Makambo, Amissi Tambwe/Haruna Moshi ‘Boban’ dk61 na Pius Buswita/Deus Kaseke dk77.

Chanzo- Binzubeiry 
Share:

Picha : SHIRIKA LA AGAPE LATOA MSAADA WA MBUZI NA KONDOO 40 KUKABILIANA NA MIMBA NA NDOA ZA UTOTONI DIDIA

Shirika la Agape AIDS Control Programme limetoa msaada wa mbuzi na kondoo 40 kwa familia 10 duni katika kata ya Didia Halmashauri ya wilaya ya Shinyanga ili kuwasaidia watoto wa kike wanaosoma kutoka familia hizo wanaoishi katika mazingira hatarishi ili kuepuka mimba na ndoa za utotoni. 

Msaada huo wa mifugo hao wenye thamani ya shilingi milioni tatu umetolewa leo Jumamosi Machi 30,2019 katika viwanja vya shule ya msingi Didia ambapo mgeni rasmi alikuwa Katibu Tawala wilaya ya Shinyanga Boniface Chambi kwa niaba ya Mkuu wa wilaya ya Shinyanga. 

Akizungumza wakati wa kukabidhi mbuzi na kondoo hao,Mkurugenzi Mtendaji wa shirika la Agape,John Myola alisema ni kwa ajili ya 10 maskini lengo likiwa ni kuwafikia watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi. 

“Hii ni sehemu ya utekelezaji wa Mradi wetu wa Kutokomeza mimba na ndoa za utotoni kwa ufadhili wa shirika la Firelight Foundation la Marekani, tunaamini kuwa tukiwezesha wazazi wao kwa kuwapa mifugo basi tutakuwa tumesaidia watoto wanaosoma kuwa katika mazingira salama ili kuondokana na vitendo vya kuolewa au kupata mimba kwa sababu ya umaskini”,alieleza Myola. 

“Kaya hizi ambazo kila moja leo zitapata mbuzi na kondoo wanne hazitokani na Mpango wa kunusuru kaya Maskini (TASAF),bali Agape kwa kushirikiana na baraza la maendeleo la vijiji lilibaini kaya hizi 10 ambapo tumechukua kaya mbili kutoka vijiji vya Mwamalulu,Mwanono,Bukumbi,Didia na Chembeli na pindi mifugo hao watakapozaana kaya zingine zitapewa mifugo waliozaliwa”,alifafanua Myola. 

Myola alisema shirika lake linaunga mkono serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na rais John Pombe Magufuli kwa kutekeleza kwa vitendo Mpango wa Taifa wa Kutokomeza Ukatili dhidi ya Wanawake na Watoto (MTAKUWWA) kwa kuwajengea uwezo kiuchumi wananchi na kukabiliana na ndoa na mimba za utotoni. 

Kwa upande wake,Katibu Tawala wilaya ya Shinyanga,Boniface Chambi alilipongeza shirika la Agape kwa kuendelea kushirikiana na serikali kuwaletea maendeleo wananchi ikiwa ni Utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi kwa kuwawezesha wananchi kiuchumi. 

Aidha aliziasa familia/kaya zilizopata msaada huo kutumia mifugo hao kwa malengo yaliyokusudiwa ili kujiinua kiuchumi huku akiwataka watendaji na wenyeviti wa vijiji kuhakikisha wanasimamia mifugo hiyo ili iendelee kunufaisha familia nyingi zaidi.

ANGALIA PICHA HAPA CHINI
 Mkurugenzi Mtendaji wa shirika la Agape,John Myola akizungumza wakati wa kukabidhi mbuzi na kondoo 40 kwa kaya 10 maskini katika kata ya Didia Halmashauri ya wilaya ya Shinyanga. Kulia kwake ni Katibu Tawala wilaya ya Shinyanga,Boniface Chambi(aliyevaa shati la kitenge) akifuatiwa na Diwani wa kata ya Didia,Richard Masele (aliyebeba kondoo) pamoja na wawakilishi wa kaya hizo.Picha zote na Kadama Malunde - Malunde1 blog
Kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji wa shirika la Agape,John Myola akitoa mwongozo wa kugawa kondoo/mbuzi wanne kwa kila kaya.
Sehemu ya kondoo na mbuzi waliotolewa na shirika la Agape kwa familia 10 katika kata ya Didia ambapo kila kaya imepata mbuzi/kondoo wanne.
Katibu Tawala wilaya ya Shinyanga,Boniface Chambi (mwenye shati la kitenge) akipokea mbuzi/kondoo kutoka shirika la Agape.
Zoezi la kukabidhi mbuzi likiendelea.
Katibu Tawala wilaya ya Shinyanga,Boniface Chambi akiwasisitiza wananchi waliopata msaada wa mbuzi na kondoo kutumia mifugo hao kwa malengo yaliyokusudiwa.
Mkurugenzi Mtendaji wa shirika la Agape,John Myola akizungumza baada ya kukabidhi kondoo na mbuzi kwa kaya 10 zilizopo katika kaya ya Didia.
Diwani wa kata ya Didia,Richard Masele akilipongeza shirika la Agape kwa kuendelea kuwa karibu na wananchi wa Didia kwani limekuwa likitoa misaada mbalimbali ili kuhakikisha mimba na ndoa za utotoni zinatokomezwa katika kata hiyo.
Bibi Njile Kulwa akitoa neno la shukrani kwa shirika la Agape kwa kuwapatia msaada wa mbuzi wawili na kondoo wawili.
Bibi Njile Kulwa akiwa amesimama wakati mbuzi na kondoo wake wakifungwa kamba tayari kwa kuondoka nao.
Awali Mkurugenzi Mtendaji wa shirika la Agape,John Myola akizungumza wakati wa hafla fupi ya kukabidhi mbuzi 19 na kondoo 21 kwa ajili ya kaya 10 kutoka kata ya Didia (kaya mbili kila kijiji kwenye vijiji vitano vya kata hiyo).
Katibu Tawala wilaya ya Shinyanga,Boniface Chambi akizungumza wakati wa kupokea mbuzi 19 na kondoo 21 waliotolewa na shirika la Agape kwa ajili ya kaya 10 katika kata ya Didia.
Katibu Tawala wilaya ya Shinyanga,Boniface Chambi akikabidhi kanga,kitenge na shuka nyeusi kwa Bi. Salma Machiya ikiwa ni zawadi kutoka shirika la Agape kwa wema aliouonesha kwa kutunza mbuzi na kondoo 40 kwa muda wa wiki moja wakisubiri kugawiwa kwa kaya 10 leo.
Binti wa Bi. Salma Machiya, naye akipokea zawadi ya madaftari na kalamu kwa ajili ya masomo yake katika shule ya Sekondari Itwangi.
Picha zote na Kadama Malunde - Malunde1 blog
Share:

Mchungaji Aonya Wachungaji Kuwa Upande Wa Adui

Mchungaji Mwangalizi Mkuu wa makanisa ya Presbyterian Tanzania, Mchungaji Sylvester Ng’welemi   ameonya tabia ya wachungaji kusemana vibaya katika huduma zao, kitu ambacho kinawafanya wawe upande wa adui wao Shetani. 

Onyo hilo amelitoa leo tarehe 30.03.2019 alipokuwa katika ibada maalum ya Uzinduzi wa Kanisa la Shekinah Presbyterian tawi la Mbopo. 

Alisema kwamba mojawapo ya changamoto kubwa kwa wachungaji siku hizi ni kuwa wanapoona huduma mpya imeanzishwa katika maeneo yao wanaamua kuiponda na kuiita majina ya ajabu ajabu kama vile “Freemasons.” Je Freemasons ndio wanapaswa kufanikiwa? aliuliza umati mkubwa watu uliokuwa umebanana kwenye jengo jipya la kanisa. Alihoji kwamba “kwa nini wachungaji wanapofanikiwa wapendwa ambao si wa madhehebu hayo huanza kuhoji maswali, kwa nini wasihoji wakati bado maskini?” 

Katika ibada hiyo ambayo ilijumuisha tukio la kuweka wakfu jengo la kanisa ambalo limejengwa kwa mfupi sana kwa ufadhili wa wamissionari kutoka Korea Kusini, Mwangalizi aliwatia moyo wachungaji wa Presbyterian Church Tanzania (PCT) kwamba wanahitaji kusimama imara kwa kufundisha ukweli, na kwamba fedha zinazotumika kujenga makanisa haya wazione kuwa ni za thamani kwa sababu watu wale wanaotoa wana haki ya kutumia pesa hizo kwa ajili ya mambo mengine

 “ kanisa la PCT linasimama katika ukweli, na miujiza inatendeka, kama ukitaka kuhakikisha njoo kanisani kwangu” alisisitiza mchungaji huyu ambaye ni mchungaji kiongozi wa kanisa la Efatha Presbyterian la Kigamboni-Mjimwema. 

Alihoji kwamba “kwa nini watu wanahoji kujengwa kwa jengo hili kwa haraka? je ni kweli kwamba Mungu wetu hawezi? kwa nini watu wanapenda tukae kwenye kanisa la makuti tu? je sisi tusiabudu kwenye makanisa ya kisasa kama hili? mtu anapoamua kusema vibaya juu ya kanisa hili, maana yake ameamua kuwa upande wa adui, na jambo hili ni hatari sana kwa sababu ni laana kwao.

Vile vile katika ibada hii kuliambatana na zoezi la kutoa Msaada wa kimasomo (Scholarship) kwa watoto wanaoishi katika mazingira magumu. watoto hamsini walipokea vyeti vya msaada kwa ajili ya kupokea sare za shule. 

Aliyesimamia utoaji wa msaada, ambaye ni mchungaji Daniel John Seni wa makanisa ya Shekinah Presbyterian alisisitiza kwamba ni lazima Watanzania tuendane na kasi ya serikali ya awamu ya tano. Alisisitiza kwamba “kanisa letu linaungana na serikali ya awamu ya tano kwa kutoa msaada wa kimasomo.”

Katika sherehe hii ambayo ilihudhuriwa na wachungaji mbalimbali wa makanisa ya Presbyterian, wachungaji wa makanisa jirani pamoja na kwaya mbalimbali; pia Mwangalizi aliwakaribisha wachungaji wote kwa ajili ya kumsimika rasmi, Mchungaji Zakayo Nashoni kwa ajili ya kutumika rasmi katika kanisa hilo.

Mwangalizi aliwasihi wachungaji kuimarisha umoja miongoni mwao, na kushirikiana na Mchungaji Zakayo Nashoni kwa ajili ya kuleta maendeleo katika eneo la Mbopo na maeneo jirani.

Taarifa hii imetolewa na:
Kitengo cha habari
Shekinah Presbyterian Church (T)
0769080629



Share:

Picha : SHIRIKA LA AGPAHI LATOA MAFUNZO YA SAIKOLOJIA KWA WATUMISHI WA AFYA MWANZA


Shirika la Ariel Glaser Pediatric AIDS Healthcare Initiative (AGPAHI) limetoa mafunzo kwa watoa huduma za afya kutoka Vituo vya Afya mkoani Mwanza, yanayolenga kuwajengea
uwezo katika kutoa msaada na huduma za kisaikolojia kwa watoto na vijana wanaoishi na maambukizi ya Virusi Vya Ukimwi (VVU).

Mafunzo hayo ya siku tano yalianza jumatatu Machi 25, 2019 hadi Ijumaa Machi 30, 2019 katika ukumbi wa “Isamilo Lodge” Jijini Mwanza ambapo yamewashirikisha wataalam wa afya zaidi ya 60 kutoka Halmashauri mbalimbali mkoani Mwanza ikiwemo Nyamagana, Ilemela, Misungwi, Magu, Ukerewe na Buchosa.

Afisa Miradi, Huduma Unganishi kwa Jamii kutoka shirika la AGPAHI, Cecilia Yona amesema mafunzo hayo yatawasaidia watoa huduma za afya katika vituo vya tiba na matunzo kutambua namna bora ya kuwahudumia wateja wao hususani watoto na vijana.

Amesema mafunzo hayo yatawasaidia pia kuwatambua watoto na vijana wenye changamoto kisaiklojia na namna ya kuwasaidia huku wakizingatia upatikanaji wa huduma bora na rafiki kwa wateja kupitia mbinu mbalimbali ikiwemo michezo.

“Tunatarajia pia wataenda kuanzisha vikundi vya akina mama wanaoishi na maambukizi ya VVU ambao wako kwenye kitengo cha kuzuia maambukizi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto ili nao waweze kujifunza kupitia uzoefu wao huku vikundi vilivyopo
vikiimarishwa zaidi”,amesema Yona.

Baadhi yawashiriki wamesema mafunzo hayo yatawasaidia kuboresha utendaji wao wa kazi tofauti na ilivyokuwa hapo awali ambapo walikuwa wakikumbana na changamoto ya kutambua mazingira halisi yanayowakabili watoto na vijana kupitia klabu zao.

Shirika la AGPAHI kwa ufadhili wa Watu wa Marekani kupitia taasisi ya Centres for Disease Control (CDC), linashirikiana na Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kutekeleza afua mbalimbali za kupambana na
maambukizi ya VVU pamoja na kuwahudumia watu wanaoishi na maambukizi hayo.

Na George Binagi-GB Pazzo, BMG
Mmoja wa Wawezeshaji, Margaret Safe kutoka Kibaha mkoani Pwani akifafanua jambo kwenye mafunzo hayo.
Mwezeshaji, Margaret Safe akiwasilisha mada kwenye mafunzo hayo.
Afisa Miradi, Huduma Unganishi kwa Jamii kutoka shirika la AGPAHI, Cecilia Yona akizungumza kwenye mafunzo hayo.
Afisa Miradi, Huduma Unganishi kwa Jamii kutoka shirika la AGPAHI, Cecilia Yona akifafanua jambo kwenye mafunzo hayo.
Washiriki wakimsikiliza Afisa Miradi, Huduma Unganishi kwa Jamii kutoka shirika la AGPAHI, Cecilia Yona.
Mwezeshaji, Dkt. Nikodemas Kikoti akiendelea kutoa mada kwenye mafunzo hayo.
Washiriki wakimsikiliza Mwezeshaji, Dkt. Nikodemas Kikoti kutoka mkoani Iringa.
Wataalam wa afya walioshiriki mafunzo hayo wakifuatilia mada kwa umakini.
Baadhi ya washiriki wa mafunzo hayo.
Timu ya wakufunzi wa mafunzo hayo.
Baadhi ya washiriki wakifuatilia mada kwenye mafunzo hayo.
Washiriki wa mafunzo pia walipewa mtihani na hapa wakiwa kwenye chumba cha mtihani ili kupima uelewa wa kile walichofundishwa.
Washiriki wakijibu mtihani kuhusu walichofundishwa.
Baada ya mafunzo ya nadharia darasani yaliyofanyika Isamilo Lodge, washiriki walielekea Lesa Garden kukutana na baadhi ya watoto na vijana kutoka klabu za elimu na makuzi kwa ajili ya kucheza na kufurahi pamoja ikiwa ni sehemu ya mafunzo kwa vitendo.
Washiriki wa mafunzo hayo wakiwasili Lesa Garden iliyopo Luchelele Jijini Mwanza.
Mafunzo kwa vitendo kupitia michezo.
Inaelezwa vijana hujifunza na kuelewa vyema kupitia michezo na hapa michezo imepamba moto.
Michezo mbalimbali ikiendela.
Mafunzo kwa vitendo kupitia michezo.
Washiriki wa mafunzo wakifurahi pamoja na vijana.
Michezo ikiendelea Lesa Garden.

Watoa huduma za afya wamehimizwa kutumia michezo kufikisha elimu kwa watoto na vijana.
Inaelezwa michezo husaidia watoto na vijana kuelewa vyema yale wanayofundishwa hivyo watoa huduma za afya wamehimizwa kutumia michezo pia kuwaelimisha vijana na watoto.
Washiriki wakifurahia pamoja na vijana.
Pia kulikuwa na burudani ya muziki ikiwa ni sehemu ya mafunzo kwa vitendo ambapo husaidia watoto na vijana kuwa huru kwa watoa huduma za afya.
Burudani ya muziki.
Washiriki wa mafunzo wakifurahia muziki pamoja na watoto/ vijana.
Michezo na burudani ni sehemu ya mafunzo kwa vitendo.

Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger