Wednesday 1 June 2016

NAFASI ZA KAZI CHUO KIKUU UDOM JUNE 2016

Share:

Magufuli: Serikali Itakomesha Watumishi na Wanafunzi Hewa

INNOCENT-THE BLOGGER-BOY


RAIS John Magufuli (pichani) amesema Serikali ya Awamu ya Tano imejipanga kumaliza makosa yote yaliyojitokeza huko nyuma ikiwemo tatizo la watumishi na wanafunzi hewa lililoibuka hivi karibuni.

Amewataka Watanzania kuacha kuingiza siasa kwenye makosa yanapojitokeza, hasa yale yanayogusa sehemu nyeti kama elimu, kwani yakiachwa kuna uwezekano wa kutengeneza taifa la watu wa ajabu.

Alisema tangu aingie madarakani amekumbana na changamoto mbalimbali, ikiwemo matatizo ya rushwa, ukwepaji kodi, watumishi hewa na sasa amekumbana na tatizo la wanafunzi hewa.

“Nchi yetu ina changamoto na mambo mengi sana hata mimi nimekumbana na changamoto naziona mwenyewe, nikigeuka hivi watumishi hewa ambao hadi sasa wamefikia 10,500, nikigeuka hivi kuna wanafunzi hewa,” alisisitiza.

Alisema ni Tanzania pekee ambayo mtu anaweza kupata daraja la nne kidato cha nne katika elimu ya sekondari, halafu akapata fursa ya kujiunga na chuo kikuu na kupatiwa mkopo wa serikali, wakati mhitimu aliyefaulu kidato cha sita akikosa fursa hiyo.

Alisema endapo kulifanyika makosa lazima yarekebishwe, kwani inafahamika fika mtu akimaliza kidato cha nne akifeli ataanzia ngazi ya Astashahada, Stashahada ndio apate nafasi ya kujiunga chuo kikuu.

“Sasa hapa kwetu ni tofauti ukifeli kidato cha nne unajiunga chuo kikuu,” alihoji na kuwataka watu waache siasa kwenye makosa kwani mambo kama hayo yakiachwa kuna hatari ya nchi kutengeneza taifa la ajabu.

Hivi karibuni, Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako aliivunja Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) na kuwasimamisha kazi viongozi wanne waandamizi kwa tuhuma za kudahili wanafunzi wasio na sifa.

Aidha, Mwenyekiti wa Bodi ya TCU, Awadh Mawenya naye alisimamishwa kazi kwa kosa la kushindwa kuwachukulia hatua watumishi waliodahili wanafunzi hao wasio na sifa. 
Profesa Ndalichako alichukua hatua hizo baada ya TCU kudahili wanafunzi 489 waliopata daraja la 4.32 katika mitihani yao ya kidato cha nne lakini walijiunga na chuo kikuu na kupatiwa mikopo yenye thamani ya Sh milioni 784.
Share:

Mauaji ya Kutisha: Watu 8 Wakamatwa Kwa Mwenyekiti wa Kitongoji na Kuchinjwa Kinyama

INNOCENT-THE BLOGGER-BOY

MAUAJI ya Watanzania kwa njia ya kuchinjwa yanaendelea kushika kasi baada ya usiku wa kuamkia jana wakazi wanane wa kitongoji cha Kibatini, kata ya Mzizima jijini Tanga kukusanywa kwa mwenyekiti wa kitongoji na kisha kuuawa kwa kuchinjwa shingo na watu wasiojulikana.

Watu hao ambao inadaiwa kuwa ni majambazi walivamia usiku wa kuamkia jana kwa kuvunja milango ya nyumba tatu ambazo wakazi hao walikuwa wamelala na kuwachinja kisha kuiba biskuti, mchele na sukari na kutokomea navyo kusikojulikana.

Wauaji hao inadaiwa wana uhusiano na wahalifu ambao wamekuwa wakijificha ndani ya mapango ya Majimoto na kujihusisha na matukio kadhaa ya uvamizi ili kupora vyakula na kusababisha mauaji ya wakazi wa Jiji la Tanga, ikiwamo katika duka kuu la Central Bakery mwishoni mwa Aprili mwaka huu.

Mmoja wa shuhuda wa mauaji hayo, Kea Leonard (70) ambaye pia ni mkazi wa Kibatini, katika mahojiano jana alisema wanaamini kwamba chanzo cha mauaji ya wenzao ni kulipiza kisasi.

“Wiki iliyopita majira ya saa tano asubuhi hapa tulikamata vijana saba kati ya wanane wenye umri wa kama miaka 13 ambao walikuwa wakiranda randa hapa kitongojini ili kutafuta namna ya kuvuka mto kwenda ng’ambo ya pili na ndipo mmoja wao alipotutoroka,” alieleza Leonard na kuongeza:

“Watoto hao tulipowaweka chini ya ulinzi na kuwahoji tukaanza kuwatilia shaka hivyo mwenyekiti aliamua kuripoti Polisi na ndipo hao wakawachukua kwa ajili ya mahojiano na hatukufuatilia tena kujua kwamba waliachiwa au la kwa sababu hao watoto sio wenyeji wala wakazi wa eneo hili.”

Aliongeza kwamba wakati wahalifu hao wanavamia nyumba ya mjumbe wa serikali ya kitongoji kabla ya kumtoa nje walisikia mmoja wa watu hao akimhoji kuhusu mahali walipopelekwa watoto saba.

Diwani wa Kata ya Mzizima, Fredrick Charles alizungumza na waandishi wa habari na kuthibitisha kwamba kati ya watu waliokufa mmoja ni Mjumbe wa Serikali ya Mtaa wa Mleni uliopo kwenye kata hiyo.

“Hali ya usalama hapa kwetu Mzizima si shwari kwa sababu wananchi wangu wa Kibatini wamevamiwa na kuchinjwa usiku wa kuamkia jana majira ya saa sita usiku,” alisema Chiluba. 
Naye Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Mleni kilichopo kitongoji hicho, Shabani Amani alisema wamepatwa na hofu kubwa kuhusu matukio hayo.

“Tunadhani kuna mapungufu katika suala la ulinzi hapa kwa sababu baada ya kutokea matukio kadhaa eneo letu hasa baada ya kudaiwa kwamba mapango waliyojificha wahalifu yako hapa jirani na kwetu kikosikazi cha mchanganyiko wa askari polisi na wa JWTZ wanafanya doria kwa saa 24 lakini tunashangaa kwa nini matukio yanaendelea,” alisema Amani.

Kwa upande wake, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, Leonard Paul alithibitisha mauaji hayo. “Mei 30, mwaka huu majambazi waliokuwa na visu na mapanga walivamia kaya tatu na kuua wananchi majira ya saa saba usiku,” alisema Kamanda Paul.

Aliwataja waliouawa ni Issa Hussein (50) ambaye ni mmiliki wa kaya hiyo pamoja na kuibwa biskuti, mchele na sukari katika duka dogo. Wa kaya nyingine ni Mkola Hussein (40) na Hamis Issa (20), Hamis Issa (20) na aliyemtaja kwa jina la Mikidadi (70).

Kamanda aliwataja marehemu wengine ni Mahamud (35) ambaye ni mkwe wa Mikidadi, Issa Ramadhani (25), Kadir (25) na Salum ambao ni wachunga ng’ombe kijijini humo. 
Hata hivyo, mashuhuda wa tukio hilo akiwemo mke wa marehemu Mkola aitwaye Aisha Saidi, alisema walipofika nyumbani hapo waligonga mlango na kumtoa nje Mkola na kuondoka naye.

“Nimeachwa mjane na watoto sita... Baada ya hao watu kuingia walimkamata Mkola na kumdai aeleze kwamba watoto wao saba wamepelekwa wapi na alipojibu sijui wakamtoa nje na kumkusanya pamoja na wanakijiji hao wengine na kuwachinja eti tu kwa sababu hawakutaja mahali walipopelekwa watoto,” alisema Aisha.

Katika hatua nyingine, Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB) imesikitishwa kupokea taarifa za vitendo vya mauaji ya kikatili vinavyoendelea kutokea katika maeneo mbalimbali nchini.

“Wimbi hili la matukio ya vitendo vya mauaji na ukatili uliojitokeza kwa kufuatana mwezi Mei 2016 yanavunja haki ya kuishi ambayo ndio msingi wa haki zote za binadamu kwa ujumla wake.

"Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora inalaani vikali mauaji haya yote na matendo yote ya kikatili dhidi ya mwanadamu yanapotokea popote nchini,” ilieleza taarifa ya Mwenyekiti wa Tume, Bahame Nyanduga.

Tume iliishauri serikali kupitia Jeshi la Polisi ichukue hatua mahsusi kuhakikisha ulinzi wa wananchi dhidi ya mauaji na vitendo hivi, kwani jukumu la kwanza la kuhakikisha usalama wa wananchi ni jukumu la serikali. 
Jeshi la Polisi lihakikishe watu wote waliohusika kutekeleza mauaji haya wanakamatwa ili sheria ichukue mkondo wake, ilieleza.
Share:

Shein: Hakuna Mtu Wala Nchi Yakuweza Kuniondoa Madarakani

INNOCENT-THE BLOGGER-BOY
RAIS wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein amesema hakuna nchi au jumuiya za kimataifa zitakazomwondoa madarakani yeye kwa sababu amechaguliwa kihalali na wananchi kwa kura nyingi kwa mujibu wa Katiba.

Dk Shein alisema hayo wakati akizungumza na wanachama na wafuasi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika matawi ya Wesha Tibirinzi, Pembeni Shengejuu na Maziwa Ng’ombe, Micheweni katika ziara ya kuwafariji kutokana na matukio ya hujuma zilizofanywa na wapinzani huko Pemba.

Aliwataka wafuasi wa CCM na wanachama wake waliopo Pemba, wasibabaishwe na kauli zinazotolewa na viongozi wa vyama vya siasa wanaopita na kudai kwamba uchaguzi mwingine unakuja.

“Mimi ndiye Rais halali wa Zanzibar nimechaguliwa katika uchaguzi ulioitishwa na Tume ya Uchaguzi... wananchi msisikilize uvumi na kauli za wapinzani zenye lengo la kuwababaisha na kuwayumbisha katika shughuli zenu za maendeleo,” alieleza Dk Shein.

Dk Shein alisema amesikitishwa na kauli za uchochezi zinazotolewa na viongozi wa vyama vya siasa zenye malengo ya kuishawishi jamii kutengana na kugombana na kususiana hata katika shughuli za jamii ikiwemo misiba.

Alisema kiongozi anayefanya vitendo vyenye lengo la kuwagawa wananchi kwa malengo ya kisiasa  huyo ameishiwa na hana nafasi katika jamii. 

“Huyo kiongozi anayewashawishi wananchi kususia shughuli za jamii na maendeleo basi huyo ameishiwa kisiasa na hana nafasi katika jamii ya wananchi na ninyi mpuuzeni.Alikuwa na nafasi ya kushiriki katika uchaguzi lakini alisusa,” alieleza.

Alisema viongozi wa Chama cha Wananchi (CUF) wameishiwa hoja kwa sasa na hawana la kufanya baada ya kugomea kushiriki katika uchaguzi halali wa marudio uliofanyika Machi 20, mwaka huu ambao umetoa nafasi kwa CCM kushinda katika uchaguzi wa kishindo.

Mapema Dk Shein ambaye ni Makamu Mwenyekiti wa CCM aliwataka wanachama wa chama hicho kutembea kifua mbele na kuachana na unyonge kwa sababu chama chao ndiyo kilichoshika dola na kuunda serikali.

Akizungumzia yanayotokea Pemba, Dk Shein alisema, “Nimesikitishwa na taarifa za matukio mbalimbali yanayofanyika huku Pemba ikiwemo watu kususiwa maiti, kushushwa katika gari za abiria baada ya kuwa na itikadi tofauti......haya matukio hayakubaliki na yanakwenda kinyume cha maamrisho ya dini zote.”

Aliwataka viongozi waliopewa majukumu kwa mujibu wa Katiba kufanya kazi zao na kupambana na vitendo vya ubaguzi ikiwemo vya kuonewa kiholela wananchi.
Share:

Waziri Mkuu: Serikali Itahakikisha Inaendelea Kulinda Rasilimali Za Nchi Ikiwemo Urithi Wa Dunia

INNOCENT-THE BLOGGER-BOY
SERIKALI ya awamu ya tano  imesema kuwa itaendeleza jitihada za kutunza na kulinda urithi wa dunia ikiwemo kutoa elimu kwa wananchi wanaoishi maeneo ya uhifadhi ili watanzania wote waweze kunufaikana rasilimali za nchi .

Hayo yalisemwa na  waziri mkuu Kassim Majaliwa alipokuwa akifungua mkutano wa kulinda urithi wa dunia wa Afrika kama nyenzo ya maendeleo endelevu unaoendelea jijini Arusha

Majaliwa alisema kuwa rasilimali zilizopo ni za watanzania na ili kuhakikisha kuwa wananufaika nazo serikali itahakikisha  inatunza na kulinda uhifadhi ili yawe endelevu na  kusaidia vizazi vijavyo.

Alisema kuwa Tanzania ni moja ya nchi tajiri yenye urithi na hivyo ili kuhakikisha kuwa wananchi wananufaika haswa waishio maeneo ya uhifadhi serikali itatoa elimu ya kutosha ili waepuke kuchangia uharibifu wa mazingira unaotokea kwenye hifadhi za taifa .
 
“Rasilimali hizi ni zetu na hivyo hata wanaoishi maeneo ya hifadhi watusaidie kwa wale wanaoingilia na kuharibu  kwani hata hizo mali asili zinatusaidia sote na ndiyo sababu  tumewekea mikakati ya kutunza maeneo hayo ili yawe endelevu" alisema

Kwa upande wake mwenyekiti wa mkutano huo ambaye ni Katibu Mkuu Wizara ya Mali asili na Utalii Meja Jenerali Gaudence Milanzi alisema kuwa madhumuni ya mkutano huo ni kutambua changamoto na mambo ambayo yanatishia  na kuathiri uhifadhi bora wa maeneo ya urithi wa dunia katika afrika .

Aidha mkutano huo utapendekeza suluhisho kwa kupitia upya shughuli zinazotekelezwa katika eneo la urithi wa dunia na kuangalia mchango wa miradi ya jamii za kiafrika na kuandaa muelekeo wa miaka kumi ijayo.

Milanzi alisema kuwa mkutano huo utapendekeza suluhisho kwa kushawishi wanawake kuongeza ushiriki wao katika miradi inayoendana na uhifadhi wa urithi na maendeleo endelevu pamoja kuchunguza jinsi mitafaruku inayotokea kwenye maeneo ya urithi wa dunia  kutokana na makundi ya kigaidi na kutunza amani utamaduni na uridhi asilia.

Aliongeza kuwa pia  mkutano huo umejikita kwenye sera ya UNESCO  ya mwaka 2015 inayohusu kujumuisha maendeleo endelevu kwenye mkataba wa uridhi wa dunia.

Mkutano huo pamoja na matokeao tegemewa kisayansi, pia utakuwa na manufaa kwa taifa na sio tu kuitangaza Tanzania kutalii na kisasa bali pia ni fursa muhimu ya kiuchumi kutokana na idadi ya wageni watakao huthudhuria  mkutano huu pamoja na kuanzisha mitandao wa kitaaluma na kujenga mitaji wa kijamii” alisema Malinzi

Aidha pia mara baada ya mkutano huu na kupata muafaka wa yote kutakuwa na tamko lililotokana na majadiliano yaliyokuwa yakifanyika siku zote za mkutano na tamko hili linatarajiwa kutolewa katika hifadhi ya taifa ya Ngorongoro
Share:

Wahadhiri UDOM Wataja Kiini cha Mgomo Kilichosababisha Wanafunzi 7802 Warudishwe Nyumbani

INNOCENT-THE BLOGGER-BOY
JUMUIYA ya Wanataaluma ya Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOMASA) imesema kilichotokea si walimu kugoma kufundisha programu ya Stashahada Maalumu ya Elimu, Sayansi, Hisabati na Tehama, bali tatizo ni kutoelewana na Menejimenti ya chuo kutokana na mazingira mabovu ya uendeshaji wa programu hiyo chuoni hapo.

Aidha, imelaani kitendo cha wanafunzi 7,802 wa Programu Maalumu ya Ualimu wa Msingi na Sekondari, waliorudishwa nyumbani bila kupewa muda wa kutosha kujiandaa kwa kuzingatia umri wao na mazingira waliyokuwa wanaishi, hali inayofanya wazagae mitaani huku wakiwa hawana pa kwenda.

Hayo yako kwenye tamko lililotolewa jana na Katibu wa jumuiya hiyo, Lameck Thomas, ambalo lilieleza kuwa lawama zimekuwa zikitupwa kwa walimu kutokana na taarifa hizo kutolewa na upande mmoja, ambao ni Menejimenti ya chuo kwenda serikalini bila kuwepo na taarifa yoyote kutoka kwa walimu kupitia jumuiya yao.

Thomas alisema si kweli kama walimu waligoma kufundisha lakini tatizo kubwa ni kutoelewana kati ya walimu na Menejimenti ya chuo kutokana na mazingira mabovu ya uendeshaji wa programu hiyo chuoni hapo.

"Hatuzungumzii fedha zaidi tunazungumzia suala la kuboresha elimu ili taifa lipate walimu wa baadaye katika kufundisha Sayansi, Hisabati na Tehama, vifaa vya kufundishia navyo ni changamoto kubwa,” alisema.

Katibu huyo alisema kama Jumuiya ya Wanataaluma wanapata hisia kwamba Wizara ya Elimu, imeamua kwa makusudi kushirikiana na uongozi wa chuo kupotosha uhalisia wa jambo hilo kwani hakuna hata wakati moja ambao wamefanya mawasiliano na walimu wenyewe kupata ukweli kutoka upande wao.

“Alichosema waziri bungeni juzi ni taarifa ya upande mmoja ambayo haitatupeleka kwenye utatuzi wa kudumu wa suala hili kutokana na ukweli kwamba walimu nao wana mengi ya kuzungumza,” alisema katibu huyo.

Alisema serikali imejenga desturi ya kuonana na menejimenti za vyuo pindi yanapotokea matatizo bila kupata taarifa kutoka vyanzo vingine hali ambayo imekuwa inasababisha vyanzo sahihi vya matatizo kutojulikana kwa uwazi.

Alisema changamoto za ufundishaji kutokana na uhaba na walimu kulingana na idadi ya wanafunzi waliopo. Akitoa mfano alisema kwa sasa Chuo cha Sayansi Asilia na Hesabu, kina upungufu wa walimu 128 waliokuwa wanahitajika kufundisha programu hiyo kwa ufanisi; na kwa muhula uliopita walimu 72 tu ndio walibeba mzigo wa upungufu huo na muhula huu hali ilikuwa inaelekea kuwa mbaya zaidi.

“Wingi wa wanafunzi na uhaba huu wa walimu ulisababisha upangaji wa ratiba na kufundisha kutokana na ukweli kwamba kozi ziligawanywa katika mikondo mingi ambayo walimu walilazimishwa kuifundisha huku wakiwa na majukumu ya kufundisha kozi za shahada na majukumu mengine,” alifafanua.

Alisema chuo kimekuwa na desturi ya kupokea wanafunzi wengi bila kuzingatia idadi ya walimu waliopo na miundombinu ya kufundishia na kujifunzia na hiyo si mara ya kwanza kwa chuo kufanya hivyo, kwani mwaka 2008 walileta wanafunzi wengi ambao matokeo yake walimu kufundisha masomo mengi kuliko uwezo wao wa kazi.

Alisema taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Taaluma ilipotoshwa, kwani haijaeleza ukweli wa madai uliowasilishwa na chuo husika. 
Alisema katika Chuo cha Sayansi Asilia na Hesabu taarifa inasema yaliyowasilishwa ni madai ya Sh milioni 367.8 na kupungua mpaka Sh milioni 90 wakati uhalisia ni kwamba madai hayo hata yangebanwa namna gani yasingepungua mpaka chini ya Sh milioni 223.7.

Alisema mfano mwingine ni Chuo cha Elimu Masafa na Sayansi za Kompyuta ambao taarifa inasema waliwasilisha madai yanayozidi Sh milioni 100 wakati taarifa ya chuo inasema ni madai ya Sh milioni 53.7 tu.

Mwenyekiti wa jumuiya hiyo, Edson Baradyana alisikitishwa na yaliyotokea na kuitaka serikali kufanya jitihada za makusudi ili kumaliza mgogoro huo na hilo litawezekana kama walimu, wanafunzi na Menejimenti kukaa pamoja.

Baradyana alisema wanafunzi hawakutendewa haki kwani ilitolewa notisi ya ghafla ya kuondoka chuoni huku wengine wakiwa hawana nauli na hawakujua pa kwenda hali inayofanya waendelee kuzurura mitaani.

Alisema wanaamini kama Menejimenti ya chuo ingeonesha ushirikiano wa karibu kwa walimu wanaofundisha programu hiyo na kushirikiana, hayo yasingetokea au yasingekuwa makubwa kiasi hicho.

“Lazima kuangaliwa na kutatuliwa kwa changamoto nyingine zilizoibuliwa na wanataaluma na wanafunzi katika uendeshaji wa programu hiyo badala ya kujikita kwenye suala la malipo tu, serikali iwe na utaratibu wa kuwasiliana na walimu na wanafunzi mara kunapotokea matatizo vyuoni ili kupata taarifa toshelezi kutoka pande zote,” alisema Mwenyekiti wa Udomasa.

Aidha, wakati wa kurejeshwa nyumbani kwa wanafunzi hao wa Udom kukibebwa kisiasa na vyama vya upinzani, taarifa ya serikali imeeleza kuwa wahadhiri waliogoma, walitaka kulipwa posho ya zaidi ya Sh milioni 900.

Akitoa taarifa ya pili bungeni juzi usiku, Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako  alisema wanafunzi hao si sehemu ya kazi zilizoko katika mikataba ya ajira ya wahadhiri hao, ila ni sehemu ya kazi ya ziada.

Kwa kuwa kazi hiyo ni ya ziada, Profesa Ndalichako alisema walikubaliana walipwe posho ya kazi ya nyongeza ambayo uongozi wa Chuo Kikuu cha Dodoma ulikuwa tayari kutoa zaidi ya Sh milioni 200.

Kwa mujibu wa Profesa Ndalichako, wahadhiri hao walisisitiza kuwa wanataka posho hiyo iwe zaidi ya Sh milioni 900, jambo lililokataliwa na Mkaguzi wa Ndani wa Mahesabu wa Udom aliyesema kuwa kiwango hicho ni kikubwa kuliko uhalisia wa kazi yenyewe.

Kutokana na kutokubaliana kati ya wahadhiri hao na uongozi wa Udom, wahadhiri hao ndio wakaitisha mgomo wa kufundisha wanafunzi hao huku wakiendelea na kazi za kufundisha walio katika programu za shahada ya kwanza na kuendelea.

Profesa Ndalichako alisema kwa uamuzi huo wa wahadhiri, serikali isingeweza kuwachukulia hatua kwa kuwa wamegomea kazi ya ziada na si kazi waliyoajiriwa na kuingia mkataba na chuo.

Kwa hali hiyo, Profesa Ndalichako alisema serikali ililazimika kuingilia kati ambapo Mei 10, mwaka huu Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Stella Manyanya alikwenda chuoni hapo kutafuta suluhu.

Mbali na Naibu Waziri, alisema hata makatibu wakuu wa wizara hiyo nao walikwenda kuzungumza na wahadhiri hao bila mafanikio, huku wanafunzi hao wakikaa chuoni bila kuingia darasani kwa wiki ya tatu.

Profesa Ndalichako alisema mbali na madai ya wahadhiri hao, pia wakati wa kutafuta suluhu ya jambo hilo, walitazama suala la tija kwa wanafunzi hao wa diploma maalumu ambao ni zaidi ya 7,800 na pia kwa wanafunzi wa shahada ya kwanza ambao pia wanapaswa kufundishwa na wahadhiri hao.

Kutokana na kukosa masomo kwa wiki tatu mfululizo na kuwepo kwa uwezekano wa kukosekana tija katika ufundishaji, Profesa Ndalichako alisema ndio uamuzi wa kuwarudisha nyumbani wanafunzi hao ukafanyika ili serikali iangalie upya utaratibu wenye tija zaidi wa kuwaendeleza wanafunzi hao.

Aidha, Profesa Ndalichako alisema wakati wanafunzi hao wakitakiwa kurudi nyumbani, walizingatia hali yao ya kipato, kwa kuwa tayari walikuwa wameshapewa fedha za kujikimu za siku 60 tangu Aprili 21, mwaka huu. 
Profesa Ndalichako aliwataka wanafunzi hao kuvuta subira wakati serikali inatafuta namna bora ya kuwapatia elimu hiyo kwa kuzingatia tija kwao.
Share:

Waziri Mkuu: Wataalamu Wa Malikale na uhifadhi wa urithi Kuweni Wabunifu

INNOCENT-THE BLOGGER-BOY
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka wataalamu wa mambo ya malikale na uhifadhi wa urithi asilia (natural heritage) watafute mbinu zitakazoimarisha utunzaji wa rasilmali hizo bila kuathiri mifumo ya uchumi ya nchi zinazoendelea.

Ametoa wito huo jana (Jumanne, Mei 31, 2016), wakati akifungua Mkutano wa Kimataifa wa siku nne unaojadili Uhifadhi wa Urithi wa Dunia wa Afrika kama Nyenzo ya kuleta Maendeleo Endelevu ulioanza leo kwenye ukumbi wa mikutano wa kimataifa wa Arusha (AICC) jijini Arusha.

Waziri Mkuu alisema kuna baadhi ya nchi ambazo ni maskini sana lakini zimebarikiwa kuwa na rasilmali kama madini na gesi asilia lakini kwa sababu rasilmali hizo ziko karibu sana na vivutio vya urithi asilia wa dunia, watu wa nchi hizo wanazuiwa kuchuma rasilmali zao ili wasiharibu vivutio hivyo.

“Tunatambua umuhimu wa kutunza rasilmali na vivutio vya urithi asilia. Hivi ni kwa nini zisitafutwe teknolojia zinazofaa ambazo zitaruhusu uvunaji wa gesi asilia na madini bila kuathiri uhifadhi wa vivutio vya urithi asilia wa dunia (world heritage sites)?”, alihoji Waziri Mkuu.

“Serikali za nchi za Kiafrika zinahitaji suluhisho kama hili wakati zikiendelea kutafuta njia sahihi za kuwianisha uhifadhi wa vivutio vya urithi wa dunia na changamoto ya kuondoa umaskini miongoni mwa wananchi wake,” amesema.

“Sisi viongozi ambao wengi wetu ni wanasiasa, hatukatai ushauri wa wataalamu lakini tunawasihi baadhi yenu ambao mnashiriki mkutano huu muhimu, mtafute njia mbadala za kufumbua tatizo hili badala ya kuendelea kutegemea njia za kizamani za kukabiliana na changamoto kama hizi ili sote tuweze kunufaika na rasilmali zilizopo ikiwa ni pamoja na kutunza vivutio vya urithi asilia wa dunia,” aliongeza.

Alisema kama rasilmali hizo zitachambuliwa vizuri na kwa njia sahihi bila kuathiri vivutio vya urithi wa dunia, ni dhahiri kuwa zitaingiza mapato ambayo kiuchumi yatasaidia kuondoa umaskini miongoni mwa wananchi ambao pia watasaidia kwenye uhifadhi wa vivutio hivyo.

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kufungua mkutano huo, Waziri Mkuu alisema Tanzania imebarikiwa kuwa na rasilmali nyingi zikiwemo za ardhini (madini), misitu, wanyama na maeneo ya kihistoria na kusisitiza kuwa Watanzania wana jukumu la kuzilinda ili zilete tija kwa wananchi wote.

“Tukizitunza rasilmali zetu zitasaidia kupata mapato kutokana na utalii Serikali itapeleka sehemu ya mapato haya katika miradi mbalimbali na hivyo kuchangia kwenye pato la Taifa,” amesema.

Kwa upande wake, Waziri wa Maliasili na Utalii, Prof. Jumanne Maghembe amesema Tanzania itaendelea kushirikiana na UNESCO hasa katika masuala yanayohusu uhifadhi wa vivutio vya dunia kutokana na umuhimu wake kwenye maendeleo endelevu.

Alisema wizara yake imelenga kusimamia, kuendeleza na kuimarisha utunzaji wa maliasili na uhifadhi wa vivutio asilia na vya kiutamaduni (natural and cultural heritage) kwa kushirikiana na wadau wengine hapa nchini.

Naye Mkurugenzi wa Uhifadhi Malikale wa UNESCO, Dk. Mechtild Rossler aliwataka washiriki wa mkutano huo kutoka nchi mbalimbali duniani wawe tayari kupitia upya shughuli zinazotekelezwa katika eneo la urithi wa dunia na kuangalia wajibu wa nchi za Kiafrika katika kuandaa mwelekeo wa miaka ijayo.

Alisema katika miaka 40 ya utendaji wa UNESCO, idadi ya vivutio vya urithi wa dunia imeongezeka na kufikia 89 ambapo kati ya hivyo viko baadhi vinakavyobiliwa na changamoto ya kufutika kutokana na athari za kigaidi, matukio ya kivita na kazi za kibinadamu.

“Vivutio 16 kati ya 48 viko katika nchi za Afrika zilizo Kusini mwa Jangwa la Sahara na hivi vinakabiliwa na tishio la kupotea kutokana na vita, harakati za kigaidi na shughuli za kiuchumi za kibinadamu zikiwemo uchimbaji wa madini na gesi asilia,” alisema.

Aliwataka washiriki wa mkutano huo wakumbuke kuwa vivutio vya urithi wa dunia ni vielelezo vya jamii na pia huchangia uchumi kwa kutoa ajira kwenye jamii husika.

Mkutano huo unaohudhuriwa na washiriki zaidi ya 150 kutoka nchi mbalimbali duniani, unajumuisha washiriki kutoka nchi 36 zikiwemo nchi 12 ambazo ni za nje ya bara la Afrika.

Waziri Mkuu amerejea mjini Dodoma  jana mchana kuendelea na vikao vya Bunge.
Share:

Serikali Yaitaka RITA Kutoa Elimu Kwa Wananchi Kuhusu Umuhimu Kuandika Wosia Wa Mirathi

INNOCENT-THE BLOGGER-BOY

SERIKALI imeitaka wakala wa usajili,Ufilisi na Udhamini, RITA, kuhakikisha inatoa elimu ya kutosha kwa wananchi kuelewa umuhimu wa kuandika wosia na mirathi ,ili kuondoa migogoro kwa familia wakati wa kugawa mirathi ya marehemu.

Rai hiyo imetolewa jana na mkuu wa wilaya ya Arusha, Fadhili Nkurlu, alipokuwa akifungua kampeni ya siku nne ya kisheria inayotolewa bure na RITA, kuhusu kuandika mirathi na wosia na kuwaelekeza eneo salama la kuhifadhi wosia ukisha andikwa na mhusika   ili kuondoa migogoro mingi kwa familia pindi mhusika anapofariki dunia.

Mkuu huyo wa wilaya, alisema,wananchi wengi hawana elimu juu ya wosia na mirathi hivyo RITA, ambayo ni wakala wa  serikali ina jukumu kubwa la kuhakikisha elimu inawafikia wengi na hivyo kuwezesha wajane na watoto ambao ndio waathirika  kupata mirathi .

Alisema wosia unasaidia kutatua migogoro ambayo ingelijitokeza wakati wa kugawa mirathi ya marehemu na mtu kuandika wosia sio uchuro bali ni kuweka utaratibu wa mali za muhusika zitakavyogawiwa pindi akisha fariki dunia.

Aliikumbusha jamii kuwa msimamizi wa mirathi sio mrithi wa mali ya marehemu bali jukumuake ni kukusanya mali yote na madeni yote ya marehemu na kusimamia ugawaji na ulipaji wake na kamwe msimamizi yeyote asijihusishe na urithi .

Jamii nyingi zimekuwa zikiingia kwenye migogoro ya kugawana mirathi kutokana na kutokuwa na elimu ya kutosha ya kuandika wosia  kabla ya kifo na matokeo yake wanaoathirika ni wajane na watoto ambao hukosa haki yao .

Awali mratibu wa kampeni hiyo,msajili na wosia kutoka makao makuu ya RITA, Augostino Mbuya, alisema migogoro mingi imekuwa ikijitokeza kwenye familia wakati wa kugawa mirathi kutokana na kutokuwepo kwa wosia ambao ni mwongozo wa jinsi ya kuigawa mali ya marehemu kwa wahusika na matokeo yake watoto na wajane hukosa haki yao ya kurithi.

Alisema kutokana na hali hiyo RITA, ipo tayari kutoa elimu kwa umma kuhusu huduma hiyo ya kuandika wosia kutokana na wananchi wengi kutokuwa na elimu na kufahamu wapi watapata huduma hiyo ya kuandika wosia na ugawaji wa  mirathi za marehemu

Mbuya,alisema mkakati uliopo ni kusogeza huduma ya kuandika wosia na mirathi ngazi za mikoa na wilaya pamoja na kuhakikisha wanakuwepo wanasheria wa kutosha lengo ni kuiwezesha jamii kuondokana na migogoro ambayo inaweza kuepukwa wakati wa kugawa mali za marehemu.

Alisema tangia kuanzishwa kwa huduma hiyo ya Rita, imeweza kusajili wosia zaidi ya 300 na 30 kati yake zimeshachukuliwakwa  utekelezaji .

Akisoma taarifa ya kazi za Rita, msajili wa mirathi na wosia, kutoka makao makuu ya Rita, Joseph Mwakatobe amesema mahakama kuu imeiteua RITA, kusimamia utatuzi wa migogoro  ya urithi na uandishi wa wosia lngo ni kuondoa migogoro inayojitokeza pindi mtu anaofariki dunia.

Alisema Rita, itaendesha kampeni hiyo ya kuhamasisha wananchi kuhusu kuandika mirathi na wosia katika mkoa wote wa Arusha,ili kuwezesha wajane na watoto wanapata haki yao ya kurithi mali za marehemu .

Aliongeza kuwa kuandka wosia ni swala lahiari ya mtu,na Rita, imekuwa ikikumbana na changamoto mbaimbali zkiwemo za kutokuwepo na wosia wakati wa mirathi .

Aliongeza kuwa mirathi inatolewa kulingana na sheria za dini ya kiislamu, mila na sheria ya India ya mwaka 1865 ambayo inahusisha makundi yote ambayo hayapo kwenye makundi ya kidini na mila.
Share:

Taarifa toka Ikulu kuhusu uteuzi Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi TANESCO

INNOCENT-THE BLOGGER-BOY

TAARIFA KWA UMMA
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Dkt. John Pombe Magufuli, amemteua Dkt. Alex L. Kyaruzi kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO).

Kufuatia uteuzi huo, Waziri wa Nishati na Madini Mhe. Profesa Sospeter M. Muhongo (Mb.), amewateua wafuatao kuwa Wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa TANESCO kuanzia tarehe 31/5/2016 hadi tarehe 30/5/2019;
1.   Dkt. Samwel Nyantahe
2.   Dkt. Lugano Wilson
3.   Bw. David Elias Alal
4.   Mhandisi Stephen Peter Mabada
5.   Mhandisi Leonard R. Masanja

Aidha, Waziri wa Nishati na Madini, Mhe. Profesa Sospeter Muhongo (Mb) amekamilisha uteuzi wa Wajumbe wa Bodi ya Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), kuanzia tarehe 30/5/2016 hadi 29/5/2019 wajumbe  hao ni :

    Bw. Abdalah H. Musa
    Dkt. Coretha Komba
    Bw. Felix M. Maagi
    Dkt. Lightness Mnzava
    Bw. John B. Seka

Uzinduzi wa Bodi hizo utafanyika Makao Makuu ya Mashiriki hayo Siku ya Alhamisi tarehe 2 Juni, 2016, saa 4:00 asubuhi kwa Bodi ya STAMICO na saa 8:00 mchana kwa Bodi ya TANESCO.

Imetolewa na;
KATIBU MKUU
31 MEI, 2016
Share:

Rais Magufuli Awatangazia Vita Wafanyabiashara ‘Wajanja’

INNOCENT-THE BLOGGER-BOY
Rais John Magufuli amesema Serikali yake itaendelea kupambana na wanaoingiza bidhaa zilizochini ya kiwango na wale wanaokwepa kodi.

Amesema kwa kufanya hivyo, wanachangia kuviua viwanda vya ndani ya nchi.

Rais Magufuli ameyasema hayo jana kwenye hafla ya utaoji wa Tuzo ya Rais ya wazalishaji bora wa viwandani kwa mwaka 2015 zilizofanyika jijini Dar es Salaam.

Tuzo hizo zimeandaliwa na Shirika la Wenye Viwanda Nchini (CTI).

Rais amesema pia hatawavumilia watendaji wote watakao wakwamisha wafanyabiashara wenye nia ya kuanzisha viwanda nchini kwa sababu zisizo za msingi na kuwaahidi kuwasaidia waweze kufanikisha ndoto zao.

Pia, amesema ni vizuri wafanyabiashara wote nchini wakatumia fursa zipatikanazo katika awamu hii ya uongozi wake, ili wasije kuzijutia baadaye.

“Nasema kwa dhati kutoka moyoni, you have my support, mkishindwa katika kipindi cha awamu ya tano basi hamtaweza tena,” alisema.

Rais Magufuli alisema nchi inapokuwa na viwanda vingi vitatoa ajira kwa Watanzania, vitaongeza mapato kwa Serikali na kuingiza fedha za kigeni kwa kuuza bidhaa nje ya nchi.

“Nina dhamira ya dhati ndani ya moyo wangu kuwasaidia wenye nia ya kuanzisha ya viwanda, siwachukii matajiri nawapenda matajiri,” alisema.

Rais Magufuli aliwapa moyo wafanyabiashara wenye viwanda kuanzisha vingine ili Serikali iweze kunufaika zaidi.

Alisema Tanzania ina rasilimali nyingi kama maliasili na madini na akawahakikishia wawekezaji kuwa lipo soko kubwa la bidhaa watakazozitengeza lenye watu milioni 160 katika nchi za Afrika Mashariki na Kati.

Magufuli alisema sekta ya viwanda ni muhimili mkubwa wa uchumi katika nchi huku akitolea mfano wa nchi za China, India, Korea Kusini, Malaysia, Thailand na Vietnam  ambazo zimekuwa kwa kasi kwa sababu ya uwepo wa viwanda.

Alisema viwanda vinapoanzishwa nchini badala ya kuuza mali ghafi kwa bei ndogo zitatengenezwa bidhaa ambazo zitauzwa nje ya nchi na kutoa ajira kwa Watanzania.

“Badala ya kuuza ngozi tutengeneze viatu hapa hapa nchini au badala ya kuuza ng’ombe Comoro tumepeke nyama iliyosindikwa,” alisema.

Alisema nchi kama ya Sudan Kusini ina mahitaji makubwa ya unga wa mahindi.

“Lakini wanaofaidika na soko hilo ni Wakenya ambao wanakuja nchini wananunua mahindi, wanasaga na kuyapeleka huko,hivi wafanyabiashara tunashindwa hata kuanzisha viwanda vya kusaga mahindi,” alisema

Alisema Mkoa wa Arusha una ng’ombe wa  maziwa lakini yananunuliwa na Wakenya ambao wanayasindika kwenye viwanda vyao na kuja kuyauza hapa nchini.

Hata hivyo, alisema Serikali inaangalia uwezekano wa kuanzisha benki ya maendeleo ya viwanda kwa lengo la kutoa mikopo yenye masharti nafuu na riba ndogo.

Kuhusu kuondoa kwa changamoto mbalimbali zinazokwamisha maendeleo ya viwanda nchini, Magufuli alisema Serikali imeshatenga Sh1trilioni katika mwaka wa fedha ujao kwa ajili ya ujenzi wa reli ya kati kwa ajili ya kurahisisha usafirishaji wa bidhaa mbalimbali.

Pia, Serikali imeunda kamati maalumu itakayoangalia mazingira ya ufanyaji biashara nchini ikiwamo kodi na tozo mbalimbali.

“Nchi yetu inakuwa na kodi za ajabu ajabu, mfano zao la kahawa kulikua na zaidi ya kodi 30. Haya ndiyo tunayoyaangalia,” alisema.

 Kuhusu upatikanaji wa mitaji na riba kubwa zinazotozwa na benki, alisema katika kukabiliana na matatizo hayo Serikali inajiandaa kuanzisha benki ya viwanda itakayowasaidia wenye wawekezaji.

Kwa upande wake  Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage alisema Serikali imejikita katika kuhamasisha ujenzi wa viwanda vingi zaidi nchini.

“Tumeandaa mkakati wa pamba hadi inakuwa nguo, alizeti hadi mafuta na tunaendelea kufufua viwanda vilivyokufa,” alisema.

Akizungumzia changamoto zinazowakabiri wenye viwanda nchini, mwenyekiti wa Shirikisho la Wenye Viwanda (CTI), Samuel Nyantahe alisema uchakavu wa miundombinu ya umeme na miundombinu ya barabara imekuwa ikiongeza gharama za uzalishaji.

Pia, alilalamikia uwapo wa utitiri wa kodi, mamlaka za usimamiaji biashara na uwapo wa bidhaa bandia zinazotishia bidhaa za ndani.
Share:

magazeti ya leo jumatano june 1 2016,kubwa zaidi watu wa 8 wachinjwa tanga

INNOCENT-THE BLOGGER-BOY
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger