Friday 18 September 2020

Sekta ya mawasiliano ya simu inavyosaidia ukuaji wa uchumi Tanzania

...
Na Mandara Mndewa, UDBS 
Kwa miaka kadhaa sasa uchumi wa Tanzania umeendelea kukua na kuiwezesha nchi kufikia lengo la kuwa nchi ya uchumi wa kati (lower-middle-income economy) ikiwa ni miaka mitano kabla ya kufikia mwisho wa muda iliyokuwa imejiwekea.

Huku hili likitokea, Tanzania imejikita katika kuboresha zaidi mazingira ya biashara kwa ujumla na kuziimarisha biashara ambazo zimekuwa na mchango mkubwa kuwezesha kufikiwa kwa lengo la uchumi jumuishi. Kwa mujibu wa Benki ya Dunia, kwa ujumla urahisi wa kufanya biashara nchini umezidi kuongezeka kutoka asilimia 49.7 mwaka 2015 hadi 54.5 mwaka 2020.

 Takwimu kama hizi ni sehemu ya uthibitisho kuwa Tanzania imefanya mabadiliko makubwa ya kimuundo ambayo yamesaidia biashara mpya kukua na kuchagiza ukuaji wa uchumi.

Wakati huo huo, mazingira ya ufanyaji biashara nchini Tanzania pia yameimarishwa na ukuaji wa matumizi ya kidijitali. 

Kwa miaka ya hivi karibuni, miundombinu ya teknolojia ya kidijitali kama vile kebo za intaneti zilizopita chini ya bahari na uzinduzi wa teknolojia ya 4G imeunganisha watu wengi zaidi na huduma za inatenti.

Maendeleo haya yana mchango mkubwa katika uchumi wa Tanzania. Kwa mfano, kupanuka kwa matumizi ya huduma za fedha kwenye simu imewasaidia watu wengi kwa kuwapa njia bora ya kusimamia matumizi ya fedha zao pamoja na kufanya malipo.

Aidha, fursa nyingine za kiuchumi na kibiashara zimeibuka katika sekta ya biashara kwa njia ya mtandao, kuunganisha biashara ndogo na za kati (SMEs) katika soko kubwa, pamoja na kuchochea usambazaji wa maarifa kati yao na biashara kubwa.

Wakati huo huo, watoa huduma za mawasiliano ya simu nchini pia wametoa huduma za kiubunifu katika kusaidia kuweka misingi ya biashara mpya na ujasiriamali. Kwa mfano, Huduma ya Tigo-Business, huduma inayotolewa na moja ya mtoa huduma ya mawasiliano mkubwa nchini (Tigo Tanzania), imeandaliwa rasmi kwa ajili ya mahitaji ya biashara za ngazi zote.

Tigo Business inatoa huduma za jumla kwa ajili ya kuunganishwa na intaneti, uhifadhi wa taarifa na sauti. Ubunifu na teknolojia hii kwa ajili ya SMEs, unatoa fursa kwa kuwezesha upatikanaji wa soko na kujenga uhusiano na wateja wapya. Ukizingatia ukweli kwamba biashara za chini, ndogo, na za kati zinachangia takribani asilimia 27 ya Pato la Taifa (GDP) na zimetoa ajira kwa zaidi ya watu milioni 5.2, ni rahisi kuona kwa namna gani huduma kama hizi zinachochea kuisogeza mbele nchi kwa ujumla.

Sekta ya mawasiliano ya simu imesaidia kwa kiasi kikubwa ukuaji wa nchi. Ili kuweza kuifanya kampuni kama Tigo iendelee kutoa huduma za namna hii ni muhimu tukaendelea kufanya kazi kwa karibu na sekta hiyo. Kwa kusisitiza uwepo wa kanuni rafiki ambazo zitachochea weledi na utendaji kazi, tutaendelea kuwa na uhakika kuwa sekta hiyo itaendelea kuchochea ukuaji wa uchumi na kuboresha maisha ya Watanzania wengi zaidi na zaidi.


Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger